Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Je, Unaongoza Maisha Yako?
    Amkeni!—2015 | Julai
    • Mwanamume mwenye huzuni akiwaza kazini

      HABARI KUU

      Je, Unaongoza Maisha Yako?

      ULIPOKUWA kijana, ulikuwa na malengo gani maishani? Huenda ulitaka kuoa au kuolewa, kujifunza stadi, au kupata kazi nzuri. Hata hivyo, mara nyingi mambo huwa tofauti na vile tulivyopanga. Changamoto zisizotarajiwa zinaweza kubadili kabisa malengo yetu. Hivyo ndivyo ilivyokuwa kwa Anja, Delina, na Gregory.

      Anja, Delina, na Gregory
      • Anja, kutoka Ujerumani, aligunduliwa kuwa ana kansa alipokuwa na umri wa miaka 21, na kufikia sasa hawezi kutoka nyumbani.

      • Delina, kutoka Marekani, ana ugonjwa wa neva za misuli unaoitwa dystonia. Pia, anawatunza ndugu zake watatu wenye ulemavu.

      • Gregory, kutoka Kanada, ana ugonjwa wa kuwa na wasiwasi kupita kiasi.

      Licha ya hali wanazokabili, Anja, Delina, na Gregory wameweza kuongoza maisha yao. Jinsi gani?

      Methali moja katika Biblia inasema hivi: “Je, umejionyesha kuwa umevunjika moyo siku ya taabu? Nguvu zako zitakuwa chache.” (Methali 24:10) Matumizi yake ni wazi: Mtazamo unaweza kuathiri hali ya mtu. Watu wenye mtazamo usiofaa kujihusu wanapoteza uwezo wa kujiongoza, lakini wale wenye mtazamo unaofaa kujihusu mara nyingi wanapata nguvu ya kuwawezesha kuendelea kuongoza maisha yao.

      Ona jinsi kufanya hivyo kulivyowasaidia Anja, Delina, na Gregory.

  • Changamoto: Hali Zisizoweza Kubadilika
    Amkeni!—2015 | Julai
    • Anja akiongea na rafiki zake kupitia simu ya intaneti yenye video

      HABARI KUU | JE, UNAONGOZA MAISHA YAKO?

      Changamoto: Hali Zisizoweza Kubadilika

      JE, UNAKABILI ugonjwa wa kudumu? talaka? au umefiwa? Unapokabili hali zisizoweza kubadilika, huenda ukahisi kwamba huwezi kufanya jambo lolote zaidi ya kutamani kwamba hali yako ibadilike. Unaweza jinsi gani kurudisha tena uwezo wa kuongoza maisha yako?

      MFANO KATIKA BIBLIA: PAULO

      Mtume Paulo alisafiri sana akiwa mmishonari mwenye bidii wa karne ya kwanza. Lakini safari zake zilikoma alipokamatwa isivyo haki na kuwekwa katika kifungo cha nyumbani kwa miaka miwili chini ya ulinzi wa askari. Badala ya kukata tamaa, Paulo alikazia fikira jambo aliloweza kufanya. Aliwafariji na kuwasaidia kiroho wote waliomtembelea. Hata aliandika barua kadhaa ambazo ni sehemu ya Biblia.—Matendo 28:30, 31.

      MAMBO ANAYOFANYA ANJA

      Kama ilivyotajwa katika makala iliyotangulia, Anja hawezi kutoka nyumbani. Anasema hivi: “Kansa imebadili maisha yangu. Ninajitahidi sana kutunza afya yangu, hivyo sina kazi na siwezi kushirikiana na wengine kwa ukawaida.” Anja anakabili jinsi gani hali yake isiyoweza kubadilika? Anasema hivi: “Kupanga ratiba kumenisaidia sana. Ninatanguliza mambo muhimu kulingana na hali zangu. Hilo limenifanya nihisi kwamba ninaongoza maisha yangu.”

      “Nimejifunza kuwa mwenye kujitosheleza katika hali zozote nilizo nazo.”​—Maneno ya Paulo katika andiko la Wafilipi 4:11

      MAMBO UNAYOWEZA KUFANYA

      Ikiwa hali zisizoweza kubadilika zinaonekana kuongoza maisha yako, jaribu kufanya mambo yafuatayo:

      • Kazia fikira jambo unaloweza kufanya. Kwa mfano, huenda huwezi kuepuka magonjwa fulani, lakini, je, unaweza kufanya mazoezi, kula chakula chenye lishe, na kupumzika vya kutosha?

      • Amua mambo ambayo ungependa kutimiza maishani. Angalia mambo unayoweza kufanya ili kutimiza lengo lako hatua kwa hatua. Kila siku Jaribu kutumia muda fulani kutimiza malengo yako.

      • Fanya kazi, hata kama ni ndogo, zitakazokufanya uhisi uradhi. Safisha meza ya jikoni na vyombo. Valia kwa unadhifu. Timiza mambo ya muhimu wakati wa asubuhi.

      • Chunguza uone mambo unayoweza kujifunza kutokana na hali zako. Kwa mfano, je, hali yako inakusaidia kujua vizuri zaidi njia mbalimbali za kukabiliana na matatizo? Je, unaweza kutumia ujuzi huo kuwasaidia wengine?

      Jambo Kuu: Huenda usiweze kubadili hali zako, lakini unaweza kudhibiti hisia zako kuelekea hali hizo.

  • Changamoto: Hisia Zisizofaa
    Amkeni!—2015 | Julai
    • Gregory akifurahia mandhari ya asili

      HABARI KUU | JE, UNAONGOZA MAISHA YAKO?

      Changamoto: Hisia Zisizofaa

      JE, WEWE hulemewa na hisia kama vile huzuni, hasira, au kinyongo? Ikiwa ndivyo, huenda jambo hilo linakufanya uwe na wakati au uwezo mdogo tu wa kutimiza mambo yaliyo muhimu zaidi kwako. Unaweza kufanya nini kuhusiana na hilo?a

      MFANO KATIKA BIBLIA: DAUDI

      Mfalme Daudi alipambana na hisia mbalimbali kutia ndani mahangaiko na huzuni. Ni nini kilichomsaidia kukabiliana na hisia hizo? Daudi alimtegemea Mungu. (1 Samweli 24:12, 15) Pia, aliandika kuhusu hisia zake. Na akiwa mwanamume mwenye imani, alisali kwa ukawaida.b

      MAMBO ANAYOFANYA GREGORY

      Kama ilivyotajwa katika makala ya kwanza, Gregory ana ugonjwa wa kuwa na wasiwasi kupita kiasi. Anasema hivi: “Nilikuwa na wasiwasi kupita kiasi, na nilishindwa kujizuia.” Gregory aliweza kushughulikia hali hiyo jinsi gani? Anasema hivi: “Ili kurudia hali yangu, nilikubali msaada wenye fadhili wa mke wangu na rafiki zangu. Pia nilizungumza na daktari na kujifunza mengi kuhusu hali yangu. Nilipofanya mabadiliko fulani maishani, nilianza kuhisi kwamba ninakabiliana vizuri na hali yangu na kwamba siongozwi nayo. Ingawa bado pindi fulani ninakuwa na wasiwasi, sasa ninajua vizuri chanzo cha hali hizo, na ninajua jinsi ya kukabiliana na hali hiyo.”

      “Moyo wenye shangwe ni dawa nzuri.”​—Methali 17:22

      MAMBO UNAYOWEZA KUFANYA

      Ikiwa unalemewa na hisia zisizofaa, jaribu kufanya yafuatayo:

      • Andika kuhusu hisia zako.

      • Mweleze ndugu au rafiki yako kuhusu hisia zako.

      • Usikubali kushindwa na hisia zisizofaa. Kwa mfano, jiulize hivi: ‘Je, kuna sababu yoyote ya msingi ya kuwa na hisia hizi zisizofaa?’

      • Usijiruhusu uwe na mahangaiko, hasira au kinyongo moyoni. Badala yake tumia nguvu zako kufanya mambo yenye faida.c

      Jambo Kuu: Mara nyingi, hisia zisizofaa hazitokani na hali tunazokabili bali mtazamo wetu kuelekea hali hizo.

      a Hisia fulani zisizofaa hutokana na matatizo ya afya ambayo huenda yakahitaji matibabu ya daktari. Gazeti la Amkeni! halipendekezi matibabu fulani hususa. Kila mtu anahitaji kuchunguza kwa makini kabla ya kufanya uamuzi.

      b Zaburi nyingi zilizo katika Biblia ni sala zilizoandikwa na Daudi.

      c Kwa habari zaidi, soma mfululizo wa makala yenye kichwa “Jinsi ya Kukabiliana na Mahangaiko,” katika gazeti la Mnara wa Mlinzi la Julai 1, 2015.

  • Je, Unaweza Kuongoza Maisha Yako?
    Amkeni!—2015 | Julai
    • HABARI KUU | JE, UNAONGOZA MAISHA YAKO?

      Je, Unaweza Kuongoza Maisha Yako?

      Mwanamume akiongoza boti yake

      KUNA msemo usemao, “Maisha bila adha huwa malegevu.” Leo, hakuna mtu ambaye hajawahi kukabiliana na matatizo. Mara nyingi, siri ya mafanikio ni kujifunza kukubaliana na hali na kufanya mambo kulingana na hali hizo. Ni jambo linalofaa ikiwa utaweza kukabiliana vema na changamoto hizo maishani. Hatimaye, itakuwa vema ikiwa hali zako zitakuwa nzuri. Hata hivyo, jambo bora zaidi linakuja.

      Biblia inaahidi wakati ambapo watu wote watakuwa na uwezo wa kuongoza maisha yao. Wataweza kuishi wakiwa na uwezo wa kutimiza mambo kikamili, bila kuwa na mahangaiko, mikazo ya kila siku, na hisia zisizofaa. (Isaya 65:21, 22) Biblia inaitaja hali hiyo kuwa “uzima ulio wa kweli.”—1 Timotheo 6:19.

      “Na hakika wao watajenga nyumba na kukaa ndani yake; na hakika wao watapanda mashamba ya mizabibu na kula matunda yake. Hawatajenga na mtu mwingine akae ndani yake; hawatapanda na mtu mwingine ale. Kwa maana siku za watu wangu zitakuwa kama siku za mti; na watu wangu waliochaguliwa wataitumia kazi ya mikono yao wenyewe kikamilifu.”—Isaya 65:21, 22.

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki