-
Kupiga Mbiu ya Kurudi kwa BwanaMashahidi wa Yehova—Wapiga-Mbiu wa Ufalme wa Mungu
-
-
Kwa miongo ya miaka Russell na washirika wake walikuwa wamekuwa wakipiga mbiu kwamba Nyakati za Mataifa zingekoma katika 1914. Matarajio yalikuwa makubwa. C. T. Russell alikuwa amechambua wale waliokuwa wameweka tarehe mbalimbali za kurudi kwa Bwana, kama vile William Miller na baadhi ya vikundi vya Waadventisti wa Pili. Hata hivyo, tangu wakati wa ushirika wake wa mapema na Nelson Barbour, yeye alisadiki kwamba kulikuwa na kronolojia iliyokuwa sahihi, ikitegemea Biblia, na kwamba ilielekeza kwenye mwaka 1914 kuwa mwisho wa Nyakati za Mataifa.
Mwaka huo wenye maana kubwa ulipokuwa ukikaribia, kulikuwa na matarajio makubwa miongoni mwa Wanafunzi wa Biblia, lakini yote waliyokuwa wakitarajia hayakuwa yamesemwa moja kwa moja katika Maandiko.
-
-
Wakati wa Kutahini (1914-1918)Mashahidi wa Yehova—Wapiga-Mbiu wa Ufalme wa Mungu
-
-
Matarajio Makubwa
Katika Juni 28, 1914, Dyuki-Mkuu Francis Ferdinand wa Austria-Hungaria alipigwa risasi na kuuawa na mwuaji. Uuaji huo ulifyatusha ile Vita Kuu, kama vile Vita ya Ulimwengu 1 ilivyoitwa hapo kwanza. Vita ilianza katika Agosti 1914 wakati Ujerumani ilipovamia Ubelgiji na Ufaransa. Kufikia vuli ya mwaka huo, vita yenye umwagaji-damu mwingi sana ilikuwa imeanza.
“Nyakati za Mataifa zimekwisha; siku za wafalme wao zimekwisha”! Ndivyo Ndugu Russell alivyopaaza sauti alipokuwa akiingia chumba cha kulia kwenye makao makuu ya Brooklyn ya Watch Tower Society, asubuhi ya Ijumaa, Oktoba 2, 1914. Msisimko ulikuwa mwingi. Wengi zaidi kati ya hao waliokuwapo walikuwa wametazamia kwa miaka mingi mwaka wa 1914. Lakini mwisho wa Nyakati za Mataifa ungeleta nini?
Vita ya Ulimwengu 1 ilikuwa inachacha, na katika wakati huo ilikuwa imeaminiwa kwamba vita hiyo ilikuwa ikiongoza kuingia kwenye wakati wa machafuko ya utawala ya duniani pote ambayo yangetokeza mwisho wa mfumo wa mambo uliopo. Pia kulikuwa na matarajio mengine kuhusu mwaka 1914. Alexander H. Macmillan, ambaye alikuwa amebatizwa Septemba 1900, alikumbuka baadaye hivi: “Wachache kati yetu tulifikiri kwa uzito sana kwamba tungeenda mbinguni wakati wa juma la kwanza la mwezi huo wa Oktoba.”a Kwa kweli, akikumbuka asubuhi ambayo Russell alitangaza mwisho wa Nyakati za Mataifa, Macmillan alikubali hivi: “Tulisisimka sana sana, nami singeshangaa kama katika nukta hiyo tungeanza tu kupaa, huku tangazo la Russell likiwa ni ishara ya kuanza kupaa kuelekea mbinguni—lakini bila shaka hakukuwa na jambo lolote kama hilo.”
Matarajio yaliyokatishwa tamaa kwa habari ya kurudi kwa Bwana Yesu katika karne ya 19 yalikuwa yamesababisha wafuasi wengi wa William Miller na vikundi vingine vya Waadventisti kupoteza imani. Lakini namna gani juu ya Wanafunzi wa Biblia walioshirikiana na Russell? Je, baadhi yao walikuwa wamevutwa na wazo la wokovu wao wenyewe wa mapema badala ya kumpenda Mungu na tamaa yenye nguvu ya kufanya mapenzi yake?
‘Ndugu Russell, Je, Wewe Hukukatishwa Tamaa?’
Ndugu Russell alikuwa amekuwa akitia moyo Wanafunzi wa Biblia waendelee kukaa macho na kuazimia kuendelea katika kazi ya Bwana hata kama mambo hayatakamilika upesi kama wao walivyokuwa wametarajia.
Oktoba 1914 ukapita, na C. T. Russell na washirika wake walikuwa wangali duniani. Kisha Oktoba 1915 ukapita. Je, Russell alikatishwa tamaa? Katika The Watch Tower la Februari 1, 1916, yeye aliandika hivi: “‘Lakini, Ndugu Russell, wazo lako ni nini kuhusu wakati wa kubadilika kwetu? Je, wewe hukukatishwa tamaa kwamba huo hukuja tulipoutazamia kwamba ungekuja?’ mtauliza. Hapana, twajibu, sisi hatukukatishwa tamaa. . . . Ndugu, wale miongoni mwetu walio na maoni yafaayo kuelekea Mungu hawakatishwi tamaa na mipango yoyote Yake. Sisi hatukutaka mapenzi yetu wenyewe yafanyike; hivyo wakati tulipopata kujua kwamba tulikuwa tukitarajia jambo lenye kosa katika Oktoba, 1914, basi tulifurahi kwamba Bwana hakubadili Mpango Wake utufae sisi. Sisi hatukutaka Yeye afanye hivyo. Sisi twataka tu tuweze kuelewa mipango na makusudi Yake.”
Hapana, Wanafunzi wa Biblia ‘hawakuchukuliwa nyumbani’ mbinguni katika Oktoba 1914. Hata hivyo, Nyakati za Mataifa zilikwisha katika mwaka huo. Kwa wazi, Wanafunzi wa Biblia walikuwa na mengi ya kujifunza kuhusu umaana wa mwaka 1914. Kwa wakati huohuo, wafanye nini? Wafanye kazi! Kama vile The Watch Tower la Septemba 1, 1916, lilivyoeleza jambo hilo: “Sisi tuliwazia kwamba kazi ya Mavuno ya kukusanya kuleta ndani Kanisa [la watiwa-mafuta] ingekamilishwa kabla ya mwisho wa Nyakati za Mataifa; lakini hamkuwa na lolote katika Biblia lililosema hivyo. . . . Je, sisi twasikitika kwa sababu kazi ya Mavuno yaendelea? Hapana, hakika . . . Maoni yetu ya sasa, ndugu wapendwa, yapasa kuwa ya shukrani nyingi kuelekea Mungu, uthamini wenye kuongezeka wa Kweli nzuri ajabu ambayo Yeye ametujalia pendeleo la kuiona na kuhusianishwa nayo, na bidii yenye kuongezeka katika kupeleka Kweli hiyo kwa wengine waijue.”
-
-
Wakati wa Kutahini (1914-1918)Mashahidi wa Yehova—Wapiga-Mbiu wa Ufalme wa Mungu
-
-
[Sanduku katika ukurasa wa 62]
“Baadhi Yetu Tulikuwa Tumekuwa Kidogo Wenye Haraka Mno”
Oktoba 1914 ulipokuwa ukikaribia, baadhi ya Wanafunzi wa Biblia walitarajia kwamba mwishoni mwa Nyakati za Mataifa, wao, wakiwa Wakristo watiwa-mafuta kwa roho, wangepokea thawabu yao ya kimbingu. Kuonyesha hilo ni tukio moja lililotukia katika mkusanyiko mmoja wa Wanafunzi wa Biblia katika Saratoga Springs, New York, Septemba 27-30, 1914. A. H. Macmillan, aliyekuwa amebatizwa miaka 14 mapema, alitoa hotuba Jumatano, Septemba 30. Katika kuitoa aliarifu hivi: “Labda hii ndiyo hotuba ya watu wote ya mwisho ambayo nitapata kutoa kwa sababu tutaenda nyumbani [mbinguni] karibuni.”
Hata hivyo, siku mbili baadaye (Ijumaa, Oktoba 2), Macmillan alitaniwa kwa uchangamfu katika Brooklyn, ambako wajumbe wa mkusanyiko wangekusanyika tena. Akiwa katika kiti chake kichwani pa meza, C. T. Russell alitangaza hivi: “Tutafanya mabadiliko fulani katika programu ya Jumapili [Oktoba 4]. Wakati wa saa 4:30 asubuhi ya Jumapili Ndugu Macmillan atatutolea hotuba.” Itikio likawaje? Macmillan aliandika baadaye hivi: “Kila mtu aliangua kicheko, wakikumbuka niliyokuwa nimesema Jumatano katika Saratoga Springs—‘hotuba yangu ya mwisho ya watu wote’!”
“Basi,” Macmillan akaendelea, “wakati huo ikawa lazima nishughulike kupata jambo la kusema. Nilipata Zaburi 74:9, ‘Hatuzioni ishara zetu, wala sasa hakuna nabii, wala kwetu hakuna ajuaye, hata lini.’ Ahaa! Hilo lilikuwa tofauti. Katika hotuba hiyo nilijaribu kuonyesha akina ndugu kwamba labda baadhi yetu tulikuwa tumekuwa kidogo wenye haraka mno katika kufikiri kwamba tungeenda mbinguni mara hiyo, na jambo linalotufaa kufanya ni kuendelea kujishughulisha na utumishi wa Bwana mpaka yeye aamue ni wakati gani yeyote kati ya watumishi wake waliokubaliwa angechukuliwa nyumbani kwenda mbinguni.”
-