-
Ni Roho Ya Aina Gani Unayoonyesha?Mnara wa Mlinzi—2012 | Oktoba 15
-
-
EPUKA ROHO YA ULIMWENGU
4. “Roho ya ulimwengu” ni nini?
4 Maandiko yanatuambia hivi: “Sisi tulipokea, si roho ya ulimwengu, bali roho inayotoka kwa Mungu.” (1 Kor. 2:12) “Roho ya ulimwengu” ni nini? Ni roho ileile inayotajwa katika andiko la Waefeso 2:2, linalosema hivi: “Wakati fulani mlitembea ndani yake kulingana na mfumo wa mambo wa ulimwengu huu, kulingana na mtawala wa mamlaka ya hewa, roho ambayo sasa hutenda katika wana wa kutotii.” “Hewa” hiyo ni roho ya ulimwengu, au mtazamo wa akili, na inatuzunguka pande zote kama hewa halisi. Roho hiyo iko kila mahali. Mara nyingi inaonyeshwa kupitia mtazamo ambao watu wengi wanao leo, mtazamo wa ‘Hakuna mtu yeyote anayepaswa kuniambia jambo la kufanya!’ au, ‘Unapaswa kupigania haki zako!’ Watu hao ni “wana wa kutotii” wa ulimwengu wa Shetani.
5. Ni roho gani mbaya ambayo baadhi ya watu walionyesha katika taifa la Israeli?
5 Mitazamo kama hiyo imekuwapo kwa muda mrefu. Wakati wa Musa, Kora aliinuka dhidi ya wale waliokuwa na mamlaka katika kutaniko la Israeli. Alimlenga hasa Haruni na wanawe, ambao walikuwa na pendeleo la kutumikia wakiwa makuhani. Huenda Kora aliona makosa yao ya kutokamilika. Au huenda alidai kwamba Musa aliwapendelea watu wake wa ukoo kwa kuwapa mapendeleo. Kwa vyovyote vile, ni wazi kwamba Kora alianza kuona mambo kwa maoni ya kibinadamu na kuwashutumu wale waliowekwa rasmi na Yehova, kwa kuwaambia hivi bila heshima: “Imetosha . . . Kwa nini, basi, mjiinue wenyewe juu ya kutaniko?” (Hes. 16:3) Vivyo hivyo, Dathani na Abiramu walilalamika dhidi ya Musa, kwa kumwambia kwamba alikuwa ‘akijaribu kujifanya mkuu juu yao kabisa.’ Walipoitwa waje mbele ya Musa, walijibu hivi kwa kiburi: “Sisi hatutakuja!” (Hes. 16:12-14) Ni wazi kwamba Yehova hakupendezwa na roho yao. Aliwaua waasi hao wote.—Hes. 16:28-35.
6. Baadhi ya watu katika karne ya kwanza walionyeshaje kwamba walikuwa na mtazamo mbaya, na kwa nini huenda walionyesha mtazamo huo?
6 Baadhi ya watu katika karne ya kwanza walianza pia kuwachambua-chambua wale waliopewa mamlaka kutanikoni, na hivyo “kupuuza mamlaka.” (Yuda 8) Inaelekea wanaume hao hawakuridhika na mapendeleo yao na walijaribu kuwashawishi wengine dhidi ya wanaume waliowekwa rasmi ambao walikuwa wakitimiza kwa moyo wote majukumu waliyopewa na Mungu.—Soma 3 Yohana 9, 10.
