Upatanisho wa Kipekee
NA MLETA-HABARI WA AMKENI! KATIKA UINGEREZA
BRUCE alikuwa na umri wa miaka miwili katika mwaka wa 1945 wakati mama yake, Marie, alipomwona mara ya mwisho. Kufuatia talaka ya Marie, baba ya Bruce alipewa malezi kisheria kwa ajili yake. Akikandamiza hisia zake za asili, Marie aliamua kwamba ingekuwa kwa faida ya mwana wake akilelewa na baba yake na mama yake wa kambo bila uvutano wowote wa kihisia-moyo kutoka kwake. Baadaye, alipoteza uwasiliano wote na Bruce.
Miaka kadhaa baadaye Marie aliolewa tena na akazaa mwana mwingine, lakini bado mawazo yake yalirudi kwa Bruce. Alikuwa wapi? Ametokewa na nini?
Baba ya Bruce alipokufa katika mwaka wa 1976, Marie alihudhuria maziko yake. Bruce, sasa akiwa mwanamume mzuri mchanga katika miaka yake ya 30, alikuwako pamoja na mama yake wa kambo. Kwa kuwa Marie bado aliamini kuwa Bruce alidhani kuwa mama yake wa kambo ndiye aliyekuwa mama yake wa asili, alihisi lingekuwa jambo lisilo la fadhili kujijulisha kwake, hasa katika wakati kama huo. Marie angetenda tofauti ikiwa angejua kuwa Bruce alikuwa amekataliwa na baba yake mara tu alipooa tena na alikuwa amelelewa na nyanya yake.
Karibu na wakati huu Marie alikutana na Sue, mmoja wa Mashahidi wa Yehova, na kwa utayari akakubali kuwa na funzo la Biblia nyumbani. Wakati huohuo, kwa sadfa, Bruce na mke wake wakaanza kujifunza Biblia pamoja na mume wa Sue, Alan. Hata hivyo, upesi, kwa sababu ya matatizo ya afya, Marie aliacha kujifunza akahama.
Marie alikutana tena na Mashahidi wa Yehova katika mwaka wa 1995. Alirudia tena funzo lake la Biblia akafanya maendeleo haraka. Alipokaribia ubatizo, Marie alimwambia mzee mmoja Mkristo siri kuhusu Bruce. Mzee huyo alifanya uchunguzi akapata si kwamba Bruce na familia yake walikuwa Mashahidi wa Yehova tu bali kuwa Bruce alikuwa mzee katika kutaniko moja katika mji wa nyumbani wa Marie!
Wazee wale wengine katika kutaniko la Bruce walikuwa wenye hofu. Ikiwa wangemwambia Bruce kuwa mama yake angebatizwa katika siku ya kusanyiko la pekee iliyofuata angetendaje? Je, alijua kuwa alikuwako? Hata hivyo, mara tu Bruce alipojua mambo ya hakika, alienda mbio pamoja na familia yake kukutana na Marie. “Mambo yaliyopita hayana maana; ya wakati ujao ndiyo yaliyo ya maana katika kweli!” yalikuwa maneno yenye kufariji ya Bruce alipokuwa akimkumbatia mama yake.
Katika Machi mwaka wa 1996, Marie, wakati huo akiwa mwenye umri wa miaka 78, alibatizwa katika Jumba la Kusanyiko la Mashahidi wa Yehova katika East Pennine Uingereza—na Bruce. Bruce alisisimuka jinsi gani kumpata mama yake akiwa dada wa kiroho!
[Picha katika ukurasa wa 24]
Bruce, na mama yake