Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Kutua kwa Njia Inayofaa
    Faidika na Elimu ya Shule ya Huduma ya Kitheokrasi
    • SOMO LA 5

      Kutua kwa Njia Inayofaa

      Unahitaji kufanya nini?

      Unahitaji kutua kabisa mahali panapofaa katika sehemu mbalimbali za hotuba yako. Nyakati nyingine unaweza kutua kifupi au kupunguza sauti kidogo. Kutua hufaa ikiwa kunatimiza kusudi zuri.

      Kwa Nini Ni Muhimu?

      Kutua mahali panapofaa ni sehemu muhimu ya usemi unaoeleweka kwa urahisi. Pia kutua hufanya mambo makuu yawe wazi.

      UNAPOONGEA, ni muhimu kutua mahali panapofaa. Na ni muhimu kutua iwe unatoa hotuba au unaongea na mtu. Bila kutua, mambo yanayosemwa yanaweza kukosa kueleweka wazi. Kutua mahali panapofaa husaidia kufanya maneno yako yawe wazi. Pia unaweza kutua ili mambo makuu yakumbukwe daima.

      Unaweza kujuaje wakati wa kutua? Na utue kwa muda gani?

      Kutua kwa Kufuata Alama za Vituo. Alama za vituo ni sehemu muhimu ya maandishi. Zinaweza kuonyesha mwisho wa taarifa au swali. Baadhi ya lugha hutumia alama za vituo kuonyesha maneno yaliyonukuliwa. Alama nyingine za vituo huonyesha uhusiano uliopo kati ya sehemu moja ya sentensi na sehemu nyingine. Mtu anayesoma anaweza kuona alama za vituo. Lakini anaposoma mbele ya wengine kwa sauti, ni lazima sauti yake ionyeshe alama za vituo zilizoko katika habari anayosoma. (Kwa maelezo zaidi, ona Somo la 1, “Kusoma kwa Usahihi.”) Ukikosa kutua mahali penye alama ya kituo, wengine wanaweza kukosa kuelewa jambo unalosoma au hata wanaweza kulielewa vibaya.

      Pia, jinsi mawazo yanavyotokezwa katika sentensi huonyesha mahali panapofaa kutua. Pindi moja mwanamuziki fulani mashuhuri aliandika hivi: “Mimi sipigi piano vizuri kuliko wengine. Lakini siri ni kutua mahali panapofaa.” Ndivyo ilivyo na kuzungumza. Kutua kwa njia inayofaa kutafanya hotuba uliyotayarisha vizuri ivutie na iwe na maana.

      Unapotayarisha kusoma mbele ya watu, inafaa kutia alama habari utakayosoma. Ukifika mahali ambapo unapaswa kutua kifupi, chora mstari mfupi ambao umesimama wima. Chora mistari miwili iliyo wima na karibu-karibu ili ujue mahali ambapo utatua kwa muda mrefu zaidi. Sentensi fulani ikiwa ngumu na kila mara unatua mahali pasipotakikana, tia alama kwa penseli maneno yote yanayounganisha sentensi hiyo ngumu. Kisha soma fungu hilo lote mwanzo hadi mwisho. Wasemaji wengi wenye uzoefu hufanya hivyo.

      Kwa kawaida hupati tatizo la kutua unapozungumza kwa sababu unajua mambo unayotaka kusema. Lakini usemi wako hautakuwa na nguvu wala hautakuwa wazi kama una tabia ya kutua kila wakati hata iwe unazungumzia nini. Madokezo yanayoonyesha jinsi ya kuboresha jambo hili yako katika Funzo la 4, “Ufasaha.”

      Kutua ili Kubadili Mawazo. Unapomaliza kuzungumzia jambo fulani na kuanza jambo tofauti, kutua kunaweza kuwasaidia wasikilizaji wafikirie, wajitayarishe, na hata kutambua kwamba unaanza kuzungumzia mambo tofauti, na kuelewa vizuri zaidi mambo utakayosema. Ni muhimu kutua unapomaliza kusema jambo moja na kuanza kusema jingine kama tu ilivyo muhimu kupunguza mwendo unapopiga kona kutoka njia moja na kushika njia nyingine.

      Wanapotoa hotuba, wasemaji wengine humaliza kuzungumzia jambo moja na kuanza jambo jingine mbio-mbio bila kutua. Hiyo ni kwa sababu wao hujaribu kuzungumzia mambo mengi mno. Wengine wana tabia hiyo katika mazungumzo yao ya kawaida. Labda watu wanaoshirikiana nao wanazungumza hivyo. Lakini huko si kufundisha kuzuri. Ikiwa unataka kusema jambo la maana ambalo litakumbukwa, basi tumia wakati kulikazia. Tambua kwamba kutua ni muhimu sana ili ueleweke vizuri.

      Ikiwa hotuba yako inategemea muhtasari, ipange vizuri ili ujue mahali pa kutua kati ya mambo makuu. Ikiwa una hotuba ya kusoma, tia alama sehemu ambayo jambo fulani kuu linaishia na jingine kuanzia.

      Mara nyingi kutua ili kubadili mawazo ni kurefu kuliko kule kutua kwa kufuata alama za vituo, lakini usitue kwa muda mrefu hivi kwamba hotuba ionekane inajivuta. Ikiwa unatua kwa muda mrefu sana, watu watafikiri hujatayarisha vizuri na unajaribu kufikiria jambo unalotaka kusema.

      Kutua ili Kutia Mkazo. Mara nyingi kutua ili kutia mkazo ni kutua kwa njia inayotokeza sana, yaani, ni kule kutua kunakotangulia au kufuata maneno yanayosemwa kwa mkazo fulani. Kutua huko kunasaidia wasikilizaji wafikirie jambo ambalo umetoka tu kusema, au kunawapa hamu ya kujua jambo linalofuata. Kuna namna nyingi za kutua kwa njia hiyo. Basi ni juu yako kuamua njia inayofaa ya kutua. Lakini ukumbuke kwamba kutua ili kukazia jambo kunafaa kutumiwa kwa mambo muhimu pekee. Ama sivyo, kutua huko hakutatimiza jambo lolote.

      Yesu aliposoma Maandiko kwa sauti katika sinagogi ya Nazareti, alitua vizuri sana. Kwanza, alisoma utume wake katika hati ya nabii Isaya. Lakini, kabla ya kufafanua maandiko hayo, alifunga hati, akampa mtumishi, akaketi. Kisha, wote katika sinagogi wakimtazama kwa makini, akasema: “Leo andiko hili ambalo mmetoka tu kusikia limetimizwa.”—Luka 4:16-21.

      Tua Kulingana na Hali. Pindi kwa pindi kelele zinaweza kufanya utue kama unazungumza. Kama unaongea na mtu katika huduma ya shambani, unaweza kutua ikiwa kuna kelele za gari linalopita au mtoto anayelia. Katika kusanyiko, unaweza kuinua sauti yako na kuendelea kuzungumza ikiwa kelele haivurugi sana. Lakini ni lazima utue ikiwa kuna kelele nyingi mno yenye kuendelea. Hata wasikilizaji hawatakuwa wakikusikiliza. Basi tua kwa njia inayofaa ili wasikilizaji wafaidike kikamili na mambo mema unayowaambia.

      Tua ili Uruhusu Wasikilizaji Wajibu. Ingawa huenda unatoa hotuba isiyoshirikisha wasikilizaji, ni muhimu kuruhusu wasikilizaji wajijibu kimoyomoyo. Ukitokeza maswali ambayo yanafanya wasikilizaji wafikiri lakini hutui kwa njia inayofaa, maswali hayo hayatakuwa na maana sana.

      Bila shaka ni muhimu kutua unapohubiria wengine na vilevile unapotoa hotuba jukwaani. Watu wengine ni kama hawatui kamwe. Kama una tatizo hilo, jaribu sana kukuza sifa hii ya usemi. Mawasiliano yako pamoja na wengine yataboreka na pia utakuwa na matokeo mazuri katika huduma ya shambani. Kutua ni ukimya wa muda mfupi na kama inavyosemekana, kwa kweli ukimya huonyesha vituo, hutia mkazo, hushika akili za mtu, na hupendeza wasikilizaji.

      Mazungumzo ya kawaida hushirikisha watu wawili au zaidi. Inaelekea wengine watakusikiliza ikiwa unawasikiliza na kuzingatia mambo wanayosema. Hiyo inamaanisha kutua kwa muda wa kutosha ili wapate nafasi ya kujieleza.

      Mahubiri yetu shambani huwa na matokeo zaidi tunapoongea na wengine kwa njia ya kawaida. Baada ya kusalimiana, Mashahidi wengi hupendelea kumjua mtu wanayemkuta kisha wamwulize swali. Wao hutua ili kumpa mtu huyo fursa ya kujibu, na kusikiliza jibu lake. Wanaweza kumpa fursa za kusema wanapozungumza naye. Wanajua kwamba kwa kawaida wanaweza kumsaidia mtu sana wakijua maoni yake juu ya jambo wanalozungumzia.—Mit. 20:5.

      Bila shaka si watu wote hujibu maswali vizuri. Lakini jambo hilo halikumzuia Yesu asitue vya kutosha ili awape hata wapinzani wake fursa ya kusema. (Mk. 3:1-5) Kumpa mtu fursa ya kusema humsaidia kufikiri na hiyo inaweza kumfanya afunue yaliyo moyoni mwake. Hata mojawapo ya makusudi yetu katika huduma ni kuchochea mioyo kwa kuwajulisha watu mambo muhimu yanayotokana na Neno la Mungu ambayo ni lazima wafanye maamuzi kuyahusu.—Ebr. 4:12.