7. Kwa nini huenda tukahitaji kujihadhari kutanikoni leo?
7 Ni wazi kwamba roho kama hiyo haina nafasi katika kutaniko la Kikristo. Ndiyo sababu tunahitaji kujihadhari kuhusiana na jambo hilo. Wanaume wazee kutanikoni si wakamilifu, kama vile tu ambavyo wanaume wazee hawakuwa wakamilifu katika siku za Musa na katika siku za mtume Yohana. Huenda wazee wakafanya makosa ambayo yanatuathiri kibinafsi. Ikiwa hilo linatukia, halitakuwa jambo linalofaa kwa mshiriki yeyote wa kutaniko kutenda kupatana na roho ya ulimwengu, kwa kudai kwa hasira “haki” itendeke, au kusema “ndugu huyu anapaswa kuchukuliwa hatua”! Huenda Yehova akaamua kupuuza makosa fulani madogo-madogo. Je, tunaweza kufanya vivyo hivyo? Kwa sababu ya ule wanaouona kuwa udhaifu wa wazee, watu fulani ambao wanatenda dhambi nzito kutanikoni wamekataa kukutana na halmashauri ya wazee waliopewa mgawo wa kuwasaidia. Jambo hilo linaweza kulinganishwa na mgonjwa anayekataa matibabu kwa sababu hapendezwi na jambo fulani kumhusu daktari.
8. Ni maandiko gani yanayoweza kutusaidia kudumisha maoni yanayofaa kuhusu wale wanaoongoza kutanikoni?
8 Tunaweza kuepuka roho ya aina hiyo tukikumbuka kwamba katika Biblia, Yesu anaonyeshwa akiwa na ‘nyota saba katika mkono wake wa kuume.’ “Nyota” hizo zinafananisha waangalizi watiwa-mafuta, na kwa maana kubwa zaidi, waangalizi wote katika makutaniko. Yesu anaweza kuziongoza “nyota” hizo zilizo mkononi mwake katika njia yoyote ile anayoona kuwa inafaa. (Ufu. 1:16, 20) Kwa hiyo, akiwa Kichwa cha kutaniko la Kikristo, Yesu anayaongoza kikamili mabaraza ya wazee. Ikiwa kwa kweli mtu fulani katika baraza la wazee anahitaji kurekebishwa, Yule aliye na ‘macho kama mwali wa moto,’ atahakikisha kwamba hatua fulani imechukuliwa kwa wakati Wake na kwa njia Yake mwenyewe. (Ufu. 1:14) Kwa sasa, tunawaheshimu inavyofaa wale waliowekwa rasmi na roho takatifu, kwa kuwa Paulo aliandika hivi: “Watiini wale wanaoongoza katikati yenu na mnyenyekee, kwa maana wanaendelea kuzilinda nafsi zenu kama wale watakaotoa hesabu; ili wafanye hivyo kwa shangwe na si kwa kuugua, kwa maana kufanya hivyo kungewadhuru ninyi.”—Ebr. 13:17.
-
-
Ni Roho Ya Aina Gani Unayoonyesha?Mnara wa Mlinzi—2012 | Oktoba 15
-
-
ONYESHA ROHO YA HESHIMA KUTANIKONI
11. (a) Kudumisha roho inayofaa kutatusaidia kuepuka nini? (b) Tunajifunza nini kutokana na mfano wa Daudi?
11 Tunapaswa kukumbuka kwamba Yehova amewapa wazee mgawo wa “kulichunga kutaniko la Mungu.” (Mdo. 20:28; 1 Pet. 5:2) Kwa hiyo, tunatambua kwamba ni jambo la hekima kuheshimu mpango wa Mungu, iwe tuna pendeleo la kutumikia tukiwa wazee au la. Kudumisha roho inayofaa kunaweza kutusaidia kuepuka kuhangaikia sana mapendeleo. Mfalme Sauli wa Israeli alipohisi kwamba Daudi alikuwa tishio kwa ufalme wake, Sauli “akawa akimtilia Daudi shaka tangu siku hiyo na kuendelea.” (1 Sam. 18:9) Mfalme huyo alisitawisha roho mbaya na hata alitaka kumuua Daudi. Badala ya kuhangaikia sana mapendeleo au mamlaka kama Sauli, ni vizuri zaidi kuwa kama Daudi. Licha ya matendo yote yasiyo ya haki aliyotendewa, kijana huyo aliendelea kumheshimu yule aliyepewa mamlaka na Mungu.—Soma 1 Samweli 26:23.
-