Upendo wa Kikristo Wenye Msingi wa Upendo wa Yehova
“Amri mpya nawapa, Mpendane. Kama vile nilivyowapenda ninyi, nanyi mpendane vivyo hivyo. Hivyo watu wote watatambua ya kuwa ninyi mmekuwa wanafunzi wangu, mkiwa na upendo ninyi kwa ninyi.”—Yohana 13:34, 35.
1, 2. (a) Kwa sababu gani mtume Yohana alistahili sana kuandika habari za upendo? (b) “Amri mpya” ambayo Yesu aliwapa wanafunzi wake ilikuwa nini?
MWANDIKAJI wa Biblia Yohana, mmoja wa mitume kumi na wawili wa Yesu Kristo, alisema mengi juu ya sifa ya Kikristo ya upendo. Yeye alikuwa mwana wa Zebedayo na Salome, na katika masimulizi yake ya Injili anatumia maneno “-penda” na “-pendwa” zaidi ya vile yanatumiwa katika yale masimulizi mengine matatu ya Injili yakiunganishwa pamoja. Bila shaka, Yohana alikuwa akiandika juu ya upendo wa agápē hasa, yaani, upendo wenye kuongozwa na kanuni.
2 Yohana alikuwa katika hali nzuri ya kuweza kuzungumza juu ya upendo kwa sababu inaelekea yeye alipendwa na kuonyeshwa shauku ya pekee na Yesu. Yohana alikuwa mmoja wa wale mitume watatu walioshirikiana na Yesu kwa usiri katika huduma yake yote ya hadharani. Yeye ndiye aliyeegemea karibu na Yesu penye siku kuu ya mwisho ya Kupitwa, wakati ambapo Chakula cha Bwana cha Jioni kilianzishwa. Alijulikana kama ‘mwanafunzi ambaye Yesu alimpenda.’ (Yohana 13:23; 19:25-27; 21:7, 20) Kwa hiyo mtume Yohana alikuwa na msingi mzuri wa kupata habari za kuandika juu ya sifa hii ya Kikristo ya upendo, naye ndiye aliyeyaandika maneno ya Yesu alipowaeleza wanafunzi wake juu ya ‘amri mpya’: “Amri mpya nawapa, Mpendane. Kama vile nilivyowapenda ninyi, nanyi mpendane vivyo hivyo. Hivyo watu wote watatambua ya kuwa ninyi mmekuwa wanafunzi wangu, mkiwa na upendo ninyi kwa ninyi.”—Yohana 13:34, 35.
3. Je! Wayahudi waliokuwa chini ya torati ya Musa waliagizwa kupendana? Toa sababu za jibu lako.
3 Hapa Yesu alionyesha kwamba upendo wa kweli ndio ungekuwa alama yenye kutambulisha wanafunzi wake wa kweli. Lakini kwa sababu gani Yesu alisema hiyo ingekuwa “amri mpya”? Yesu alikuwa akisema na wanafunzi wake, na wote walikuwa wa taifa la Kiyahudi. Chini ya torati ya Musa Wayahudi walipaswa kupenda mwanadamu mwenzao kama nafsi zao wenyewe. Kwa mfano, katika Mambo ya Walawi 19:18 Torati ilisema hivi: “Usifanye kisasi, wala kuwa na kinyongo juu ya wana wa watu wako; bali umpende jirani yako kama nafsi yako.” Kwa kweli, katika kufundisha kwake, Yesu alielekeza fikira kwenye amri hiyo iliyokuwa katika Torati aliposema hivi: “[Amri] ya pili yafanana nayo, nayo ni hii, Mpende jirani yako kama nafsi yako.”—Mt. 22:39.
4. Ni upendo wa namna gani alioutaja Yesu katika Yohana 13:34, 35, na upendo huo ulionyeshwaje wazi?
4 Torati ya Musa ilitaka watu wapende jirani, haikutaka wawe na upendo wa kujitoa wenye kuongozwa na kanuni. Walakini, alipokuwa akiwapa wafuasi wake “amri mpya,” Yesu alikuwa akimaanisha kwamba iliwapasa kutambuliwa kwa upendo wa kujitoa, kwa maana aliendelea kusema hivi: “Kama vile nilivyowapenda ninyi, nanyi mpendane vivyo hivyo.” Upendo wa Yesu ulikuwa upendo wa kujitoa na wenye kuongozwa na kanuni, yaani, upendo wa agápē. Alikuwa na nia ya kufikia hata hatua ya kutoa uhai wake mwenyewe kwa ajili ya wanafunzi wake. Alitumia miaka ya huduma yake ya hadharani akifanyia wanadamu wenzake mema, hasa kwa kufundisha watu na kuwasaidia kiroho. Kwa hiyo imewapasa wanafunzi wake wafanye vivyo hivyo, si kusita-sita wakingoja nafasi itokee ikionyesha wanapaswa kufanya mema kwa wanadamu wenzao. Bali, imewapasa Wakristo wachukue hatua ya kwanza na kujibidiisha wafanyie wanadamu wenzao mema, hasa wakifuata mfano wa Yesu kwa kufundisha na kuhubiri, kwa njia hiyo wakijitahidi kuletea wengine faida na afya ya kiroho. Lakini; juu ya yote, wanafunzi wa Yesu walipaswa kuwa na upendo wao kwa wao. Kwa hiyo iliwapasa wawe wenye kutokeza kwa kuonyeshana upendo. Lilipaswa kuwa jambo lenye kuwatofautisha kwa vyepesi na walimwengu kwa ujumla.
5, 6. (a) Yohana anazungumza nini katika barua yake ya kwanza? (b) Yohana anamtambulishaje Mungu na upendo?
5 Mtume Yohana aliithamini sana alama hii yenye kutambulisha ya Ukristo hata akaitilia mkazo, si katika masimulizi yake ya Injili tu, bali pia katika barua zake. Kwa mfano, barua ya kwanza ya Yohana inaonyesha kweli kwamba Yohana alipenda ndugu zake wa Kikristo. Iliandikwa ili kuwalinda na mafundisho ya uongo ya wapinga Kristo wa siku zake. Katika barua yote Yohana anakazia upendo wa Mungu, akionyesha vile inavyowapasa Wakristo kuiiga sifa hii ya kutokeza ya Mungu Mwenye Nguvu Zote, Yehova.
6 Katika Yohana wa Kwanza sura ya 4, mstari wa 8, Yohana anamtambulisha Mungu na sifa hii ya upendo, akisema: “Yeye asiyependa, hakumjua Mungu, kwa maana Mungu ni upendo.” Kwa hiyo hapa Yohana anaonyesha Yehova ndiye Chanzo cha upendo, Mungu wa upendo kweli kweli. Bila shaka, hapa Yohana hamaanishi kwamba Mungu ni sifa ya kuwazika tu. Sivyo kabisa. Yohana alijua kwamba Mungu ni mtu, na kwa kuwa Yehova ni mtu ana sifa nyingi, nao upendo ndiyo sifa kubwa ya zote.
7. Wanafunzi wa Yesu wanatambuliwaje leo?
7 Mwana wa Mungu, Yesu Kristo, alitokeza sana pia kwa kuwa na sifa hii ya upendo, upendo wa kujitoa, akaonyesha kwamba hiyo ndiyo ingekuwa alama ya kutambulisha wanafunzi wake wa kweli. Kwa hiyo, leo mashahidi wa Yehova wa Kikristo wanaoishi katika sehemu zote za dunia ni waabudu wa Yehova, Mungu wa upendo, nao ni wanafunzi au wafuasi wa nyayo za Yesu, Mwanawe mwenye upendo. Kwa hiyo leo mashahidi wa Yehova wa Kikristo lazima waonyeshe upendo wa kweli wa kujitoa katika maisha zao za kila siku ili wapate kutambuliwa kuwa Wakristo wa kweli. Kwa sababu hiyo Yohana anapendekeza Mkristo amwige Yehova Mungu kwa upendo, akisema hivi: “Sisi twapenda kwa maana yeye [Mungu] alitupenda sisi kwanza.”—1 Yohana 4:19.
WONYESHO MKUU ZAIOI YA WOTE WA UPENDO WA YEHOVA
8. Watu wengi wangeonyesha nini kuwa ushuhuda wa kwamba Yehova “alitupenda sisi kwanza”?
8 Ni kwa njia gani Yehova ‘ametupenda sisi kwanza’? Ametufanyia nini sisi viumbe vya kibinadamu kuonyesha upendo wake, kuonyesha kwamba anapendezwa nasi bila choyo? Kuna ushuhuda mwingi mbalimbali wa kuonyesha Yehova anatupenda. Lakini tunaweza kusema wonyesho mkuu zaidi ya wote wa upendo wa Yehova ni nini? Wengi wangefikiria uzima mara moja, kwa sababu sisi tunaishi kwa sababu ya Yehova tu, Chanzo cha uzima wote. (Zab. 36:9) Lakini Yehova amevipa viumbe vingine pia uzima hapa duniani, sivyo? Tunastaajabia wanyama wengi wa namna namna, samaki na viumbe vingine vya baharini vilivyo hai, ndege na wadudu; na kwa wazi viumbe vyote hivyo vinafurahia kuwa hai ingawa havimfahamu aliye Chanzo cha uzima, Yehova. Kwa hiyo kwa kweli wonyesho mkuu zaidi ya wote wa upendo wa Yehova ungekuwa si zawadi ya uzima wenyewe tu.
9. Yehova ‘ametupendaje sisi kwanza,’ naye Yohana anahakikishaje hilo katika 1 Yohana 4:10?
9 Yehova amepangia wanadamu uzima bora kuliko tulio nao sasa, yaani uwezekano wa kupata uzima wa milele kwa wale wanaompenda na kumtumikia Yeye. Lakini Yehova amefanyaje jambo hilo? Ni kwa kumtoa Mwanawe mzaliwa wa pekee aliye mwaminifu, Yesu Kristo, kama zawadi ya upendo. Wanadamu wenye dhambi hawakuuomba mpango huo wenye upendo ili wapate kuishi milele, bali Yehova ndiye aliyechukua hatua ya kwanza kutoa zawadi hiyo nzuri sana, kuonyesha upendo wake. Kwa hiyo Yohana anaandika hivi: “Hili ndilo pendo, si kwamba sisi tulimpenda Mungu, bali kwamba yeye alitupenda sisi, akamtuma Mwanawe kuwa kipatanisho kwa dhambi zetu.”—1 Yohana 4:10.
10. (a) Paulo anahakikishaje wonyesho huu wa upendo wa Mungu? (b) Je! Mungu alichukua hatua hiyo haraka haraka tu hila ya kufikiria matokeo vizuri?
10 Mtume Paulo anahakikisha jambo hili, akionyesha kwamba Yehova anatupendekezea upendo wake mwenyewe kupitia kwa zawadi hiyo yenye upendo ya Mwanawe. Katika Warumi 5:7, 8, Paulo aliandika hivi: “Kwa kuwa ni shida mtu kufa kwa ajili ya mtu mwenye haki; lakini yawezekana mtu kuthubutu kufa kwa ajili ya mtu aliye mwema. Bali Mungu aonyesha pendo lake yeye mwenyewe kwetu sisi, kwa kuwa Kristo alikufa kwa ajili yetu, tulipokuwa tungali wenye dhambi.” Zawadi hiyo yenye upendo haikutolewa haraka haraka tu bila ya matokeo kufikiriwa vizuri, bali lilikuwa jambo alilokuwa amekusudia Yehova karne nyingi mapema wakati wa kuwahukumu Adamu na Hawa huko nyuma katika Edeni. (Mwa. 3:15) Kweli, lazima tuseme kwamba Yehova ndiye Chanzo cha upendo, na kama vile alivyoandika Yohana, yeye “alitupenda sisi kwanza,” kwa njia hiyo akapendekeza upendo kama sifa kubwa zaidi inayopaswa kupatikana kati ya waabudu wake.
USHUHUDA WENYE KUONEKANA WA UPENDO WA YEHOVA
11. Ushuhuda mwingine wa upendo wa Yehova tunaofurahia kila siku ni nini?
11 Zaidi ya zawadi yenye upendo ya Mwanawe iliyotolewa ili kuokoa na kukomboa wanadamu, na zaidi ya uzima wenyewe pamoja na uwezekano wa uzima wenyewe kuwa wa milele, uko ushuhuda mwingine mwingi wa upendo wa Yehova katika uumbaji wote. Bila shaka Yehova ameonyesha wazi upendo wake kwa kufanya maisha yawe ya kupendeza na kufurahika sana. Kwa mfano, kila siku tunafurahia kula, kwa kawaida mara kadha kwa siku. Hilo ni jambo la kuchosha? Yehova ametupa vyakula vingi vya kupendeza navyo ni vya namna namna zilizo nzuri sana. Vyakula vyetu vina rangi nyingi na maumbo ya kupendeza, na vilevile ladha ladha na harufu harufu zisizoelezeka. Katika nchi zenye utajiri tunaweza kufurahia wakaa zetu za kula kwa siku nyingi sana bila kula ‘namna ile ile ya chakula mara mbili. Lazima tule kila siku ndiyo tuishi, lakini lo! Yehova amefanya kula kwetu kwenye kupendeza na kufurahika kwa upendo ulioje!
12, 13. Kazi za uumbaji wa Yehova, za kimbinguni na za kidunia, zinashuhudiaje kwamba anapenda wanadamu?
12 Vilevile tunaona ushuhuda wa upendo wa Yehova katika kazi zake za uumbaji, uumbaji wenye kuonekana. (Rum. 1:20) Hata mwanadamu awe anaishi wapi katika dunia hii anaona uzuri wake, uwe katika misitu mikubwa ya sehemu zenye joto jingi au katika milima yenye fahari iliyofunikwa na theluji katika maeneo mbalimbali katika dunia. Halafu ziko bahari zenye maji safi ya rangi ya samawati na pwani zenye mchanga mweupe za sehemu zenye joto jingi na la kiasi, na vilevile nyanda kuu zenye kujawa na nafaka nyingi zilizo nzuri sana. Au yako maziwa ya samawati yenye vina virefu na misitu mizuri ya kijani ya misunobari. Naam, hata majangwa yasiyozaa yana uzuri wa pekee. Na je! hatufurahii kuziona mbingu zenye nyota katika usiku usio na mawingu? Si kwamba nyota ni zenye utukufu tu zinapotazamwa, bali pia zinaongoza mwanadamu katika safari zake. Kwa hiyo zinafaa sana vilevile. Ni ushuhuda mwingine wa upendo wa Yehova katika uumbaji.
13 Katika sehemu zote za dunia tunaona ushuhuda mwingine wa upendo wa Yehova kwa wanadamu, kama vile katika namna namna za wanyama na ndege wengi wenye uzuri na rangi za kumfurahisha mwanadamu, na vilevile wenye urafiki naye. Lo! Yehova ameumba viumbe vya namna nyingi sana ili afaidi na kufurahisha wanadamu hapa duniani! Watu wengine wanatumia maisha yao yote wakichunguza ushuhuda huo wa ufundi wa Yehova wenye upendo.
14. (a) Ni kwa njia gani Yehova ameumba mwanadamu akiwa na cheo cha juu kuliko wanyama? (b) Uwezo wa kuthamini mambo ya kiroho unawezesha wanadamu kufanya nini kupatana na Yohana 4:24?
14 La maana hata zaidi ni kwamba, Yehova ameumba wanadamu wakiwa na cheo cha juu kuliko wanyama. Ameonyesha upendo wake kwa kumfanya mwanadamu kwa sura na mfano wake mwenyewe. (Mwa. 1:26, 27) Hivyo, sisi tukiwa viumbe vyenye mfano wa Yehova, tunayo akili ya kupenda, na vilevile tunayo akili ya kuthamini mambo ya kiroho. Tunao uwezo wa kumjua, kumpenda na kumwabudu Muumba wetu mwenye upendo. Mnyama hawezi kufanya hivyo. Huenda mtu akawa na mbwa-rafiki au paka-rafiki na huenda akawa anasema na rafiki huyo, lakini hatumwoni wakati wo wote akizungumza mambo ya kiroho na mbwa au paka wake, sivyo? Mnyama mwenye cheo cha chini hana akili ya kuthamini mambo ya kiroho. Lakini wanadamu wanaweza na imewapasa kufanya hivyo. Hatumwoni Yehova Mungu, lakini tunaona ushuhuda mwingi sana wa upendo wake tunapotazama vyote alivyoumba. Nasi tunapopata kumjua, tunaweza kumpenda na kumwabudu. Kama vile Yesu alivyosema, tunaweza kumwabudu “katika roho na kweli.” (Yohana 4:24) Naam, Yehova ametendea wanadamu mengi sana kwa sababu anawapenda. Kwa hiyo, bila shaka tutakubaliana na aliyoandika Yohana, kwamba “sisi twapenda kwa maana yeye alitupenda sisi kwanza.”—1 Yohana 4:19.
15. Yesu anahakikishaje kwamba Yehova ni Baba mwenye upendo kwa watumishi wake?
15 Tunaporudia kujikumbusha ushuhuda wa upendo wa Yehova tunaweza kufahamu kwamba yeye ni Baba mwenye kutupenda sote tuliopo duniani. Kama Baba mwenye upendo anachagua mambo yanayoweza kufaidi watoto wake. Anataka kuona tukiwa na hali njema na anatutimizia mahitaji yetu. Yesu alitufundisha tusisumbuke kupita kiasi juu ya tutakachokula au kunywa au tutakachovaa, ikiwa kweli tunatanguliza ibada ya Yehova katika maisha zetu. Akionyesha namna Baba yetu alivyo mwenye upendo, Yesu alisema hivi: “Msisumbukie maisha yenu, mle nini au mnywe nini; wala miili yenu, mvae nini. . . . Kwa sababu Baba yenu wa mbinguni anajua ya kuwa mnahitaji hayo yote. Bali utafuteni kwanza ufalme wake, na haki yake; na hayo yote mtazidishiwa.” (Mt. 6:25, 32, 33) Kwa hiyo kama Baba mwenye upendo, Yehova anapendezwa na watoto wake, nasi tukimtumikia na kufanya mapenzi yake, yeye atahakikisha kwamba tunapata riziki yetu.
16. Sala zetu kwa Yehova zimepaswa zionyeshe tuna uhusiano gani naye?
16 Kwa hiyo, imewapasa watumishi wa Mungu leo wawe na uhusiano wa karibu na Yehova, wamtambue, si kama mungu tu, bali kama Baba, Baba mwenye upendo. Kwa hiyo uhusiano wetu naye umepaswa kuwa kama wa mtoto na baba yake. Hivyo imetupasa kujaribu kupashana habari na Baba yetu kwa kawaida na kumweleza mahitaji na tamaa zetu na magumu yetu, na vilevile kumshukuru kwa baraka nyingi anazotoa. Paulo aliandika hivi: “Msijisumbue kwa neno lo lote; bali katika kila neno kwa kusali na kuomba, pamoja na kushukuru, haja zenu na zijulikane na Mungu.” (Flp. 4:6) Alipokuwa akifundisha wanafunzi wake kusali, Yesu hakuwafundisha kumwita Yehova “Mungu wetu” bali kumwita “Baba yetu” aliye katika mbingu. (Mt. 6:9) Kwa hiyo ni vizuri kuendelea kuwa na uhusiano wa karibu na wa kipekee pamoja na Yehova ambaye ni Baba mwenye upendo na kupashana habari naye kwa kawaida.
UTAWALA WA MUNGU WA UPENDO—TOFAUTI SANA NA UTAWALA MBAYA WA IBILISI WA CHUK!
17. (a) Upendo wa Mkristo umepaswa ufike wapi? (b) Yehova ameonyesha kanuni gani katika habari hii?
17 Yehova anapenda viumbe vyake sana hata kufikia hatua ya kupenda wale wasiompenda yeye. Kumbuka kwamba Yesu alifundisha wafuasi wake hivi: “Endeleeni kupenda adui zenu.” (Mt. 5:44, NW) Lakini Yesu angeweza kufundisha hivyo akiwa na msingi gani? Msingi ulikuwa ndio mfano mwema wa Baba yake mwenye upendo, kwa maana Mathayo 5:45 inasema hivi: “Ili mpate kuwa wana wa Baba yenu aliye mbinguni; maana yeye huwaangazia jua lake waovu na wema, huwanyeshea mvua wenye haki na wasio haki.” Kwa hiyo Yehova anabariki wote kwa kuwapa mwangaza wa jua, mvua na vitu vinavyohitajiwa kuendeleza uhai. Hata wale wasiomtumikia au wasiomjua wanapokea baraka hizo. Tena, tumekwisha jifunza namna Yehova alivyoweka kanuni ya kupenda adui zetu kwa kumtuma Mwanawe duniani ili akomboe wanadamu wote wakiwa wenye dhambi na kutenganishwa na Mungu. (Rum. 5:8-10) Kwa hiyo Yesu angeweza kufundisha kwamba imetupasa kupenda hata adui zetu, akiwa na msingi wa kanuni iliyokuwa imekwisha wekwa na Yehova, Baba yake mwenye upendo. Kwa kweli upendo wa Yehova unaonyeshwa kwa wote nao unapita mambo mengine yote. Yeye ni mfano mzuri namna gani akiwa ndiye Chanzo cha upendo wenye kuongozwa na kanuni (agápē)!
18. (a) Ni kwa msingi gani Yehova anatawala akiwa Mkuu Zaidi Kuliko Wote na akiwa Mwenye Enzi Kuu? (b) Ni kwa njia gani nzuri Zaburi 84:10, 11 inavyoonyesha mawazo ya ndani ya wale wanaounga mkono enzi kuu ya Yehova?
18 Akiwa ndiye Mkuu Zaidi Kuliko Wote na Mwenye Enzi Kuu wa ulimwengu wote, Yehova hatawali kwa kuogopesha watu isivyofaa wala kwa kuwachukia. Yeye ni Mungu mwenye upendo, kama alivyoandika Yohana, na kwa hiyo msingi wa enzi kuu yake ni upendo. Kwa hiyo wale wanaomtumikia Yehova na kuunga mkono enzi kuu yake wanafanya hivyo kwa sababu wanampenda sana sana na kumheshimu, si kwa sababu ya kumwogopa kiutumwa. Wale wanaounga mkono enzi ya Yehova wanautambua upendo wake, hekima yake, uwezo wake na hukumu yake ya haki iliyo bora, nao wanachagua kipekee kumwabudu na kumtumikia, kwa njia hiyo wakiiunga mkono enzi kuu yake. Mawazo yao ya ndani yanaelezwa vizuri kwa ufupi na mtunga zaburi ambaye alisema hivi: “Hakika siku moja katika nyua zako ni bora kuliko siku elfu [kwingineko]. Kwa kuwa [Yehova], Mungu, ni jua na ngao, [Yehova] atatoa neema na utukufu. Hatawanyima kitu chema hao waendao kwa ukamilifu.”—Zab. 84:10, 11.
19. (a) Alipokuwa akimtuma mwanawe mzaliwa wa kwanza duniani, Yehova alikuwa akionyeshaje wanadamu upendo wake? (b) Nalo jambo hilo lilimhakikishaje Shetani kuwa mwongo?
19 Bila shaka, Shetani amepinga utawala wa Yehova wa upendo akajiondoa katika upendo wa Yehova, kwa sababu hiyo akasema kwamba Yehova ni Mungu asiye na upendo. Lakini shtaka hilo la uongo halifanyi Mungu asipende viumbe vyake. Wengi wamemfuata Shetani kwa kuondoka kwa Yehova, lakini hiyo haizuii Yehova asionyeshe upendo wala haizuii wengine wasiunge mkono enzi kuu ya Yehova kwa kuonyesha wanampenda. Kwa upendo Yehova Mungu alimtuma Mwanawe kutoka mbinguni akashuhudie jina la Mungu kwa wanaompenda Yeye na kuwahakikishia kwamba Yeye anawatumaini. Mwanawe Yesu alihakikisha kwamba Baba yake alimtumaini yeye ilivyofaa. Alihakikisha pia alimpenda Baba yake na wanadamu kufikia hatua ya kutoa uhai wake na kufa kama mvunja sheria wa kikawaida juu ya mti wa mateso. Kupitia kwa wonyesho huo wa upendo wa Mungu na Mwanawe, wanadamu wanaweza kutumaini kukombolewa na dhambi na mauti na kupata uzima wa milele. Ni kama vile Yohana 3:16 inavyosema: “Kwa maana jinsi hii Mungu aliupenda ulimwengu, hata akamtoa Mwanawe pekee, ili kila mtu amwaminiye asipotee, bali awe na uzima wa milele.”
TENGENEZO LENYE KUONYESHA UPENDO WA MUNGU
20. Ni tengenezo gani jipya lililoanzishwa na Yesu, na ni nini kilichounganisha tengenezo hilo?
20 Kwa sababu ya huduma ya Yesu yenye bidii duniani aliyoifanya kwa miaka mitatu na nusu, tengenezo jipya lilianzwa duniani, tengenezo la wahubiri na waalimu wanaofuata mfano wa Yesu. Hivyo, kupitia kwa mazoezi ya Yesu yenye upendo na mafaa, wanaume wa vyeo vya chini na elimu ya chini kama mitume Petro na Yohana walipata kuwa wasemaji na waalimu wenye nguvu na wenye kufaa. (Matendo 4:4, 13) Kundi lenye umoja la watu wa mbari na makabila na mataifa yote liliungana kumwabudu Yehova Mungu kwa sababu ya kumpenda, bila shaka wakitambua kwamba Yehova “alitupenda sisi kwanza.” (1 Yohana 4:19) Wakristo wa kwanza walikuwa wameunganishwa pamoja na upendo wa agápē, upendo wenye msingi wa kanuni za kimungu na wenye kuongozwa nazo. Ni kama vile alivyosema Paulo: “Upendo . . . ndio kifungo cha ukamilifu.”—Kol. 3:14.
21. Ni akina nani leo walio waabudu wa kweli wa Yehova, nao wanajitambulishaje kuwa hivyo?
21 Tengenezo hilo la waabudu wa Kikristo wa Mungu mwenye upendo Yehova lingali liko leo katika sehemu zote za dunia. Limejitenga na ulimwengu usio na upendo, kama Yesu alivyosema imewapasa wafuasi wake wafanye. Kwa hiyo yeye alipokuwa akisali kwa Yehova, alisema hivi: “Mimi siombi kwamba uwatoe katika ulimwengu; bali uwalinde na yule mwovu. Wao si wa ulimwengu, kama mimi nisivyo wa ulimwengu.” (Yohana 17:15, 16) Leo tengenezo hilo linajulikana kama mashahidi wa Kikristo wa Yehova, nao wana sifa ulimwenguni pote ya kupendana na kupenda wanadamu wenzao. Lo! namna ilivyo vizuri kwa wale walio sehemu ya tengenezo hilo leo kumwabudu na kumtumikia Yehova wakiwa watu wenye umoja, watu mmoja mmoja wa mbari zote na mataifa wakiwa wameunganishwa pamoja na “kifungo cha ukamilifu”—upendo wa kimungu! Naam, mashahidi wa Yehova wa Kikristo leo wanayo alama yenye kuwatofautisha, sifa ya kuwa wenye kutokeza katika upendo wao kwa Mungu Yehova na kati ya wao kwa wao. Kwa njia hiyo wanajihakikisha kuwa waigaji wa Mungu wao mwenye upendo na wanafunzi wa kweli wa Mwanawe, Yesu Kristo.—Efe. 5:1; Yohana 13:34, 35.
[Picha katika ukurasa wa 105]
Uzima wa milele katika ukamilifu unawezekana kwa sababu ya Mungu kumtoa Mwanawe kama zawadi
[Picha katika ukurasa wa 107]
Uumbaji wote uonekanao unashuhudia upendo wa Muumba wetu
Kwa sababu ya upendo, Yehova alimfanya mwanadamu akiwa na akili ya kuthamini mambo ya kiroho