      Kwa kweli kutua kwa njia inayofaa tukiwa katika huduma kunahitaji ustadi. Tunapotua kwa njia inayofaa, mambo tunayosema hueleweka vizuri zaidi na kukumbukwa daima.

      JINSI YA KUFAULU

      • Zingatia sana alama za vituo unaposoma kwa sauti.

      • Wasikilize kwa makini wasemaji wazuri, na uone jinsi wanavyotua na muda wanaotua.

      • Baada ya kusema jambo ambalo unataka sana wengine wakumbuke, tua ili jambo hilo liwaingie vizuri.

      • Unapozungumza na wengine, wape pia nafasi za kuzungumza, kisha usikilize majibu yao. Acha wamalize kusema. Usiwakatize.

      MAZOEZI: Soma Marko 9:1-13 kwa sauti; tua kwa njia inayofaa unapofikia alama za vituo. Usijivute unaposoma. Baada ya kufanya mazoezi, omba mtu akusikilize na akupe mashauri ya jinsi unavyoweza kutua vizuri.

  • Kukazia Maana kwa Njia Inayofaa
    Faidika na Elimu ya Shule ya Huduma ya Kitheokrasi
    • SOMO LA 6

      Kukazia Maana kwa Njia Inayofaa

      Unahitaji kufanya nini?

      Unahitaji kukazia maneno kwa njia ambayo ni rahisi kwa wasikilizaji kukuelewa.

      Kwa Nini Ni Muhimu?

      Kukazia maana kwa njia inayofaa humsaidia msemaji kushika akili za wasikilizaji na kuwahimiza au kuwachochea.

      UNAPOZUNGUMZA au unaposoma kwa sauti, ni muhimu kusema neno mojamoja vizuri na kukazia kwa njia inayotokeza wazi maneno muhimu na yale yanayowasilisha mawazo yako.

      Kukazia maana kwa njia inayofaa si kukazia tu maneno machache au hata kukazia maneno mengi. Ni lazima maneno yanayofaa yakaziwe. Ukikazia maneno ambayo hayastahili kukaziwa, huenda wasikilizaji wasielewe jambo unalomaanisha, na akili zao zinaweza kuanza kutangatanga. Hata kama habari yenyewe inapendeza, haitachochea wasikilizaji sana ikiwa maana haikaziwi vizuri.

      Unaweza kutia mkazo zaidi kwa njia kadhaa, na mara nyingi njia hizo hutumika pamoja: kuinua sauti, kuongeza hisia, kupunguza mwendo na kutamka kila neno kwa utaratibu, kutua kabla au baada ya kusema jambo (au kutua kabla na baada ya kusema jambo), na kwa ishara za mwili na za uso. Katika lugha nyinginezo, mtu anaweza kutia mkazo kwa kupunguza sauti au kuiinua. Fikiria habari hiyo na hali zake ili uone jambo linalofaa kukaziwa.

      Unapofikiria jambo la kukazia, zingatia yafuatayo. (1) Maneno yanayopaswa kukaziwa zaidi katika sentensi yoyote hutegemea sehemu inayobaki ya sentensi hiyo na pia muktadha. (2) Unaweza kukazia maana unapoanza wazo jipya, iwe ni jambo kuu au iwe unabadili tu mawazo yako na kuanza kuzungumzia jambo jingine. Pia unaweza kukazia maana ili kuonyesha kwamba unamaliza kusema jambo fulani. (3) Msemaji anaweza kukazia maana anapotaka kuonyesha jinsi anavyohisi kuhusu jambo fulani. (4) Unaweza kukazia maana kwa njia inayofaa ili kudhihirisha mambo makuu ya hotuba.

      Ili kukazia maana katika njia hizo ambazo zimeonyeshwa, ni lazima mtu anayehutubia watu au anayesoma mbele ya watu aelewe vizuri habari hiyo na awe anataka wasikilizaji waielewe. Andiko la Nehemia 8:8 linasema hivi kuhusu maagizo yaliyotolewa wakati wa Ezra: “Nao wakasoma katika kitabu, katika torati ya Mungu, kwa sauti ya kusikilika; wakaeleza maana yake, hata wakayafahamu yaliyosomwa.” Ni wazi kwamba wale waliosoma Neno la Mungu na kulifafanua katika pindi hiyo walitambua umuhimu wa kuwasaidia wasikilizaji waelewe yaliyosomwa, wayashike, na kuyafuata maishani.

      Tatizo Linaweza Kutokezwa na Nini? Watu wengi wanaweza kuongea kwa njia inayoeleweka vizuri katika mazungumzo ya kila siku. Lakini, wanaposoma habari iliyoandikwa na mtu mwingine, wanaweza kushindwa mambo ya kukazia. Basi siri ni kuelewa vizuri habari hiyo. Hiyo inamaanisha kuchunguza kwa makini habari hiyo. Kwa hiyo, ukipewa mgawo wa kusoma katika mkutano wa kutaniko, tayarisha kwa bidii.

      Watu wengine hukazia maneno baada ya kila pindi fulani badala ya kukazia maana, iwe mkazo huo unafaa au haufai. Wengine hukazia maneno ambayo hayapaswi kukaziwa, labda wakikazia mno vihusishi na viunganishi. Ikiwa mkazo haufanyi jambo liwe wazi, ni rahisi sana uwe zoea linalokengeusha watu.

      Ili kukazia maana, wasemaji wengine huinua sauti zao hivi kwamba wasikilizaji wanaona ni kana kwamba wanazomewa. Kwa wazi si rahisi njia hiyo iwe na matokeo mazuri. Kama hukazii maneno kwa njia ya kawaida, wasikilizaji wanaweza kufikiri kwamba msemaji anawashusha chini. Ni afadhali kama nini kuwachochea kwa upendo na kuwasaidia waone kwamba mambo wanayosikia yanatokana na Maandiko na yanafaa!

      Jinsi ya Kufanya Maendeleo. Mara nyingi mtu ambaye hukazia maana kwa njia isiyofaa hajui ana tatizo hilo. Ni mtu mwingine anayeweza kumtajia. Ikiwa unahitaji kufanya maendeleo kuhusu jambo hili, mwangalizi wa shule atakusaidia. Pia, unaweza kumwomba mtu mwingine ambaye ni msemaji mzuri akusaidie. Mwambie akusikilize kwa makini unaposoma na unaposema na akushauri mahali unapohitaji kufanyia maendeleo.

      Kwanza, mwenye kukushauri anaweza kupendekeza ufanye mazoezi kwa kusoma sehemu fulani ya Mnara wa Mlinzi. Yamkini, atakuambia uchunguze kila sentensi ili ujue ni maneno yapi au mafungu yapi ya maneno yanayopaswa kukaziwa ili maana ieleweke kwa urahisi. Anaweza kukukumbusha utilie maanani maneno fulani ambayo yameandikwa kwa italiki. Kumbuka kwamba maneno yanayofanyiza sentensi yameungana ili kutokeza maana. Mara nyingi ni fungu la maneno linalopaswa kukaziwa, bali si neno moja tu. Katika lugha nyinginezo, wanafunzi wanaweza kuambiwa wazingatie kwa makini jinsi alama za matamshi zinavyoonyesha mkazo unaofaa.

      Hatua inayofuata sasa ni kujifunza jambo la kukazia, na mwenye kukushauri anaweza kukuhimiza ufikirie muktadha na si sentensi tu. Fungu lote linazungumzia jambo gani kuu? Jambo hilo linahusikaje na kile unachokazia katika sentensi? Tazama kichwa kikuu cha habari unayosoma na kichwa chake kidogo chenye maandishi mazito. Vichwa hivyo vina uhusiano gani na habari unayochagua kukazia? Unapaswa kuzingatia mambo hayo yote. Lakini jihadhari usikazie maneno mengi mno.

      Iwe utatoa hotuba au utasoma, mwenye kukushauri anaweza pia kukuambia ukazie maana kulingana na hoja zako. Unahitaji kujua mahali ambapo hoja zako zinaishia au mahali ambapo unaanza kuzungumzia jambo jingine muhimu. Wasikilizaji watathamini ikiwa jinsi unavyotoa hotuba inawasaidia kutambua mambo hayo kimbele. Unaweza kufaulu kwa kukazia maneno kama kwanza kabisa, halafu, hatimaye, basi, na kwa kufaa.

      Mwenye kukushauri pia atakuambia uzingatie maneno ambayo unataka kusema kwa hisia. Ili ufanye hivyo huenda ukahitaji kukazia maneno kama sana, bila shaka, kwa vyovyote vile, haiwezekani, muhimu, na siku zote. Ukifanya hivyo, wasikilizaji wako wanaweza kuona jinsi unavyohisi kuhusu jambo unalosema. Tutazungumzia zaidi jambo hili katika Somo la 11, “Zungumza kwa Hisia.”

      Ili uboreshe njia yako ya kukazia maana, pia utatiwa moyo uyaweke wazi akilini mambo makuu ambayo unataka wasikilizaji wakumbuke. Jambo hili litafafanuliwa zaidi tutakapozungumzia kusoma mbele ya watu katika Somo la 7, “Kukazia Mawazo Makuu,” na pia katika hali ya usemaji katika Somo la 37, “Kukazia Mambo Makuu.”

      Ikiwa unajaribu kuboresha huduma yako ya shambani, fikiria sana jinsi unavyosoma maandiko. Jiulize hivi kila mara, ‘Kwa nini ninasoma andiko hili?’ Ukiwa mwalimu, haitoshi kusema tu maneno ifaavyo. Huenda hata kusoma andiko hilo kwa hisia tu hakutoshi. Kama unajibu swali la mtu au unafundisha kweli ya msingi, unaposoma maandiko ni vizuri kukazia maneno yanayotegemeza jambo unalozungumzia. Usipofanya hivyo mtu unayemsomea anaweza kukosa kukuelewa.

      Kwa kuwa kukazia maana kunaongezea mkazo maneno mengine, msemaji ambaye hana uzoefu anaweza kuwa na mwelekeo wa kukazia maneno hayo kupita kiasi. Anafanana na mtu ambaye anaanza kujifunza ala fulani ya muziki. Lakini akiendelea kufanya mazoezi, hatimaye atafaulu kucheza muziki mtamu unaofurahisha.

      Baada ya kujifunza mambo ya msingi, utafaidika ukiwasikiliza wasemaji wenye uzoefu. Upesi utatambua jinsi mkazo wa kadiri tofauti-tofauti unavyoweza kutimiza mengi. Na utaona faida ya kukazia maana kwa njia mbalimbali ili mambo unayosema yawe wazi. Utaboresha sana usomaji wako na usemaji wako ukijua jinsi ya kukazia maana kwa njia inayofaa.

      Usijifunze kukazia maana ili tu utimize wajibu. Ili uwe msemaji mzuri, endelea kujizoeza mpaka uwe umejua sana kukazia maana na kuweza kufanya hivyo kwa njia inayoonekana kuwa ya kawaida kwa wasikilizaji.

      JINSI YA KUJIFUNZA KUKAZIA MAANA

      • Jizoeze kutambua maneno makuu na mafungu makuu ya maneno katika sentensi. Fikiria muktadha unapofanya hivyo.

      • Jaribu kutumia mkazo ili kuonyesha (1) badiliko la mawazo na (2) jinsi unavyohisi kuhusu jambo unalosema.

      • Unaposoma maandiko, uwe na mazoea ya kukazia maneno ambayo yanategemeza sababu zako za kurejelea maandiko hayo.

      MAZOEZI: (1) Chagua maandiko mawili ambayo wewe hutumia mara nyingi katika huduma ya shambani. Tambua jambo unalojaribu kuthibitisha katika kila andiko unalosoma. Soma maandiko hayo kwa sauti ili kukazia maneno au fungu la maneno ambayo yanategemeza hoja hizo. (2) Chunguza Waebrania 1:1-14. Kwa nini ni lazima maneno “manabii” (mst. 1), “Mwana” (mst. 2), na “malaika” (mst. 4, 5) yakaziwe kipekee ili sababu zinazoonyeshwa ziwe wazi katika sura hii? Fanya mazoezi ya kusoma sura hiyo kwa sauti ukikazia maana ili sababu hizo ziwe wazi.

  • Kukazia Mawazo Makuu
    Faidika na Elimu ya Shule ya Huduma ya Kitheokrasi
    • SOMO LA 7

      Kukazia Mawazo Makuu

      Unahitaji kufanya nini?

      Unaposoma kwa sauti, kazia kwa njia maalumu mawazo makuu ya habari yote unayosoma, na si kutia mkazo katika sentensi mojamoja.

      KWA NINI NI MUHIMU?

      Ujumbe wako utakumbukwa kwa urahisi ukikazia mawazo makuu.

      MSOMAJI mzuri hazingatii sentensi moja tu, wala hazingatii tu fungu ambalo lina sentensi hiyo. Anaposoma, anazingatia mawazo makuu ya habari nzima anayosoma. Hiyo humsaidia kujua mahali pa kutia mkazo.

      Mtu asipofanya hivyo, usomaji wake utakosa vilele. Hakuna jambo litakalokuwa wazi. Na anapomaliza kusoma, inaweza kuwa vigumu kukumbuka jambo lolote kuu.

      Kukazia mawazo makuu kwa njia inayofaa mara nyingi kunaweza kuboresha sana usomaji wa simulizi lolote la Biblia. Mkazo kama huo unaweza kufanya usomaji wa mafungu uwe na maana sana kwenye funzo la Biblia la nyumbani au kwenye mkutano wa kutaniko. Na mkazo huo ni muhimu sana unapotoa hotuba ya kusomwa, kama ambavyo nyakati nyingine inafanywa katika makusanyiko yetu.

      Jinsi ya Kufaulu. Unaweza kupokea mgawo wa kusoma Biblia katika shule. Ukazie nini? Ikiwa kuna wazo kuu au tukio muhimu linalozungumziwa katika habari unayosoma, ingefaa kulikazia.

      Iwe sehemu unayosoma ni shairi au si shairi, mithali au masimulizi, wasikilizaji watafaidika ukiisoma vizuri. (2 Tim. 3:16, 17) Ili uweze kusoma vizuri, ni lazima uzingatie mafungu ambayo utasoma na vilevile uwafikirie wasikilizaji.

