MALAKI
1 Tangazo:
Neno la Yehova kwa Waisraeli kupitia Malaki:*
2 “Nimewaonyesha ninyi watu upendo,”+ asema Yehova.
Lakini mnauliza: “Umetuonyeshaje upendo?”
“Je, Esau hakuwa ndugu ya Yakobo?”+ asema Yehova. “Lakini nilimpenda Yakobo, 3 nami nikamchukia Esau;+ nikafanya milima yake kuwa ukiwa+ na urithi wake nikawaachia mbwamwitu wa nyikani.”+
4 “Ingawa Waedomu wanasema, ‘Tumevunjwavunjwa, lakini tutarudi na kujenga tena magofu,’ Yehova wa majeshi anasema hivi: ‘Watajenga, lakini nitabomoa, nao wataitwa “eneo la uovu” na “watu ambao Yehova amewahukumu milele.”+ 5 Macho yenu wenyewe yataona hilo, nanyi mtasema: “Yehova na atukuzwe katika eneo la Israeli.”’”
6 “‘Mwana humheshimu baba yake,+ na mtumishi bwana wake. Basi ikiwa mimi ni baba,+ iko wapi heshima ninayostahili?+ Na ikiwa mimi ni bwana,* iko wapi hofu* ninayostahili?’ Mimi Yehova wa majeshi ninawauliza ninyi makuhani mnaolidharau jina langu.+
“‘Lakini mnauliza: “Tumelidharau jina lako kwa njia gani?”’
7 “‘Kwa kutoa chakula kilichochafuliwa* juu ya madhabahu yangu.’
“‘Nanyi mnauliza: “Tumekuchafua jinsi gani?”’
“‘Kwa kusema: “Meza ya Yehova+ ni kitu cha kudharauliwa.” 8 Na mnapomtoa mnyama kipofu kuwa dhabihu, mnasema: “Si vibaya.” Na mnapomtoa mnyama kilema au mgonjwa mnasema: “Si vibaya.”’”+
“Tafadhali, jaribuni kumtolea gavana wenu vitu hivyo. Je, atapendezwa nanyi au kuwapokea ninyi kwa kibali?” asema Yehova wa majeshi.
9 “Na sasa, tafadhali, msihini* Mungu ili atuonyeshe kibali. Mkitoa dhabihu za aina hiyo kwa mikono yenu, je, atampokea yeyote kati yenu kwa kibali?” auliza Yehova wa majeshi.
10 “Na ni nani miongoni mwenu aliye tayari kufunga milango?*+ Kwa maana hata hamtawasha moto kwenye madhabahu yangu bila malipo.+ Sipendezwi nanyi,” asema Yehova wa majeshi, “nami sipendezwi na zawadi yoyote kutoka mikononi mwenu.”+
11 “Kwa maana tangu jua linapochomoza mpaka linapotua,* jina langu litakuwa kuu miongoni mwa mataifa.+ Kila mahali dhabihu zitafukizwa moshi, na matoleo yatatolewa kwa jina langu, yakiwa zawadi safi; kwa sababu jina langu litakuwa kuu miongoni mwa mataifa,”+ asema Yehova wa majeshi.
12 “Lakini ninyi mnalitia unajisi*+ kwa kusema, ‘Meza ya Yehova imechafuliwa, matunda yake, chakula chake, ni kitu cha kudharauliwa.’+ 13 Pia mnasema, ‘Tazama! Inachosha kwelikweli!’ na kwa pua zenu mnaishushia pumzi kwa dharau,” asema Yehova wa majeshi. “Nanyi mnaleta wanyama walioibwa, vilema, na wagonjwa. Naam, mnaleta vitu hivyo kuwa zawadi! Je, niikubali kutoka mikononi mwenu?”+ auliza Yehova.
14 “Amelaaniwa mtu mjanja aliye na mnyama asiye na kasoro katika kundi lake, lakini anaapa na kumtolea Yehova dhabihu ya mnyama mwenye kasoro.* Kwa maana mimi ni Mfalme mkuu,”+ asema Yehova wa majeshi, “na jina langu litakuwa lenye kuogopesha miongoni mwa mataifa.”+
2 “Na sasa, enyi makuhani, amri hii inawahusu.+ 2 Mkikataa kusikiliza na kuitia moyoni mwenu ili kulitukuza jina langu,” asema Yehova wa majeshi, “nitawaletea laana,+ nami nitabadili baraka zenu ziwe laana.+ Naam, nimebadili baraka ziwe laana, kwa sababu hamwitii moyoni mwenu.”
3 “Tazameni! Nitaharibu* mbegu zenu zilizopandwa kwa sababu yenu,+ nami nitawapaka kinyesi cha wanyama usoni, kinyesi cha sherehe zenu; nanyi mtabebwa na kupelekwa kwenye kinyesi hicho.* 4 Ndipo mtakapojua kwamba nimewapa amri hii ili agano langu pamoja na Lawi liendelee,”+ asema Yehova wa majeshi.
5 “Agano langu pamoja naye lilikuwa la uzima na amani, ambalo nilimpa, pamoja na hofu.* Aliniogopa, naam, aliliheshimu jina langu. 6 Sheria ya kweli ilikuwa* kinywani mwake,+ na ukosefu wa uadilifu haukupatikana midomoni mwake. Alitembea pamoja nami kwa amani na kwa unyoofu,+ naye aliwageuza wengi kutoka katika uovu. 7 Kwa maana midomo ya kuhani inapaswa kulinda ujuzi, na watu wanapaswa kutafuta sheria* kutoka kinywani mwake,+ kwa sababu yeye ni mjumbe wa Yehova wa majeshi.
8 “Lakini ninyi wenyewe mmegeuka na kuiacha njia. Mmewafanya wengi wajikwae kuhusiana na sheria.*+ Mmeliharibu agano la Lawi,”+ asema Yehova wa majeshi. 9 “Kwa hiyo nitawafanya ninyi mdharauliwe na kuwa duni mbele ya watu wote, kwa sababu hamkushika njia zangu badala yake mliitekeleza sheria kwa upendeleo.”*+
10 “Je, sisi sote hatuna baba mmoja?+ Je, hatukuumbwa na Mungu yuleyule? Basi kwa nini tunatendeana kwa hila,+ na kulitia unajisi agano la mababu zetu? 11 Yuda ametenda kwa hila, na jambo fulani lenye kuchukiza limetendwa Israeli na Yerusalemu; kwa maana Yuda ameutia unajisi utakatifu wa* Yehova,+ Anaoupenda, naye amemchukua binti ya mungu wa kigeni kuwa bibi harusi.+ 12 Yehova atamwangamiza kutoka katika mahema ya Yakobo mtu yeyote anayefanya hivyo, mtu yeyote yule,* hata ingawa anamtolea zawadi Yehova wa majeshi.”+
13 “Na kuna jambo lingine* mnalotenda linalofanya madhabahu ya Yehova ifunikwe kwa machozi na kilio na maombolezo, hivi kwamba hakazii tena uangalifu zawadi mnayomtolea wala kutazama kwa kibali kitu chochote kinachotoka mikononi mwenu.+ 14 Nanyi mnauliza, ‘Kwa sababu gani?’ Ni kwa sababu Yehova amekuwa shahidi kati yako na mke wa ujana wako, ambaye umemtendea kwa hila, ingawa yeye ni mwenzi wako na mke wako kupitia agano.*+ 15 Lakini kuna mtu ambaye hakufanya hivyo, kwa sababu ya roho iliyobaki ndani yake. Na mtu huyo alikuwa akitafuta nini? Uzao wa* Mungu. Basi jilindeni kuhusiana na roho yenu, na usimtendee kwa hila mke wa ujana wako. 16 Kwa maana ninachukia* talaka,”+ asema Yehova Mungu wa Israeli, “na pia yule anayefunika vazi lake kwa ukatili,”* asema Yehova wa majeshi. “Nanyi jilindeni wenyewe kuhusiana na roho yenu, na hampaswi kutenda kwa hila.+
17 “Mmemchosha Yehova kwa maneno yenu.+ Lakini mnauliza, ‘Tumemchoshaje?’ Kwa kusema, ‘Kila mtu anayetenda maovu ni mwema machoni pa Yehova, naye hupendezwa na mtu huyo,’+ au kwa kuuliza, ‘Yuko wapi Mungu wa haki?’”
