Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Kukua Katika Ujuzi Sahihi Juu ya Kweli
    Mashahidi wa Yehova—Wapiga-Mbiu wa Ufalme wa Mungu
    • Mwisho wa Nyakati za Mataifa

      Kwa muda mrefu habari ya kronolojia ya Biblia ilikuwa imewavutia sana wanafunzi wa Biblia. Waelezaji walikuwa wameonyesha maoni mbalimbali juu ya unabii wa Yesu kuhusu “nyakati za Mataifa” na maandishi ya Danieli juu ya ndoto ya Nebukadreza kuhusu kile kisiki cha mti kilichofungwa kwa pingu muda wa “nyakati saba.”—Luka 21:24, KJ; Dan. 4:10-17.

      Mapema kama 1823, John A. Brown, ambaye kitabu chake kilitangazwa katika London, Uingereza, alihesabu zile “nyakati saba” za Danieli sura ya 4 kuwa zenye urefu wa miaka 2,520. Lakini yeye hakutambua waziwazi tarehe ambayo kipindi hicho cha wakati wa kiunabii kilianza au wakati kingekoma. Hata hivyo, yeye alihusianisha hizo “nyakati saba” na Nyakati za Mataifa za Luka 21:24. Katika 1844, E. B. Elliott, kasisi Mwingereza, alivuta uangalifu kwenye 1914 kuwa tarehe iwezekanayo kuwa ukomo wa “nyakati saba” za Danieli, lakini yeye alionyesha pia maoni tofauti yaliyoelekeza kwenye wakati wa Mapinduzi ya Ufaransa. Robert Seeley, wa Uingereza, katika 1849, alishughulikia habari hiyo kwa njia iyo hiyo. Angalau kufikia 1870, kichapo kilichohaririwa na Joseph Seiss na washiriki wake na kuchapwa katika Philadelphia, Pennsylvania, kilikuwa kikionyesha hesabu ambazo zilielekeza kwenye 1914 kuwa tarehe ya maana, hata ingawa sababu kiliyotoa ilitegemea kronolojia ambayo C. T. Russell alikataa baadaye.

      Halafu, katika matoleo ya Agosti, Septemba, na Oktoba 1875 ya Herald of the Morning, N. H. Barbour alisaidia kupatanisha mambo madogomadogo ambayo yalikuwa yameonyeshwa na wengine. Akitumia kronolojia iliyotungwa na Christopher Bowen, ambaye ni kasisi katika Uingereza, na kutangazwa na E. B. Elliott, Barbour alihusianisha mwanzo wa Nyakati za Mataifa na kuondolewa kwa Mfalme Sedekia kutoka kwenye ufalme wake kama ilivyotabiriwa kwenye Ezekieli 21:25, 26, akaelekeza kwenye 1914 kuwa waonyesha mwisho wa Nyakati za Mataifa.

      Mapema katika 1876, C. T. Russell alipokea nakala moja ya Herald of the Morning. Mara hiyo yeye aliandikia Barbour kisha akatumia wakati pamoja naye katika Philadelphia wakati wa kiangazi, wakizungumzia, miongoni mwa mambo mengine, vipindi vya wakati wa kiunabii. Muda mfupi baada ya hapo, katika makala moja yenye kichwa “Nyakati za Mataifa: Zakoma Wakati Gani?,” Russell pia alitoa sababu juu ya habari hiyo kwa kutumia Maandiko akataarifu kwamba uthibitisho ulionyesha kwamba “nyakati saba zitakoma katika A.D. 1914.” Makala hiyo ilichapwa katika toleo la Oktoba 1876 la Bible Examiner.j Kile kitabu Three Worlds, and the Harvest of This World, kilichotokezwa katika 1877 na N. H. Barbour kwa kushirikiana na C. T. Russell, kilielekeza kwenye mkataa huohuo. Baada ya hapo, matoleo ya mapema ya Watch Tower, kama yale ya tarehe ya Desemba 1879 na Julai 1880, yalivuta fikira kwenye 1914 W.K. kuwa mwaka wa maana sana kwa maoni ya unabii wa Biblia. Katika 1889 sura nzima ya nne ya Buku 2 la Millennial Dawn (baadaye liliitwa Studies in the Scriptures) ilitumiwa kuzungumzia “Nyakati za Mataifa.” Lakini ukomo wa Nyakati za Mataifa ungemaanisha nini?

