Wewe Ni Mdogo Mno Hivi Kwamba Hufai Kitu?
JE! NYAKATI nyingine wewe unajisikia kwamba hakuna mtu anayekujali? Umepata kujisikia mpweke ingawa ulikuwa umezungukwa na watu? Kwa sababu gani mawazo kama hayo yakusumbue-sumbue? Ni kwa sababu mara nyingi leo watu wameacha kumhesabu mtu binafsi kuwa wa maana.
Katika nchi nyingi utawala usiofuata sana maoni ya watu umewatumia wao kama vidude au vinyangarika tu. Je! Nyakati nyingine wewe unajisikia ukiwa hivyo?
Au labda wewe ni mfanya kazi wa shirika kubwa lenye mamia ya maelfu ya wafanya kazi. Kwa sababu hiyo unajisikia wewe ni katu kadogo tu. Hata wale wanaokaa katika majiji wanaweza kujisikia wapweke kabisa. Kwa sababu gani? Kwa sababu mara nyingi majirani wanawatendea kama kwamba ni watu ambao hawajapata kuwaona hata siku moja. Wanawaona kuwa akina fulani tu wa nyumba namba fulani tu.
Ndiyo, ni jambo jepesi sana kuamini kwamba wewe ni mdogo mno hivi kwamba hufai kitu, kwamba wewe ni kabwela tu asiyefaa kufikiriwa katika pilikapilika za maisha ya kisasa. Ndivyo ilivyo hasa katika jamii ya kisasa, ambamo hali ya kushindana imetokeza watu wengi sana wasiojali wenzao. Hali ya kuheshimu watu inapuzwa kabisa. Watu wanafikiria maneno kama “Potelea mbali, ni shauri lako” ni jibu zuri kutolea wenzao.
Lakini ndivyo Mungu pia alivyo? Je! yeye, Bwana Mwenye Enzi Kuu wa ulimwengu mzima wote, anajiona mkubwa sana kuliko wanadamu hivi kwamba sisi sote tunakuwa wadogo mno tusifae kitu mbele zake? Biblia inaonyesha kwamba pindi moja Yehova Mungu alikuwa na malaika “elfu kumi mara elfu kumi [milioni 100]” wakiwa wamesimama mbele zake. (Danieli 7:10) Yeye pia ndiye Muumba wa nyota zisizohesabika zilizo katika ulimwengu mzima wote. Je! inaweza kuwa kwamba yeye amesahau vingine vya viumbe vyote hivyo vya kiroho na vya kimwili? Biblia inajibu hivi: “Huihesabu idadi ya nyota, huzipa zote majina.” (Zaburi 147:4) Kwa uhakika, hayo madude ya mbinguni hayakosi mtu wa kuyatolea uongozi. Kwa habari ya hao malaika waadilifu, bila shaka Yehova anawaita kwa jina, ingawa ni majina ya wawili tu kati yao, Mikaeli na Gabrieli, yamefunuliwa kwa mwanadamu.—Danieli 12:1; Luka 1:26.
Basi namna gani wanadamu? Je! Mungu anajali? Mtunga zaburi Daudi aliandika hivi: “[Yehova], unijulishe mwisho wangu, na kiasi cha siku zangu ni kiasi gani; nijue jinsi nilivyo dhaifu. Tazama, umefanya siku zangu kuwa mashubiri; maisha yangu ni kama si kitu mbele zako. Kila mwanadamu . . . ni ubatili [mpumuo, NW].” (Zaburi 39:4, 5) Ikiwa mwanadamu ni kitu cha muda mfupi tu kama mpumuo (mvuke), basi tunawezaje kuwe na uhakika kwamba yeye si mdogo mno na wa muda mfupi mno hata Mungu akose kumjali? Kulingana na maoni ya Mungu, je! wanadamu ni watu wa maana kweli? Je! WEWE unahesabiwa kuwa mtu wa maana kweli?