Jumapili, Oktoba 19
Mshushe nyavu zenu, mvue samaki.—Luka 5:4.
Yesu alimhakikishia mtume Petro kwamba Yehova angemtegemeza. Yesu aliyefufuliwa alimsaidia Petro na mitume wenzake kuvua tena samaki kimuujiza. (Yoh. 21:4-6) Bila shaka, muujiza huo ulimhakikishia Petro kwamba Yehova angemwandalia mahitaji yake ya kimwili. Labda mtume huyo alikumbuka maneno ya Yesu kwamba Yehova angewaandalia wale ambao wanaendelea “kuutafuta kwanza Ufalme.” (Mt. 6:33) Hilo lilimsaidia Petro kutanguliza huduma maishani badala ya kazi ya kuvua samaki. Alitoa ushahidi kwa ujasiri siku ya Pentekoste mwaka wa 33 W.K., na kuwasaidia maelfu kukubali habari njema. (Mdo. 2:14, 37-41) Baadaye, aliwasaidia Wasamaria na Watu wa Mataifa kuwa Wakristo. (Mdo. 8:14-17; 10:44-48) Bila shaka, Yehova alimtumia Petro kwa njia kubwa kuwasaidia watu wa kila namna wajiunge na kutaniko. w23.09 20 ¶1; 23 ¶11
Jumatatu, Oktoba 20
Msiponiambia ndoto yangu na kunieleza maana yake, mtakatwa vipandevipande.—Dan. 2:5.
Karibu miaka miwili baada ya Wababiloni kuharibu jiji la Yerusalemu, Mfalme Nebukadneza wa Babiloni aliota ndoto yenye kutisha kuhusu sanamu kubwa sana. Alitishia kuwaua wanaume wake wote wenye hekima, kutia ndani Danieli, ikiwa hawangemwambia ndoto aliyoota na pia ufafanuzi wake. (Dan. 2:3-5) Danieli alihitaji kutenda haraka; la sivyo, watu wengi wangekufa. Alienda “na kumwomba mfalme ampe muda ili amweleze maana ya ndoto yake.” (Dan. 2:16) Hilo lilihitaji ujasiri na imani. Biblia haina habari zozote zinazoonyesha kwamba Danieli alikuwa amewahi kufafanua ndoto kabla ya wakati huo. Aliwaomba rafiki zake “wasali ili Mungu wa mbinguni awaonyeshe rehema na kuwajulisha siri hiyo.” (Dan. 2:18) Yehova alijibu sala hizo. Kwa msaada wa Mungu, Danieli alifafanua ndoto ya Nebukadneza. Uhai wa Danieli na rafiki zake uliokolewa. w23.08 3 ¶4
Jumanne, Oktoba 21
Yule atakayevumilia mpaka mwisho ndiye atakayeokolewa.—Mt. 24:13.
Fikiria manufaa ya kuonyesha subira. Tunapoonyesha subira, tunakuwa wenye furaha na watulivu zaidi. Hivyo, subira inaweza kutusaidia tuwe na hali nzuri kiakili na kimwili. Tunapowaonyesha wengine subira, tunakuwa na uhusiano mzuri zaidi pamoja nao. Kutaniko letu linakuwa na umoja zaidi. Ikiwa mtu fulani atatuudhi, hatutakasirika upesi na hivyo tutazuia hali isiwe mbaya zaidi. (Zab. 37:8, maelezo ya chini; Met. 14:29) Lakini jambo muhimu zaidi, tunamwiga Baba yetu wa mbinguni na kumkaribia hata zaidi. Subira ni sifa yenye kupendeza na ambayo inatunufaisha sana! Ingawa huenda isiwe rahisi sikuzote kuonyesha subira, kwa msaada wa Yehova tunaweza kuendelea kusitawisha sifa hiyo. Na tunapoendelea kuungoja ulimwengu mpya kwa subira, tunaweza kuwa na uhakika kwamba “jicho la Yehova linawalinda wale wanaomwogopa, wale wanaongojea upendo wake mshikamanifu.” (Zab. 33:18) Acheni sisi sote tuazimie kuendelea kujivika subira. w23.08 22 ¶7; 25 ¶16-17