      Hawa Wanafunzi wa Biblia hawakuwa na uhakika kabisa ni jambo gani lingetukia. Walisadikishwa kwamba tokeo halingekuwa kuteketezwa kwa dunia na kufutiliwa mbali kwa uhai wa kibinadamu. Badala ya hivyo, walijua kwamba ingeonyesha hatua yenye maana katika utawala wa kimungu. Mwanzoni, walifikiri kwamba kufikia tarehe hiyo Ufalme wa Mungu ungekuwa umepata udhibiti kamili, wa ulimwengu wote mzima. Wakati jambo hilo halikutukia, uhakika wao katika unabii mbalimbali wa Biblia ulioonyesha tarehe hiyo haukuyumbayumba. Walifikia mkataa kwamba, badala ya hivyo, tarehe hiyo ilionyesha tu mwanzo kwa habari ya utawala wa Ufalme.

      Hali kadhalika, mwanzoni walifikiri pia kwamba taabu za duniani pote zikifikia upeo katika machafuko ya utawala (ambayo walielewa kwamba yangeshirikishwa na vita ya “siku kubwa ya Mungu Mweza-Yote”) yangetangulia tarehe hiyo. (Ufu. 16:14, NW) Lakini, miaka kumi kabla ya 1914, Watch Tower lilidokeza kwamba msukosuko wa ulimwenguni pote ambao ungetokeza kuangamizwa kwa mipango yote ya kibinadamu ungekuja mara tu baada ya mwisho wa Nyakati za Mataifa. Walitarajia mwaka 1914 ulete badiliko kubwa kwa Yerusalemu, kwa kuwa unabii ulikuwa umesema kwamba ‘Yerusalemu ungekanyagwa’ mpaka Nyakati za Mataifa zitimie. Walipoona 1914 ukikaribia na bado hawakuwa wamekufa wakiwa wanadamu na ‘kunyakuliwa katika mawingu’ wamlaki Bwana—kupatana na matarajio ya mapema—walitumaini sana kwamba badiliko lao lingetukia mwishoni mwa Nyakati za Mataifa.—1 The. 4:17.

      Kadiri miaka ilivyopita nao wakachunguza na kuchunguza tena Maandiko, imani yao katika unabii mbalimbali iliendelea kuwa yenye nguvu, nao hawakusita kutaarifu yale waliyotarajia yangetukia. Kwa mafanikio ya kiwango mbalimbali, walijaribu kuepuka kushikilia bila uthibitisho mambo madogomadogo ambayo hayakutajwa moja kwa moja katika Maandiko.

      Je, “Kengele ya Saa” Ililia Mapema Mno?

      Bila shaka msukosuko mkubwa ulikumba ulimwengu katika 1914 kwa kufyatuka kwa Vita ya Ulimwengu 1, ambayo kwa miaka mingi iliitwa tu ile Vita Kuu, lakini haikuongoza mara hiyo kwenye kupinduliwa kwa tawala zote za kibinadamu zilizokuwako. Kadiri matukio kuhusiana na Palestina yalivyositawi kufuatia 1914, Wanafunzi wa Biblia walifikiri kwamba waliona uthibitisho wa mabadiliko ya maana kwa ajili ya Israeli. Lakini kadiri miezi na kisha miaka ilivyopita, Wanafunzi wa Biblia hawakupokea thawabu yao ya kimbingu, kama walivyokuwa wametarajia. Waliitikiaje jambo hilo?

