Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Nchi Ambazo Zilikuwa Sehemu ya Yugoslavia
    2009 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
    • “Mei 16, 1992 (16/5/1992), tukiwa watu 13, tulikusanyika pamoja katika nyumba fulani wakati makombora yaliporushwa huko Sarajevo. Makombora mawili yaligonga jengo ambamo tulikuwa tumekusanyikia. Ingawa wengine wetu walikuwa Wakroatia, Waserbia, na Wabosnia—makabila yaleyale matatu ambayo yalikuwa yakiuana kule nje—tuliunganishwa na ibada safi. Kufikia asubuhi, kulipokuwa na utulivu kidogo, tuliondoka kwenye nyumba hiyo na kutafuta mahali salama. Kama tulivyokuwa tumefanya usiku uliotangulia, tulimlilia Yehova kwa sauti katika sala, naye akatusikia.”—Halim Curi.

      Sarajevo, ambalo lilikuwa na wakaaji zaidi ya 400,000, lilikabili mazingiwa ya muda mrefu zaidi na yenye kuogopesha zaidi katika historia ya leo.

  • Nchi Ambazo Zilikuwa Sehemu ya Yugoslavia
    2009 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
    • JIJI LAZINGIRWA

      Kama tulivyoona, ndugu wa Yugoslavia waliguswa moyo sana na upendo na umoja uliokuwepo katika kusanyiko la mwaka wa 1991 la “Wapendao Uhuru wa Kimungu” huko Zagreb, Kroatia. Kusanyiko hilo lisiloweza kusahaulika liliwatia nguvu kukabiliana na matatizo ambayo yangetokea baadaye. Wakati fulani, Wabosnia, Waserbia, na Wakroatia walikuwa wakiishi pamoja kwa amani huko Sarajevo. Kisha, jeshi likazingira jiji hilo na kila mtu akanaswa ndani—kutia ndani ndugu zetu. Ingawa kulikuwa na msukosuko wa kisiasa, hakuna aliyejua hali hiyo ingeendelea kwa muda gani.

      Halim Curi, mzee wa kutaniko huko Sarajevo, alisema hivi: “Watu wanakufa njaa. Kila mwezi wanapewa kilo chache tu za unga, gramu 100 za sukari, na nusu lita ya mafuta. Wakipata kipande chochote kidogo cha ardhi jijini, wanakitumia kupandia mboga. Watu wanakata miti ya Sarajevo ili wapate kuni. Miti inapokwisha, wanabomoa sakafu za mbao za nyumba zao ili wazitumie kupikia na kupasha joto nyumba zao. Wanatumia chochote kinachoweza kuteketea, hata viatu vilivyochakaa.”

      Jiji la Sarajevo lilipozingirwa, Ljiljana Ninković na mume wake Nenad walinaswa jijini na kutenganishwa na binti zao wawili. Ljiljana anasema: “Tulikuwa familia ya kawaida yenye watoto wawili, nasi tulikuwa na nyumba na gari. Halafu kwa ghafula, mambo yakabadilika kabisa.”

      Lakini mara nyingi waliona mkono wa Yehova ukiwalinda. Ljiljana anaendelea kusimulia: “Nyumba yetu ililipuliwa kwa bomu mara mbili baada tu ya sisi kuondoka. Ingawa tulipata matatizo, tulifurahia mambo madogo-madogo. Kwa mfano, tulifurahia kwenda kwenye bustani kuchuna majani fulani (ya dandelion) ili kutengeneza saladi, hivyo hatukula wali mkavu. Tulijifunza kutosheka na vitu tulivyokuwa navyo na kutochezea kitu chochote.”

      KUPATA MAANDALIZI YA KIMWILI NA YA KIROHO

      Tatizo moja kubwa lilikuwa kupata maji. Nyumba hazikuwa na maji ya bomba. Iliwabidi watu watembee kilomita tano kupitia maeneo yenye wavamizi ili kupata maji. Na walipofika mahali pa kuteka maji, walipanga foleni kwa saa nyingi wakisubiri kujaza mitungi yao, halafu iliwabidi kuanza safari ndefu ya kurudi nyumbani wakiwa wamejitwika mitungi hiyo.

      Halim anasema: “Imani yetu ilijaribiwa tuliposikia kwamba maji yangepatikana nyumbani kwa muda mfupi. Wakati huo kila mtu alioga, alifua nguo, na kuteka na kuhifadhi maji katika mitungi mingi iwezekanavyo. Lakini namna gani ikiwa maji yangepatikana wakati wa mkutano wa kutaniko? Ilitubidi tuamue—ama kwenda kwenye mkutano au kubaki nyumbani kuteka maji.”

      Ingawa maandalizi ya kimwili yalihitajiwa sana, akina ndugu walithamini sana maandalizi ya kiroho. Kwenye mikutano, ndugu walipata chakula cha kiroho na pia habari kuhusu wale waliofungwa gerezani, wale walioumizwa, au hata wale waliouawa. Milutin Pajić, ambaye ni mzee wa kutaniko, anasema: “Tulikuwa kama familia. Tulipohudhuria mikutano, hatukutaka kuondoka. Baada ya mikutano mingi, tulibaki kwa saa nyingi tukizungumza kuhusu kweli.”

  • Nchi Ambazo Zilikuwa Sehemu ya Yugoslavia
    2009 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
    • Tuliahidi Kurudi

      HALIM CURI

      ALIZALIWA 1968

      ALIBATIZWA 1988

      MAELEZO MAFUPI KUMHUSU Alisaidia kupanga na kusambaza misaada huko Sarajevo. Sasa anatumika akiwa mzee, mshiriki wa Halmashauri ya Uhusiano na Hospitali, na wakili wa Mashahidi wa Yehova huko Bosnia na Herzegovina.

      MWAKA wa 1992, jiji la Sarajevo lilizingirwa na wanajeshi. Tulipokosa kupata magazeti mapya, tulijifunza magazeti ya zamani. Akina ndugu walitumia taipureta nzee kunakili makala za funzo zilizopatikana. Ingawa kulikuwa na wahubiri 52 tu, watu zaidi ya 200 walihudhuria mikutano yetu, nasi tuliongoza mafunzo ya Biblia 240 hivi.

      Mnamo Novemba 1993, wakati vita vilipokuwa vimepamba moto, binti yetu, Arijana, alizaliwa. Haikuwa rahisi hata kidogo kumlea mtoto wakati huo. Nyakati nyingine, hatukuwa na maji ya bomba wala umeme kwa majuma mengi. Tulipata kuni kwa kupasua vyombo vya nyumbani vya mbao, nasi tulipitia maeneo hatari ili kufika kwenye mikutano. Wavamizi walifyatua risasi kiholela, hivyo ilitubidi tukimbie ili kuvuka barabara fulani na vizuizi.

      Siku moja yenye utulivu, tulipokuwa tukirudi nyumbani kutoka kwenye mkutano pamoja na mke wangu na mtoto wetu na Ndugu Dražen Radišić, risasi zilianza kufyatuliwa ghafula. Tulilala chini barabarani, lakini nilipigwa risasi tumboni. Nilikuwa na maumivu makali sana. Watu wengi waliona kilichotukia kupitia madirisha ya nyumba zao, na vijana fulani wenye ujasiri walitoka nje ya nyumba haraka na kutupeleka mahali salama. Nilikimbizwa hospitalini, ambako walitaka kunitia damu mishipani haraka. Nilimweleza daktari kwamba dhamiri yangu haiwezi kuniruhusu nitiwe damu mishipani. Walinishinikiza nifikirie tena jambo hilo; lakini niliazimia kusimama imara na nilikuwa tayari kwa matokeo yoyote yale. Nilifanyiwa upasuaji kwa muda wa saa mbili na nusu, na nilipata nafuu bila kutiwa damu mishipani.

      Baada ya upasuaji, nilihitaji kupumzika, lakini ilikuwa vigumu kufanya hivyo kwa sababu ya vita. Tuliamua kutembelea familia yetu huko Austria. Hata hivyo, njia pekee ya kutoka Sarajevo ilipitia chini ya uwanja wa ndege. Njia hiyo ilikuwa na urefu wa mita 900 na kimo cha sentimita 120 hivi. Mke wangu alimbeba mtoto, nami nikajaribu kubeba mizigo. Lakini kwa sababu ya upasuaji, ilibidi mke wangu anisaidie.

      Tulifurahia sana kukaa Austria. Tulipokuwa tukiondoka Sarajevo, tuliwaahidi ndugu zetu na Muumba wetu kwamba tutarudi. Haikuwa rahisi hata kidogo kuiacha familia yetu huko Austria, hasa mama yangu. Lakini tuliwaeleza kwamba tulikuwa tumemwahidi Mungu tutarudi Sarajevo ikiwa angetusaidia kutoka huko na kupumzika kidogo. Sasa je, kweli tungeweza kumwambia Mungu: “Asante kwa kutusaidia kufika huku. Tunafurahia sana kuwa huku, na sasa tungependa kukaa huku”? Pia, akina ndugu wa Sarajevo walituhitaji. Mke wangu, Amra, alinitegemeza sana katika mambo yote hayo.

      Hivyo, Desemba 1994, tulifika kwenye ile njia ya chini ya ardhi huko Sarajevo. Wakati huu tulikuwa tukiingia Sarajevo kutoka nje. Watu walipotuona tukirudi kupitia mfereji huo, walituuliza: “Mnafanya nini? Kila mtu anataka kuondoka, lakini ninyi mnarudi katika jiji lililozingirwa?” Siwezi kueleza kikamili shangwe tuliyokuwa nayo tulipokutana tena na ndugu zetu kwenye Jumba la Ufalme la Sarajevo. Hatujawahi kamwe kujuta kwamba tulirudi.

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki