Maswali Kutoka kwa Wasomaji
● Je! ni jambo linalolingana na Maandiko kutenda kama mdhamini wa ubatizo au kuchagua wadhamini wa ubatizo kwa watoto wa mtu?—U.S.A.
Mazoea ya kumchagua mtu fulani au watu wasio wazazi kama wadhamini wa ubatizo kwa kitoto au mtoto wakati wa ubatizo wake wa kidini na, nyumaye, katika Kipa imara cha mtu huyo, ni kawaida ya Kanisa la Katoliki. Mazoea hayo vile vile yanatumika kwa watu wazima wanapobatizwa au kupata Kipa imara.
Katika ubatizo wa vitoto wadhamini wa ubatizo (kwa kawaida watu wa udugu au marafiki waliobatizwa) wanauliza “imani kutoka kwa Kanisa la Mungu katika jina la mtoto.” (The Catholic Encyclopedia) Vile vile wanafanya ungamo na tangazo la imani na kuomba ubatizo, katika jina la mtoto. Kwa habari ya ukosefu wa wazazi, yaani, kushindwa kwao kumlea mtoto katika imani ya Kikatoliki, wadhamini wa ubatizo wana wajibu wa kumfundisha juu ya imani na adili.
Katika kanuni ya Kipa imara (kama ubatizo, unaoonwa kama sakramenti) kwa kawaida mtu mwingine (au watu), asiye mdhamini (au wadhamini) wa ubatizo aliyechaguliwa wakati wa ubatizo wa mtoto, anatenda kama mdhamini. Kama ni mwanamume au mwanamke ni lazima awe anajua mengi katika imani ya Katoliki.
Nia ya Maandiko ni nini juu ya mazoea haya? Kwanza, ubatizo wa vitoto vichanga haulingani na Maandiko. Kwa sababu ya uhakika wa kwamba ‘kupokea neno kwa masikio ya mtu’ na ‘kufanya toba’ vinatangulia ubatizo wa maji, na kwamba ubatizo unamtaka mtu mwenyewe afanye uamuzi mzito, ni wazi kwamba ni lazima awe mwenye umri wa kujifanyia mambo mwenyewe. (Matendo 2:14, 38, 41, Douay Version) Mtume Paulo anaandika: “Kwa kuwa, kwa moyo, tunaamini mpaka haki: lakini, kwa kinywa, ungamo linafanywa mpaka wokovu.” (Rum. 10:10, Dy) Hili kitoto au mtoto mdogo sana hangeweza kufanya. Hivyo ubatizo wa vitoto unakatazwa na Maandiko.
Tena, hakuna mtu anayeweza kwa kweli kuamini kwa moyo au kufanya ungamo kwa kinywa kwa ajili ya mtu mwingine. Kweli, mtume Paulo alionyesha kwamba watoto wadogo watiifu ni “watakatifu” kwa sababu ya mzazi mwaminifu. Hii ni kwa sababu Mungu anawaona wazazi, si watu wengine nje, wana daraka kwa watoto. (1 Kor. 7:14) Mungu kwa hiyo anafanya mpango wenye fadhili kwa ajili ya watumishi wake waaminifu. Lakini wakati watoto hao wanapofikia umri wa kuchukua daraka hawako tena chini ya mpango huu. Kila mmoja lazima asimame au aanguke kulingana na imani yake mwenyewe.—Rum. 14:4; Eze. 18:20.
Ni kweli kwamba mtume Paulo alisema kwa kundi la Korintho: “Kwa kuwa mkiwa na waalimu elfu kumi katika Kristo, hata hivyo si baba wengi. Kwa kuwa katika Kristo Yesu, kwa injili, mimi nimewazaa.” (1 Kor. 4:15, Dy) Lakini, Paulo hakuwa “mdhamini wa ubatizo” kwa kundi hili. Pahali pake, mbeleni alikuwa amewaletea injili ambayo kwayo wakawa waamini. Katika maana ya kiroho akawa baba kwao kupitia kwa habari hii yenye kutoa uzima, ingawa watu wengine walishiriki nyumaye katika kuwafundisha. Ilimlazimu Paulo kuwakumbusha Wakristo Wakorintho juu ya uhakika huu kwa kuwa walikuwa wakipotoshwa kutoka kwa Kristo na mitume wa uongo. Si kwamba alitaka aitwe “Baba”, au kwamba alikuwa akielekeza kwa cheo kilichowekwa na kanisa cha mdhamini wa ubatizo.—2 Kor. 11:3, 13.
Leo katika sehemu nyingi mazoea ya kuwa na wadhamini wa ubatizo ni desturi tu. Kwa kawaida mdhamini wa ubatizo anampa mtoto zawadi, na nyuma ya hapo mara nyingi hajishugulishi sana na mtoto mwenyewe, kama kwa habari ya kumzoeza katika imani. Hata hivyo, kwa kuwa kanuni hiyo ina msingi wa mapokeo ya kikatoliki na inatofautiana na maandiko, Wakristo wa kweli wataepuka kukamatana ko kote na mazoea hayo.
● Je! neno por·neiʹa (ufisadi mbaya sana) linalotajwa katika Biblia linatia na kupiga punyeto, ikifanya kupiga punyeto msingi halali wa talaka inayolingana na Maandiko?—Ecuador.
Biblia haitaji kupiga punyeto wala kujichua, na hakuna kinachoonyesha kwamba neno la Kigiriki por·neiʹa lilitia ndani tendo hili.
Kwa wazi kupiga punyeto ni tabia chafu. Hii ni wazi kutokana na uhakika wa kwamba hata kutoka kwa shahawa kwa kutokusudia kulimfanya mwanamume mchafu kwa sherehe mpaka jioni, kulingana na sheria ya Musa. (Law. 15:16; Kum. 23:10, 11) Kwa kuwa ndivyo ilivyokuwa, kutoa shahawa kwa makusudi kwa kupiga punyeto kungekuwa uchafu mkubwa zaidi. Lakini haukuwa mzito kama ufisadi mbaya sana unaoonyeshwa na neno la Kigiriki por·neiʹa mwenzake na kulalana na mnyama (namna mbalimbali za por·neiʹa) yalikuwa makosa makubwa chini ya Torati na kwa hiyo yalifanya iwezekane kwa mwenzi yule mwingine aoe au aolewe. (Law. 20:10, 13, 15, 16) Lakini hatuwezi tukaonyesha ushuhuda wa kwamba ndivyo ilivyokuwa kwa habari ya kupiga punyeto.
Hata hivyo, Biblia inakanya kwa nguvu matendo hayo machafu. Mtume Paulo aliyeongozwa na roho ya Mungu aliwaandikia waamini wenzake hivi: “Mungu hakutuitia uchafu, bali tuwe katika utakaso.” (1 The. 4:7) Kwa hiyo, imempasa Mkristo ajitahidi sana kuepuka tabia zo zote zilizo chafu, kutia na kupiga punyeto.a
[Maelezo ya Chini]
a Kwa habari ya kuacha kupiga punyeto, tazama Mnara wa Mlinzi wa Machi 15, 1974.