3 “Tazama! Ninamtuma mjumbe wangu, naye atafungua* njia mbele yangu.+ Na ghafla Bwana wa kweli, mnayemtafuta, atakuja katika hekalu lake;+ na mjumbe wa agano atakuja, mnayependezwa naye. Tazama! Kwa hakika atakuja,” asema Yehova wa majeshi.
2 “Lakini ni nani atakayestahimili siku atakayokuja, na ni nani atakayeweza kusimama atakapotokea? Kwa maana atakuwa kama moto wa msafishaji wa madini na kama sabuni+ ya wafuaji wa nguo. 3 Naye ataketi kama msafishaji na mtakasaji wa fedha,+ naye atawatakasa wana wa Lawi; atawasafisha kama dhahabu na kama fedha, nao hakika watakuwa watu wanaomtolea Yehova zawadi kwa uadilifu. 4 Na kwa kweli zawadi ya Yuda na Yerusalemu itampendeza* Yehova, kama ilivyokuwa katika siku za kale na kama ilivyokuwa katika miaka ya zamani za kale.+
5 “Nitawakaribia ili niwahukumu, nami nitakuwa shahidi asiyesita* dhidi ya walozi,+ dhidi ya wazinzi, dhidi ya watu wanaotoa viapo vya uwongo,+ dhidi ya wale wanaomlaghai kibarua,+ mjane, na yatima,*+ na dhidi ya wale wanaokataa kumsaidia* mgeni.+ Watu hao hawaniogopi,” asema Yehova wa majeshi.
6 “Kwa maana mimi ni Yehova; sibadiliki.*+ Nanyi ni wana wa Yakobo; bado hamjaangamia. 7 Tangu siku za mababu zenu mmegeuka na kuacha masharti yangu nanyi hamjayashika.+ Nirudieni, nami nitawarudia,”+ asema Yehova wa majeshi.
Lakini mnauliza: “Tukurudie jinsi gani?”
8 “Je, mwanadamu anaweza kumwibia Mungu? Lakini ninyi mnaniibia.”
Nanyi mnauliza: “Tumekuibia jinsi gani?”
“Katika sehemu za kumi na michango. 9 Kwa hakika mmelaaniwa,* kwa maana mnaniibia—naam, taifa zima linafanya hivyo. 10 Leteni ghalani sehemu yote ya* kumi,+ ili kuwe na chakula nyumbani mwangu;+ tafadhali, nijaribuni kwa njia hii,” asema Yehova wa majeshi, “mwone kama sitawafungulia malango ya mbinguni ya mafuriko+ na kuwamwagia baraka hivi kwamba hamtakosa chochote.”+
11 “Na kwa ajili yenu nitamkemea yule anayenyafua,* naye hataharibu mazao ya nchi yenu, wala mzabibu wa shamba lenu hautakosa matunda,”+ asema Yehova wa majeshi.
12 “Mataifa yote yatalazimika kuwatangaza ninyi kuwa wenye furaha,+ kwa maana mtakuwa nchi ya kupendeza,” asema Yehova wa majeshi.
13 “Maneno yenu dhidi yangu yamekuwa makali,” asema Yehova.
Nanyi mnauliza: “Ni katika njia gani tumesema maneno makali dhidi yako miongoni mwetu?”+
14 “Mnasema, ‘Hakuna faida yoyote ya kumtumikia Mungu.+ Tumefaidikaje kwa kutimiza wajibu wetu kwake na kutembea kwa huzuni mbele za Yehova wa majeshi? 15 Sasa tunawaona watu wenye kimbelembele kuwa wenye furaha. Pia, watu wanaotenda maovu wanafanikiwa.+ Wanathubutu kumjaribu Mungu, nao hawaadhibiwi.’”
