Ijumaa, Septemba 19
Tuendelee kupendana.—1 Yoh. 4:7.
Sote tunataka ‘kuendelea kupendana.’ Hata hivyo, ni muhimu kukumbuka kwamba Yesu alionya kuwa “upendo wa wengi [ungepoa].” (Mt. 24:12) Yesu hakumaanisha kwamba wanafunzi wake wengi wangeacha kupendana. Hata hivyo, tunapaswa kuwa makini ili tusiathiriwe na mtazamo wa ulimwengu wa kutopendana. Tukiwa na wazo hilo akilini, acheni tujiulize swali hili muhimu: Je, kuna njia yoyote ya kupima ikiwa upendo wetu kwa ndugu zetu una nguvu au ni dhaifu? Njia moja ya kupima ikiwa upendo wetu una nguvu au ni dhaifu ni kwa kuchunguza jinsi tunavyoshughulikia hali fulani maishani. (2 Kor. 8:8) Mojawapo ya hali hizo inatajwa na mtume Petro, alisema hivi: “Zaidi ya mambo yote, pendaneni sana, kwa sababu upendo hufunika dhambi nyingi.” (1 Pet. 4:8) Hivyo, udhaifu na kutokamilika kwa wengine kunaweza kujaribu upendo wetu. w23.11 10-11 ¶12-13
Jumamosi, Septemba 20
Mpendane.—Yoh. 13:34.
Hatuwezi kutii amri ya Yesu kuhusu kupendana ikiwa tunawaonyesha upendo baadhi ya watu kutanikoni na kuwabagua wengine. Ukweli ni kwamba huenda tukawa na uhusiano wa karibu zaidi na baadhi ya watu kama ilivyokuwa kwa Yesu. (Yoh. 13:23; 20:2) Lakini mtume Petro anatuonyesha kwamba tunapaswa kujitahidi kuonyesha “upendo wa kindugu”—uhusiano mchangamfu kama wa familia—kuwaelekea ndugu na dada zetu wote. (1 Pet. 2:17) Petro alituhimiza ‘tupendane sana kutoka moyoni.’ (1 Pet. 1:22) Katika muktadha huo, kupendana “sana” kunatia ndani kumpenda mtu hata kama ni vigumu kumwonyesha upendo. Namna gani ikiwa ndugu anatukasirisha au anatuumiza kwa njia fulani? Huenda tukashawishiwa kulipiza kisasi badala ya kuonyesha upendo. Ingawa hivyo, Petro alijifunza kutoka kwa Yesu kwamba Mungu hafurahishwi na watu wanaolipiza kisasi. (Yoh. 18:10, 11) Petro aliandika hivi: “Msilipe ubaya kwa ubaya au matukano kwa matukano. Badala yake, lipeni kwa baraka.” (1 Pet. 3:9) Unapowaonyesha wengine upendo mwingi, utachochewa kuwatendea kwa fadhili na ufikirio. w23.09 28-29 ¶9-11
Jumapili, Septemba 21
Vilevile wanawake wanapaswa . . . wawe wenye kiasi katika mazoea, na waaminifu katika mambo yote.—1 Tim. 3:11
Tunastaajabishwa na jinsi mtoto anavyokua haraka na kuwa mtu mzima. Inaonekana ni kama watoto wanakua tu bila kufanya jitihada yoyote. Hata hivyo, jitihada inahitajika ili kuwa Mkristo mkomavu. (1 Kor. 13:11; Ebr. 6:1) Ili kufikia lengo hilo, tunahitaji kuwa na uhusiano wa karibu pamoja na Yehova. Pia, tunahitaji roho takatifu ili tusitawishe sifa zinazompendeza Yehova, tuwe na ustadi unaofaa, na tujitayarishe kwa ajili ya majukumu ya wakati ujao. (Met. 1:5) Yehova alimuumba mwanamume na mwanamke. (Mwa. 1:27) Ni wazi kwamba wanaume na wanawake wanatofautiana kimwili, lakini wanatofautiana kwa njia nyingine pia. Kwa mfano, Yehova aliwapatia wanaume na wanawake majukumu hususa, hivyo wanahitaji sifa na ustadi ili waweze kutimiza majukumu yao.—Mwa. 2:18. w23.12 18 ¶1-2