-
Barnaba Yule “Mwana wa Faraja”Mnara wa Mlinzi—1998 | Aprili 15
-
-
Wapata mwaka wa 36 W.K., Sauli wa Tarso (aliyekuja kuwa mtume Paulo), aliyekuwa Mkristo sasa, alikuwa akijaribu kujiunga na kutaniko la Yerusalemu, “lakini wote walimwogopa, kwa sababu hawakuamini alikuwa mwanafunzi.” Angeweza kulisadikishaje kutaniko kwamba mgeuzo wake wa imani ulikuwa wa kweli na si hila tu ya kuliangamiza kabisa hata zaidi? “Barnaba akaja kumsaidia na kumwongoza kwa mitume.”—Matendo 9:26, 27; Wagalatia 1:13, 18, 19.
Sababu ambayo ilimfanya Barnaba amwitibari Sauli haitajwi. Kwa vyovyote vile, “Mwana wa Faraja” aliishi kupatana na jina lake la ziada kwa kumsikiliza Sauli na kumsaidia atoke katika shaka zilizoonekana kuwa bila matumaini. Ijapokuwa wakati huo Sauli alirudi Tarso alikozaliwa, urafiki ulikuwa umefanyizwa kati ya wanaume hao wawili. Katika miaka iliyofuata, hilo lilipaswa kuwa na matokeo ya maana.—Matendo 9:30.
-
-
Barnaba Yule “Mwana wa Faraja”Mnara wa Mlinzi—1998 | Aprili 15
-
-
Barnaba alimfikiria Sauli. Labda sana, Barnaba alijua ufunuo wa kiunabii wa Anania wakati wa mgeuzo wa imani wa Sauli, kwamba yule mnyanyasaji wa zamani alikuwa ‘chombo-kichaguliwa, ili kupeleka jina la Yesu kwa mataifa.’ (Matendo 9:15) Kwa hiyo Barnaba alikwenda Tarso—safari ya mwendo mmoja wa kilometa zipatazo 200—ili kumtafuta Sauli. Wote wawili walihubiri pamoja kwa mwaka mzima wakiwa wenzi, na “ilikuwa kwanza katika Antiokia” katika pindi hiyo “kwamba wanafunzi kwa uongozi wa kimungu waliitwa Wakristo.”—Matendo 11:25, 26.
Wakati wa utawala wa Klaudio, njaa kali ilizipata sehemu mbalimbali za Milki ya Roma. Kulingana na mwanahistoria Myahudi Josephus, katika Yerusalemu “watu wengi walikufa kutokana na ukosefu wa kilichohitajiwa ili kupata chakula.” Hivyo, wanafunzi katika Antiokia “wakaamua, kila mmoja kwa kadiri ambayo yeyote angeweza kutoa, kupeleka uhudumiaji wa kutuliza kwa akina ndugu wenye kukaa katika Yudea; na hilo wakafanya, wakiipeleka kwa wanaume wazee kwa mkono wa Barnaba na Sauli.” Baada ya kutimiza utume huo kikamili, hao wawili walirudi Antiokia wakiwa na Yohana Marko, ambako walihesabiwa miongoni mwa manabii na walimu wa kutaniko.—Matendo 11:29, 30; 12:25; 13:1.
Mgawo wa Pekee wa Umishonari
Kisha tukio lisilo la kawaida likatokea. “Walipokuwa wakimhudumia Yehova hadharani na kufunga, roho takatifu ikasema: ‘Kati ya watu wote wekeni kando Barnaba na Sauli kwa ajili yangu kwa kazi ambayo nimewaitia.’” Ebu wazia! Roho ya Yehova iliamuru kwamba hao wawili wapewe mgawo wa pekee. “Basi watu hawa, waliotumwa na roho takatifu, wakateremka kwenda Seleukia, na kutoka huko wakasafiri kwa mashua kwenda zao Saiprasi.” Kwa kufaa, Barnaba pia aweza kuitwa mtume, au yule aliyetumwa.—Matendo 13:2, 4; 14:14.
Baada ya kusafiri kupitia Saiprasi na kumgeuza imani Sergio Paulo, liwali wa mkoa Mroma wa kisiwa hicho, walienda hadi Perga, upande wa kusini ya pwani ya Asia Ndogo, ambako Yohana Marko alijiondoa na kurejea Yerusalemu. (Matendo 13:13) Yaonekana kwamba hadi wakati huo Barnaba alikuwa na daraka la kuongoza, labda akiwa mwenzi mwenye uzoefu zaidi. Kuanzia wakati huo na kuendelea, ni Sauli (sasa anayerejezewa kuwa Paulo) anayechukua uongozi. (Linganisha Matendo 13:7, 13, 16; 15:2.) Je, Barnaba alihisi vibaya kwa sababu ya tukio hilo? La, alikuwa Mkristo aliyekomaa ambaye alitambua kwa unyenyekevu kwamba Yehova pia alikuwa akitumia mwenzake katika njia yenye nguvu sana. Kupitia kwao, Yehova alitaka hata maeneo mengine yasikie habari njema.
