Maswali Kutoka kwa Wasomaji
■ Katika Israeli wa kale mzingo wa miaka 49 ulifuatwa na mwaka wa Yubile (mwaka wa 50). Je, Yubile hiyo ilikuwa kivuli cha kipindi kitakachoifuata miaka 49,000 ya ‘juma la uumbaji’ la Mungu?
Kwa sababu tarakimu ya 49 inaonekana katika visa vyote viwili, huenda ikaonekana kama kwamba Yubile ingekuwa kivuli cha wakati utakaoufuata mwisho wa ‘juma la uumbaji’ lenye miaka 49,000. Lakini yaliyotukia wakati wa mwaka wa Yubile ya Israeli yanalingana zaidi na yale yatakayotukia wakati wa utawala wa mileani ya Kristo, ile miaka ya mwisho wa ‘juma la uumbaji.’ wala hayalingani na yale yanayofuata baada ya juma hilo. Fikiria msingi wa kusema hivyo:
Kwanza, Torati ya Musa ilitaka kwamba kila mwaka wa saba uwe sabato kwa ajili ya nchi; mazao hayakupasa kupandwa, kulimwa, wala kuvunwa. Baada ya mwaka wa saba wa Sabato (mwaka wa 49), ulifika mwaka wa pekee wa Yubile, mwaka wa 50. Huo ulikuwa ni wakati wa sabato ambapo nchi ilipasa kupumzika tena. Jambo la maana zaidi ni kwamba, uhuru wa kuachiliwa kwa watu ulitangazwa. Waebrania waliokuwa wamejiuzwa utumwani walipata uhuru wa kutokuwa na madeni na kutokuwa utumwani. Pia, zilirudishiwa nchi yao ya urithi jamaa zile zilizokuwa zimelazimika kuiuza. Kwa hiyo Yubile ulikuwa wakati wa Waisraeli kuachiliwa huru na kurudishwa kwenye hali iliyowafaa.—Mambo ya Walawi 25:1-46.
Pili, kwa kuchunguza utimizo wa unabii wa Biblia na mahali tulipofika katika historia, Mashahidi wa Yehova wameonyesha kwamba ‘siku za uumbaji’ (Mwanzo sura ya 1) zina urefu wa miaka 7,000 kila moja. Imekwisha kufahamiwa kwamba utawala wa Kristo wa miaka 1,000 utaimaliza ‘siku ya pumziko’ la Mungu ya miaka 7,000, ambayo ndiyo ‘siku’ ya mwisho ya ‘juma la uumbaji.’ (Ufunuo 20:6; Mwanzo 2:2, 3) Kwa kutegemea kuwaza huko, ‘juma la uumbaji’ lote lingekuwa na urefu wa miaka 49,000.
Kwa kuona kwamba tarakimu zinafanana, watu wengine wamelinganisha miaka ile 49 ya mzingo wa Yubile na miaka hiyo 49,000 ya ‘juma la uumbaji.’ Kwa kuwaza hivyo, wamefikiri kwamba mwaka wa Yubile (ulio wa 50) unapasa kuwa kivuli cha mambo yatakayokuja baada ya mwisho wa ‘juma la uumbaji.’
Lakini, zingatia akilini kwamba Yubile ulikuwa hasa mwaka wa kufunguliwa na kurudishwa kwa watu kwenye hali iliyowafaa. Sasa, ‘juma’ la uumbaji linahusiana sana-sana na sayari-Dunia na kusitawishwa kwayo. Lakini, kwa habari ya hatua-hatua za kutimizwa kwa kusudi la Mungu kwa ajili ya mwanadamu duniani, dunia yenyewe haikuuzwa katika utumwa na hivyo hahitaji kuwekwa huru. Wanadamu ndio wanaohitaji kuwekwa huru, na wanadamu wamekuwapo, si kwa miaka 49,000, bali kwa karibu miaka 6,000. Biblia inaonyesha kwamba muda fulani baada ya Adamu na Hawa kuumbwa walimwasi Mungu, hivyo wakaingia katika hali ya kutekwa na dhambi, kutokukamilika, na kifo. Kulingana na Warumi 8:20, 21, Yehova Mungu anakusudia kuwaachilia huru watoke katika utumwa huo wanadamu wenye kuamini. Matokeo ni kwamba waabudu wa kweli ‘watawekwa huru na kutolewa katika utumwa wa uharibifu, hata waingie katika uhuru wa utukufu wa watoto wa Mungu.’—Ona pia Warumi 6:23.
Maandiko yanaonyesha kwamba watawekwa huru hivyo wakati wa Utawala wa Mileani wa Kristo anapozitumia juu ya wanadamu faida za dhabihu yake. Kufikia mwisho wa Mileani, wanadamu watakuwa wamekwisha kuinuliwa wakafikia ukamilifu wa kibinadamu, wawe huru kabisa bila dhambi na kifo kilichorithiwa. Baada ya kummaliza hivyo adui wa mwisho (kifo kilichoendelea kurithiwa tangu Adamu) Kristo atamrudishia Baba yake Ufalme mwishoni mwa ‘juma la uumbaji’ la miaka 49,000.—1 Wakorintho 15:24-26.
Kwa hiyo, kuwekwa huru na kurudishwa kulikotokea mwaka wa Yubile katika Israeli wa kale kutapata ulinganifu unaofaa wakati wa Sabato ya mileani kwa kuwaweka huru na kuwarudisha katika hali inayofaa wanadamu wenye kuamini. Jambo hilo litatukia chini ya utawala wa Kristo, “kwa maana Mwana wa Adamu ndiye Bwana wa sabato.”—Mathayo 12:8.