      Ikiwa utasoma kwa sauti kichapo fulani katika funzo la Biblia au kwenye mkutano wa kutaniko, unahitaji kukazia mawazo gani makuu? Chukua majibu ya maswali yaliyochapishwa kuwa mawazo makuu. Pia kazia mambo yanayopatikana chini ya vichwa vidogo vyenye herufi nzito yanayohusiana na vichwa hivyo.

      Haipendekezwi kusoma hotuba za kutaniko. Hata hivyo, mara kwa mara hotuba za kusomwa huandaliwa katika kusanyiko ili mawazo yaleyale yatolewe kwa njia ileile katika makusanyiko yote. Ili kukazia mawazo makuu katika hotuba kama hizo za kusomwa, kwanza ni lazima msemaji achunguze hotuba hiyo kwa makini. Mambo makuu ni yapi? Anapaswa kuyatambua. Mambo makuu si mawazo ambayo yeye anafikiri yanapendeza. Ni yale mambo muhimu ambayo yanategemeza hotuba hiyo. Mara nyingi taarifa fupi ya wazo kuu katika hotuba ya kusomwa hutanguliza masimulizi fulani au kusababu fulani. Kwa kawaida, taarifa yenye nguvu hutolewa baada ya kutajwa kwa mambo yanayothibitisha jambo fulani. Baada ya kutambua mambo makuu, msemaji anapaswa kuyatia alama katika hotuba yake ya kusomwa. Mawazo hayo makuu huwa machache, labda hayazidi manne au matano. Kisha anahitaji kujizoeza kusoma ili wasikilizaji waweze kutambua kwa urahisi hayo mambo makuu. Mambo hayo makuu ndiyo vilele vya hotuba. Hotuba hiyo ikitolewa kwa mkazo unaofaa, inaelekea mawazo hayo makuu yatakumbukwa. Msemaji anapaswa kuwa na lengo la kufanya mawazo makuu yakumbukwe.

      Kuna njia kadhaa ambazo msemaji anaweza kutumia kutia mkazo unaofaa ili wasikilizaji watambue mambo makuu. Anaweza kuongeza shauku, anaweza kubadili mwendo wake wa kusoma, anaweza kuongeza hisia, au anaweza kutumia ishara zinazofaa na kadhalika.

      MAMBO YA KUKUMBUKA

      • Chunguza habari hiyo ili utambue mawazo yake makuu. Uyatie alama.

      • Ili mawazo makuu yawe dhahiri unaposoma kwa sauti, ongeza shauku, punguza mwendo, au badili hisia kama ina- vyofaa.

      MAZOEZI: Chagua mafungu matano katika funzo la Mnara wa Mlinzi ambalo limeratibiwa kusomwa. Piga mistari majibu ya maswali ya mafungu hayo. Soma mafungu hayo kwa sauti kwa njia itakayofanya wasikilizaji watambue majibu kwa urahisi.

  • Kiasi Kinachofaa cha Sauti
    Faidika na Elimu ya Shule ya Huduma ya Kitheokrasi
    • SOMO LA 8

      Kiasi Kinachofaa cha Sauti

      Unahitaji kufanya nini?

      Unahitaji kuzungumza kwa sauti ya kutosha au mkazo wa kutosha. Ili ujue kiasi kinachofaa cha sauti, fikiria (1) idadi ya wale wanaokusikiliza na pia ufikirie wao ni watu wa aina gani, (2) kelele zinazokengeusha, (3) habari unayozungumzia, na (4) kusudi lako.

      Kwa Nini Ni Muhimu?

      Ikiwa wengine hawakusikii vizuri, akili zao zinaweza kutangatanga, na huenda wasielewe mambo unayosema. Ukizungumza kwa sauti kubwa sana, unaweza kuudhi watu—na hata wanaweza kufikiri huna heshima.

      IKIWA msemaji anaongea kwa sauti ya chini, baadhi ya wasikilizaji wanaweza kuanza kusinzia. Ikiwa mhubiri anazungumza kwa sauti ya chini sana katika huduma ya shambani, huenda mwenye nyumba asimsikilize. Na ikiwa wasikilizaji wanatoa maelezo kwa sauti ya chini katika mikutano, wengine hawatapata kitia-moyo kinachohitajika. (Ebr. 10:24, 25) Kwa upande mwingine, msemaji akiinua sauti yake wakati usiofaa, wasikilizaji wanaweza kushangaa na hata kuudhika.—Mit. 27:14.

      Wafikirie Wale Wanaokusikiliza. Je, unazungumza na mtu mmoja? familia? kikundi kinachokutana kwa ajili ya huduma ya shambani? kutaniko zima? au unazungumza mbele ya kusanyiko kubwa? Ni wazi kwamba kiasi cha sauti kinachofaa hali moja huenda kisifae hali nyingine.

      Katika pindi kadhaa, watumishi wa Mungu wamehutubia umati. Katika siku za Solomoni, vikuza-sauti havikuwako wakati wa kuwekwa wakfu kwa hekalu la Yerusalemu. Kwa hiyo Solomoni alisimama jukwaani akabariki watu “kwa sauti kuu.” (1 Fal. 8:55; 2 Nya. 6:13) Karne nyingi baadaye, baada ya kumwagwa kwa roho takatifu siku ya Pentekoste 33 W.K., umati ulizingira kikundi cha Wakristo katika Yerusalemu. Watu wengine walipendezwa lakini wengine waliwadhihaki Wakristo hao. Petro alitumia hekima, “akasimama . . . na kuinua sauti yake.” (Mdo. 2:14) Akatoa ushahidi wenye nguvu sana.

      Unaweza kutambuaje kama kiasi cha sauti yako kinafaa? Mojawapo ya njia bora za kutambua jambo hilo ni jinsi wasikilizaji wanavyoitikia. Ukiona baadhi ya wasikilizaji waking’ang’ana kukusikiliza, jaribu kuinua sauti yako.

      Iwe tunazungumza na mtu mmoja au tunazungumza mbele ya kikundi, ni vizuri kufikiria wasikilizaji. Ikiwa kuna mmoja ambaye hasikii vizuri, huenda ukahitaji kuinua sauti yako. Lakini labda watu wenye umri mkubwa ambao huenda wasiitikie upesi wasifurahi ukizungumza kwa sauti ya juu sana. Kupiga kelele hata kunaweza kuonwa kuwa kukosa adabu. Katika jamii fulani-fulani kuongea kwa sauti kubwa sana huonwa kuwa ishara ya kukasirika au kukosa subira.

      Fikiria Kelele Zinazokengeusha. Unapokuwa katika huduma ya shambani, kiasi cha sauti yako hutegemea hali unazopata. Huenda kuna kelele za magari, watoto, mbwa wanaobweka, mdundo wa juu wa muziki, au televisheni iliyowashwa kwa sauti ya juu. Kwa upande mwingine, katika maeneo ambamo nyumba ziko karibu-karibu, mwenye nyumba anaweza kuaibika ukizungumza kwa sauti ya juu hivi kwamba hata majirani wanakusikia.

      Akina ndugu ambao hutoa hotuba kutanikoni au kwenye makusanyiko pia hulazimika kukabili hali tofauti-tofauti. Kuzungumza na watu kule nje ni tofauti na kutoa hotuba katika jumba lenye vikuza-sauti vinavyofaa. Katika Amerika Kusini mishonari wawili walishiriki kutoa hotuba ya watu wote katika baraza ya nyumba ya mtu mmoja aliyependezwa. Hotuba ilipokuwa ikitolewa, fataki zilikuwa zikilipuliwa katika uwanja fulani uliokuwa karibu, na jogoo mmoja alikuwa akiwika bila kukoma!

      Kitu chochote kinaweza kutukia unapoendelea kutoa hotuba na huenda ukahitaji kutua kidogo mpaka kelele hiyo ipungue au unaweza kuinua sauti yako. Kwa mfano, ikiwa mikutano inafanywa katika jengo lenye paa ya mabati, mvua kubwa inaweza kufanya wasikilizaji wasimsikie msemaji. Mtoto anayelia au kelele zinazosababishwa na watu wanaofika wakiwa wamechelewa zinaweza kukuvuruga. Jifunze kukabiliana na kelele hizo zinazokengeusha ili wasikilizaji wafaidike kabisa na hotuba yako.

      Vikuza-sauti vinaweza kusaidia ikiwa vinapatikana, lakini bado msemaji anahitaji kuinua sauti yake kulingana na hali. Katika maeneo mengine ambamo umeme hupotea-potea, wasemaji hulazimika kuendelea kuongea bila kutumia maikrofoni.

      Fikiria Habari Unayozungumzia. Kiasi cha sauti yako pia hutegemea habari unayozungumzia katika hotuba yako. Ikiwa jambo unalosema linahitaji mkazo, usilidhoofishe kwa kuongea kwa sauti dhaifu mno. Kwa mfano, unaposoma mashutumu makali katika Maandiko, sauti yako inapasa kuwa na nguvu kuliko sauti unayotumia kusoma shauri linalohusu kuonyesha upendo. Fanya kiasi cha sauti yako kifae habari unayozungumzia, lakini ujihadhari usipite kiasi na kujielekezea fikira.

      Fikiria Kusudi Lako. Ukitaka kuchochea wasikilizaji watie bidii katika utendaji, huenda ukahitaji kutumia sauti yenye nguvu kwa kiasi fulani. Ukitaka kubadili fikira zao, usitumie sauti kubwa kupita kiasi. Kama unajaribu kuwafariji, mara nyingi ni afadhali kutumia sauti ya upole.

      Kutumia Vizuri Sauti ya Juu. Unapojaribu kuita mtu ambaye ana shughuli, kwa kawaida inafaa kuinua sauti. Wazazi wanajua jambo hili na basi wao huwaita watoto wao kwa sauti kubwa wakati ukifika wa kuacha kucheza na kurudi nyumbani. Pia mwenyekiti anaweza kuhitajika kuinua sauti anapotaka watu wawe makini kutanikoni au kusanyikoni. Wahubiri wanapokuwa katika huduma ya shambani, wanaweza kusalimiana kwa sauti na watu ambao wanaendelea na shughuli zao nje.

      Hata baada ya kuvuta fikira za mtu, ni muhimu uendelee kutumia kiasi kinachofaa cha sauti. Sauti ya chini sana inaweza kufanya wengine wadhani mwenye kuongea hajajitayarisha vizuri au hasadiki mambo anayosema.

      Ukitoa amri kwa sauti kubwa, watu wanaweza kuchochewa kuchukua hatua. (Mdo. 14:9, 10) Hali kadhalika, amri inayotolewa kwa sauti kuu inaweza kuepusha msiba. Kule Filipi, mlinzi mmoja wa jela karibu ajiue kwa sababu alidhani wafungwa aliokuwa akilinda wametoroka. ‘Paulo akapaaza sauti kubwa, akisema: “Usijiumize, kwa maana sisi sote tupo hapa!”’ Kwa njia hiyo waliepusha msiba kwa kumzuia mlinzi huyo asijiue. Kisha Paulo na Sila wakamhubiria mlinzi huyo na jamaa yake, wote wakakubali kweli.—Mdo. 16:27-33.

      Jinsi ya Kuboresha Kiasi cha Sauti Yako. Wengine wanahitaji kujitahidi sana kujifunza kutumia kiasi kinachofaa cha sauti. Mtu anaweza kuongea kwa sauti ya chini kwa sababu ana sauti ndogo. Lakini, akitia bidii anaweza kufanya maendeleo, hata ingawa bado hawezi kuongea kwa sauti yenye nguvu. Fikiria jinsi unavyopumua na jinsi unavyokaa. Fanya mazoezi ya kuketi vizuri na kusimama vizuri. Sogeza nyuma mabega yako kisha uvute pumzi nyingi. Hakikisha unajaza sehemu za chini za mapafu yako hewa. Ukitumia vizuri hewa hiyo, unaweza kudhibiti kiasi cha sauti yako unapoongea.

      Wengine wana tatizo la kusema kwa sauti kubwa sana. Labda wamezoea tabia hiyo kwa sababu ya kufanya kazi sehemu za nje au katika mazingira yenye kelele nyingi. Kwa upande mwingine, labda walilelewa katika mazingira ambamo kila mtu alikuwa akipiga kelele na kukatiza-katiza mazungumzo. Na basi wanadhani kwamba njia ya pekee ya kushiriki katika mazungumzo ni kuongea kwa sauti ya juu kuliko wengine wote. Lakini wanapoendelea kutii shauri la Biblia la kujivika “shauku nyororo za huruma, fadhili, hali ya akili ya kujishusha chini, upole, na ustahimilivu,” wao watarekebisha kiasi cha sauti yao wanapoongea na wengine.—Kol. 3:12.

      Mambo yatakayokusaidia kuzungumza kwa kiasi kinachofaa cha sauti ni matayarisho mazuri, uzoefu unaopata kwa kushiriki kwa ukawaida katika utumishi wa shambani, na sala kwa Yehova. Iwe unatoa hotuba jukwaani au unaongea na mtu katika huduma ya shambani, jaribu kufikiria jinsi mambo unayosema yanavyoweza kuwasaidia watu.—Mit. 18:21.

      WAKATI AMBAPO SAUTI YA JUU INAWEZA KUHITAJIKA

      • Unapotaka kundi la watu liwe makini.

      • Kunapokuwa na kelele.

      • Unapotaka usikilizwe unaposema jambo muhimu sana.

      • Unapotaka kufanya watu wachukue hatua fulani.

      • Unapoita mtu au kikundi fulani cha watu.

      JINSI YA KUFANYA MAENDELEO

      • Tazama jinsi watu unaoongea nao wanavyoitikia; tumia kiasi kinachofaa cha sauti ili waweze kusikia kwa njia inayofaa.

      • Jifunze kujaza sehemu za chini za mapafu yako hewa.

      MAZOEZI: Kwanza soma Matendo 19:23-41 kimoyo-kimoyo ukifikiria hali ya mistari hiyo kama inavyoonyeshwa na masimulizi na muktadha. Tambua yule anayeongea na pia roho inayoonyeshwa. Sasa soma kila sehemu kwa sauti inayofaa.

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki