Hatua ya Hekima Kabla ya Maafa
KWA kuwa sasa watoto wa Mary walikuwa wamekua, yeye alikuwa na wakati wa kufanya mambo naye akaamua kupata kazi ya kimwili ya nusu-wakati. Hata hivyo, alipomwambia Enos mume wake, mwanamume huyu alijulisha wazi kwamba hakukuwa na uhitaji afanye hivyo. “Ikiwa niliweza kuandaa riziki kwa ajili yako na watoto, hakika naweza kutunza sisi wawili sasa,” akasema. Badala ya kuacha mke wake afanye kazi ya kimwili, alidokeza kwamba afikirie kwa sala kuwa painia, mpiga mbiu ya Ufalme wa wakati wote.
Ingawa Mary aliona shangwe kushiriki ujumbe wa Ufalme pamoja na jirani zake, alikuwa mwenye haya na alikosa uhakika. Hata hivyo, yeye alitaka kufuata shauri la mume wake. Kwa hiyo, akiwa na hisia za mchanganyiko, alijiandikisha kuwa painia msaidizi katika Aprili 1981.
Upesi Mary alisitawisha upendo kwa kazi ya kuhubiri Ufalme kwa kadiri asiyokuwa ameiona kamwe. Muda si muda, alikuwa akiongoza mafunzo manne ya nyumbani ya Biblia kwa watu wenye kupendezwa. Katika muda wa mwaka mmoja akawa amekuwa painia wa kawaida, akiongoza mafunzo kumi ya Biblia. Christine, Shahidi wa Yehova mwenye watoto wawili wakiwa wangali shuleni, alijiunga na Mary kwa idili ili awe mwenzi wake wa kipainia. Wapya wenye kupendezwa walianza kuhudhuria mikutano kwenye Jumba la Ufalme la kwao, ambako roho nzuri ya upainia ilikuwa ikikua. Na shangwe kubwa kabisa ya Mary ikaja wakati mwana wake mwenyewe, Christopher, alipochagua kufuata kielelezo chake naye pia akawa painia.
Halafu, kwa ghafula, katika 1985 tanzia ikatokea. Mary alizimia. Kutanuka kwa mshipa wa kichwani kulifanya ubongo uvuje damu, na katika muda wa siku tatu Mary mwenye umri wa miaka 45 akafa.
Hata hivyo, wakati wa hiyo miaka minne ya kupainia Mary alikuwa amejenga msimamo mzuri katika jumuiya yake. Maziko yake yalihudhuriwa na watu zaidi ya 300, kutia na majirani wengi. Mmoja wa waliokuwapo alikuwa amekuwa rafiki wa shuleni aliyekuwa amevutwa na imani ya Mary, akataka kujua mengi zaidi juu yayo, na kuomba funzo la Biblia. Huduma ya Mary ilikuwa ingali ikizaa matunda.
“Mimi mwenyewe sasa ni painia msaidizi,” asema Enos, “lakini naona ni laiti ningalijiunga na Mary alipokuwa akipainia. Sikuzote yeye alikuwa akiongea juu ya maono yake na alikuwa mwenye furaha. Kwa uhakika, miaka hiyo michache ilikuwa ndiyo miaka yenye furaha kabisa ya maisha yetu pamoja, lakini sasa tu ndiyo nimethamini ni kwa nini.”
Hakuna mtu awezaye kutabiri ni lini “wakati na tukio lisilotazamiwa” laweza kuleta kifo, kama lilivyofanya kwa ghafula isiyotarajiwa sana katika kisa cha Mary. Hata hivyo, wale wabakio waaminifu wakiwa wapiga mbiu ya Ufalme hujihakikishia kupata utambuzi wenye kupendelewa na Mungu na binadamu pia, hata kwa kukabili maafa.—Mhubiri 9:11; 11:1, 2, NW.
[Picha katika ukurasa wa 31]
Kushiriki katika huduma ni wakati wenye kutumiwa vizuri