-
Kwa Nini Watoto Hawana Nidhamu?Amkeni!—2015 | Aprili
-
-
HABARI KUU
Kwa Nini Watoto Hawana Nidhamu?
Katika miaka ya hivi karibuni, maisha ya familia katika nchi za Magharibi yamebadilika sana. Zamani watoto walitii mwongozo wa wazazi wao. Leo, katika familia nyingi inaonekana kwamba watoto wanawaongoza wazazi wao. Kwa mfano, fikiria hali zifuatazo zinazoonyesha jinsi hali ilivyo.
Mvulana wa miaka minne yuko dukani pamoja na mama yake, na anachukua kigari cha kuchezea. Mama yake anamkataza kwa kusema: “Si una vifaa vya kutosha vya kuchezea?” Hata hivyo, anatambua kwamba hakupaswa kumwuliza swali hilo. Mvulana anajibu huku akilia “ninataka hiki!” Akijua kwamba mwana wake ana kawaida ya kulipuka kwa hasira, mama huyo anamruhusu achukue.
Msichana mwenye umri wa miaka mitano anakatiza mazungumzo kati ya baba yake na mtu fulani. Anamwambia hivi: “Nimechoka kusubiri, nataka kwenda nyumbani!” Hata kabla baba yake hajamaliza alichokuwa akisema, anainama na kumweleza binti yake hivi kwa sauti ya upole: “Binti yangu mpendwa, subiri tu kwa dakika chache, sawa?”
James mwenye umri wa miaka 12 ameshtakiwa tena kuwa amemfokea mwalimu wake. Baba ya James amemkasirikia sana mwalimu wa James. “Mwalimu huyo amezoea kukusumbua,” anamwambia James. “Nitamshtaki kwenye kamati ya shule!”
Hali hizo ni za kuwaziwa tu, ingawa kwa kweli zinaweza kutokea kihalisi. Zinaonyesha tatizo kubwa katika familia ambazo wazazi huruhusu watoto wajiendeshe bila adabu, hukubaliana na chochote wanachotaka, na hata huwatetea wanapojiendesha kwa njia isiyofaa. Kitabu The Narcissism Epidemic, kinasema hivi: “Limekuwa jambo la kawaida kuona wazazi wakikosa kutumia mamlaka yao kuelekea watoto wao. Miaka michache iliyopita, watoto walijua ni nani alikuwa mwenye mamlaka, nao walitii.”
Ni kweli kwamba wazazi wengi hujitahidi kufundisha watoto wao maadili yanayofaa kwa kuwawekea mfano mzuri na kwa kuwarekebisha kwa njia ya upendo wanapokosea. Hata hivyo, kulingana na kitabu kilichonukuliwa hapo mwanzoni, wazazi wanaotambua faida za kufanya hivyo, wanaonwa “kana kwamba wanapinga tamaduni za kwao.”
Kwa nini mambo yamebadilika hivyo? Kwa nini watoto wamekosa adabu?
Wazazi Walegeza Mamlaka Yao
Inasemekana kwamba wazazi walianza kulegeza mamlaka yao katika miaka ya 1960, wakati watu waliodai kuwa wataalamu walipopendekeza kwamba wazazi hawapaswi kuwawekea watoto wao sheria. Walisema hivi: ‘Mnapaswa kuwa marafiki, wala si wenye mamlaka. Kusifu ni bora kuliko kutia nidhamu. Badala ya kurekebisha makosa yao, tambua wanapofanya mambo mazuri.’ Hivyo, badala ya kuwa na usawaziko kati ya kupongeza na kurekebisha, inaonekana wataalamu walihisi kwamba hisia za watoto zingeumizwa baada ya kutiwa nidhamu na kuwafanya wawachukie wazazi wao watakapokuwa watu wazima.
Baada ya muda, wataalamu walianza kukazia sana umuhimu wa kujiamini. Ni kana kwamba waligundua siri hii mpya ya kuwa mzazi bora: Wasaidie watoto wako wajione kuwa wa maana. Ni kweli kwamba ni muhimu kusaidia watoto wajiamini. Hata hivyo, kampeni hiyo ilipita mipaka kwa kuwa wataalamu waliwaambia wazazi hivi: ‘Msitumie maneno kama vile hapana na vibaya. Endeleeni kuwaambia watoto wenu kwamba wao ni wa pekee na wanaweza kufanya lolote watakalo.’ Ni kana kwamba jambo muhimu zaidi lilikuwa kuwafanya wahisi vizuri badala ya kuwasaidia wawe na tabia nzuri.
