Njia Kumi za Kuacha Kuvuta Sigareti
1. Uwe na kichocheo cha kweli kweli. Uwe na sababu thabiti za kutaka kuacha kabisa—kujistahi (kujiheshimu); kuhangaikia afya yako, ya sasa na ya wakati ujao; kuhangaikia wapendwa wenye kuathiriwa na tabia yako hatari; tamaa ya kuwa safi, kimwili na kiadili, mbele yako mwenyewe na mbele za Mungu.
2. Jiwekee tarehe ya kuacha kabisa, kisha uifuate. Jipige konde la kifua uamue kuacha ghafula; njia hiyo huumiza haraka-haraka, lakini huponya haraka-haraka pia.
3. Chukua hatua hakika ili uvunje tabia hiyo. Zivunje-vunje sigareti zozote zilizo ndani ya nyumba, na umwage maji juu yazo. Fua nguo zako zote zenye harufu ya tumbako. Anza mambo yako upya, uhisi ukiwa na hali ya upya!
4. Unapokuwa ukikamilisha kujiondoa kabisa kwenye nikotini, epuka mazingira yenye tumbako nyingi na uepuke marafiki wavutaji. Zuru sehemu-sehemu ambako kuvuta sigareti hukatazwa, kama majumba ya vitu vya makumbusho na maktaba.
5. Weka akiba ya pesa ambazo ungalitumia kwa tumbako na uzihesabu baada ya mwezi mmoja! Nunua kitu ambacho wakihitaji kweli kweli. Au mnunulie zawadi mpendwa ambaye pia aweza kuushangilia ushindi wako.
6. Jitie wewe mwenyewe na mikono yako katika shughuli nyingi wakati ambapo kwa kawaida ungenyoosha mkono uchukue sigareti. Tafuna gamu (si gamu yenye nikotini) au umumunye peremende ukikazwa-kazwa na tamaa ya kuvuta sigareti. Badala ya kuvuta sigareti baada ya nyakati za chakula, safisha meno yako. Tembea mwendo fulani, andika barua, shona nguo, fanya kazi ya bustani, tengeneza vitu vilivyoharibika, safisha gari, na kadhalika.
7. Ukihisi ukiwa na wasiwasi au ukiwa chini ya mkazo, pumua kwa kina kirefu na polepole. Badala ya kunyoosha mkono uchukue sigareti, kunywa maji mengi na majimaji ya matunda. Maji husafisha mwili.
8. Fanya mazoezi bila kuruka mipaka ya uwezo wako wa kimwili. Kwanza chunguza na daktari wako ujue ni kiasi gani kifaacho. Hali yako yenye maendeleo ya kimwili itakutia moyo.
9. Punguza kiasi cha kileo ambacho wewe hunywa. Mara nyingi kileo na sigareti “huenda pamoja,” kwa kuwa kileo chaweza kuamsha tamaa ya kuvuta sigareti. Punguza pindi za kujifurahisha ambapo jambo hili lingeweza kutukia. Yaone matangazo ya tumbako kwa njia yenye uchambuzi—changanua jambo la kwamba matangazo huonekana kuwa bora kijuu-juu tu tena ni ya udanganyifu. Usinaswe tena.
10. Ikiwa wewe unatafakari kuwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova, mpelekee Mungu sala za moyo wa bidii ili kuomba msaada halafu utende kupatana na sala zako. Usitarajie muujiza; jitahidi ili iwezekane kuacha.