Hiyo Haiwezekani!
“NI RAHISI zaidi ngamia kupenya tundu ya sindano, kuliko tajiri kuingia katika ufalme wa Mungu.” (Mathayo 19:24) Yesu Kristo alisema hayo ili kufundisha wanafunzi wake somo. Mtawala tajiri mchanga alikuwa ametoka tu kukataa mwaliko kuwa mfuasi wa Yesu na kushiriki nafasi nyingi za kiroho zilizo nzuri ajabu. Mwanamume huyo alichagua kushikilia mali zake nyingi kuliko kumfuata Mesiya.
Yesu hakuwa akisema kwamba haiwezekani kabisa kwa tajiri kupata uhai wa milele katika mpango wa Ufalme, kwani matajiri fulani walikuja kuwa wafuasi wake. (Mathayo 27:57; Luka 19:2, 9) Hata hivyo, hiyo haiwezekani kwa tajiri yeyote anayependa mali zake zaidi ya mambo ya kiroho. Ni kwa kuja tu kutambua uhitaji wake wa kiroho na kutafuta msaada wa kimungu ndipo mtu huyo aweza kupokea wokovu wa kupewa na Mungu.—Mathayo 5:3; 19:16-26.
Kielezi cha ngamia na tundu ya sindano hakipaswi kuchukuliwa kihalisi. Yesu alikuwa akitumia chuku ili kukazia ugumu unaokabili matajiri wanaojaribu kumpendeza Mungu huku wakidumisha mtindo-maisha wenye utajiri, wa kufuatia vitu vya kimwili.—1 Timotheo 6:17-19.
Wengine husema kwamba tundu ya sindano ilikuwa lango dogo katika ukuta wa jiji ambalo ngamia angeweza kupitia kwa ugumu ikiwa angeondolewa mzigo wake. Lakini neno la Kigiriki rha·phisʹ, linalotafsiriwa “sindano” kwenye Mathayo 19:24 na Marko 10:25, hutokana na kitenzi kinachomaanisha “kushona.” Kwenye Luka 18:25 neno be·loʹne huonyesha sindano ya kushonea, na hapo New World Translation husomwa hivi: “Ni rahisi zaidi, kwa kweli, kwa ngamia kupitia tundu ya sindano ya kushonea kuliko kwa mwanamume tajiri kuingia ndani ya ufalme wa Mungu.” Mamlaka mbalimbali huunga mkono fasiri hiyo. W. E. Vine husema hivi: “Wazo la kutumia ‘tundu ya sindano’ kuhusu malango madogo laonekana kuwa la ki-siku-hizi; hakuna wonyesho wowote wa kale walo.”—An Expository Dictionary of New Testament Words.
Ngamia mkubwa kujaribu kupitia tundu ya sindano ya kushonea ndogo sana “huonyesha hali ya utiaji chumvi wa Mashariki,” chasema kitabu kimoja cha marejezeo. Na kuhusu wale werevu sana hivi kwamba walionekana kana kwamba walifanya yasiyowezekana, The Babylonian Talmud husema hivi: “Wao huvuta ndovu kupitia tundu ya sindano.” Yesu alitumia chuku ya kawaida sana na utofautisho wenye kuonekana wazi sana kukazia jambo lisilowezekana. Haiwezekani kwa ngamia, au ndovu, kupitia tundu ya sindano ya kushonea. Hata hivyo, kwa msaada wa kimungu, tajiri anaweza kuacha maoni ya kufuatia vitu vya kimwili na kutafuta kikweli uhai wa milele. Ni vivyo hivyo kwa wote wenye tamaa ya kuhisiwa moyoni ya kujifunza na kufanya mapenzi ya Mungu Aliye Juu Zaidi, Yehova.