16 Wakati huo wale wanaomwogopa Yehova walizungumza kila mmoja na mwenzake, na Yehova akaendelea kuwakazia uangalifu na kusikiliza. Na kitabu cha kumbukumbu kikaandikwa mbele zake+ kwa ajili ya wale wanaomwogopa Yehova na wale wanaolitafakari* jina lake.+
17 “Nao watakuwa wangu,”+ asema Yehova wa majeshi, “siku nitakayotokeza mali ya pekee.*+ Nitawahurumia, kama mwanamume anavyomhurumia mwana wake anayemtumikia.+ 18 Nanyi mtaona tena tofauti kati ya mtu mwadilifu na mtu mwovu,+ kati ya yule anayemtumikia Mungu na yule asiyemtumikia.”
4 “Kwa maana tazama! siku inakuja inayowaka kama tanuru,+ wakati ambapo wote wenye kimbelembele na wote wanaotenda uovu watakuwa kama majani makavu. Siku hiyo inayokuja kwa hakika itawateketeza,” asema Yehova wa majeshi, “nayo haitawaachia mzizi wala tawi. 2 Lakini ninyi mnaoliheshimu* jina langu, jua la uadilifu litawaangazia likiwa na miale inayoponya;* nanyi mtaruka huku na huku kama ndama waliononeshwa.”
3 “Nanyi mtawakanyaga-kanyaga waovu chini ya miguu yenu, kwa sababu watakuwa kama mavumbi chini ya nyayo zenu siku nitakayochukua hatua,” asema Yehova wa majeshi.
4 “Kumbukeni Sheria ya Musa mtumishi wangu, masharti na maamuzi niliyoamuru kule Horebu ili Waisraeli wote wayatii.+
5 “Tazama! Namtuma kwenu nabii Eliya+ kabla haijaja ile siku kuu ya Yehova yenye kuogopesha.+ 6 Naye ataigeuza mioyo ya akina baba iwarudie wana,+ na mioyo ya wana iwarudie akina baba, ili nisije na kuipiga dunia, na hivyo kuiangamiza.”
(Mwisho wa tafsiri ya Maandiko ya Kiebrania na Kiaramu. Ifuatayo ni tafsiri ya Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo)
Maana yake “Mjumbe Wangu.”
Au “bwana mkubwa.”
Au “heshima.”
Tnn., “mkate uliotiwa unajisi.”
Tnn., “utulizeni uso wa.”
Inaonekana ni wajibu wa kufunga milango ya hekalu.
Au “kutoka mashariki mpaka magharibi.”
Au labda, “mnanitia unajisi.”
Au “dosari.”
Tnn., “Nitakemea.”
Yaani, mahali ambapo kinyesi cha wanyama wa dhabihu kilitupwa.
Au “heshima, adhama.”
Au “Mafundisho ya kweli yalikuwa.”
Au “mafundisho.”
Au labda, “kwa mafundisho yenu.”
Au “ubaguzi.”
Au labda, “ametia unajisi mahali patakatifu pa.”
Tnn., “yule aliye macho na yule anayejibu.”
Tnn., “la pili.”
Au “mke wako halali.”
Tnn., “Mbegu ya.”
Tnn., “anachukia.”
Tnn., “anayetenda ukatili.”
Au “atatayarisha.”
Au “itamridhisha.”
Tnn., “mwepesi.”
Tnn., “mtoto asiye na baba.”
Au “wanaomnyima haki.”
Au “sijabadilika.”
Au labda, “Kwa laana mnanilaani.”
Au “sehemu zote za.”
Inaonekana ni pigo la wadudu.
Au “wanaolifikiria.” Au labda, “wanaolithamini.”
Au “mali ninayothamini sana.”
Tnn., “mnaoliogopa.”
Tnn., “mabawa yanayoponya.”