      The Watch Tower la Februari 1, 1916, lilivuta fikira hususa kwenye Oktoba 1, 1914, kisha likasema: “Hiyo ilikuwa ndiyo hatua ya mwisho ya wakati ambayo kronolojia ya Biblia ilielekeza kwetu kuwa ilihusiana na mambo ambayo yangelipata Kanisa la Katoliki ya Roma. Je, Bwana alituambia kwamba tungechukuliwa huko [mbinguni]? Hapana. Yeye alisema nini? Neno lake na matimizo ya unabii yalionekana yakielekeza bila kukosea kwamba tarehe hiyo ilionyesha mwisho wa Nyakati za Mataifa. Sisi tuliamua kutokana na hilo kwamba ‘badiliko’ la Kanisa lingetukia katika au kabla ya tarehe hiyo. Lakini Mungu hakutuambia kwamba ingekuwa hivyo. Yeye alituruhusu tufikie uamuzi huo; nasi tunaamini kwamba umethibitika kuwa mtihani uliohitajiwa juu ya watakatifu wapendwa wa Mungu kila mahali.” Lakini je, matukio hayo yalithibitisha kwamba tumaini lao tukufu lilikuwa limekuwa la bure? Hapana. Ilimaanisha tu kwamba si kila kitu kilikuwa kikitukia upesi kama walivyokuwa wametarajia.

      Miaka kadhaa kabla ya 1914, Russell alikuwa ameandika hivi: “Kwa wazi kronolojia (unabii wa wakati kwa ujumla) haikukusudiwa kuwapa watu wa Mungu habari sahihi ya kronolojia muda wa karne zote. Kwa wazi ilikusudiwa zaidi itumike kama kengele ya saa iwaamshe na kuwatia nishati watu wa Bwana katika wakati ufaao. . . . Lakini tuseme, mathalani, kwamba Oktoba, 1914, ungepita na kusitukie anguko kubwa la serikali za Mataifa. Hilo lingethibitisha au lisingethibitisha nini? Lisingeondoa uthibitisho wa sehemu yoyote ya Mpango wa Kimungu wa Zile Enzi. Bei ya fidia iliyokamilishwa huko Kalvari bado ingekuwa uthibitisho wa utimizo wa mwisho wa Programu ya Kimungu iliyo kubwa kwa ajili ya rudisho la wanadamu. Ule ‘mwito wa juu’ wa Kanisa lipate kuteseka pamoja na Mkombozi na kutukuzwa pamoja naye likiwa washiriki wake au likiwa Bibi-Arusi wake bado ungekuwa vile vile. . . . Jambo pekee lililoathiriwa na kronolojia lingekuwa wakati wa kutimizwa kwa matumaini hayo matukufu kwa ajili ya Kanisa na kwa ajili ya ulimwengu. . . . Na tarehe hiyo ikipita ingethibitisha tu kwamba kronolojia yetu, ‘kengele ya saa’ yetu, ililia mapema kidogo kabla ya wakati. Je, sisi tungefikiri kwamba ni msiba mkuu ikiwa kengele ya saa yetu ingetuamsha nukta chache mapema zaidi asubuhi ya siku fulani kuu yenye kujawa na shangwe na furaha? Hakika sivyo!”

      Lakini hiyo “kengele ya saa” haikuwa imelia mapema mno. Kwa kweli, mambo waliyoona ambayo “saa” ilikuwa imewaamsha ndiyo hayakuwa mambo barabara waliyokuwa wametarajia.

      Miaka fulani baadaye, wakati nuru ilipokuwa imekuwa nyangavu zaidi, wao walikiri hivi: “Walio wengi kati ya watakatifu hao wapendwa walifikiri kwamba kazi yote ilikuwa imefanywa. . . . Walishangilia kwa sababu ya uthibitisho ulio wazi kwamba ulimwengu ulikuwa umekwisha, kwamba ufalme wa mbingu ulikuwa umekaribia, na kwamba siku ya ukombozi wao ilikaribia. Lakini walikuwa wamekosa kuona jambo jingine ambalo lazima lifanywe. Habari njema ambazo walikuwa wamepokea lazima wangeambia wengine; kwa sababu Yesu alikuwa ameamuru: ‘Habari njema ya ufalme itahubiriwa katika ulimwengu wote, kuwa ushuhuda kwa mataifa yote; hapo ndipo ule mwisho utakapokuja.’ (Mathayo 24:14)”—The Watch Tower, Mei 1, 1925.

      Kadiri matukio yaliyofuata 1914 yalivyoanza kufunuka, nao Wanafunzi wa Biblia wakayalinganisha na yale ambayo Bwana-Mkubwa alikuwa ametabiri, walikuja kuthamini hatua kwa hatua kwamba walikuwa wakiishi katika siku za mwisho za mfumo wa kale na kwamba zilianza 1914. Pia walikuja kuelewa kwamba katika mwaka 1914 ndipo kuwapo kusikoonekana kwa Kristo kulipokuwa kumeanza na kwamba, huko hakukuwa katika maana ya kurudi kwake binafsi (hata kwa kutoonekana) kwenye ujirani wa dunia, bali kwa kuelekeza uangalifu wake kwenye dunia akiwa Mfalme anayetawala. Waliona nao wakakubali daraka muhimu lililokuwa lao la kupiga mbiu ya hii “habari njema ya ufalme” kwa ajili ya ushahidi kwa mataifa yote katika huu wakati wa hatari wa historia ya kibinadamu.—Mt. 24:3-14.

  • Kukua Katika Ujuzi Sahihi Juu ya Kweli
    Mashahidi wa Yehova—Wapiga-Mbiu wa Ufalme wa Mungu
    • Kufikia 1914, watumishi waaminifu wa Mungu wa nyakati za kabla ya Ukristo hawakuwa wamefufuliwa duniani wakiwa wakuu wenye kuwakilisha Mfalme wa Kimesiya, kama ilivyokuwa imetarajiwa, wala wabakio wa “kundi dogo” hawakuwa wamejiunga na Kristo katika Ufalme wa kimbingu katika mwaka huo. Hata hivyo The Watch Tower la Februari 15, 1915, lilitaarifu kwa uhakika kwamba 1914 ulikuwa ndio wakati uliowekwa “wa Bwana wetu kutwaa uweza Wake mkuu na kuanza kutawala,” hivyo kumaliza zile mileani nyingi za utawala usiokatizwa wa Mataifa. Katika toleo lalo la Julai 1, 1920, The Watch Tower lilithibitisha tena msimamo huo na kuushirikisha na zile habari njema ambazo Yesu alikuwa ametabiri kwamba zingehubiriwa duniani pote kabla ya mwisho. (Mt. 24:14) Kwenye mkusanyiko wa Wanafunzi wa Biblia huko Cedar Point, Ohio, katika 1922, uelewevu huo ulitaarifiwa upya katika azimio la ujumla, na Ndugu Rutherford akahimiza wakusanyikaji hivi: “Mtangazeni, mtangazeni, mtangazeni, Mfalme na ufalme wake.”

  • Kukua Katika Ujuzi Sahihi Juu ya Kweli
    Mashahidi wa Yehova—Wapiga-Mbiu wa Ufalme wa Mungu
    • Vita ya Ile Siku Kubwa ya Mungu Mweza Yote

      Ile vita ya ulimwengu iliyoanza katika 1914 ilitikisa mfumo wa mambo ulioko hadi kwenye misingi yao. Kwa wakati fulani ilionekana kana kwamba matukio yangesonga mbele kama vile Wanafunzi wa Biblia walivyokuwa wametarajia.

      Huko nyuma katika Agosti 1880, Ndugu Russell alikuwa ameandika hivi: “Sisi twaelewa kwamba kabla familia ya kibinadamu haijarudishwa au hata kuanza kubarikiwa, serikali za dunia ambazo sasa hufunga na kuonea wanadamu zitapinduliwa zote na kwamba ufalme wa Mungu utatwaa udhibiti na kwamba baraka na rudisho zitakuja kupitia huo ufalme mpya.” ‘Kupinduliwa kwa falme’ kungetukiaje? Akitegemea hali ambazo angeweza kuona wakati ule zikitukia katika ulimwengu, Russell aliamini kwamba wakati wa vita ya Har–Magedoni, Mungu angetumia vikundi vyenye kuzozana vya wanadamu kupindua mipango iliyoko. Alisema hivi: “Kazi ya kubomoa milki ya kibinadamu inaanza. Mamlaka itakayozipindua inatenda kazi sasa. Tayari watu wanapanga majeshi yao chini ya jina la Wakomunisti, Wasosholisti, na Wanamapinduzi, n.k.”

      Kitabu The Day of Vengeance (baadaye kiliitwa The Battle of Armageddon), kilichotangazwa katika 1897, kiliongeza habari zaidi juu ya njia ambayo Wanafunzi wa Biblia wakati ule walielewa jambo hilo, kikisema hivi: “Bwana, kwa maongozi yake ya kimungu yenye kushinda, atatwaa uongozi wa ujumla wa jeshi hili kubwa la wasioridhika—wazalendo, warekebishaji, wasosholisti, wateteaji-maadili, wanamachafuko, wajinga na wasio na tumaini—na kutumia matumaini yao, hofu, upumbavu na ubinafsi, kulingana na hekima yake ya kimungu, kutimiza makusudi yake mwenyewe makuu katika kupindua mipango ya sasa, na katika kutayarisha binadamu kwa ajili ya Ufalme wa Uadilifu.” Hivyo wao walielewa kwamba vita ya Har–Magedoni ingeshirikishwa na mapinduzi ya kijamii yenye jeuri.

      Lakini je, Har–Magedoni ingekuwa mng’ang’ano tu kati ya vikundi vyenye kuzozana vya wanadamu, mapinduzi ya kijamii yenye kutumiwa na Mungu kupindua mipango iliyoko? Kadiri uangalifu zaidi ulivyokazwa juu ya maandiko yaliyohusu habari hiyo, The Watch Tower la Julai 15, 1925, lilivuta fikira kwenye Zekaria 14:1-3 na kusema: “Kwa hilo tungeelewa kwamba mataifa yote ya dunia, chini ya mwelekezo wa Shetani, yangekusanywa kwenye vita dhidi ya jamii ya Yerusalemu, yaani, wale ambao huchukua msimamo wao upande wa Bwana . . . Ufunuo 16:14, 16.”

      Mwaka uliofuata, katika kitabu Deliverance, uangalifu ulikazwa juu ya kusudi la kweli la vita hiyo, kusema: “Sasa Yehova, kulingana na Neno lake, atafanya wonyesho wa nguvu zake kwa wazi sana na kwa njia isiyo na shaka hivi kwamba watu wataweza kusadikishwa juu ya mwendo wao usio wa kimungu na waweze kuelewa kwamba Yehova ndiye Mungu. Hiyo ndiyo sababu iliyofanya Mungu alete lile furiko kuu, aangushe chini Mnara wa Babeli, aharibu jeshi la Senakeribu yule mfalme wa Ashuru, na kumeza Wamisri; na ndiyo pia sababu sasa ataleta taabu nyingine kuu juu ya ulimwengu. Maafa hayo ya hapo kwanza yalikuwa vivuli tu vya lile linalokuja sasa. Kukusanywa huko ni [kuletwa] kwenye siku ile kuu ya Mungu Mweza Yote. Ndiyo ile ‘siku kuu na itishayo ya Bwana’ (Yoe. 2:31), wakati ambapo Mungu atajifanyia mwenyewe jina. Katika pambano hilo kuu na la mwisho vikundi vya watu wa kila taifa, kabila na lugha vitajifunza kwamba Yehova ndiye mwenye nguvu zote, mwenye hekima yote na Mungu mwenye haki.” Lakini watumishi wa Yehova duniani walitahadharishwa hivi: “Katika vita hiyo kuu hakuna Mkristo atakayerusha ngumi. Sababu inayofanya wasifanye hivyo ni kwamba Yehova amesema: ‘Vita si yenu, bali ya Mungu.’” Vita inayozungumzwa hapa kwa wazi si ile ambayo ilipiganwa miongoni mwa mataifa, kuanzia 1914. Ilikuwa ingali inakuja.

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki