Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • ‘Endeleeni Kuushinda Uovu’ kwa Kuizuia Hasira
    Mnara wa Mlinzi—2010 | Juni 15
    • ‘Endeleeni Kuushinda Uovu’ kwa Kuizuia Hasira

      ‘Wapendwa, msijilipizie kisasi wenyewe, bali endeleeni kuushinda uovu kwa wema.’—ROM. 12:19, 21.

      1, 2. Mashahidi fulani waliokuwa wakisafiri walionyesha mfano gani mzuri?

      MASHAHIDI WA YEHOVA 34 walikuwa wakisafiri ili kuhudhuria programu ya kuweka wakfu ofisi moja ya tawi lakini ndege ikachelewa kwa sababu ya matatizo ya kiufundi. Ndege hiyo ilitazamiwa kutua kwa muda wa saa moja ili iongezwe mafuta, hata hivyo, ilikaa kwa muda wa saa 44 kwenye uwanja huo ulio mbali sana ambao hauna chakula, maji, wala vyoo vya kutosha. Wasafiri wengi walikasirika na kuwatisha wafanyakazi wa uwanja wa ndege. Lakini akina ndugu na dada walikuwa watulivu.

      2 Mwishowe, Mashahidi hao walifika mahali walipokuwa wakienda na kupata sehemu ya mwisho ya programu ya wakfu. Ingawa walikuwa wamechoka, hawakuondoka baada ya programu, walifurahia kuzungumza na ndugu wa nchi hiyo. Baadaye, walipata habari kwamba kuna watu ambao waliona jinsi walivyoonyesha subira na kujizuia. Msafiri mmoja aliwaambia hivi wafanyakazi wa kampuni hiyo ya ndege: “Kama si hao Wakristo 34 waliokuwa katika ndege hiyo, kungekuwa na fujo kwenye uwanja wa ndege.”

      Kuishi Katika Ulimwengu Wenye Hasira

      3, 4. (a) Hasira yenye jeuri ilianza jinsi gani katika jamii ya wanadamu na imekuwapo kwa muda mrefu kadiri gani? (b) Je, Kaini angeweza kuizuia hasira yake? Eleza.

      3 Mikazo ya maisha katika mfumo huu mwovu wa mambo inaweza kuwafanya watu wakasirike. (Mhu. 7:7) Mara nyingi, hasira hiyo inatokeza chuki na hata jeuri. Kuna vita vikali ndani ya nchi nyingi na kati ya nchi mbalimbali, na mikazo katika familia inasababisha ugomvi katika nyumba nyingi. Hasira na jeuri kama hiyo ilianza zamani sana. Kaini, mwana wa kwanza wa Adamu na Hawa, alimuua ndugu yake mdogo Abeli kwa sababu ya hasira iliyochochewa na wivu. Kaini alitenda tendo hilo ovu hata ingawa Yehova alikuwa amemsihi azuie hasira yake na kumwahidi kwamba angembariki ikiwa angefanya hivyo.—Soma Mwanzo 4:6-8.

      4 Hata ingawa alirithi hali ya kutokamilika, Kaini angeweza kuchagua jambo la kufanya. Angeweza kuzuia hasira yake. Kwa hiyo, alikuwa na hatia kwa sababu ya tendo lake la jeuri. Vivyo hivyo, hali yetu ya kutokuwa wakamilifu inafanya iwe vigumu zaidi kwetu kuepuka hasira na matendo ya hasira. Pia, matatizo mengine mazito yanaweza kuzidisha mikazo katika ‘nyakati hizi za hatari.’ (2 Tim. 3:1) Kwa mfano, tunaweza kupata mikazo ya kihisia kwa sababu ya matatizo ya kiuchumi. Polisi na mashirika ya kusaidia familia yanasema kwamba misukosuko ya kiuchumi inasababisha kuongezeka kwa milipuko ya hasira na jeuri nyumbani.

      5, 6. Ni mtazamo gani wa ulimwengu kuhusu hasira unaoweza kuwa na uvutano juu yetu?

      5 Zaidi ya hayo, watu wengi tunaokutana nao ni “wenye kujipenda wenyewe,” “wenye majivuno,” na hata ni “wakali.” Ni rahisi sana kwetu kuiga sifa mbaya kama hizo na zinaweza hata kutufanya tuwe na hasira. (2 Tim. 3:2-5) Kwa kweli, mara nyingi sinema na programu za televisheni zinaonyesha kwamba kulipiza kisasi ni jambo zuri na kutenda kijeuri ni njia ya kawaida na inayokubalika ya kusuluhisha matatizo. Kwa kawaida, sinema zinazopendwa zinawafanya watazamaji wangoje kwa hamu kumwona adui “akipata kile anachostahili,” kwa kawaida anaangamizwa kwa jeuri na shujaa wa sinema hiyo.

      6 Propaganda kama hizo hazifundishi njia za Mungu, badala yake zinasitawisha “roho ya ulimwengu” na ya mtawala wake mwenye hasira, Shetani. (1 Kor. 2:12; Efe. 2:2; Ufu. 12:12) Roho hiyo inawachochea watu kutosheleza tamaa za mwili wenye dhambi na inapingana kabisa na roho takatifu ya Mungu na tunda lake. Kwa kweli, fundisho la msingi la Ukristo ni kutolipiza kisasi unapochokozwa. (Soma Mathayo 5:39, 44, 45.) Basi, tunaweza jinsi gani kufuata kikamili zaidi mafundisho ya Yesu?

      Mifano Mizuri na Mibaya

      7. Ni nini kilichotukia Simeoni na Lawi walipokosa kuzuia hasira yao?

      7 Biblia ina mashauri mengi kuhusu kuzuia hasira na pia ina mifano halisi inayoonyesha matokeo ya kufanya hivyo na kutofanya hivyo. Fikiria kilichotukia wakati Simeoni na Lawi, wana wa Yakobo, walipolipiza kisasi juu ya Shekemu kwa sababu ya kumnajisi dada yao Dina. ‘Waliumia hisia zao, wakakasirika sana.’ (Mwa. 34:7) Kisha, wale wana wengine wa Yakobo wakashambulia mji wa Shekemu, wakapora vitu, na wakawateka nyara wanawake na watoto. Hawakufanya mambo yote hayo kwa sababu tu ya Dina bali pia inaelekea ni kwa sababu ya kiburi, yaani, hawakutaka kudharauliwa na wengine. Walihisi kwamba Shekemu alikuwa amewakosea na kumkosea baba yao, Yakobo. Lakini Yakobo alikuwa na maoni gani kuhusu mwenendo wao?

      8. Simulizi la Simeoni na Lawi linaonyesha nini kuhusu kulipiza kisasi?

      8 Bila shaka, msiba uliompata Dina ulimhuzunisha sana Yakobo; hata hivyo, alishutumu hatua ya watoto wake ya kulipiza kisasi. Bado Simeoni na Lawi walijaribu kutetea matendo yao, kwa kusema hivi: “Je, yeyote anapaswa kumtendea dada yetu kama kahaba?” (Mwa. 34:31) Lakini huo haukuwa mwisho wa mambo, kwa kuwa Yehova hakufurahi. Baada ya miaka mingi kupita, Yakobo alitabiri kwamba kwa sababu ya matendo ya jeuri na hasira ya Simeoni na Lawi, wazao wao wangetawanyika kati ya makabila ya Israeli. (Soma Mwanzo 49:5-7.) Ndiyo, walipoteza kibali cha Mungu na cha baba yao kwa sababu ya kutozuia hasira yao.

      9. Ni wakati gani ambapo Daudi alikuwa karibu kushindwa kuzuia hasira yake?

      9 Mfalme Daudi alitenda kwa njia tofauti kabisa. Alipata nafasi nyingi za kulipiza kisasi, lakini hakufanya hivyo. (1 Sam. 24:3-7) Hata hivyo, pindi moja alikuwa karibu kushindwa kuzuia hasira yake. Mwanamume fulani tajiri aliyeitwa Nabali aliwatukana kwa ukali wanaume wa Daudi, ingawa walikuwa wamelinda makundi ya Nabali na wachungaji wake. Akiwa amekasirika labda kwa sababu ya jinsi wanaume wake walivyotendewa, Daudi alikuwa karibu kulipiza kiasi kwa ukali. Daudi na wanaume wake walipokuwa wakienda kumshambulia Nabali na familia yake, kijana mmoja alimjulisha Abigaili, mke mwenye busara wa Nabali, kuhusu jambo lililotukia naye akamsihi achukue hatua. Papo hapo, Abigaili alichukua zawadi kubwa na kwenda kukutana na Daudi. Kwa unyenyekevu, aliomba msamaha kwa sababu ya ukaidi wa Nabali naye akamsihi Daudi kwa msingi wa kwamba Daudi alimwogopa Yehova. Daudi alirudiwa na fahamu zake naye akasema hivi: “Nawe ubarikiwe, ambaye umenizuia leo nisiingie katika hatia ya damu.”—1 Sam. 25:2-35.

      Mtazamo wa Kikristo

      10. Wakristo wanapaswa kuwa na mtazamo gani kuhusu kulipiza kisasi?

      10 Kisa cha Simeoni na Lawi na kisa cha Daudi na Abigaili kinaonyesha waziwazi kwamba Yehova anapinga hasira inayopita mipaka na jeuri na kwamba anawabariki wale wanaojitahidi kufanya amani. Mtume Paulo aliandika hivi: “Ikiwezekana, kwa kadiri inavyowategemea ninyi, iweni wenye kufanya amani na watu wote. Wapendwa, msijilipizie kisasi wenyewe bali iachieni nafasi ghadhabu; kwa maana imeandikwa: ‘Kisasi ni changu; mimi nitalipa, asema Yehova.’ Lakini, ‘ikiwa adui yako ana njaa, mlishe; ikiwa ana kiu, mpe kitu anywe; kwa maana kwa kufanya hivyo utakusanya makaa yenye moto juu ya kichwa chake.’ Usiache ushindwe na uovu, bali endelea kuushinda uovu kwa wema.”—Rom. 12:18-21.a

      11. Dada mmoja alijifunza jinsi gani kuzuia hasira yake?

      11 Tunaweza kutumia shauri hilo. Kwa mfano, dada mmoja alilalamika kwa mzee wa kutaniko lao kuhusu msimamizi wake mpya kazini ambaye ni mwanamke. Dada huyo alisema kwamba msimamizi huyo alimwonea na hakumtendea kwa fadhili. Dada huyo alimkasirikia sana mwanamke huyo na alitaka kuacha kazi. Mzee huyo alimshauri asifanye uamuzi wa haraka-haraka. Mzee alitambua kwamba mambo yalizidi kuwa mabaya wakati dada huyo alipokasirika kwa sababu ya kutendewa vibaya na msimamizi wake. (Tito 3:1-3) Mzee alimwambia dada huyo kwamba hata ikiwa mwishowe angepata kazi nyingine, bado angehitaji kubadili njia yake ya kukabiliana na matendo yasiyo ya fadhili. Alimshauri dada huyo amtendee msimamizi wake jinsi ambavyo angependa kutendewa, kama Yesu alivyotufundisha tufanye. (Soma Luka 6:31.) Dada huyo alikubali kwamba angejaribu kufanya hivyo. Matokeo yakawa nini? Baada ya muda, yule msimamizi alibadili mtazamo wake akawa mwenye fadhili, na hata alimshukuru dada huyo kwa sababu ya kazi yake.

      12. Kwa nini kutoelewana kati ya Wakristo kunaweza kutokeza maumivu zaidi?

      12 Huenda tusishangae tukitendewa hivyo na mtu ambaye si mshiriki wa kutaniko la Kikristo. Tunajua kwamba mara nyingi tunatendewa kwa njia isiyo ya haki kwa kuwa tunaishi katika mfumo huu wa Shetani na hivyo tunahitaji kujitahidi ili watenda-dhambi wasitukasirishe. (Zab. 37:1-11; Mhu. 8:12, 13; 12:13, 14) Hata hivyo, matatizo yanapotokea kati yetu na ndugu na dada yetu wa kiroho tunaumia sana moyoni. Shahidi mmoja alikumbuka hivi: “Tatizo kubwa zaidi ambalo nilikabili nilipoingia katika kweli lilikuwa kukubali uhakika wa kwamba watu wa Yehova si wakamilifu.” Tulitoka katika ulimwengu usio na upendo na usiojali, tukitumaini kwamba watu wote katika kutaniko wangetendeana kwa fadhili ya Kikristo. Hivyo, Mkristo mwenzetu, hasa yule aliye na mapendeleo katika kutaniko, akitutendea bila kufikiri au kwa njia isiyo ya Kikristo, tunaweza kuumia au kukasirika. Huenda tukajiuliza: ‘Mambo kama hayo yanaweza kutokea jinsi gani kati ya watu wa Yehova?’ Kwa kweli, mambo kama hayo yalitokea hata kati ya Wakristo watiwa-mafuta katika siku za mitume. (Gal. 2:11-14; 5:15; Yak. 3:14, 15) Tunapaswa kufanya nini tukitendewa hivyo?

      13. Tunapaswa kushirikiana kusuluhisha tofauti zetu jinsi gani na kwa nini?

      13 Dada aliyetajwa hapo juu alisema hivi: “Nilijifunza kusali kwa ajili ya mtu yeyote anayeniumiza moyoni. Sikuzote kufanya hivyo kunanisaidia.” Kama vile ambavyo tayari tumesoma, Yesu alitufundisha kusali kwa ajili ya wale wanaotutesa. (Mt. 5:44) Basi, je, hatupaswi kusali hata zaidi kwa ajili ya ndugu na dada zetu wa kiroho? Kama vile baba anavyotaka watoto wake wapendane, ndivyo Yehova anavyotaka watumishi wake duniani wawe na uhusiano mzuri kati yao. Tunatazamia kwa hamu kuishi pamoja kwa amani na furaha milele, na Yehova anatufundisha kufanya hivyo sasa. Anataka tushirikiane katika kufanya kazi yake kuu. Kwa hiyo, acheni tusuluhishe matatizo au ‘tupite’ tu makosa na kusonga mbele kwa umoja. (Soma Methali 19:11.) Badala ya kujitenga na ndugu zetu tunapokosana, tunapaswa kusaidiana kubaki kati ya watu wa Mungu, na kukaa kwa usalama katika “mikono ya milele” ya Yehova.—Kum. 33:27, American Standard Version.

      Kuwa Wapole kwa Wote Kunaleta Matokeo Mazuri

      14. Tunaweza kupambana jinsi gani na uvutano wa Shetani unaotokeza migawanyiko?

      14 Ili kutuzuia tusieneze habari njema, Shetani na roho wake waovu wanajaribu sana kuvuruga familia na makutaniko yenye furaha. Wanajaribu kuleta migawanyiko, kwa kuwa wanajua kwamba migawanyiko ya ndani inaweza kusababisha uharibifu. (Mt. 12:25) Ili tushinde uvutano wao mwovu, tunapaswa kufuata shauri hili la Paulo: “Mtumwa wa Bwana hahitaji kupigana, bali anahitaji kuwa mpole kwa wote.” (2 Tim. 2:24) Kumbuka kwamba vita vyetu si, “juu ya damu na mwili, bali . . . juu ya majeshi ya roho waovu.” Ili tufanikiwe katika vita hivi, tunahitaji kuvaa mavazi ya silaha za kiroho, ambayo yanatia ndani “viatu vya habari njema ya amani.”—Efe. 6:12-18.

      15. Tunapaswa kutenda namna gani tukishambuliwa kutoka nje ya kutaniko?

      15 Maadui wa Yehova wanawashambulia vikali watu wake wenye amani kutoka nje ya kutaniko. Wengine kati ya maadui hao wanawashambulia kimwili Mashahidi wa Yehova. Wengine wanaeneza uwongo kutuhusu katika vyombo vya habari na mahakamani. Yesu aliwaambia wafuasi wake watazamie mambo hayo. (Mt. 5:11, 12) Tunapaswa kutenda namna gani? Hatupaswi kamwe ‘kulipa uovu kwa uovu,’ kwa maneno au kwa matendo.—Rom. 12:17; soma 1 Petro 3:16.

      16, 17. Kutaniko moja lilikabili hali gani yenye kujaribu?

      16 Hata Ibilisi akituletea majaribu gani, tunaweza kutoa ushahidi mzuri kwa “kuushinda uovu kwa wema.” Kwa mfano, kutaniko moja kwenye kisiwa kimoja cha Pasifiki lilikodi jumba fulani kwa ajili ya Ukumbusho. Wakuu wa kanisa moja walipopata habari hizo, waliwaambia wafuasi wa kanisa lao wakusanyike katika jumba hilo kwa ajili ya ibada ya kanisa siku yetu ya kuadhimisha Ukumbusho. Hata hivyo, mkuu wa polisi aliwaamuru wakuu wa kanisa hilo waondoke kwenye jumba hilo wakati huo ili Mashahidi walitumie. Lakini, wakati ulipofika, wafuasi wa kanisa hilo walijaa ndani ya jumba hilo na wakaanza ibada yao.

      17 Polisi walipokuwa wakijitayarisha kuwafukuza kwa nguvu kutoka katika jumba hilo, msimamizi wa kanisa hilo alimfikia mzee wetu mmoja na kumuuliza hivi: “Je, mmepanga kufanya jambo lolote la pekee leo jioni?” Ndugu huyo alimwambia kuhusu Ukumbusho, na mwanamume huyo akamjibu hivi: “Oh, sikujua!” Papo hapo, polisi mmoja akasema hivi: “Lakini tuliwaambia leo asubuhi!” Kiongozi huyo wa kanisa alimgeukia yule mzee huku akitabasamu kwa dhihaka na kumuuliza hivi: “Sasa mtafanya nini? Watu wetu wamejaa katika jumba hili. Je, mtawaambia polisi watufukuze?” Alibadili mambo kwa ujanja ili ionekane kwamba Mashahidi ndio waliokuwa wakiwatesa! Ndugu zetu wangefanya nini?

      18. Ndugu zetu walifanya nini walipokasirishwa, na matokeo yakawa nini?

      18 Mashahidi waliamua kuruhusu kanisa hilo lifanye ibada ya dakika 30, na baadaye akina ndugu waadhimishe Ukumbusho. Ibada ya kanisa hilo ilipita wakati, lakini baada ya wafuasi wa kanisa hilo kuondoka, ndugu waliadhimisha Ukumbusho. Siku iliyofuata, serikali iliunda halmashauri rasmi ya kuchunguza jambo hilo. Baada ya kuchunguza ukweli wa mambo, halmashauri hiyo iliagiza kanisa hilo litangaze kwamba kiongozi wa kanisa hilo ndiye aliyesababisha tatizo hilo bali si Mashahidi. Halmashauri hiyo pia iliwashukuru Mashahidi wa Yehova kwa sababu ya kushughulikia hali hiyo ngumu kwa subira. Jitihada za Mashahidi za “kufanya amani na watu wote” zilikuwa na matokeo mazuri.

  • Maneno Yenye Neema Yanadumisha Mahusiano Mazuri
    Mnara wa Mlinzi—2010 | Juni 15
    • Maneno Yenye Neema Yanadumisha Mahusiano Mazuri

      “Maneno yenu na yawe yenye neema sikuzote.”—KOL. 4:6.

      1, 2. Ndugu mmoja alipata matokeo gani mazuri alipotumia maneno yenye neema?

      NDUGU mmoja anaripoti hivi: “Nilipokuwa nikihubiri nyumba kwa nyumba, nilikutana na mwanamume fulani ambaye alikasirika sana hivi kwamba midomo yake na mwili wake wote ulitetemeka. Nilijaribu kuzungumza naye kwa utulivu kwa kutumia Maandiko, lakini hasira yake iliendelea tu kupanda. Mke na watoto wake walijiunga naye kunishambulia kwa maneno, hivyo nikaona kwamba ni wakati wa kuondoka. Niliihakikishia familia hiyo kwamba nilikuja kwa amani na ningependa kwenda kwa amani. Niliwaonyesha andiko la Wagalatia 5:22 na 23, ambalo linataja upendo, upole, kujizuia, na amani. Kisha nikaondoka.

      2 “Baadaye, nilipotembelea nyumba zilizokuwa upande wa pili wa barabara, niliona familia hiyo ikiwa imeketi mbele ya mlango wa nyumba yao. Waliniita. Nikajiuliza, ‘Sasa kuna nini?’ Mwanamume huyo alikuwa na kopo la maji baridi akaniuliza ikiwa nilitaka maji ya kunywa. Aliniomba msamaha kwa sababu ya kunishambulia kwa maneno kisha akanipongeza kwa sababu ya imani yangu yenye nguvu. Tuliachana kwa amani.”

      3. Kwa nini hatupaswi kuwaruhusu wengine watukasirishe?

      3 Katika ulimwengu wa leo uliojaa mikazo, kwa kawaida hatuwezi kuepuka kukutana na watu wenye hasira, hata katika huduma yetu. Tunapokutana nao, ni jambo la maana kwetu kuonyesha “tabia-pole na heshima kubwa.” (1 Pet. 3:15) Kama ndugu aliyetajwa hapo juu angeruhusu hasira na ukosefu wa fadhili wa wenye nyumba umchochee kukasirika, inaelekea kwamba mtazamo wa yule mwanamume haungebadilika; huenda angekasirika hata zaidi. Lakini kwa sababu ndugu huyo alijizuia na kusema maneno yenye neema, matokeo yalikuwa mazuri.

      Ni Nini Kinachofanya Maneno Yawe Yenye Neema?

      4. Kwa nini ni jambo la maana kutumia maneno yenye neema?

      4 Iwe tunashughulika na watu walio nje au ndani ya kutaniko, hata na washiriki wa familia yetu, ni jambo la maana sana kufuata shauri hili la mtume Paulo: “Maneno yenu na yawe yenye neema sikuzote, yenye kukolezwa chumvi.” (Kol. 4:6) Maneno hayo yenye kupendeza na yanayofaa yanadumisha amani na mahusiano mazuri.

      5. Kuzungumza waziwazi hakumaanishi nini? Toa mfano.

      5 Kuzungumza waziwazi hakumaanishi kusema jambo lolote ambalo unafikiria na kuhisi wakati wowote ule, hasa unapokasirika. Maandiko yanasema kwamba mtu anayeonyesha hasira bila kujizuia anathibitisha kwamba ana udhaifu bali si nguvu. (Soma Methali 25:28; 29:11.) Musa ambaye alikuwa “mpole zaidi” kuliko watu wote walioishi siku zake, pindi moja aliruhusu uasi wa taifa la Israeli umfanye akasirike na kukosa kumpa Mungu utukufu. Musa alisema waziwazi jinsi alivyohisi, lakini Yehova hakufurahi. Baada ya kuwaongoza Waisraeli kwa miaka 40, Musa alipoteza pendeleo la kuwaingiza katika Nchi ya Ahadi.—Hes. 12:3; 20:10, 12; Zab. 106:32.

      6. Kuzungumza kwa busara kunamaanisha nini?

      6 Maandiko yanawapongeza watu ambao wanajizuia na kuzungumza kwa busara au hekima. “Katika wingi wa maneno hapakosi kuwa na kosa, lakini anayezuia midomo yake anatenda kwa busara.” (Met. 10:19; 17:27) Hata hivyo, kutumia busara hakumaanishi kwamba mtu hapaswi kamwe kutoa maoni yake. Kunamaanisha kuongea kwa “neema,” na kutumia ulimi kuponya badala ya kuumiza.—Soma Methali 12:18; 18:21.

      “Wakati wa Kukaa Kimya na Wakati wa Kusema”

      7. Ni maneno ya aina gani ambayo hatupaswi kusema, na kwa nini?

      7 Kama vile tu tunavyohitaji kutumia maneno yenye neema na kujizuia tunapozungumza na wafanyakazi wenzetu au watu tusiowajua katika huduma, tunahitaji pia kufanya hivyo kutanikoni na nyumbani. Tunapomwaga hasira bila kujali matokeo ya kufanya hivyo tunaweza kujiumiza na kuwaletea wengine madhara makubwa sana ya kiroho, kihisia, na kimwili. (Met. 18:6, 7) Ni lazima tuzuie hisia mbaya ambazo zinasababishwa na hali yetu ya kutokamilika. Maneno ya matukano, dhihaka, dharau, na maneno ya hasira yenye chuki hayafai kamwe. (Kol. 3:8; Yak. 1:20) Yanaweza kuharibu mahusiano yenye thamani sana na watu wengine na pamoja na Yehova. Yesu alifundisha hivi: “Kila mtu anayeendelea kuwa na ghadhabu na ndugu yake atatoa hesabu mahakamani; lakini yeyote yule anayemwambia ndugu yake neno la dharau lisilosemeka atatoa hesabu katika Mahakama Kuu Zaidi; na yeyote yule anayesema, ‘Wewe mpumbavu wa kudharauliwa!’ atastahili Gehena ya moto.”—Mt. 5:22.

      8. Ni wakati gani tunapopaswa kusema jinsi tunavyohisi, lakini kwa njia gani?

      8 Hata hivyo, kuna mambo fulani ambayo tunaweza kuona kwamba ni vizuri kuyasema. Ikiwa ndugu fulani amesema au kufanya jambo fulani ambalo limekuumiza sana hivi kwamba huwezi kuliachilia tu, usiruhusu hisia za chuki zisitawi katika moyo wako. (Met. 19:11) Mtu akikukasirisha, zuia hisia zako kisha uchukue hatua zinazofaa ili kutatua tatizo hilo. Paulo aliandika hivi: “Jua lisitue mkiwa katika hali ya kuchokozeka.” Kwa kuwa tatizo hilo linaendelea kukuumiza, lishughulikie kwa fadhili wakati unaofaa. (Soma Waefeso 4:26, 27, 31, 32.) Zungumza na ndugu yako kuhusu jambo hilo waziwazi lakini ukitumia maneno yenye neema, ukiwa na kusudi la kupatana naye.—Law. 19:17; Mt. 18:15.

      9. Kwa nini tunapaswa kuzuia hisia zetu kabla ya kuzungumza na wengine?

      9 Bila shaka, unapaswa kuchagua kwa uangalifu wakati unaofaa. Kuna “wakati wa kukaa kimya na wakati wa kusema.” (Mhu. 3:1, 7) Zaidi ya hayo, “moyo wa mwadilifu hutafakari ili kujibu.” (Met. 15:28) Huenda ukahitaji kungoja ili mzungumze na kusuluhisha matatizo hayo. Mambo yanaweza kuharibika zaidi mkizungumza wakati bado mmekasirika sana; lakini pia si jambo la hekima kungoja kwa muda mrefu sana.

      Matendo ya Fadhili Yanadumisha Mahusiano Mazuri

      10. Kuwatendea wengine kwa fadhili kunaweza kuboresha mahusiano jinsi gani?

      10 Kusema maneno yenye neema na kuzungumza kwa njia nzuri kunaweza kusitawisha na kudumisha mahusiano yenye amani. Kwa kweli, kufanya yote tunayoweza ili kuboresha mahusiano yetu na wengine kunaweza kuboresha mazungumzo yetu pamoja nao. Kuchukua hatua ya kuwatendea wengine mambo ya fadhili kutoka moyoni, na kutafuta nafasi za kuwasaidia, kuwapa zawadi kwa nia nzuri, na kuwakaribisha, kunaweza kuchangia mazungumzo mazuri. Hata kunaweza ‘kukusanya makaa yenye moto’ juu ya mtu na kumfanya aonyeshe sifa nzuri, na hivyo inakuwa rahisi zaidi kuzungumza waziwazi na kusuluhisha matatizo.—Rom. 12:20, 21.

      11. Yakobo alichukua hatua gani ili kuboresha uhusiano wake na Esau, na matokeo yalikuwa nini?

      11 Mzee wa ukoo Yakobo alielewa jambo hilo. Esau, ndugu yake pacha, alimkasirikia sana hivi kwamba Yakobo akakimbia kwa sababu aliogopa kuwa Esau angemuua. Baada ya miaka mingi kupita, Yakobo alirudi. Esau alienda na wanaume 400 ili akutane naye. Yakobo alisali ili Yehova amsaidie. Kisha, kabla ya kukutana na Esau, akapeleka zawadi kubwa ya wanyama wa kufugwa. Zawadi hiyo ilitimiza kusudi lake. Walipokutana, moyo wa Esau ulikuwa umebadilika, akakimbia na kumkumbatia Yakobo.—Mwa. 27:41-44; 32:6, 11, 13-15; 33:4, 10.

      Watie Moyo Wengine kwa Maneno Yenye Neema

      12. Kwa nini tunapaswa kutumia maneno yenye neema tunapozungumza na ndugu zetu?

      12 Wakristo wanamtumikia Mungu, bali si wanadamu wenzao. Hata hivyo, tuna tamaa ya asili ya kukubaliwa na wengine. Maneno yetu yenye neema yanaweza kupunguza mizigo ya ndugu na dada zetu. Hata hivyo, kuwachambua kwa ukali kunaweza kufanya mizigo hiyo iwe mizito zaidi na hata kuwafanya wengine wafikiri kwamba wamepoteza kibali cha Yehova. Kwa hiyo, acheni tuwaambie wengine kwa unyoofu mambo yenye kutia moyo, “neno lolote ambalo ni jema kwa ajili ya kujenga kulingana na uhitaji, ili liwape wasikiaji lile linalofaa.”—Efe. 4:29.

      13. Wazee wanapaswa kukumbuka nini (a) wanapotoa shauri? (b) wanapoandika barua?

      13 Wazee, hasa, wanapaswa kuwa “wapole” na kulitendea kundi kwa wororo. (1 The. 2:7, 8) Wazee wanapohitajika kutoa shauri, kusudi lao ni kufanya hivyo kwa “upole,” hata wanapoongea na wale “wasio na mwelekeo unaofaa.” (2 Tim. 2:24, 25) Wazee wanapaswa pia kutumia maneno yenye neema wanapoandikia baraza lingine la wazee au ofisi ya tawi. Wanapaswa kuwa wenye fadhili na busara, kama tunavyosoma katika andiko la Mathayo 7:12.

      Kutumia Maneno Yenye Neema Katika Familia

      14. Paulo anawapa waume shauri gani, na kwa nini?

      14 Ni rahisi kufikiri kwamba maneno yetu, ishara zetu za uso na za mwili hazina matokeo yoyote juu ya watu wengine. Kwa mfano, huenda wanaume fulani wasijue kikamili jinsi maneno yao yanavyowaumiza sana wanawake. Dada mmoja alisema hivi: “Ninashtuka wakati mume wangu anaponifokea kwa hasira.” Maneno makali yanaweza kumuumiza sana mwanamke kuliko mwanamume na huenda akayakumbuka kwa muda mrefu. (Luka 2:19) Na jambo hilo ni la kweli hasa inapohusu maneno yanayosemwa na mtu fulani ambaye mwanamke anampenda na anataka kumheshimu. Paulo aliwashauri hivi waume: “Endeleeni kuwapenda wake zenu nanyi msiwakasirikie kwa uchungu.”—Kol. 3:19.

      15. Toa mfano ambao unaonyesha kwa nini mume anapaswa kumtendea mke wake kwa upole.

      15 Kuhusu jambo hilo, ndugu mmoja mwenye uzoefu ambaye ameoa alitoa mfano unaoonyesha kwa nini mume anapaswa kumtendea mke wake kwa upole, kama “chombo dhaifu zaidi.” Alisema hivi: “Unapobeba chombo chenye thamani kinachoweza kuvunjika kwa urahisi, hupaswi kukishika kwa nguvu sana, kinaweza kuvunjika. Hata kikirekebishwa, huenda alama hiyo bado itaonekana. Mume akimwambia mke wake maneno makali sana, anaweza kumuumiza. Hilo linaweza kusababisha madhara yenye kudumu katika uhusiano wao.”—Soma 1 Petro 3:7.

      16. Mke anaweza kujenga familia yake jinsi gani?

      16 Wanaume pia wanaweza kutiwa moyo au kuvunjwa moyo na maneno ya watu wengine, kutia ndani na wake zao. “Mke mwenye busara,” ambaye mume wake anaweza kwa kweli ‘kumtegemea,’ anajali hisia za mume, kama vile anavyotaka mume ajali hisia zake. (Met. 19:14; 31:11) Kwa kweli, mke anaweza kuwa na uvutano mkubwa katika familia, kwa njia nzuri au mbaya. “Mwanamke mwenye hekima kwelikweli amejenga nyumba yake, lakini aliye mpumbavu huibomoa kwa mikono yake mwenyewe.”—Met. 14:1.

      17. (a) Watoto wanapaswa kuzungumza jinsi gani na wazazi wao? (b) Watu wazima wanapaswa kuzungumza jinsi gani na watoto, na kwa nini?

      17 Wazazi na pia watoto wanapaswa kutumia maneno yenye neema wanapozungumza pamoja. (Mt. 15:4) Ufikirio utatusaidia kuepuka ‘kuwakasirisha’ au kuwachokoza watoto tunapozungumza nao. (Kol. 3:21; Efe. 6:4) Hata ikiwa ni lazima watoto watiwe nidhamu, wazazi na wazee wanapaswa kuzungumza nao kwa heshima. Kwa njia hiyo, watu wazima wanafanya iwe rahisi zaidi kwa vijana kurekebisha mwenendo wao na kudumisha urafiki wao pamoja na Mungu. Kufanya hivyo ni bora zaidi kuliko kuonyesha kwamba tumechoka nao, jambo ambalo linaweza kuwavunja moyo. Huenda watoto wasikumbuke mashauri yote waliyopewa, lakini watakumbuka jinsi wengine walivyozungumza nao.

      Kusema Mambo Mazuri Kutoka Moyoni

      18. Tunaweza kuondoa jinsi gani mawazo na hisia zenye kuumiza?

      18 Kuzuia hasira hakumaanishi tu kuonekana kwa nje kuwa mtulivu. Kusudi letu halipaswi kuwa tu kutuliza hasira yetu kali. Tunapata mkazo tunapojifanya kuwa watulivu kwa nje huku tukichemka kwa hasira moyoni. Ni kama kujaribu kukanyaga breki ya gari na wakati huohuo kujaribu kuliendesha gari hilo. Kufanya hivyo kunaweza kuliharibu gari. Kwa hiyo, usifungie hasira moyoni na kuiacha ilipuke baadaye. Sali ili Yehova akusaidie kuondoa hisia zenye kuumiza moyoni mwako. Acha roho ya Yehova igeuze akili na moyo wako kupatana na mapenzi yake.—Soma Waroma 12:2; Waefeso 4:23, 24.

      19. Ni hatua gani zinazoweza kutusaidia kuepuka ugomvi wenye hasira?

      19 Chukua hatua zinazofaa. Ukikabili hali yenye kufadhaisha ambayo inakuchochea kukasirika, huenda ikafaa uondoke mahali hapo, ili upate wakati wa kutuliza hasira yako. (Met. 17:14) Ikiwa mtu unayeongea naye anaanza kukasirika, jitahidi sana kutumia maneno yenye neema. Kumbuka: “Jibu, linapokuwa la upole, hugeuza ghadhabu, lakini neno linaloumiza hufanya hasira ipande.” (Met. 15:1) Maneno makali au yenye kuumiza yataongeza kuni kwenye moto hata ikiwa yatasemwa kwa sauti ya upole. (Met. 26:21) Kwa hiyo, hali fulani inapojaribu sifa yako ya kujizuia, uwe “mwepesi wa kusema, si mwepesi wa ghadhabu.” Sali ili roho ya Yehova ikusaidie kusema mambo mazuri, wala si mabaya.—Yak. 1:19.

      Kusamehe Kutoka Moyoni

      20, 21. Ni nini kinachoweza kutusaidia kuwasamehe wengine, na kwa nini ni lazima tufanye hivyo?

      20 Inahuzunisha kwamba hakuna yeyote kati yetu anayeweza kuuzuia kikamili ulimi wake. (Yak. 3:2) Hata wakijitahidi kadiri gani, nyakati nyingine washiriki wa familia yetu na ndugu na dada zetu wa kiroho wapendwa wanaweza kusema bila kufikiri maneno ambayo yanatuumiza hisia. Badala ya kukasirika haraka, fikiria kwa subira sababu zilizowafanya waseme mambo hayo. (Soma Mhubiri 7:8, 9.) Je, walikuwa na mkazo, woga, hawakuwa wakijisikia vizuri, au walikuwa wakipambana na tatizo fulani mwilini mwao au kutoka chanzo kingine?

      21 Mambo kama hayo si kisingizio cha kumwaga hasira. Lakini tukitambua mambo hayo, tunaweza kuelewa kwa nini nyakati nyingine watu wanasema na kufanya mambo ambayo hayafai na hilo linaweza kutuchochea kuwasamehe. Sote tunasema au kufanya mambo ambayo yanawaumiza wengine, na tunatumaini kwamba watatusamehe kwa fadhili. (Mhu. 7:21, 22) Yesu alisema kwamba ili Mungu atusamehe, ni lazima tuwasamehe wengine. (Mt. 6:14, 15; 18:21, 22, 35) Kwa hiyo, tunapaswa kuomba haraka msamaha na kuwasamehe wengine haraka, na hivyo kudumisha upendo, ambao ni “kifungo kikamilifu cha muungano,” katika familia na katika kutaniko.—Kol. 3:14.

      22. Kwa nini jitihada zetu za kutumia maneno yenye neema si za bure?

      22 Inaelekea kwamba itakuwa vigumu zaidi kudumisha shangwe na umoja wetu kadiri mfumo huu wa mambo uliojaa watu wenye hasira unavyokaribia mwisho wake. Kufuata kanuni bora za Neno la Mungu kutatusaidia kutumia ulimi wetu kusema mambo mazuri, bali si mabaya. Tutafurahia mahusiano mazuri katika kutaniko na katika familia, na mfano wetu utawatolea wengine ushahidi mzuri sana kumhusu ‘Mungu wetu mwenye furaha,’ Yehova.—1 Tim. 1:11.

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki