Ni Kweli Kwamba Kuna “Mbwa-Mwitu” Wanadamu
● Gazeti “Family Health” la Oktoba 1976 linasema: “Visa viwili vilivyotokea majuzi katika Appalachia [jimbo moja la United States], vilivyoripotiwa na madaktari wa Chuo Kikuu cha Kentucky, vinaonyesha kwamba ile hali ya mtu kujisikia akibadilika kuwa mbwa-mwitu ingali inatokea leo kwa sababu ya watu kuharibika akili.” Mmoja wa watu waliopatwa na hali hiyo ni mwanamume wa makamu ambaye “alilala makaburini mara nyingi na kuupigia mwezi kelele kama mbwa-mwitu.” Yule mwingine, aliyekuwa mwanamume kijana, alizidi tu kujisikia akitaka kukimbiza sungara walio hai na kuwala, bila kutaka kuacha kufanya hivyo.”
Ingawa huenda wasomaji fulani wakadhani kwamba ripoti hizo zimeandikwa ili kuchekesha watu tu, wengine wanaweza kuona kwamba visa hivyo vinazidi kuhakikisha ukweli wa masimulizi ya Biblia yanayosema kwamba Mfalme Nebukadreza alipatwa na wazimu. Ili kutimiza ndoto ya unabii aliyoelezwa na nabii Danieli, mkuu huyo wa Babeli alipigwa kwa wazimu muda wa miaka saba, “akala majani kama ng’ombe.” Kwa habari ya vile alivyoharibika akili, imesemwa hivi: “Namna ya wazimu aliopata kwa sababu ya kujawa na kiburi ni ugonjwa ule unaofanya mgonjwa adhani yeye ni mmoja wa wanyama na kutenda mambo kama mnyama.” (“The Westminster Dictionary of the Bible,” uku. 422) Baada ya miaka saba, Mungu alimrudishia Nebukadreza fahamu zake.