Kwa kweli, kabla ya hao wawili kutolewa Antiokia katika Pisidia, eneo lote lilisikia neno la Mungu kutoka kwa Paulo na Barnaba, na idadi fulani ilikubali huo ujumbe. (Matendo 13:43, 48-52) Katika Ikoniamu, “umati mkubwa wa Wayahudi na pia Wagiriki ukapata kuwa waamini.” Hilo lilimchochea Paulo na Barnaba watumie wakati mwingi huko, ‘wakisema kwa ujasiri kwa mamlaka ya Yehova, aliyeruhusu ishara na mambo ya ajabu kutukia kupitia mikono yao.’ Waliposikia kwamba njama ilikuwa imefanywa kisiri ya kuwapiga kwa mawe, hao wawili walikimbia na kuendelea na kazi yao katika Likaonia, Listra, na Derbe. Yajapokuwa mambo ya kutisha uhai waliyojionea katika Listra, Barnaba na Paulo waliendelea “[ku]zitia nguvu nafsi za wanafunzi, wakiwatia moyo kubaki katika imani na kusema: ‘Lazima tuingie katika ufalme wa Mungu kupitia dhiki nyingi.’”—Matendo 14:1-7, 19-22.
Wahubiri hawa wawili wenye nguvu hawakujiruhusu wahofishwe. Kinyume cha hilo, walirudi kuwajenga Wakristo wapya mahali ambapo walikuwa tayari wamepata upinzani mkali, yaelekea wakisaidia wanaume wenye sifa za ustahili waongoze katika makutaniko mapya.
Suala la Tohara
Yapata miaka 16 hivi baada ya Pentekoste 33 W.K., Barnaba alihusika katika kisa cha kihistoria kuhusu suala la tohara. “Watu fulani wakateremka [Antiokia ya Siria] kutoka Yudea na kuanza kuwafundisha ndugu: ‘Msipotahiriwa kulingana na desturi ya Musa, hamwezi kuokolewa.’” Barnaba na Paulo walijua kutokana na uzoefu kwamba haikuwa hivyo, nao walibisha hiyo hoja. Badala ya kusisitiza mamlaka yao, walitambua kwamba hili lilikuwa swali ambalo lilipasa kutatuliwa kwa manufaa ya ushirika mzima wa akina ndugu. Kwa hiyo walilipeleka hilo swali kwa baraza linaloongoza katika Yerusalemu, ambako ripoti zao zilisaidia kutatua suala hilo. Baadaye, Paulo na Barnaba, wafafanuliwao kuwa “wapendwa . . . ambao wametoa nafsi zao kwa ajili ya jina la Bwana wetu Yesu Kristo,” walikuwa miongoni mwa wale waliopewa mgawo wa kuwasilisha uamuzi huo kwa ndugu katika Antiokia. Barua kutoka kwa baraza linaloongoza iliposomwa na hotuba kutolewa, kutaniko ‘lilishangilia juu ya kitia-moyo hicho’ na ‘lilitiwa nguvu.’—Matendo 15:1, 2, 4, 25-32.
“Mfoko Mkali wa Hasira”
Baada ya masimulizi mengi yafaayo kumhusu, huenda tukahisi kwamba hatungeweza kamwe kuishi kupatana na kielelezo cha Barnaba. Hata hiyo, “Mwana wa Faraja” alikuwa asiye mkamilifu kama vile sisi tusivyo wakamilifu. Wakati yeye na Paulo walipokuwa wakipanga safari ya pili ya umishonari ya kutembelea makutaniko, hali ya kutokubaliana ilitokea. Barnaba alikuwa ameazimia kumchukua binamu yake Yohana Marko, lakini Paulo hakufikiri kuwa yafaa, kwa kuwa Yohana Marko alikuwa amewaacha katika safari ya kwanza ya umishonari. Kukatokea “mfoko mkali wa hasira, hivi kwamba wakatengana; na Barnaba akamchukua Marko pamoja naye na kusafiri kwa mashua kwenda Saiprasi,” huku ‘Paulo akimteua Sila na kuondoka kwenda zake’ upande mwingine.—Matendo 15:36-40.
-