Kampeni ya kuwafanya watoto wajihisi kuwa wa maana imewafanya wahisi kwamba watu wengine wanapaswa kuwatumikia
Matokeo ni kwamba, watu fulani wanasema kampeni hiyo iliwafanya watoto wahisi kwamba watu wote wanapaswa kuwatumikia. Kwa sababu ya mtazamo huo, kitabu Generation Me, kinasema kwamba vijana wengi “hawako tayari kukabiliana na matatizo halisi maishani kama vile uchambuzi watakaopata na pindi za kutofanikiwa maishani.” Baba mmoja ananukuliwa katika kitabu hicho akisema hivi: “Ukiwa kazini, hakuna mtu atakayejali ikiwa unajihisi kuwa mtu wa maana. . . . Ikiwa utaandika ripoti mbaya, mwajiri wako hatasema, ‘Ninapendezwa sana na rangi ya karatasi uliyotumia kuandika ripoti hii.’ Kulea watoto kwa njia hii kutawaletea madhara makubwa baadaye.”
Maoni Yanayobadilika-Badilika
Kwa miaka mingi, watu wamekuwa wakibadili maoni yao kuhusu mbinu za kulea watoto. Mwalimu Ronald G. Morrish, aliandika hivi: “Nidhamu hubadilika kila mara kutokana na mabadiliko katika jamii.”a Ni rahisi sana kwa wazazi ‘kurushwa huku na huku kama kwa mawimbi na kuchukuliwa huku na huku na kila upepo wa fundisho,’ kama vile Biblia inavyosema.—Waefeso 4:14.
Ni wazi kwamba mtazamo uliopo wa kutotia nidhamu watoto umekuwa na matokeo mabaya. Hali hiyo imewafanya wazazi kulegeza mamlaka yao na pia kuwaacha watoto bila mwongozo wanaohitaji ili wafanye maamuzi mazuri na kujiamini kikweli maishani.
Je, kuna njia bora zaidi?
a Italiki ni zetu; kutoka katika kitabu Secrets of Discipline: 12 Keys for Raising Responsible Children.
-
-
Nidhamu InayofaaAmkeni!—2015 | Aprili
-
-
HABARI KUU | KWA NINI WATOTO HAWANA NIDHAMU?
Nidhamu Inayofaa
NI WAZI kwamba kulea watoto ni kazi ngumu. Lakini kutomwadhibu mtoto anapokosea huifanya kazi hiyo iwe ngumu zaidi. Kwa nini? Kwa sababu bila kupewa nidhamu (1) watoto hukosa mwongozo, na hilo huwachosha sana wazazi, na (2) wazazi hutoa maagizo bila msimamo na hilo huwafanya watoto wachanganyikiwe.
Kwa upande mwingine, kumtia mtoto nidhamu yenye usawaziko na upendo, kunaweza kumzoeza kufikiri kwa njia nzuri na kuwa na tabia nzuri. Pia, hilo husaidia watoto wajiamini na wawe wenye kutegemeka wanapokuwa watu wazima. Hata hivyo, unaweza kupata wapi mwongozo wenye kutegemeka wa jinsi ya kutia nidhamu watoto wako?
Umuhimu wa Kanuni za Biblia
Wachapishaji wa gazeti hili, Mashahidi wa Yehova, wanaamini kwamba Biblia ni ‘yenye faida kwa kufundisha, kwa kukaripia, kwa kunyoosha mambo, kwa kutia nidhamu.’ (2 Timotheo 3:16) Biblia si kitabu tu chenye maagizo ya jinsi ya kulea mtoto wako; bali ina kanuni zinazotoa mwongozo unaofaa kwa ajili ya familia. Chunguza kanuni zifuatazo.
BIBLIA INASEMA: “Ujinga umefungwa pamoja na moyo wa mvulana.”—Methali 22:15.
Ingawa watoto hufikiria wengine na ni wenye fadhili, bado wao hutenda kwa njia isiyofaa. Hivyo, watoto wanahitaji kutiwa nidhamu. (Methali 13:24) Kutambua ukweli huo kutakusaidia kutimiza daraka lako ukiwa mzazi.
BIBLIA INASEMA: “Usimnyime mvulana nidhamu.”—Methali 23:13.
Usiogope kuwatia nidhamu watoto wako kwa usawaziko eti kwa sababu tu utawavunja moyo au watakuchukia watakapokuwa watu wazima. Badala yake, nidhamu inapotolewa kwa njia ya upendo, itawasaidia watoto wako kujifunza jinsi ya kukubali shauri kwa unyenyekevu, sifa itakayowafaa watakapokuwa watu wazima.—Waebrania 12:11.
BIBLIA INASEMA: “Lolote lile analopanda mtu, atavuna hilo pia.”—Wagalatia 6: 7.
Kwa kawaida wazazi wanapenda kuwalinda watoto wao, na jambo hilo linafaa. Hata hivyo, unapaswa kuwa na usawaziko. Hutawasaidia watoto wako ikiwa utajaribu “kuwaokoa” wanapoadhibiwa kwa sababu ya makosa yao au kuwatetea mwalimu wao au mtu mwingine anapokueleza kuhusu tabia yao mbaya. Badala yake, unapaswa kuwaona watu hao kuwa rafiki zako. Unapofanya hivyo, unamfundisha mtoto wako kuheshimu mamlaka—kutia ndani yako.—Wakolosai 3:20.
BIBLIA INASEMA: “Mvulana aliyeachiliwa atamletea mama yake aibu.”—Methali 29:15.
Uwe mwenye upendo, mwenye msimamo, na mwenye usawaziko
Ingawa wazazi hawapaswi kuwa wakali kupita kiasi, wanapaswa kuepuka kuendekeza watoto wao. Kitabu The Price of Privilege kinasema hivi: “Watoto wanaoendekezwa na wazazi wao, huenda wakaanza kupuuza mamlaka ya watu wazima walio nyumbani.” Usipotumia mamlaka yako, huenda mtoto wako akahisi kwamba yeye ndiye mtawala. Hivyo, atafanya maamuzi yasiyofaa yatakayoleta madhara kwake na kwako pia.—Methali 17:25; 29:21.
BIBLIA INASEMA: “Mwanamume . . . atashikamana na mke wake, na hao wawili watakuwa mwili mmoja.”—Mathayo 19:5.
Kulingana na Biblia, mwanamume na mwanamke wanapaswa kuwa wamefunga ndoa kabla ya kuanza kupata watoto na wanapaswa kuendelea kuwa pamoja hata baada ya watoto hao kuwa watu wazima na kuondoka nyumbani. (Mathayo 19:5, 6) Hilo linamaanisha kwamba unakuwa mwenzi wa ndoa kwanza, na mzazi baadaye. Ikiwa hutafanya hivyo, huenda mtoto wako akaanza ‘kujifikiria mwenyewe zaidi kuliko ilivyo lazima kufikiri.’ (Waroma 12:3) Pia wenzi wa ndoa “wanaoendekeza mtoto wao,” wanaweza kudhoofisha ndoa yao.
Msaada kwa Wazazi
Ili utimize daraka lako ukiwa mzazi, unapaswa kumtia nidhamu mtoto wako kulingana na kanuni zifuatazo.
Uwe mwenye upendo. “Msiwe mkiwakasirisha watoto wenu, ili wasivunjike moyo.”—Wakolosai 3:21.
Uwe na msimamo. “Acheni tu neno lenu Ndiyo limaanishe Ndiyo, Siyo yenu, Siyo.”—Mathayo 5:37.
Uwe na usawaziko. “Nitakurekebisha kwa kiwango kinachofaa.”—Yeremia 30:11.a
a Kwa habari zaidi, tembelea Tovuti ya jw.org/sw. Tafuta kwenye MAFUNDISHO YA BIBLIA > WENZI WA NDOA NA WAZAZI, kisha utapata makala kama vile “Kuwatia Watoto Nidhamu,” “Jinsi ya Kushughulika na Mtoto Mwenye Milipuko ya Hasira,” “Wafundishe Watoto Wako Maadili Mema,” na “Jinsi ya Kumtia Nidhamu Kijana Wako.”
-