Ripoti ya Watangazaji Ufalme
Katika Siku Tisa Tu!
“MAAJABU! ” Neno hilo moja tu ndilo lililokuwa kichwa cha makala ya mhariri katika gazeti moja la Vancouver Island, Kanada tarehe ya Agosti 14, 1985. Makala hiyo ya mhariri ilieleza habari za ujenzi wa Jumba la Kusanyiko la mita 2,300 za mraba katika muda wa siku tisa tu.
Katika muda wa miaka zaidi ya 10 iliyopita, Mashahidi wa Yehova wamesitawisha ufundi fulani wa kujenga upesi Majumba ya Ufalme katika maeneo yao. Lakini Jumba la Kusanyiko la Mashahidi wa Yehova katika Vancouver Island ndilo jengo la kwanza la namna hiyo katika Kanada lililoundwa hasa kwa ajili ya makusanyiko ya mizunguko ya mafungu ya makundi. Jumba hilo lililo jipya kabisa liko katika uwanja wa ekari nane katika Cassidy, British Columbia. Miti mirefu inayodumu ikiwa mibichi-mibichi daima inafanya mazingira ya nyuma yapendeze, hali hori ya kupendeza inatiririka ikipita katika uwanja huo upande wa nyuma wa jengo hilo. Ndani ya uwanja mna jumba lenye viti 900, kafeteria yenye viti 250, eneo la viburudisho, kidimbwi kidogo cha ubatizo chenye vigai vya kukanyaga, na Jumba la Ufalme lenye viti 200 linalotumiwa na makundi ya mahali hapo. Hata wale walioshiriki ujenzi walo wanasema ni vigumu kuamini kwamba lilijengwa na kumalizwa katika siku tisa.
Bila shaka, kabla ya ujenzi huo wa siku tisa, kulikuwa na kazi nyingi ya matayarisho. Jengo lililokuwa katika uwanja huo zamani lilibomolewa na kuondolewa vitu vyenye thamani vilivyokuwamo—wakati wa bubujiko la mvua. Wafanya kazi wa kujitolea walijikaza katika kipindi cha Oktoba chenye mvua na baridi ili wakate vipande vinene vya mwerezi mwekundu wa magharibi ambavyo vikiwa msituni vinakuwa tayari kwa kuezekea. Ilikuwa lazima matayarisho yafanywe mapema kuhusu mahali pa kupitishia mabomba ya maji, vifaa vya kupashia jumba joto, vya kupepea hewa wakati wa joto jingi, vya umeme, na mifumo mingine. Kati ya mambo mengine, uwanja wenyewe ulipaswa kutayarishwa na kuzungushiwa mabamba ya mawe ya futi za mraba 25,000.
Lakini, mwishowe kila kitu kikawa tayari. Siku ya Jumamosi, Agosti 3, saa 2 asubuhi, baada ya kufikiria andiko moja la Biblia, wafanya kazi wa kujitolea wenye nyundo walisimama wakiwa tayari kuyazunguka mabamba ya mawe yaliyozungushwa uwanjani. “Akina ndugu, nyundo na zianze kazi! ” sauti ikapaazwe katika vikuza sauti. Nyundo nyingi zikaanza kusikika zikigonga misumari wakati wenye kujitolea waliokadiriwa kuwa 4,500 walipoanza kazi Wenye kujitolea wengi na jamaa zao walikuwa wa kutoka United States na wengine kutoka mbali sana kufikia Newfoundland, Norway, na Uingereza. Majirani wenye huruma waliruhusu nyanja zao zitumiwe kupigia kambi na kuegesha magari, kisha mahema, wapiga-kambi, magari ya kuchukulia mizigo, na motokaa zikachukua nafasi ya ekari 35 kuuzunguka uwanja huo.
Watazamaji walivutwa sana. Fundi mmoja anayefanya kazi za mikataba alileta wafanya kazi wake waitazame kazi na kuiona roho iliyohusika wakati wa kufanya kazi. Majirani wenye fadhili walichanga mboga kwenye idara ya matayarisho ya chakula, ambayo iliwatayarishia wafanya kazi vyakula kwa ukawaida. Majirani wengine walikuja kusaidia kazi yenyewe. Mwanamume mmoja, alisema hivi baada ya kutembelea mahali hapo: “Hakika naweza kuona kwamba Mungu yu pamoja nanyi.” Sasa mwanamume huyu anafanya maendeleo mazuri katika kujifunza Biblia pamoja na Mashahidi.
Makala moja ya mhariri katika kichapo kinachoitwa Lady Smith Chemainus Chronicle ilieleza hivi: “Hata wewe uwe una imani gani ya kidini, au huna, inakupasa uipokeze kwa Mashahidi wa Yehova 4,500 waliofanya kazi usiku na mchana muda wa juma moja na nusu lililopita kujenga Jumba la Kusanyiko katika Cassidy lenye eneo la futi za mraba 25,000 . . . Kufanya hivyo kwa uchangamfu bila kubishana, mgawanyiko au kujinyakulia utukufu ni alama ya Ukristo wa kweli.”
Jumapili, Agosti 11, saa 12 jioni, mkutano wa kwanza ulifanywa katika Jumba la Kusanyiko lililomalizwa likiwa na uwanja ulilopandwa nyasi vizuri!