-
Jinsi Biblia Ilivyotufikia—Sehemu ya KwanzaMnara wa Mlinzi—1997 | Agosti 15
-
-
Hata hivyo, katika karne ya nne K.W.K., tatizo lilizuka. Aleksanda Mkubwa alitaka watu wote wa ulimwengu waelimishwe utamaduni wa Kigiriki. Ushindi wake mbalimbali ulithibitisha Kigiriki cha kawaida, au Kikoine, kuwa lugha iliyotumika kotekote katika Mashariki ya Kati. Tokeo ni kwamba, Wayahudi wengi walikua bila kujifunza kusoma Kiebrania na kwa hiyo hawakuweza kusoma Maandiko. Kwa hiyo, wapata mwaka wa 280 K.W.K., kikundi cha wasomi Waebrania kilikusanyika Aleksandria, Misri, ili kutafsiri Biblia ya Kiebrania katika lugha ya watu wengi ya Kikoine. Tafsiri yao ikaja kujulikana kuwa Septuagint, neno la Kilatini linalomaanisha “Sabini,” likirejezea idadi takriban ya watafsiri walioaminika kuwa walihusika. Ilimalizwa wapata mwaka wa 150 K.W.K.
Wakati wa Yesu, Kiebrania kilikuwa kingali kikisemwa katika Palestina. Lakini Kikoine ndicho kilichoenea sana huko na katika ile mikoa mingine ya mbali ya ulimwengu wa Roma. Kwa hiyo, waandikaji Wakristo wa Biblia, walitumia aina hiyo ya kawaida ya Kigiriki ili kufikia watu wengi iwezekanavyo wa mataifa. Pia, walinukuu sana kutoka katika Septuagint na kutumia mengi ya maneno yake.
Kwa kuwa Wakristo wa mapema walikuwa wamishonari wenye bidii, upesi wakawa stadi wa kutumia Septuagint ili kuthibitisha kwamba Yesu alikuwa Mesiya aliyekuwa amengojewa kwa muda mrefu. Hilo liliwafadhaisha Wayahudi na kuwachochea watokeze tafsiri kadhaa mpya katika Kigiriki, zilizokusudiwa kuwanyima Wakristo majibizano yao kwa kufanyia marekebisho maandiko yao ya ithibati waliyopenda sana. Kwa kielelezo, kwenye Isaya 7:14 Septuagint ilitumia neno la Kigiriki linalomaanisha “bikira,” ikirejezea kiunabii mama ya Mesiya. Hizo tafsiri mpya zilitumia neno tofauti la Kigiriki, linalomaanisha “mwanamke mchanga.” Kuendelea kwa hao Wakristo kuitumia Septuagint hatimaye kulisukuma Wayahudi waache mbinu zao zote na kuunga mkono kurudia maandishi ya Kiebrania. Mwishowe, tendo hilo likawa baraka kwa tafsiri za Biblia za baadaye kwa sababu ilisaidia kudumisha lugha ya Kiebrania.
-
-
Jinsi Biblia Ilivyotufikia—Sehemu ya KwanzaMnara wa Mlinzi—1997 | Agosti 15
-
-
Kuenea kwa itikadi za Kikristo upesi kulitokeza uhitaji wa tafsiri za Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo na pia Maandiko ya Kiebrania. Tafsiri kadha wa kadha katika lugha kama vile Kiarmenia, Kikoptiki, Kigeorgia, na Kisiria zilifanyizwa hatimaye. Mara nyingi ilikuwa lazima kubuni alfabeti kwa kusudi hilo tu. Mathalani, Ulfilas, askofu wa karne ya nne wa Kanisa la Kiroma, alisemwa kuwa alibuni alfabeti ya Kigothi ili kuitafsiri Biblia. Lakini aliacha vitabu vya Wafalme kwa sababu alifikiri kwamba hivyo vingetia moyo yale maelekeo ya kivita ya Wagothi. Hata hivyo, tendo hilo halikuwazuia Wagothi “Waliofanywa Wakristo” wasiteke nyara Roma mwaka wa 410 W.K.!
Biblia ya Kilatini na ya Kislavoni
Wakati uleule, Kilatini kikapata umaana, na tafsiri kadhaa za Kilatini cha Kale zikatokea. Lakini zilitofautiana katika mtindo na usahihi. Kwa hiyo mwaka wa 382 W.K., Papa Damasus alimpa mwandishi wake, Jerome, utume wa kutayarisha Biblia ya Kilatini yenye mamlaka.
Jerome alianza kwa kufanyia marekebisho tafsiri za Kilatini za Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo. Hata hivyo, alisisitiza kutafsiri Maandiko ya Kiebrania kutoka katika Kiebrania cha awali. Hivyo, mwaka wa 386 W.K., alihamia Bethlehemu ili kujifunza Kiebrania na kutafuta msaada wa rabi. Kwa tendo hilo, aliamsha ubishi mkubwa miongoni mwa makanisa. Wengine, kutia na Augustine, aliyeishi wakati uleule na Jerome, waliamini kwamba Septuagint ilikuwa imepuliziwa, nao walimshtaki Jerome kuwa “alikosa uaminifu-mshikamanifu kwa kuwaendea Wayahudi ili kupata msaada.” Akisonga mbele, Jerome alimaliza kazi yake wapata mwaka wa 400 W.K. Kwa kukaribia chanzo cha lugha na hati za awali na kwa kuzitafsiri katika lugha zilizosemwa wakati huo, Jerome alizitangulia kwa miaka elfu moja njia za kisasa za kutafsiri. Biblia yake ikaja kujulikana kuwa Vulgate, au Tafsiri ya Kawaida, nayo iliwanufaisha watu kwa karne kadhaa.
Katika Jumuiya ya Wakristo ya mashariki bado wengi wangeweza kusoma Septuagint na yale Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo. Hata hivyo, lugha na lahaja za Kislavoni, au Kislavi, zikaja kutumiwa kwa ukawaida katika sehemu za mashariki za Ulaya. Mwaka wa 863 W.K., ndugu wawili wenye kusema Kigiriki, Cyril na Methodius, walienda Moravia, ambayo sasa iko katika Jamhuri ya Cheki. Walianza kuitafsiri Biblia katika Kislavoni cha Kale. Ili kufanya hivyo, walibuni alfabeti ya Kiglagoliti, ambayo baadaye ilipitwa na alfabeti ya Kisirili, iliyopata jina kutokana na Cyril. Hiyo ndiyo iliyokuwa chanzo cha maandishi ya lugha ya kisasa ya Kirusi, ya Kiukrainia, ya Kiserbia, na ya Kibulgaria. Biblia ya Kislavoni ilitumiwa na watu wa eneo hilo kwa vizazi kadhaa. Ingawa hivyo, punde si punde, lugha zilipokuwa zikibadilika, ikawa isiyofahamika kwa mtu wa kawaida.
-
-
Jinsi Biblia Ilivyotufikia—Sehemu ya KwanzaMnara wa Mlinzi—1997 | Agosti 15
-
-
Kutafsiriwa kwa Biblia Kwakabili Upinzani
Mwaka wa 1079, Papa Gregory wa Saba alitoa ya kwanza kati ya zile amri nyingi za kanisa la enzi za kati za kupiga marufuku kutokezwa na nyakati nyingine hata kuwa na tafsiri za lugha za kienyeji. Aliondoa ruhusa ya Misa kusherehekewa katika Kislavoni kwa sababu kufanya hivyo kungetaka visehemu vya Andiko Takatifu vitafsiriwe. Tofauti kabisa na msimamo wa Wakristo wa mapema, aliandika hivi: “I[me]mpendeza Mungu Mweza-Yote kwamba andiko takatifu lapaswa kuwa siri katika mahali fulani-fulani.” Huo ukiwa ndio msimamo rasmi wa kanisa, waendelezaji wa usomaji wa Biblia walionwa kuwa hatari zaidi na zaidi.
Zijapokuwa hali zisizopendeza, kule kunakili na kutafsiri Biblia katika lugha za kawaida kuliendelea. Tafsiri za lugha nyingi zilienea kisiri katika Ulaya. Zote hizo zilinakiliwa kwa mkono, kwa kuwa kupiga chapa hakukubuniwa Ulaya mpaka miaka ya katikati ya 1400. Lakini kwa kuwa nakala zilikuwa za bei ghali na chache, mwananchi wa kawaida angeweza kujiona kuwa mwenye furaha kumiliki kisehemu tu cha kitabu kimoja cha Biblia au kurasa chache tu. Watu fulani walikariri moyoni sehemu kubwa-kubwa, hata Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo yote!
Hata hivyo, baada ya muda fulani kulikuwa na harakati zenye kushtusha zilizoenea sana za marekebisho ya kanisa. Kwa sehemu zilichochewa na ufahamu uliofanywa upya kuhusu umaana wa Neno la Mungu katika maisha ya kila siku. Harakati hizo na maendeleo ya uchapaji yangeiathirije Biblia? Na ni nini kilichompata William Tyndale na tafsiri yake, iliyotajwa mwanzoni? Tutaendeleza simulizi hili lenye kuvutia sana hadi nyakati zetu wenyewe katika matoleo ya wakati ujao.
-