-
Ushirika wa Akina NduguMashahidi wa Yehova—Wapiga-Mbiu wa Ufalme wa Mungu
-
-
Sehemu 3
Ushirika wa Akina Ndugu
Je, inawezekana kwa mamilioni ya watu kutoka mataifa na lugha zote kufanya kazi pamoja wakiwa ushirika wa kweli wa akina ndugu?
Rekodi ya Mashahidi wa siku ya kisasa wa Yehova yatoa jibu kwa sauti kubwa kusema Ndiyo! Kata hii (Sura ya 15 hadi 21) inaeleza jinsi tengenezo lao linavyofanya kazi. Inaonyesha bidii ambayo wao hupiga mbiu ya Ufalme wa Mungu na upendo unaodhihirika wanapofanya kazi pamoja na wanaposaidiana katika nyakati za taabu.
-
-
Usitawi wa Muundo wa TengenezoMashahidi wa Yehova—Wapiga-Mbiu wa Ufalme wa Mungu
-
-
Sura ya 15
Usitawi wa Muundo wa Tengenezo
UTENDAJI wa tengenezo la Mashahidi wa Yehova umepata mabadiliko ya maana tangu Charles Taze Russell na washirika wake waanze kwa mara ya kwanza funzo la Biblia pamoja katika 1870. Wanafunzi wa Biblia walipokuwa wachache, hawakuwa na chochote ambacho watu wa nje wangeona kuwa ni tengenezo. Hata hivyo, leo, watu watazamapo makutaniko ya Mashahidi wa Yehova, mikusanyiko yao, na kazi yao ya kuhubiri habari njema katika nchi zaidi ya 200, wao hustaajabia jinsi tengenezo liendeshavyo mambo kwa utaratibu. Yote yalisitawije?
Wanafunzi wa Biblia walipendezwa sana na kuelewa si mafundisho ya Biblia tu bali pia ile njia ambayo utumishi wa Mungu ungepasa kufanywa, kama ionyeshwavyo katika Maandiko. Walijua kwamba Biblia haikufanya uandalizi kwa ajili ya makasisi wenye majina ya vyeo, kukiwa na watu wa kawaida ambao wangewahubiri. Ndugu Russell alikuwa ameazimia kwamba hakungekuwa na jamii ya makasisi miongoni mwao.a Kupitia safu za Watch Tower, wasomaji walo walikumbushwa mara nyingi kwamba Yesu aliwaambia wafuasi wake: “Kiongozi wenu ni mmoja, Kristo,” lakini, “Nyinyi nyote ni akina ndugu.”—Mt. 23:8, 10, NW.
Ushirika wa Mapema wa Wanafunzi wa Biblia
Wasomaji wa Watch Tower na vichapo vilivyohusiana waliona upesi kwamba ili wampendeze Mungu, ilikuwa lazima wakate uhusiano na kanisa lolote lililojithibitisha lenyewe kutokuwa jaminifu kwa Mungu kwa kuweka itikadi ya kidini na mapokeo ya wanadamu mbele ya Neno lake lililoandikwa. (2 Kor. 6:14-18) Lakini baada ya kujiondoa katika makanisa ya Jumuiya ya Wakristo, wao walienda wapi?
Katika makala yenye kichwa “Ile Ekklesia,”b Ndugu Russell alionyesha kwamba kanisa la kweli, kutaniko la Kikristo, si tengenezo lenye washiriki ambao wametoa kibali na utegemezo kwa itikadi za kidini zilizofanyizwa na wanadamu na ambao majina yao yameandikwa katika rejesta ya kanisa fulani. Badala ya hivyo, akaeleza, washiriki walo ni watu ambao “wametakasa” (au, kuweka wakfu) wakati, vipawa, na maisha zao kwa Mungu, na ambao mbele yao wana taraja la kushiriki katika Ufalme wa kimbingu pamoja na Kristo. Hao, akasema, ni Wakristo ambao wameunganishwa katika vifungo vya upendo wa Kikristo na mambo yawapendezao wote, waitikiao mwelekezo wa roho ya Mungu, na watiio ukichwa wa Kristo. Ndugu Russell hakupendezwa na kusimamisha mpango mwingine, naye alipinga sana kuchangia kwa njia yoyote ufarakano uliokuwamo miongoni mwa wadaio kuwa Wakristo.
Wakati uleule, yeye alithamini sana uhitaji wa watumishi wa Bwana kukusanyika pamoja, kupatana na shauri kwenye Waebrania 10:23-25. Yeye binafsi alisafiri ili kutembelea na kujenga wasomaji wa Watch Tower na kuwaleta pamoja na wengine katika eneo lao wenyewe waliokuwa na kusudi lilelile. Mapema katika 1881 aliomba kwamba wale waliokuwa wakifanya mikutano kwa ukawaida wajulishe ofisi ya Watch Tower mahali mikutano hiyo ilipofanyiwa. Aliona thamani ya kuwawezesha kuwasiliana.
Hata hivyo, Ndugu Russell alikazia kwamba wao hawakuwa wakijaribu kuanzisha “tengenezo la kidunia.” Badala ya hivyo, akasema, “sisi twashikamana tu na hilo tengenezo la kimbingu—‘ambalo majina yalo yameandikwa mbinguni.’ (Ebr. 12:23; Luka 10:20.)” Kwa sababu ya historia mbaya ya Jumuiya ya Wakristo, rejezo kwa “tengenezo la kanisa” kwa kawaida lilikumbusha mtu juu ya ufarakano, kutawalwa na makasisi, na kuwa mshirika kwa msingi wa kushikamana na imani zilizotungwa na baraza la kidini. Hivyo, walipokuwa wakijitaja wenyewe, Ndugu Russell alihisi kwamba neno “ushirika” lilikuwa bora zaidi.
Yeye alijua sana kwamba mitume wa Kristo walikuwa wamefanyiza makutaniko na kuweka wazee katika kila moja. Lakini aliamini kwamba Kristo alikuwapo tena, ingawa ni kwa kutoonekana, na yeye binafsi alikuwa akitoa mwelekezo wa kuvunwa kwa mwisho kwa wale ambao wangekuwa warithi pamoja naye. Kwa sababu ya hali hizo, Ndugu Russell mwanzoni alihisi kwamba wakati wa pindi ya mavuno mpango wa wazee uliokuwa katika makutaniko ya Kikristo ya karne ya kwanza haukuhitajiwa.
Hata hivyo, kadiri Wanafunzi wa Biblia walivyoongezeka idadi, Ndugu Russell alipata kujua kwamba Bwana alikuwa akielekeza mambo kwa njia tofauti na ile ambayo yeye mwenyewe alikuwa ametarajia. Rekebisho katika maoni lilihitajiwa. Lakini kwa msingi gani?
Kutimiza Mahitaji ya Mapema ya Ushirika Wenye Kukua
Toleo la Watch Tower la Novemba 15, 1895, karibu lote lilizungumzia habari “Kwa Uzuri na kwa Utaratibu.” Kwa unyoofu, Ndugu Russell alikiri humo hivi: “Mitume walikuwa na mengi ya kusema kwa Kanisa la mapema kuhusu utaratibu katika makusanyiko ya watakatifu; na kwa wazi tumekuwa kidogo wenye kupuuza shauri hilo la hekima, tukihisi kidogo kuwa la umaana mdogo, kwa sababu Kanisa liko karibu sana na mwisho wa mwendo walo na mavuno ni wakati wa kutenganisha.” Ni kitu gani kilichowasukuma kulifikiria tena shauri hilo?
Makala hiyo iliorodhesha hali nne: (1) Ilikuwa wazi kwamba ukuzi wa kiroho wa watu mmoja-mmoja ulitofautiana na ule wa mwingine. Kulikuwa vishawishi, majaribu, magumu, na hatari ambazo wote hawakuwa tayari kwa kiwango kilekile kuyakabili. Hivyo, kulikuwa uhitaji wa waangalizi wenye hekima na wenye busara, wanaume wenye uzoefu na uwezo, wenye kupendezwa sana na kutunza masilahi ya kiroho ya wote na wenye uwezo wa kuwafundisha katika kweli. (2) Ilikuwa imeonwa kwamba kundi lilihitaji kulindwa na ‘mbwa-mwitu wenye kuvaa mavazi ya kondoo.’ (Mt. 7:15, KJ) Walihitaji kuimarishwa kwa kusaidiwa wapate maarifa kamili ya kweli. (3) Mambo yaliyoonwa yalikuwa yameonyesha kwamba kusipokuwa na mpango wa kuweka wazee kulinda kundi, wengine wangechukua cheo hicho waje kuona kundi kuwa lao wenyewe. (4) Bila mpango wenye utaratibu, watu mmoja-mmoja wenye uaminifu-mshikamanifu kuelekea kweli huenda wakaona utumishi wao mbalimbali kuwa usiotakwa kwa sababu ya uvutano wa wachache wasiokubaliana nao.
Kwa kufikiria hayo, Watch Tower lilitaarifu hivi: “Hatusiti kupendekeza kwa Makanisac kila mahali, iwe idadi yao ni kubwa au ndogo, shauri hilo la Kimitume, kwamba, katika kila kampuni, wazee wachaguliwe kutoka miongoni mwa idadi yao ‘kulisha’ na ‘kuangalia’ kundi.” (Mdo. 14:21-23; 20:17, 28) Makutaniko ya mahali yalifuata shauri hilo timamu la Kimaandiko. Hiyo ilikuwa hatua ya maana katika kuanzisha muundo wa kutaniko kupatana na yale yaliyokuwako katika siku za mitume.
Hata hivyo, kulingana na njia waliyoelewa mambo wakati ule, kuteuliwa kwa wazee, na mashemasi ili kuwasaidia, kulifanywa kwa kura ya kutaniko. Kila mwaka, au mara nyingi zaidi ikihitajiwa, sifa za wale wawezao kutumikia zilifikiriwa, na kura ikapigwa. Kwa msingi ulikuwa utaratibu wa kidemokrasi, lakini ambao ulibanwa na mipaka iliyokusudiwa kutenda kuwa ulinzi salama. Wote katika kutaniko walihimizwa wapitie kwa uangalifu sifa za Kibiblia na kuonyesha kwa kura, si maoni yao wenyewe, bali yale ambayo waliamini kuwa mapenzi ya Bwana. Kwa kuwa ni wale tu “waliojitakasa kabisa” waliokuwa na haki ya kupiga kura, kura yao ya umoja, ikiongozwa na Neno na roho ya Bwana, ilionwa kuwa yaonyesha mapenzi ya Bwana katika jambo hilo. Ijapokuwa huenda ikawa Ndugu Russell hakujua kabisa, pendekezo lake la mpango huo labda lilivutwa kwa kadiri fulani na azimio lake la kuepuka mfano wowote wa jamii ya makasisi iliyokwezwa na pia malezi yake mwenyewe akiwa tineja katika Congregational Church.
Buku la Millennial Dawn liitwalo The New Creation (lililotangazwa katika 1904) lilipozungumza tena kirefu juu ya fungu la wazee na njia ambayo walipaswa kuteuliwa, uangalifu wa pekee ulielekezwa kwenye Matendo 14:23. Konkodansi zilizotungwa na James Strong na Robert Young zilitajwa kuwa mamlaka kwa maoni ya kwamba ile taarifa “walikuwa wamewaweka rasmi kuwa wazee” (KJ) yapasa kutafsiriwa “walikuwa wamewateua kuwa wazee kwa wonyesho wa mikono.”d Baadhi ya tafsiri za Biblia hata husema kwamba wazee ‘waliwekwa kwa kura.’ (Literal Translation of the Holy Bible ya Young; Emphasised Bible ya Rotherham) Lakini ni nani aliyepaswa kupiga kura hiyo?
Kuchukua maoni ya kwamba kupiga kura kulipasa kufanywe na kutaniko lote hakukuleta matokeo yaliyotumainiwa sikuzote. Wale waliopiga kura walipaswa kuwa watu “waliojitakasa kabisa,” na baadhi ya wale waliochaguliwa walitimiza kikweli sifa za Kimaandiko nao walitumikia ndugu zao kwa unyenyekevu. Lakini kupiga kura mara nyingi kulionyesha upendeleo wa kibinafsi badala ya Neno na roho ya Mungu. Hivyo, katika Halle, Ujerumani, wakati wengine waliofikiri kwamba walipaswa kuwa wazee hawakupata vyeo walivyotaka, walisababisha migawanyiko mibaya. Katika Barmen, Ujerumani, miongoni mwa wale waliokuwa wachaguliwa katika 1927 mlikuwa wanaume waliopinga kazi ya Sosaiti, na kelele nyingi ilipigwa wakati wa kuonyesha mikono kwenye uchaguzi. Hivyo ilikuwa lazima kugeukia njia ya kupiga kura kwa siri.
Huko nyuma katika 1916, miaka mingi kabla ya visa hivyo, Ndugu Russell, akiwa na hangaiko kubwa, alikuwa ameandika: “Hali mbaya sana ya mambo huwa katika Madarasa fulani wakati wa kufanywa uchaguzi. Watumishi wa Kanisa hujaribu kuwa watawala, madikteta—nyakati nyingine hata wakishika uenyekiti wa mkutano yaonekana kwa lengo la kuona kwamba wao na marafiki wao wa pekee watachaguliwa kuwa Wazee na Mashemasi. . . . Baadhi yao hujaribu kutumia Darasa kwa faida yao kwa siri kwa kuwa na uchaguzi wakati fulani unaowafaa hasa wao na marafiki wao. Wengine hutafuta kujaza mkutano marafiki wao, wakileta watu walio wageni, ambao hawana wazo la kuhudhuria kwa ukawaida kwenye Darasa, bali huja tu kwa sababu ya urafiki ili kupigia kura mmoja wa marafiki wao.”
Je, walihitaji tu kujifunza jinsi ya kushughulikia machaguzi kwa utaratibu zaidi, wakitumia njia za kidemokrasi au kulikuwa jambo fulani katika Neno la Mungu ambalo walikuwa hawajalitambua?
Kupanga Mambo Kitengenezo ili Habari Njema Zipate Kuhubiriwa
Katika hatua ya mapema sana, Ndugu Russell alitambua kwamba mojapo madaraka ya maana sana kwa kila mshiriki wa kutaniko la Kikristo lilikuwa kazi ya kueneza evanjeli. (1 Pet. 2:9) Watch Tower lilieleza kwamba maneno ya kiunabii ya Isaya 61:1 hayakuhusu Yesu pekee bali pia wafuasi wake wote watiwa-mafuta kwa roho, yaani: “Bwana amenitia mafuta, niwahubiri wanyenyekevu habari njema,” au, kama vile King James Version hutafsiri nukuu la Yesu la fungu hilo, ‘Amenitia mafuta kuhubiri gospeli.’—Luka 4:18.
Mapema sana kama 1881, Watch Tower lilikuwa na makala “Wahubiri 1,000 Watakwa.” Hiyo ilikuwa sihi kwa kila mshiriki wa kutaniko atumie wakati wowote ambao angeweza (nusu saa, saa moja, au mbili, au tatu) kushiriki katika kueneza kweli ya Biblia. Wanaume na wanawake ambao hawakuwa na familia zilizowategemea na ambao wangeweza kutoa kabisa nusu au zaidi ya wakati wao kwa kazi ya Bwana walitiwa moyo waanze kazi wakiwa waeneza-evanjeli makolpota. Idadi hiyo ilitofautiana sana mwaka mmoja na mwingine, lakini kufikia 1885 kulikuwa tayari kama 300 waliokuwa wakishiriki kazi hiyo wakiwa makolpota. Baadhi yao pia walishiriki lakini kwa kadiri ndogo zaidi. Madokezo yalitolewa kwa makolpota kuhusu jinsi ya kufanya kazi yao. Lakini shamba lilikuwa kubwa, na angalau mwanzoni, waliteua eneo lao wenyewe na kwenda toka eneo moja hadi jingine sanasana kama walivyoona kuwa vema. Halafu walipokutana kwenye mikusanyiko, walikuwa wakifanya marekebisho yaliyohitajiwa ili kuratibu jitihada zao.
Mwaka huohuo ambao utumishi wa kolpota ulianza, Ndugu Russell alichapisha idadi fulani ya trakti (au vijitabu) vigawanywe bila malipo. Chenye kutokeza miongoni mwazo kilikuwa kile kijitabu Food for Thinking Christians, kilichogawanywa kufikia idadi ya nakala 1,200,000 katika miezi minne ya kwanza. Kazi iliyohusika katika kupanga uchapaji na ugawanyaji huo ndiyo iliyosababisha kufanyizwa kwa Zion’s Watch Tower Tract Society ili kuangalia mambo ya muhimu. Kuzuia kukatizwa kwa kazi ikiwa kifo chake chatukia, na ili kurahisisha kushughulikiwa kwa michango ipaswayo kutumiwa katika kazi, Ndugu Russell aliomba Sosaiti isajiliwe kisheria, na jambo hilo lilitiwa katika rekodi Desemba 15, 1884. Jambo hilo lilitokeza chombo cha kisheria kilichohitajiwa.
Uhitaji ulipozuka, ofisi za tawi za Watch Tower Society zilianzishwa katika nchi nyinginezo. Ya kwanza ilikuwa katika London, Uingereza, katika Aprili 23, 1900. Nyingine, katika Elberfeld, Ujerumani, katika 1902. Miaka miwili baadaye, kwenye ule upande mwingine wa dunia, tawi lilipangwa kitengenezo katika Melbourne, Australia. Wakati wa kuandika kitabu hiki, kuna matawi 99 ulimwenguni pote.
Ijapokuwa mipango ya kitengenezo iliyohitajiwa ili kutayarisha kiasi kikubwa cha fasihi ya Biblia ilikuwa ikisitawishwa, mwanzoni makutaniko yaliachwa yafanye mipango yao ya kugawanya hadharani habari hiyo. Katika barua yenye tarehe ya Machi 16, 1900, Ndugu Russell alieleza jinsi alivyoliona jambo hilo. Barua hiyo aliyopelekewa “Alexander M. Graham, na Kanisa katika Boston, Mass[achusetts],” ilisema hivi: “Kama vile nyinyi nyote mjuavyo, kusudi langu thabiti ni kuacha kila kampuni ya watu wa Bwana kusimamia mambo yao wenyewe, kulingana na maamuzi yao wenyewe, nikitoa madokezo, si kwa njia ya kuingilia [mambo], bali kwa njia tu ya shauri.” Hilo lilitia ndani si mikutano yao tu bali pia njia ambayo waliendesha huduma yao ya shambani. Hivyo, baada ya kuwapa akina ndugu shauri fulani litumikalo, alimalizia kwa elezo hili: “Hili ni dokezo tu.”
Utendaji fulani ulitaka mwelekezo hususa zaidi kutoka kwa Sosaiti. Kuhusiana na kuonyeshwa kwa ile “Photo-Drama of Creation,” kila kutaniko liliachwa liamue kama walikuwa na nia na uwezo wa kukodi jumba la maonyesho au jumba jingine katika mahali pao la kuionyeshea. Hata hivyo, ilikuwa lazima kuhamisha vifaa toka jiji hadi jiji, na ilikuwa lazima kufuata ratiba; hivyo, kwa sababu hizo mwelekezo kutoka makao makuu ulitolewa na Sosaiti. Kila kutaniko lilitiwa moyo liwe na Halmashauri ya Drama ya kushughulikia mipango ya kwao. Lakini msimamizi aliyepelekwa na Sosaiti alishughulikia kwa uangalifu yale mambo madogo-madogo ili kuhakikisha kwamba kila jambo limefanywa kwa utaratibu.
Kadiri miaka 1914 na kisha 1915 ilivyopita, Wakristo hao watiwa-mafuta kwa roho walingojea kwa hamu utimizo wa tumaini lao la kimbingu. Wakati uleule, walitiwa moyo waendelee kujishughulisha na utumishi wa Bwana. Hata ingawa waliona wakati wao uliobaki katika mwili kuwa mfupi, ilipata kuwa wazi kwamba ili kuendeleza kazi ya kuhubiri habari njema kwa njia ya utaratibu, mwelekezo zaidi ulihitajiwa kuliko wakati ambao walikuwa na idadi ya mamia wachache tu. Muda mfupi baada ya J. F. Rutherford kuwa msimamizi wa pili wa Watch Tower Society, mwelekezo huo ulianza kuwa na sura mpya. Toleo la Machi 1, 1917, la The Watch Tower lilitangaza kwamba, kuanzia hapo na kuendelea, ofisi ya Sosaiti itakuwa ikiwagawia makolpota na wafanyakazi wa uchungajie katika makutaniko maeneo yote ya kufanyia kazi. Mahali palipokuwa na wafanyakazi wenyeji na makolpota pia wakishiriki katika utumishi kama huo wa shambani katika jiji au wilaya, eneo liligawanywa miongoni mwao na halmashauri ya wilaya ya mahali iliyowekwa. Mpango huo ulichangia ugawanyaji wenye kutokeza kikweli wa The Finished Mystery katika muda wa miezi michache tu katika 1917-1918. Mpango huo ulikuwa wenye thamani pia katika kupata ugawanyaji wa kasi wa nakala 10,000,000 za ufichuo wenye nguvu wa Jumuiya ya Wakristo katika trakti iliyozungumzia habari “Kuanguka kwa Babiloni.”
Muda mfupi baada ya hilo, washiriki wa wafanyakazi wa usimamizi wa Sosaiti walikamatwa, na Juni 21, 1918, wakahukumiwa vifungo vya miaka 20 gerezani. Kazi ya kuhubiri habari njema ikakaribia sana kukoma. Je, huo ulikuwa ndio wakati ambao hatimaye wangeunganishwa na Bwana katika utukufu wa kimbingu?
Miezi michache baadaye, vita ikaisha. Mwaka uliofuata wakuu wa Sosaiti wakafunguliwa. Walikuwa wangali katika mwili. Hawakuwa wametarajia hilo, lakini walikata kauli kwamba lazima Mungu awe na kazi aliyotaka waifanye hapa duniani.
Walikuwa ndipo wametoka tu katika mitihani mikali ya imani yao. Hata hivyo, katika 1919, The Watch Tower liliwaimarisha kwa mafunzo ya Kimaandiko yenye kuwachochea juu ya kichwa “Wabarikiwa Ni Wasioogopa.” Hayo yalifuatwa na makala “Fursa za Utumishi.” Lakini ndugu hawakuwazia usitawi mkubwa wa kitengenezo ambao ungetukia wakati wa miongo ambayo ingefuata.
Kielelezo Kifaacho kwa Kundi
Ndugu Rutherford alijua kwamba ili kazi iendelee kusonga mbele kwa njia ya utaratibu na ya umoja, hata wakati uwe mfupi kadiri gani, kielelezo kifaacho kwa kundi ni cha muhimu. Yesu alikuwa amewaeleza wafuasi wake kuwa kama kondoo, na kondoo hufuata mchungaji wao. Bila shaka, Yesu mwenyewe ndiye Mchungaji Mwema, lakini yeye hutumia pia wanaume wazee, au wazee, wakiwa wachungaji wadogo wa watu wake. (1 Pet. 5:1-3) Wazee hao lazima wawe wanaume ambao wao wenyewe hushiriki katika kazi ambayo Yesu aliwagawia na ambao huwatia wengine moyo wafanye hivyo. Ni lazima wawe kikweli na roho ya kueneza evanjeli. Hata hivyo, wakati wa ugawanyaji wa The Finished Mystery, baadhi ya wazee walikuwa wamekataa; wengine hata walisema waziwazi sana wakiwavunja wengine moyo wasishiriki.
Hatua ya maana sana kuelekea kusahihishwa kwa hali hiyo ilichukuliwa katika 1919 gazeti The Golden Age lilipoanza kutangazwa. Hilo lingekuwa kifaa chenye nguvu cha kutangaza Ufalme wa Mungu kuwa utatuzi pekee wenye kudumu kwa matatizo ya wanadamu. Kila kutaniko ambalo lilitaka kushiriki katika utendaji huo lilialikwa liombe kwamba lisajiliwe na Sosaiti kuwa “tengenezo la utumishi.” Halafu mwelekezi, au mwelekezi wa utumishi kama alivyokuja kujulikana, ambaye hakulazimika kuchaguliwa kila mwaka, aliwekwa na Sosaiti.f Akiwa ndiye mwakilishi wa Sosaiti mwenyeji, alipaswa kupanga kazi, kutoa migawo ya eneo, na kutia kutaniko moyo lishiriki katika utumishi wa shambani. Hivyo, sambamba na wazee na mashemasi waliochaguliwa kidemokrasi, mpango wa kitengenezo wa aina nyingine ulianza kufanya kazi, ambao ulitambua mamlaka yenye kuweka rasmi yaliyo nje ya kutaniko la mahali na ambao ulitia mkazo mwingi zaidi katika kuhubiriwa kwa habari njema za Ufalme wa Mungu.g
Wakati wa miaka iliyofuata, kazi ya kupiga mbiu ya Ufalme ilipewa msukumo mkubwa, kana kwamba kwa kani isiyoweza kukinzwa. Matukio ya 1914 na baada ya hapo yalikuwa yameonyesha wazi kwamba ule unabii mkubwa ambao katika huo Bwana Yesu Kristo alikuwa ameueleza umalizio wa mfumo wa kale ulikuwa ukitimizwa. Kukiwa na maoni hayo, katika 1920, The Watch Tower lilionyesha kwamba kama ilivyotabiriwa kwenye Mathayo 24:14, huu ndio wakati wa kupiga mbiu ya habari njema kuhusu “mwisho wa utaratibu wa mambo wa kale na kusimamishwa kwa ufalme wa Mesiya.”h (Mt. 24:3-14) Baada ya kuhudhuria mkusanyiko wa Wanafunzi wa Biblia katika Cedar Point, Ohio, katika 1922, wajumbe waliondoka shime hii ikiwa inalia masikioni mwao: “Mtangazeni, mtangazeni, mtangazeni, Mfalme na ufalme wake.” Daraka la Wakristo wa kweli lilipata kutambuliwa wazi zaidi na likakaziwa zaidi katika 1931 wakati jina Mashahidi wa Yehova lilipokubaliwa.
Ilikuwa wazi kwamba Yehova alikuwa amegawia watumishi wake kazi ambayo wote wangeweza kushiriki. Kulikuwa itikio lenye idili. Wengi walifanya marekebisho katika maisha zao ili kutumia wakati wao wote katika kazi hiyo. Hata miongoni mwa wale waliotumia sehemu tu ya wakati, idadi kubwa ilitumia siku nzimanzima katika utumishi wa shambani mwishoni mwa juma. Wakiitikia kitia-moyo kilichokuwa katika Mnara wa Mlinzi na Informant (Mpasha-Habari) katika 1938 na 1939, wengi kati ya Mashahidi wa Yehova wakati huo walijitahidi kwa kudhamiria kutumia saa 60 kila mwezi katika utumishi wa shambani.
Miongoni mwa Mashahidi hao wenye bidii, walikuwamo watumishi wa Yehova wengi wanyenyekevu na waliojitoa, ambao walikuwa wazee katika makutaniko. Hata hivyo, katika sehemu nyingine, wakati wa miaka ya 1920 na mapema katika miaka ya 1930, kulikuwako pia ukinzani mwingi kwa wazo la kila mtu kushiriki katika utumishi wa shambani. Wazee waliochaguliwa kidemokrasi mara nyingi walisema waziwazi wakipinga yale ambayo The Watch Tower lilisema juu ya daraka la kuhubiria watu walio nje ya kutaniko. Kukataa kusikiliza yale ambayo roho ya Mungu ilihitaji kuliambia kutaniko juu ya jambo hilo kwa njia ya Maandiko Matakatifu, kulizuia umiminikaji wa roho ya Mungu katika vikundi hivyo.—Ufu. 2:5, 7.
Hatua zilichukuliwa katika 1932 kusahihisha hali hiyo. Jambo la kuhangaikiwa zaidi halikuwa kama baadhi ya wazee mashuhuri wangeudhiwa au kama baadhi ya wale walioshirikiana na makutaniko wangeondoka. Bali, tamaa ya akina ndugu ilikuwa kumpendeza Yehova na kufanya mapenzi yake. Kwa kusudi hilo, matoleo ya Agosti 15 na Septemba 1 ya Mnara wa Mlinzi (Kiingereza) mwaka huo yalizungumzia habari “Tengenezo la Yehova.”
Makala hizo zilionyesha waziwazi kwamba wote ambao walikuwa sehemu ya tengenezo la Yehova kwelikweli wangeshiriki kazi ambayo Neno lake lilisema lazima ifanywe katika pindi hii ya wakati. Makala hizo zilitetea maoni ya kwamba uzee wa Kikristo si cheo ambacho kwacho mtu angeweza kuchaguliwa bali ilikuwa hali ifikiwayo kwa ukuzi wa kiroho. Mkazo wa pekee ulitolewa kwenye sala ya Yesu kwamba wafuasi wake wangeweza ‘wote kuwa mmoja’—katika muungano na Mungu na Kristo, na hivyo kuwa na umoja mtu na mwenzake katika kufanya mapenzi ya Mungu. (Yn. 17:21, NW) Nayo matokeo yakawa nini? Makala ya pili ilijibu hivi kwamba “kila mmoja wa mabaki lazima awe shahidi kwa jina na ufalme wa Yehova Mungu.” Wowote walioshindwa au waliokataa kufanya yale ambayo wangeweza kwa kadiri fulani kushiriki katika kutoa ushahidi hadharani hawangepewa uangalizi.
Kwenye umalizio wa funzo la makala hizo, makutaniko yalialikwa yapitishe azimio yakionyesha kukubali kwao. Hivyo uchaguzi wa kila mwaka wa kutaniko wa wanaume kuwa wazee na mashemasi ukaondolewa. Katika Belfast, Ireland Kaskazini, kama kwingineko, baadhi ya wale waliokuwa hapo kwanza “wazee wa kuchaguliwa” waliondoka; wengine mmoja-mmoja walioshiriki maoni yao waliondoka pamoja nao. Hilo lilitokeza upungufu wa idadi lakini kuimarishwa kwa tengenezo zima. Wale waliobaki walikuwa watu waliokuwa tayari kubeba daraka la Kikristo la kutoa ushahidi. Badala ya kupigia wazee kura, makutaniko—yakiwa bado yanatumia njia ya kidemokrasi—yaliteua halmashauri ya utumishii ambayo washiriki wayo walikuwa wanaume wakomavu kiroho walioshiriki kwa bidii kutoa ushahidi hadharani. Washiriki wa kutaniko pia walipiga kura kuchagua mwenyekiti wa kusimamia mikutano yao pamoja na mwandishi na mweka-hazina. Wote hao walikuwa wanaume waliokuwa mashahidi wa Yehova watendaji.
Wanaume waliopendezwa si na cheo chao binafsi bali na kufanya kazi ya Mungu wakiwa sasa wamepewa uangalizi wa kutaniko—kutoa ushahidi kwa jina na Ufalme wake—na ambao walikuwa wakiweka kielelezo kwa kuishiriki wao wenyewe, kazi ilisonga mbele kwa utaratibu zaidi. Ijapokuwa hawakuwa wakijua wakati ule, kulikuwa mengi ya kufanywa, ushahidi ulioenezwa zaidi kuliko ule uliokuwa tayari umetolewa, kukusanya ndani ambako hawakuwa wametarajia. (Isa. 55:5) Kwa wazi Yehova alikuwa akiwatayarisha kwa ajili ya kazi hiyo.
Wachache wenye tumaini la uhai wa milele duniani walikuwa wameanza kushirikiana nao.j Hata hivyo, Biblia ilitabiri kukusanywa kwa halaiki kubwa (au, umati mkubwa) kwa kusudi la kuhifadhiwa kwao kuipita dhiki kubwa. (Ufu. 7:9-14) Katika 1935 utambulisho wa hii halaiki kubwa ulielezwa wazi. Mabadiliko katika kuteuliwa kwa waangalizi wakati wa miaka ya 1930 yalilitayarisha tengenezo liweze kutunza vizuri zaidi kazi ya kuwakusanya, kuwafundisha, na kuwazoeza.
Kwa walio wengi kati ya Mashahidi wa Yehova, kazi hiyo iliyopanuka ilikuwa usitawi wenye kusisimua. Huduma yao ya shambani ilichukua umaana mpya. Hata hivyo, baadhi yao hawakuwa na hamu ya kuhubiri. Walijizuia kushiriki kazi, nao walijaribu kutetea kutotenda kwao kwa kutoa hoja kwamba hakuna halaiki kubwa ambayo ingekusanywa mpaka baada ya Har–Magedoni. Lakini walio wengi walitambua fursa iliyoongezwa ya kuonyesha uaminifu-mshikamanifu wao kwa Yehova na upendo wao kwa wanadamu wenzao.
Wale wa umati mkubwa walifaanaje na muundo wa tengenezo? Walionyeshwa daraka ambalo Neno la Mungu liligawia lile “kundi dogo” la watiwa-mafuta kwa roho, nao walifanya kazi kwa nderemo kupatana na mpango huo. (Luka 12:32-44, NW) Pia walijifunza kwamba, kama vile watiwa-mafuta kwa roho, walikuwa na daraka la kushiriki habari njema na wengine. (Ufu. 22:17) Kwa kuwa walitaka kuwa raia za kidunia za Ufalme wa Mungu, Ufalme huo ulipaswa kutangulizwa maishani mwao, nao walipaswa kuwa wenye bidii katika kuambia wengine juu yao. Ili wafaane na elezo la Biblia la wale ambao wangehifadhiwa kuipita ile dhiki kubwa kuingia katika ulimwengu mpya wa Mungu, lazima wawe watu ambao ‘hufuliza kulia kwa sauti kubwa, wakisema: “Sisi tunawiwa wokovu na Mungu wetu, aketiye juu ya hicho kiti cha ufalme, na kwa Mwana-Kondoo.”’ (Ufu. 7:10, 14, NW) Katika 1937, idadi zao zilipoanza kukua na bidii yao kwa ajili ya Bwana ikadhihirika, walialikwa pia wasaidie kuchukua furushi la daraka katika uangalizi wa kutaniko.
Hata hivyo, walikumbushwa kwamba tengenezo ni la Yehova, si la mwanadamu yeyote. Hakukupaswa kuwe na mgawanyiko kati ya mabaki ya watiwa-mafuta kwa roho na wale wa umati mkubwa wa kondoo wengine. Walipaswa kufanya kazi pamoja wakiwa ndugu na dada katika utumishi wa Yehova. Kama vile Yesu alivyokuwa amesema, “Nina kondoo wengine, ambao si wa zizi hili; hao pia lazima niwalete, nao watasikiliza sauti yangu, nao watakuwa kundi moja, mchungaji mmoja.” (Yn. 10:16, NW) Uhalisi wa jambo hilo ulikuwa ukidhihirika.
Usitawi wenye kustaajabisha ulikuwa umetukia katika tengenezo katika kipindi kifupi cha wakati. Lakini je, yalikuwako mambo zaidi yaliyohitaji kufanywa ili mambo ya makutaniko yaweze kuongozwa kwa upatani kabisa na njia za Yehova kama zilivyoonyeshwa katika Neno lake lililopuliziwa?
Tengenezo la Kitheokrasi
“Theokrasi” humaanisha “utawala wa Mungu.” Je, hiyo ndiyo aina ya utawala iliyoongoza makutaniko? Je, waliabudu Yehova na pia kumtegemea kwa mwelekezo wa mambo yao ya kutaniko? Je, walipatana kabisa na yale yaliyosemwa juu ya mambo hayo katika Neno lake lililopuliziwa? Makala yenye sehemu mbili kuhusu “Tengenezo” iliyotokea katika Mnara wa Mlinzi (Kiingereza) la Juni 1 na 15, 1938, ilitaarifu waziwazi hivi: “Tengenezo la Yehova si la kidemokrasi hata kidogo. Yehova ndiye mkuu kupita wote, na serikali yake au tengenezo ni ya kitheokrasi kabisa.” Hata hivyo, katika makutaniko ya mahalimahali ya Mashahidi wa Yehova wakati ule, taratibu za kidemokrasi zilikuwa zingali zinatumiwa katika kuteua walio wengi kati ya wale waliokabidhiwa uangalizi wa mikutano na utumishi wa shambani. Mabadiliko zaidi yalifaa.
Lakini je, Matendo 14:23 halikuonyesha kwamba wazee katika makutaniko walikuwa wamewekwa kwenye cheo kwa ‘kunyoosha mkono,’ kama katika kupiga kura? Ya kwanza kati ya makala hizo za Mnara wa Mlinzi yenye kichwa “Tengenezo” ilikiri kwamba andiko hilo lilikuwa limeeleweka kimakosa wakati uliopita. Haikuwa kwa ‘kunyoosha mkono’ upande wa washiriki wote wa kutaniko kwamba kuweka rasmi kulikuwa kumefanywa miongoni mwa Wakristo wa karne ya kwanza. Badala ya hivyo, ilionyeshwa, mitume na wale waliopewa mamlaka nao ndio ‘walionyoosha mikono yao.’ Hilo lilifanywa si kwa kushiriki kupiga kura katika kutaniko bali kwa kuweka mikono yao juu ya watu mmoja-mmoja waliostahili. Hiyo ilikuwa ishara ya uthibitisho, kibali, au uwekaji rasmi.k Nyakati nyingine makutaniko ya Kikristo ya mapema yalipendekeza wanaume waliostahili, lakini uteuzi au kibali cha mwisho vilitolewa na mitume, ambao walikuwa wamepewa utume moja kwa moja na Kristo, au kibali kilitolewa na wale waliopewa mamlaka na mitume. (Mdo. 6:1-6) Mnara wa Mlinzi lilivuta uangalifu kwenye uhakika wa kwamba ni katika barua kwa waangalizi wenye daraka tu (Timotheo na Tito) kwamba mtume Paulo, chini ya mwelekezo wa roho takatifu, alitoa maagizo waangalizi wawekwe. (1 Tim. 3:1-13; 5:22; Tito 1:5) Hakuna yoyote ya barua zilizopuliziwa ambazo zilipelekwa kwenye makutaniko zilizokuwa na maagizo kama hayo.
Basi, kuweka rasmi kwenye utumishi kwa sasa katika makutaniko kungefanywaje? Uchanganuzi wa Mnara wa Mlinzi la tengenezo la kitheokrasi ulionyesha kutoka Maandiko kwamba Yehova alimweka rasmi Yesu Kristo kuwa “Kichwa cha . . . kutaniko”; kwamba Kristo akiwa Bwana-Mkubwa aliporudi, angeaminisha “mtumwa [wake] mwaminifu na mwenye busara” daraka “juu ya mali zake zote”; kwamba washiriki wa mtumwa mwaminifu huyo ni wale wote duniani waliokuwa wametiwa mafuta kwa roho takatifu kuwa warithi-washirika wa Kristo na ambao kwa umoja watumikia chini ya mwelekezo wake; na kwamba Kristo angetumia jamii ya mtumwa huyo ikiwa chombo chake katika kuandaa uangalizi uliohitajiwa kwa makutaniko. (Kol. 1:18; Mt. 24:45-47; 28:18, NW) Ungekuwa wajibu wa jamii ya mtumwa huyo kutumia kwa njia ya sala maagizo yaliyotaarifiwa waziwazi katika Neno la Mungu lililopuliziwa, akilitumia kuamua ni nani waliostahili kuwekwa rasmi kwenye vyeo vya utumishi.
Kwa kuwa chombo kionekanacho ambacho kingetumiwa na Kristo ni mtumwa mwaminifu na mwenye busara (na mambo ya hakika ya historia ya kisasa ambayo tayari yamefikiriwa huonyesha kwamba “mtumwa” huyo hutumia Watch Tower Society ikiwa chombo cha kisheria), Mnara wa Mlinzi lilifafanua kwamba utaratibu wa kitheokrasi ungetaka kwamba kuwekwa rasmi kwenye utumishi kwapasa kufanywe kupitia chombo hicho. Kama vile makutaniko katika karne ya kwanza yalivyotambua baraza lenye kuongoza katika Yerusalemu, ndivyo leo makutaniko hayangesitawi kiroho bila kitovu cha usimamizi.—Mdo. 15:2-30; 16:4, 5.
Hata hivyo, ili kuona mambo kama yanavyohusiana, ilionyeshwa kwamba Mnara wa Mlinzi lirejezeapo “Sosaiti,” hilo halimaanishi, chombo cha kisheria tu, bali kikundi cha Wakristo watiwa-mafuta kilichosimamisha chombo hicho cha kisheria na ambacho hukitumia. Hivyo neno hilo lilimaanisha mtumwa mwaminifu na mwenye busara na Baraza Linaloongoza layo.
Hata kabla ya makala za Mnara wa Mlinzi zenye kichwa “Tengenezo” kutangazwa katika 1938, wakati makutaniko katika London, New York, Chicago, na Los Angeles yalikuwa yamekua kufikia hatua ya kwamba ilifaa kuyagawanya kuwa vikundi vidogo zaidi, yalikuwa yameomba Sosaiti iweke watumishi wayo wote. Toleo la Juni 15, 1938, la Mnara wa Mlinzi (Kiingereza) sasa lilialika makutaniko mengine yote yachukue hatua kama hiyo. Kwa kusudi hilo, azimio lifuatalo lilidokezwa:
“Sisi, kampuni ya watu wa Mungu waliochukuliwa kwa ajili ya jina lake, na sasa tukiwa kwenye . . . . . . . . . . . . , twatambua kwamba serikali ya Mungu ni theokrasi kabisa na kwamba Kristo Yesu yumo hekaluni na anasimamia na kudhibiti kabisa tengenezo la Yehova lionekanalo, pamoja na lile lisiloonekana, na kwamba ‘SOSAITI’ ndiyo mwakilishi aonekanaye wa Bwana duniani, na hivyo sisi twaomba ‘Sosaiti’ ipange kitengenezo kampuni hii kwa ajili ya utumishi na kuweka wale watumishi mbalimbali humo, ili sisi sote tuweze kufanya kazi pamoja katika amani, uadilifu, upatani na umoja kabisa. Twashikamanisha hapa orodha ya majina ya watu katika kampuni hii ambao kwetu waonekana kuwa wakomavu kikamili zaidi na ambao kwa hiyo waonekana kuwa ndio wafaao zaidi kujaza vile vyeo vihusuvyo vionyeshwavyo kwa ajili ya utumishi.”l
Karibu makutaniko yote ya Mashahidi wa Yehova yalikubali mara moja mpango huo. Yale machache yaliyokataa kuufuata yaliacha upesi kuwa na ushiriki wowote katika kupiga mbiu ya Ufalme na hivyo yakaacha kuwa Mashahidi wa Yehova.
Manufaa za Mwelekezo wa Kitheokrasi
Ni wazi kwamba ikiwa mafundisho, viwango vya mwenendo, na taratibu za kitengenezo au za kutoa ushahidi zingeamuliwa kimahali, upesi tengenezo lingepoteza utambulisho na umoja walo. Ndugu wangeweza kwa urahisi kugawanywa na tofauti za kijamii, kitamaduni, na kitaifa. Mwelekezo wa kitheokrasi, kwa upande mwingine, ungehakikisha kwamba manufaa kutoka kwa maendeleo ya kiroho zingefikia makutaniko yote ulimwenguni pote bila kizuizi. Kungekuja kuwako kwa njia hiyo ule umoja wa kweli ambao Yesu alisali kwamba ungekuwako miongoni mwa wafuasi wake wa kweli, na kazi ya kueneza evanjeli ambayo aliamuru ingetimizwa kikamili.—Yn. 17:20-22.
Hata hivyo, imedaiwa na baadhi ya watu kwamba kwa kutetea badiliko hilo la kitengenezo, J. F. Rutherford alikuwa tu akijaribu kupata udhibiti zaidi juu ya Mashahidi na kwamba alitumia njia hiyo kuonyesha mamlaka yake mwenyewe. Je, kweli ndivyo ilivyokuwa? Hakuna shaka kwamba Ndugu Rutherford alikuwa mwanamume mwenye masadikisho imara. Alisema waziwazi na kwa nguvu, bila kuridhiana kwa ajili ya yale aliyoamini kuwa kweli. Angeweza kutenda kwa ukali katika kushughulikia hali atambuapo kwamba watu walijihangaikia zaidi wao binafsi kuliko kuhangaikia kazi ya Bwana. Lakini Ndugu Rutherford alikuwa mnyenyekevu kikweli mbele za Mungu. Kama vile Karl Klein, ambaye alikuja kuwa mshiriki wa Baraza Linaloongoza katika 1974, alivyoandika baadaye: “Sala za Ndugu Rutherford kwenye ibada ya asubuhi . . . zilinifanya nimpende sana. Ingawa alikuwa na sauti yenye nguvu sana, asemapo na Mungu alisikika kama kivulana tu mwenye kuongea na baba. Lo! hilo lilifunua uhusiano mzuri pamoja na Yehova kama nini!” Ndugu Rutherford alisadiki kabisa utambulisho wa tengenezo la Yehova lionekanalo, naye alijaribu kuhakikisha kwamba hakuna mwanamume au kikundi cha wanaume ambacho kingeweza kuzuia ndugu wa mahali fulani wasipokee manufaa kamili za chakula cha kiroho na mwelekezo ambao Yehova alikuwa akiandalia watumishi Wake.
Ijapokuwa Ndugu Rutherford alitumikia kwa miaka 25 akiwa msimamizi wa Watch Tower Society naye alitumia nishati zake zote kusogeza mbele kazi ya tengenezo, hakuwa ndiye kiongozi wa Mashahidi wa Yehova, naye hakutaka kuwa hivyo. Kwenye mkusanyiko katika St. Louis, Missouri, katika 1941, muda mfupi kabla ya kifo chake, alitoa hotuba kuhusu uongozi, akisema: “Mimi nataka wageni wowote waliopo hapa wajue nyinyi mwafikiri nini juu ya mwanamume fulani kuwa kiongozi wenu, ili wasipate kusahau. Kila wakati kitu fulani kizukapo na kuanza kukua, wao husema kuna mwanamume fulani kiongozi aliye na wafuasi wengi. Ikiwa kuna mtu yeyote katika wasikilizaji hawa afikiriye kwamba mimi, mwanamume huyu anayesimama hapa, ndiye kiongozi wa mashahidi wa Yehova, sema Ndiyo.” Itikio lilikuwa kimya chenye kutia mkazo, kikikatizwa tu na “La” yenye mkazo kutoka kwa watu kadhaa katika wasikilizaji. Msemaji akaendelea: “Ikiwa nyinyi mlio hapa mwaamini kwamba mimi ni mmoja tu wa watumishi wa Bwana, nasi tunafanya kazi bega kwa bega katika umoja, tukimtumikia Mungu na kumtumikia Kristo, semeni Ndiyo.” Kwa umoja kusanyiko likanguruma “Ndiyo!” yenye kukata maneno. Mwezi uliofuata wasikilizaji katika Uingereza waliitikia kwa njia hiyohiyo kabisa.
Katika sehemu fulani manufaa za tengenezo la kitheokrasi zilihisiwa upesi. Kwingineko, ilichukua muda mrefu kidogo; wale ambao hawakuthibitika kuwa watumishi wanyenyekevu, wenye kukomaa, waliondolewa baada ya wakati, na wengine wakawekwa rasmi.
Hata hivyo, kadiri taratibu za kitheokrasi zilivyopata kuimarika kikamili zaidi, Mashahidi wa Yehova walishangilia kuona likitukia lile lililotabiriwa kwenye Isaya 60:17. Akitumia maneno ya kitamathali kuonyesha hali bora zaidi ambazo zingekuja kuwako miongoni mwa watumishi wa Mungu, Yehova asema humo hivi: “Badala ya shaba nitaleta dhahabu, na badala ya chuma nitaleta fedha, na badala ya mti, shaba, na badala ya mawe, chuma; tena nitawafanya wasimamizi wako wawe amani, na hao wakutozao fedha kuwa haki.” Hiyo haielezi yale ambayo wanadamu wangefanya, bali, yale ambayo Mungu mwenyewe angefanya na manufaa ambazo watumishi wake wangepokea wayatiipo. Lazima amani ienee kati yao. Upendo wa uadilifu lazima uwe kani iwasukumayo kutumikia.
Kutoka Brazili, Maud Yuille, mke wa mwangalizi wa tawi, alimwandikia Ndugu Rutherford hivi: “Ile makala ‘Tengenezo’ katika Minara ya Juni 1 na 15 [1938] ilinisukuma nikueleze kwa maneno machache wewe, ambaye utumishi wako wa uaminifu Yehova anatumia, shukrani zangu kwa Yehova kwa mpango mzuri sana ambao ameufanya kwa ajili ya tengenezo lake lionekanalo, kama ilivyoelezwa katika Minara ya Mlinzi hii miwili. . . . Ni kitulizo kama nini kuona mwisho wa ‘Uhuru wa Vijiji,’ kutia na ‘haki za wanawake’ na utaratibu mwingineo usiopatana na Maandiko uliotiisha baadhi ya watu kwa maoni ya kimahali na maamuzi ya watu mmoja-mmoja, badala ya kwa [Yehova Mungu na Yesu Kristo], na hivyo kuleta suto juu ya jina la Yehova. Ni kweli kwamba ni ‘katika wakati uliopita juzijuzi tu kwamba Sosaiti imewaweka wote katika tengenezo kuwa “watumishi”’, hata hivyo naona kwamba kwa miaka mingi kabla ya wakati huo katika kuandikiana kwako na ndugu zako umejikiri mwenyewe kuwa ‘ndugu yenu na mtumishi, kwa neema Yake’.”
Kuhusu rekebisho hilo la kitengenezo, tawi katika British Isles liliripoti hivi: “Matokeo mazuri yalo yalikuwa yenye kushangaza sana. Lile elezo lalo la kimashairi na kiunabii katika Isaya sura ya sitini linajaa uzuri lakini si lenye kutiwa chumvi. Kila mtu katika kweli alikuwa akiongea juu yalo. Ndilo lililokuwa kichwa kikuu cha mazungumzo. Hisi ya ujumla ya kutiwa nguvu ilienea—utayari wa kusonga mbele na pigano lenye kuelekezwa vizuri. Kadiri wasiwasi wa ulimwengu ulivyoongezeka, shangwe katika utawala wa kitheokrasi ilikuwamo tele.”
Waangalizi Wasafirio Waimarisha Makutaniko
Vifungo vya kitengenezo viliimarishwa zaidi likiwa tokeo la utumishi wa waangalizi wasafirio. Katika karne ya kwanza, mtume Paulo alishiriki kwa kutokeza sana katika utendaji huo. Nyakati nyingine, wanaume kama vile Barnaba, Timotheo, na Tito waliushiriki pia. (Mdo. 15:36; Flp. 2:19, 20; Tito 1:4, 5) Wote walikuwa waeneza-evanjeli wenye bidii. Kwa kuongezea, walitia moyo makutaniko kwa hotuba zao. Masuala yalipozuka ambayo yangeweza kuathiri umoja wa makutaniko, yalipelekwa kwenye baraza kuu lenye kuongoza. Halafu, “walipoendelea kusafiri kuyapitia majiji,” wale waliokabidhiwa madaraka walikuwa “wakiwakabidhi wale wa huko maagizo yaliyokuwa yameamuliwa na mitume na wanaume wazee waliokuwa katika Yerusalemu ili yashikwe.” Matokeo yakawa nini? “Makutaniko yakaendelea kufanywa imara katika imani na kuongezeka idadi siku baada ya siku.”—Mdo. 15:1–16:5; 2 Kor. 11:28, NW.
Tayari katika miaka ya 1870, Ndugu Russell alikuwa akizuru vile vikundi vya Wanafunzi wa Biblia—vya watu wawili na vya watatu pamoja na vikundi vikubwa zaidi—ili kuwajenga kiroho. Ndugu wengine wachache walishiriki katika miaka ya 1880. Halafu, katika 1894, mipango ilifanywa kwa Sosaiti ili wasemaji waliostahili vizuri wasafiri kwa ukawaida zaidi ili kusaidia Wanafunzi wa Biblia wakue katika ujuzi na uthamini kwa ajili ya kweli na kuwavuta karibukaribu zaidi.
Ikiwezekana, msemaji alikuwa akitumia siku moja au labda siku kadhaa pamoja na kikundi, akitoa hotuba moja au mbili za watu wote na kisha, kuzuru vile vikundi vidogo zaidi na watu mmoja-mmoja ili kuzungumza mambo yenye kina zaidi ya Neno la Mungu. Jitihada ilifanywa ili kila kikundi katika Marekani na Kanada kitembelewe mara mbili kwa mwaka, ingawa kwa kawaida si ndugu yuleyule alifanya hivyo. Katika kuteua wasemaji hao wasafirio, mkazo uliwekwa juu ya upole, unyenyekevu, na uelewevu mzuri wa kweli pamoja na ushikamano kwayo wa uaminifu-mshikamanifu na uwezo wa kuifundisha kwa uwazi. Wao hawakuwa jamii ya wahudumu wenye kulipwa. Waliandaliwa tu chakula na mahali pa kulala na ndugu wenyeji, na kwa kadiri ilivyohitajiwa, Sosaiti iliwasaidia kwa gharama za usafiri. Wakaja kujulikana kuwa “mapilgrimu” (wasafiri).
Wengi kati ya wawakilishi hao wa Sosaiti wasafirio walipendwa sana na wale waliotumikia. A. H. Macmillan, Mkanada, anakumbukwa kuwa ndugu ambaye kwake Neno la Mungu lilithibitika kuwa “kama moto uwakao.” (Yer. 20:9) Alilazimika kuongea juu yalo, naye aliongea, akisema kwa wasikilizaji katika Kanada na pia katika sehemu nyingi za Marekani na nchi nyinginezo. William Hersee, pilgrimu mwingine, hukumbukwa kwa shauku nyingi kwa sababu ya uangalifu wa pekee aliowapa vijana. Sala zake pia ziliacha uvutano wenye kudumu akilini mwao kwa sababu zilionyesha hali ya kiroho yenye kina iliyovuta sana mioyo ya wote vijana kwa wazee.
Usafiri haukuwa rahisi kwa mapilgrimu katika siku hizo za mapema. Kwa kielelezo, ili kutumikia kikundi karibu na Klamath Falls, Oregon, Edward Brenisen alisafiri kwanza kwa garimoshi, kisha usiku kwa gari la kukokotwa na farasi, na hatimaye kwa kigari chenye kutikisatikisa wasafiri kilipokuwa kikisafiri milimani kuelekea kwenye shamba ambako wangekutana. Mapema asubuhi, siku baada ya mkutano wao, ndugu mmoja alimpa farasi amwendeshe kilometa zipatazo 100 kwenda kwenye kituo cha garimoshi kilichokuwa karibu zaidi ili aweze kusafiri kwenda kwenye mgawo wake uliofuata. Yalikuwa maisha magumu, lakini jitihada za mapilgrimu zilikuwa na matokeo mazuri. Watu wa Yehova waliimarishwa, wakaunganishwa pamoja katika uelewevu wao wa Neno la Mungu, na wakavutwa pamoja karibu zaidi hata ingawa walitawanyika sana kijiografia.
Katika 1926, Ndugu Rutherford alianza kutumia mipango iliyobadili kazi ya mapilgrimu kutoka ile ya wasemaji wasafirio tu kuwa ile ya wasimamizi na waendelezaji wasafirio wa utumishi wa shambani wa makutaniko. Ili kukazia madaraka yao mapya, katika 1928 waliitwa waelekezi wa utumishi wa kimkoa. Walifanya kazi pamoja na ndugu wenyeji, wakiwapa maagizo ya kibinafsi katika utumishi wa shambani. Wakati huo iliwezekana kwao kufikia kila kutaniko katika Marekani na katika baadhi ya nchi nyinginezo mara moja hivi kwa mwaka, huku wakizuru pia watu mmoja-mmoja na vikundi vidogo ambavyo havikuwa vimepangwa kitengenezo kwa ajili ya utumishi.
Wakati wa miaka iliyofuata, kazi ya waangalizi wasafirio ilipata marekebisho mbalimbali.a Ilizidishwa sana katika 1938 watumishi wote katika makutaniko walipowekwa rasmi kwa njia ya kitheokrasi. Ziara kwenye makutaniko kwa vipindi vya ukawaida wakati wa miaka michache iliyofuata zilitoa fursa ya kuandaa mazoezi ya kibinafsi kwa kila mmoja wa watumishi waliowekwa rasmi na kuongeza msaada katika utumishi wa shambani kwa kila mmoja. Katika 1942, kabla ya waangalizi wasafirio kupelekwa tena kwenye makutaniko, walipewa mafunzo mengi sana; likiwa tokeo, kazi yao ilitekelezwa kwa upatani mkubwa zaidi. Ziara zao zilikuwa fupi sana (siku moja hadi tatu, ikitegemea ukubwa wa kutaniko). Katika pindi hiyo walichunguza rekodi za kutaniko, wakakutana na watumishi wote ili kutoa shauri lolote lililohitajiwa, wakatoa hotuba moja au zaidi kwa kutaniko, na kuongoza katika utumishi wa shambani. Katika 1946 ziara zilirefushwa kuwa juma moja kwa kila kutaniko.
Katika 1938 mpango huo wa kuzuru makutaniko uliongezewa utumishi wa mtumishi wa kimkoa akiwa na daraka jipya. Alisafiri eneo kubwa zaidi, akitumia juma moja pindi kwa pindi pamoja na ndugu waliokuwa wakisafiri katika kanda ya dunia (mzunguko) kuzuru makutaniko. Wakati wa ziara yake alitumikia katika programu ya kusanyiko lililohudhuriwa na makutaniko yote katika kanda hiyo ya dunia.b Mpango huo ulikuwa kichocheo kikubwa kwa akina ndugu na uliandaa fursa ya ukawaida kwa ajili ya ubatizo wa wanafunzi wapya.
“Mtu Apendaye Utumishi”
John Booth alikuwa miongoni mwa wale walioshiriki katika utumishi huo kuanzia 1936 na ambaye, katika 1974, alipata kuwa mshiriki wa Baraza Linaloongoza. Alipokuwa akihojiwa akiwa mmoja awezaye kuwa msimamizi asafiriye, aliambiwa: “Wasemaji wenye ufasaha sio wanaohitajiwa, ni mtu apendaye utumishi tu na ambaye ataongoza katika huo na kuongea juu yao kwenye mikutano.” Ndugu Booth alikuwa na upendo huo kwa ajili ya utumishi wa Yehova, kama ithibitishwavyo na utumishi wake wa bidii wa painia tangu 1928, naye alichochea bidii ya kueneza evanjeli katika wengine kwa kielelezo na maneno ya kitia-moyo pia.
Kutaniko la kwanza alilozuru, katika Machi 1936, lilikuwa katika Easton, Pennsylvania. Baadaye aliandika: “Kwa kawaida nilikuwa nikiwasili mahali ili niwahi utumishi wa shambani asubuhi, nifanye mkutano na watumishi wa kampuni mapema jioni na baadaye mwingine na kampuni nzima. Kwa kawaida nilikuwa nikitumia siku mbili tu pamoja na kampuni na siku moja tu na kikundi kidogo zaidi, nyakati nyingine nikizuru vikundi sita kama hivyo kila juma. Nilikuwa nikisafiri daima.”
Miaka miwili baadaye, katika 1938, alipewa mgawo, akiwa mtumishi wa kimkoa, asimamie kusanyiko la kanda ya dunia (sasa lajulikana kuwa kusanyiko la mzunguko) kila juma. Hilo lilisaidia kuimarisha akina ndugu wakati ambapo mnyanyaso ulikuwa ukizidi kuwa mkali katika baadhi ya maeneo. Akikumbuka siku hizo na madaraka yake tofauti-tofauti, Ndugu Booth alisema hivi: “Katika juma lilelile [ambalo nilikuwa shahidi katika kesi ya mahakama iliyohusu Mashahidi wapatao 60 katika Indianapolis, Indiana] nilikuwa mshtakiwa katika kesi nyingine katika Joliet, Illinois, na wakili wa ndugu mmoja katika [kesi] nyingine katika Madison, Indiana, na, kwa kuongezea, nilisimamia kusanyiko la kanda ya dunia kila mwisho-juma.”
Miaka miwili baada ya makusanyiko haya ya kanda ya dunia kurudishwa katika 1946 (sasa yakiwa makusanyiko ya mzunguko), Carey Barber alikuwa miongoni mwa wale waliopewa migawo wakiwa watumishi wa wilaya. Tayari alikuwa amekuwa mshiriki wa familia ya Betheli katika Brooklyn, New York, kwa miaka 25. Wilaya yake ya kwanza ilienea sehemu yote ya magharibi mwa Marekani. Mwanzoni, safari kati ya makusanyiko ilikuwa kilometa kama 1,600 kila juma. Kadiri wingi na ukubwa wa makutaniko ulivyoongezeka, umbali huo ulipungua, na makusanyiko mengi ya mzunguko yalifanywa mara nyingi katika kanda moja ya jiji. Baada ya uzoefu wa miaka 29 akiwa mwangalizi asafiriye, Ndugu Barber alialikwa arudi kwenye makao makuu ya ulimwengu katika 1977 akiwa mshiriki wa Baraza Linaloongoza.
Katika nyakati za vita na mnyanyaso mkali, waangalizi wasafirio mara nyingi walihatarisha uhuru na maisha zao ili kutosheleza hali-njema ya kiroho ya ndugu zao. Katika wakati wa kukaliwa kwa Ubelgiji na Wanazi, André Wozniak aliendelea kuzuru makutaniko na kusaidia kuyapelekea ugavi wa fasihi. Mara nyingi Gestapo walikuwa karibu sana kumkamata lakini hawakufaulu kumnasa.
Katika Rhodesia (sasa hujulikana kuwa Zimbabwe) katika miaka ya mwisho-mwisho ya 1970, watu waliishi kwa hofu, na usafiri ulipungua wakati wa pindi ya vita ya wenyewe kwa wenyewe. Lakini waangalizi wasafirio wa Mashahidi wa Yehova, wakiwa wachungaji na waangalizi wenye upendo, walithibitika kuwa kama “mahali pa kujificha na upepo” kwa ndugu zao. (Isa. 32:2) Baadhi yao walikuwa wakitembea kwa siku kadhaa kupitia vichaka, wakisafiri kupanda na kushuka milima, wakivuka mito yenye hatari, wakilala nje usiku—yote hayo ili kufikia makutaniko na wahubiri walio peke yao, kuwatia moyo wadumu imara katika imani. Miongoni mwao alikuwa Isaiah Makore, aliyeponea chupuchupu risasi zilipokuwa zikipita juu ya kichwa chake wakati wa pigano kati ya jeshi la serikali na “wapigania uhuru.”
Waangalizi wengine wasafirio wametumikia tengenezo kimataifa kwa miaka mingi. Wasimamizi wa Watch Tower Society wamesafiri mara nyingi kwenda nchi nyinginezo kushughulikia mahitaji ya kitengenezo na kuhutubia mikusanyiko. Ziara hizo zimesaidia kuwafahamisha sana Mashahidi wa Yehova kila mahali kuhusu udugu wao wa kimataifa. Hasa Ndugu Knorr alifuatia utendaji huo kwa ukawaida, akizuru kila tawi na makao ya mishonari. Kadiri tengenezo lilivyokua, ulimwengu uligawanywa kuwa kanda kumi za dunia za kimataifa, na kuanzia Januari 1, 1956, ndugu wenye kustahili, chini ya mwelekezo wa msimamizi, walianza kusaidia kutoa utumishi huo ili uweze kushughulikiwa kwa ukawaida. Zile ziara za kanda za dunia, zifanywazo sasa chini ya mwelekezo wa Halmashauri ya Utumishi ya Baraza Linaloongoza, huendelea kuchangia umoja wa duniani pote na mwendo wa kusonga mbele wa tengenezo zima.
Usitawi mwingine wa maana umechangia muundo wa sasa wa tengenezo.
Upatanisho Zaidi wa Kitheokrasi
Katikati ya Vita ya Ulimwengu 2, Joseph F. Rutherford alikufa, katika Januari 8, 1942, na Nathan H. Knorr akawa msimamizi wa tatu wa Watch Tower Society. Tengenezo lilikuwa chini ya msongo mkali kwa sababu ya marufuku iliyowekwa juu ya utendaji walo katika nchi nyingi, jeuri ya wafanyaghasia chini ya kisingizio cha uzalendo, na kukamatwa kwa Mashahidi walipokuwa wakigawanya fasihi za Biblia katika huduma yao hadharani. Je, badiliko la usimamizi lingetokeza kupunguka kwa mwendo wa kazi katika wakati huo wa hatari? Ndugu washughulikiao mambo ya usimamizi walimtegemea Yehova kwa ajili ya mwelekezo na baraka. Kupatana na tamaa yao ya mwongozo wa kimungu, walichunguza upya muundo wenyewe wa tengenezo kuona kama kulikuwa maeneo yoyote ambamo upatani zaidi na njia za Yehova ungeweza kuwamo.
Ndipo, katika 1944, kusanyiko la utumishi likafanywa Pittsburgh, Pennsylvania, kuhusiana na mkutano wa kila mwaka wa Watch Tower Society. Katika Septemba 30, kabla ya mkutano huo wa kila mwaka, mfululizo wa hotuba za maana sana ulitolewa juu ya lile ambalo Maandiko husema kwa habari ya tengenezo la watumishi wa Yehova.c Uangalifu ulikazwa juu ya Baraza Linaloongoza. Katika pindi hiyo ilikaziwa kwamba kanuni ya kitheokrasi lazima itumike juu ya mashirika yote yatumiwayo na jamii ya mtumwa mwaminifu na mwenye busara. Ilifafanuliwa kwamba shirika la kisheria halikuwa na watu wote wa Mungu “waliojitakasa” wakiwa washiriki. Liliwawakilisha tu, likitenda kuwa shirika la kisheria kwa niaba yao. Hata hivyo, kwa kuwa Sosaiti ndiyo chombo chenye kutangaza kitumiwacho kuandalia Mashahidi wa Yehova fasihi zenye nuru ya kiroho, lilikuwa jambo la akili na lisiloepukika kwamba Baraza Linaloongoza lilishirikishwa karibukaribu na maofisa na waelekezi wa Sosaiti hiyo ya kisheria. Je, kanuni za kitheokrasi zilikuwa zikitumiwa kikamili katika mambo yayo?
Katiba ya Sosaiti ilieleza mpango wa hisa ambao katika huo jumla ya mchango wa kila mtu wa dola 10 (Marekani) ulimpa mchangaji haki ya kupiga kura kuhusiana na kuteuliwa kwa washiriki wa baraza la waelekezi na maofisa wa Sosaiti. Labda ilionekana kwamba michango hiyo ilitoa uthibitisho wa kupendezwa kihalisi na kazi ya tengenezo. Hata hivyo, mpango huo ulitokeza matatizo. Ndugu Knorr, msimamizi wa Sosaiti, alieleza hivi: “Kutokana na maandalizi ya katiba ya Sosaiti, ingeonekana kwamba kuwa sehemu ya baraza linaloongoza kulitegemea juu ya michango iliyotolewa kwa Sosaiti ya kisheria. Lakini kulingana na mapenzi ya Mungu haingeweza kuwa hivyo miongoni mwa watu wake wa kweli wachaguliwa.”
Ni jambo la hakika kwamba Charles Taze Russell, ambaye kwa miaka 32 ya kwanza ya Sosaiti alikuwa mwenye kutokeza sana katika baraza linaloongoza, alikuwa ndiye mchangaji mkubwa zaidi kwa Sosaiti kifedha, kimwili, na kiakili. Lakini si mchango wa kifedha ulioamua jinsi Bwana alivyomtumia. Ilikuwa wakfu wake kamili, bidii yake ya bila kuchoka, msimamo wake wa bila kuridhiana kwa ajili ya Ufalme wa Mungu, na uaminifu-mshikamanifu na uaminifu wake usioweza kuvunjwa ndivyo vilivyomfanya aonekane machoni pa Mungu kuwa afaa kwa ajili ya utumishi. Kwa habari ya tengenezo la kitheokrasi, kanuni hii yatumikia: “Mungu ameviweka viungo katika mwili, kila kimoja chavyo, kama vile alivyopendezwa.” (1 Kor. 12:18, NW) “Hata hivyo,” akafafanua Ndugu Knorr, “kwa kuwa katiba ya Sosaiti iliandalia hisa za kupiga kura zitolewe kwa wachangaji wa fedha kwa kazi ya Sosaiti, ilielekea kufunika au kuingilia kanuni hiyo ya Kitheokrasi kwa habari ya baraza linaloongoza; na pia ilielekea kuihatarisha au kuiwekea vizuizi.”
Kwa sababu hiyo, kwenye mkutano wa kishughuli wa wenye hisa wote wa Sosaiti katika Oktoba 2, 1944, kura yenye umoja ilipigwa kwamba katiba ya Sosaiti irekebishwe upya na kupatanishwa zaidi na kanuni za kitheokrasi. Sasa kuwa mshiriki hakungekuwa na idadi isiyo na kikomo bali kungekuwa na washiriki kati ya 300 na 500, wote hao wangekuwa wanaume waliochaguliwa na baraza la waelekezi, si kwa msingi wa michango ya kifedha, bali kwa sababu wao ni Mashahidi wa Yehova waaminifu, waliokomaa na watendaji watumikiao wakati wote katika kazi ya tengenezo au walio wahudumu watendaji wa makutaniko ya Mashahidi wa Yehova. Washiriki hao wangepigia kura baraza la waelekezi, ndipo baraza la waelekezi lingeteua maofisa walo. Mipango hiyo mipya ilianza kutenda mwaka uliofuata, katika Oktoba 1, 1945. Hilo limethibitika kuwa ulinzi kama nini katika enzi hii ambapo vikundi vyenye uhasama mara nyingi vimetumia hila katika mambo ya kibiashara ili kuchukua udhibiti wa mashirika kisha kuyaunda upya ili yafae malengo yao!
Baraka ya Yehova juu ya hatua hizo za kusonga mbele kupatana na kanuni za kitheokrasi imedhihirika. Ujapokuwa msongo wenye kupita kiasi ulioletwa juu ya tengenezo wakati wa Vita ya Ulimwengu 2, idadi ya wapiga-mbiu wa Ufalme iliendelea kukua. Bila kuacha, waliendelea kutoa ushahidi kwa juhudi juu ya Ufalme wa Mungu. Kutoka 1939 hadi 1946, kulikuwa na ongezeko lenye kustaajabisha la asimilia 157 la idadi ya Mashahidi wa Yehova, nao walifikia nchi sita zaidi kwa kazi ya kuhubiri habari njema. Wakati wa miaka 25 iliyofuata, idadi ya Mashahidi watendaji ilikua kwa karibu asilimia 800 nyingine, nao waliripoti utendaji wa ukawaida katika nchi 86 zaidi.
Mazoezi ya Pekee kwa Waangalizi
Baadhi ya watazamaji wa nje waliliona kuwa jambo lisiloepukika kwamba wakati tengenezo lingekuwa kubwa zaidi, viwango vyalo vingelegezwa. Lakini, tofauti na hilo, Biblia ilitabiri kwamba uadilifu na amani vingeenea miongoni mwa watumishi wa Yehova. (Isa. 60:17) Hilo lingetaka waangalizi wenye daraka waelimishwe kwa uangalifu wenye kuendelea katika Neno la Mungu, uelewevu ulio wazi wa viwango vyake vya kihukumu, na utumizi wenye upatani wa viwango hivyo. Elimu hiyo imeandaliwa. Funzo kamili la matakwa yenye uadilifu ya Mungu limeandaliwa kwa kuendelea katika Mnara wa Mlinzi, na kila kutaniko la Mashahidi wa Yehova ulimwenguni pote limejifunza habari hiyo kwa utaratibu. Lakini, kwa kuongezea hilo, waangalizi wa kundi wamepewa wamepewa mafunzo mengi zaidi.
Waangalizi wakuu wa matawi ya Sosaiti wameletwa pamoja kwa ajili ya mazoezi ya pekee wakati wa mikusanyiko ya kimataifa. Kutoka 1961 kufika 1965, mitaala ya shule iliyobuniwa kipekee, ya urefu wa miezi minane hadi kumi, iliongozwa kwa ajili yao katika New York. Kutoka 1977 kufika 1980, kulikuwa mfululizo mwingine wa mitaala ya pekee ya majuma matano kwa ajili yao. Mazoezi yao yalitia ndani funzo la mstari kwa mstari la vitabu vyote vya Biblia pamoja na ufikirio wa mambo mengi ya kitengenezo na njia ambazo katika hizo wangesogeza mbele kazi ya kuhubiri habari njema. Hakuna migawanyiko ya kitaifa miongoni mwa Mashahidi wa Yehova. Si kitu hata wawe wanaishi wapi, wao hushikamana na viwango vilevile vya juu vya Biblia na huamini na kufundisha mambo yaleyale.
Waangalizi wa mzunguko na wa wilaya wamepewa pia uangalifu wa pekee. Wengi wao wamehudhuria Shule ya Biblia ya Gileadi ya Watchtower au mojawapo Matanzu ya Shule yayo. Pindi kwa pindi wao pia hukutanishwa pamoja kwenye ofisi za tawi za Sosaiti, au hukutana mahali penginepo pafaapo, kwa semina ya siku chache au juma moja.
Katika 1959 uandalizi mwingine wenye kutokeza ulianza kutenda. Ulikuwa Shule ya Huduma ya Ufalme, iliyohudhuriwa na waangalizi wa mzunguko na wa wilaya pamoja na waangalizi wa kutaniko. Ilianza ikiwa mtaala wa funzo wa mwezi mzima. Baada ya kuwa imetumiwa kwa mwaka mmoja Marekani, habari ya mtaala huo ilitafsiriwa katika lugha nyinginezo na kutumiwa kwa kuendelea duniani pote. Kwa kuwa waangalizi wote hawakuweza kupanga kuwa mbali na kazi zao za kimwili kwa mwezi mzima, namna ya mtaala wa majuma mawili ilianza kutumiwa katika 1966.
Shule hiyo haikuwa seminari ambamo wanaume walikuwa wakizoezwa ili wajitayarishe kuagizwa rasmi. Wale waliokuwa wakihudhuria walikuwa tayari wahudumu walioagizwa rasmi. Wengi wao walikuwa wamekuwa waangalizi na wachungaji wa kundi kwa miongo kadhaa. Mtaala wa funzo lao ulikuwa fursa ya kuzungumzia kikamili mafunzo kutoka Neno la Mungu kuhusu kazi yao. Mkazo mkubwa uliwekwa juu ya umaana wa huduma ya shambani na jinsi ya kuifanya kwa matokeo. Kwa sababu viwango vya adili vya ulimwengu vilikuwa vikibadilikabadilika, wakati mwingi ulitumiwa pia kuzungumzia utegemezaji wa viwango vya Biblia vya adili. Mtaala huo ulifuatwa katika nyakati za karibuni na semina kila miaka miwili au mitatu, pamoja na mikutano yenye kusaidia iliyoongozwa na waangalizi wasafirio pamoja na wazee wa mahali mara kadhaa kila mwaka. Hiyo hutoa fursa ya kutoa uangalifu wa pekee kwa mahitaji ya sasa. Ni ulinzi salama dhidi ya kupeperuka kokote kutoka kwenye viwango vya Biblia, na huchangia ushughulikiaji hali wenye upatano katika makutaniko yote.
Mashahidi wa Yehova huzingatia moyoni lile shauri la upole kwenye 1 Wakorintho 1:10 (NW): “Nawahimiza nyinyi kwa bidii, akina ndugu, kupitia jina la Bwana wetu Yesu Kristo kwamba nyote mseme kwa upatano, na kwamba kusiwe na migawanyiko miongoni mwenu, bali kwamba mpate kuunganishwa kwa kufaa katika akili ileile na katika mstari ule ule wa fikira.” Huo si upatano wa kulazimishwa; hutokana na kuelimishwa katika njia za Mungu kama zilivyorekodiwa katika Biblia. Mashahidi wa Yehova hufurahia njia za Mungu na kusudi lake. Ikiwa wowote waacha kufurahia kuishi kulingana na viwango vya Biblia, wako huru kuacha tengenezo. Lakini wowote wakianza kuhubiri imani nyinginezo au kupuuza adili ya Biblia, waangalizi huchukua hatua kulinda salama kundi. Tengenezo hutumia shauri hili la Biblia: “Mfulize kuangalia wale wasababishao migawanyiko na sababu za kukwaza kinyume cha fundisho ambalo mmejifunza, na mwaepuke.”—Rum. 16:17, NW; 1 Kor. 5:9-13, NW.
Biblia ilitabiri kwamba Mungu angesababisha hali hiyohiyo iwemo miongoni mwa watumishi wake, hali ambayo katika hiyo uadilifu ungeenea na kuzaa tunda lenye amani. (Isa. 32:1, 2, 17, 18) Hali hizo huvutia sana watu wapendao yaliyo sawa.
Ni wangapi kati ya wapendao uadilifu hao watakaokusanywa kabla ya mwisho wa mfumo wa kale? Mashahidi wa Yehova hawajui. Lakini Yehova ajua kile ambacho kazi yake itahitaji, na kwa wakati wake mwenyewe na njia yake mwenyewe yeye huhakikisha kwamba tengenezo lake limepewa vifaa ili kuitekeleza.
Kujitayarishia Ukuzi wa Kasi
Utafiti ulipokuwa ukifanywa chini ya usimamizi wa Baraza Linaloongoza katika kutayarisha kitabu cha marejezo Aid to Bible Understanding, uangalifu ulielekezwa tena kwenye njia ambayo kutaniko la Kikristo la karne ya kwanza lilipangwa. Funzo la uangalifu lilifanywa juu ya maneno ya Biblia kama “mwanamume mzee,” “mwangalizi,” na “mhudumu.” Je, tengenezo la Mashahidi wa Yehova la kisasa lingeweza kupatana kikamili zaidi na kigezo kilichokuwa kimehifadhiwa katika Maandiko kuwa mwongozo?
Watumishi wa Yehova walikuwa wameazimia kuendelea kutii mwelekezo wa kimungu. Kwenye mfululizo wa mikusanyiko iliyofanywa katika 1971, uangalifu ulielekezwa kwenye mipango ya kuongoza ya kutaniko la Kikristo la mapema. Ilionyeshwa kwamba neno pre·sbyʹte·ros (mwanamume mzee, mzee), kama litumiwavyo katika Biblia, halikuwahusu watu wa umri mkubwa tu, wala halikuwahusu wote katika makutaniko waliokuwa wakomavu kiroho. Lilitumiwa hasa katika maana ya cheo kuwarejezea waangalizi wa makutaniko. (Mdo. 11:30; 1 Tim. 5:17; 1 Pet. 5:1-3) Hao walipokea vyeo vyao kwa kuwekwa rasmi, kupatana na matakwa yaliyokuja kuwa sehemu ya Maandiko yaliyopuliziwa. (Mdo. 14:23; 1 Tim. 3:1-7; Tito 1:5-9) Mahali ambako wanaume waliostahili wa kutosha walipatikana, kulikuwa na zaidi ya mzee mmoja kutanikoni. (Mdo. 20:17; Flp. 1:1) Hao walijumuika kuwa “baraza la wanaume wazee,” wote wakiwa na cheo rasmi kilekile, na hakuna mmoja wao aliyekuwa mshiriki mashuhuri zaidi au mwenye nguvu zaidi katika kutaniko. (1 Tim. 4:14, NW) Ilifafanuliwa kwamba, ili kusaidia wazee, kulikuwa pia “watumishi wa huduma” waliowekwa rasmi, kupatana na matakwa yaliyoonyeshwa na mtume Paulo.—1 Tim. 3:8-10, 12, 13, NW.
Mipango ilianzishwa mara moja ili kupatanisha tengenezo kwa ukaribu zaidi na kigezo hicho cha Biblia. Hilo lilianza na Baraza Linaloongoza lenyewe. Washiriki walo waliongezwa kupita wale saba ambao, wakiwa washiriki wa baraza la waelekezi la Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania, walikuwa wakitumikia wakiwa baraza linaloongoza kwa ajili ya Mashahidi wa Yehova. Hakuna idadi kamili ya washiriki wa Baraza Linaloongoza iliyowekwa. Katika 1971, walikuwa 11; kwa miaka michache, kulikuwa wengi kama 18; katika 1992, walikuwa 12. Wote ni wanaume waliotiwa mafuta na Mungu wakiwa warithi-washirika na Yesu Kristo. Wale 12 waliokuwa wakitumikia wakiwa washiriki wa Baraza Linaloongoza katika 1992 walikuwa wakati huo na rekodi ya miaka zaidi ya 728 ya utumishi wa wakati wote miongoni mwao wakiwa wahudumu wa Yehova Mungu.
Iliamuliwa katika Septemba 6, 1971, kwamba uenyekiti kwenye mikutano ya Baraza Linaloongoza wapasa kupokezanwa zamu kila mwaka kulingana na mpango wa alfabeti ya majina ya familia ya washiriki walo. Kwa kweli ulianza kutenda katika Oktoba 1. Washiriki wa Baraza Linaloongoza walipokezana zamu pia, kila juma, katika kusimamia ibada ya asubuhi na Funzo la Mnara wa Mlinzi kwa ajili ya washiriki wa wafanyakazi wa makao makuu.d Mpango huo ulianza kutenda katika Septemba 13, 1971, wakati Frederick W. Franz alipoongoza programu ya ibada ya asubuhi kwenye makao makuu ya Sosaiti katika Brooklyn, New York.
Wakati wa mwaka uliofuata, matayarisho yalifanywa kwa ajili ya marekebisho katika uangalizi wa makutaniko. Hakungekuwa tena na mtumishi mmoja tu wa kutaniko akisaidiwa na idadi fulani iliyotajwa hususa ya watumishi wengine. Wanaume wastahilio Kimaandiko wangewekwa watumikie wakiwa wazee. Wengine, waliotimiza matakwa ya Biblia, wangewekwa rasmi wawe watumishi wa huduma. Jambo hilo lilifungulia njia idadi kubwa zaidi ishiriki katika madaraka ya kutaniko na hivyo kupata uzoefu wenye thamani. Hakuna yeyote wa Mashahidi wa Yehova aliyekuwa na wazo lolote wakati ule kwamba idadi ya makutaniko ingeongezeka kwa asilimia 156 wakati wa miaka 21 iliyofuata, yakifikia jumla ya 69,558 katika 1992. Lakini Bwana Yesu Kristo, Kichwa cha kutaniko, kwa wazi alikuwa akifanya matayarisho kwa ajili ya yale yaliyokuwa yakija.
Katika miaka ya mapema ya 1970, ilifikiriwa kwa uangalifu kulipanga upya zaidi kitengenezo Baraza Linaloongoza. Tangu Watch Tower Society ifanyizwe kuwa shirika katika 1884, utangazaji wa fasihi, usimamizi wa kazi ya kueneza evanjeli ya duniani pote, na mipango kwa ajili ya shule mbalimbali na mikusanyiko imekuwa ikishughulikiwa chini ya mwelekezo wa ofisi ya msimamizi wa Watch Tower Bible and Tract Society. Lakini baada ya uchanganuzi wa uangalifu na mazungumzo ya mambo kikamili kwa kipindi cha miezi mingi, mpango mpya ulikubaliwa kwa umoja katika Desemba 4, 1975. Halmashauri sita za Baraza Linaloongoza zilifanyizwa.
Halmashauri ya Mwenyekiti (washiriki wayo wakiwa mwenyekiti wa sasa wa Baraza Linaloongoza, mwenyekiti aliyetangulia, na yule atakayefuata kuwa mwenyekiti) hupokea ripoti za matukio makubwa ya dharura, misiba, na kampeni za mnyanyaso, na kuhakikisha kwamba hizo zinashughulikiwa mara hiyo pamoja na Baraza Linaloongoza. Halmashauri ya Uandikaji husimamia kuwekwa kwa chakula cha kiroho katika namna ya maandishi, ya mirekodi, na vidio kwa ajili ya Mashahidi wa Yehova na kwa ajili ya kugawanywa kwa umma, na husimamia kazi ya kutafsiri katika mamia ya lugha. Daraka la Halmashauri ya Ufundishaji ni kusimamia shule na makusanyiko, pia mikusanyiko ya wilaya na ya kimataifa, kwa ajili ya watu wa Yehova, pamoja na mafunzo ya familia ya Betheli na kutayarishwa kwa habari ipaswayo kutumiwa kwa makusudi hayo. Halmashauri ya Utumishi husimamia maeneo yote ya kazi ya kueneza evanjeli, kutia na utendaji wa makutaniko na waangalizi wasafirio. Uchapaji, utangazaji, na usafirishaji wa fasihi pamoja na uendeshaji wa viwanda na ushughulikiaji wa mambo ya kisheria na ya kishughuli yote husimamiwa na Halmashauri ya Utangazaji. Nayo Halmashauri ya Wafanyakazi huwa na usimamizi juu ya mipango kwa ajili ya usaidizi wa kibinafsi na kiroho wa washiriki wa familia za Betheli na ndiyo yenye daraka la kualika washiriki wapya watumikie katika familia za Betheli ulimwenguni pote.
Halmashauri zaidi zenye kusaidia hugawiwa kusimamia viwanda, makao ya Betheli, na mashamba yashirikianayo na makao makuu ya ulimwengu. Katika halmashauri hizo Baraza Linaloongoza hutumia kwa kikamili uwezo wa washiriki wa “umati mkubwa.”—Ufu. 7:9, 15, NW.
Marekebisho yalifanywa pia katika uangalizi wa matawi ya Sosaiti. Tangu Februari 1, 1976, kila tawi limesimamiwa na halmashauri ya washiriki watatu au zaidi, ikitegemea mahitaji na ukubwa wa tawi. Hao hufanya kazi chini ya Baraza Linaloongoza katika kutimiza kazi ya Ufalme katika kanda zao.
Katika 1992, usaidizi zaidi uliandaliwa kwa ajili ya Baraza Linaloongoza wakati idadi ya wasaidizi, sanasana kutoka miongoni mwa umati mkubwa, walipopewa migawo ya kushiriki katika mikutano na kazi ya halmashauri za Uandikaji, Ufundishaji, Utumishi, Utangazaji, na Wafanyakazi.e
Kusambazwa huko kwa madaraka kumethibitika kuwa kwenye kunufaisha sana. Pamoja na marekebisho yaliyofanywa tayari katika makutaniko, kumesaidia kuondolea mbali kizuizi chochote ambacho kingeweza kukengeusha watu mmoja-mmoja wasifahamu kwamba Kristo ndiye Kichwa cha kutaniko. Limethibitika kuwa jambo lenye kunufaisha kuwa na idadi ya akina ndugu wakishauriana pamoja juu ya mambo yahusuyo kazi ya Ufalme. Kwa kuongezea, kupanga upya kitengenezo huko kumewezesha kuandaa usimamizi uhitajiwao katika maeneo mengi ambako umehitajiwa kwa haraka wakati wa enzi ambayo kumekuwa na ukuzi wa kasi kwelikweli wa kitengenezo. Muda mrefu uliopita, Yehova alitabiri kupitia nabii Isaya hivi: “Mdogo atakuwa elfu, na mnyonge atakuwa taifa hodari; Mimi, BWANA, nitayahimiza hayo wakati wake.” (Isa. 60:22) Si kwamba tu ameyahimiza bali pia ameandaa mwelekezo uhitajiwao ili tengenezo lake lionekanalo liweze kuyasimamia.
Hivi sasa Mashahidi wa Yehova wanapendezwa na kazi ambayo Mungu amewapa wakati wa siku hizi za mwisho za ulimwengu wa kale, nao wamepangwa vizuri kitengenezo kuikamilisha. Mashahidi wa Yehova huona uthibitisho ulio wazi kwamba tengenezo hili si la wanadamu bali ni la Mungu na kwamba Mwana wa Mungu mwenyewe, Yesu Kristo, analielekeza. Akiwa Mfalme anayetawala, Yesu atalinda salama raia zake waaminifu kuipita dhiki kubwa inayokuja na kuhakikisha kwamba wamepangwa kitengenezo kwa mafanikio kwa ajili ya kutekeleza mapenzi ya Mungu wakati wa Mileani ijayo.
[Maelezo ya Chini]
a Katika 1894, Ndugu Russell alipanga Zion’s Watch Tower Tract Society itume ndugu waliostahili wawe wasemaji. Ili wazitumie katika kujijulisha kwa vikundi vya mahali, walipewa vyeti vilivyotiwa sahihi. Vyeti hivyo havikutoa mamlaka ya kuhubiri wala havikuonyesha kwamba aliyosema mwenye cheti yalipasa kukubaliwa bila uchunguzi ufaao kwa msaada wa Neno la Mungu. Hata hivyo, kwa kuwa watu fulani walitumia vibaya kusudi lavyo, katika muda wa mwaka mmoja Ndugu Russell aliagiza arudishiwe vyeti hivyo. Kwa tahadhari yeye alijaribu kuepuka chochote ambacho watazamaji wangeweza kufasiri kuwa hata chafanana na jamii ya makasisi.
b Zion’s Watch Tower, Oktoba-Novemba 1881, kur. 8-9.
c Nyakati nyingine vikundi vya mahali vilirejezewa kuwa “makanisa,” kupatana na lugha inayotumiwa katika Biblia ya Kiswahili. Yaliitwa pia eklesia, kupatana na neno linalotumiwa katika maandishi ya Biblia ya Kigiriki. Neno “madarasa” vilevile lilitumiwa, maana kwa kweli walikuwa vikundi vya wanafunzi waliokutana kwa ukawaida kwa ajili ya funzo. Baadaye, walipoitwa kampuni, hilo lilionyesha kujua kwao kwamba walikuwa katika vita ya kiroho. (Ona Zaburi 68:11, KJ, pambizoni.) Baada ya kutangazwa kwa New World Translation of the Christian Greek Scriptures katika 1950, neno “kutaniko” la lugha ya Biblia ya kisasa likaja kutumiwa kwa ukawaida katika nchi nyingi zaidi.
d Maana halisi ya neno lililotumiwa katika maandishi ya Biblia ya Kigiriki (khei·ro·to·neʹo) ni “tandaza, nyoosha, au inua mkono,” na, kwa kupanua, lingeweza pia kumaanisha, “kuteua au kuchagua kwa ajili ya cheo kwa kuinua mikono.”—A Greek and English Lexicon to the New Testament, ya John Parkhurst, 1845, uku. 673.
e Kwa habari zaidi, ona Sura 25, “Kuhubiri Hadharani na Kutoka Nyumba Hadi Nyumba.”
f Kupitia mwelekezi wa utumishi, utumishi wa shambani wa wale walioshirikiana na kutaniko, au darasa, ungeripotiwa kwa Sosaiti kila juma, kuanzia 1919.
g Kama ilivyoonyeshwa katika kijitabu Organization Method, kila kutaniko lilipaswa kuchagua mwelekezi-msaidizi na mweka-hazina. Hao, pamoja na mwelekezi aliyewekwa na Sosaiti walifanyiza halmashauri ya utumishi ya mahali.
h The Watch Tower, Julai 1, 1920, kur. 195-200.
i Halmashauri ya utumishi wakati huo ilitia ndani washiriki wasiozidi kumi. Mmoja wao alikuwa mwelekezi wa utumishi, ambaye hakuchaguliwa mahali hapo bali aliwekwa na Sosaiti. Wale wengine walifanya kazi pamoja naye katika kupanga na kuendeleza kazi ya ushahidi.
j Kwa miaka kadhaa, tokea 1932 na kuendelea, hao walirejezewa kuwa Wayonadabu.
k Kitenzi cha Kigiriki khei·ro·to·neʹo kifafanuliwapo kuwa chamaanisha tu ‘kuchagua kwa kunyoosha mkono,’ hilo hushindwa kuangalia maana ya baadaye ya neno hilo. Hivyo, A Greek-English Lexicon, ya Liddell na Scott, iliyohaririwa na Jones na McKenzie na kuchapwa upya katika 1968, hufafanua neno hilo kuwa likimaanisha “kunyoosha mkono, kwa kusudi la kutoa kura ya mtu katika kusanyiko . . . II. c. acc. pers. [kwa kuhusu mtu], kuchagua, [kwa kufaa] kwa wonyesho wa mikono . . . b. baadaye, kijumla, kuweka rasmi, . . . kuweka rasmi kwenye cheo Kanisani, [pre·sby·teʹrous] Act. Ap. [Matendo ya Mitume] 14.23.” Utumizi huo wa baadaye ulikuwa ukiendelea katika siku za mitume; neno hilo lilitumiwa katika maana hiyo na mwanahistoria wa Kiyahudi Yosefo wa karne ya kwanza katika Jewish Antiquities, Buku 6, sura ya 4, fungu 2, na sura ya 13, fungu 9. Muundo wa kisarufi wenyewe wa Matendo 14:23 katika Kigiriki cha awali huonyesha kwamba Paulo na Barnaba ndio waliofanya yale yaliyoelezwa humo.
l Baadaye katika mwaka huohuo, 1938, Organization Instructions, kilichotangazwa kikiwa kijarida cha kurasa nne, kilitoa mambo mengi zaidi. Kilieleza kwamba kutaniko la mahali lilipaswa kuweka rasmi halmashauri ya kutenda kwa niaba yalo. Halmashauri hiyo ilipaswa kufikiria akina ndugu kwa msaada wa sifa zilizoonyeshwa katika Maandiko na kutoa mapendekezo kwa Sosaiti. Wawakilishi wa Sosaiti wasafirio walipotembelea makutaniko, walipitia sifa na uaminifu wa ndugu wa mahali katika kutunza migawo yao. Mapendekezo yao yalifikiriwa pia na Sosaiti wakati wa kuwekwa rasmi kwayo.
a Kutoka 1894 hadi 1927, wasemaji wasafirio waliopelekwa na Sosaiti walijulikana kwanza kuwa wawakilishi wa Tower Tract Society, kisha kuwa mapilgrimu. Kutoka 1928 hadi 1936, kukiwa na mkazo ulioongezeka juu ya utumishi wa shambani, waliitwa waelekezi wa utumishi wa kimkoa. Kuanzia na Julai 1936, ili kukazia uhusiano wao ufaao na ndugu wenyeji, wakaja kujulikana kuwa watumishi wa kimkoa. Kutoka 1938 hadi 1941, watumishi wa kanda (eneo) ya dunia walipewa migawo kufanya kazi pamoja na idadi ndogo ya makutaniko kwa njia ya mzunguko, na hivyo kurudi kwenye vikundi vilevile kwa vipindi vya ukawaida. Baada ya kukatizwa kwa kama mwaka mmoja, utumishi huo ulianzishwa upya katika 1942 kukiwa na watumishi kwa akina ndugu. Katika 1948 maneno mtumishi wa mzunguko yalianza kutumiwa; sasa, mwangalizi wa mzunguko.
Kutoka 1938 kufika 1941, watumishi wa kimkoa, wakiwa na daraka jipya, walitumikia makusanyiko ya mahali kwa ukawaida, ambapo Mashahidi kutoka kanda ndogo ya dunia walikutana kwa ajili ya programu ya pekee. Kazi hiyo ilipoanzishwa upya katika 1946, waangalizi hao wasafirio walijulikana kuwa watumishi wa wilaya; sasa, waangalizi wa wilaya.
b Mpango huo ulianza kutumika katika Oktoba 1, 1938. Kulikuwa magumu yenye kuongezeka katika kupanga makusanyiko wakati wa miaka ya vita, hivyo makusanyiko ya kanda ya dunia yaliahirishwa mwishoni-mwishoni mwa 1941. Hata hivyo, kwa mara nyingine tena, katika 1946, mpango huo ulianzishwa upya, na pindi ambazo idadi fulani ya makutaniko ilikutana pamoja kwa ajili ya maagizo ya pekee ziliitwa makusanyiko ya mzunguko.
c Maana halisi ya hotuba hizo inapatikana katika matoleo ya Oktoba 15 na Novemba 1, 1944, ya Mnara wa Mlinzi (Kiingereza).
d Baadaye, waliteua washiriki wengine wa familia ya Betheli washiriki katika kutunza migawo hiyo.
[Blabu katika ukurasa wa 204]
Jamii ya makasisi haikuwa na nafasi miongoni mwao
[Blabu katika ukurasa wa 205]
Hawakuwa wakijaribu kuanzisha “tengenezo la kidunia”
[Blabu katika ukurasa wa 206]
Wazee walichaguliwaje?
[Blabu katika ukurasa wa 212]
Mwelekezi aliyewekwa rasmi na Sosaiti
[Blabu katika ukurasa wa 213]
Baadhi ya wazee hawakutaka kuhubiri nje ya kutaniko
[Blabu katika ukurasa wa 214]
Upungufu wa idadi lakini kuimarishwa kwa tengenezo
[Blabu katika ukurasa wa 218]
Kuweka rasmi kungefanywaje?
[Blabu katika ukurasa wa 220]
Je, Rutherford alikuwa akijaribu tu kupata udhibiti zaidi?
[Blabu katika ukurasa wa 222]
Kuzuru vikundi vya watu wawili na vya watatu pamoja na vikundi vikubwa zaidi
[Blabu katika ukurasa wa 223]
Madaraka mapya kwa waangalizi wasafirio
[Blabu katika ukurasa wa 234]
Baraza Linaloongoza lenye washiriki walioongezwa likiwa na uenyekiti wenye kupokezanwa zamu
[Blabu katika ukurasa wa 235]
Usimamizi uhitajiwao wakati wa enzi ya ukuzi wa kasi
[Sanduku katika ukurasa wa 207]
Kwa Nini Badiliko?
Alipoulizwa swali juu ya badiliko lake la maoni kuhusu kuteuliwa kwa wazee katika vile vikundi mbalimbali vya watu wa Bwana, C. T. Russell alijibu hivi:
“Kwanza kabisa nafanya haraka kuwahakikishia kwamba mimi sijadai kamwe kuwa asiyeweza kufanya kosa. . . . Sisi hatukani kukua katika ujuzi, na kwamba twaona sasa kwa nuru iliyo tofauti kidogo mapenzi ya Bwana kwa habari ya Wazee au viongozi katika vile vikundi vidogo mbalimbali vya watu wake. Kosa letu katika uamuzi lilikuwa katika kutazamia mengi mno kutoka kwa ndugu zetu wapendwa ambao, wakija mapema katika Kweli, walipata kiasili kuwa viongozi wa makampuni haya madogo. Maoni ya kuwaziawazia tuliyokuwa nayo kuwahusu yalikuwa, kwamba ujuzi juu ya Kweli ungekuwa na matokeo ya kuwanyenyekeza sana, ukiwafanya wafahamu hali yao ya kutokuwa wa maana, na kwamba lolote walilojua na waliloweza kutolea wengine lilikuwa wakiwa vinywa vya Mungu na kwa sababu watumiwa naye. Matumaini yetu ya kuwaziawazia yalikuwa kwamba hao wangekuwa katika kila maana ya hilo neno vielelezo kwa kundi; na kwamba mwelekezo wa Bwana ukileta katika kampuni dogo mmoja au zaidi wenye uhodari wa kadiri hiyohiyo, au hodari zaidi, wa kuitoa Kweli, kwamba roho ya upendo ingewaongoza kustahiana kwa heshima mmoja na mwenzake, na hivyo kusaidiana na kuhimizana mmoja na mwenzake kushiriki katika utumishi wa Kanisa, mwili wa Kristo.
“Tukiwa na wazo hilo akilini tulikata kauli kwamba vile vipimo vikubwa vya neema na kweli vilivyopo sasa na vinavyothaminiwa na watu wa Bwana waliojitakasa vingefanya isihitajiwe kwao kufuata mwendo ulioonyeshwa na mitume katika Kanisa la mapema. Kosa letu lilikuwa kushindwa kujua kwamba mipango iliyoonyeshwa na mitume chini ya usimamizi wa kimungu ni bora kuliko chochote ambacho wengine wangeweza kutunga, na kwamba Kanisa kwa ujumla litahitaji kuwa na kanuni hizo zilizoanzishwa na mitume mpaka sisi sote tuwe tumefanywa watimilifu na wakamilifu kwa kubadilishwa kwetu katika ufufuo, tuwe na ushirika wa moja kwa moja na Bwana-Mkubwa.
“Kosa letu tulilifahamu hatua kwa hatua tulipoona miongoni mwa ndugu wapendwa kadiri fulani ya roho ya ushindani, na kwa upande wa wengi tamaa ya kushika uongozi wa mikutano kuwa cheo badala ya kuwa utumishi, na kutohusisha na kuzuia ndugu wengine wasisitawi wakiwa viongozi wenye uwezo uleule kiasili na wenye ujuzi uleule juu ya Kweli na uhodari katika kutumia upanga wa Roho.”—“Zion’s Watch Tower,” Machi 15, 1906, uku. 90.
[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 208, 209]
Vifaa Vilivyotumiwa na Sosaiti Karne Moja Iliyopita Katika Eneo la Pittsburgh
Bible House, inayoonyeshwa hapa, ilitumika kuwa makao makuu kwa miaka 19, kutoka 1890 hadi 1909f
Ndugu Russell alifanyia funzo lake hapa
Washiriki wa familia ya Bible House ambao walitumikia hapa katika 1902
Jengo hilo lilitia ndani idara hii ya kupanga herufi za chapa na kupanga maandishi (kulia juu), idara ya usafirishaji (kulia chini), uhifadhi wa fasihi, makao kwa ajili ya wafanyakazi, na mahali pa ibada (jumba la kusanyiko) ambapo pangetoshea watu kama 300
[Maelezo ya Chini]
f Katika 1879, makao makuu yalikuwa kwenye 101 Fifth Avenue, Pittsburgh, Pennsylvania. Ofisi zilihamishiwa 44 Federal Street, Allegheny (Upande wa Kaskazini mwa Pittsburgh), katika 1884; na baadaye mwaka huohuo, kwenye 40 Federal Street. (Katika 1887, hiyo iliitwa 151 Robinson Street.) Nafasi zaidi ilipohitajiwa, katika 1889, Ndugu Russell alijenga Bible House, ionyeshwayo upande wa kushoto, kwenye 56-60 Arch Street, Allegheny. (Baadaye hiyo ilipewa nambari mpya 610-614 Arch Street.) Kwa kipindi kifupi katika 1918-1919, kwa mara nyingine tena walikuwa na ofisi yao kuu katika Pittsburgh, katika orofa ya tatu kwenye 119 Federal Street.
[Sanduku kaitika ukurasa wa 211]
Ni Kazi ya Nani?
Kuelekea mwisho wa maisha yake ya kidunia, Charles Taze Russell aliandika hivi: “Ni mara nyingi mno watu wa Mungu husahau kwamba Bwana Mwenyewe ndiye anayeongoza kazi Yake. Mara nyingi mno wazo ni, Sisi tutafanya kazi na kumfanya Mungu ashirikiane nasi katika kazi yetu. Acheni tupate maoni sahihi juu ya jambo hili, na kutambua kwamba Mungu amekusudia na anatimiza kazi kubwa; na kwamba itafanikiwa, kabisakabisa bila kujali sisi na jitihada zetu; na kwamba ni pendeleo kubwa walilopewa watu wa Mungu kushirikiana kufanya kazi na Mfanyi wao katika kutimiza mipango Yake, makusudio Yake, Aliyoratibu, kwa njia Yake. Kwa kuyatazama mambo kwa maoni hayo, sala zetu na kukesha kwetu kwapaswa kuwe kwa kusudi la kujua na kufanya mapenzi ya Bwana, tukiridhika na daraka lolote tupewalo, kwa kuwa ni Mungu wetu atuongozaye. Hii ndiyo programu ambayo Watch Tower Bible and Tract Society imejaribu kufuata.”—“The Watch Tower,” Mei 1, 1915.
[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 215]
Maswali ya V.D.M.
Herufi V.D.M. huwakilisha maneno ya Kilatini “Verbi Dei Minister,” au Mhudumu wa Neno la Mungu.
Katika 1916 orodha ya maswali juu ya mambo ya Kimaandiko ilitayarishwa na Sosaiti. Wale ambao wangewakilisha Sosaiti wakiwa wasemaji waliombwa wajibu kila moja la maswali hayo kwa kuandika. Hilo liliwezesha Sosaiti kujua mawazo, maoni, na uelewevu wa ndugu hao kwa habari ya kweli za Biblia za msingi. Majibu yaliyoandikwa yalichunguzwa kwa uangalifu na baraza la kutahini katika ofisi za Sosaiti. Wale waliotambuliwa kuwa wastahili kuwa wasemaji walipaswa kuwa na gredi ya asilimia 85 au zaidi.
Baadaye, wengi kati ya wazee, mashemasi, na Wanafunzi wa Biblia wengine waliomba kama wangeweza kuwa na orodha ya maswali hayo. Baada ya wakati, ilitaarifiwa kwamba ingefaa ikiwa madarasa yangeteua wawakilishi wao kuwa watu wale tu waliokuwa wamestahili kuwa V.D.M.
Sosaiti ilipotoa shahada (digrii) ya Mhudumu wa Neno la Mungu, hiyo haikumaanisha kuwa mtu huyo alikuwa akiagizwa rasmi. Ilionyesha tu kwamba baraza la kutahini katika ofisi za Sosaiti lilikuwa limepitia ukuzi wa kimafundisho wa mtu huyo, na sifa yake kwa kadiri ifaayo, na kukata kauli kwamba alikuwa amestahili kuitwa Mhudumu wa Neno la Mungu.
Maswali ya V.D.M. ni kama yafuatavyo:
(1) Ni nini lililokuwa tendo la kwanza la uumbaji wa Mungu?
(2) Ni nini maana ya neno “Logosi,” kama lishirikishwavyo na Mwana wa Mungu? na ni nini linalomaanishwa na maneno Baba na Mwana?
(3) Ni lini na jinsi gani dhambi ilipoingia ulimwenguni?
(4) Ni nini adhabu ya Kimungu ya dhambi juu ya watenda dhambi? na watenda dhambi ni nani?
(5) Kwa nini ilihitajiwa “Logosi” afanywe kuwa mwili? na je, Yeye “alivikwa mwili”?
(6) Mwanadamu Kristo Yesu alikuwa wa asili gani kutoka utoto hadi kifo?
(7) Yesu alikuwa wa asili gani tangu ufufuo; na ni upi ulio uhusiano Wake rasmi na Yehova?
(8) Ni nini iliyo kazi ya Yesu wakati wa hii Enzi ya Gospeli—katika pindi ya tangu wakati wa Pentekoste mpaka sasa?
(9) Kufikia hapo ulimwengu wa wanadamu umefanyiwa nini na Yehova Mungu? na Yesu?
(10) Ni nini lililo kusudi la Kimungu kwa habari ya Kanisa likamilishwapo?
(11) Ni nini lililo kusudi la Kimungu kwa habari ya wanadamu?
(12) Ni nini yatakayokuwa matokeo kwa wale ambao hatimaye watakuwa wasiobadilika?
(13) Ni nini zitakazokuwa thawabu au baraka zitakazoujia ulimwengu wa wanadamu kupitia utii kwa Ufalme wa Mesiya?
(14) Ni kwa kuchukua hatua zipi mtenda dhambi aweza kuja katika uhusiano ulio muhimu pamoja na Kristo na pamoja na Baba wa Kimbingu?
(15) Baada ya Mkristo kuzaliwa kwa Roho Takatifu, mwendo wake ni upi, kama ielekezwavyo katika Neno la Mungu?
(16) Je, wewe umegeuka kutoka katika dhambi umtumikie Mungu aliye hai?
(17) Je, umetakasa kabisa maisha yako na uwezo wako na vipawa vyako kwa Bwana na utumishi Wake?
(18) Je, umefananisha utakaso huo kwa uzamisho wa maji?
(19) Je, umechukua Nadhiri ya I.B.S.A. [International Bible Students Association] ya utakatifu wa uhai?
(20) Je, umesoma kikamili na kwa uangalifu yale mabuku sita ya STUDIES IN THE SCRIPTURES?
(21) Je, umepata nuru nyingi ya elimu na manufaa kutokana nayo?
(22) Je, wewe unaamini kwamba una ujuzi wa Biblia wa kutosha na wenye kudumu utakaokufanya uwe mwenye mafanikio zaidi ukiwa mtumishi wa Bwana muda wote ubakio wa maisha yako?
[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 216, 217]
Majengo Yaliyotumiwa Siku za Mapema Brooklyn
Kao la Betheli
122-124 Columbia Heights
Chumba cha kulia katika Kao la Betheli
Tabenakulo
Ofisi, chumba cha kuweka fasihi, idara ya kupeleka barua, vifaa vya kupanga chapa, na jumba la kukusanyikia lenye viti 800 vilikuwa hapa, kwenye 17 Hicks Street (iliyotumiwa kutoka 1909 hadi 1918)
Jumba la kukusanyikia
Viwanda vya Mapema
Washiriki wa familia ya Betheli waliofanya kazi kwenye kiwanda cha Myrtle Avenue katika 1920 (kulia)
35 Myrtle Avenue (1920-1922)
18 Concord Street (1922-1927)
117 Adams Street (1927- )
[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 224, 225]
Waangalizi Wasafirio Wachache Kati ya Maelfu Ambao Wametumikia
Kanada, 1905-1933
Uingereza, 1920-1932
Finland, 1921-1926, 1947-1970
Marekani, 1907-1915
Kusafiri kati ya makutaniko—
Greenland
Venezuela
Lesotho
Mexico
Peru
Sierra Leone
Makao ya kuhamishwa katika Namibia
Kushiriki pamoja na Mashahidi wenyeji katika utumishi wa shambani katika Japani
Kukutana na wazee wenyeji katika Ujerumani
Kutoa shauri litumikalo kwa mapainia katika Hawaii
Kufunza kutaniko katika Ufaransa
[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 229]
Mashirika ya Kisheria ya Mapema
Zion’s Watch Tower Tract Society. Lilifanyizwa katika 1881 na kisha likafanywa kuwa shirika kisheria katika mkoa wa Pennsylvania katika Desemba 15, 1884. Katika 1896 jina lalo lilibadilishwa kuwa Watch Tower Bible and Tract Society. Tangu 1955 limejulikana kuwa Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania.
Peoples Pulpit Association. Lilifanyizwa katika 1909 kuhusiana na kuhamishwa kwa ofisi kuu za Sosaiti kupelekwa Brooklyn, New York. Katika 1939 jina hilo lilibadilishwa kuwa Watchtower Bible and Tract Society, Inc. Tangu 1956 limejulikana kuwa Watchtower Bible and Tract Society of New York, Inc.
International Bible Students Association. Lilifanywa kuwa shirika kisheria katika London, Uingereza, Juni 30, 1914.
Ili kutimiza matakwa ya kisheria, mashirika mengine yamefanyizwa na Mashahidi wa Yehova katika jumuiya na nchi nyingi. Hata hivyo, Mashahidi wa Yehova hawajagawanyika kuwa matengenezo ya kitaifa au kimkoa. Wao ni udugu wa duniani pote wenye umoja.
[Sanduku katika ukurasa wa 234]
‘Kama Jamii ya Kikristo ya Mapema’
Kichapo cha kidini “Interpretation” kilitaarifu hivi katika Julai 1956: “Katika tengenezo na kazi yao ya kutoa ushahidi, wao [Mashahidi wa Yehova] hukaribia sana kuliko kikundi kingine chochote kuwa sawa na jamii ya Kikristo ya mapema. . . . Si vikundi vingine vingi vinavyotumia sana Maandiko katika jumbe zao, za mdomo na zilizoandikwa pia, kama wafanyavyo.”
[Picha katika ukurasa wa 210]
Ili kuandaa usimamizi wa karibu zaidi, ofisi za tawi zilianzishwa. Ya kwanza ilikuwa katika London, Uingereza, katika jengo hili
[Picha katika ukurasa wa 221]
J. F. Rutherford katika 1941. Mashahidi walijua yeye hakuwa kiongozi wao
[Picha katika ukurasa wa 226]
John Booth, mwangalizi asafiriye katika Marekani kutoka 1936 hadi 1941
[Picha katika ukurasa wa 227]
Carey Barber, ambaye wilaya yake ilitia ndani sehemu kubwa mno ya Marekani
[Picha katika ukurasa wa 228]
Ndugu Knorr alizuru kwa ukawaida kila tawi na makao ya mishonari
[Picha katika ukurasa wa 230]
Waangalizi wakuu wa matawi ya Sosaiti wameletwa pamoja kwa ajili ya mazoezi ya pekee (New York, 1958)
[Picha katika ukurasa wa 231]
Shule ya Huduma ya Ufalme imeandaa mafunzo yenye thamani kwa waangalizi kote duniani
Shule ya Huduma ya Ufalme kwenye kambi ya wakimbizi katika Thailand, 1978; katika Filipino, 1966 (kushoto juu zaidi)
[Picha katika ukurasa wa 232]
Maagizo ya tengenezo yalitangazwa kwa kuendelea (kwanza katika Kiingereza, kisha katika lugha nyinginezo) ili kuratibu utendaji wa Mashahidi na kuwaarifu wote kuhusu maandalizi yaliyofanywa kuwasaidia katika huduma yao
-
-
Mikutano Kwa Ajili ya Ibada, Funzo, na Kitia-moyoMashahidi wa Yehova—Wapiga-Mbiu wa Ufalme wa Mungu
-
-
Sura ya 16
Mikutano Kwa Ajili ya Ibada, Funzo, na Kitia-moyo
MIKUTANO ya kutaniko ni sehemu ya maana ya utendaji wa Mashahidi wa Yehova. Hata hali zinapoifanya iwe vigumu sana, wao hujitahidi kuhudhuria mikutano yao kwa ukawaida, kupatana na himizo hili la Biblia: “Acheni tufikiriane ili kuchocheana kwenye upendo na kazi zilizo bora, si kuachilia mbali kukusanyika pamoja sisi wenyewe, kama vile wengine walivyo na desturi, bali kutiana moyo, na zaidi sana hivyo kwa kadiri mwonavyo siku ikikaribia.” (Ebr. 10:24, 25, NW) Iwezekanapo, kila kutaniko hufanya mikutano mara tatu kwa juma, kwa jumla ya saa 4 na dakika 45. Hata hivyo, hali ya mikutano, pamoja na mara ifanywapo, imetofautiana kulingana na kilichokuwa kimehitajiwa wakati ule.
Katika karne ya kwanza, madhihirisho ya karama za kimuujiza za roho yalikuwa sehemu yenye kutokeza ya mikutano ya Kikristo. Kwa nini? Kwa sababu kwa njia ya karama hizo, Mungu alitoa ushahidi kwenye uhakika wa kwamba yeye hakuwa akitumia tena mfumo wa kidini wa Kiyahudi bali kwamba sasa roho yake ilikuwa juu ya kutaniko la Kikristo lililofanyizwa karibuni. (Mdo. 2:1-21; Ebr. 2:2-4) Kwenye mikutano ya Wakristo wa mapema, sala zilitolewa, nyimbo za kumsifu Mungu ziliimbwa, na mkazo ulitiwa juu ya kutoa unabii (yaani, kuwasilisha mafunuo ya mapenzi na kusudi la kimungu) na kutoa mafunzo ambayo yangejenga walioyasikia. Wakristo hao waliishi wakati ambao kulikuwa matukio yenye kustaajabisha kuhusiana na kusudi la Mungu. Walihitaji kuelewa hayo na kujua jinsi ya kufanya kazi kupatana nayo. Hata hivyo, njia ambayo baadhi yao walishughulikia mambo kwenye mikutano yao haikuwa yenye usawaziko, na kama vile Biblia ionyeshavyo, shauri lilihitajiwa ili mambo yafanywe kwa njia yenye kunufaisha zaidi.—1 Kor. 14:1-40.
Je, sehemu zilizoitambulisha mikutano ya Wakristo hao wa mapema zilionekana pia wakati Wanafunzi wa Biblia walipokutana pamoja katika miaka ya 1870 na baada ya hapo?
Kutimiza Mahitaji ya Kiroho ya Wanafunzi wa Biblia wa Mapema
Charles Taze Russell na kikundi kidogo cha washirika katika Allegheny, Pennsylvania, walifanyiza darasa kwa ajili ya funzo la Biblia katika 1870. Likiwa tokeo la mikutano yao, walikua hatua kwa hatua katika kumpenda Mungu na Neno lake na kwa kuendelea wakaja kujua yale ambayo Biblia yenyewe hufundisha. Hakukuwa na kusema kimuujiza katika ndimi kwenye mikutano hiyo. Kwa nini? Karama hizo za kimuujiza zilikuwa zimetimiza lengo lazo katika karne ya kwanza, na kama vile Biblia ilivyotabiri, zilikuwa zimekoma. “Hatua iliyofuata ya maendeleo,” Ndugu Russell akaeleza, “ilikuwa udhihirisho wa matunda ya Roho, kama vile Mta. Paulo aonyeshavyo wazi sana.” (1 Kor. 13:4-10) Zaidi ya hilo, kama vile katika karne ya kwanza pia, kulikuwa na kazi muhimu ya kufanya ya kueneza evanjeli, na kwa ajili ya hiyo walihitaji kitia-moyo. (Ebr. 10:24, 25) Kabla ya muda mrefu, wakawa wakifanya mikutano miwili ya ukawaida kila juma.
Ndugu Russell aling’amua kwamba lilikuwa jambo la maana kwa watumishi wa Yehova kuwa watu walioungamanika, si kitu wawe wametawanyika wapi duniani pote. Hivyo, katika 1879, muda mfupi baada ya Watch Tower kuanza kutangazwa, wasomaji walo walialikwa waombe Ndugu Russell au mmoja wa washirika wake awazuru. Takwa lililotaarifiwa wazi lilikuwa “Hakuna kutozwa wala fedha kuchukuliwa.” Baada ya maombi kadhaa kupokewa, Ndugu Russell akaanza safari ya mwezi mzima iliyompeleka mbali sana kufika Lynn, Massachusetts, akifanya mikutano kwa saa nne kufika sita kila siku katika kila kituo. Habari iliyotolewa ilikuwa “Mambo Yahusuyo Ufalme wa Mungu.”
Mapema katika 1881, Ndugu Russell aliwahimiza wasomaji wa Watch Tower ambao walikuwa hawafanyi mikutano kwa ukawaida katika eneo lao: “Anzisha mmoja katika makao yako mwenyewe pamoja na familia yako mwenyewe, au hata wachache ambao huenda wakapendezwa. Someni, jifunzeni, toeni sifa na kuabudu pamoja, na wakutanapo wawili au watatu katika jina Lake, Bwana atakuwa kati yenu—mwalimu wenu. Hiyo ndiyo iliyokuwa hali ya baadhi ya mikutano ya kanisa katika siku za Mitume. (Ona Filemoni, 2).”
Programu ya mikutano ilisitawi hatua kwa hatua. Madokezo yalitolewa, lakini kila kikundi cha mahali kiliachwa kiamue lililofaa zaidi hali zao. Msemaji angetoa hotuba pindi kwa pindi, lakini mkazo zaidi ulitolewa kwa mikutano ambamo kila mtu angeweza kujisikia huru kushiriki. Baadhi ya madarasa ya Wanafunzi wa Biblia mwanzoni hayakutumia sana vichapo vya Sosaiti kwenye mikutano yao, lakini wahudumu wasafirio, wale mapilgrimu, waliwasaidia waone thamani ya kufanya hivyo.
Baada ya baadhi ya yale mabuku ya Millenial Dawn kutangazwa, hayo yakaanza kutumiwa kuwa msingi wa funzo. Katika 1895 vikundi vya funzo vikaja kujulikana kuwa Vikundi vya Mapambazuko kwa Ajili ya Funzo la Biblia.a Wengine katika Norway baadaye walivirejezea kuwa “mikutano ya kusoma na kuzungumza,” wakiongeza: “Vifungu kutoka vitabu vya Ndugu Russell vilisomwa kwa sauti, na watu walipokuwa na maelezo au maswali, waliinua mikono yao.” Ndugu Russell alipendekeza kwamba kwenye mafunzo hayo washiriki watumie tafsiri tofauti-tofauti za Maandiko, marejezo ya pambizoni katika Biblia, na konkodansi za Biblia. Mara nyingi mafunzo yalifanywa pamoja na vikundi vyenye ukubwa wa kiasi, katika makao ya watu binafsi, katika jioni iliyokifaa kikundi. Mikutano hiyo ilikuwa tangulizi za Funzo la Kitabu la Kutaniko la siku hizi.
Ndugu Russell aling’amua kwamba mengi yalihitajiwa zaidi ya kujifunza mambo ya kimafundisho tu. Lazima kuwe pia na wonyesho wa ujitoaji ili mioyo ya watu isukumwe na uthamini wa upendo wa Mungu na tamaa ya kumheshimu na kumtumikia. Madarasa yalihimizwa yapange mkutano wa pekee kwa kusudi hilo mara moja kila juma. Ilirejezewa nyakati nyingine kuwa “Mikutano ya Nyumbani” kwa sababu ilifanywa katika makao ya watu binafsi. Programu ilitia ndani sala, nyimbo za sifa, na shuhuda zilizosimuliwa na wale waliohudhuria.b Shuhuda hizo zilikuwa nyakati nyingine mambo yaliyoonwa yenye kutia moyo; majaribu, magumu, na matatizo yaliyokabiliwa wakati wa siku za karibuni yalitiwa ndani pia. Katika sehemu fulanifulani mikutano hiyo ilipungukiwa sana katika lengo layo kwa sababu ya kukazia kupita kiasi mambo ya kibinafsi. Madokezo yenye fadhili ya kufanyia maendeleo yalionyeshwa katika The Watch Tower.
Akikumbuka mikutano hiyo, Edith Brenisen, mke wa mmojawapo mapilgrimu wa mapema katika Marekani, alisema hivi: “Ilikuwa jioni ya kutafakari juu ya utunzaji wenye upendo wa Yehova na ya ushirika wa karibu pamoja na ndugu na dada zetu. Tulipokuwa tukisikiliza baadhi ya mambo waliyoona tulizidi kuwajua vema zaidi. Kutazama uaminifu wao, kuona jinsi walivyoshinda magumu yao, mara nyingi kulitusaidia kutatua baadhi ya matatizo yetu wenyewe.” Hata hivyo, baada ya wakati ikawa wazi kwamba mikutano iliyokusudiwa kutayarisha kila mmoja kushiriki katika kazi ya kueneza evanjeli ilikuwa yenye kunufaisha zaidi.
Njia ambayo mikutano ya Jumapili iliendeshwa katika sehemu fulani ilihangaisha akina ndugu. Madarasa fulani yalijaribu kuzungumza Biblia mstari kwa mstari. Lakini nyakati nyingine tofauti za maoni kuhusu maana hazikuwa zenye kujenga hata kidogo. Ili kuleta maendeleo katika hali hiyo, watu fulani katika kutaniko la Los Angeles, California, walitayarisha mihtasari yenye kichwa cha habari kwa ajili ya funzo la Biblia. Mihtasari hiyo ilikuwa na maswali na marejezo ya kuchunguzwa na darasa zima kabla ya kuja kwenye mkutano. Katika 1902 Sosaiti ilitoa Biblia iliyokuwa na “Misaada ya Funzo la Biblia la Kiberoya,” kutia na fahirisi ya vichwa vya habari.c Ili kusahilisha mambo zaidi, kuanzia na Watch Tower la Machi 1, 1905, mihtasari kwa ajili ya mazungumzo ya kutaniko ilitangazwa, ikiwa na maswali pamoja na marejezo kwenye Biblia na vichapo vya Sosaiti kwa ajili ya utafiti. Mihtasari hiyo iliendelea mpaka 1914, kufikia wakati ambapo maswali ya funzo katika mabuku ya Studies in the Scriptures yalitangazwa ili kutumiwa yakiwa msingi kwa ajili ya Mafunzo ya Kiberoya.
Habari ileile ilipatikana kwa madarasa yote, lakini hesabu ya mikutano ya kila juma ilitofautiana kuanzia mmoja kufika minne au zaidi, kulingana na mipango ya mahali. Katika Colombo, Ceylon (sasa ni Sri Lanka), kuanzia 1914, mikutano ilikuwa kwa kweli ikifanywa siku saba kila juma.
Wanafunzi wa Biblia walitiwa moyo wajifunze kufanya utafiti, ili “kuthibitisha mambo yote,” na kueleza mawazo kwa maneno yao wenyewe. (1 The. 5:21, KJ) Ndugu Russell alitia moyo ushiriki kamili na wa hiari wa mazungumzo ya habari ya funzo. Pia alitahadharisha hivi: “Msisahau kamwe kwamba Biblia ndiyo Kiwango chetu na kwamba hata misaada yetu iwe yenye kubarikiwa na Mungu kadiri gani hiyo ni ‘misaada’ na haiwi badala ya Biblia.”
Mwadhimisho wa Kifo cha Bwana
Kuanzia kama 1876, mipango ilifanywa kila mwaka na Wanafunzi wa Biblia kwa ajili ya mwadhimisho wa kifo cha Bwana.d Mwanzoni, kikundi katika Pittsburgh, Pennsylvania, na sehemu za karibu kilikutana katika makao ya mmoja wa akina ndugu. Kufikia 1883, hudhurio lilikuwa limekua kufikia mia moja hivi katika Pittsburgh, na jumba lililokodiwa lilitumiwa. Ili kuwe na nafasi kwa ajili ya idadi kubwa ya wasikilizaji iliyotazamiwa huko katika 1905, ndugu waliamua kujipatia Carnegie Hall lenye nafasi kubwa ili walitumie.
Wanafunzi wa Biblia walitambua huo kuwa mwadhimisho wa kila mwaka, si jambo lililopasa kufanywa kila juma. Tarehe waliyoshika mwadhimisho ililingana na Nisani 14 katika kalenda ya Kiyahudi, wakati wa kifo cha Yesu. Katika muda wa miaka iliyopita, kumekuwako na kusafishwa katika njia ambayo tarehe hiyo ilihesabiwa.e Lakini jambo kuu la kuhangaikiwa ni umaana wa tukio lenyewe.
Ijapokuwa Wanafunzi wa Biblia walikutana kwa ajili ya mwadhimisho huo katika vikundi vyenye ukubwa unaotofautiana katika sehemu nyingi, wowote ambao wangeweza kujiunga na akina ndugu katika Pittsburgh walikaribishwa. Tokea 1886 kufika 1893, wasomaji wa Watch Tower hasa walialikwa waje Pittsburgh ikiwezekana, nao walifanya hivyo, kutoka sehemu mbalimbali za Marekani na Kanada. Hilo halikuwawezesha tu kuadhimisha Ukumbusho pamoja bali pia liliwasaidia kuimarisha vifungo vya umoja wa kiroho. Hata hivyo, kadiri idadi ya madarasa ilivyokua, katika Marekani na sehemu nyingine za ulimwengu pia, halikuwa jambo liwezalo kutumika kujaribu kukutana katika mahali pamoja, nao wakang’amua kwamba mambo mengi mazuri yangeweza kutimizwa kwa kukutana na waamini wenzao katika eneo la nyumbani kwa mtu.
Kama vile Watch Tower lilivyoonyesha, kulikuwa na wengi waliodai kuiamini fidia, na hakuna wowote wa hawa walioukosa mwadhimisho huo wa kila mwaka. Lakini pindi hiyo ilikuwa na umaana wa pekee kwa wale waliokuwa kikweli wa “kundi dogo” la Kristo. Hao ndio ambao wangeshiriki katika Ufalme wa kimbingu. Katika usiku wa kabla ya kifo cha Yesu, wakati alipoanzisha Ukumbusho, watu mmoja-mmoja waliokuwa wakitolewa tumaini hilo ndio ambao Kristo aliambia: “Fulizeni kufanya hili katika ukumbuko wangu.”—Luka 12:32; 22:19, 20, 28-30, NW.
Hasa kuanzia miaka ya 1930, waliotazamiwa kuwa washiriki wa “halaiki kubwa,” au “umati mkubwa” wa kondoo wengine, walianza kujidhihirisha. (Ufu. 7:9, 10, KJ; Yn. 10:16, NW) Wakati huo hao walikuwa wakirejezewa kuwa Wayonadabu. Kwa mara ya kwanza, katika toleo lalo la Februari 15, 1938, Mnara wa Mlinzi (Kiingereza) liliwaalika hususa wawepo kwenye Ukumbusho, likisema: “Baada ya saa 12 jioni katika Aprili 15 kila kampuni ya watiwa-mafuta na ikusanyike kuadhimisha Ukumbusho, waandamani wao Wayonadabu wakiwapo pia.” Walihudhuria, si wakiwa washiriki, bali wakiwa watazamaji. Kuwapo kwao kulianza kuongeza idadi ya wale waliokuwapo wakati wa Ukumbusho wa kifo cha Kristo. Katika 1938 jumla ya hudhurio ilikuwa 73,420, hali idadi ya walioshiriki mifano ya mkate na divai ilikuwa 39,225. Katika miaka iliyofuata, wale waliokuwapo wakiwa watazamaji walianza kutia ndani pia idadi kubwa za wapya wenye kupendezwa na wengine ambao hawakuwa wamekuwa Mashahidi wa Yehova watendaji. Hivyo, katika 1992, wakati kilele cha idadi ya wale waliokuwa wakishiriki katika huduma ya shambani ilipokuwa 4,472,787, hudhurio kwenye Ukumbusho lilikuwa 11,431,171, na idadi ya washiriki wa mifano ilikuwa 8,683 tu. Katika nchi fulani hudhurio limekuwa kubwa sana kama mara tano au sita zaidi ya idadi ya Mashahidi watendaji.
Kwa sababu ya kustahi sana umaana wa kifo cha Kristo, Mashahidi wa Yehova huadhimisha Ukumbusho hata wanapokabiliwa na hali ngumu sana. Wakati wa miaka ya 1970, kafyu (sheria ya kutotoka nje) za usiku za wakati wa vita katika Rhodesia (sasa yaitwa Zimbabwe) zilipofanya iwe vigumu kutoka nje jioni, akina ndugu katika maeneo fulani walikuwa wakikusanyika wote katika makao ya mmoja wa Mashahidi wa Yehova wakati wa mchana na kisha kuadhimisha Ukumbusho jioni. Bila shaka, hawangeweza kurudi nyumbani baada ya mkutano, hivyo walikuwa wakikaa humo usiku huo. Saa za jioni zilizobaki zilitumiwa kuimba nyimbo za Ufalme na kusimulia yaliyoonwa, jambo lililokuwa chanzo cha kiburudisho cha ziada.
Katika kambi za mateso wakati wa Vita ya Ulimwengu 2, Ukumbusho uliadhimishwa, hata ingawa kufanya hivyo kungalitokeza adhabu kali kama walinzi wangaligundua. Alipofungwa peke yake katika gereza la China ya Kikomunisti kutoka 1958 hadi 1963 kwa sababu ya imani yake ya Kikristo, Harold King aliadhimisha Ukumbusho vizuri kadiri alivyoweza chini ya hali hizo. Baadaye alisema hivi: “Kutoka dirisha la gereza langu nilitazama mwezi ukipevuka karibu na mwanzo wa masika. Nilihesabu tarehe ya mwadhimisho kwa uangalifu kadiri nilivyoweza.” Alifanyiza mifano iliyohitajiwa, akafanya vivi hivi divai kidogo kutokana na zabibu nyeusi na kutumia wali, usio na chachu, kama mkate. Alisema pia hivi: “Niliimba na nikasali na nikatoa hotuba kwa ukawaida kwa ajili ya pindi hiyo, kama vile ingefanywa katika kutaniko lolote la watu wa Yehova. Hivyo nilihisi kwamba kila mwaka niliungamana na ndugu zangu ulimwenguni pote katika pindi hiyo ya maana zaidi sana.”
Mahali pa Wachanga
Wakati wa miaka ya mapema, vichapo na mikutano ya Wanafunzi wa Biblia haikutayarishwa hasa ili kutosheleza mahitaji ya wachanga. Wangeweza kuhudhuria mikutano, na baadhi yao walifanya hivyo na wakasikiliza kwa hamu. Lakini hakukuwa na jitihada ya pekee ya kuwahusisha katika yale yaliyotukia. Kwa nini?
Uelewevu wa akina ndugu wakati ule ulikuwa kwamba ni muda mfupi sana uliobaki mpaka washiriki wote wa bibi-arusi wa Kristo waunganishwe naye katika utukufu wa kimbingu. Watch Tower, katika 1883 lilieleza hivi: “Sisi tulio katika mazoezi kwa ajili ya mwito wa juu hatuwezi kukengeushwa kutoka ile kazi ya pekee ya enzi hii—kazi ya kumtayarisha ‘Bibi-arusi, mke wa Mwana-Kondoo.’ Bibi-arusi apaswa kujiweka tayari; na katika muda huuhuu, wakati ambapo mapambo ya mwisho yanapowekwa katika matayarisho ya arusi, utumishi wa kila mshiriki unatakwa katika kazi hii iliyopo, iliyo ya maana zaidi ya zote.”
Wazazi walihimizwa sana wachukue daraka lao wenyewe walilopewa na Mungu la kuhangaikia ufunzaji wa kiroho wa watoto wao. Haikupendekezwa kuwa na shule za Jumapili zilizo tofauti kwa ajili ya vijana. Ilikuwa wazi kwamba utumizi wa shule za Jumapili wa Jumuiya ya Wakristo ulikuwa umeleta madhara makubwa. Wazazi waliopeleka watoto wao kwenye shule hizo walikuwa na maoni ya kwamba mpango huo uliwaondolea daraka la kuwapa watoto wao mafunzo ya kidini. Watoto, kwa upande wao, kwa sababu hawakutegemea wazazi wao kuwa chanzo cha msingi cha mafunzo juu ya Mungu, hawakusukumwa wawaheshimu wazazi wao na kuwatii kama iwapasavyo.
Hata hivyo, kutoka 1892 kufika 1927, Watch Tower lilitenga nafasi kwa ajili ya maelezo juu ya andiko lililotolewa katika “Masomo ya Shule ya Jumapili ya Kimataifa,” yaliyopendwa na wengi wakati huo katika makanisa ya Protestanti. Maandiko hayo yaliteuliwa kwa miaka mingi na F. N. Peloubet, kasisi wa Congregational Church, na wasaidizi wake. Watch Tower lilizungumzia maandiko hayo kutokana na maoni ya uelewevu wa hali ya juu wa Maandiko wa Wanafunzi wa Biblia, usiofungwa na imani za Jumuiya ya Wakristo. Ilitumainiwa kwamba kwa njia hiyo Watch Tower lingeingizwa ndani ya baadhi ya makanisa, kwamba kwa njia hiyo kweli ingetolewa, na kwamba baadhi ya washiriki wa kanisa wangeikubali. Bila shaka, tofauti ilikuwa wazi, na hilo liliwakasirisha makasisi wa Protestanti.
Mwaka 1918 ukaja, na mabaki, au wabakio wa watiwa-mafuta, walikuwa wangali duniani. Idadi ya watoto kwenye mikutano yao ilikuwa pia imeongezeka sana. Mara nyingi watoto waliruhusiwa kucheza tu huku wazazi wao wakijifunza. Hata hivyo, vijana pia, walihitaji kujifunza ‘kutafuta sana haki, kutafuta sana unyenyekevu,’ ikiwa ‘wangefichwa katika siku ya hasira ya BWANA.’ (Sef. 2:3, KJ) Kwa hiyo, katika 1918 Sosaiti ilitia makutaniko moyo yapange darasa la vijana kwa ajili ya watoto kuanzia umri wa miaka 8 hadi 15. Katika sehemu fulani hata kulikuwa na madarasa ya msingi kwa ajili ya wale walio wachanga mno kuweza kuhudhuria darasa la vijana. Wakati uleule, daraka la wazazi kuelekea watoto lilikaziwa tena.
Hilo liliongoza kwenye matukio zaidi. The Golden Age, katika 1920, lilikuwa na sehemu yenye kichwa “Funzo la Biblia kwa Vijana,” ikiwa na maswali yakiambatana na mitajo ya Maandiko ambamo majibu yangepatikana. Mwaka huohuo, The Golden Age ABC kilitangazwa; kilikuwa kijitabu chenye vielezi kwa matumizi ya wazazi katika kufundisha watoto wao kweli za msingi za Biblia na sifa za Kikristo. Kitabu chenye kichwa The Way to Paradise (Njia ya Kwenda Paradiso), kilichoandikwa na W. E. Van Amburgh, kilifuata katika 1924. Kiliwafaa “wanafunzi wa Biblia wenye ujuzi wa kadiri.” Kwa wakati fulani kilitumiwa kwenye mikutano ya walio wachanga zaidi. Kwa kuongezea, katika Amerika, “Mashahidi Wachanga” walikuwa na mipango yao wenyewe kwa ajili ya utumishi wa shambani. Katika Uswisi kikundi cha vijana kilifanyiza shirika lililoitwa “Vijana wa Yehova,” kwa ajili ya wale wa umri wa miaka kati ya 13 na 25. Walikuwa na ofisi ya mwandishi wao wenyewe katika Berne, na gazeti la pekee, Jehovah’s Youth, lilihaririwa na kuchapwa kwa matbaa za Sosaiti huko. Vijana hao walikuwa na mikutano yao wenyewe na hata walifanya drama za Biblia, kama walivyofanya katika jengo la Volkshaus katika Zurich kwa ajili ya wasikilizaji 1,500.
Hata hivyo, lililokuwa likitukia ni kwamba tengenezo lilikuwa likisitawi ndani ya tengenezo la watumishi wa Yehova. Jambo hilo halingechangia umoja, nalo lilikomeshwa katika 1936. Katika Aprili 1938, wakati wa ziara yake katika Australia, J. F. Rutherford, msimamizi wa Sosaiti, alipata kwamba darasa la watoto lilikuwa likiongozwa kando na mkusanyiko wa watu wazima. Alipanga mara moja watoto wote waletwe katika mkusanyiko mkuu, jambo ambalo liliwanufaisha sana.
Mwaka huohuo, Mnara wa Mlinzi lilipitia jambo hilo lote la madarasa tofauti kwa ajili ya vijana kutanikoni. Funzo hilo lilikazia tena uhakika wa kwamba wazazi wana daraka la kufunza watoto wao. (Efe. 6:4; linganisha Kumbukumbu la Torati 4:9, 10; Yeremia 35:6-10.) Lilionyesha pia kwamba Biblia haitoi kiolezo cha kutenga wachanga kwa njia ya madarasa ya watoto. Badala ya hivyo, walipaswa kuwapo pamoja na wazazi wao kusikia Neno la Mungu. (Kum. 31:12, 13; Yos. 8:34, 35) Maelezo zaidi ya habari ya funzo yalipohitajiwa, hayo yangeweza kutolewa na wazazi nyumbani. Zaidi ya hilo, makala hizo zilieleza kwamba mipango kwa ajili ya madarasa hayo tofauti kwa kweli ilikuwa ikiondoa fikira kwenye kazi ya kuhubiri habari njema nyumba hadi nyumba. Jinsi gani hivyo? Kwa sababu walimu hawakuwa wakienda nje kwenye utumishi wa shambani ili watayarishe kwa ajili ya madarasa hayo na kuyaongoza. Hivyo, madarasa yote tofauti kwa ajili ya vijana yakakomeshwa.
Hadi leo hii, ingali ni desturi miongoni mwa Mashahidi wa Yehova kwa familia yote kuhudhuria mikutano ya kutaniko pamoja. Watoto husaidiwa na wazazi wao kutayarisha ili waweze kushiriki katika njia zifaazo. Kwa kuongezea, wazazi wameandaliwa mfululizo mzuri wa vichapo wautumie katika kuwapa wachanga mafunzo nyumbani. Miongoni mwavyo kumekuwa vitabu Children (Watoto, Kiingereza), katika 1941; Kumsikiliza Mwalimu Mkuu, katika 1971; Kupata Faida Zote za Ujana Wako, katika 1976; Kitabu Changu cha Hadithi za Biblia, katika 1978; na Maswali Ambayo Vijana Huuliza—Majibu Yafanyayo Kazi, katika 1989.
Kuwatayarisha Wote kwa Vifaa Wawe Waeneza-Evanjeli Wenye Bidii
Tangu matoleo ya kwanza ya Watch Tower yatangazwe, wasomaji wayo wamekumbushwa kwa ukawaida juu ya pendeleo na daraka la Wakristo wote wa kweli la kupiga mbiu ya habari njema juu ya kusudi la Mungu. Mikutano ya kutaniko imesaidia kutayarisha mioyo na akili zao kwa ajili ya utendaji huo kwa kujenga upendo wao kwa Yehova na ujuzi wao wa kusudi lake. Hasa kufuatia mkusanyiko katika Cedar Point, Ohio, katika 1922, mkazo ulioongezeka sana uliwekwa juu ya jambo lililokuwa likitimizwa katika utumishi wa shambani na jinsi ya kuushiriki kwa mafanikio.
Kichapo Bulletinf (Taarifa Rasmi), kijarida kilichokuwa na habari iliyohusiana moja kwa moja na utumishi wa shambani, kilikuwa na ushuhuda mfupi, ulioitwa wakati ule mazungumzo, ambayo yalipasa kukaririwa na kutumiwa wakati wa kutoa ushahidi kwa watu. Wakati wa sehemu kubwa ya 1923, kwenye tarehe ya kwanza ya kila mwezi, kama kichocheo cha jitihada ya umoja ya kutangaza Ufalme, nusu ya vipindi vya Sala ya usiku wa Jumatano, Mkutano wa Sifa na Ushuhuda, ilitengwa itumiwe kutoa shuhuda kuhusu utumishi wa shambani.
Angalau kufikia 1926, mikutano ya kila mwezi ambamo utumishi wa shambani ulizungumzwa iliitwa Mikutano ya Wafanyakazi. Kwa kawaida wale walioshiriki hasa katika utumishi ndio waliohudhuria. Kwenye mikutano hiyo, njia zilizokuwa zikitumiwa kutoa ushahidi kwa wengine zilizungumzwa, na mipango ya utendaji wa wakati ujao ilifanywa. Kufikia 1928, Sosaiti ilikuwa ikihimiza makutaniko yafanye mikutano hiyo kila juma. Katika muda wa miaka mingine minne, badala ya Mikutano ya Ushuhuda (au, Julisho) Makutaniko yalikuwa yanaanza kufanya ule uliokuja kujulikana kuwa Mkutano wa Utumishi, na Sosaiti ilitia kila mtu moyo ahudhurie. Kwa zaidi ya miaka 60, makutaniko yamefanya mkutano huu wa kila juma. Kwa njia ya hotuba, mazungumzo yahusishayo ushirika wa wasikilizaji, maonyesho, na mahoji, msaada hususa umeandaliwa kuhusiana na pande zote za huduma ya Kikristo.
Kwa hakika namna hii ya mkutano haikuanzishwa katika karne ya 20. Yesu mwenyewe alitoa maagizo kamili kwa wanafunzi wake kabla ya kuwatuma nje kuhubiri. (Mt. 10:5–11:1; Luka 10:1-16) Baadaye, walijengana mmoja na mwenzake kwa kukutana kusimulia mambo waliyoona walipokuwa wakishiriki katika huduma.—Mdo. 4:21-31; 15:3.
Kwa habari ya mazoezi katika kutoa hotuba za watu wote, katika miaka ya mapema, hilo halikufanywa kwenye mikutano ya kutaniko ya kawaida. Hata hivyo, angalau kufikia 1916, ilidokezwa kwamba wale waliohisi kwamba walikuwa na uwezekano fulani wa kuwa wasemaji wa hadhara wangeweza kuwa na darasa lao wenyewe, kukiwa labda na mzee mmoja akiwa mratibu ili kuwasikiliza na kutoa shauri kwa ajili ya kufanyia maendeleo habari inayozungumzwa na utoaji wa hotuba zao. Mikutano hiyo iliyohudhuriwa na wanaume pekee kutanikoni, baadaye ilikuja kujulikana kuwa Shule za Manabii. Alipokuwa akipitia matukio ya siku hizo, Grant Suiter alikumbuka hivi: “Uchambuzi wenye kujenga niliopata katika shule haukuwa kitu ukilinganishwa na ule niliopokea mimi binafsi kutoka kwa baba baada ya yeye kuhudhuria kimojawapo vipindi hivyo ili kunisikia nikijaribu kutoa hotuba.” Ili kusaidia wale waliokuwa wakijaribu kufanya maendeleo, ndugu walitunga na wakachapa wao wenyewe kitabu cha mafundisho cha maagizo juu ya kusema, pamoja na mihtasari ya hotuba tofauti-tofauti. Hata hivyo, baada ya wakati, hizo Shule za Manabii zilikomeshwa. Ili kujazia uhitaji wa pekee uliokuwako wakati ule, uangalifu kamili ulikuwa ukikazwa juu ya kumtayarisha kila mshiriki wa kutaniko ili kushiriki kikamili katika kazi ya kueneza evanjeli nyumba hadi nyumba.
Je, yawezekana kumtayarisha kila mshiriki wa tengenezo hili la kimataifa lenye kukua aweze kutoa ushahidi mfupi na kutoa fasihi ya Biblia na pia kusema kwa matokeo na kuwa mwalimu wa Neno la Mungu? Hilo ndilo lililokuwa lengo la shule ya pekee iliyoanzishwa katika kila kutaniko la Mashahidi wa Yehova, kuanzia 1943. Tayari ilikuwa imekuwa ikiongozwa katika makao makuu ya ulimwengu ya Mashahidi wa Yehova tangu Februari 1942. Kila juma, maagizo yalitolewa, nao wanafunzi walitoa hotuba na kushauriwa juu yazo. Mwanzoni, ni wanaume pekee waliokuwa wakitoa hotuba katika shule hiyo, ingawa kutaniko lote lilitiwa moyo lihudhurie, litayarishe masomo, na kushiriki katika mapitio. Katika 1959 dada walipata pia pendeleo la kujiandikisha, kwa ajili ya mazoezi katika mazungumzo juu ya habari za Biblia katika kikao cha mmoja akizungumza na mwingine.
Kuhusu matokeo ya shule hiyo, tawi la Watch Tower Society la Afrika Kusini liliripoti hivi: “Mpango huo mzuri sana ulifaulu katika muda mfupi kusaidia ndugu wengi waliokuwa wamewaza kwamba hawangeweza kuwa wasemaji mbele ya watu wengi wawe wenye matokeo sana jukwaani na wenye mafanikio zaidi shambani. Katika sehemu zote za Afrika Kusini ndugu walikaribisha upaji huo mpya wa Yehova na wakautumia kwa idili. Hilo lilifanywa vijapokuwa vizuizi vikubwa vya lugha na ukosefu wa elimu wa baadhi yao.”
Shule ya Huduma ya Kitheokrasi huendelea kuwa mkutano wa maana katika makutaniko ya Mashahidi wa Yehova. Karibu wote wawezao kufanya hivyo huandikishwa. Vijana kwa wazee, Mashahidi wapya na wale wenye ujuzi mwingi hushiriki. Ni programu ya kutoa elimu yenye kuendelea.
Umma Waalikwa Uone na Kusikia
Mashahidi wa Yehova si sosaiti ya siri katika maana yoyote. Imani zao zenye msingi wa Biblia huelezwa kikamili katika vichapo vinavyopatikana kwa yeyote. Kwa kuongezea, wao hutia jitihada ya pekee kualika umma uhudhurie mikutano yao wajionee na kusikia wao wenyewe lile litukialo.
Yesu Kristo aliwapa wanafunzi wake mafunzo ya faragha, lakini pia alisema hadharani—kando ya bahari, mlimani, katika masinagogi, katika eneo la hekalu katika Yerusalemu—mahali ambapo umati ungeweza kusikia. (Mt. 5:1, 2; 13:1-9; Yn. 18:20) Katika kuiga hilo, mapema sana kama miaka ya 1870, Wanafunzi wa Biblia walianza kupanga mikutano ambamo marafiki na majirani na wengine ambao huenda wakapendezwa wangeweza kusikia hotuba juu ya kusudi la Mungu kwa wanadamu.
Jitihada ya pekee ilifanywa ili hotuba hizo zitolewe mahali ambapo pangeufaa umma. Hiyo ilijulikana kuwa kazi ya darasa la nyongeza. Katika 1911, makutaniko yaliyokuwa na wasemaji wa kutosha wenye vipawa yalitiwa moyo yapange baadhi yao waende kwenye miji na vijiji vilivyo karibu wapange na kutoa hotuba katika majumba ya umma. Mahali ilipowezekana, walipanga mfululizo wa hotuba sita. Baada ya ile ya mwisho, msemaji aliuliza ni wangapi katika wasikilizaji waliohisi kupendezwa vya kutosha katika funzo la Biblia kuweza kukutana kwa ukawaida. Hotuba kama hizo zaidi ya 3,000 zilitolewa mwaka wa kwanza.
Kuanzia 1914, ile “Photo-Drama of Creation” pia ilipelekwa kwa umma. Ndugu hawakutoza malipo ya kuingia. Tangu hapo, wametumia sinema nyinginezo na maonyesho ya slaidi. Kuanzia miaka ya 1920, redio ilianza kutumiwa sana na Watch Tower Society kuwezesha watu wasikie hotuba za Biblia nyumbani mwao wenyewe. Halafu, katika miaka ya 1930, hotuba zilizotolewa na J. F. Rutherford zilirekodiwa na kupigwa kwenye maelfu ya mikusanyiko ya watu wote.
Kufikia 1945, kulikuwa idadi kubwa ya wasemaji wa watu wote waliozoezwa katika Shule ya Huduma ya Kitheokrasi. Katika Januari wa mwaka huo, kampeni iliyoratibiwa vizuri ya mikutano ya watu wote ilianzishwa. Sosaiti iliandaa mihtasari kwa ajili ya mfululizo wa hotuba nane zenye kuufaa wakati. Vikaratasi vya ukaribishaji, na nyakati nyingine mabango, zilitumiwa kutangazia hotuba hizo. Zaidi ya kutumia mahali pa kawaida pa mikutano ya kutaniko, ndugu walitia jitihada za pekee kupangia mikutano hiyo ya watu wote katika maeneo ambayo hayakuwa na kutaniko. Wote kutanikoni wangeweza kushiriki—kwa kutangaza mikutano hiyo, kwa kuhudhuria, pamoja na kukaribisha wapya na kujibu maswali yao. Wakati wa mwaka wa kwanza wa utendaji huu wa pekee, mikutano ya watu wote 18,646 ilifanywa katika Marekani, kukiwa na jumla ya hudhurio la 917,352. Mwaka uliofuata idadi ya mikutano ya watu wote ilipanda kufikia 28,703 katika shamba la Amerika. Na katika Kanada, ambako mikutano kama hiyo 2,552 ilikuwa imepangwa katika 1945, kulikuwa 4,645 mwaka uliofuata.
Katika mengi zaidi ya makutaniko ya Mashahidi wa Yehova, Mikutano ya Watu Wote sasa ni sehemu ya ratiba ya kawaida ya mikutano ya kila juma. Mikutano hiyo inafanywa kwa namna ya hotuba ambapo kila mtu hutiwa moyo aangalie Maandiko makuu yanaposomwa na kuzungumzwa. Mikutano hiyo ni chanzo tajiri cha mafunzo ya kiroho kwa kutaniko na wapya pia.
Watu wahudhuriao mikutano ya Mashahidi wa Yehova kwa mara ya kwanza mara nyingi hupata mshangao wenye kupendeza. Mwanasiasa mashuhuri katika Zimbabwe alienda kwenye Jumba la Ufalme apate kujua yaliyokuwa yakitukia humo. Alikuwa mtu mjeuri, naye alienda bila kunyoa ndevu na bila kuchana nywele kimakusudi. Alitarajia kwamba Mashahidi wangemfukuza. Badala ya hivyo, walionyesha kupendezwa naye kikweli na wakamtia moyo awe na funzo la Biblia nyumbani. Sasa yeye ni Shahidi Mkristo mnyenyekevu na mwenye amani.
Kihalisi kuna mamilioni ya watu ambao, wakiisha kuhudhuria mikutano ya Mashahidi wa Yehova, wamehisi wakisukumwa kusema: “Mungu kwa kweli yumo miongoni mwenu.”—1 Kor. 14:25, NW.
Mahali Pafaapo pa Kukutania
Katika siku za mitume wa Yesu Kristo, mara nyingi Wakristo walifanya mikutano yao katika nyumba za watu binafsi. Katika sehemu fulani waliweza kusema katika masinagogi ya Kiyahudi. Katika Efeso mtume Paulo alitoa hotuba kwa miaka miwili katika jumba la shule. (Mdo. 19:8-10; 1 Kor. 16:19; Flm. 1, 2) Vivyo hivyo, katika sehemu ya pili ya karne ya 19, Wanafunzi wa Biblia walikutana katika nyumba za watu binafsi, nyakati nyingine walisema katika chapeli (vikanisa) za makanisa, na wakatumia majumba mengine ambayo yangeweza kukodiwa. Katika visa vichache, baadaye walinunua majengo ambayo hapo kwanza yalikuwa yametumiwa na vikundi vingine vya kidini na kuyatumia kwa ukawaida. Ndivyo ilivyokuwa kwa habari ya Brooklyn Tabernacle na London Tabernacle.
Lakini hawakuhitaji wala hawakutaka majengo yaliyopambwa kupita kiasi kwa ajili ya mikutano yao. Makutaniko machache yalinunua na kurekebisha majengo yenye kufaa; mengine yalijenga majumba mapya. Baada ya 1935 jina Jumba la Ufalme likaja kutumiwa hatua kwa hatua kuita mahali hapo pa mikutano ya kutaniko. Kwa kawaida hayo ni yenye sura yenye kuvutia lakini si ya kujionyesha. Huenda muundo ukatofautiana mahali na mahali, lakini kusudi la jengo ni kuwa lenye kutumika.
Programu Yenye Umoja ya Mafunzo
Wakati wa sehemu ya pili ya karne ya 19 na sehemu ya kwanza ya karne ya 20, ukuzi wa kiroho na utendaji ulitofautiana sana kutaniko moja na lingine. Walishiriki pamoja imani fulani za msingi zilizowatenga na Jumuiya ya Wakristo. Hata hivyo, ingawa baadhi ya akina ndugu walikuwa wakithamini sana njia ambayo Yehova alikuwa akilisha watu wake, wengine walikengeushwa vyepesi na maoni ya kibinafsi yaliyoshikiliwa sana na watu mmoja-mmoja tofauti juu ya mambo.
Kabla ya kifo chake Yesu alisali kwamba wafuasi wake wangekuwa ‘wote na umoja’—wenye umoja pamoja na Mungu na Kristo na mmoja na mwenzake. (Yn. 17:20, 21) Huo haukupaswa kuwa umoja wa kulazimishwa. Ungetokana na programu yenye umoja ya elimu ipatayo itikio katika mioyo yenye kuitikia. Kama ilivyokuwa imetabiriwa muda mrefu uliopita: “Na watoto wako wote watafundishwa na BWANA; na amani ya watoto wako itakuwa nyingi.” (Isa. 54:13) Ili kupata shangwe ya amani hiyo kwa kipimo kamili, wote walihitaji fursa ya kunufaika na funzo lenye kuendelea ambalo Yehova alikuwa akiandaa kupitia chombo chake kionekanacho cha mawasiliano.
Kwa miaka mingi Wanafunzi wa Biblia walitumia yale mabuku mbalimbali ya Studies in the Scriptures, pamoja na Biblia, vikiwa msingi wa mazungumzo. Yaliyokuwamo yalikuwa, kwelikweli, ‘chakula [cha kiroho] kwa wakati ufaao.’ (Mt. 24:45, NW) Hata hivyo, uchunguzi zaidi wa Maandiko chini ya mwelekezo wa roho ya Mungu ulifanya iwe wazi kwamba kulikuwa mengi zaidi ya kujifunza na kwamba watumishi wa Yehova walikuwa wangali wanahitaji usafishaji mwingi wa kiroho. (Mal. 3:1-3; Isa. 6:1-8) Zaidi ya hilo, baada ya Ufalme kusimamishwa katika 1914, unabii mwingi ulikuwa ukitimizwa kwa mfululizo wenye kufuatana kasi, nao ulielekeza kwenye kazi ya haraka ambayo Wakristo wote wa kweli walipaswa kushiriki. Habari hii ya Kimaandiko yenye kuufaa wakati ilikuwa ikiandaliwa kwa ukawaida kupitia safu za The Watch Tower.
Waking’amua kwamba si kila mtu makutanikoni aliyekuwa akinufaishwa na makala hizo, baadhi ya wawakilishi wasafirio wa Sosaiti walipendekeza kwa ofisi ya makao makuu kwamba kwenye mikutano ya kawaida ya kila juma makutaniko yote yajifunze The Watch Tower. Pendekezo hilo lilipitishwa kwenye makutaniko, na “Maswali ya Kiberoya” ya kutumiwa katika funzo la makala kuu za Watch Tower yakawa sehemu ya kawaida ya gazeti hilo kuanzia na toleo la Mei 15, 1922. Makutaniko mengi zaidi yalikuwa na funzo kama hilo mara moja au zaidi kila juma, lakini kadiri ambayo walijifunza kikweli yaliyokuwamo gazetini ilitofautiana. Katika sehemu fulani, kwa sababu kiongozi alikuwa na mengi ya kusema, funzo hilo liliendelea kwa saa mbili au zaidi.
Hata hivyo, katika miaka ya 1930, mpango wa kitheokrasi ulichukua mahali pa taratibu za kidemokrasi. Jambo hilo lilikuwa na uvutano mwingi juu ya jinsi funzo la Mnara wa Mlinzig lilivyoonwa. Uangalifu mwingi zaidi ulielekezwa katika kuelewa yaliyokuwamo katika habari ya funzo iliyoandaliwa na Sosaiti. Wale waliokuwa wametumia mikutano kuwa fursa za kutetea maoni yao ya kibinafsi na ambao walikinza daraka la kushiriki katika huduma ya shambani waliondoka hatua kwa hatua. Kwa msaada wenye saburi ndugu walijifunza kumaliza funzo kwa saa moja. Likiwa tokeo, kukawa na ushirika zaidi; mikutano ikawa yenye uchangamfu zaidi. Roho ya umoja wa kweli ikaja pia kuenea makutanikoni, ikitegemea programu yenye kuungamanisha ya ulishaji wa kiroho ambamo Neno la Mungu lilikuwa ndilo kiwango cha kupimia kweli.
Katika 1938, Mnara wa Mlinzi lilikuwa likitangazwa katika lugha kama 20. Kila kitu kilitokea kwanza katika Kiingereza. Kwa kawaida halikupatikana katika lugha nyinginezo kwa miezi kadhaa, au labda hata mwaka, kwa sababu ya wakati uliohitajiwa wa kulitafsiri na kulichapa. Hata hivyo, kwa sababu ya badiliko katika njia za kuchapa, wakati wa miaka ya 1980, utangazaji sawia wa Mnara wa Mlinzi uliwezekana katika lugha nyingi. Kufikia 1992, makutaniko yaelewayo yoyote ya lugha 66 yaliweza kujifunza habari ileile kwa wakati uleule mmoja. Hivyo idadi iliyo kubwa zaidi ya Mashahidi wa Yehova ulimwenguni pote hushiriki chakula cha kiroho kilekile juma kwa juma. Katika Amerika Kaskazini na Kusini yote, katika sehemu kubwa zaidi ya Ulaya, nchi kadhaa katika Mashariki, katika sehemu nyingi za Afrika, na visiwa vingi duniani pote, watu wa Yehova hufurahia mpango sawia wa ulishaji wa kiroho. Pamoja, ‘wanaunganishwa katika akili ileile na katika mstari ule ule wa fikira.’—1 Kor. 1:10, NW.
Tarakimu za mikutano yao ya kutaniko huonyesha kwamba Mashahidi wa Yehova huchukua mikutano yao kwa uzito. Katika Italia, ambako kulikuwa na Mashahidi watendaji kama 172,000 katika 1989, hudhurio la kila juma kwenye mikutano inayofanywa katika Jumba la Ufalme lilikuwa 220,458. Kwa kutofautisha, chombo cha habari cha Katoliki kilisema kwamba Waitalia asilimia 80 husema kwamba ni Wakatoliki lakini kwamba ni asilimia ipatayo 30 tu huhudhuria ibada za kanisa kwa kadiri fulani ya ukawaida. Ikionwa kwa kukadiria, hali ni hiyohiyo katika Brazili. Katika Denmark, kufikia 1989, Kanisa la Taifa lilidai asilimia 89.7 ya idadi ya watu kuwa washiriki walo, lakini ni asilimia 2 tu waliokuwa wakihudhuria kanisa kila juma! Miongoni mwa Mashahidi wa Yehova katika Denmark, tarakimu za hudhurio wakati huo zilijumlika kuwa asilimia 94.7. Katika Ujerumani, uchunguzi uliofanywa na Taasisi ya Utafiti wa Maoni ya Allensbach katika 1989 ulionyesha kwamba asilimia 5 ya Walutheri na asilimia 25 ya Wakatoliki katika Jamhuri ya Muungano ilihudhuria kanisa kwa ukawaida. Hata hivyo, kwenye Majumba ya Ufalme ya Mashahidi wa Yehova, hudhurio la kila juma lilizidi idadi ya Mashahidi.
Wale wahudhuriao huwa mara nyingi wametia jitihada kubwa ili wawepo. Katika miaka ya 1980, mwanamke mmoja katika Kenya mwenye umri wa miaka 70, alikuwa akitembea kwa ukawaida kilometa 10 na kuvuka mto ili kufika kwenye mikutano kila juma. Ili ahudhurie mikutano katika lugha yake mwenyewe, Shahidi Mkorea katika Marekani alisafiri kwa ukawaida saa tatu kwenda tu, akipanda basi, garimoshi, na mashua, pamoja na kutembea. Katika Suriname, familia moja yenye pato dogo ilitumia mshahara wa siku nzima kulipia nauli ya basi kila juma ili kufika kwenye mikutano. Katika Argentina, familia moja ilisafiri kwa ukawaida kilometa 50 na kutumia robo moja ya pato la familia ili kuhudhuria mikutano kwa ajili ya funzo la Biblia. Iwapo ugonjwa unawazuia kabisa baadhi yao kuhudhuria mikutano ya kutaniko, mara nyingi mipango hufanywa ya kuwaunganisha kwa simu au wasikie programu iliyorekodiwa katika utepe.
Mashahidi wa Yehova huchukua kwa uzito shauri la Biblia la kutoacha kukusanyika pamoja kwa ajili ya kujengwa kiroho. (Ebr. 10:24, 25) Wao hawahudhurii mikutano ya makutaniko ya kwao tu. Kuhudhuria mikusanyiko pia ni jambo kuu la programu yao ya mambo ya kila mwaka.
[Maelezo ya Chini]
a Baadaye mikutano hiyo iliitwa Vikundi vya Kiberoya kwa Ajili ya Funzo la Biblia, katika kuiga Waberoya wa karne ya kwanza waliosifiwa kwa ‘kuyachunguza Maandiko kwa uangalifu.’—Mdo. 17:11, NW.
b Kwa sababu ya yale yaliyoandikwa, mikutano hiyo iliitwa pia Mikutano ya Sala, Sifa na Ushuhuda. Kwa sababu ya umaana wa sala, baada ya wakati ilipendekezwa kwamba mara moja kila miezi mitatu mkutano uwe ibada ya sala tu, kutia na nyimbo lakini bila yaliyoonwa.
c Katika 1907 misaada ya funzo la Kiberoya ilisahihishwa, ikaongezwa sana, na kufanywa kuwa ya karibuni zaidi. Kurasa zaidi zipatazo 300 za habari yenye kusaidia ziliongezwa katika chapa ya 1908.
d Mkutano huo, nyakati nyingine, ulirejezewa kuwa Sikukuu ya Kupitwa ya ufananisho, yaani, mwadhimisho wa kifo cha Yesu Kristo, aliyefananishwa na mwana-kondoo wa Sikukuu ya Kupitwa na hivyo akaitwa “Kristo kafara wetu wa sikukuu ya kupitwa,” kwenye 1 Wakorintho 5:7. (NW) Kupatana na 1 Wakorintho 11:20, uliitwa pia Mlo wa Jioni wa Bwana. Nyakati nyingine uliitwa “Mlo wa Jioni wa Kila Mwaka,” ili kuvuta fikira kwenye uhakika wa kwamba ulikuwa mwadhimisho wa kila mwaka.
e Linganisha matoleo ya Mnara wa Mlinzi (Kiingereza) ya Machi 1891, kurasa 33-34; Machi 15, 1907, ukurasa 88; Februari 1, 1935, ukurasa 46; na Februari 1, 1948, kurasa 41-43.
f Hata kabla ya 1900 kijitabu kiitwacho Suggestive Hints to Colporteurs kilipelekwa kwa wale waliojiandikisha kwa ajili ya utumishi huo wa pekee. Kuanzia 1919 kichapo Bulletin kilitangazwa kuandaa kichocheo kwa ajili ya utumishi wa shambani, kwanza katika kugawanya The Golden Age na baadaye kwa habari ya namna zote mbalimbali za utendaji wa kueneza evanjeli.
g Jina Zion’s Watch Tower and Herald of Christ’s Presence lilibadilishwa, katika Januari 1, 1909, kuwa The Watch Tower and Herald of Christ’s Presence. Tokea Oktoba 15, 1931, jina likawa The Watchtower and Herald of Christ’s Presence.
[Blabu katika ukurasa wa 237]
Mikutano iliyotaka ushiriki wa kibinafsi
[Blabu katika ukurasa wa 238]
Si falsafa ya kiakili tu bali maneno ambayo yangeweza kuusukuma moyo
[Blabu katika ukurasa wa 246]
Wote katika familia hutiwa moyo wahudhurie mikutano pamoja
[Blabu katika ukurasa wa 252]
Kuungamanisha programu ya ulishaji wa kiroho
[Blabu katika ukurasa wa 253]
Mashahidi huchukua mikutano yao kwa uzito
[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 239]
Makutaniko ya Mapema
Kufikia 1916, kulikuwako vikundi vipatavyo 1,200 vya Wanafunzi wa Biblia ulimwenguni pote
Durban, Afrika Kusini, 1915 (juu kabisa kulia); Guiana ya Uingereza (Guyana), 1915 (katikati kulia); Trondheim, Norway, 1915 (chini kulia); Hamilton, Ontario, Kanada, 1912 (chini kabisa); Ceylon (Sri Lanka), 1915 (chini kushoto); India, 1915 (juu kushoto)
[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 240, 241]
Kumsifu Yehova kwa Wimbo
Kama vile Waisraeli wa kale na Yesu mwenyewe walivyotumia nyimbo katika ibada, ndivyo wafanyavyo Mashahidi wa Yehova katika nyakati za kisasa. (Neh. 12:46; Mk. 14:26) Huku kukiwa kunatoa sifa kwa Yehova na uthamini kwa ajili ya kazi zake, kuimba kama huko kumesaidia kukaza kweli za Biblia katika akili na moyo pia.
Mkusanyo mwingi wa nyimbo umetumiwa na Mashahidi wa Yehova kwa miaka iliyopita. Maneno ya kisasa zaidi yametumiwa kupatana na uelewevu wenye kuendelea wa Neno la Mungu.
1879: “Songs of the Bride” (Nyimbo za Bibi-Arusi)
(Nyimbo 144 zikieleza tamaa na matumaini ya bibi-arusi wa Kristo)
1890: “Poems and Hymns of Millennial Dawn” (Mashairi na Nyimbo za Mapambazuko ya Mileani)
(Mashairi 151 na Nyimbo 333, zilizotangazwa bila muziki. Nyingi zazo zilikuwa mitungo ya waandikaji mashuhuri)
1896: “Watch Tower” la Februari 1 lilitumiwa kabisa kwa ajili ya “Zion’s Glad Songs of the Morning” (Nyimbo za Nderemo za Asubuhi za Zayoni)
(Maneno ya nyimbo 11, yenye muziki; mashairi yaliyoandikwa na Wanafunzi wa Biblia)
1900: “Zion’s Glad Songs” (Nyimbo za Nderemo za Zayoni)
(Nyimbo 82, nyingi zazo zikiwa zimeandikwa na Mwanafunzi wa Biblia; kuongezea ule mkusanyo wa mapema)
1905: “Hymns of the Millennial Dawn” (Nyimbo za Mapambazuko ya Mileani)
(Nyimbo 333 zilizotangazwa katika 1890, lakini zikiwa na muziki)
1925: “Kingdom Hymns” (Nyimbo za Ufalme)
(Nyimbo 80, pamoja na muziki, hasa kwa watoto)
1928: “Songs of Praise to Jehovah” (Nyimbo za Sifa kwa Yehova)
(Nyimbo 337, mchanganyiko wa nyimbo mpya zilizoandikwa na Wanafunzi wa Biblia na nyimbo za zamani zaidi. Katika maneno hayo, jitihada ya pekee ilifanywa ili kuondoa mawazo ya dini bandia na ibada ya kiumbe)
1944: “Kingdom Service Song Book” (Kitabu cha Nyimbo za Utumishi wa Ufalme)
(Nyimbo 62. Zilizopatanishwa na mahitaji ya utumishi wa Ufalme wa nyakati zile. Sifa hazikutolewa kwa watungaji)
1950: “Songs to Jehovah’s Praise” (Nyimbo kwa Sifa ya Yehova)
(Nyimbo 91. Kitabu hicho cha nyimbo kilikuwa na vichwa vya kisasa zaidi nacho kiliacha kutumia lugha ya kikale. Kilitafsiriwa katika lugha 18)
1966: “Kuimba na Kufuatana Wenyewe kwa Muziki Katika Mioyo Yenu”
(Nyimbo 119 zenye kutia ndani kila upande wa maisha na ibada ya Kikristo. Muziki uliojulikana kuwa ulitokana na vyanzo vya kilimwengu au vya dini bandia ulifutwa. Mirekodi ya okestra ya kitabu chote ilifanywa na ikatumiwa sana kuwa ufuatanisho katika mikutano ya kutaniko. Nyimbo fulani zenye sauti ziliteuliwa zikarekodiwa pia. Kuanzia na 1980, mirekodi ya okestra ya “Melodia za Ufalme” ilitokezwa ili watu mmoja-mmoja waweze kufurahia nyumbani muziki uwezao kujenga)
1984: “Mwimbieni Yehova Sifa”
(Nyimbo za Ufalme 225, zenye maneno na melodia zikiwa zote zimetungwa na watumishi wa Yehova walio wakfu kutoka sehemu zote za dunia. Mirekodi ya sahani za santuri na kaseti ilitokezwa ili kufuatana na uimbaji)
Kwenye Mikutano ya Nyumbani ya mapema, Wanafunzi wa Biblia walitia ndani nyimbo za sifa. Upesi kuimba kukawa pia sehemu ya mikusanyiko yao. Baadhi yao waliimba mmojawapo nyimbo hizo kabla ya kiamshakinywa, wakati wa ibada yao ya asubuhi, kama ilivyofanywa kwa miaka mingi kwenye Bible House. Ingawa kuimba katika makutaniko ya mahali kuliachwa kwa sehemu kubwa kama katika mwaka 1938, kulianza tena katika 1944 na huendelea kuwa sehemu ya maana ya mikutano ya kutaniko na programu za mikusanyiko ya Mashahidi wa Yehova.
[Picha]
Karl Klein akiongoza okestra ya mkusanyiko katika 1947
[Grafu katika ukurasa wa 242]
(Ona mpangilio kamili katika nakala iliyochapishwa)
Ukumbusho wa Kifo cha Kristo
Mashahidi Watendaji
Hudhurio
11,000,000
10,000,000
9,000,000
8,000,000
7,000,000
6,000,000
5,000,000
4,000,000
3,000,000
2,000,000
1,000,000
1935 1945 1955 1965 1975 1985 1992
[Picha katika ukurasa wa 243]
Ajapofungwa peke yake katika gereza la China, Harold King aliendelea kuadhimisha Ukumbusho
[Picha katika ukurasa wa 244]
Darasa la Biblia kwa vijana katika Ujerumani, katika miaka ya mapema ya 1930
[Picha katika ukurasa wa 244]
Katika Uswisi, katika miaka ya katikati ya 1930, vijana Mashahidi walitangaza gazeti hili (chini) na wakafanya drama za Biblia (kama ionyeshwavyo chini katikati) kwa idadi kubwa za watazamaji
[Picha katika ukurasa wa 247]
“Bulletin” (Taarifa Rasmi) (1919-1935), “Director” (Mwelekezi) (1935-1936), “Informant” (Mpasha-Habari) (1936-1956), na sasa “Huduma ya Ufalme Yetu” katika lugha 100—vijarida vyote hivyo vimeandaa maagizo ya ukawaida kwa ajili ya huduma ya shambani yenye umoja ya Mashahidi wa Yehova
[Picha katika ukurasa wa 248]
Maonyesho kwenye Mikutano ya Utumishi husaidia Mashahidi kuifanya huduma yao ya shambani ya kibinafsi iwe bora (Sweden)
[Picha katika ukurasa wa 249]
Shahidi mchanga katika Kenya apata ujuzi kwa kumtolea baba yake hotuba katika Shule ya Huduma ya Kitheokrasi
[Picha katika ukurasa wa 250]
Kufikia 1992, habari ya funzo la Biblia kwa ajili ya makutaniko ya Mashahidi wa Yehova ilikuwa ikitangazwa sawia katika lugha 66, na zaidi huendelea kuongezwa
-
-
Mikusanyiko Uthibitisho wa Udugu WetuMashahidi wa Yehova—Wapiga-Mbiu wa Ufalme wa Mungu
-
-
Sura ya 17
Mikusanyiko Uthibitisho wa Udugu Wetu
MIKUSANYIKO imekuwa sehemu ya kawaida ya tengenezo la kisasa la Mashahidi wa Yehova. Lakini mikusanyiko ya kitaifa na kimataifa ya waabudu wa Yehova ilifanywa muda mrefu kabla ya karne ya 20.
Yehova aliamuru wanaume wote katika Israeli la kale wakusanyike Yerusalemu kwa ajili ya sikukuu tatu za kimajira kila mwaka. Baadhi ya wanaume walikuja na familia yao yote. Kwa kweli, Sheria ya Musa iliamuru kwamba kila mshiriki wa familia—wanaume, wanawake, na watoto—wawepo katika pindi fulani. (Kut. 23:14-17; Kum. 31:10-13; Luka 2:41-43) Mwanzoni, wahudhuriaji walikuwa watu walioishi ndani ya mipaka ya Israeli. Baadaye, Wayahudi walipotawanyika sana, wahudhuriaji wakaja kutoka mataifa mengi. (Mdo. 2:1, 5-11) Walisukumwa waje si kwa sababu tu Israeli na Abrahamu walikuwa babu zao bali kwa sababu walimtambua Yehova kuwa Baba yao mkuu wa kimbingu. (Isa. 63:16) Sikukuu hizo zilikuwa pindi za furaha. Pia zilisaidia wote waliokuwapo kuweka akili zao juu ya neno la Mungu na kutojihusisha sana na mambo ya kila siku ya maisha hivi kwamba wangesahau mambo ya kiroho yaliyo ya maana zaidi.
Vivyo hivyo, mikusanyiko ya Mashahidi wa Yehova katika nyakati za kisasa hutegemea masilahi ya kiroho. Kwa watazamaji wenye mioyo myeupe mikusanyiko hiyo hutoa uthibitisho usiokanushika kwamba Mashahidi wanaunganishwa na vifungo imara vya udugu wa Kikristo.
Mikusanyiko ya Mapema ya Wanafunzi wa Biblia
Mipango ya mikusanyiko ya Wanafunzi wa Biblia kutoka majiji na nchi mbalimbali ilisitawi hatua kwa hatua. Tofauti na vikundi vya makanisa ya kimapokeo, Wanafunzi wa Biblia, kwa njia ya mikusanyiko yao, walipata kujua upesi waamini wenzao katika sehemu nyinginezo. Mwanzoni, mikusanyiko hiyo ilifanywa Allegheny, Pennsylvania, kuhusiana na mwadhimisho wa kila mwaka wa kifo cha Bwana. Katika 1891 tangazo lilitolewa hususa kwamba kungekuwako na “mkusanyiko kwa ajili ya funzo la Biblia na kwa ajili ya kuadhimisha Ukumbusho wa Mlo wa Jioni wa Bwana.” Mwaka uliofuata Watch Tower lilikuwa na kichwa chenye kutokeza kikitangaza “MKUSANYIKO WA WAAMINI, ALLEGHENY, PA., . . . APRILI 7 HADI 14, KUTIA NDANI TAREHE HIZO MBILI, 1892.”
Umma kwa ujumla haukualikwa kwenye mikusanyiko hiyo ya mapema. Lakini, katika 1892, watu kama 400 waliokuwa wametoa uthibitisho wa imani katika fidia na kupendezwa kwa moyo mweupe na kazi ya Bwana walikuwapo. Programu ilitia ndani siku tano za funzo la Biblia lenye bidii na siku nyingine mbili za shauri lenye kusaidia kwa makolpota.
Mwanamume mmoja aliyekuwapo kwa mara ya kwanza kwenye mikusanyiko hiyo alisema hivi: “Nimekuwa kwenye Mikusanyiko mingi, lakini sijapata kamwe kabla ya hapo kuwa kwenye mmoja kama huu, ambapo mapenzi na mpango wa Mungu ndiyo mazungumzo pekee na yasiyokoma tokea kuamka hadi kwenda kulala; nyumbani, barabarani, kwenye mkutano, kwenye chakula cha mchana na kila mahali.” Kuhusu roho iliyoonyeshwa na wajumbe, mwanamume mmoja kutoka Wisconsin, Marekani, aliandika: “Nilivutiwa sana na roho ya upendo na fadhili za kidugu zilizodhihirishwa katika pindi zote.”
Badiliko katika mipango kwa ajili ya mkusanyiko wa kila mwaka lilitukia katika 1893. Ili kujifaidi na nauli zenye nafuu za garimoshi kuhusiana na Columbian Exposition kiangazi hicho Wanafunzi wa Biblia walikusanyika katika Chicago, Illinois, kuanzia Agosti 20 hadi 24. Huo ulikuwa ndio mkusanyiko wao wa kwanza nje ya eneo la Pittsburg. Hata hivyo, ili kutumia vizuri zaidi iwezekanavyo wakati na pesa kwa kazi ya Bwana, hakuna mikusanyiko zaidi mikuu iliyofanywa kwa miaka kadhaa.
Halafu, kuanzia 1898, Wanafunzi wa Biblia katika sehemu mbalimbali walianza kuchukua hatua ya kwanza katika sehemu zao kupanga makusanyiko, ambayo yangehudhuriwa na watu katika eneo dogo. Katika 1900 kulikuwa mikusanyiko 3 iliyopangwa na Sosaiti; lakini kulikuwa pia makusanyiko 13 ya mahali katika Marekani na Kanada, iliyo mingi yayo ilikuwa ya siku moja tu na mara nyingi ilifanywa kuhusiana na ziara ya mmoja wa mapilgrimu. Hesabu ilizidi kukua. Kufikia 1909 kulikuwa angalau makusanyiko 45 ya mahali katika Amerika Kaskazini kuongezea mikusanyiko iliyotumikiwa na Ndugu Russell katika safari za pekee zilizompeleka kwenye sehemu mbalimbali za bara hilo. Sehemu ya programu kwenye makusanyiko ya siku moja ilikusudiwa hasa kuchochea kupendezwa upande wa umma. Hudhurio lilikuwa la kuanzia labda mia moja kufika maelfu kadhaa.
Kwa upande mwingine, mikusanyiko mikuu, iliyohudhuriwa sanasana na Wanafunzi wa Biblia, ilikazia funzo kwa ajili ya wale walioimarika kwa kadiri fulani katika njia ya kweli. Kwa ajili ya mikusanyiko hiyo, magarimoshi ya pekee yakiwa yamejaa wajumbe yalikuwa yakija kutoka majiji makubwa. Pindi kwa pindi hudhurio lilikuwa juu kama 4,000, hata kutia wajumbe wachache kutoka Ulaya. Hizo zilikuwa nyakati za kiburudisho cha kweli cha kiroho kilichotokeza bidii na upendo ulioongezeka upande wa watu wa Yehova. Mwishoni mwa mkusanyiko mmoja katika 1903 kama huo ndugu mmoja alisema hivi: “Singepokea dola elfu kwa ajili ya wema ambao nimepokea kutoka Mkusanyiko huu;—ingawa mimi ni mtu maskini.”
Ndugu mapilgrimu ambao huenda wakawa katika eneo hilo walisema kwenye makusanyiko hayo. Ndugu Russell pia alijitahidi kuhudhuria na kutumikia katika programu kwenye makusanyiko ya mahali na kwenye mikusanyiko mikubwa zaidi katika Marekani na mara nyingi katika Kanada. Hilo lilihusisha kusafiri sana. Kwingi kati ya huko kulifanywa katika safari za mwisho wa juma. Lakini, katika 1909, ndugu mmoja katika Chicago alikodi mabehewa kadhaa ya garimoshi ili kusafirisha wajumbe waliosafiri pamoja na Ndugu Russell kutoka mkusanyiko mmoja hadi mwingine katika safari. Katika 1911 na 1913, magarimoshi mazima yalikodiwa na ndugu huyohuyo ili kupeleka mamia ya wajumbe katika safari za mkusanyiko zilizoendelea kwa mwezi mmoja au zaidi na kuenea magharibi mwa Marekani na Kanada.
Safari katika garimoshi la mkusanyiko kama hilo lilikuwa jambo la kukumbukwa. Katika 1913, Malinda Keefer alipanda moja katika Chicago, Illinois. Miaka mingi baadaye, alisema hivi: “Haikuchukua muda mrefu kujua kwamba tulikuwa familia moja kubwa . . . na garimoshi lilikuwa makao yetu kwa mwezi mmoja.” Garimoshi lilipokuwa likiondoka kituoni, wale waliokuja kuaga waliimba “Mungu Awe Nanyi Hadi Tuonanapo Tena,” muda wote huo wakipungapunga kofia na vitambaa vyao mpaka garimoshi lilipotoweka. Dada Keefer aliongeza: “Kwenye kila kituo safarini ilikuwako mikusanyiko iliyokuwa ikifanywa—mingi ilikuwa ya siku tatu, nasi tulikaa siku moja na kila mkusanyiko. Wakati wa vituo hivyo Ndugu Russell alitoa hotuba mbili, moja kwa akina ndugu alasiri, na nyingine kwa umma jioni juu ya kichwa ‘Baada ya Kifo.’”
Pia katika nchi nyingine makusanyiko yalikuwa yakiongezeka. Mara nyingi yalikuwa madogo sana. Kama 15 walikuwapo kwa ajili ya ule wa kwanza katika Norway, katika 1905; lakini ulikuwa mwanzo tu. Miaka sita baadaye, wakati Ndugu Russell alipotembelea Norway, jitihada ya pekee ilifanywa kualika umma, na hudhurio katika pindi hiyo lilikadiriwa kuwa 1,200. Wakati wa 1909, alipohudhuria mikusanyiko katika Scotland, alisema kwa watu karibu 2,000 katika Glasgow na wengine 2,500 katika Edinburgh juu ya habari yenye kuamsha kupendezwa “Mwivi Katika Paradiso, Tajiri Katika Helo, na Lazaro Kifuani mwa Abrahamu.”
Kwenye umalizio wa mikusanyiko ya mapema, ndugu walikuwa na kile walichokiita karamu ya upendo, kuonyesha hisia yao ya udugu wa Kikristo. Hiyo “karamu ya upendo” ilitia ndani nini? Kama kielelezo, wasemaji walikuwa wakipanga mstari wakiwa na sahani za mikate iliyokatwakatwa kuwa vipande vya umbo la dadu, kisha wasikilizaji walikuwa wakipita kwa mstari wakishiriki mkate, kusalimu kwa mkono, na kuimba “Na Vibarikiwe Vifungo Vifungavyo Mioyo Yetu Katika Upendo wa Kikristo.” Mara nyingi machozi ya shangwe yalikuwa yakitiririka mashavuni mwao walipokuwa wakiimba. Baadaye, kadiri hesabu zao zilivyokua, waliacha kusalimu kwa mkono na kushiriki mkate lakini walikuwa wakimalizia kwa wimbo na sala na, mara nyingi, kupiga makofi sana kuonyesha uthamini wao.
Kuanzisha Kampeni ya Duniani Pote ya Kupiga Mbiu ya Ufalme
Mkusanyiko mkubwa wa kwanza baada ya Vita ya Ulimwengu 1 ulifanywa Cedar Point, Ohio (kwenye Ziwa Erie, kilometa 96 magharibi mwa Cleveland), kutoka Septemba 1 hadi 8 katika 1919. Kufuatia kifo cha Ndugu Russell, baadhi ya wale waliokuwa wameshirikiana kimashuhuri na tengenezo waliacha kweli. Ndugu walipatwa na mitihani mikali. Mapema kidogo katika 1919, msimamizi wa Sosaiti na washirika wake walikuwa wamefunguliwa kutoka kifungo chao kisicho cha haki gerezani. Hivyo kulikuwa tarajio kubwa sana. Ijapokuwa hudhurio la siku ya kwanza lilikuwa chini, baadaye katika siku hiyo wajumbe zaidi waliwasili kwa magarimoshi ya pekee. Ndipo mameneja wa hoteli mbalimbali waliokuwa wamejitolea kuwapa wajumbe mahali pa kulala wakalemewa sana na kazi. R. J. Martin na A. H. Macmillan (wote wawili walikuwa miongoni mwa kile kikundi kilichofunguliwa toka gerezani karibuni) wakajitolea kusaidia. Walifanya kazi kuwagawia wajumbe vyumba mpaka kupita usiku wa manane, na Ndugu Rutherford na wengi kati ya wale wengine walifurahia kutumikia wakiwa wabeba-mizigo, wakibeba mizigo na kusindikiza akina ndugu kwenye vyumba vyao. Mlikuwamo roho yenye kuenea ya idili miongoni mwao wote.
Kama 2,500 walitazamiwa kuhudhuria. Hata hivyo, katika kila njia mkusanyiko ulithibitika kuwa zaidi ya ilivyotarajiwa. Kufikia siku ya pili, tayari jumba lilikuwa limejaa kupita kiasi na majumba zaidi yalitumiwa. Hilo lilipothibitika kuwa halitoshi, vipindi vilihamishwa kupelekwa nje katika eneo lililokuwa na bustani nzuri ya miti. Wanafunzi wa Biblia kama 6,000 kutoka Marekani na Kanada walikuwapo.
Kwa ajili ya hotuba kuu Jumapili, angalau 1,000 wa umma walikuja pia, hiyo iliongeza wasikilizaji kufikia 7,000 kamili, ambao msemaji alihutubia peupe bila msaada wowote wa maikrofoni au mfumo wa vikuza-sauti. Katika hotuba hiyo, “Tumaini kwa Ajili ya Wanadamu Wenye Kutaabika,” J. F. Rutherford alionyesha wazi kwamba Ufalme wa Kimesiya wa Mungu ndio utatuzi kwa matatizo ya wanadamu, na alionyesha pia kwamba Ushirika wa Mataifa (uliokuwa wakati huo ukizaliwa na ambao ulikuwa tayari umepewa kibali na makasisi) haukuwa hata kidogo wonyesho wa kisiasa wa Ufalme wa Mungu. Register gazeti la Sandusky lilikuwa na ripoti ndefu juu ya hotuba hiyo, pamoja na muhtasari wa utendaji wa Wanafunzi wa Biblia. Nakala za gazeti hilo zilipelekwa kwenye mashirika ya magazeti ya habari kotekote katika Marekani na Kanada. Lakini kulikuwako mengi zaidi yaliyomaanishwa na utangazaji uliotokana na mkusanyiko huo.
Upeo halisi wa mkusanyiko wote ulikuwa “Hotuba kwa Wafanyakazi Wenzi” ya Ndugu Rutherford, ambayo baadaye ilitangazwa chini ya kichwa “Kuutangaza Ufalme.” Ilielekezwa kwa Wanafunzi wa Biblia wenyewe. Wakati wa hotuba hiyo umaana wa herufi GA zilizokuwa zimeonekana katika programu ya mkusanyiko na katika mahali mbalimbali katika mahali pa mkusanyiko ulipata kuwa wazi. Tangazo lilitolewa kuhusu kuchapwa kwa gazeti jipya kulikokuwa kukikaribia, The Golden Age, ambalo lingetumiwa katika kuelekeza fikira za watu kwenye Ufalme wa Kimesiya. Baada ya kueleza kazi ipasayo kufanywa, Ndugu Rutherford aliambia wasikilizaji hivi: “Mlango wa fursa unafunguka mbele yenu. Uingieni upesi. Kumbukeni kwamba mwendapo mbele katika kazi hii hamsihi watu mkiwa mawakili wa gazeti tu, bali nyinyi ni mabalozi wa Mfalme wa wafalme na Bwana wa mabwana, mkitangazia watu kwa njia hiyo yenye kuheshimikia kuja kwa Enzi Bora Kabisa, ufalme wenye utukufu wa Bwana na Mkubwa wetu, ambao Wakristo wa kweli wameutumaini na kuuomba kwa karne nyingi.” (Ona Ufunuo 3:8.) Msemaji alipouliza ni wangapi waliotaka kushiriki katika kazi hiyo, itikio lenye idili lilikuwa lenye kuchochea kuliona. Wasikilizaji 6,000, wakasimama kwa umoja. Kufikia mwaka uliofuata, zaidi ya 10,000 walikuwa wakishiriki katika utumishi wa shambani. Mkusanyiko mzima ulikuwa na matokeo yenye kuleta umoja na kutia nguvu wahudhuriaji.
Miaka mitatu baadaye, katika 1922, mkusanyiko mwingine wenye kukumbukwa ulifanywa Cedar Point. Ilikuwa programu ya siku tisa, tokea Septemba 5 hadi 13. Kuongezea wajumbe kutoka Marekani na Kanada, wengine walikuja kutoka Ulaya. Mikutano iliongozwa katika lugha kumi. Wastani wa hudhurio kila siku ulikuwa kama 10,000; na kwa ajili ya hotuba “Mamilioni Wanaoishi Sasa Hawatakufa Kamwe,” wengi sana kati ya umma walikuwamo kati ya wasikilizaji hivi kwamba hudhurio lilikaribia kuwa mara mbili.
Wanafunzi wa Biblia hawakukusanyika kwenye mkusanyiko huo wakiwa na wazo la kwamba walikuwa wakipangia kazi hapa duniani ambayo ingeendelea kwa makumi ya miaka katika wakati ujao. Kwa kweli, walisema kwamba huenda ukawa ndio mkusanyiko wao mkuu wa mwisho kabla ya “kanisa kukombolewa . . . kuingizwa katika sehemu ya kimbingu ya ufalme wa Mungu, na kwa kweli katika kuwapo kwenyewe na kuliko halisi kwa Bwana wetu na Mungu wetu.” Lakini hata wakati uwe mfupi jinsi gani, kufanya mapenzi ya Mungu kulikuwa ndilo hangaiko lao la kwanza. Akifikiria hilo, katika Ijumaa, Septemba 8, Ndugu Rutherford alitoa hotuba yenye kukumbukwa “Ule Ufalme.”
Kabla ya hapo, beramu kubwa zenye herufi ADV zilikuwa zimeangikwa katika sehemu mbalimbali za uwanja. Wakati wa hotuba maana ya herufi hizo ikawa wazi msemaji alipohimiza hivi: “Iweni mashahidi waaminifu na wa kweli wa Bwana. Songeni mbele katika vita mpaka kila kisehemu cha Babiloni kiwe ukiwa. Utangazeni ujumbe kotekote. Lazima ulimwengu ujue kwamba Yehova ni Mungu na kwamba Yesu Kristo ni Mfalme wa wafalme na Bwana wa mabwana. Hii ndiyo siku ya siku zote. Tazameni, Mfalme atawala! Nyinyi ndio mawakili wa kumtangaza. Kwa hiyo mtangazeni, mtangazeni, mtangazeni, Mfalme na ufalme wake.” Wakati huo beramu kubwa, yenye urefu wa meta 11, ikakunjuka mbele ya wasikilizaji. Juu yake ilikuwapo ile shime yenye kuchochea “Mtangazeni [Kiingereza: ‘Advertise,’ ikiwakilishwa na ‘ADV’] Mfalme na Ufalme.” Ulikuwa muda wenye kutazamisha. Wasikilizaji walipiga makofi kwa idili. Ndugu Pfannebecker mwenye umri mkubwa, katika okestra ya kusanyiko, alipungapunga zeze lake juu ya kichwa chake na kusema kwa sauti kubwa kwa lahaja yake nzito ya Kijerumani: “Ach, Ya! Und now ve do it, no [Naam, na sasa tutaifanya, sivyo?]?” Nao waliifanya.
Siku nne baadaye, wakati mkusanyiko ulipokuwa ungali unaendelea, Ndugu Rutherford alishiriki binafsi pamoja na wakusanyikaji wengine walipokuwa wakishiriki kazi ya kupiga mbiu ya Ufalme nyumba hadi nyumba katika eneo ambalo halikuzidi umbali wa kilometa 72 kutoka uwanja wa mkusanyiko. Haikuishia hapo. Kazi ya kupiga mbiu ya Ufalme ilikuwa imepewa msukumo wenye nguvu ambao ungefika duniani pote. Mwaka huo zaidi ya wafanyakazi 17,000 wenye bidii katika nchi 58 walishiriki kutoa ushahidi. Miongo mingi ya miaka baadaye, George Gangas aliyekuwa kwenye mkusanyiko huo na ambaye baadaye akawa mshiriki wa Baraza Linaloongoza, alisema hivi kuhusu programu katika Cedar Point: “Ni jambo lililokazwa kikiki katika akili na moyo wangu, ambalo sitasahau kamwe maadamu ninaishi.”
Hatua za Maana Katika Ukuzi wa Kiroho
Mikusanyiko yote imekuwa nyakati za burudisho na funzo katika Neno la Mungu. Lakini baadhi yayo imekumbukwa kwa miongo ya miaka kuwa ilikuwa hatua kubwa za kiroho.
Mikusanyiko saba kati ya hiyo, ilifanywa mwaka mmoja baada ya mwingine, kuanzia 1922 hadi 1928, katika Marekani, Kanada, na Uingereza. Sababu moja ya umaana wa mikusanyiko hiyo ilikuwa yale maazimio yenye nguvu yaliyokubaliwa, yote saba yanaorodheshwa katika kisanduku katika ukurasa ufuatao. Ijapokuwa Mashahidi walikuwa wachache, waligawanya nakala nyingi kufikia milioni 45 za azimio moja, na nyingine kadhaa milioni 50, katika lugha nyingi ulimwenguni pote. Baadhi yayo yalisambazwa katika redio za kimataifa zilizounganishwa. Hivyo ushahidi wenye kutokeza ukatolewa.
Mkusanyiko mwingine tena wenye kufanyiza historia ulifanywa Columbus, Ohio, katika 1931. Jumapili, Julai 26, baada ya Wanafunzi wa Biblia kusikia hoja za Kimaandiko walikubali jina jipya—Mashahidi wa Yehova. Lilifaa kama nini! Hapa palikuwa na jina ambalo huelekeza uangalifu wa kwanza kwa Muumba mwenyewe na ambalo hutambulisha daraka la wale wamwabuduo. (Isa. 43:10-12) Kukubaliwa kwa jina hilo kuliwatia akina ndugu bidii nyingi zaidi ya vile walivyopata kuwa wakati wowote wakiwa wapiga-mbiu wa jina na Ufalme wa Mungu. Kama vile barua moja iliyoandikwa mwaka huo na Shahidi Mdenmark ilivyolieleza jambo hilo: “Oh, ni jina tukufu kama nini, Mashahidi wa Yehova, naam, kwelikweli sisi sote na tuwe hivyo.”
Katika 1935 mkusanyiko mwingine wenye kukumbukwa ulifanywa, katika Washington D.C. Katika siku ya pili ya mkusanyiko huo, Ijumaa, Mei 31, Ndugu Rutherford alizungumza juu ya halaiki kubwa, au umati mkubwa, urejezewao kwenye Ufunuo 7:9-17. Kwa zaidi ya nusu karne, Wanafunzi wa Biblia walikuwa wamejaribu bila mafanikio kutambulisha kikundi hicho kwa usahihi. Sasa, wakati wa Yehova ulipowadia, kwa msaada wa matukio ambayo tayari yalikuwa yakitukia, ilielezwa kwamba hao ni watu walio na taraja la kuishi milele papa hapa duniani. Uelewevu huo uliipa kazi ya kueneza evanjeli umaana mpya na ukaeleza Kimaandiko badiliko lililokuwa likianza tu kutukia wakati huo katika muundo wa tengenezo la kisasa la Mashahidi wa Yehova.
Mkusanyiko katika St. Louis, Missouri, katika 1941, hukumbukwa na wengi waliokuwapo kwa ajili ya hotuba ya siku ya kufungua yenye kichwa “Uaminifu-Maadili,” ambayo Ndugu Rutherford alikazia fikira lile suala kuu linalokabili viumbe vyote vyenye akili. Tangu itolewe ile hotuba “Mtawala kwa Ajili ya Watu,” katika 1928, masuala yaliyozushwa na uasi wa Shetani yameelekezewa uangalifu mara nyingi. Lakini sasa ilionyeshwa kwamba “suala kuu lililozushwa na ushindani wenye ukaidi wa Shetani lilikuwa na lingali ni lile la UTAWALA WA ULIMWENGU WOTE MZIMA.” Kuthamini suala hilo na umaana wa kudumisha uaminifu-maadili kwa Yehova akiwa Mwenye Enzi Kuu ya Ulimwengu Wote Mzima kumekuwa msukumo wenye nguvu katika maisha za watumishi wa Yehova.
Katikati ya Vita ya Ulimwengu 2, katika 1942, wakati wengine walipokuwa wakitaka kujua kama kazi ya kuhubiri ilikuwa labda karibu kwisha, hotuba ya watu wote ya mkusanyiko iliyotolewa na N. H. Knorr, msimamizi mpya aliyewekwa wa Watch Tower Society, ilikuwa “Amani—Je, Inaweza Kudumu?” Ule ufafanuzi uliotolewa katika hotuba hiyo juu ya yule “hayawani-mwitu wa rangi-nyekundu-nyangavu” wa Ufunuo sura ya 17 uliwafungulia Mashahidi wa Yehova waone kipindi kilichofuata Vita ya Ulimwengu 2 ambacho katika hicho kungekuwako fursa ya kuelekeza watu zaidi kwenye Ufalme wa Mungu. Hilo lilitoa msukumo kwa kampeni ya duniani pote ambayo kwa muda wa miaka iliyopita imefika katika nchi zaidi ya 235 na haijakwisha.
Hatua nyingine ya maana ilifikiwa wakati wa mkusanyiko katika Yankee Stadium ya New York katika Agosti 2, 1950. Katika pindi hiyo wasikilizaji wenye kushangaa na wenye furaha sana walipokea kwa mara ya kwanza New World Translation of the Christian Greek Scriptures. Sehemu iliyobaki ya New World Translation ilitolewa kwa visehemu wakati wa mwongo wa miaka uliofuata. Tafsiri hiyo ya lugha ya kisasa ya Maandiko Matakatifu ilirudisha jina la kibinafsi la Mungu kwenye mahali palifaapo katika Neno lake. Uaminifu wayo kwa yale yaliyo katika lugha za awali za Biblia umeifanya kuwa kitu chenye thamani kubwa kwa Mashahidi wa Yehova katika funzo lao wenyewe la Maandiko na katika kazi yao ya kueneza evanjeli.
Katika siku iliyotangulia ile ya mwisho ya mkusanyiko huo, F. W. Franz, wakati huo akiwa makamu wa msimamizi wa Watch Tower Society, alihutubia wasikilizaji juu ya “Mfumo Mpya wa Mambo.” Kwa miaka mingi Mashahidi wa Yehova walikuwa wameamini kwamba hata kabla ya Har–Magedoni baadhi ya watumishi wa Yehova wa kabla ya Ukristo wangefufuliwa kutoka kwa wafu wawe wakuu wa ulimwengu mpya, kwa utimizo wa Zaburi 45:16. Basi, waweza kuwazia matokeo juu ya idadi kubwa ya wasikilizaji msemaji alipouliza: “Je, kusanyiko hili la kimataifa lingefurahi kujua kwamba hapa, usiku huu, katikati yetu, mna idadi fulani ya watarajiwao kuwa wakuu wa ile dunia mpya?” Kukawa na makofi mengi yenye kuendelea sana pamoja na vigelegele vya shangwe. Halafu msemaji akaonyesha kwamba matumizi ya Kibiblia ya neno litafsiriwalo “mkuu” pamoja na rekodi ya uaminifu wa wengi wa “kondoo wengine” katika nyakati za kisasa huruhusu kuwe na imani ya kwamba baadhi ya wale wanaoishi sasa huenda wakateuliwa na Yesu Kristo kwa ajili ya utumishi wa kuwa wakuu. Hata hivyo, alieleza pia kwamba, wale wakabidhiwao utumishi huo hawangepewa majina ya cheo. Akimalizia hotuba yake, alihimiza hivi: “Haya basi, tusonge mbele, tukiwa imara, sisi sote pamoja, tukiwa jamii ya Ulimwengu Mpya!”
Kumekuwa hotuba nyingine nyingi zenye maana sana zilizotolewa kwenye mikusanyiko ya Mashahidi wa Yehova: Katika 1953, “Sosaiti ya Ulimwengu Mpya Yashambuliwa Kutoka Kaskazini ya Mbali” ulikuwa ufafanuzi wenye kunasa fikira juu ya umaana wa shambulio lifanywalo na Gogu wa Magogu kama ielezwavyo katika Ezekieli sura ya 38 na 39. Mwaka huohuo, ile hotuba: “Kuijaza Nyumba Utukufu” ilisisimua wale walioisikia walipoona mbele ya macho yao uthibitisho dhahiri wa utimizo wa ahadi ya Yehova, kwenye Hagai 2:7, wa kuleta ndani ya nyumba ya Yehova, vitu vyenye thamani, vile vitu vyenye kutamanika, kutoka kwa mataifa yote.
Hata hivyo, mkusanyiko wenye kutokeza zaidi wa nyakati za kisasa ulifanywa New York katika 1958, wakati zaidi ya watu robo milioni walipojaa na kufurika vifaa vikubwa zaidi vilivyopatikana ili kusikia hotuba “Ufalme wa Mungu Watawala—Je, Mwisho wa Ulimwengu U Karibu?” Wajumbe walikuwapo kutoka nchi 123, nazo ripoti zao kwa wasikilizaji wa mkusanyiko zilisaidia kuimarisha vifungo vya udugu wa kimataifa. Ili kuchangia ukuzi wa kiroho wa wale waliokuwapo na kuvitumia kufundisha wengine, vichapo vilitolewa kwa lugha 54 wakati wa mkusanyiko huo wenye kutokeza.
Katika 1962, mfululizo wa hotuba juu ya kichwa “Kujitiisha Chini ya Mamlaka Zilizo Kubwa” ulisahihisha uelewevu waliokuwa nao Mashahidi kuhusu maana ya Warumi 13:1-7. (NW) Katika 1964, “Kupita Kutoka Kwenye Kifo Kuja Kwenye Uhai” na “Kutoka Makaburini Kuja Kwenye Ufufuo” ilipanua uthamini wao wa rehema kuu ya Yehova kama idhihirishwavyo katika uandalizi wa ufufuo. Na mambo makuu mengi zaidi kama hayo ya mikusanyiko yangeweza kutajwa.
Kila mwaka kuna makumi ya maelfu, naam, mamia ya maelfu, ya wapya wahudhuriao mikusanyiko. Ijapokuwa habari itolewayo si mpya siku zote kwa tengenezo kwa ujumla, mara nyingi huwafungulia wahudhuriaji wapya uelewevu wa mapenzi ya kimungu ambayo huwasisimua kwelikweli. Huenda wakaona na kusukumwa wachukue fursa ya utumishi ambao hubadili mwendo wao wote wa maisha.
Kwenye mikusanyiko mingi fikira zimekazwa juu ya maana ya vitabu fulani vya Biblia. Kwa kielelezo, katika 1958 na tena katika 1977, vitabu vilivyojalidiwa vilitolewa ambavyo vilizungumzia hasa unabii uliorekodiwa na nabii Danieli kuhusu kusudi la Mungu la kuwa na serikali moja ya ulimwengu Kristo akiwa Mfalme. Katika 1971, kitabu cha Ezekieli ndicho kilichoelekezewa fikira, pamoja na mkazo wacho juu ya julisho la kimungu, “Mataifa yatalazimika kujua kwamba mimi ni Yehova.” (Eze. 36:23, NW) Katika 1972, unabii mbalimbali uliorekodiwa na Zekaria na Hagai ulizungumzwa kirefu. Katika 1963, 1969, na 1988, yalikuwako mazungumzo mapana ya unabii wenye kusisimua wa Ufunuo, ambao hutabiri waziwazi kuanguka kwa Babiloni Mkubwa na kuja kwa mbingu mpya na dunia mpya za Mungu zenye utukufu.
Mikusanyiko imekazia vichwa mbalimbali—Ongezeko la Theokrasi, Ibada safi, Wafanyakazi Wenye Umoja, Wahudumu Wajasiri, Matunda ya Roho, Kufanya Wanafunzi, Habari Njema kwa Mataifa Yote, Jina la Kimungu, Enzi Kuu ya Kimungu, Utumishi Mtakatifu, Imani Ishindayo, Uaminifu-Mshikamanifu wa Ufalme, Washika Uaminifu-Maadili, Tumaini Katika Yehova, Ujitoaji Kimungu, Wachukuaji Nuru, na vingine vingi. Kila kimojawapo kilichangia ukuzi wa kiroho wa tengenezo na wale washirikianao nalo.
Kichocheo cha Kufanya Kazi ya Kueneza Evanjeli
Mikusanyiko mikubwa, pamoja na makusanyiko madogo zaidi imekuwa kitia-moyo kikubwa kuhusiana na kazi ya kuhubiri habari njema. Hotuba na maonyesho zimetoa mafunzo yenye kutumika. Mambo yenye kufurahisha yaliyoonwa katika huduma ya shambani pamoja na yale yaliyosimuliwa na watu waliosaidiwa karibuni kujifunza kweli ya Biblia huwa sikuzote katika programu. Kwa kuongezea, utumishi halisi wa shambani ulioratibiwa wakati wa mkusanyiko kwa miaka mingi ulikuwa wenye kunufaisha sana. Ulitoa ushahidi mzuri katika jiji la mkusanyiko na ulikuwa chanzo cha kitia-moyo kwa Mashahidi wenyewe.
Utumishi wa shambani ulipata kuwa sehemu ya utendaji ulioratibiwa wa mkusanyiko katika Winnipeg, Manitoba, Kanada, katika Januari 1922. Pia ulikuwa sehemu ya mkusanyiko mkuu uliofanywa katika Cedar Point, Ohio, baadaye mwaka huo. Baada ya hapo, likawa zoea la kawaida kutenga siku moja, au sehemu ya siku au sehemu za siku kadhaa, ili wajumbe washiriki pamoja katika utendaji wa kuhubiri humohumo katika jiji la mkusanyiko. Katika maeneo ya majiji makubwa, hilo liliwapa watu wanaopatikana mara chache fursa ya kusikia habari njema juu ya kusudi la Mungu la kuwapa uhai wa milele wapendao uadilifu.
Katika Denmark ya kwanza ya siku hizo za utumishi kwenye mkusanyiko ilipangwa katika 1925, wakati 400 hadi 500 walipokutana katika Nørrevold. Kwa wengi kati ya wale 275 walioshiriki katika utumishi wa shambani kwenye mkusanyiko huo, ulikuwa ndio wakati wao wa kwanza. Baadhi yao walikuwa na hofu. Lakini baada ya kuwa wameuonja, wakawa waeneza-evanjeli wenye idili katika maeneo ya kwao pia. Kufuatia mkusanyiko huo na mpaka mwisho wa Vita ya Ulimwengu 2, kulikuwa na makusanyiko mengi ya siku moja ya utumishi yaliyofanywa katika Denmark, na ndugu walialikwa kutoka majiji ya karibu. Bidii yenye kuongezeka ilionekana wazi waliposhiriki kwa umoja katika huduma na kisha wakakutana kusikia hotuba kadhaa. Makusanyiko ya utumishi kama hayo—lakini ya urefu wa siku mbili—yalifanywa katika Uingereza na Marekani.
Kwenye mikusanyiko mikubwa zaidi utendaji wa shambani ulikuwa wa kadiri kubwa. Kuanzia 1936, hotuba ya watu wote ya mkusanyiko ilitangazwa kwa gwaride zenye utaratibu za Mashahidi waliovaa mabango na kugawanya vikaratasi vya kukaribisha umma wahudhurie mkusanyiko. (Mwanzoni mabango hayo yaliitwa “ishara za pachipachi” kwa sababu yalivaliwa moja mbele na moja nyuma.) Nyakati nyingine, Mashahidi elfu moja au zaidi walishiriki katika gwaride hizo kwenye mkusanyiko wowote ule mmoja. Wengine walishiriki katika ziara za kawaida za nyumba hadi nyumba, wakiwaalika wote waje wasikie programu. Lilikuwa jambo lenye kutia moyo sana kwa Mashahidi mmoja-mmoja kufanya kazi na kuona mamia, hata maelfu, ya Mashahidi wengine wakishiriki katika huduma pamoja nao. Wakati uleule, umma waliokuwa katika umbali mkubwa toka mjini walikuja kujua kwamba Mashahidi wa Yehova walikuwa mjini; watu walikuwa na fursa ya kusikia wao wenyewe yale ambayo Mashahidi walifundisha na kutazama wao wenyewe mwenendo wao.
Mara nyingi hotuba zilizotolewa kwenye mikusanyiko zilisikiwa na wengi sana, zaidi ya wasikilizaji wenye kuonekana. Ndugu Rutherford alipotoa hotuba, “Uhuru kwa Ajili ya Vikundi vya Watu,” kwenye mkusanyiko katika Toronto, Kanada, katika 1927, ilipelekwa kwenye idadi kubwa ya wasikilizaji wa redio wa kimataifa kwa mfululizo wenye kufanyiza historia wa vituo 53 vya usambazaji. Mwaka uliofuata, kutoka Detroit, Michigan (Marekani), ile hotuba “Mtawala kwa Ajili ya Watu” ilisambazwa na vituo vingi mara mbili ya hivyo, na mawimbi mafupi ya redio yaliipeleka kwa wasikilizaji waliokuwa mbali sana kama vile Australia, New Zealand, na Afrika Kusini.
Katika 1931, mifumo mikubwa ya redio ilikataa kushirikiana na mipango ya kusambaza hotuba ya Ndugu Rutherford; hivyo Watch Tower Society, ikifanya kazi pamoja na American Telephone and Telegraph Company, ilifanyiza mfumo wayo wenyewe wa vituo 163, kutia ndani mfumo mkubwa zaidi wa nyuzi zilizounganishwa uliopata kusambazwa, ili kupeleka mbali ujumbe “Ufalme, Tumaini la Ulimwengu.” Kuongezea, zaidi ya vituo vingine 300 katika sehemu nyingi za ulimwengu vilisambaza programu hiyo kwa kutumia sahani za santuri.
Wakati wa mkusanyiko katika Washington, D.C., katika 1935, Ndugu Rutherford alisema juu ya habari “Serikali,” akivuta fikira kwa nguvu kwenye uhakika wa kwamba karibuni mahali pa serikali zote za kibinadamu patachukuliwa na Ufalme wa Yehova chini ya Kristo. Zaidi ya 20,000 katika Washington Auditorium waliisikia. Hotuba hiyo ilipelekwa pia kwa redio na kwa nyuzi za simu duniani pote, ikafika Amerika ya Kati na ya Kusini, Ulaya, Afrika Kusini, na visiwa vya Pasifiki, na nchi za Mashariki. Wale waliosikia hotuba hiyo kwa njia hiyo huenda ikawa ilifikia mamilioni. Magazeti mawili makubwa ya habari ya Washington yalivunja mikataba ya kusambaza hotuba hiyo. Lakini magari yenye vikuza-sauti yalipelekwa na akina ndugu kwenye vituo 3 katika jiji na mahali pengine 40 katika Washington, na kutoka kwayo hotuba ilisambazwa upya kwa idadi zaidi ya wasikilizaji waliokadiriwa kuwa 120,000.
Halafu, katika 1938, ile hotuba yenye kutoboa mambo “Yakabili Mambo ya Hakika” ilipelekwa kwenye majiji 50 ya mkusanyiko duniani pote, kutoka Royal Albert Hall, katika London, Uingereza, kukiwa na jumla ya hudhurio la 200,000 hivi. Kwa kuongezea, idadi kubwa ya wasikilizaji wa redio walisikiliza hotuba hiyo.
Hivyo, ijapokuwa Mashahidi wa Yehova walikuwa wachache, mikusanyiko yao ilitimiza fungu la maana katika kupiga mbiu ya ujumbe wa Ufalme hadharani.
Mikusanyiko ya Baada ya Vita Katika Ulaya
Kwa wale waliokuwapo, mikusanyiko fulani huwa yenye kutokeza kuliko mingine. Ndivyo ilivyokuwa kuhusu ile ya Ulaya mara tu baada ya Vita ya Ulimwengu 2.
Mkusanyiko mmoja kama huo ulifanywa Amsterdam, Uholanzi, Agosti 5, 1945, miezi iliyopungua minne baada ya Mashahidi kufunguliwa kutoka kambi za mateso za Ujerumani. Wajumbe kama 2,500 walitarajiwa; 2,000 wao wangehitaji mahali pa kulala. Ili kutimiza uhitaji huo wa mahali pa kulala Mashahidi wenyeji walitandaza nyasi juu ya sakafu ya nyumba zao. Wajumbe walikuja kutoka pande zote kwa kila njia iwezekanayo—kwa mashua, kwa malori, kwa baiskeli, na kwa kuomba usaidizi wa usafiri barabarani.
Kwenye mkusanyiko huo walicheka na kutoa machozi, waliimba na kumshukuru Yehova kwa wema wake. Kama vile mmoja aliyehudhuria alivyosema: “Yao ilikuwa shangwe isiyoneneka ya tengenezo la kitheokrasi lililofunguliwa sasa hivi kutoka minyororo!” Kabla ya vita, kulikuwako Mashahidi karibu 500 katika Uholanzi. Jumla ya 426 walikamatwa na kutiwa gerezani; kati ya hao, 117 walikufa likiwa tokeo la moja kwa moja la mnyanyaso. Ilikuwa shangwe kama nini wakati wengine walipowapata kwenye kusanyiko wapendwa wao waliokuwa wamefikiria walikufa! Wengine walitoa machozi walipokuwa wakitafuta sana bila mafanikio. Jioni hiyo 4,000 walisikiliza kwa hamu sana hotuba ya watu wote iliyoeleza kwa nini Mashahidi wa Yehova walikuwa wamekuwa shabaha ya mnyanyaso mkali sana hivyo. Yajapokuwa yale yaliyokuwa yamewapata, walikuwa wakijipanga kitengenezo wasonge mbele na kazi waliyopewa na Mungu.
Mwaka uliofuata, 1946, akina ndugu katika Ujerumani walipanga kuwe na mkusanyiko katika Nuremberg. Waliruhusiwa kutumia Zeppelinwiese, zilizokuwa hapo kwanza nyanja za kufanyia gwaride za Hitler. Katika siku ya pili ya mkusanyiko, Erich Frost, ambaye alikuwa amepatwa kibinafsi na unyama wa Gestapo na alikuwa ametumia miaka kadhaa katika kambi ya mateso ya Nazi, alitoa hotuba ya watu wote “Wakristo Watahiniwa Vikali.” Watu 3,000 kati ya umma wa Nuremberg walijiunga na wale Mashahidi 6,000 waliohudhuria kwa pindi hiyo.
Siku ya mwisho ya mkusanyiko ilithibitika kuwa wakati ambapo hukumu zingetangazwa kwenye majaribio ya uhalifu wa wakati wa vita huko katika Nuremberg. Wenye mamlaka wa kijeshi walitangaza kafyu kwa siku hiyo, lakini baada ya mazungumzo marefu walikubali kwamba kwa sababu ya msimamo ambao Mashahidi wa Yehova walichukua ujapokuwa upinzani wa Nazi, haingefaa kuwazuia wasimalizie mkusanyiko wao kwa amani. Hivyo, katika siku hiyo ya mwisho, ndugu walikusanyika wasikie ile hotuba yenye kuchochea hisia “Wasio na Hofu Ijapokuwa Njama ya Ulimwengu.”
Waliona mkono wa Yehova katika yale yaliyokuwa yakitukia. Wakati uleule ambao wanaume waliowakilisha utawala wa kimabavu uliokuwa umejaribu kuwaangamiza walipokuwa wakihukumiwa, Mashahidi wa Yehova walikuwa wakikutana kumwabudu Yehova mahali penyewe ambapo Hitler alikuwa ameonyesha nguvu zake za Kinazi zenye kutazamisha. Mwenyekiti wa mkusanyiko alisema: “Kuweza kuona tu siku hii, ambayo ni ono tu la kimbele la ushindi wa watu wa Mungu juu ya maadui wao kwenye vita ya Har–Magedoni, ilistahilisha miaka tisa ya kuwa katika kambi ya mateso.”
Mikusanyiko Mingine Yenye Kukumbukwa
Kadiri ambavyo utendaji wa Mashahidi wa Yehova umepanuka, mikusanyiko imefanywa duniani pote. Yote imekuwa na sehemu zenye kutokeza kwa wale waliokuwapo.
Katika Kitwe, Rhodesia Kaskazini (sasa Zambia), katika kitovu cha Kanda ya Shaba, mkusanyiko uliratibiwa ufanywe wakati wa ziara ya msimamizi wa Watch Tower Society katika 1952. Mahali palikuwa eneo kubwa katika viunga vya mojawapo kambi za kuchimba shaba, katika mahali pajulikanapo sasa kuwa Chamboli. Sehemu ya juu ya kichuguu ilisawazishwa, na paa ikajengwa juu yayo itumike kuwa jukwaa. Vibanda vingine vilijengwa kwa ajili ya mahali pa kulala, pamoja na vitanda, kimoja juu ya kingine, zikitokeza meta 180 kutoka eneo kuu la kuketi kama njukuti (spoku) katika gurudumu la baiskeli. Wanaume na wavulana walilala katika baadhi yavyo; na wanawake na wasichana katika vile vingine. Baadhi ya wajumbe walikuwa wamesafiri kwa baiskeli kwa majuma mawili ili wawepo. Wengine walikuwa wametembea kwa siku kadhaa na kisha wakamaliza safari kwa kupanda basi la kikale.
Wakati wa vipindi wale waliokuwa miongoni mwa wasikilizaji walisikiliza kwa hamu sana, ingawa waliketia mabenchi magumu ya mianzi katika mahali palipo wazi. Walikuwa wamekuja kusikia, nao hawakutaka kukosa neno hata moja. Uimbaji wa idadi hiyo ya wasikilizaji 20,000 na kutoa machozi machoni—ulikuwa mzuri sana. Hakukuwa na ufuatishaji wa vyombo vya muziki, lakini upatano wa sauti ulikuwa mzuri sana. Si katika kuimba kwao tu bali katika kila njia, umoja ulidhihirika miongoni mwa Mashahidi hawa, ingawa walitoka katika malezi ya namna nyingi na makabila mengi.
Na je, unaweza kuwazia hisia za Mashahidi wa Yehova wa Ureno wakati baada ya kupigania uhuru wa ibada kwa karibu miaka 50, Mashahidi walipata kutambuliwa kisheria katika Desemba 18, 1974. Wakati huo walikuwa na idadi kama 14,000 tu. Katika muda wa siku chache, 7,586 wao walijaa jengo la michezo katika Porto. Siku iliyofuata, 39,284 walijaa na kuzidi stediamu ya mpira wa miguu katika Lisbon. Ndugu Knorr na Ndugu Franz walikuwa pamoja nao kwa ajili ya pindi hiyo ya furaha, ambayo wengi hawatasahau kamwe.
Kupanga Kitengenezo Mikusanyiko ya Kimataifa
Kwa zaidi ya nusu karne, Mashahidi wa Yehova wamefanya mikusanyiko mikubwa, mikusanyiko iliyofanywa sawia katika majiji mengi katika nchi nyingi. Hisi yao ya udugu wa kimataifa imeongezeka katika pindi hizo walipokuwa wameweza wote kusikia hotuba kuu zikitoka jiji moja kuu.
Hata hivyo, haikuwa mpaka 1946, wakati mkusanyiko mkubwa wa kimataifa ulipoleta pamoja katika jiji moja wajumbe kutoka sehemu nyingi za dunia. Hiyo ilikuwa katika Cleveland, Ohio. Ijapokuwa bado ilikuwa vigumu kusafiri baada ya vita, hudhurio lilifika 80,000, kutia wajumbe 302 kutoka nchi 32 nje ya Marekani. Vipindi viliongozwa kwa lugha 20. Mafunzo mengi mazuri yenye kutumika yalitolewa kwa lengo la kupanua kazi ya kueneza evanjeli. Mojawapo mambo makuu ya mkusanyiko lilikuwa hotuba ya Ndugu Knorr juu ya matatizo ya kujenga upya na kupanua. Wasikilizaji walipiga makofi kwa idili waliposikia mipango ya kuongeza vifaa vya uchapaji na vya ofisi vya makao makuu ya Sosaiti, pamoja na vifaa vyao vya usambazaji wa redio na kuanzisha ofisi za tawi katika nchi kubwakubwa za ulimwengu, kupanua vifaa vyayo vya usambazaji wa redio, kuongezea kazi ya mishonari. Mara baada ya mkusanyiko huo, mambo mengi yalitayarishwa ili Ndugu Knorr na Ndugu Henschel waweze kufunga safari ya ulimwenguni pote kutekeleza yaliyokuwa yamezungumzwa.
Katika miaka iliyofuata, mikusanyiko yenye kufanyiza historia kwelikweli ilifanywa katika Yankee Stadium ya New York City. Kwenye ule wa kwanza wayo, kuanzia Julai 30 hadi Agosti 6, 1950, wajumbe walikuwapo kutoka nchi 67. Programu ilitia ndani ripoti fupi zilizotolewa na watumishi wa matawi, wamishonari, na wajumbe wengine. Hao waliupa mkusanyiko mambo yenye kusisimua kuonyesha ile kazi ya bidii ya kueneza evanjeli iliyokuwa ikifanywa katika nchi zote walikokuwa wametoka. Siku ya mwisho, hudhurio lilipanda kufika 123,707 kwa ajili ya hotuba “Je, Unaweza Kuishi Milele kwa Furaha Duniani?” Kichwa cha mkusanyiko kilikuwa “Ongezeko la Theokrasi.” Uangalifu ulielekezwa kwenye ongezeko kubwa la idadi. Hata hivyo, kama vile mwenyekiti, Grant Suiter, alivyoonyesha kwa mkazo, hilo halikufanywa ili kusifu watu wenye akili sana katika tengenezo lionekanalo. Bali, alijulisha: “Yehova ndiye wa kusifiwa kwa ajili ya idadi hiyo kubwa. Yapaswa kuwa hivyo, nasi hatungetaka iwe vingine.”
Katika 1953, mkusanyiko mwingine ulifanywa Yankee Stadium katika New York. Wakati huo hudhurio lilikuwa na kilele cha 165,829. Kama ilivyokuwa kwa mkusanyiko wa kwanza hapo, programu ilijaa mazungumzo ya unabii mbalimbali wa Biblia wenye kusisimua, shauri lenye kutumika juu ya jinsi ya kufanya kazi ya kuhubiri habari njema, na ripoti kutoka nchi nyingi. Ijapokuwa vipindi vilianza kama saa 3:30 asubuhi, kwa kawaida havikumalizika mpaka 3:00 au 3:30 usiku. Mkusanyiko huo uliandaa siku nane kamili za karamu ya kiroho yenye shangwe.
Kwa ajili ya mkusanyiko wao mkubwa kupita yote, katika New York katika 1958, ilikuwa lazima kutumia Yankee Stadium na pia Polo Grounds ulio karibu pamoja na maeneo ya ziada nje ya stediamu ili umati wa ziada wa mkusanyiko upate mahali pa kukaa. Siku ya mwisho, wakati kila kiti kilipokuwa kimekaliwa, ruhusa ya pekee ilitolewa kutumia hata sehemu ya ndani ya uwanja wa michezo wa Yankee Stadium, na ilisisimua kama nini kuona maelfu yakimiminika, yakatoa viatu, na kuketi kwenye nyasi! Idadi ilionyesha kuwa 253,922 walihudhuria kusikia hotuba ya watu wote. Uthibitisho zaidi wa baraka ya Yehova juu ya huduma ya watumishi wake ulionwa wakati 7,136 kwenye mkusanyiko huo walipoonyesha wakfu wao kwa uzamisho wa maji—zaidi ya mara mbili ya idadi ya waliobatizwa katika ile pindi yenye kufanyiza historia ya Pentekoste 33 W.K., kama ilivyoripotiwa katika Biblia!—Mdo. 2:41.
Uendeshaji wote wa mikusanyiko hiyo ulitoa uthibitisho wa jambo lililo zaidi ya tengenezo lenye ufanisi. Ulikuwa udhihirisho wa roho ya Mungu ikifanya kazi miongoni mwa watu wake. Upendo wa kidugu ambao msingi wao ni kumpenda Mungu ulionekana wazi kila mahali. Hakukuwa na wapangaji mambo wenye kulipwa mshahara. Kila idara iliendeshwa na wenye kujitolea wasiolipwa. Ndugu na dada Wakristo, mara nyingi vikundi vya familia, walishughulikia viburudisho. Pia walitayarisha milo yenye moto, na katika mahema makubwa nje ya stediamu, walipakulia wajumbe milo kwa mwendo wa kufikia elfu moja kwa dakika moja. Makumi ya maelfu—wote wakiwa na furaha ya kushiriki kazi—walitumikia wakiwa wakaribishaji na wakashughulikia ujenzi wote uliohitajiwa, upishi na upakuaji wa milo, usafi, na mengi zaidi.
Wenye kujitolea wengine wengi walitumia mamia ya maelfu ya saa ili kutimiza mahitaji ya mahali pa kulala ya wajumbe. Katika miaka fulani, ili kutimiza mahitaji ya angalau baadhi ya wakusanyikaji, majiji yalipangwa kwa kutumia mahema na trela. Katika 1953 Mashahidi walimvunia mkulima mmoja katika New Jersey hekta 16 za nafaka bila malipo, ambaye aliwakodisha shamba lake kwa ajili ya jiji lao la trela. Vyoo, umeme, mabafu, madobi, kafeteria, na maduka, yalijengwa ili kutimiza mahitaji ya idadi iliyozidi 45,000. Walipoingia mahali hapo, jiji lilijengwa kwa usiku mmoja. Maelfu mengi zaidi walipata mahali pa kulala katika mahoteli na nyumba za watu binafsi katika New York. Ilikuwa kazi kubwa mno. Kwa baraka za Yehova, ilitimizwa kwa mafanikio.
Mikusanyiko Katika Mwendo
Washiriki wa udugu huu wa kimataifa wanapendezwa sana na Mashahidi wenzao katika nchi nyinginezo. Likiwa tokeo, wametumia fursa ili kuhudhuria mikusanyiko nje ya nchi za nyumbani kwao.
Wakati kusanyiko la kwanza kati ya ule mfululizo wa Ibada Safi Kusanyiko lilipofanywa katika Wembley Stadium katika London, Uingereza, katika 1951, Mashahidi kutoka nchi 40 walikuwapo. Programu ilikazia upande wenye kufaa wa ibada ya kweli na kufaa kwa mtu kufanya huduma kuwa kazi yake ya maisha. Kutoka Uingereza, Mashahidi wengi walisafiri kwenda Bara Ulaya, ambapo mikusanyiko mingine tisa ilifanywa wakati wa miezi miwili iliyofuata. Mkubwa kupita yote kati yayo ulikuwa katika Frankfurt am Main, Ujerumani, ambapo 47,432 walikuwapo kutoka nchi 24. Uchangamfu wa akina ndugu ulionyeshwa mwishoni mwa programu wakati okestra ilipoanza kupiga muziki nao ndugu Wajerumani wakaanza ghafula kuimba kutoka moyoni wimbo wa kuaga wakiwakabidhi kwa Mungu Mashahidi wenzao waliokuwa wamekuja kutoka ng’ambo kujiunga nao. Vitambaa vya mkononi vilipungwapungwa, na mamia wakamiminika uwanjani kuonyesha uthamini wao binafsi kwa ajili ya karamu hiyo nzuri ya kitheokrasi.
Katika 1955, Mashahidi zaidi walipanga kutembelea ndugu zao Wakristo katika ng’ambo wakati wa mkusanyiko. Kwa njia ya meli mbili zilizokodiwa (kila moja ikiwa na abiria 700) na ndege 42 zilizokodiwa, wajumbe kutoka Marekani na Kanada walienda Ulaya. Chapo la Ulaya la gazeti The Stars and Stripes, lililosambazwa katika Ujerumani, lilieleza mmiminiko wa Mashahidi kuwa ‘labda ndio Waamerika wengi zaidi waliopata kwenda Ulaya tangu uvamizi wa Mataifa Marafiki wakati wa Vita ya Ulimwengu 2.’ Wajumbe wengine walikuja kutoka Amerika ya Kati na ya Kusini, Asia, Afrika, na Australia. Zijapokuwa jitihada za makasisi wa Jumuiya ya Wakristo za kuzuia Mashahidi wasifanye mikusanyiko yao katika Roma na Nuremberg, hiyo miwili na mingine sita ilifanywa katika Ulaya wakati wa kiangazi. Hudhurio lilikuwa kuanzia 4,351 katika Roma kufika 107,423 katika Nuremberg. Kikundi kingine cha 17,729 kilikusanyika Waldbühner katika ile iliyokuwa wakati huo Berlin Magharibi, ambapo ndugu kutoka eneo la Mashariki la enzi hiyo wangeweza kufika bila hatari kubwa. Wengi kati yao walikuwa wamekuwa katika gereza kwa ajili ya imani yao au walikuwa na washiriki wa familia waliokuwa gerezani wakati huo, lakini walikuwa wangali thabiti katika imani. Kichwa cha mkusanyiko kilifaa kama nini—“Ufalme Wenye Kushinda”!
Ingawa tayari kulikuwa kumekuwa mikusanyiko mingi ya kimataifa, lililotukia katika 1963 lilikuwa la kwanza la aina yake. Ulikuwa mkusanyiko wa ulimwenguni pote. Ukianzia Milwaukee, Wisconsin, katika Marekani, ulisonga mbele kwenda New York; kisha, kwenye majiji makubwa manne katika Ulaya; kupitia Mashariki ya Kati; kusonga mbele hadi India, Burma (sasa Myanmar), Thailand, Hong Kong, Singapore, Filipino, Indonesia, Australia, Taiwan, Japani, New Zealand, Fiji, Jamhuri ya Korea, na Hawaii; na kisha kurudi kwenye bara la Amerika Kaskazini. Kwa ujumla, wajumbe kutoka nchi 161 walikuwapo. Jumla ya hudhurio ilizidi 580,000. Walikuwapo 583, kutoka nchi kama 20, walioandamana na mkusanyiko, wakihudhuria katika nchi moja baada ya nyingine, duniani pote. Safari za utalii za pekee ziliwawezesha kuona sehemu za kidini zenye kupendeza, na pia walishiriki pamoja na ndugu na dada wenyeji katika huduma ya nyumba hadi nyumba. Wasafiri hao walijilipia gharama zao wenyewe.
Wajumbe wa Amerika ya Latin walikuwa wamewakilishwa vizuri kwenye mingi ya mikusanyiko hiyo ya kimataifa. Lakini katika 1966-1967, ilikuwa zamu yao ya kuwa wakaribishaji wa mikusanyiko. Wale waliohudhuria hawatasahau kamwe ile drama iliyolifanya kuwa na uhai lile simulizi la Biblia kuhusu Yeremia na ambayo ilisaidia kila mtu kuthamini maana yalo kwa siku yetu.a Vifungo vya upendo wa Kikristo viliimarishwa wageni walipokuwa wakijionea wenyewe hali ambazo katika kampeni kubwa ya elimu ya Biblia ilikuwa ikitimizwa katika Amerika ya Latin. Walivutwa sana na imani yenye nguvu ya waamini wenzao, wengi wao walikuwa wameshinda vizuizi vilivyoelekea kutoshindika—upinzani wa familia, mafuriko, kupoteza mali—ili wahudhurie. Walitiwa moyo sana na mambo yaliyoonwa kama lile la dada painia wa pekee kutoka Uruguai dhaifu aliyehojiwa na ambaye alikuwa jukwaani na wengi kati ya watu 80 ambao tayari alikuwa amesaidia kufanya maendeleo kufikia hatua ya ubatizo wa Kikristo! (Kufikia 1992, dada huyo alikuwa amesaidia watu 105 kufikia hatua ya ubatizo. Yeye alikuwa angali dhaifu na angali ni painia wa pekee!) Pia ilichangamsha moyo kama nini kukutana na wamishonari kutoka yale madarasa ya mapema zaidi ya Gileadi wakiwa wangali wanafanya kazi katika migawo yao! Mikusanyiko hiyo ilikuwa kichocheo kizuri kwa kazi iliyokuwa ikifanywa katika sehemu hiyo ya ulimwengu. Katika nyingi za nchi hizo, sasa kuna wasifaji wa Yehova wengi kama mara 10, 15, au hata 20 kama wale waliokuwako wakati ule.
Miaka michache baadaye, katika 1970-1971, iliwezekana kwa Mashahidi kutoka ng’ambo kuwa na ushirika pamoja na ndugu zao kwenye mikusanyiko ya kimataifa iliyofanywa barani Afrika. Mkubwa kupita yote kati ya mikusanyiko hiyo ya Kiafrika ulikuwa Lagos, Nigeria, ambapo ilikuwa lazima kujenga vifaa vyote kuanzia chini kwenda juu. Ili kukinga wajumbe na jua kali, jiji la mianzi lilijengwa—maeneo ya kuketi, mabweni, kafeteria, na idara nyinginezo. Ilitaka nguzo za mianzi 100,000 na mikeka mikubwa 36,000, iliyofumwa kwa matete—yote ikiwa imetayarishwa na ndugu na dada. Programu ilitolewa katika lugha 17 wakati uleule mmoja. Hudhurio lilifika 121,128, na Mashahidi wapya 3,775 wakabatizwa. Vikundi vingi vya Kikabila viliwakilishwa, na wengi wa wale waliokuwapo walikuwa watu waliozoea kupigana. Lakini sasa, ilikuwa shangwe kama nini kuwaona wakiwa wameungana katika vifungo vya udugu halisi wa Kikristo!
Baada ya mkusanyiko, baadhi ya wajumbe wa nchi za kigeni walisafiri kwa basi kwenda nchi ya Waigbo kuona lile eneo lililoathiriwa vibaya sana na vita ya hivi karibuni ya wenyewe kwa wenyewe. Udadisi mwingi ulitokezwa katika mji baada ya mji wageni walipokuwa wakisalimiwa na kukumbatiwa na Mashahidi wenyeji. Watu walikimbia barabarani kutazama. Wonyesho huo wa upendo na umoja kati ya weusi na weupe ulikuwa jambo ambalo hawakuwa wamepata kuona kamwe.
Katika nchi fulani idadi ya Mashahidi wa Yehova hufanya isiwezekane kwao wote kukusanyika pamoja katika mahali pamoja. Hata hivyo, pindi kwa pindi, mikusanyiko kadhaa imefanywa kwa wakati mmoja, mingine zaidi ikifuata, juma baada ya juma. Katika 1969, umoja uliohisiwa kwenye mikusanyiko iliyopangwa kwa njia hiyo ulizidishwa na uhakika wa kwamba baadhi ya wasemaji wakuu walisafiri kwa ndege kwenda na kurudi kati ya mikusanyiko hiyo, hivyo kuitumikia yote. Katika 1983 na 1988, umoja kama huo ulihisiwa wakati idadi fulani ya mikusanyiko mikubwa yenye kutumia lugha moja ilipounganishwa pamoja, hata kimataifa, kwa kupisha kwa njia ya simu hotuba kuu zilizotolewa na washiriki wa Baraza Linaloongoza. Hata hivyo, msingi halisi wa umoja miongoni mwa Mashahidi wa Yehova ni uhakika wa kwamba wote humwabudu Yehova akiwa ndiye Mungu wa pekee wa kweli, wote hushikamana na Biblia ikiwa mwongozo wao, wote hunufaika kutokana na programu ileile moja ya ulishaji wa kiroho, wote humtegemea Yesu Kristo akiwa Kiongozi wao, wote hutafuta kudhihirisha matunda ya roho ya Mungu katika maisha zao, wote huweka tumaini lao katika Ufalme wa Mungu, na wote hushiriki katika kupelekea wengine habari njema za Ufalme huo.
Wamefanywa Tengenezo ili Wamsifu Yehova Kimataifa
Mashahidi wa Yehova wameongezeka idadi kiasi cha kuzidi idadi ya watu wa mataifa mengi moja moja. Ili mikusanyiko yao itimize mengi zaidi yaliyo mema, mipango mingi ya uangalifu hutakwa. Hata hivyo, maombi sahili yaliyochapwa kuhusu mahali ambapo Mashahidi kutoka maeneo mbalimbali wapaswa kuhudhuria kwa kawaida ndiyo tu huhitajiwa ili kuhakikisha kwamba kutakuwa nafasi ya kutosha kwa kila mtu. Mikusanyiko ya kimataifa inapopangwa, mara nyingi sasa Baraza Linaloongoza linahitaji kufikiria idadi ya Mashahidi kutoka nchi nyingine ambao wangependa kwenda na walio katika hali ya kuweza kufanya hivyo na pia ukubwa wa vifaa vipatikanavyo vya mkusanyiko, idadi ya Mashahidi wenyeji ambao watahudhuria, na kiasi cha mahali pa kulala panapopatikana kwa ajili ya wajumbe; kisha tarakimu isiyopasa kuzidi yaweza kugawiwa kila nchi. Ndivyo ilivyokuwa kuhusu ile Mikusanyiko mitatu ya “Ujitoaji Kimungu” iliyofanywa Poland katika 1989.
Kwa ajili ya mikusanyiko hiyo Mashahidi wa Yehova kama 90,000 walitazamiwa kutoka Poland kuongezea maelfu ya watu wapya wenye kupendezwa. Pia wengi walialikwa wahudhurie kutoka Uingereza, Kanada, na Marekani. Vikundi vikubwa vya wajumbe vilikaribishwa kutoka Italia, Ufaransa, na Japani. Vingine vilikuja kutoka nchi za Skandinevia na Ugiriki. Angalau nchi 37 ziliwakilishwa. Kwa ajili ya sehemu fulani za programu, ilikuwa lazima kutafsiri Kipoland au Kiingereza katika lugha nyingine nyingi kama 16. Jumla ya hudhurio ilikuwa 166,518.
Vikundi vikubwa vya Mashahidi kwenye mikusanyiko hiyo vilikuwa vimekuja kutoka ule uliokuwa wakati huo Muungano wa Sovieti na kutoka Chekoslovakia; vikundi vikubwa vilikuwapo pia kutoka nchi nyingine za Ulaya Mashariki. Hoteli na mabweni ya shule hayangeweza kuwaandalia wote mahali pa kulala. Kwa ukaribishaji-wageni, Mashahidi Wapoland walifungua mioyo na makao yao, wakishiriki kwa furaha walivyokuwa navyo. Kutaniko moja la wahubiri 146 liliandalia wajumbe zaidi ya 1,200 mahali pa kulala. Kwa baadhi ya wale waliohudhuria mikusanyiko hiyo, ilikuwa mara ya kwanza ambayo walipata wakati wowote kuwa kwenye mkusanyiko mkubwa wa watu wa Yehova zaidi ya 15 au 20. Mioyo yao ilijaa uthamini walipokuwa wakitazama makumi ya maelfu katika stediamu hizo, wakijiunga katika sala, na kuunganisha sauti zao katika nyimbo za sifa kwa Yehova. Walipochangamana pamoja kati ya vipindi, kulikuwako kukumbatiana kwa uchangamfu, hata ingawa tofauti za lugha mara nyingi ziliwazuia kusema kwa maneno yale yaliyokuwa mioyoni mwao.
Mkusanyiko ulipokuwa ukifikia mwisho, mioyo yao ilijaa shukrani kwa Yehova, aliyeyawezesha yote. Katika Warsaw, baada ya maelezo ya kuaga ya mwenyekiti, wasikilizaji walipiga makofi ghafula ambayo yaliendelea bila kupungua kwa angalau dakika kumi. Baada ya wimbo na sala ya mwisho, makofi yakarudiwa, nao wasikilizaji walikawiakawia vitini kwa muda mrefu. Walikuwa wamengojea pindi hiyo kwa miaka mingi, nao hawakutaka iishe.
Mwaka uliofuata, 1990, muda ulio punde kuliko miezi mitano baada ya kuondolewa marufuku ya miaka 40 juu ya Mashahidi wa Yehova katika ile iliyokuwa wakati ule Ujerumani Mashariki, mkusanyiko mwingine wa kimataifa wenye kusisimua ulifanywa, huo katika Berlin. Miongoni mwa wale 44,532 waliokuwapo mlikuwamo wajumbe kutoka nchi 65 tofauti. Kutoka nchi fulani, ni wachache tu waliokuwa wamekuja; kutoka Poland, kama 4,500 walikuja. Maneno hayangeweza kueleza zile hisia zenye kina za wale ambao hawakuwa wamepata kamwe uhuru wa kuhudhuria mkusanyiko kama huo, na wakati wasikilizaji wote walipojiunga katika nyimbo za sifa kwa Yehova, hawangeweza kuzuia machozi ya shangwe.
Baadaye mwaka huo, mkusanyiko kama huo ulipofanywa katika São Paulo, Brazili, stediamu mbili kubwa zilihitajiwa kukaliwa na wasikilizaji wa kimataifa 134,406. Hiyo ilifuatwa na mkusanyiko katika Argentina, ambako kwa mara nyingine tena stediamu mbili zilitumiwa sawia kuandaa mahali pa kuketi kwa ajili ya wasikilizaji wa Kimataifa. Mwaka 1991 ulipokuwa ukianza, mikusanyiko zaidi ya kimataifa ilikuwa ikianza katika Filipino, Taiwan, na Thailand. Idadi kubwa za wasikilizaji kutoka mataifa mengi zilikuwapo pia mwaka huo kwa ajili ya mikusanyiko katika Ulaya Mashariki—katika Hungaria, Chekoslovakia, na ile ambayo sasa ni Kroatia. Na katika 1992, wajumbe kutoka nchi 28 waliliona kuwa pendeleo la pekee kuwa miongoni mwa wale 46,214 waliokuwa katika St. Petersburg kwa ajili ya mkusanyiko wa kwanza ulio wa kimataifa kwelikweli wa Mashahidi wa Yehova katika Urusi.
Fursa za Burudisho la Kiroho la Ukawaida
Si mikusanyiko yote ifanywayo na Mashahidi wa Yehova huwa mikusanyiko ya kimataifa. Hata hivyo, Baraza Linaloongoza hupangia mikusanyiko mikubwa mara moja kwa mwaka, na programu ileile moja hufurahiwa ulimwenguni pote katika lugha nyingi. Mikusanyiko hiyo yaweza kuwa mikubwa sana, ikiandaa fursa ya ushirika pamoja na Mashahidi wengine kutoka sehemu nyingi, au yaweza kuwa midogo zaidi ikifanywa katika majiji mengi, ikifanya iwe rahisi kwa wapya kuhudhuria na kuwezesha umma katika mamia ya majiji madogo zaidi kujionea karibukaribu kikundi kikubwa chenye kuwakilisha Mashahidi wa Yehova.
Kwa kuongezea, mara moja kwa mwaka kila mzunguko (labda wenye makutaniko 20) hukusanyika kwa ajili ya programu ya siku mbili ya shauri na kitia-moyo cha kiroho.b Pia, tangu Septemba 1987, siku ya kusanyiko la pekee, programu ya siku moja yenye kujenga, hupangiwa kila mzunguko mara moja kwa mwaka. Inapowezekana, mshiriki wa wafanyakazi wa makao makuu ya Sosaiti au mtu fulani kutoka katika ofisi ya tawi ya mahali hutumwa akashiriki katika programu hiyo. Programu hizo huthaminiwa sana na Mashahidi wa Yehova. Katika maeneo mengi mahali pa kusanyiko hapako mbali wala si vigumu kupafika. Lakini haiwi hivyo sikuzote. Mwangalizi mmoja asafiriye hukumbuka mume na mke wenye umri mkubwa waliotembea kilometa 76 wakiwa na masanduku na mablanketi ili kuhudhuria kusanyiko la mzunguko katika Zimbabwe.
Utumishi wa shambani wakati wa mkusanyiko hauwi sehemu tena hata kidogo kwenye makusanyiko hayo, lakini hiyo si kwa sababu Mashahidi huuona kwa vyovyote kuwa wenye maana ndogo. Katika visa vingi watu wanaoishi karibu na mahali pa makusanyiko wanatembelewa sasa kwa ukawaida na Mashahidi wenyeji—katika visa fulani, kila baada ya majuma machache. Wajumbe wa kusanyiko hufuliza kuwa macho waone fursa za kutoa ushahidi wa vivi hivi, na mwenendo wao wa Kikristo hutoa ushahidi wenye nguvu kwa njia nyingine.
Uthibitisho wa Udugu wa Kweli
Udugu udhihirikao miongoni mwa Mashahidi kwenye mikusanyiko hiyo huonekana wazi kwa urahisi na watazamaji. Wanaweza kuona kwamba hakuna upendeleo miongoni mwao na kwamba uchangamfu halisi uko wazi hata miongoni mwa wale ambao huenda wakakutana kwa mara ya kwanza. Wakati wa Mapenzi ya Kimungu Kusanyiko la Kimataifa katika New York katika 1958, gazeti Amsterdam News la New York (Agosti 2) liliripoti hivi: “Kila mahali Wanegro, weupe na watu wa Mashariki, kutoka tabaka zote maishani na sehemu zote za ulimwengu, walichangamana pamoja kwa furaha na uhuru. . . . Mashahidi waabuduo kutoka nchi 120 wameishi na kuabudu pamoja kwa amani, wakawaonyesha Waamerika jinsi hilo linavyowezekana kwa urahisi. . . . Kusanyiko hilo ni kielelezo bora sana cha kuonyesha jinsi watu wanavyoweza kufanya kazi na kuishi pamoja.”
Hivi karibuni zaidi, Mashahidi wa Yehova walipofanya mikusanyiko wakati uleule mmoja katika Durban na katika Johannesburg, Afrika Kusini, katika 1985, kati ya wajumbe mlikuwamo vikundi vyote vikubwa vya kijamii na vya lugha katika Afrika Kusini, pamoja na wawakilishi kutoka nchi nyingine 23. Ushirika mchangamfu miongoni mwa watu 77,830 waliohudhuria ulionekana wazi kwa urahisi. “Hii ni maridadi sana,” akasema mwanamke mmoja kijana Mhindi. “Kuona Machotara, Wahindi, weupe, na weusi wote wakichangamana pamoja kumebadili maoni yangu yote juu ya maisha.”
Hisia hii ya udugu huwa ni zaidi ya tabasamu, salamu za mkono, na kuitana “ndugu” na “dada.” Kikiwa kielelezo, mipango ilipokuwa ikifanywa kwa ajili ya “Habari Njema za Milele” Kusanyiko ulimwenguni pote katika 1963, Mashahidi wa Yehova walijulishwa kwamba ikiwa wangependa kusaidia wengine kifedha wahudhurie mkusanyiko mmoja, Sosaiti ingefurahia kuhakikisha kwamba fedha hizo zilinufaisha ndugu katika sehemu zote za dunia. Hakukuwa na kuombaomba, na hakuna kitu kilichochukuliwa kwa ajili ya gharama za usimamizi. Fedha zote zilitumiwa kwa kusudi lile lililotaarifiwa. Kwa njia hiyo, 8,179 walisaidiwa kuhudhuria mkusanyiko. Wajumbe kutoka kila nchi ya Amerika ya Kati na ya Kusini walipewa msaada, pamoja na maelfu kutoka Afrika na wengi katika Mashariki ya Kati na Mashariki ya Mbali. Kadiri kubwa ya wale waliosaidiwa walikuwa ndugu na dada waliokuwa wametumia miaka mingi katika huduma ya wakati wote.
Kuelekea mwisho wa 1978, mkusanyiko uliratibiwa kufanywa katika Auckland, New Zealand. Mashahidi katika Visiwa vya Cook walijua juu yao na walitamani kuwapo. Lakini uchumi katika visiwa hivyo ulikuwa katika hali ya kwamba ingalimgharimu kila mmoja kiasi kikubwa kufanya safari hiyo. Hata hivyo, ndugu na dada za kiroho wenye upendo katika New Zealand walichanga nauli za kwenda na kurudi za wanavisiwa kama 60. Walifurahi kama nini kuwapo ili kushiriki karamu ya kiroho pamoja na ndugu zao Wamaori, Wasamoa, Waniue, na Wakaukasi!
Kielelezo cha roho iliyo miongoni mwa Mashahidi wa Yehova ni jambo lililotukia kwenye umalizio wa “Haki ya Kimungu” Mkusanyiko wa Wilaya katika Montreal, Kanada, katika 1988. Kwa siku nne wajumbe Waarabu, Wafaransa, Wagiriki, Wahispania, Waingereza, Waitalia, na Wareno walikuwa wamekuwa wakifurahia programu ileile moja lakini katika lugha zao wenyewe. Hata hivyo, mwishoni mwa kipindi cha mwisho, wote 45,000 walijiunga pamoja katika Olympic Stadium katika wonyesho wenye kuvutia wa udugu na umoja wa kusudi. Pamoja waliimba, kila kikundi kwa lugha yacho chenyewe, “Imba nasi . . . ‘Atawala; E dunia.’”
[Maelezo ya Chini]
a Drama 70 zaidi kama hiyo zilionyeshwa kwenye mikusanyiko wakati wa miaka 25 iliyofuata.
b Kuanzia 1947 hadi 1987, yalikuwa yakifanywa mara mbili kwa mwaka. Kufikia 1972, yalikuwa makusanyiko ya siku tatu; kisha ile programu ya siku mbili ikaanzishwa.
[Blabu katika ukurasa wa 255]
“Nilivutiwa sana na roho ya upendo na fadhili za kidugu”
[Blabu katika ukurasa wa 256]
Magarimoshi ya mkusanyiko—wote wamo ndani!
[Blabu katika ukurasa wa 275]
Si wapangaji wa mkusanyiko wenye kulipwa mshahara mnono, bali wenye kujitolea wasiolipwa
[Blabu katika ukurasa wa 278]
Umoja kati ya weusi na weupe
[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 261]
Maazimio Saba ya Mkusanyiko Yenye Umaana
Katika 1922, azimio lenye kichwa “Mwito kwa Viongozi wa Ulimwengu” uliwataka wathibitishe kwamba wanadamu wana hekima ya kutawala dunia hii, la sivyo wakubali kwamba amani, uhai, uhuru, na furaha isiyo na mwisho vyaweza kuja tu kutoka kwa Yehova kupitia Yesu Kristo.
Katika 1923, kulikuwa “Onyo kwa Wakristo Wote” juu ya uhitaji wa haraka wa kukimbia matengenezo yanayodai kwa kusingizia kumwakilisha Mungu na Kristo.
Katika 1924, “Makasisi Washtakiwa” lilifunua wazi mafundisho na mazoea yasiyo ya Kimaandiko ya makasisi wa Jumuiya ya Wakristo.
Katika 1925, “Ujumbe wa Tumaini” lilionyesha kwa nini wale ambao hudai kuwa mianga yenye kuongoza ya ulimwengu wameshindwa kutosheleza uhitaji mkubwa zaidi wa mwanadamu na jinsi ni Ufalme wa Mungu tu uwezao kufanya hivyo.
Katika 1926, “Ushuhuda kwa Watawala wa Ulimwengu” liliwajulisha kwamba Yehova ndiye Mungu wa pekee wa kweli na kwamba sasa Yesu Kristo atawala akiwa Mfalme wa dunia anayestahili. Liliwahimiza watawala watumie uvutano wao wageuze akili za watu kuelekea Mungu wa kweli ili wasipatwe na msiba.
Katika 1927, “Azimio kwa Watu wa Jumuiya ya Wakristo” lilifunua wazi muungano wa kifedha, kisiasa, na kidini ambao hukandamiza wanadamu. Lilihimiza watu waiache Jumuiya ya Wakristo na kuweka tumaini lao katika Yehova na Ufalme wake ulio mikononi mwa Kristo.
Katika 1928, “Tangazo Dhidi ya Shetani na la Kusimama Upande wa Yehova” lilionyesha wazi kwamba Mfalme mtiwa-mafuta wa Yehova, Yesu Kristo, atamzuia Shetani karibuni na kuharibu tengenezo lake bovu, nalo lilihimiza wote wapendao uadilifu wachukue msimamo wao upande wa Yehova.
[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 272, 273]
Pande za Baadhi ya Mikusanyiko Mikubwa
Mamia ya wajumbe wenye idili waliwasili kwa meli, maelfu kwa ndege, makumi ya maelfu kwa magari na basi
Mpango mzuri wa kitengenezo ulihitajiwa na wafanyakazi wengi wenye moyo wa kupenda walitakwa ili kupata na kugawa mahali pa kulala pa kutosha
Wakati wa mikusanyiko hiyo ya siku nane, milo yenye moto—makumi ya maelfu yayo—walipakuliwa wajumbe kwa ukawaida
Katika 1953, jiji la trela na la mahema liliwapa makao wajumbe zaidi ya 45,000
New York City, katika 1958, watu 7,136 walibatizwa—wengi zaidi ya wakati mwingine wowote tangu Pentekoste ya 33 W.K.
Ishara zenye salamu kutoka nchi nyingi zilionyeshwa, na vipindi viliongozwa katika lugha 21, New York City katika 1953
[Picha katika ukurasa wa 256]
Wajumbe kwenye mkusanyiko wa IBSA katika Winnipeg, Manitoba, Kanada, katika 1917
[Picha katika ukurasa wa 258]
J. F. Rutherford akisema kwenye Cedar Point, Ohio, katika 1919. Aliwahimiza wote washiriki kwa bidii katika kutangaza Ufalme wa Mungu, kwa kutumia “The Golden Age”
[Picha katika ukurasa wa 259]
Mkusanyiko katika Cedar Point katika 1922. Mwito ulitolewa: “Tangazeni Mfalme na Ufalme”
[Picha katika ukurasa wa 260]
George Gangas alikuwapo Cedar Point katika 1922. Kwa miaka kama 70 tangu hapo amepiga mbiu ya Ufalme wa Mungu kwa bidii
[Picha katika ukurasa wa 262, 263]
Wajumbe kwenye mkusanyiko wa 1931 katika Columbus, Ohio, ambao kwa idili walikubali jina Mashahidi wa Yehova
[Picha katika ukurasa wa 264]
“New World Translation of the Christian Greek Scriptures” ikitolewa na N. H. Knorr katika 1950
[Picha katika ukurasa wa 264]
Hotuba zikitolewa na F. W. Franz juu ya utimizo wa unabii wa Biblia zilikuwa jambo kuu la mkusanyiko (New York, 1958)
[Picha katika ukurasa wa 265]
Kwa miaka mingi utumishi wa shambani ulikuwa sehemu kuu ya kila mkusanyiko.
Los Angeles, Marekani, 1939 (chini kabisa); Stockholm, Sweden, 1963 (picha ndogo)
[Picha katika ukurasa wa 266]
J. F. Rutherford aliposema kutoka Washington, D.C., katika 1935, ujumbe ulipelekwa kwa redio na nyuzi za simu kwenye mabara sita
[Picha katika ukurasa wa 268]
Katika Nuremberg, Ujerumani, mwaka 1946, Erich Frost alitoa hotuba motomoto “Wakristo Watahiniwa Vikali”
[Picha katika ukurasa wa 269]
Mkusanyiko wa mahali palipo wazi katika Kitwe, Rhodesia Kaskazini, wakati wa ziara ya N. H. Knorr katika 1952
[Picha katika ukurasa wa 270, 271]
Katika 1958 idadi ya wasikilizaji 253,922, walijaa pomoni na wakazidi stediamu mbili kubwa katika New York, walisikia ujumbe “Ufalme wa Mungu Watawala—Je, Mwisho wa Ulimwengu U Karibu?”
Polo Grounds
Yankee Stadium
[Picha katika ukurasa wa 274]
Grant Suiter, mwenyekiti wa mkusanyiko katika Yankee Stadium katika 1950
[Picha katika ukurasa wa 274]
John Groh, (aketiye), akizungumzia mipango ya mkusanyiko pamoja na George Couch katika 1958
[Picha katika ukurasa wa 277]
Katika 1963 mkusanyiko wa ulimwenguni pote ulifanywa, wajumbe kutoka nchi zipatao 20 wakisafiri nao duniani pote
Kyoto, Japani, (chini kushoto), lilikuwa moja la majiji 27 ya mkusanyiko. Wajumbe katika Jamhuri ya Korea walipata kujuana (katikati). Salamu ya Kimaori katika New Zealand (chini kulia)
[Picha katika ukurasa wa 279]
Mkusanyiko uliotumikia vikundi 17 vya lugha wakati uleule mmoja, katika jiji la mianzi lililojengwa kwa ajili ya pindi hiyo (Lagos, Nigeria, 1970)
[Picha katika ukurasa wa 280]
Mikusanyiko mikubwa mitatu ilifanywa Poland katika 1989, wajumbe wakiwepo kutoka nchi 37
T. Jaracz (kulia) alihutubia wajumbe katika Poznan
Maelfu walibatizwa katika Chorzów
Wasikilizaji walipiga makofi kwa muda mrefu sana katika Warsaw
Wajumbe kutoka iliyokuwa wakati huo U.S.S.R. (chini)
Visehemu vya programu katika Chorzów vilitafsiriwa katika lugha 15
-
-
“Kutafuta Kwanza Ufalme”Mashahidi wa Yehova—Wapiga-Mbiu wa Ufalme wa Mungu
-
-
Sura ya 18
“Kutafuta Kwanza Ufalme”
KICHWA kikuu cha Biblia ni kutakaswa kwa jina la Yehova kupitia Ufalme. Yesu Kristo aliwafunza wafuasi wake kutafuta kwanza Ufalme, wakiutanguliza badala ya faida nyinginezo za maisha. Kwa nini?
Mara nyingi Mnara wa Mlinzi limeeleza kwamba kwa sababu ya jambo la kwamba yeye ndiye Muumba, Yehova ndiye Mwenye Enzi Kuu ya Ulimwengu Wote Mzima. Yeye ana haki ya kustahiwa kabisa na viumbe vyake. (Ufu. 4:11) Hata hivyo, mapema sana katika historia ya kibinadamu, mwana wa kiroho wa Mungu aliyejifanya Shetani Ibilisi alipinga kwa ukaidi enzi kuu ya Yehova. (Mwa. 3:1-5) Zaidi ya hivyo, Shetani alisingizia kwamba wote waliomtumikia Yehova walifanya hivyo kwa makusudi ya kibinafsi. (Ayu. 1:9-11; 2:4, 5; Ufu. 12:10) Hivyo amani ya ulimwengu wote mzima iliharibiwa.
Kwa muda wa miongo sasa, vichapo vya Watch Tower vimefafanua kwamba Yehova amefanya uandalizi wa kusuluhisha masuala hayo kwa njia inayokuza, si nguvu yake ya uweza yote tu, bali pia ukuu wa hekima yake, haki yake, na upendo wake. Sehemu kuu ya uandalizi huo ni Ufalme wa Mungu wa Kimesiya. Kupitia Ufalme huo, wanadamu wamepewa fursa nyingi kujifunza njia za uadilifu. Kupitia Ufalme huo, waovu wataangamizwa, enzi kuu ya Yehova itatetewa, na kusudi lake litatimizwa la kufanya dunia kuwa paradiso iliyojaa watu wanaopenda Mungu na wenzao kikweli na ambao wanabarikiwa kwa ukamilifu wa uhai.
Kwa sababu ya umaana wao, Yesu alishauri wafuasi wake hivi: “Fulizeni kutafuta kwanza ufalme.” (Mt. 6:10, 33, NW) Mashahidi wa Yehova katika nyakati za kisasa wametoa uthibitisho mwingi kwamba wanajitahidi kufuata shauri hilo.
Kuacha Yote kwa Ajili ya Ufalme
Katika tarehe ya mapema, Wanafunzi wa Biblia walifikiria kile kilichomaanishwa na kutafuta kwanza Ufalme. Walizungumzia kielezi cha Yesu ambacho alilinganisha Ufalme na lulu ya thamani kubwa sana hivi kwamba mtu mmoja ‘aliuza vyote alivyo navyo, akainunua.’ (Mt. 13:45, 46) Walitafakari juu ya umaana wa shauri la Yesu kwa mtawala kijana aliyekuwa tajiri auze kila kitu, agawanye kwa maskini, na kumfuata. (Mk. 10:17-30)a Waling’amua kwamba ikiwa wangestahili kuwa na sehemu katika Ufalme wa Mungu, ni lazima watangulize masilahi ya Ufalme, wakitumia maisha zao, uwezo wao, na mali zao, kwa furaha katika utumishi wao. Vitu vinginevyo vyote maishani vingechukua mahali pa pili.
Charles Taze Russell alitumia binafsi shauri hilo. Aliuza biashara yake ya kuuza nguo za wanaume, akapunguza hatua kwa hatua faida nyinginezo za kibiashara, kisha akatumia mali yake yote ya kidunia kusaidia watu katika njia ya kiroho. (Linganisha Mathayo 6:19-21.) Hilo si jambo alilofanya kwa miaka michache tu. Kufikia kifo chake, alitumia uwezo wake wote—uwezo wake wa kiakili, afya yake ya kimwili, mali zake za kimwili—kuwafunza wengine ujumbe wa maana wa Ufalme wa Mesiya. Kwenye maziko ya Russell, mshirika mmoja, Joseph F. Rutherford, alisema: “Charles Taze Russell alikuwa mwaminifu-mshikamanifu kwa Mungu, mwaminifu-mshikamanifu kwa Kristo Yesu, na mwaminifu-mshikamanifu kwa kusudi la Ufalme wa Mesiya.”
Katika Aprili 1881 (wakati ambapo mamia machache ya watu walipokuwa wakihudhuria mikutano ya Wanafunzi wa Biblia), Watch Tower lilitangaza makala yenye kichwa “Wahubiri 1,000 Watakwa.” Hiyo ilitia ndani mwaliko kwa wanaume na wanawake ambao hawakuwa na familia zenye kuwategemea waanze kazi wakiwa makolpota waeneza-evanjeli. Kwa kutumia maneno ya kielezi cha Yesu kwenye Mathayo 20:1-16, Watch Tower liliuliza: “Ni nani aliye na tamaa inayowaka ya kwenda kufanya kazi ngumu katika Shamba la Mizabibu, na ambaye amekuwa akisali kwamba Bwana atafungua njia”? Wale ambao wangeweza kutoa angalau nusu ya wakati wao kwa ajili ya kazi ya Bwana kihususa walitiwa moyo watoe maombi. Ili kuwasaidia na gharama za usafiri, chakula, mavazi, na makao, Zion’s Watch Tower Tract Society iliwapa makolpota hao wa mapema fasihi za Biblia ili wazigawanye, ikataarifu mchango wa kiasi ambao ungeweza kuombwa kwa ajili ya fasihi, na kuwaalika makolpota watumie sehemu ya fedha zilizopokewa. Ni nani waliokubali mipango hiyo na kuchukua utumishi wa kolpota?
Kufikia 1885 kulikuwa na makolpota 300 hivi walioshirikiana na Sosaiti. Hatimaye katika 1914 idadi hiyo ilipita 1,000. Haikuwa kazi rahisi. Baada ya kuzuru nyumba nyingi katika miji minne midogo na kupata watu watatu au wanne tu waliopendezwa kwa kiasi fulani, mmoja wa makolpota aliandika: “Ni lazima niseme kwamba nilihisi upweke kidogo kusafiri mbali hivyo, kukutana na wengi sana, na kupata upendezi mdogo sana ulioonyeshwa juu ya mpango wa Mungu na Kanisa. Nisaidieni kwa sala zenu, ili niweze kutoa kweli kwa njia ifaayo na kwa ujasiri, na nisichoke katika kutenda mema.”
Walijitoa Wenyewe kwa Hiari
Makolpota hao walikuwa watanguliza-njia kwelikweli. Waliingia hadi kwenye sehemu za nchi zisizoweza kufikika katika wakati ambapo usafiri ulikuwa wa nyuma sana na sehemu kubwa ya barabara ilikuwa vijia tu vya mikokoteni. Dada Early, katika New Zealand, ni mmoja wa wale waliofanya hivyo. Akianza mapema kabla ya Vita ya Ulimwengu 1, alitumia miaka 34 katika utumishi huo wa wakati wote kabla hajafa katika 1943. Alienda sehemu nyingi za nchi hiyo kwa baiskeli. Hata alipolemaa kwa ugonjwa wa yabisi kavu na hivyo hangeweza kuiendesha, alitumia baiskeli ili aiegemee na kubebea vitabu vyake katika eneo la kibiashara la Christchurch. Yeye angeweza kupanda ngazi, lakini alilazimika kuzishuka kwa kwenda kinyumenyume kwa sababu ya udhaifu wake wenye kulemaza. Hata hivyo maadamu alikuwa na nguvu kidogo, aliitumia katika utumishi wa Yehova.
Watu hao hawakufanya kazi hiyo kwa sababu walijitumainia. Wengine walikuwa wenye woga sana kiasili, lakini walimpenda Yehova. Kabla ya kutoa ushahidi katika eneo la kibiashara, dada mmoja wa namna hiyo aliomba kila Mwanafunzi wa Biblia katika eneo lake asali kwa ajili yake. Baada ya muda, alipata ujuzi, akawa mwenye idili sana katika utendaji huo.
Malinda Keefer alipozungumza na Ndugu Russell katika 1907 kuhusu tamaa yake ya kuanza utumishi wa wakati wote, alisema kwamba alihisi uhitaji wa kupata ujuzi zaidi kwanza. Kwa kweli, ni mwaka mmoja tu uliokuwa umepita alipoona fasihi za Wanafunzi wa Biblia kwa mara ya kwanza. Jibu la Ndugu Russell lilikuwa: “Ikiwa unataka ungoje hadi utakapoyajua yote hutaanza kamwe, bali utajifunza unapoendelea kuifanya.” Bila kusita, yeye alianza upesi katika Ohio, Marekani. Mara nyingi alikumbuka Zaburi 110:3, inayosema: “Watu wako wanajitoa kwa hiari.” Kwa miaka 76 iliyofuata, aliendelea kufanya ivyo hivyo.b Alianza utumishi huo akiwa mseja. Kwa miaka 15 alifurahia kutumikia akiwa ameolewa. Lakini baada ya mume wake kufa, aliendelea tu, kwa msaada wa Yehova. Akikumbuka muda wa miaka iliyopita, yeye alisema: “Nina shukrani kama nini kwamba nilijitoa kwa hiari kuwa painia nilipokuwa mwanamke mchanga na nikatanguliza masilahi ya Ufalme nyakati zote!”
Mikusanyiko ya ujumla ilipofanywa katika siku za mapema, mara nyingi mipango ilifanywa kwa ajili ya vipindi vya pekee pamoja na makolpota. Maswali yalijibiwa, mazoezi yaliandaliwa kwa ajili ya wapya, na kitia-moyo kilitolewa.
Kuanzia 1919 kuendelea, kulikuwa na watumishi wengi zaidi wa Yehova waliothamini Ufalme wa Mungu sana hivi kwamba wao pia walitegemeza maisha zao kikweli juu ya Ufalme. Wengine wao waliweza kuacha kufuatia miradi ya kilimwengu na kujitoa wenyewe kikamili katika huduma.
Kushughulikia Mahitaji ya Kimwili
Walishughulikiaje mahitaji yao ya kimwili? Anna Petersen (baadaye Rømer), mweneza-evanjeli wa wakati wote katika Denmark, akumbuka: “Tulipata msaada kutoka kwa fasihi tulizoangusha ili kulipia gharama za kila siku, na mahitaji yetu hayakuwa makubwa. Kulipokuwa na gharama kubwa zaidi, hizo zililipiwa kwa njia moja au nyingine. Dada walikuwa wakitupatia nguo, marinda au makoti, na tungeyavaa mara hiyo, na hivyo tulivalia vizuri. Na katika nyakati fulani za baridi kali, nilifanya kazi ya ofisi kwa miezi kadhaa. . . . Kwa kununua mavazi wakati bei zilipokuwa chini, ningeweza kununua nguo nilizohitaji za mwaka mzima. Mambo yalienda sawa. Hatukuwa kamwe na uhitaji.” Vitu vya kimwili havikuwa hangaiko lao kuu. Upendo wao kwa Yehova na njia zake ulikuwa kama moto uwakao ndani yao, na ilikuwa lazima wauonyeshe tu.
Ili kupata malazi, wangekodi chumba kidogo huku wakihubiria watu katika eneo hilo. Wengine wao walitumia trela—kitu sahili, mahali tu pa kulala na kulia. Wengine walilala katika mahema na kuhamahama. Mahali pengine, ndugu walipanga kuwa na “kambi za mapainia.” Huenda Mashahidi katika eneo hilo wakaandaa makao, na mtu mmoja angegawiwa kuyasimamia. Mapainia waliotumikia katika eneo hilo wangeweza kutumia makao hayo, na wangeshiriki kulipa gharama zilizohusika.
Wafanyakazi hao wa wakati wote hawakuruhusu ukosefu wa pesa uwazuie watu wenye mfano wa kondoo kupata fasihi za Biblia. Mara nyingi mapainia walibadilishana fasihi kwa mazao kama viazi, siagi, mayai, matunda yaliyotoka kuchumwa au ya mkebe, kuku, sabuni na karibu kitu kingine chochote. Hawakuwa wanakuwa matajiri; badala yake, hiyo ilikuwa njia ya kuwasaidia watu wanyoofu wapate ujumbe wa Ufalme, hali wakati uleule wakipata mahitaji ya kimwili yaliyo ya lazima kwa maisha ili mapainia waweze kuendelea na huduma yao. Walikuwa na uhakika katika ahadi ya Yesu kwamba ikiwa ‘wangetafuta kwanza Ufalme na uadilifu wa Mungu,’ basi chakula na mavazi yanayohitajiwa yangeandaliwa.—Mt. 6:33, NW.
Wenye Nia Kutumika Kokote Kulikokuwa na Uhitaji
Tamaa yao ya moyoni ya kufanya kazi ambayo Yesu alikuwa amewagawia wanafunzi wake iliwaongoza wafanyakazi hao wa wakati wote kwenye maeneo mapya, hata kwa nchi mpya. Frank Rice alipoalikwa aondoke Australia ili akafungue kazi ya kuhubiri habari njema katika Java (sasa ni sehemu ya Indonesia) katika 1931, alikuwa amepata ujuzi wa miaka kumi katika huduma ya wakati wote. Lakini sasa kulikuwa na desturi mpya, kutia na lugha mpya za kujifunza. Angeweza kutumia Kiingereza kutoa ushahidi kwa wengine madukani au maofisini, lakini alitaka kutolea wengine ushahidi pia. Yeye alijifunza kwa bidii, na katika miezi mitatu alijua Kiholanzi cha kutosha kuanza kwenda nyumba hadi nyumba. Kisha akajifunza Kimaleya.
Frank alikuwa na miaka 26 tu alipoenda Java, na kwa sehemu kubwa ya miaka sita aliyokuwa huko na Sumatra, alifanya kazi akiwa peke yake. (Kuelekea mwisho wa 1931, Clem Deschamp na Bill Hunter walikuja kutoka Australia ili kusaidia kazi. Wakiwa kikundi, walifanya ziara ya kuhubiri kuelekea bara, huku Frank akifanya kazi katika jiji kuu la Java. Baadaye, Clem na Bill pia walipokea migawo iliyowapeleka sehemu nyinginezo.) Hakukuwa na mikutano ya kutaniko ambayo Frank angeweza kuhudhuria. Nyakati nyingine alikuwa mpweke sana, na mara kadhaa alishindana na mawazo ya kuacha na kurudi Australia. Lakini aliendelea tu. Jinsi gani? Chakula cha kiroho kilichomo katika The Watch Tower kilimtia nguvu. Katika 1937 alienda kwenye mgawo katika Indochina, ambapo alinusurika kufa wakati wa misukosuko ya jeuri iliyofuata Vita ya Ulimwengu 2. Roho hiyo ya kutaka kutumikia ilikuwa ingali hai katika miaka ya 1970 alipoandika ili kuonyesha shangwe yake kwa sababu familia yake yote ilikuwa ikimtumikia Yehova na kusema kwamba yeye na mke wake walikuwa wakijitayarisha tena kuhamia sehemu fulani katika Australia kulikokuwa na uhitaji mkubwa zaidi.
‘Kumtumaini Yehova kwa Moyo Wao Wote’
Claude Goodman aliazimia ‘kumtumaini Yehova kwa moyo wake wote bila kutegemea akili zake mwenyewe,’ kwa hiyo alichagua utumishi wa kolpota akiwa mweneza-evanjeli Mkristo badala ya fursa ya kufuatia biashara ya kilimwengu. (Mit. 3:5, 6) Akiwa pamoja na Ronald Tippin, aliyekuwa amemsaidia kujifunza kweli, alitumikia akiwa kolpota katika Uingereza kwa zaidi ya mwaka mmoja. Kisha, katika 1929, hao wawili walijitoa ili waende India.c Hilo lilitokeza ugumu kama nini!
Katika miaka iliyofuata, hawakusafiri tu kwa miguu na kwa garimoshi la abiria, na kwa basi bali pia kwa garimoshi la mizigo, gari la kukokotwa na ng’ombe, ngamia, mashua ndogo, riksho, na hata ndege na garimoshi la kukodiwa. Nyakati nyingine walitandika matandiko yao katika vyumba vya kungoja garimoshi, katika zizi la ng’ombe, kwenye nyasi ya msituni, au juu ya sakafu ya samadi ya ng’ombe katika nyumba ndogo, lakini pia kulikuwa na nyakati walipolala katika mahoteli ya starehe na katika jumba la mfalme. Kama vile mtume Paulo, walijifunza siri ya kuridhika iwe walikuwa na vitu vichache ama vitu vingi. (Flp. 4:12, 13) Mara nyingi walikuwa na vitu vichache sana vya thamani, lakini wakati wote walikuwa na vitu walivyohitaji kwelikweli. Wao binafsi waliona utimizo wa ahadi ya Yesu kwamba ikiwa wangetafuta kwanza Ufalme na uadilifu wa Mungu, vitu vya lazima vya maisha vingeandaliwa.
Kulikuwa na maambukizo mabaya ya homa ya kidingapopo, malaria, na homa ya matumbo, lakini utunzi wenye upendo uliandaliwa na Mashahidi wenzi. Kulikuwa na utumishi wa kufanywa miongoni mwa majiji yenye nyumba mbovumbovu kama vile Calcutta, na kulikuwa ushahidi wa kutolewa katika mashamba ya chai katika milima ya Ceylon (sasa yajulikana kuwa Sri Lanka). Ili kujazia mahitaji ya kiroho ya watu, fasihi zilitolewa, rekodi zilichezwa katika lugha za wenyeji, na hotuba zilitolewa. Kadiri kazi ilivyoongezeka, Claude alijifunza pia jinsi ya kuendesha matbaa ya uchapaji na kushughulikia kazi katika ofisi za tawi za Sosaiti.
Katika mwaka wake wa 87, yeye angeweza kutazama nyuma kwenye maisha yaliyojaa maono katika utumishi wa Yehova katika Uingereza, India, Pakistan, Ceylon, Burma (sasa ni Myanmar), Maleya, Thailand, na Australia. Akiwa kijana mseja na mume na baba pia, alitanguliza Ufalme maishani mwake. Haikupita miaka miwili baada ya ubatizo wake ndipo akaingia katika utumishi wa wakati wote, naye aliona huo kuwa kazi-maisha yake kwa maisha yake yote.
Uwezo wa Mungu Wafanywa Kuwa Kamili Katika Udhaifu
Ben Brickell alikuwa mwingine wa wale Mashahidi wenye bidii—aliyekuwa kama watu wengine, kwa vile alikuwa na mahitaji na udhaifu kama wao. Yeye alikuwa mwenye kutokeza katika imani. Katika 1930 alianza kazi ya kolpota katika New Zealand, ambako alitoa ushahidi katika maeneo ambayo hayakuenezwa tena kwa miongo mingi ya miaka. Miaka miwili baadaye, katika Australia, alianza safari ya miezi mitano ili kuhubiri akipitia nchi ya jangwa ambako hakukuwa na ushahidi uliokuwa umepata kutolewa. Alipakia baiskeli yake mzigo mkubwa wa mablanketi, nguo, chakula, na vitabu vilivyojalidiwa vya kuangusha. Ingawa watu wengine walikuwa wameangamia walipojaribu kusafiri kupitia eneo hilo, yeye alijikakamua, akiwa na tumaini katika Yehova. Kisha, akatumikia katika Malasia, ambako alipata matatizo mabaya ya moyo. Yeye hakuacha. Baada ya kupata nafuu, aliendelea na utendaji wa kuhubiri wakati wote katika Australia. Karibu mwongo mmoja hivi baadaye, ugonjwa mbaya ulimfanya alazwe hospitalini, na alipotoka humo aliambiwa na daktari kwamba “hangeweza kufanya kazi kwa asilimia 85.” Yeye hata hangeweza kutembea kwenda dukani bila kupumzikapumzika njiani.
Lakini Ben Brickell aliazimia kuendelea tena, na alifanya hivyo, akitua ili kupumzika kama ilivyohitajika. Upesi akawa anatoa ushahidi katika sehemu za mbali za Australia. Alifanya yote aliyoweza kutunza afya yake, lakini utumishi wake kwa Yehova ndio uliokuwa jambo kuu maishani mwake hadi kifo chake miaka 30 baadaye akiwa na umri wa kama miaka 65.d Yeye alitambua kwamba upungufu uliokuwako kwa sababu ya udhaifu wake ungejazwa na uwezo wa Yehova. Kwenye mkusanyiko katika Melbourne katika 1969, alitumikia kwenye dawati ya painia akiwa na beji kubwa kwenye shavu la koti lake, ikisema: “Ikiwa unataka kujua kuhusu upainia, niulize.”—Linganisha 2 Wakorintho 12:7-10.
Kufikia Vijiji vya Msituni na Kambi za Migodi za Milimani
Bidii katika utumishi wa Yehova ilisukuma si wanaume tu bali pia wanawake kuanza kazi katika mashamba yasiyofikiwa. Freida Johnson alikuwa mmoja wa watiwa-mafuta, mwenye umbo dogo na mwenye umri wa miaka 50 na kitu alipofanya kazi peke yake katika sehemu za Amerika ya Kati, akieneza sehemu kama vile pwani ya kaskazini ya Honduras kwa farasi. Kulitaka imani ili afanye kazi peke yake katika sehemu hiyo, kutembelea mashamba ya ndizi yaliyotapakaa, miji ya La Ceiba, Tela, na Trujillo, na hata vijiji vilivyo peke yavyo vya Carib. Alitoa ushahidi huko katika 1930 na 1931, tena katika 1934, na katika 1940 na 1941, akaangusha maelfu ya fasihi zenye kweli ya Biblia.
Wakati wa miaka hiyo, mfanyakazi mwingine mwenye bidii alianza kazi-maisha yake katika huduma ya wakati wote. Huyo alikuwa Kathe Palm, aliyezaliwa katika Ujerumani. Kilichomsukuma achukue hatua ilikuwa kuhudhuria mkusanyiko katika Columbus, Ohio, katika 1931, ambako Wanafunzi wa Biblia walikubali jina Mashahidi wa Yehova. Ulikuwa wakati huo alipoazimia kutafuta sana kwanza Ufalme, na katika 1992, akiwa mwenye umri wa miaka 89, alikuwa angali akifanya hivyo.
Utumishi wake wa painia ulianza katika New York City. Baadaye katika South Dakota, alikuwa na mwenzi kwa miezi michache kisha akaendelea peke yake, akisafiri kwa kupanda farasi. Alipoalikwa atumikie katika Kolombia, Amerika Kusini, alikubali mara hiyo, akafika huko mwishoni mwa 1934. Kwa mara nyingine tena, alikuwa na mwenzi kwa muda fulani kisha akawa peke yake. Hilo halikumfanya ahisi kwamba ni lazima aache.
Alialikwa na mume na mke mmoja ajiunge nao katika Chile. Huko kulikuwa na eneo jingine kubwa, lililotanuka kilometa 4,265 katika pwani ya magharibi ya bara la Amerika ya Kusini. Baada ya kuhubiri katika ofisi za jiji kuu, alienda kwenye sehemu ya mbali ya kaskazini. Alitoa ushahidi mlango kwa mlango katika kila kambi ya migodi, katika miji ya kampuni, iwe mikubwa au midogo. Wafanyakazi waliokuwa juu ya mlima Andes walishangaa kumwona mwanamke aliye peke yake akiwatembelea, lakini yeye aliazimia asimkose mtu hata mmoja katika eneo hilo alilogawiwa. Baadaye, alihamia kusini, mahali ambapo estancias (malisho ya kondoo) kadhaa yalienea kufikia hektari kama 100,000. Watu huko walikuwa wenye urafiki na wakaribishaji-wageni na walimkaribisha kwenye meza yao wakati wa kula. Kwa njia hiyo na nyinginezo, Yehova alimtunza, hivi kwamba alikuwa na vitu vya kimwili vilivyo vya lazima kwa maisha.
Kuhubiri habari njema za Ufalme wa Mungu kumejaa maisha yake.e Alipotazama nyuma kwenye miaka yake ya utumishi, yeye alisema: “Ninahisi kwamba nimekuwa na maisha bora sana. Kila mwaka ninapohudhuria kusanyiko la watu wa Yehova, ninapata hisi changamfu ya uradhi ninapoona watu wengi ambao nimejifunza nao Biblia wakitangaza habari njema, wakisaidia wengine waje kwenye maji ya uhai.” Amekuwa na shangwe ya kuona idadi ya wasifaji wa Yehova katika Chile ikikua kutoka 50 hivi hadi zaidi ya 44,000.
“Mimi Hapa, Nitume Mimi”
Baada ya kusikia mhadhara uliotegemea mwaliko wa Yehova kwenye utumishi kama ulivyorekodiwa kwenye Isaya 6:8 na itikio lenye maoni mazuri la nabii, “Mimi hapa, nitume mimi,” Martin Poetzinger, katika Ujerumani, alibatizwa. Miaka miwili baadaye, katika 1930, aliingia katika huduma ya wakati wote katika Bavaria.f Kabla ya muda mrefu kupita, maofisa huko walizuia kuhubiri kwa Mashahidi, mahali pa kukutania pakafungwa, na fasihi zikachukuliwa. Gestapo walikuwa ni tisho. Lakini matukio hayo katika 1933 hayakukomesha huduma ya Ndugu Poetzinger.
Alialikwa atumikie katika Bulgaria. Kadi za ushuhuda katika Kibulgaria zilitumiwa kutoa utangulizi kwa fasihi za Biblia. Lakini watu wengi hawakujua kusoma na kuandika. Kwa hiyo, Ndugu Poetzinger alianza kujifunza lugha yao, iliyotumia alfabeti ya Kisirili. Familia ilipoangushiwa fasihi, mara nyingi ilikuwa lazima wazazi wasomewe na watoto wao.
Kwa sehemu kubwa ya mwaka wa kwanza, Ndugu Poetzinger alikuwa peke yake, naye aliandika: “Kwenye Ukumbusho, nilitoa hotuba mimi mwenyewe, nikasali mwenyewe, na kufunga mkutano nikiwa peke yangu.” Wakati wa 1934, wageni walifukuzwa, kwa hiyo alienda Hungaria. Huko alilazimika kujifunza lugha nyingine mpya ili aweze kutoa habari njema. Kutoka Hungaria alienda kwenye nchi zilizoitwa wakati huo Chekoslovakia na Yugoslavia.
Alipata maono mengi yenye kufurahisha—kupata wapendao kweli alipoenda sehemu za mashambani na vijijini, na fasihi zikiwa zimepakiwa juu ya mgongo wake; kuona utunzaji wa Yehova wakati wakaribishaji-wageni walipompa chakula na hata malazi ya usiku huo; kuzungumza hadi jioni sana na wale waliokuja mahali alipolala ili wasikie zaidi kuhusu ujumbe wa Ufalme wenye kufariji.
Kulikuwa pia na majaribu makubwa ya imani. Alipokuwa akitumikia nje ya nchi alikozaliwa, na bila fedha, alipatwa na ugonjwa mbaya. Hakuna daktari aliyetaka kumwona. Lakini Yehova aliandaa. Jinsi gani? Hatimaye, mshauri wa cheo cha juu wa hospitali ya mahali hapo alifikiwa. Mtu huyo, aliyeamini sana Biblia, alimtunza Ndugu Poetzinger kama vile ambavyo angefanya kwa mwanae, akifanya hivyo bila malipo. Daktari huyo alivutiwa na roho ya kujidhabihu ya kijana huyo, iliyodhihirika katika kazi ambayo alikuwa akifanya, na alikubali vitabu kadhaa vya Sosaiti kuwa zawadi.
Jaribu jingine kubwa lilikuja miezi minne baada ya kufunga ndoa. Ndugu Poetzinger alikamatwa Desemba 1936 na kufungiwa kwanza katika kambi moja ya mateso kisha katika nyingine, huku mke wake akifungiwa katika kambi nyingine kama hizo. Hawakuonana kwa miaka tisa. Yehova hakuzuia mnyanyaso huo wenye ukatili, lakini alimtia nguvu Martin, na mke wake Gertrud, na maelfu ya wengineo ili wauvumilie.
Baada ya yeye na mke wake kuachiliwa, Ndugu Poetzinger alionea shangwe miaka mingi ya utumishi akiwa mwangalizi asafiriye katika Ujerumani. Alikuwako kwenye mikusanyiko yenye kusisimua iliyofanywa baada ya vita katika viwanja vya Nuremberg vilivyokuwa vya gwaride ya Hitler hapo awali. Lakini sasa viwanja hivyo vilijawa umati mkubwa wa wategemezaji wa Ufalme wa Mungu walio waaminifu-washikamanifu. Alihudhuria mikusanyiko isiyoweza kusahaulika katika Yankee Stadium katika New York. Alionea shangwe kikamili mazoezi yake kwenye Shule ya Biblia ya Gileadi ya Watchtower. Na katika 1977 akawa mshiriki wa Baraza Linaloongoza la Mashahidi wa Yehova. Mtazamo wake, hadi alipomaliza mwendo wake wa kidunia katika 1988, waweza kuelezwa vema zaidi kwa maneno: ‘Jambo hili moja nilifanyalo—kutafuta kwanza Ufalme.’
Kujifunza Yale Yanayomaanishwa Hasa
Kwa wazi roho ya kujidhabihu si jambo jipya miongoni mwa Mashahidi wa Yehova. Buku la kwanza kabisa la Millennial Dawn lilipotangazwa huko nyuma katika 1886, jambo la kujitakasa (au, kama vile tungesema leo, kujiweka wakfu) lilizungumzwa kwa uwazi. Ilionyeshwa kwa msingi wa Maandiko kwamba Wakristo wa kweli “hutakasa” kila kitu kwa Mungu; hiyo hutia ndani uwezo wao, mali zao za kimwili, maisha zao. Ni lazima Wakristo wawe watumishi wa yale “yaliyotakaswa” kwa Mungu, na wakiwa watumishi, ni lazima watoe hesabu—si kwa wanadamu bali kwa Mungu.
Idadi iliyozidi kukua ya Wanafunzi wa Biblia ilijitoa yenyewe kwelikweli katika utumishi wa Mungu. Walitumia kikamili uwezo wao, mali zao, nishati muhimu zao katika kufanya mapenzi yake. Kwa upande ule mwingine, kuna wale waliohisi kwamba kile kilichokuwa cha maana zaidi ni kusitawisha ile iliyoitwa tabia ya Kikristo ili wastahili kushiriki katika Ufalme pamoja na Kristo.
Ingawa daraka la kila Mkristo wa kweli la kutoa ushahidi kwa wengine kuhusu Ufalme wa Mungu lilikuwa limesemwa mara nyingi na Ndugu Russell, hilo lilikaziwa hata zaidi baada ya Vita ya Ulimwengu 1. Kielelezo chenye kutokeza ni makala “Tabia au Agano—Jipi Kati ya Hayo?” katika The Watch Tower la Mei 1, 1926. Lilizungumzia kwa uwazi matokeo mabaya ya kile kilichoitwa usitawishaji tabia kisha likakazia umaana wa mtu kutimiza madaraka yake kwa Mungu kwa njia ya vitendo.
Mapema zaidi, The Watch Tower la Julai 1, 1920, lilikuwa limechunguza unabii mkubwa wa Yesu kuhusu ‘ishara ya kuwapo kwake na ya mwisho wa ulimwengu.’ (Mt. 24:3, KJ) Lilikazia fikira kazi ya kuhubiri ambayo lazima ifanywe kwa utimizo wa Mathayo 24:14 na likatambulisha ujumbe utakaotangazwa, likisema: “Habari njema hapa zinahusu mwisho wa utaratibu wa mambo wa kale na kusimamishwa kwa ufalme wa Mesiya.” The Watch Tower lilieleza kwamba kwa msingi wa mahali Yesu aliposema hayo kuhusiana na sehemu nyinginezo za ile ishara, kazi hii ingetimizwa “kati ya wakati wa vita ile kuu ya ulimwengu [Vita ya Ulimwengu 1] na wakati wa ‘dhiki kubwa’ iliyotajwa na Bwana-Mkubwa katika Mathayo 24:21, 22.” Hiyo kazi ilikuwa ya haraka. Ni nani angeifanya?
Kwa wazi daraka hilo lilikuwa juu ya washiriki wa “kanisa,” kutaniko la kweli la Kikristo. Hata hivyo, katika 1932, kupitia toleo la Agosti 1 la Mnara wa Mlinzi (Kiingereza), hao walishauriwa watie moyo “jamii ya Kiyehonadabu” kushiriki nao katika kazi, kwa kupatana na roho ya Ufunuo 22:17. Jamii ya Kiyehonadabu—ambayo tumaini layo ni uhai wa milele katika dunia-Paradiso—iliitikia, na wengi wao walifanya hivyo kwa bidii.
Umaana mkubwa wa kazi hii umekaziwa sana: “Ni jambo la maana kushiriki katika utumishi wa Bwana kama vile ilivyo kuhudhuria mkutano,” likasema The Watch Tower katika 1921. “Kila mmoja lazima awe mhubiri wa gospeli,” likaonyesha katika 1922. “Yehova amefanya kuhubiri kuwe kazi ya maana sana awezayo yeyote kati yetu kufanya katika ulimwengu huu,” likasema katika 1949. Julisho rasmi la mtume Paulo kwenye 1 Wakorintho 9:16 (NW), limenukuliwa mara nyingi: “Nimewekewa sharti. Kwa kweli, ole wangu mimi ikiwa sikutangaza habari njema!” Andiko hilo limetumiwa kuhusu kila mmoja wa Mashahidi wa Yehova.
Ni Wangapi Wanaohubiri? Kwa Kadiri Gani? Kwa Nini?
Je, kuna wowote waliokuwa wakilazimishwa kushiriki katika kazi hii kinyume cha mapenzi yao? “La,” The Watch Tower likajibu, katika toleo lalo la Agosti 1, 1919, “hakuna yeyote anayeshurutishwa kufanya chochote. Wote ni utumishi wa kujitolea, unaofanywa kwa kumpenda Bwana na kusudi lake la uadilifu. Yehova haandikishi kamwe yeyote kwa nguvu.” Kuhusu kusudi la utumishi huo, The Watch Tower la Septemba 1, 1922, lilisema zaidi hivi: “Mtu ambaye kwa kweli ana shukrani moyoni mwake na anathamini yale ambayo Mungu amemfanyia atataka kufanya jambo fulani kwa upande wake; na kadiri ambavyo uthamini wake kwa fadhili za Mungu uongezekavyo, ndivyo upendo wake utakavyokuwa mkubwa; na kadiri upendo wake ulivyo mkubwa, ndivyo tamaa ya kumtumikia itakavyokuwa kubwa zaidi.” Ilielezwa kwamba kupenda Mungu huonyeshwa kwa kushika amri zake, na mojapo amri hizo ni kuhubiri habari njema za Ufalme wa Mungu.—Isa. 61:1, 2; 1 Yoh. 5:3.
Wale ambao wanafanya utendaji huu hawakuvutwa na wazo lolote la kilimwengu la kujitakia makuu. Wameambiwa kinaganaga kwamba wanapoenda nyumba hadi nyumba au kutoa fasihi barabarani, wataonwa kuwa ‘wapumbavu, dhaifu, wa hali ya chini,’ kwamba ‘watadharauliwa, wataudhiwa,’ na kwamba wataonwa kuwa ‘wasiofaa kitu katika maoni ya kilimwengu.’ Lakini wanajua kwamba Yesu na wanafunzi wake wa zamani walitendwa kwa njia iyo hiyo.—Yn. 15:18-20; 1 Kor. 1:18-31.
Je, Mashahidi wa Yehova hufikiri kwamba kwa njia fulani wanastahili wokovu kwa utendaji wao wa kuhubiri? La hasha! Kitabu Wenye Umoja Katika Ibada ya Mungu wa Pekee wa Kweli, ambacho kimetumiwa tangu 1983 kusaidia wanafunzi kuendelea kufikia ukomavu wa Kikristo, kinazungumzia jambo hilo. Kinasema: “Vilevile dhabihu ya Yesu imetufungulia nafasi ya kupata uzima wa milele . . . Hiyo si thawabu tunayojipatia kwa ustahili wa kufanya kazi. Hata tufanye mengi namna gani katika utumishi wa Yehova, hatuwezi kamwe kujifanyia ustahili huo hata Mungu awe na deni kwetu la kutulipa uzima. Uzima wa milele ni ‘zawadi anayotoa Mungu . . . kwa njia ya Kristo Yesu, Bwana wetu.’ (Rum. 6:23; Efe. 2:8-10, NW) Hata hivyo, tukiwa na imani katika zawadi hiyo na kuthamini ni kwa jinsi gani ilifanywa iwezekane, tutaonyesha hilo. Kwa kufahamu namna Yehova ametumia Yesu kwa njia ya ajabu katika kutimiza mapenzi Yake na namna lilivyo jambo la maana sana kwetu sote kufuata sana hatua za Yesu, tutaifanya huduma ya Kikristo iwe mojapo mambo ya maana zaidi katika maisha zetu.”
Je, yaweza kusemwa kwamba Mashahidi wa Yehova wote ni watangazaji wa Ufalme wa Mungu? Ndiyo! Kuwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova kwamaanisha hivyo. Zaidi ya nusu karne iliyopita, kuna wale waliohisi kwamba haikuwa lazima kwao kushiriki katika utumishi wa shambani, kwenda hadharani na nyumba hadi nyumba. Lakini leo hakuna yeyote kati ya Mashahidi wa Yehova anayedai asihusishwe na utumishi huo kwa sababu ya daraka lake katika kutaniko la mahali au katika tengenezo la ulimwenguni pote. Wanaume na wanawake pamoja na wachanga na wazee hushiriki. Wao huuona kuwa pendeleo lenye thamani, utumishi mtakatifu. Watu wengi hupiga mbiu wajapokuwa na udhaifu mbaya. Na kwa wowote ambao hawawezi kimwili kwenda nyumba hadi nyumba, wao hupata njia nyinginezo za kuwafikia watu na kuwapa ushahidi kibinafsi.
Nyakati nyingine zamani, kulikuwa na mwelekeo wa kuruhusu wapya zaidi washiriki katika utumishi wa shambani mapema mno. Lakini katika miongo ya hivi karibuni, mkazo mkubwa umewekwa juu ya kustahili kabla ya kualikwa. Hilo linamaanisha nini? Halimaanishi kwamba ni lazima waweze kueleza kila kitu katika Biblia. Lakini, kama vile kitabu Tumefanywa Tengenezo Tutimize Huduma Yetu kinavyofafanua, ni lazima wajue na waamini mafundisho ya msingi ya Biblia. Ni lazima pia wawe wanaishi maisha safi, kupatana na viwango vya Biblia. Ni lazima kila mmoja atake kikweli kuwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova.
Haitazamiwi kwamba Mashahidi wa Yehova wote watafanya kiasi kilekile cha kuhubiri. Hali za watu mmoja-mmoja hutofautiana. Umri, afya, madaraka ya familia, na kina cha uthamini yote ni mambo yanayoamua. Jambo hilo limetambuliwa nyakati zote. Hilo lilikaziwa na toleo la Mnara wa Mlinzi (Kiingereza) la Desemba 1, 1950, lilipozungumza kuhusu “udongo mzuri” katika kielezi cha Yesu cha mpanzi, kwenye Luka 8:4-15. Kingdom Ministry School Course, waliotayarishiwa wazee katika 1972, ulichanganua takwa la ‘kumpenda Yehova kwa nafsi yote’ na ukaeleza kwamba “lililo la maana si wingi wa yale ambayo mtu anafanya kwa kulinganisha na yale ambayo mwingine anafanya, bali ni kufanya yale ambayo mtu anaweza kufanya.” (Mk. 14:6-8) Hata hivyo, likitia moyo kujichanganua kibinafsi kwa uzito, pia lilionyesha kwamba upendo kama huo humaanisha “kwamba kila jambo la maisha ya mtu linahusika katika kumtumikia Mungu kwa upendo; hakuna utendaji, uwezo au tamaa maishani ambayo haihusiki.” Uwezo wetu wote wa kufikiri, nafsi yetu yote, lazima zisukumwe kufanya mapenzi ya Mungu. Kitabu hicho cha mafunzo kilikazia kwamba “Mungu hutaka, si ushiriki tu, bali utumishi wa nafsi yote.”—Mk. 12:30.
Kwa kusikitisha, mwelekeo wa wanadamu wasio wakamilifu ni kupita kiasi, wakikazia jambo moja huku wakipuuza jingine. Kwa hiyo, huko nyuma katika 1906, Ndugu Russell aliliona kuwa jambo la lazima kutahadharisha kwamba kujidhabihu hakumaanishi kudhabihu wengine. Hakumaanishi kushindwa kuandalia ifaavyo mke wako, watoto wanaokutegemea, au wazazi wazee-wazee ili mtu awe huru kuhubiria wengine. Mara kwa mara tangu wakati huo, vikumbusho kama hivyo vimetokea katika vichapo vya Watch Tower.
Hatua kwa hatua, kwa msaada wa Neno la Mungu, tengenezo zima limetafuta kupata usawaziko wa Kikristo—kudhihirisha bidii kwa ajili ya utumishi wa Mungu, huku mtu akitoa uangalifu ufaao kwa mambo yote ya kuwa Mkristo halisi. Ingawa “usitawishaji wa tabia” ulikuzwa juu ya uelewevu usiofaa, Mnara wa Mlinzi limeonyesha kwamba matunda ya roho na mwenendo wa Kikristo hayapaswi kupuuzwa. Katika 1942 Mnara wa Mlinzi lilisema kwa njia ya waziwazi: “Wengine kwa kukosa hekima wamefikia mkataa kwamba ikiwa wangekuwa wakishiriki katika kazi ya kutoa ushahidi nyumba hadi nyumba wangeweza kufuatia mwendo wowote ambao ungeweza kuridhisha mibetuko na tamaa zao bila kupata adhabu. Mtu apaswa akumbuke kwamba kushiriki tu katika kazi ya kutoa ushahidi si ndilo jambo pekee linalotakwa.”—1 Kor. 9:27.
Kutanguliza Mambo ya Maana Zaidi
Mashahidi wa Yehova wamekuja kuthamini kwamba ‘kutafuta kwanza Ufalme na uadilifu wa Mungu’ kunamaanisha kutanguliza maishani mambo ya maana zaidi. Kunatia ndani kuweka mahali pafaapo maishani, funzo la kibinafsi la Neno la Mungu na hudhurio la kawaida kwenye mikutano ya kutaniko bila kuruhusu faida nyinginezo zichukue mahali pa kwanza. Kunatia ndani kufanya maamuzi yanayoonyesha tamaa ya kweli ya kujipatanisha na matakwa ya Ufalme wa Mungu, kama yanavyoonyeshwa katika Biblia. Hilo linatia ndani kutumia kanuni za Biblia kama msingi wa maamuzi yanayohusu maisha ya familia, tafrija, elimu ya kilimwengu, kazi ya kuajiriwa, shughuli za kibiashara, na uhusiano na wenzetu.
Kutafuta kwanza Ufalme kwatia ndani mengi kuliko kuwa na ushirika fulani kila mwezi katika kuzungumza na wengine kuhusu makusudi ya Mungu. Kwamaanisha kupatia faida za Ufalme mahali pa kwanza katika maisha yote ya mtu, huku akishughulikia ifaavyo madaraka mengine ya Kimaandiko.
Kuna njia nyingi ambazo kwazo Mashahidi wa Yehova waliojitoa huendeleza faida za Ufalme.
Pendeleo la Utumishi wa Betheli
Wengine hutumikia wakiwa washiriki wa familia ya Betheli ya duniani pote. Hao ni wafanyakazi walio wahudumu wa wakati wote ambao wamejitolea kufanya lolote watakalogawiwa kufanya katika kutayarisha na kuchapa fasihi za Biblia, katika kushughulikia kazi ya lazima ofisini, na katika kuandaa utumishi wa kutegemeza shughuli hizo. Hiyo si kazi ambayo wao hujipatia umashuhuri wa kibinafsi au mali za kimwili. Tamaa yao ni kumheshimu Yehova, na wanaridhika na upaji wanaopewa kama vile chakula, malazi, na rudishio la fedha la kiasi kwa ajili ya matumizi ya kibinafsi. Kwa sababu ya aina ya maisha ya familia ya Betheli, wenye mamlaka wa kilimwengu katika Marekani, kwa kielelezo, huwaona kuwa jamii ya dhehebu la kidini ambao wamechukua nadhiri ya umaskini. Wale walio katika Betheli hupata shangwe kuweza kutumia maisha zao kikamili katika utumishi wa Yehova na katika kufanya kazi ambayo hunufaisha idadi kubwa ya ndugu zao za Kikristo na watu ambao wamependezwa karibuni, nyakati nyingine kimataifa. Kama vile wale Mashahidi wa Yehova wengineo, wao pia hushiriki kwa ukawaida katika huduma ya shambani.
Familia ya kwanza ya Betheli (au familia ya Bible House, kama walivyojulikana wakati huo) ilikuwa katika Allegheny, Pennsylvania. Kufikia 1896, wafanyakazi walikuwa 12. Katika 1992, kulikuwa na washiriki wa familia ya Betheli zaidi ya 12,900, wakitumikia katika nchi 99. Kwa kuongezea, wakati nafasi ya nyumba katika majengo ya Sosaiti imekuwa haitoshi, mamia ya wafanyakazi wengine wa kujitolea wamesafiri kwenda kwenye makao ya Betheli na viwanda kila siku ili kushiriki katika kazi. Wao hulihesabu kuwa pendeleo kuwa na sehemu katika kazi inayofanywa. Kunapokuwa na uhitaji, maelfu ya Mashahidi wengineo hujitolea kuacha kazi za kimwili na utendaji mwingineo kwa vipindi vya wakati vinavyotofautiana ili kusaidia katika kujenga vifaa vinavyohitajiwa na Sosaiti vya kutumiwa kuhusiana na kuhubiri habari njema za Ufalme wa Mungu duniani pote.
Washiriki wengi wa familia ya Betheli ya duniani pote wameifanya iwe kazi-maisha yao. Frederick W. Franz, ambaye katika 1977 alikuja kuwa msimamizi wa nne wa Watch Tower Society, alikuwa tayari amekuwa mshiriki wa familia ya Betheli katika New York kwa miaka 57, na akaendelea katika utumishi wa Betheli kwa miaka mingine 15, mpaka alipokufa katika 1992. Heinrich Dwenger alianza utumishi wa Betheli Ujerumani katika 1911, baadaye akatumikia kwa unyenyekevu mahali popote alipogawiwa; na katika 1983, mwaka aliokufa, bado alikuwa anafurahia utumishi wake akiwa mshiriki wa familia ya Betheli katika Thun, Uswisi. George Phillips, kutoka Scotland, alikubali mgawo wa kwenda ofisi ya tawi ya Afrika Kusini katika 1924 (ilipokuwa ikisimamia utendaji wa kuhubiri toka Cape Town hadi Kenya) na akaendelea kutumikia katika Afrika Kusini hadi kifo chake katika 1982 (wakati ambapo ofisi za tawi saba za Sosaiti na Mashahidi 160,000 walikuwa watendaji katika eneo hilo). Dada Wakristo, kama vile Kathryn Bogard, Grace DeCecca, Irma Friend, Alice Berner, na pia Mary Hannan, wakiwa watu wazima walitoa maisha zao katika utumishi wa Betheli, wakifanya hivyo hadi kifo chao. Vilevile washiriki wengineo wa familia ya Betheli wamekuwa wakitumikia kwa miaka 10, 30, 50, 70, na zaidi.g
Waangalizi Wasafirio Wenye Kujidhabihu
Ulimwenguni pote, kuna waangalizi wa mzunguko na wa wilaya kama 3,900 ambao, wakiwa na wake zao, hushughulikia pia migawo mahali popote wanapohitajiwa, sana sana katika nchi za kwao. Wengi wao wameacha makao na sasa wanaenda kila juma au kila baada ya majuma machache kutumikia makutaniko waliyogawiwa. Hawapokei mshahara wowote lakini wao hushukuru kwa chakula na malazi mahali wanapotumikia, pamoja na kiasi cha upaji kwa ajili ya matumizi ya kibinafsi. Katika Marekani, ambako waangalizi wa mzunguko na wa wilaya 499 walikuwa wakitumikia katika 1992, wazee hao wenye kusafiri walikuwa na wastani wa umri wa miaka 54, na wengine wao wamekuwa wakitumikia katika daraka hilo kwa miaka 30, 40, au zaidi. Katika nchi kadhaa, waangalizi hao husafiri kwa gari. Eneo katika sehemu ya Pasifiki mara nyingi hutaka ndege na mashua za kibiashara. Katika sehemu nyingi waangalizi wa mzunguko hufikia makutaniko ya mbali kwa kupanda farasi au kwa miguu.
Mapainia Watoa Msaada Mkubwa
Ili kuanza kuhubiri habari njema katika sehemu zisizo na Mashahidi, au kutoa msaada ambao huenda ukahitajiwa kihususa katika eneo fulani, huenda Baraza Linaloongoza likapanga kupeleka mapainia wa pekee. Wao ni waeneza-evanjeli wa wakati wote wanaotumia angalau saa 140 kila mwezi katika huduma ya shambani. Wao hujitolea ili watumikie popote wanapohitajiwa katika nchi yao au, katika visa fulani, katika nchi jirani. Kwa kuwa matakwa ya utumishi wao huwaacha wakiwa na wakati mchache au bila wakati wa kufanya kazi ya kimwili ili kujiandalia mahitaji ya kimwili, wao hupewa rudishio la kiasi kwa ajili ya kugharimia makao na mahitaji mengineyo. Katika 1992, kulikuwa na mapainia wa pekee zaidi ya 14,500 katika sehemu mbalimbali za dunia.
Mapainia wa pekee wa kwanza walipotumwa katika 1937, waliongoza katika kazi ya kuwapigia kinanda wenye nyumba milangoni pao ili wasikilize hotuba za Biblia zilizorekodiwa kisha kutumia rekodi hizo kuwa msingi wa mazungumzo ya Biblia kwenye ziara za kurudia. Hilo lilifanywa katika miji mikubwa ambako tayari kulikuwa na makutaniko. Baada ya miaka kadhaa, mapainia wa pekee wakaanza kuelekezwa hasa kwenye sehemu ambako makutaniko hayakuwako au ambako makutaniko yalikuwa na uhitaji mkubwa wa msaada. Kwa sababu ya kazi yao yenye matokeo, mamia ya makutaniko mapya yalifanyizwa.
Badala ya kueneza eneo na kusonga mbele, wangefanya kazi kwenye eneo hususa kwa kurudiarudia, wakifuatia kupendezwa kote na kuongoza mafunzo ya Biblia. Mikutano ilipangwa kwa ajili ya waliopendezwa. Hivyo, katika Lesotho, kusini mwa Afrika, kwenye juma lake la kwanza katika mgawo mpya, painia wa pekee alialika kila mtu aliyekutana naye aje aone jinsi Mashahidi wa Yehova huongoza Shule ya Huduma ya Kitheokrasi. Yeye na familia yake walifanya programu nzima. Kisha akawaalika wote kwenye Funzo la Mnara wa Mlinzi. Baada ya udadisi wa kwanza kuridhishwa, watu 30 waliendelea kuhudhuria Funzo la Mnara wa Mlinzi, na wastani wa hudhurio kwenye shule ulikuwa 20. Katika nchi ambako wamishonari waliozoezwa Gileadi walifanya mengi kuanzisha kuhubiriwa kwa habari njema, nyakati nyingine ukuzi wa haraka ulitokea wakati Mashahidi wenyeji walipoanza kustahili kutumikia katika utumishi wa painia wa pekee, kwani hao wangeweza kufanya kazi kwa matokeo zaidi miongoni mwa wenyeji.
Kwa kuongezea wafanyakazi hao wenye bidii, kuna mamia ya maelfu ya Mashahidi wa Yehova wanaoendeleza faida za Ufalme kwa juhudi. Hao ni vijana kwa wazee, wanaume kwa wanawake, waliofunga ndoa na waseja. Mapainia wa kawaida hutumia saa zisizopungua 90 kila mwezi kwenye huduma ya shambani; mapainia wasaidizi, angalau saa 60. Wao huamua mahali ambako wangependa kuhubiri. Walio wengi hufanya kazi pamoja na makutaniko yaliyoanzishwa tayari; wengine huhamia sehemu za mbali. Wao hushughulikia mahitaji yao wenyewe kwa kufanya kazi ya kimwili, au huenda washiriki wao wa familia wakasaidia kuwapa upaji huo. Wakati wa 1992, zaidi ya 914,500 walishiriki utumishi huo wakiwa mapainia wa kawaida au wasaidizi kwa angalau sehemu ya mwaka huo.
Shule Zenye Malengo ya Pekee
Ili kuwatayarisha wenye kujitolea kwa ajili ya aina fulani za utumishi, masomo ya pekee huandaliwa. Kwa kielelezo, tangu 1943, Shule ya Gileadi imezoeza maelfu ya wahudumu wenye ujuzi kwenye kazi ya mishonari, na wahitimu wamepelekwa kwenye sehemu zote za dunia. Katika 1987 Shule ya Mazoezi ya Kihuduma ilianza kutenda ili kusaidia kujazia mahitaji ya pekee, kutia na kushughulikia makutaniko na madaraka mengine. Mpango wa kwamba shule hii ifanywe katika mahali tofauti-tofauti hupunguza gharama za usafiri za wanafunzi kwenda mahali fulani pa kati na vilevile uhitaji wa kujifunza lugha nyingine ili kunufaika na shule hiyo. Wote wanaoalikwa kuhudhuria shule hii ni wazee au watumishi wa huduma ambao wamedhihirisha kwamba kwelikweli wao wanatafuta kwanza Ufalme. Wengi wanajitolea kutumikia katika nchi nyinginezo. Roho yao ni kama ile ya nabii Isaya, aliyesema: “Mimi hapa, nitume mimi.”—Isa. 6:8.
Ili kufanya ufanisi wa wale ambao tayari wanatumikia wakiwa mapainia wa kawaida na wa pekee uwe bora zaidi, Shule ya Utumishi wa Painia ilianzishwa katika 1977. Mahali ilipowezekana, shule hiyo ilipangwa katika kila mzunguko kotekote ulimwenguni. Mapainia wote walialikwa wanufaike kutokana na mtaala huo wa majuma mawili. Kwa kuendelea tokea wakati huo, mapainia ambao wamemaliza mwaka wao wa kwanza wa utumishi wamepewa mazoezi ayo hayo. Kufikia 1992, zaidi ya mapainia 100,000 walikuwa wamezoezwa katika shule hiyo katika Marekani pekee; zaidi ya 10,000 walikuwa wakizoezwa kila mwaka. Wengine 55,000 walikuwa wamezoezwa katika Japani, 38,000 katika Mexico, na 25,000 katika Brazili na 25,000 katika Italia. Kuongezea mtaala huo, kwa kawaida mapainia hufurahia mkutano wa pekee na mwangalizi wa mzunguko wakati wa ziara zake za mara mbili kila mwaka kwa kila kutaniko na kipindi cha mazoezi ya pekee pamoja na mwangalizi wa mzunguko na wa wilaya wakati wa kusanyiko la mzunguko la kila mwaka. Hivyo, wale wanaofanyiza jeshi kubwa la wapiga-mbiu wa Ufalme wanaotumikia wakiwa mapainia si wafanyakazi wenye nia tu bali pia ni wahudumu waliozoezwa vyema.
Kutumikia Sehemu Zenye Uhitaji Mkubwa Zaidi
Maelfu mengi ya Mashahidi wa Yehova—wengine wao wakiwa mapainia, na wengine si mapainia—wamejitoa ili kutumikia si katika jumuiya yao ya nyumbani tu bali pia katika maeneo mengine ambako kuna uhitaji mkubwa zaidi wa wapiga-mbiu wa habari njema. Kila mwaka maelfu hutumia kipindi cha majuma au miezi, kulingana na yale ambayo mtu binafsi aweza kupanga, katika maeneo ambayo kwa kawaida huwa mbali na kwao ili kutolea ushahidi watu ambao hawatembelewi kwa ukawaida na Mashahidi wa Yehova. Maelfu zaidi wameondoka wanakoishi na kuishi kwingineko ili kutoa msaada huo kwa kipindi kirefu. Wengi wa hawa ni waume na wake au familia zenye watoto. Kuhama kwao mara nyingi kumehusisha kwenda mwendo mfupi kwa kulinganishwa, lakini wengine wamehamahama hivyo kwa muda wa miaka. Wengi wa hao Mashahidi wenye bidii hata wameanza utumishi katika nchi za kigeni—wengine kwa miaka michache, wengine kwa kudumu. Wao hufanya kazi yoyote ya kimwili inayohitajiwa ili kushughulikia mahitaji yao, na wao huhama kwa gharama yao wenyewe. Tamaa yao kuu ni kushiriki kikamili kueneza ujumbe wa Ufalme kadiri hali zao zinavyoruhusu.
Inapokuwa kichwa cha familia si Shahidi, huenda yeye akahama na familia yake kwa sababu za kikazi. Lakini huenda washiriki wa familia ambao ni Mashahidi wakaona hiyo kuwa fursa ya kueneza ujumbe wa Ufalme. Ilikuwa hivyo kwa Mashahidi wawili kutoka Marekani waliojipata katika kambi ya ujenzi katika msitu wa Suriname mwishoni mwa miaka ya 1970. Mara mbili kwa juma waliamka saa 10:00 za usiku, wakapanda basi ya kampuni kwa safari ya saa moja isiyostarehesha kwenda kwenye kijiji, na kutumia siku wakihubiri. Kabla ya muda mrefu walikuwa wakiongoza mafunzo ya Biblia 30 kila juma na watu wenye njaa ya kiroho. Leo, kuna kutaniko katika sehemu hiyo ya msitu wa mvua ambayo hapo awali haikuwa imefikiwa.
Kutumia Kila Fursa Inayofaa ili Kutoa Ushahidi
Bila shaka, si Mashahidi wa Yehova wote wanaohamia nchi nyingine, au hata kwenye miji mingine, ili kuendeleza huduma yao. Hali zao huenda zisiwaruhusu wapainie. Hata hivyo, wao wanajua vema juu ya himizo la Biblia kutia ‘jitihada yote’ na kuwa ‘na mengi ya kufanya katika kazi ya Bwana.’ (2 Pet. 1:5-8; 1 Kor. 15:58, NW) Wao huonyesha kwamba wanatafuta kwanza Ufalme wanapotanguliza faida za huo mbele ya kazi ya kimwili na tafrija. Wale ambao mioyo yao imejaa uthamini kwa ajili ya Ufalme hushiriki kwa ukawaida katika huduma ya shambani kwa kadiri ambayo hali zao huwaruhusu, na wengi wao hubadili hali zao ili waweze kushiriki kwa ukamili zaidi. Pia wako macho wakati wote kutumia fursa zifaazo kutoa ushahidi kwa wengine kuhusu Ufalme.
Kielelezo kimoja, John Furgala, ambaye alikuwa na biashara ya kuuza bidhaa za chuma katika Guayaquil, Ekuado, aliweka fasihi za Biblia dukani mwake kwa wonyesho wa kuvutia. Wakati msaidizi wake angemhudumia mteja, John angemtolea mteja ushahidi.
Katika Nigeria Shahidi mwenye bidii aliyeruzuku familia yake kwa kufanya kazi akiwa mwenye kondrati ya umeme aliazimia pia kutumia vema fursa alizokuwa nazo kukutana na watu na kuwatolea ushahidi. Kwa kuwa yeye ndiye aliyekuwa mwenye biashara, alipanga ratiba ya utendaji. Kila asubuhi, kabla ya kazi ya kila siku, alikusanya mke wake, watoto, wafanyakazi, na wanagenzi (wafunzwa-kazi) kwa ajili ya mazungumzo ya andiko la Biblia la siku hiyo, pamoja na mambo yaliyoonwa kutoka Yearbook of Jehovah’s Witnesses. Mwanzoni mwa kila mwaka, angewapatia wateja wake nakala ya kalenda ya Watch Tower Society, pamoja na magazeti mawili. Kama tokeo, baadhi ya wafanyakazi wake na wateja wamejiunga naye katika kumwabudu Yehova.
Kunao wengi kati ya Mashahidi wa Yehova walio na roho hiyohiyo. Hata iwe wanafanya nini, wakati wote wanatafuta fursa za kushiriki habari njema pamoja na wengine.
Jeshi Kubwa la Waeneza-Evanjeli wa Wakati Wote Wenye Furaha
Bidii ya Mashahidi wa Yehova ya kuhubiri habari njema haijakwisha kwa kupita kwa miaka. Hata ingawa wenye nyumba wengi wamewaambia kwa uthabiti kwamba hawapendezwi, kuna idadi kubwa ya wale ambao wanashukuru kwamba Mashahidi huwasaidia kuelewa Biblia. Azimio la Mashahidi wa Yehova ni kuendelea kuhubiri hadi Yehova mwenyewe atoe mwelekezo wa wazi kwamba kazi hiyo imekamilika.
Badala ya kupunguza mwendo, shirika la ulimwenguni pote la Mashahidi wa Yehova hasa limeongeza utendaji walo wa kuhubiri. Katika 1982 ripoti ya duniani pote ya kila mwaka ilionyesha kwamba muda wa saa 384,856,662 zilitolewa kwenye huduma ya shambani. Miaka kumi baadaye (katika 1992) saa 1,024,910,434 zilitumiwa katika kazi hiyo. Ni nini kilichosababisha ongezeko hilo kubwa la utendaji?
Ni kweli kwamba idadi ya Mashahidi wa Yehova imekua. Lakini si kwa kadiri ileile ya muda wa saa. Wakati wa kipindi hicho, idadi ya Mashahidi ilipoongezeka kwa asilimia 80, idadi ya mapainia ilipanda ikawa asilimia 250. Kwa wastani kila mwezi, 1 kati ya Mashahidi wa Yehova 7 ulimwenguni pote alikuwa katika aina fulani ya kazi ya kuhubiri ya wakati wote.
Ni nani waliokuwa wakishiriki katika utumishi huo wa painia? Kwa kielelezo, katika Jamhuri ya Korea, Mashahidi wengi ni wake wa nyumbani. Huenda madaraka ya familia yasiwaruhusu wote kupainia kwa ukawaida, lakini idadi kubwa wametumia likizo ndefu za shule wakati wa kipupwe kuwa fursa za kufanya utumishi wa painia msaidizi. Kama tokeo, asilimia 53 ya Mashahidi wote katika Jamhuri ya Korea walikuwa katika aina fulani ya utumishi wa wakati wote katika Januari 1990.
Katika miaka ya mapema, ilikuwa ni roho ya upainia wa bidii kwa upande wa Mashahidi Wafilipino iliyowawezesha kufikia mamia ya visiwa vinavyokaliwa na watu katika Filipino kwa ujumbe wa Ufalme. Bidii hiyo imekuwa wazi hata zaidi tangu wakati huo. Katika 1992, kwa wastani kila mwezi, wahubiri 22,205 walikuwa wakishiriki katika huduma ya shambani wakiwa mapainia katika Filipino. Hiyo ilitia ndani vijana wengi waliokuwa wamechagua ‘kumkumbuka Muumba wao’ na kutumia nguvu yao ya ujana katika utumishi wake. (Mhu. 12:1) Baada ya mwongo mmoja wa miaka ya utumishi wa painia, mmoja wa vijana hao alisema: “Nimejifunza kuwa mwenye saburi, kuwa na maisha sahili, kumtegemea Yehova, na kuwa mnyenyekevu. Ni kweli kwamba nimepata magumu na kuvunjika moyo pia, lakini yote hayo si kitu ninapoyalinganisha na baraka ambazo upainia umeniletea.”
Wakati wa Aprili na Mei 1989, Mnara wa Mlinzi lilikazia kufunuliwa kwa Babiloni Mkubwa, ambayo ni dini bandia katika namna yayo mbalimbali ulimwenguni pote. Makala hizo zilitangazwa wakati uleule katika lugha 39 na kugawanywa sana. Katika Japani, ambako idadi ya Mashahidi wanaopainia mara nyingi imekuwa zaidi ya asilimia 40, kilele kipya cha mapainia wasaidizi 41,055 walijiandikisha kusaidia katika kazi hiyo mwezi Aprili. Katika Wilaya ya Osaka, Jiji la Takatsuki, Kutaniko la Otsuka, wahubiri waliobatizwa 73 kati ya 77 walikuwa katika aina fulani ya utumishi wa painia mwezi huo. Mnamo Aprili 8, wahubiri wote katika Japani walipohimizwa kuwa na sehemu katika kugawanya ujumbe huo muhimu, mamia ya makutaniko, kama vile Kutaniko la Ushioda, katika Jiji la Yokohama, yalipanga kuwa na utumishi wa siku nzima kwenda barabarani na nyumba hadi nyumba, kuanzia saa 1:00 asubuhi hadi saa 2:00 usiku, ili kufikia kila mtu katika eneo hilo kwa kadiri ilivyowezekana.
Kama vile ilivyo kila mahali, Mashahidi wa Yehova katika Mexico hufanya kazi ili kushughulikia mahitaji yao ya kimwili. Hata hivyo, kila mwezi wakati wa 1992, kwa wastani 50,095 kati ya Mashahidi wa Yehova huko walipanga mambo yao ili washiriki katika utumishi wa painia ili wasaidie watu wenye njaa ya kiroho wajifunze kuhusu Ufalme wa Mungu. Katika familia nyingine, wote katika nyumba walishirikiana ili kuwezesha kikundi kizima, au angalau baadhi yao, wapainie. Wanaonea shangwe huduma yenye mazao. Wakati wa 1992, Mashahidi wa Yehova katika Mexico walikuwa wakiongoza mafunzo ya Biblia nyumbani 502,017 pamoja na watu mmoja-mmoja na vikundi vya familia.
Wazee wanaotumikia mahitaji ya makutaniko ya Mashahidi wa Yehova wana madaraka mazito. Wengi wa wazee katika Nigeria ni wanaume wenye familia, na ndivyo ilivyo pia na wazee katika mahali pengine pengi. Na zaidi ya kutayarisha ili kuongoza au kushiriki katika mikutano ya kutaniko, pamoja na kufanya uchungaji unaohitajiwa wa kundi la Mungu, baadhi ya wanaume hao hupainia pia. Hilo huwezekanaje? Kuratibu wakati kwa uangalifu na ushirikiano mzuri wa familia mara nyingi huwa mambo ya maana.
Ni wazi kwamba, ulimwenguni pote, Mashahidi wa Yehova wamezingatia moyoni himizo la Yesu la ‘kufuliza kutafuta kwanza Ufalme.’ (Mt. 6:33, NW) Yale wanayofanya ni wonyesho wa kutoka moyoni wa upendo wao kwa Yehova na uthamini wao kwa ajili ya enzi kuu yake. Kama vile mtunga zaburi Daudi, wao husema: “Ee Mungu wangu, Mfalme, nitakutukuza, nitalihimidi jina lako milele na milele.”—Zab. 145:1.
[Maelezo ya Chini]
a Watch Tower, Agosti 15, 1906, kur. 267-271.
b Ona Mnara wa Mlinzi (Kiingereza), Februari 1, 1967, kurasa 92-95.
c Ona Mnara wa Mlinzi (Kiingereza), Desemba 15, 1973, kurasa 760-765.
d Ona Mnara wa Mlinzi (Kiingereza), Septemba 1, 1972, kurasa 533-536.
e Mnara wa Mlinzi (Kiingereza), Desemba 15, 1963, kur. 764-766.
f Ona Mnara wa Mlinzi, (Kiingereza) Desemba 1, 1969, kurasa 729-732; Septemba 15, 1988, ukurasa 31.
g Ona Mnara wa Mlinzi, Mei 1, 1987, kurasa 22-30; Aprili 1, 1964 (Kiingereza), kurasa 212-215; Desemba 1, 1956, kurasa 712-719; Agosti 15, 1970, kurasa 507-510; Oktoba 1, 1960, kurasa 601-605; Juni 15, 1968, kurasa 378-381; Aprili 1, 1968, kurasa 217-221; Aprili 1, 1959, kurasa 220-223.
[Blabu katika ukurasa wa 292]
Mkazo ulioongezwa juu ya daraka la kutoa ushahidi
[Blabu katika ukurasa wa 293]
Wao huona kutoa ushahidi nyumba hadi nyumba kuwa pendeleo lenye thamani
[Blabu katika ukurasa wa 294]
Kuelewa kinachomaanishwa na utumishi wa nafsi yote
[Blabu katika ukurasa wa 295]
Kinachomaanishwa hasa na “kutafuta kwanza Ufalme”
[Blabu katika ukurasa wa 301]
Mashahidi wenye bidii walitanguliza faida za Ufalme mbele ya kazi ya kimwili na tafrija
[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 288]
“Where Are the Nine?”
Kwenye Ukumbusho wa kifo cha Kristo, katika 1928, trakti ambayo kila mtu aliyehudhuria alipewa ilikuwa yenye kichwa “Where Are the Nine?” Mazungumzo yayo ya Luka 17:11-19 yaligusa moyo wa Claude Goodman na yakamsukuma kuingia katika kazi ya kolpota, au painia na kustahimili katika utumishi huo.
[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 296, 297]
Utumishi wa Betheli
Kufikia 1992, kulikuwa na 12,974 waliokuwa wakishiriki katika utumishi wa Betheli katika nchi 99
[Picha]
Funzo la kibinafsi ni la maana kwa washiriki wa familia ya Betheli
Hispania
Kwenye kila Kao la Betheli, siku huanza kwa mazungumzo ya andiko la Biblia
Finland
Kama vile ilivyo na Mashahidi wa Yehova kila mahali, washiriki wa familia ya Betheli hushiriki katika utumishi wa shambani
Uswisi
Kila Jumatatu jioni familia ya Betheli hujifunza “Mnara wa Mlinzi” pamoja
Italia
Kazi hutofautiana, lakini yote hufanywa kwa kutegemeza kazi ya kupiga mbiu ya Ufalme wa Mungu
Ufaransa
Papua New Guinea
Marekani
Ujerumani
Filipino
Mexico
Uingereza
Nigeria
Uholanzi
Brazili
Japani
Afrika Kusini
[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 298]
Wachache Wenye Muda Mrefu wa Utumishi wa Betheli
F. W. Franz—Marekani (1920-1992)
Heinrich Dwenger—Ujerumani (karibu miaka 15 ya 1911-1933), Hungaria (1933-1935), Chekoslovakia (1936-1939), kisha Uswisi (1939-1983)
George Phillips—Afrika Kusini (1924-1966, 1976-1982)
Dada za kimwili (Kathryn Bogard na Grace DeCecca) waliotoa jumla ya miaka 136 kwenye utumishi wa Betheli—Marekani
[Grafu katika ukurasa wa 303]
(Ona mpangilio kamili katika nakala iliyochapishwa)
Mapainia Wanaoongezeka!
Mapainia
Wahubiri
Asilimia ya Ongezeko Tangu 1982
250%
200%
150%
100%
50%
1982 1984 1986 1988 1990 1992
[Picha katika ukurasa wa 284]
Dada Early alisafiri sehemu kubwa ya New Zealand kwa baiskeli ili kushiriki ujumbe wa Ufalme
[Picha katika ukurasa wa 285]
Kwa miaka 76—akiwa mseja, akiwa ameolewa, na kisha akiwa mjane—Malinda Keefer alijitoa mwenyewe kwenye huduma ya wakati wote
[Picha katika ukurasa wa 286]
Magari yenye nyumba sahili yaliandaa malazi kwa baadhi ya mapainia wa zamani walipohama kutoka mahali pamoja hadi pengine
Kanada
India
[Picha katika ukurasa wa 287]
Frank Rice (anayesimama upande wa kulia), Clem Deschamp (aliyeketi mbele ya Frank, pamoja na mke wa Clem, Jean, kando yao), na kikundi katika Java kutia na Mashahidi wenzi na watu waliopendezwa karibuni
[Picha katika ukurasa wa 288]
Maisha ya Claude Goodman ya huduma ya wakati wote yalimpeleka kwenye utumishi katika India na nchi nyinginezo saba
[Picha katika ukurasa wa 289]
Ben Brickell alipokuwa na afya nzuri, alifurahia kuitumia katika utumishi wa Yehova; matatizo mabaya ya afya katika miaka ya baadaye hayakumfanya aache
[Picha katika ukurasa wa 290]
Kathe Palm alitoa ushahidi katika kila aina ya eneo, kuanzia ofisi za majiji makubwa hadi kwenye kambi za migodi na malisho ya kondoo ya mbali katika Chile
[Picha katika ukurasa wa 291]
Azimio la Martin na pia Gertrud Poetzinger linaonyeshwa katika maneno: ‘Jambo hili moja nilifanyalo—kutafuta kwanza Ufalme’
[Picha katika ukurasa wa 300]
Shule ya Utumishi wa Painia (kama inavyoonyeshwa hapa katika Japani) imeandaa mazoezi ya pekee kwa makumi ya maelfu ya wafanyakazi wenye bidii
-
-
Kukua Pamoja Katika UpendoMashahidi wa Yehova—Wapiga-Mbiu wa Ufalme wa Mungu
-
-
Sura ya 19
Kukua Pamoja Katika Upendo
WAKATI walipoandikia Wakristo wenzao, mitume wa Yesu Kristo walitaja uhitaji wa watu mmoja-mmoja kukua si katika ujuzi sahihi tu bali pia katika upendo. Msingi wa jambo hilo ulikuwa ule upendo ulioonyeshwa na Mungu mwenyewe na ule upendo wa kujidhabihu wa Kristo, ambaye walijitahidi kufuata hatua zake. (Yn. 13:34, 35; Efe. 4:15, 16; 5:1, 2; Flp. 1:9; 1 Yoh. 4:7-10) Walikuwa udugu, na waliposaidiana mmoja na mwenzake, vifungo vya upendo vilipata kuwa vyenye nguvu hata zaidi.
Wakati njaa ilipotokeza magumu ya kiuchumi kwa akina ndugu katika Yudea, Wakristo katika Siria na katika Ugiriki walishiriki mali zao ili kuwasaidia. (Mdo. 11:27-30; Rum. 15:26) Wakati baadhi yao waliponyanyaswa, mateso waliyopata yalihisiwa sana na Wakristo wengine, nao walitafuta kutoa usaidizi.—1 Kor. 12:26; Ebr. 13:3.
Bila shaka, wanadamu wote wana uwezo wa kupenda, na wengine mbali na Wakristo hushiriki katika vitendo vya fadhili za kibinadamu. Lakini watu katika ulimwengu wa Kiroma walitambua kwamba ule upendo ulioonyeshwa na Wakristo ulikuwa tofauti. Tertuliano, aliyekuwa amekuwa stadi wa sheria katika Roma, alinukuu maneno ya watu wa ulimwengu wa Roma kuhusu Wakristo, akisema: “‘Tazama,’ wao husema, ‘jinsi wanavyopendana mmoja na mwenzake . . . na jinsi walivyo tayari kufa kwa ajili ya mmoja na mwenzake.’” (Apology, 39, 7) John Hurst, katika kitabu chake History of the Christian Church (Buku 1, ukurasa 146), husimulia kwamba watu katika Kartheji na Aleksandria la kale, wakati wa vipindi vya ugonjwa wa kipuku, waliwafukuza kutoka mbele yao wale waliougua na kuvua kutoka kwa miili ya wenye kufa chochote kilichokuwa chenye thamani. Kwa kutofautisha, yeye aripoti, Wakristo katika sehemu hizo walishiriki mali zao, wakatunza wagonjwa, na kuzika wafu.
Je, Mashahidi wa Yehova katika nyakati za kisasa hushiriki katika kazi ambazo huonyesha hangaiko kama hilo kwa hali njema ya wengine? Ikiwa ndivyo, hizo hufanywa na watu mmoja-mmoja tu wachache waliotawanyika, au je, tengenezo kwa ujumla hutia moyo na kuunga mkono jitihada kama hizo?
Msaada Wenye Upendo Katika Makutaniko ya Mahali
Miongoni mwa Mashahidi wa Yehova, utunzaji wa mayatima na wajane kutanikoni, pamoja na waaminifu wowote wapatwao na msiba mkali, huonwa kuwa sehemu ya ibada yao. (Yak. 1:27; 2:15-17; 1 Yoh. 3:17, 18) Kwa kawaida serikali za kilimwengu hufanya maandalizi ya hospitali, makao kwa wazee-wazee, na mipango ya misaada ya kijamii kwa watu wasioajiriwa kazi katika jumuiya kwa ujumla, na Mashahidi wa Yehova huunga mkono mipango hiyo kwa kulipa kodi zao kwa kudhamiria. Hata hivyo, wakitambua kwamba Ufalme wa Mungu tu ndio uwezao kutatua matatizo ya wanadamu kwa njia ya kudumu, Mashahidi wa Yehova hujitoa wenyewe na mali zao kwanza kabisa ili kufundisha wengine juu ya ufalme huo. Huo ni utumishi muhimu ambao hakuna serikali ya kibinadamu inayouandaa.
Katika makutaniko zaidi ya 69,000 ya Mashahidi wa Yehova ulimwenguni pote, mahitaji ya pekee ambayo hutokea kwa sababu ya uzee na udhaifu wa watu mmoja-mmoja hushughulikiwa kwa kawaida na watu mmoja-mmoja. Kama inavyoonyeshwa kwenye 1 Timotheo 5:4, 8, daraka hilo hukalia kwanza kabisa kila Mkristo kutunza wale wa nyumba yake mwenyewe. Watoto, wajukuu, au wengine wa jamaa ya karibu huonyesha upendo wa Kikristo kwa kuandaa usaidizi kwa wazee-wazee na wenye udhaifu. Makutaniko ya Mashahidi wa Yehova hayadhoofishi hisi hii ya kuwa na daraka kwa kujitwalia wajibu mbalimbali wa familia. Hata hivyo, ikiwa hakuna washiriki wa familia wa karibu, au ikiwa wale wenye daraka hawawezi hata kidogo kubeba mzigo huo peke yao, wengine katika kutaniko huja kuwasaidia kwa upendo. Ikihitajiwa, kutaniko kwa ujumla laweza kufanya uandalizi wa usaidizi fulani kwa ndugu au dada mwenye uhitaji ambaye ana rekodi ndefu ya utumishi wa uaminifu.—1 Tim. 5:3-10.
Kushughulikia mahitaji hayo hakuachiwi nasibu. Kwenye vipindi vya Shule ya Huduma ya Ufalme, ambayo wazee wamehudhuria kwa kurudiarudia tangu 1959, wajibu wao mbele za Mungu kuhusiana na jambo hilo wakiwa wachungaji wa kundi umefikiriwa kipekee mara nyingi. (Ebr. 13:1, 16) Si kwamba hawakujua uhitaji huo kabla ya hapo. Kwa kielelezo, katika 1911, msaada wa vitu vya kimwili uliandaliwa na Kutaniko la Oldham katika Lancashire, Uingereza, kwa wale miongoni mwao waliokuwa wakikabili matatizo makali ya kiuchumi. Hata hivyo, tangu hapo tengenezo la duniani pote limekua, idadi ya wale wenye kupatwa na matatizo makali imeongezeka, na Mashahidi wa Yehova wamezidi kujua juu ya yale ambayo Biblia huonyesha wapaswa kufanya katika hali hizo. Hasa katika miaka ya majuzi, madaraka ya kila Mkristo kuelekea wale miongoni mwao wenye mahitaji ya pekee—wazee-wazee, wenye udhaifu, familia zenye mzazi mmoja, na wale walio na magumu ya kiuchumi—yamezungumzwa na makutaniko yote kwenye mikutano yao.a
Hangaikio ambalo Mashahidi mmoja-mmoja huonyesha kwa wengine huwa zaidi ya kusema, “mkaote moto na kushiba.” Wao binafsi huonyesha hangaikio lenye upendo. (Yak. 2:15, 16) Fikiria vielelezo vichache.
Wakati mwanamke mmoja kijana Msweden, mmoja wa Mashahidi wa Yehova, alipougua ugonjwa wa meningitis (wa ngozi inayofunika ubongo) alipokuwa akitembelea Ugiriki katika 1986, alipata pia kuona yanayomaanishwa na kuwa na ndugu na dada Wakristo katika nchi nyingi. Baba yake katika Sweden alijulishwa. Mara hiyo aliwasiliana na mzee katika kutaniko la Mashahidi wa Yehova la kwao Sweden na, kupitia yeye, akawasiliana na Shahidi katika Ugiriki. Mpaka dada huyo alipoweza kurudi Sweden majuma matatu baadaye, marafiki hao wapya wa Shahidi huyo kijana katika Ugiriki hawakumwacha kamwe bila mtu wa kumhudumia.
Vivyo hivyo, wakati Shahidi mmoja mzee-mzee, aliyekuwa mjane wa kiume katika Wallaceburg, Ontario, Kanada, alipohitaji usaidizi, familia moja aliyokuwa amesaidia kiroho ilionyesha uthamini kwa kumfanya sehemu ya familia. Miaka michache baadaye wakati walipohamia Barry’s Bay, alienda pamoja nao. Aliishi nao, naye alitunzwa nao kwa upendo kwa miaka 19, mpaka alipokufa katika 1990.
Katika New York City, wenzi wa ndoa Mashahidi walitunza mwanamume mmoja mzee-mzee aliyekuwa akihudhuria mikutano katika Jumba la Ufalme lao, wakafanya hivyo kwa miaka kama 15, mpaka alipokufa katika 1986. Alipougua ugonjwa wa ghafula, walimnunulia vitu dukani, wakamfanyia kazi ya usafi, wakampikia, na kumfulia nguo. Walimtendea kana kwamba alikuwa baba yao wenyewe.
Mahitaji ya aina nyingine yanapewa uangalifu wa upendo pia. Wenzi wa ndoa Mashahidi katika Marekani waliuza nyumba yao na kuhamia Montana ili kusaidia kutaniko huko. Hata hivyo, baada ya wakati, matatizo mazito ya afya yalitokea, ndugu huyo akafutwa kazi, na fedha zao zikaisha. Wangeiishije? Ndugu huyo alisali kwa Yehova apate msaada. Alipokuwa akimaliza kusali, Shahidi mwenzi alibisha mlango. Walienda nje pamoja kunywa kahawa. Ndugu huyo aliporudi, alipata meza ya jikoni imejaa vyakula na vitu vingine. Pamoja na vitu hivyo ilikuwako bahasha mlimokuwa fedha na taarifa iliyosema hivi: “Kutoka kwa ndugu na dada zenu, wawapendao sana sana.” Kutaniko lilikuwa limepata kujua uhitaji wao, nao wote walikuwa wameshiriki kuutimiza. Kwa kuguswa sana moyo na upendo wao, yeye na mke wake hawangeweza kujizuia wasitoe machozi na kumshukuru Yehova, ambaye kielelezo chake cha upendo husukuma watumishi wake.
Hangaikio lenye ukarimu ambalo Mashahidi wa Yehova huonyesha wale miongoni mwao ambao hupatwa na uhitaji limepata kujulikana sana. Nyakati nyingine, wadanganyi wamejifaidi nalo. Hivyo Mashahidi wamelazimika kujifunza kuwa wenye hadhari, na wakati huohuo kutokandamiza tamaa yao ya kusaidia wastahilio.
Wakati Vita Inapoacha Watu Wakiwa Maskini
Katika sehemu nyingi za dunia, watu wameachwa katika umaskini kama tokeo la vita. Mashirika ya kupunguza shida hujaribu kuandaa msaada, lakini mara nyingi mfumo wayo wa kutenda hufanya kazi polepole. Mashahidi wa Yehova hawachukui maoni ya kwamba kazi ifanywayo na mashirika hayo huwaondolea daraka kuelekea ndugu zao Wakristo katika maeneo hayo. Wanapopata kujua kwamba ndugu zao wana uhitaji, wao ‘hawawazuilii hao huruma zao’ bali mara hiyo wao hufanya wawezayo kuwaletea kitulizo.—1 Yoh. 3:17, 18.
Wakati wa Vita ya Ulimwengu 2, hata ndani ya nchi zilizokuwa zimesongwa sana na upungufu mbalimbali, Mashahidi katika sehemu za mashambani waliokuwa wangali wana ugavi wa chakula waliushiriki na wale ndugu wasiokuwa katika hali nzuri majijini. Katika Uholanzi hilo lilifanywa katika hali ya hatari kubwa kwa sababu ya vizuizi vikali vilivyowekwa na Wanazi. Alipokuwa katika shughuli kama hiyo ya kupeleka vitulizo katika pindi moja, Gerrit Böhmermann alikuwa akiongoza kikundi cha akina ndugu wakiendesha baiskeli za usafirishaji zilizokuwa zimepakiwa vyakula vilivyofunikwa kwa vyandarua. Ghafula wakaja kwenye kituo cha ukaguzi katika jiji la Alkmaar. “Hakukuwa na la kufanya ila kumtumaini Yehova,” akasema Gerrit. Bila kupunguza sana mwendo, alipaaza sauti kwa ofisa: “Wo ist Amsterdam?” (Njia ni ipi ya kwenda Amsterdam?) Yule ofisa akaenda kando na kuelekeza mbele huku akipaaza sauti: “Geradeaus!” (Moja kwa moja, mbele!) “Danke schön!” (Asante!) lilikuwa ndilo jibu la Gerrit huku msafara wote wa baiskeli za usafirishaji ukipita kwa mwendo wa kasi kabisa na umati wenye kushangaa ukitazama. Katika pindi nyingine, Mashahidi walifaulu kuletea ndugu zao katika Amsterdam shehena nzima ya viazi kwa njia ya mashua.
Mlemle ndani ya kambi za mateso katika Ulaya, roho hiyo ilionyeshwa na Mashahidi wa Yehova. Alipokuwa amefungwa katika kambi moja karibu na Amersfoort, Uholanzi, kijana mmoja wa miaka 17 alipoteza uzani mpaka akawa mifupa mitupu. Lakini katika miaka ya baadaye, hakusahau kamwe kwamba baada ya kulazimishwa kufanya mazoezi katika mvua yenye kunya mpaka katikati ya usiku kisha kunyimwa chakula, Shahidi mmoja kutoka sehemu nyingine ya kambi aliweza kumfikia na kutia kipande cha mkate mkononi mwake. Na katika kambi ya mateso ya Mauthausen katika Austria, Shahidi mmoja ambaye mgawo wake ulimtaka kwenda kutoka sehemu moja ya kambi hadi nyingine alihatirisha maisha yake mara nyingi kwa kuchukua chakula ambacho Mashahidi walikuwa wameokoa kutoka vipimo vyao vidogo kupelekea Mashahidi wengine ambao walikuwa wakinyimwa chakula zaidi.
Kufuatia vita, Mashahidi wa Yehova walioibuka kutoka magereza na kambi za mateso za Ujerumani hawakuwa na chochote ila lile vazi la gereza walilokuwa wamevaa. Mali za wengi wasiokuwa gerezani zilikuwa zimeharibiwa kabisa. Chakula, nguo, na mafuta vilikuwa vichache katika sehemu kubwa ya Ulaya. Upesi Mashahidi wa Yehova katika nchi hizo walipanga kitengenezo mikutano ya kutaniko na kuanza kusaidia wengine kiroho kwa kushiriki pamoja nao habari njema za Ufalme wa Mungu. Lakini wao wenyewe walihitaji msaada katika njia nyinginezo. Wengi wao walikuwa dhaifu sana kutokana na njaa hivi kwamba mara nyingi walizimia wakati wa mikutano.
Hiyo ilikuwa hali ambayo Mashahidi hawakuwa wametangulia kukabili kwa kadiri kubwa jinsi hiyo. Hata hivyo, mwezi uleule ambao vita ilikwisha kirasmi katika eneo la Pasifiki, Mashahidi wa Yehova walifanya mkusanyiko wa pekee katika Cleveland, Ohio, ambao katika huo walizungumza kuhusu jambo lililohitaji kufanywa ili kuandaa kitulizo kwa ajili ya ndugu zao Wakristo katika nchi zilizoharibiwa na vita na jinsi ya kutekeleza jambo hilo. Ile hotuba yenye kuchangamsha moyo “Zawadi Yake Isiyoelezeka,” iliyotolewa na F. W. Franz, ilitoa shauri la Kimaandiko ambalo lilitimiza kabisa mahitaji ya hali hiyo.b
Katika muda wa majuma machache, mara tu usafiri katika eneo hilo uliporuhusiwa, N. H. Knorr, msimamizi wa Watch Tower Society, na M. G. Henschel walisafiri kwenda Ulaya ili kujionea wenyewe hali. Hata kabla ya kuondoka ili waanze safari hiyo mipango ya msaada ilikuwa imeanzishwa.
Shehena za mapema zilisafirishwa kutoka Uswisi na Sweden. Shehena zaidi zilifuata kutoka Kanada, Marekani, na nchi nyinginezo. Ijapokuwa idadi ya Mashahidi katika nchi ambazo zilikuwa katika hali ya kuweza kuandaa msaada kama huo wakati ule ilikuwa karibu 85,000, walijichukulia daraka la kupeleka nguo na chakula kwa Mashahidi wenzao katika Austria, Bulgaria, Chekoslovakia, China, Denmark, Filipino, Finland, Hungaria, Italia, Norway, Poland, Rumania, Ubelgiji, Ufaransa, Ugiriki, Uholanzi, Uingereza na Ujerumani. Hiyo haikuwa jitihada ya pindi moja. Shehena za msaada ziliendelea kwa miaka miwili na nusu. Kati ya Januari 1946 na Agosti 1948, walipeleka kilo 479,114 za nguo, jozi 124,110 za viatu, na kilo 326,081 za chakula zikiwa zawadi kwa Mashahidi wenzao. Hapana zozote za fedha hizo zilizotumiwa kwa ajili ya gharama za usimamizi. Kazi ya kupanga kulingana na aina na kupakia ilifanywa na wenye kujitolea wasiolipwa. Fedha zilizochangwa zote zilitumiwa kusaidia watu ambao zilikusudiwa.
Bila shaka, uhitaji wa kitulizo kwa wakimbizi na kwa wengine walioachwa na vita wakiwa maskini haukukoma huko nyuma katika miaka ya 1940. Kumekuwako mamia ya vita tangu 1945. Na hangaikio lilelile lenye upendo limeendelea kuonyeshwa na Mashahidi wa Yehova. Hangaikio hilo lilionyeshwa katika na baada ya ile vita ya Biafra katika Nigeria, tokea 1967 hadi 1970. Msaada kama huo uliandaliwa katika Msumbiji wakati wa miaka ya 1980.
Katika Liberia pia, kulikuwa njaa kuu ikiwa tokeo la vita iliyoanza katika 1989. Watu walipokuwa wakikimbia, ua wa Watch Tower katika Monrovia ulijaa mamia ya wakimbizi. Mashahidi walishiriki pamoja na majirani wasio Mashahidi chakula chochote kilichopatikana humo, na pia maji kutoka kisimani. Kisha, mara tu hali ziliporuhusu, ugavi zaidi wa msaada ukaja kutoka kwa Mashahidi katika Sierra Leone na Côte d’Ivoire katika Afrika Magharibi, Uholanzi na Italia katika Ulaya, na Marekani.
Kwa mara nyingine tena, katika 1990, baada ya vita katika Lebanoni kuacha sehemu za Beirut zikionekana kama kwamba zimepigwa na tetemeko la dunia, wazee miongoni mwa Mashahidi wa Yehova walipanga halmashauri ya kushughulikia utoaji wa kitulizo cha dharura ili kutoa msaada uliohitajiwa kwa akina ndugu. Hawakuwajibika kuuliza wenye kujitolea waje; kila siku wengi walitoa msaada wao.
Wakati wa pindi ya msukosuko mkubwa wa kisiasa na kiuchumi katika Ulaya, Mashahidi wa Yehova katika Austria, Chekoslovakia, Hungaria, na Yugoslavia walipelekea ndugu zao Wakristo katika Rumania tani zaidi ya 70 za vitu vyenye kuhitajiwa katika 1990.
Hiyo ilifuatwa na shughuli zaidi za kutoa vitulizo katika Ulaya Mashariki. Baraza Linaloongoza liliomba ofisi ya tawi ya Watch Tower Society katika Denmark kupanga utolewaji wa vitulizo kwa ajili ya Mashahidi wenye uhitaji katika Ukrainia. Makutaniko yalijulishwa nayo yalikuwa na hamu ya kushiriki. Katika Desemba 18, 1991, malori makubwa matano na mawili madogo yakiendeshwa na Mashahidi wenye kujitolea yalifika Lviv yakiwa na tani 22 za ugavi—wonyesho wa hangaikio lenye upendo kwa ndugu zao Wakristo. Msaada ukiendelea kuingia katika mwaka wa 1992, shehena ziliwasili pia kutoka kwa Mashahidi katika Austria—zaidi ya tani 100 za chakula na nguo. Ugavi zaidi ulipelekwa kutoka kwa Mashahidi katika Uholanzi—kwanza tani 26 za chakula, kisha msafara wa malori 11 yakiwa na nguo, kisha chakula zaidi ili kukabiliana na uhitaji wenye kuendelea. Wapokeaji walishukuru Mungu nao walimtegemea awape hekima katika kutumia vitu walivyokuwa wameandaliwa. Waliungana katika sala kabla ya kupakua malori hayo, na tena wakati kazi ilipokuwa imekwisha fanywa. Shehena nyingine kubwa za vitulizo zilipelekwa na Mashahidi katika Italia, Finland, Sweden, na Uswisi. Wakati yote hayo yalipokuwa yakiendelea, hali zenye msukosuko miongoni mwa jamhuri zilizojumuika hapo kwanza kufanyiza Yugoslavia zilitokeza uhitaji huko. Ugavi wa chakula, nguo, na dawa ulipelekwa pia katika eneo hilo. Wakati uleule, Mashahidi katika majiji huko walifungua makao yao ili kutunza wale ambao makao yao yalikuwa yameharibiwa.
Nyakati nyingine wale wanaohitaji msaada haraka sana huwa wako sehemu za pekee za mbali, na hali yao haijulikani sana. Ndivyo ilivyokuwa kwa familia 35 za Mashahidi wa Yehova katika Guatemala. Vijiji vyao vilikuwa vimevamiwa na vikundi vyenye kupigana. Wakati walipoweza kurudi hatimaye katika 1989, walihitaji msaada ili kujenga upya. Ili kuongezea msaada uliotolewa na serikali kwa wenye kurudi, ofisi ya tawi ya Watch Tower Society iliunda halmashauri ya dharura ili kusaidia familia hizo za Mashahidi, na Mashahidi wengine kama 500 kutoka makutaniko 50 walijitolea kusaidia kazi ya kujenga upya.
Kuna hali nyingine ambazo pia huingiza watu katika uhitaji mkubwa pasipo wao wenyewe kuwa na kosa. Matetemeko ya dunia, vimbunga, na mafuriko hutukia mara nyingi. Yasemekana kwamba, kwa wastani, ulimwengu hupigwa na misiba mikubwa zaidi ya 25 kila mwaka.
Wakati Kani za Asili Zinapopiga Vikali
Wakati dharura mbalimbali zenye kuathiri Mashahidi wa Yehova zinapotokea kwa sababu ya misiba, hatua za mara hiyo huchukuliwa ili kuandaa usaidizi unaohitajiwa. Wazee wenyeji wamejifunza kwamba wakabiliwapo na hali kama hizo, wapaswa kujitahidi kwa bidii kuwasiliana na kila mmoja katika kutaniko. Ofisi ya tawi ya Watch Tower Society ambayo husimamia kazi ya Ufalme katika eneo hilo hukagua hali bila kukawia kisha hutoa ripoti kwa makao makuu ya ulimwengu. Msaada zaidi unapohitajiwa kuliko ule unaoweza kuandaliwa na mahali hapo, mipango iliyoratibiwa kwa uangalifu hufanywa, nyakati nyingine hata kwa kadiri ya kimataifa. Lengo si kujaribu kuinua hali ya maisha ya wale walioathiriwa bali kuwasaidia wapate mahitaji ya lazima ya maisha kama yale waliyozoea kuwa nayo.
Ripoti tu juu ya msiba katika televisheni yatosha kusukuma Mashahidi wengi wapigie simu wazee wenye daraka katika eneo hilo ili kutoa utumishi wao au kuandaa fedha au vifaa. Huenda wengine wakapeleka fedha kwenye ofisi ya tawi au kwenye makao makuu ya ulimwengu ili zitumiwe kwa makusudi ya kutoa kitulizo. Wanajua kwamba msaada wahitajiwa, nao wanataka kushiriki. Kunapokuwa na uhitaji mkubwa zaidi, Watch Tower Society yaweza kujulisha akina ndugu katika eneo fulani ili waweze kusaidia kadiri wawezavyo. Halmashauri ya kushughulikia utoaji wa kitulizo huundwa ili kuratibu shughuli za mambo katika eneo lenye msiba.
Hivyo, wakati sehemu iliyo kubwa ya Managua, Nikaragua, ilipopigwa na tetemeko la dunia katika Desemba 1972, waangalizi wa makutaniko ya Mashahidi wa Yehova katika eneo hilo walikutana katika muda wa saa chache ili kuratibu jitihada zao. Ukaguzi wa mara hiyo ulifanywa kwa habari ya hali njema ya kila Shahidi jijini. Siku iyo hiyo ugavi wa vitulizo ulianza kuwasili kutoka makutaniko ya karibu; kisha upesi ukatoka Kosta Rika, Honduras, na El Salvador. Vituo 14 vya kugawanyia vitulizo vilianzishwa katika viunga vya Managua. Fedha na ugavi kutoka kwa Mashahidi katika sehemu nyingi za dunia vilielekezwa kuingia Nikaragua kupitia makao makuu ya kimataifa ya Watch Tower Society. Chakula na ugavi mwingine (kutia mishumaa, viberiti, na sabuni) viligawanywa kulingana na ukubwa wa kila familia, kila familia ikipewa ugavi wa siku saba. Kwenye upeo wa shughuli hizo, watu 5,000 hivi—Mashahidi, familia zao, na watu wa ukoo waliokuwa wakikaa nao—walikuwa wakipewa chakula. Shughuli hizo za kutoa msaada ziliendelea kwa miezi kumi. Walipoona yaliyokuwa yakifanywa, mashirika ya serikali pamoja na Shirika la Msalaba Mwekundu pia walitoa chakula, mahema, na ugavi mwingine ulioweza kupatikana.
Katika 1986, wakati milipuko ya volkano ilipolazimisha kuhamishwa kwa watu kama 10,000 kutoka kisiwa cha Izu-Oshima, karibu na pwani ya Japani, mashua zenye kubeba wakimbizi zililakiwa na Mashahidi wa Yehova ambao walitafuta ndugu zao za kiroho kwa bidii-nyendelevu. Mhamishwa mmoja alisema: “Tulipoondoka Oshima, sisi wenyewe hatukujua tulikokuwa tukienda.” Mambo yote yalikuwa yametukia haraka sana. “Hata hivyo, tulipokuwa tukishuka kutoka mashuani, tuliona ishara ikisema, ‘Mashahidi wa Yehova.’ . . . Machozi yakatoka machoni pa mke wangu kwa kushindwa na hisia za utulizo wa kupata ndugu zetu wakitulaki gatini.” Baada ya kuona jinsi wahamishwa Mashahidi walivyotunzwa, si wakati wa kuwasili tu bali pia na baada ya hapo, hata watu ambao walikuwa hapo kwanza wamewalaani walisema: “Mlifanya vema kushikamana na dini hiyo.”
Kila jitihada hufanywa na Mashahidi kupeleka msaada katika maeneo yenye misiba upesi iwezekanavyo. Katika 1970, wakati Peru ilipopigwa na tetemeko la dunia lililo baya zaidi katika historia yayo, fedha za kitulizo cha dharura zilipelekwa haraka kutoka makao makuu ya ulimwengu katika New York, na tani 15 za nguo zikafuata. Hata hivyo kabla ya shehena hiyo kufika, Mashahidi walikuwa wameendesha msafara wa magari yakiwa na ugavi wa vitulizo katika maeneo ambayo majiji na vijiji vilikuwa vimeharibiwa, wakifanya hivyo katika muda wa saa chache baada ya barabara kufunguliwa. Kwa kuendelea katika siku na majuma yaliyofuata, waliandalia vikundi mbalimbali vilivyo juu katika milima Andes msaada uliohitajiwa kimwili na kiroho. Na, katika 1980, wakati sehemu za Italia zilipotikiswa na tetemeko la dunia kali wakati wa jioni ya Novemba 23, ugavi wa kwanza wa malori yaliyojaa shehena uliopelekwa na Mashahidi uliwasili siku iliyofuata katika eneo lililopatwa na pigo. Mara hiyo walitengeneza jiko lao wenyewe, ambapo kutoka hapo chakula kilichopikwa na akina dada kiligawanywa kila siku. Mtazamaji mmoja wa kazi ya kutoa vitulizo katika kisiwa kimoja cha Karibea alisema hivi: “Mashahidi walifanya kazi haraka zaidi ya serikali.” Labda hiyo ni kweli nyakati nyingine, lakini hakika Mashahidi wa Yehova huthamini msaada wa maofisa ambao hurahisisha jitihada zao za kufikia haraka maeneo kama hayo yenye msiba.
Wakati wa pindi ya njaa kuu katika Angola katika 1990, ilipata kujulikana kwamba Mashahidi huko walikuwa katika uhitaji mkubwa wa chakula na nguo. Hata hivyo, kuwafikia kungekuwa tatizo kwa sababu Mashahidi wa Yehova walikuwa wamepigwa marufuku kwa miaka mingi katika nchi hiyo. Hata hivyo, ndugu zao Wakristo katika Afrika Kusini walipakia tani 25 za ugavi wa vitulizo katika lori. Wakiwa njiani walitembelea ubalozi wa Angola nao wakapewa ruhusa wavuke mpaka. Ili wafikie akina ndugu, ilikuwa lazima wapite vizuizi 30 vya barabarani vya kijeshi, na mahali ambapo daraja lilikuwa limelipuliwa, iliwalazimu kuvuka mto uliofurika kupitia kivukio cha muda kilichokuwa kimejengwa mahali palo. Yajapokuwa hayo yote, shehena yote ilifikishwa salama.
Katika nyakati za msiba, mengi zaidi hufanywa kuliko tu kusafirisha ugavi wa vitulizo kwenye eneo. Wakati milipuko na moto vilipoteketeza eneo moja katika kiunga cha Jiji la Mexico katika 1984, Mashahidi waliwasili upesi ili kuandaa msaada. Lakini Mashahidi wengi katika eneo hilo hawangeweza kujulikana walikokuwa, hivyo wazee walipanga jitihada ya kutafuta kwa utaratibu ili kujua mahali kila mmoja aliko. Baadhi yao walikuwa wametawanyika hadi maeneo mengine. Hata hivyo, wazee waliendelea mpaka walipojua mahali wote waliko. Usaidizi ulitolewa kulingana na kilichohitajiwa. Katika kisa cha dada mmoja ambaye mume na mwana wake walikuwa wamekufa, hiyo ilihusu kushughulikia mipango ya maziko na kisha kuandaa utegemezo kamili, kimwili na kiroho, kwa ajili ya dada huyo na watoto wake waliobaki.
Msaada unaohitajiwa mara nyingi ni zaidi ya ugavi wa kitiba, milo michache, na nguo fulani. Katika 1989 tufani moja iliharibu kabisa makao 117 ya Mashahidi katika Guadeloupe na kuharibu sana makao mengine 300. Mashahidi wa Yehova katika Martinique wakaja upesi kuwasaidia; kisha Mashahidi katika Ufaransa walisafirisha tani zaidi ya 100 za vifaa vya ujenzi vikiwa zawadi ili kuwasaidia. Katika kisiwa cha St. Croix, wakati Shahidi mmoja aliyekuwa amepoteza kao lake alipowaambia wafanyakazi wenzake kwamba Mashahidi wenzake walikuwa wakija kutoka Puerto Riko kusaidia, walisema: “Hawatakufanyia lolote. Wewe ni mweusi, si Mhispania kama wao.” Lo! ulikuwa mshangao kama nini kwa wafanyakazi hao wenzi wakati upesi dada huyo alipokuwa na nyumba mpya kabisa! Kufuatia tetemeko la dunia katika Kosta Rika katika 1991, Mashahidi wenyeji na wenye kujitolea wa kimataifa walifanya kazi pamoja ili kusaidia Mashahidi wenzao katika eneo lenye msiba. Bila kutazamia kulipwa chochote, walijenga upya makao 31 na Majumba ya Ufalme 5 na kurekebisha mengine. Watazamaji walisema: ‘Vikundi vingine husema juu ya upendo; nyinyi mwauonyesha.’
Njia zenye matokeo ambazo kwazo jitihada za kutoa kitulizo zimetekelezwa na Mashahidi wa Yehova mara nyingi hushangaza watazamaji. Katika California, Marekani, katika 1986, ukingo kwenye Mto Yuba ulibomoka nayo maji ya furiko yakalazimisha makumi ya maelfu ya watu kuyaacha makao yao. Wazee Wakristo katika eneo hilo waliwasiliana na makao makuu katika New York, nayo halmashauri ya kushughulikia utoaji wa kitulizo ikaundwa. Mara tu maji yalipoanza kupungua, mamia ya wenye kujitolea walikuwa tayari kufanya kazi. Kabla ya mashirika ya kilimwengu ya kutoa msaada hayajaweza kuanza, makao ya Mashahidi yalikuwa tayari yakirekebishwa. Kwa nini waliweza kutenda kwa haraka hivyo?
Jambo kuu lilikuwa ule moyo wa kupenda wa Mashahidi wa kujitolea mara hiyo bila malipo, pamoja na kutoa kwao upaji wa vifaa vyenye kuhitajiwa. Jambo jingine lilikuwa kwamba walikuwa na ujuzi katika kupanga na kufanya kazi pamoja, kwa kuwa wao hufanya hivyo kwa ukawaida ili kuendesha mikusanyiko yao na kujenga Majumba ya Ufalme mapya. Jambo jingine muhimu ni kwamba wamefikiria sana yale ambayo Biblia humaanisha wakati inaposema, “Iweni na upendo wenye juhudi nyingi.”—1 Pet. 4:8, NW.
Michango ambayo hutolewa ili kutimiza mahitaji hayo mara nyingi hutoka kwa watu mmoja-mmoja ambao wana vitu vichache sana wao wenyewe. Kama vile barua zao zenye kuandamana mara nyingi husema: ‘Zawadi hii ni ndogo, lakini moyo wetu wote waendea dada na ndugu zetu.’ ‘Tamaa yangu ni kupeleka zaidi, lakini kile ambacho Yehova ameniruhusu niwe nacho nataka kushiriki.’ Kama Wakristo wa karne ya kwanza katika Makedonia, wao huomba kwa bidii wapewe pendeleo la kushiriki katika kuandaa mahitaji ya lazima ya maisha kwa wale ambao wamekuwa wahitaji. (2 Kor. 8:1-4) Wakati Wakorea zaidi ya 200,000 walipoachwa bila makao kama tokeo la furiko katika 1984, Mashahidi wa Yehova katika Jamhuri ya Korea waliitikia kwa ukarimu sana hivi kwamba ofisi ya tawi ililazimika kujulisha kwamba msaada zaidi haukuhitajiwa.
Watazamaji wanaweza kuona kwa urahisi kwamba jambo fulani zaidi ya hisi za kuwa na daraka au ubinadamu wa kawaida huchochea Mashahidi. Wao kwelikweli wapenda ndugu na dada zao Wakristo.
Kuongezea kutunza mahitaji ya kimwili, Mashahidi wa Yehova hutoa uangalifu wa pekee kwa mahitaji ya kiroho ya ndugu zao katika maeneo yenye msiba. Mipango hufanywa vivyo hivyo upesi kwa kadiri iwezekanayo ili mikutano ya kutaniko ianze tena. Katika Ugiriki, katika 1986, hema kubwa ilihitajiwa nje ya jiji la Kalamata litumiwe kama Jumba la Ufalme, na mengine madogo kwenye sehemu mbalimbali kwa ajili ya Mafunzo ya Kitabu ya Kutaniko katikati ya juma. Vivyo hivyo, baada ya mahitaji ya kimwili ya waokokaji wa poromoko la tope lenye kuharibu sana katika Armero, Kolombia, katika 1985, yalipokuwa yameshughulikiwa, fedha zilizobaki zilitumiwa kujenga Majumba ya Ufalme mapya kwa ajili ya makutaniko matatu katika eneo hilo.
Hata wakati kazi kama hiyo ya kujenga tena inapokuwa ikiendelea, Mashahidi wa Yehova huendelea kufariji wengine kwa majibu yenye kutosheleza ambayo Neno la Mungu hutoa kwa maswali yao juu ya kusudi la uhai, sababu ya misiba na kifo, na tumaini la wakati ujao.
Jitihada za kutoa kitulizo za Mashahidi hazikusudiwi kutosheleza mahitaji ya kimwili ya kila mtu katika eneo lenye msiba. Kulingana na Wagalatia 6:10 (NW) hizo hukusudiwa kwanza kabisa kwa ajili ya ‘wale ambao katika imani ni jamaa zetu.’ Wakati uo huo, wao husaidia kwa furaha wengine kadiri wawezavyo. Kwa kielelezo, wamefanya hivyo, wakati walipokuwa wakiandaa chakula kwa ajili ya waliopatwa na maafa ya tetemeko la dunia katika Italia. Katika Marekani, walipokuwa wakisaidia waliopatwa na maafa ya furiko na tufani, wamesafisha na kurekebisha pia makao ya majirani wa Mashahidi wenye kusumbuka. Waulizwapo kwa nini wangefanya matendo kama hayo ya fadhili kwa watu wasiowajua, wao hujibu tu kwamba wao wanapenda majirani wao. (Mt. 22:39) Kufuatia kimbunga chenye kuleta uharibifu katika kusini mwa Florida, Marekani, katika 1992, programu ya kutoa vitulizo yenye mipango mizuri ya Mashahidi ilijulikana vizuri sana hivi kwamba baadhi ya mashirika ya kibiashara na watu mmoja-mmoja ambao hawakuwa Mashahidi na ambao walitaka kutoa upaji mkubwa wa ugavi wa vitulizo waliwapa Mashahidi ugavi huo. Wao walijua kwamba zawadi yao haingeachwa tu irundamane, wala haingetumiwa ili kupata faida, bali ingewanufaisha kikweli wale waliokumbwa na kimbunga, Mashahidi na wasio-Mashahidi pia. Moyo wao wa kupenda kusaidia wasio-Mashahidi katika wakati wa msiba ulithaminiwa sana katika Davao del Norte, katika Filipino, hivi kwamba maofisa wa mji walipitisha azimio la kusema hivyo.
Hata hivyo, si kila mtu anayependa Wakristo wa kweli. Mara nyingi, wao huwa shabaha ya mnyanyaso mkali. Hali hiyo, pia, huleta mmiminiko wa ukarimu wa utegemezo wenye upendo kwa Wakristo wenzi.
Wakati wa Kukabili Mnyanyaso Wenye Ukatili
Mtume Paulo alilinganisha kutaniko la Kikristo na mwili wa kibinadamu, akasema: “Viungo vyao viwe na utunzaji uleule kimoja na chenzake. Na kiungo kimoja kikiteseka, viungo vingine vyote huteseka pamoja nacho.” (1 Kor. 12:25, 26, NW) Hivyo ndivyo Mashahidi wa Yehova huitikia wakati wanaposikia ripoti juu ya mnyanyaso wa ndugu zao Wakristo.
Katika Ujerumani wakati wa enzi ya Nazi, serikali ilichukua hatua kali za kukandamiza Mashahidi wa Yehova. Kulikuwa na Mashahidi kama 20,000 tu katika Ujerumani wakati ule, ambao kidogo walikuwa wachache waliodharauliwa na Hitler. Tendo la pamoja lilihitajiwa. Katika Oktoba 7, 1934, kila kutaniko la Mashahidi wa Yehova kotekote katika Ujerumani lilikutana kwa siri, likasali pamoja, na kupelekea serikali barua iliyotaarifu azimio lao la kuendelea kutumikia Yehova. Kisha wengi miongoni mwa wale waliohudhuria walitoka kwa ujasiri kwenda kutoa ushahidi kwa majirani wao juu ya jina na Ufalme wa Yehova. Siku iyo hiyo, Mashahidi wa Yehova kotekote katika sehemu nyingine za dunia walikutana pia katika makutaniko yao na, baada ya sala ya pamoja, walipelekea serikali ya Hitler barua ya kebo katika kuunga mkono ndugu zao Wakristo.
Katika 1948, baada ya mnyanyaso uliochochewa na makasisi juu ya Mashahidi wa Yehova katika Ugiriki kufichuliwa, rais wa Ugiriki na mawaziri mbalimbali wa serikali walipokea maelfu ya barua kutoka kwa Mashahidi wa Yehova kwa niaba ya ndugu zao Wakristo. Hizo zilitoka Filipino, Australia, Amerika ya Kaskazini na Kusini, na maeneo mengine.
Wakati gazeti Amkeni! lilipofichua njia za mabaraza ya kuhukumia wazushi wa kidini zilizokuwa zikitumiwa dhidi ya Mashahidi katika Hispania katika 1961, barua za kupinga ziligharikisha wenye mamlaka huko. Maofisa walishtuka kujua kwamba watu ulimwenguni pote walijua barabara waliyokuwa wakifanya, na kama tokeo, hata ingawa mnyanyaso uliendelea, baadhi ya polisi walianza kushughulika na Mashahidi kwa njia ya kujizuia zaidi. Katika nchi mbalimbali za Afrika pia, maofisa wamesikia kutoka kwa Mashahidi katika sehemu nyinginezo nyingi za ulimwengu wakati walipopata kujua kwamba ndugu na dada zao Wakristo huko walikuwa wakitendwa kikatili.
Ikiwa itikio zuri haliji kutoka kwa serikali, Mashahidi wenye kunyanyaswa hawasahauliwi. Kwa sababu ya kuendelea katika mnyanyaso wa kidini kwa miaka mingi, baadhi ya serikali zimegharikishwa tena na tena kwa barua za kusihi na za kuteta. Ndivyo ilivyokuwa kwa habari ya Argentina. Katika pindi moja katika 1959, katibu wa Wizara ya Mambo ya Nchi za Kigeni na Dini alimpeleka mmoja wa ndugu zetu katika chumba kimoja ambamo masanduku kadhaa ya vitabu yalijaa barua zilizokuwa zimemiminika kwa wingi kutoka kotekote ulimwenguni. Alishangaa kwamba mtu fulani aliye mbali sana kama vile Fiji angeweza kuandika akiomba kuwe na uhuru wa ibada katika Argentina.
Katika visa fulani uhuru zaidi umetolewa wakati watawala walipopata kujua kwamba watu ulimwenguni pote walijua waliyokuwa wakifanya na kwamba kulikuwa wengi waliojali kwelikweli. Ndivyo ilivyokuwa katika Liberia katika 1963. Wajumbe wa mkusanyiko katika Gbarnga walikuwa wametendwa vibaya sana na majeshi ya serikali. Rais wa Liberia aligharikishwa na barua za kuteta kutoka kote ulimwenguni, nayo Idara ya Serikali ya Marekani iliingilia mambo kwa sababu raia wa Marekani alihusika. Hatimaye, Rais Tubman alipeleka telegramu kwa makao makuu ya Watch Tower Society akionyesha nia ya kupokea ujumbe wa Mashahidi wa Yehova ili kuzungumza mambo. Wawili katika ujumbe huo—Milton Henschel na John Charuk—walikuwa katika Gbarnga. Bw. Tubman alikubali kwamba lililokuwa limetukia lilikuwa “jambo baya sana” na kusema: “Nasikitika jambo hilo lilitukia.”
Kufuatia mahoji hayo, Amri ya Serikali ilitolewa ikijulisha “watu wote kotekote nchini, kwamba Mashahidi wa Yehova watakuwa na haki na pendeleo la kufikia sehemu yoyote ya nchi bila kizuizi ili kuendeleza kazi yao ya kimishonari na ibada ya kidini bila kusumbuliwa na yeyote. Watakuwa na ulinzi wa sheria juu yao wao binafsi na mali zao pia na haki ya kuabudu Mungu kwa uhuru kulingana na miongozo ya dhamiri zao, wakati uleule wakishika sheria za Jamhuri kwa kuonyesha staha kwa bendera ya taifa wakati inapopandishwa au kuteremshwa kwenye sherehe kwa kusimama wima.” Lakini hawakutakwa kuisalimu, wahalifu dhamiri yao ya Kikristo.
Hata hivyo, kufikia 1992, tangazo kama hilo rasmi halikuwa limetoka Malawi ingawa jeuri dhidi ya Mashahidi huko imepungua kwa kadiri kubwa. Mashahidi wa Yehova wamekuwa wakipatwa na mmojawapo minyanyaso ya kidini yenye ukatili zaidi katika historia ya Afrika. Wimbi moja la mnyanyaso kama huo lilienea nchini katika 1967; jingine lilianza mapema katika miaka ya 1970. Makumi ya maelfu ya barua ziliandikwa kwa niaba yao kutoka sehemu zote za ulimwengu. Simu zilipigwa. Barua za kebo zilitumwa. Kwa msingi wa ubinadamu watu wengi mashuhuri wa ulimwengu walisukumwa kuteta.
Unyama ulikuwa mbaya sana hivi kwamba kama 19,000 kati ya Mashahidi wa Yehova na watoto wao walikimbia kuvuka mpaka kwenda Zambia katika 1972. Makutaniko ya karibu ya Mashahidi katika Zambia yalikusanya chakula na mablanketi upesi kwa ajili ya ndugu zao. Fedha na vifaa vilivyochangwa na Mashahidi wa Yehova ulimwenguni pote vilimiminika kwenye ofisi za tawi za Watch Tower nazo zilielekezwa kwa wakimbizi na ofisi ya makao makuu katika New York. Vitu vya kutosha na kuzidi vilimiminika ili kutosheleza mahitaji yote ya wakimbizi katika kambi kwenye Sinda Misale. Habari zilipokuwa zikienea kotekote kambini kuhusu kuwasili kwa malori yenye kubeba chakula, nguo, na vyandarua ili kuandaa vitu vya kujifunikia, ndugu wa Malawi hawakuweza kujizuia kutokwa na machozi ya shangwe kwa sababu ya uthibitisho huo wa upendo wa ndugu zao Wakristo.
Wakati wengine kati yao wanapozuiwa kifungoni, Mashahidi wenzao hawawaachi, hata inapohusu hasara ya kibinafsi. Wakati wa marufuku katika Argentina, kikundi cha Mashahidi kilipozuiwa kwa muda wa saa 45, Mashahidi wengine wanne waliwaletea chakula na nguo, nao vilevile walitiwa gerezani. Katika 1989 mke wa mwangalizi wa mzunguko katika Burundi, alipopata kujua hali mbaya ya ndugu zake Wakristo, alijaribu kuwapelekea chakula gerezani. Lakini yeye mwenyewe alikamatwa na kuzuiwa akiwa mateka kwa majuma mawili, kwa sababu polisi walikuwa wakijaribu kumnasa mume wake.
Pamoja na yoyote wawezayo kufanya katika njia hizo zote, kupenda ndugu zao Wakristo husukuma Mashahidi wa Yehova wainue sauti zao katika sala kumpelekea Mungu kwa niaba yao. Wao hawasali Mungu akomeshe mara hiyo vita na upungufu wa chakula kwa sababu Yesu Kristo alitabiri mambo hayo kwa wakati wetu. (Mt. 24:7) Wala hawasali ili Mungu azuie mnyanyaso wote, kwa sababu Biblia hutaarifu waziwazi kwamba Wakristo wa kweli watanyanyaswa. (Yn. 15:20; 2 Tim. 3:12) Lakini wao huomba kwa bidii kwamba ndugu na dada zao Wakristo watiwe nguvu ili wasimame imara katika imani katika kuelekeana na gumu lolote liwajialo. (Linganisha Wakolosai 4:12.) Mambo ya hakika yakishuhudia nguvu zao za kiroho hutoa uthibitisho mwingi kwamba sala hizo zimejibiwa.
[Maelezo ya Chini]
a Ona Mnara wa Mlinzi, Machi 1, 1981, kurasa 10-17; Oktoba 15, 1986, kurasa 10-21; Juni 1, 1987, kurasa 4-18; Julai 15, 1988, kurasa 21-23; Machi 1, 1990, kurasa 20-22.
b Ona Mnara wa Mlinzi, (Kiingereza) Desemba 1, 1945, kurasa 355-363.
[Blabu katika ukurasa wa 305]
Kushughulikia visa vya uhitaji wa pekee hakuachiwi nasibu
[Blabu katika ukurasa wa 307]
Msaada ambao hutokana na hangaikio la binafsi lenye upendo
[Blabu katika ukurasa wa 308]
Kutosheleza uhitaji mkubwa wa kitulizo
[Blabu katika ukurasa wa 312]
Jitihada ya kutafuta kwa utaratibu ili kujua aliko kila Shahidi katika eneo lenye msiba
[Blabu katika ukurasa wa 315]
Kuwatendea mema wasio-Mashahidi pia
[Blabu katika ukurasa wa 317]
Machozi ya shangwe kwa sababu ya upendo ulioonyeshwa na ndugu zao Wakristo
[Sanduku katika ukurasa wa 309]
“Nyinyi Mwapendana Kwelikweli”
Baada ya kutazama Mashahidi wenye kujitolea katika Lebanoni yenye kusumbuliwa na vita wakirekebisha kao lililoharibiwa sana la mmoja wa dada zao Wakristo, majirani wake walihisi kusukumwa waulize: “Upendo huu hutoka wapi? Nyinyi ni watu wa aina gani?” Na mwanamke Mwislamu, aliyekuwa akitazama wakati kao la Shahidi mmoja lilipokuwa likisafishwa na kurekebishwa, alijulisha hivi: “Nyinyi mwapendana kwelikweli. Yenu ndiyo dini ya kweli.”
[Sanduku katika ukurasa wa 316]
Ndugu na Dada wa Kweli
Kuhusu Mashahidi wakimbizi wa Kuba katika Fort Chaffee, Arkansas, “Arkansas Gazette” lilisema hivi: “Walikuwa ndio wa kwanza kabisa kuhamishwa kwenda katika makao mapya kwa sababu ‘ndugu na dada’ zao Waamerika—Mashahidi wa Yehova wenzao—waliwatafuta. . . . Wakati Mashahidi waitapo wenzao wa kiroho katika nchi yoyote ‘ndugu na dada,’ wao humaanisha hivyo kwelikweli.”—Toleo la Aprili 19, 1981.
[Picha katika ukurasa wa 306]
Baada ya Vita ya Ulimwengu 2, walipeleka chakula na nguo kwa Mashahidi wenzao wenye uhitaji katika nchi 18
Marekani
Uswisi
[Picha katika ukurasa wa 310]
Katika 1990, Mashahidi katika nchi za karibu waliunganisha jitihada zao ili kusaidia waamini wenzao katika Rumania
[Picha katika ukurasa wa 311]
Mashahidi waliookoka tetemeko la dunia katika Peru walijenga jiji lao wenyewe la kimbilio na wakasaidiana
Ugavi wa vitulizo ulioletwa na Mashahidi wengine (chini) ulikuwa miongoni mwa ule wa kwanza kufika katika eneo hilo
[Picha katika ukurasa wa 313]
Jitihada za kutoa kitulizo mara nyingi hutia ndani kuandaa vifaa na wenye kujitolea ili kusaidia Mashahidi wenzi wajenge upya makao yao
Guatemala
Panama
Mexico
[Picha katika ukurasa wa 314]
Jitihada za kutoa kitulizo za Mashahidi hutia ndani kujengana kiroho. Katika Kalamata, Ugiriki, na pia nje ya jiji, mahema yalisimamishwa haraka kwa ajili ya mikutano
-
-
Kujenga Pamoja Duniani PoteMashahidi wa Yehova—Wapiga-Mbiu wa Ufalme wa Mungu
-
-
Sura ya 20
Kujenga Pamoja Duniani Pote
ILE hisi ya udugu wa kweli miongoni mwa Mashahidi wa Yehova inadhihirika kwa njia nyingi. Wale ambao huhudhuria mikutano yao huona ithibati yayo. Kwenye mikusanyiko yao inaonyeshwa kwa kadiri kubwa zaidi. Pia inaonekana wazi wanapofanya kazi pamoja ili kuandaa mahali pafaapo pa kukutania kwa ajili ya makutaniko yao.
Mwongo wa 1990 ulipokuwa ukianza, kulikuwa zaidi ya makutaniko 60,000 ya Mashahidi wa Yehova ulimwenguni pote. Wakati wa mwongo uliotangulia, wastani wa makutaniko mapya 1,759 yalikuwa yakiongezwa, kila mwaka. Kufikia miaka ya mapema ya 1990, mwendo huo ulikuwa umeongezeka kufikia 3,000 kwa mwaka. Kuyaandalia yote mahali pafaapo pa kukutanikia kumekuwa kazi kubwa sana.
Majumba ya Ufalme
Kama ilivyokuwa kwa Wakristo wa karne ya kwanza, mwanzoni makutaniko mengi ya Mashahidi wa Yehova yalitumia makao ya faragha kwa mikutano yao mingi. Katika Stockholm, Sweden, wale wachache wa kwanza waliofanya mikutano ya ukawaida huko walitumia duka la useremala, ambalo walikodi ili walitumie baada ya kazi ya siku kufanywa. Kwa sababu ya mnyanyaso, kikundi kidogo katika mkoa wa La Coruña, Hispania, kilifanya mikutano yao ya kwanza katika bohari, au ghala ndogo.
Wakati nafasi zaidi ilipohitajiwa, katika nchi zilizokuwa na uhuru wa kufanya hivyo, makutaniko ya mahali ya Mashahidi wa Yehova yangekodi mahali pa mikutano. Hata hivyo, ikiwa jumba hilo lilikuwa likitumiwa pia na matengenezo mengine, ilibidi kusafirisha vifaa au kuviandaa kwa matumizi kwa ajili ya kila mkutano, na mara nyingi kulikuwako harufu ya tumbako iliyobakia. Mahali ilipowezekana, akina ndugu wangekodi duka lisilotumiwa au chumba cha orofa ambacho kingetumiwa na kutaniko pekee. Lakini, baada ya wakati, katika mahali pengi gharama za juu za kukodi na kutopatikana kwa mahali pafaapo kulifanya iwe lazima kufanya mipango mingine. Katika visa fulani majengo yalinunuliwa na kurekebishwa upya.
Kabla ya Vita ya Ulimwengu 2, yalikuwako makutaniko machache yaliyojenga mahali pa kukutana palipokusudiwa hasa kwa matumizi yao. Hata mapema sana kama 1890, kikundi cha Wanafunzi wa Biblia katika Marekani katika Mount Lookout, West Virginia, kilijenga mahali pacho chenyewe pa kukutanikia.a Hata hivyo, ujenzi wa Majumba ya Ufalme wenye kuenea haukuanza mpaka miaka ya 1950.
Jina Jumba la Ufalme lilidokezwa katika 1935 na J. F. Rutherford, aliyekuwa wakati huo msimamizi wa Watch Tower Society. Kuhusiana na vifaa vya tawi la Sosaiti katika Honolulu, Hawaii, alipanga ndugu wajenge jumba ambamo mikutano ingefanyiwa. Wakati James Harrub alipouliza Ndugu Rutherford angeliitaje jengo hilo, yeye alijibu: “Waonaje tukiliita kwa jina ‘Jumba la Ufalme,’ kwa kuwa ndivyo tunavyofanya, kuhubiri habari njema za Ufalme?” Baada ya hapo, ilipowezekana, majumba yaliyokuwa yakitumiwa kwa ukawaida na Mashahidi yakaanza hatua kwa hatua kutambulishwa kwa ishara zilizosema “Jumba la Ufalme.” Hivyo, wakati London Tabernacle liliporekebishwa upya katika 1937-1938, lilipewa jina jipya Jumba la Ufalme. Baada ya wakati, mahali pakuu pa mikutano pa makutaniko ulimwenguni pote pakaja kuitwa Jumba la Ufalme la Mashahidi wa Yehova.
Njia Zaidi ya Moja za Kujenga
Maamuzi juu ya kama watakodi au kujenga Majumba ya Ufalme hufanywa na makutaniko yenyewe mojamoja. Pia hayo hulipia gharama zozote za ujenzi na udumishaji. Ili kuokoa fedha, makutaniko mengi yamejitahidi kufanya kazi nyingi ya ujenzi kadiri inavyowezekana bila kuajiri wafanyakazi wa mkataba wa kulipwa.
Majumba yenyewe yaweza kujengwa kwa matufali, mawe, na mbao, au vifaa vingine, ikitegemea gharama pamoja na vifaa vinavyopatikana katika eneo. Katika Katima Mulilo, Namibia, nyasi ndefu zilitumiwa kwa ajili ya paa, na udongo kutoka vichuguu (ambao hukauka na kuwa imara sana) ulifinyangwa kuwa ukuta na sakafu. Mashahidi katika Segovia, Kolombia, walitengeneza matufali ya saruji yao wenyewe ya kujengea. Mawe ya volkano kutoka Mlima Lasen yalitumiwa katika Colfax, California.
Hudhurio la mikutano mara nyingi likiwa linazidi 200 katika 1972, kutaniko katika Maseru, Lesotho, lilijua kwamba walihitaji kujenga Jumba la Ufalme lifaalo. Kila mtu alisaidia katika mradi huo. Ndugu wazee-wazee walitembea kufikia kilometa 32 ili kushiriki. Watoto walivingirisha mapipa ya maji kuyaleta kwenye mahali pa ujenzi. Dada waliandaa milo. Pia walitumia nyayo zao kutwanga ardhi, ili kuiimarisha katika kuitayarisha kwa ajili ya kumwagwa kwa bamba la zege, wakati wote wakiimba nyimbo za Ufalme na kukanyagakanyaga chini kwa kufuatana na mwendo wa muziki. Changarawe, iliyogharimu kuisafirisha tu kutoka milima ya karibu, ilitumiwa kwa ajili ya kuta. Tokeo likawa Jumba la Ufalme ambalo lingeweza kutoshea watu kama 250.
Nyakati nyingine, Mashahidi kutoka makutaniko ya karibu walisaidia kazi ya ujenzi. Hivyo, katika 1985, wakati Mashahidi wa Yehova katika Imbali, mji wa weusi katika Afrika Kusini, walipojenga jumba ambalo lingeweza kutoshea watu 400 vizuri, Mashahidi wenzao kutoka majiji ya karibu ya Pietermaritzburg na Durban walikuja kusaidia. Je, waweza kuwazia jinsi majirani walivyoshangaa wakati, katika pindi ya siku hizo za msukosuko wa tofauti za rangi katika Afrika Kusini, walipoona vikundi vya Mashahidi weupe, Machotara, na Wahindi wakimiminika katika mji na kufanya kazi bega kwa bega pamoja na ndugu zao Waafrika weusi? Kama vile meya mwenyeji alivyojulisha: “Laweza kufanywa kwa upendo tu.”
Hata roho ya kupenda iweje, makutaniko yaliona kwamba hali za mahali zilizuia yale ambayo ndugu wangeweza kufanya. Wanaume kutanikoni walikuwa na familia za kuruzuku na kwa kawaida wangeweza kufanya kazi kwenye mradi huo wakati wa miisho-juma tu na labda kidogo jioni. Makutaniko mengi yalikuwa na mafundi wa ujenzi wachache tu. Hata hivyo, jengo ambalo kidogo ni rahisi, lililo wazi kidogo lifaalo hali za tropiki lingeweza kujengwa kwa siku chache au labda majuma machache. Kwa msaada wa Mashahidi katika makutaniko ya karibu, majengo imara zaidi yangeweza kukamilishwa kwa miezi mitano au sita. Katika visa vingine ilitaka mwaka mmoja au miwili.
Hata hivyo, walipokuwa wakisonga kuingia katika miaka ya 1970, Mashahidi wa Yehova ulimwenguni pote walikuwa wakiongezeka kwa kadiri ya makutaniko mawili au matatu mapya kila siku. Kufikia miaka ya mapema ya 1990, kadiri ya ongezeko ilifikia makutaniko tisa kwa siku. Je, uhitaji wao mkubwa wa Majumba ya Ufalme mapya ungeweza kutimizwa?
Kusitawisha Mbinu za Ujenzi wa Haraka
Mapema katika miaka ya 1970, katika Marekani, Mashahidi zaidi ya 50 kutoka makutaniko ya karibu walikuja pamoja ili kusaidia kujenga Jumba la Ufalme jipya katika Carterville, Missouri, kwa ajili ya kikundi kilichokuwa kikikutana katika Jiji la Webb. Katika mwisho-juma mmoja walijenga kiunzi kikuu na kufanya kazi kubwa kwenye paa. Kulikuwa kungali na mengi ya kufanywa, na ilichukua miezi kadhaa kumaliza kazi; lakini sehemu ya maana yalo ilikuwa imekamilishwa kwa kipindi kifupi.
Wakati wa mwongo uliofuata, kadiri akina ndugu walivyofanya kazi pamoja kujenga majumba kama 60, vizuizi vilishindwa, na njia zenye matokeo zaidi zikasitawishwa. Baada ya wakati, walipata kuona kwamba baada ya kazi ya msingi kufanywa, wangeweza kukaribia kukamilisha Jumba la Ufalme lote kwa mwisho-juma mmoja.
Waangalizi kadhaa wa makutaniko—wote kutoka magharibi-kati mwa Marekani—walianza kujitahidi kufikia mradi huo. Wakati makutaniko yalipoomba msaada wa kujenga Jumba la Ufalme lao, mmoja au zaidi wa akina ndugu hao angezungumzia mradi huo pamoja nao na kuandaa mambo mengi madogomadogo kuhusu matayarisho ambayo lazima yashughulikiwe na wenyeji kabla ya kazi kuanza kufanywa. Miongoni mwa mambo mengine, ilibidi ruhusa za ujenzi zipatikane, ilibidi msingi na bamba la sakafu la zege vimwagwe, ilibidi umeme uwe unafanya kazi, ilibidi mabomba ya maji ya chini ya ardhi yawe yamewekwa mahali payo, na ilibidi ifanywe mipango yenye kutegemeka ya kuleta vifaa vya ujenzi. Kisha tarehe ingeweza kuwekwa ya ujenzi wa Jumba la Ufalme lenyewe. Jengo hilo halingekuwa limetangulia kuundwa; lingejengwa toka chini hadi juu mahali papo hapo pa ujenzi.
Ni nani wangefanya hasa kazi ya ujenzi? Kwa kadiri ilivyowezekana, ilifanywa na wafanyakazi wa kujitolea, wasiolipwa. Familia nzimanzima mara nyingi zilishiriki. Wale wenye kupanga mradi huo waliwasiliana na Mashahidi waliokuwa mafundi na ambao walikuwa wameeleza nia yao ya kushiriki katika miradi hiyo. Wengi wao walitazamia kwa hamu kila mradi mpya wa ujenzi. Mashahidi wengine waliopata kujua juu ya miradi hiyo walitaka kushiriki; mamia kutoka eneo la karibu—na kutoka sehemu za mbali zaidi—walimiminika kwenye mahali pa ujenzi, wakiwa na hamu ya kutoa utumishi wao mbalimbali katika njia yoyote waliyoweza. Walio wengi wao hawakuwa wajenzi stadi, lakini hakika walitoa ithibati kwamba wao walifaana na maelezo ya wale ambao wangekuwa waungaji mkono wa Mfalme wa Kimesiya wa Yehova kama ilivyoandikwa kwenye Zaburi 110:3, ambalo husema: “Watu wako wanajitoa kwa hiari.”
Alhamisi jioni kabla ya ile jitihada kubwa kuanza, wale waliokuwa wakisimamia ujenzi walikutana ili kupanga mambo madogomadogo ya mwisho. Jioni iliyofuata, wafanyakazi walionyeshwa slaidi juu ya utaratibu ili waelewe jinsi ambavyo kazi ingefanywa. Mkazo ulitiwa juu ya umaana wa sifa za kimungu. Ndugu walitiwa moyo wafanye kazi pamoja kwa upendo, wawe wenye fadhili, na kuonyesha saburi na ufikirio. Kila mtu alitiwa moyo afanye kazi kwa mwendo wa taratibu lakini asiharakishe na asisite kuchukua dakika chache kushiriki pamoja na mwingine jambo lililoonwa lenye kujenga. Mapema asubuhi iliyofuata, ujenzi ulianza.
Katika wakati uliopangwa mapema Jumamosi asubuhi, kila mtu angeacha kufanya alilokuwa akifanya ili kusikiliza mazungumzo ya Andiko la siku. Sala ilitolewa, maana ilifahamiwa vema kwamba fanikio la mradi wote lilitegemea baraka ya Yehova.—Zab. 127:1.
Kazi ilipoanza, hiyo ilisonga mbele kasi. Katika muda wa saa moja kuta zilikuwa zimesimama. Farasi za paa zilifuata. Kufunika kuta kukamalizwa. Mafundi wa umeme wakaanza kuzungusha waya. Vitundu vya visawazishahewa vikawekwa. Kabati zikajengwa pahali pazo. Nyakati nyingine kulinyesha mwisho-juma wote, au halihewa iligeuka kuwa baridi sana au joto sana, lakini kazi ilisonga mbele. Hakukuwa na mashindano au ushindani miongoni mwa mafundi.
Mara nyingi, kabla ya jua kushuka katika siku ya pili, Jumba la Ufalme lilikuwa limekamilishwa—limepambwa vizuri ndani, labda hata kupambwa mandhari ya nje. Ilipofaa zaidi, kazi ziliratibiwa ziendelee kwa siku tatu, au labda miisho-juma miwili. Mwishoni mwa mradi, walio wengi kati ya wafanyakazi wangebaki, wakiwa wamechoka lakini wenye furaha sana, wafurahie mkutano wa kwanza wa kawaida wa kutaniko, funzo la Mnara wa Mlinzi.
Wakitia shaka kwamba kazi nzuri ingeweza kufanywa kwa haraka sana jinsi hiyo, watu kadhaa katika Guymon, Oklahoma, Marekani, waliita mkaguzi wa ujenzi wa jiji. “Niliwaambia kwamba kama walitaka kuona jambo lililofanywa sawasawa, yawapasa kuzuru jumba hilo!” akasema mkaguzi huyo baadaye alipokuwa akisimulia Mashahidi kisa hicho. “Nyinyi watu hata mnafanya sawasawa yale yaliyofichika na yasiyoonekana!”
Kadiri uhitaji wa Majumba ya Ufalme ulivyoongezeka, ndugu waliokuwa wamesitawisha zile njia nyingi za ujenzi wa haraka walizoeza wengine. Ripoti za yale yaliyokuwa yakifanywa zilienea kwenye nchi nyinginezo. Je, njia hizo za ujenzi zingeweza kutumiwa huko pia?
Ujenzi wa Haraka Wafanywa Kuwa wa Kimataifa
Ujenzi wa Majumba ya Ufalme katika Kanada ulikuwa ukiachwa nyuma sana na mahitaji ya makutaniko. Mashahidi katika Kanada walialika wale waliokuwa wakipanga miradi ya ujenzi wa haraka katika Marekani waje wawaeleze jinsi walivyoufanya. Mwanzoni, Wakanada walikuwa na shaka kidogo kwamba wangeweza kujenga hivyo katika Kanada, lakini waliamua kujaribu. Jumba la Ufalme la kwanza lililojengwa kwa njia hiyo katika Kanada lilijengwa katika Elmira, Ontario, katika 1982. Kufikia 1992, kulikuwa Majumba ya Ufalme 306 katika Kanada yaliyokuwa yamejengwa kwa njia hiyo.
Mashahidi katika Northampton, Uingereza, walifikiri kuwa wangeweza kufanya hivyo pia. Mradi wao, katika 1983, ulikuwa ndio wa kwanza katika Ulaya. Ndugu wenye ujuzi katika namna hiyo ya ujenzi walisafiri kutoka Marekani na Kanada ili kusimamia mradi huo na kusaidia Mashahidi wenyeji wajifunze jinsi ya kuufanya. Wenye kujitolea wengine walikuwapo kutoka mbali sana kama vile Japani, India, Ufaransa, na Ujerumani. Walikuwapo wakiwa wenye kujitolea, si ili kulipwa. Yote yaliwezekanaje? Kama vile mwangalizi wa kikundi kimoja cha Mashahidi wa Ireland kilichofanya kazi katika mradi kama huo alivyosema, ‘Yanafanikiwa kwa sababu ndugu na dada wote hushirikiana chini ya uvutano wa roho ya Yehova.’
Hata wakati sheria za ujenzi za mahali zinapoonekana zikifanya miradi kama hiyo isiwezekane, Mashahidi wamepata kwamba, mara nyingi, wakati maofisa wa jiji wanapoelezwa mambo kirefu, wanakuwa na furaha kushirikiana.
Baada ya mradi wa ujenzi wa haraka katika Norway, kaskazini mwa Mzingo wa Aktiki, gazeti Finnmarken lilieleza kwa mshangao hivi: “Ajabu kabisa. Hayo ndiyo maneno pekee tuwezayo kupata ya kuelezea waliyofanya Mashahidi wa Yehova mwisho-juma uliopita.” Vivyo hivyo, wakati Mashahidi katika Kisiwa cha Kaskazini cha New Zealand walipojenga Jumba la Ufalme lenye kuvutia kwa siku mbili na nusu, kichwa kikuu cha habari kwenye ukurasa wa mbele katika gazeti la mahali hapo kilijulisha: “Mradi Wakaribia Kuwa Muujiza.” Makala hiyo iliongeza: “Labda sehemu ya mradi huo yenye kuduwaza akili zaidi ni upangaji mzuri wa mambo na uendeshaji-mambo wenye utulivu kabisa.”
Umbali wa mahali panapohitaji Jumba la Ufalme hauthibitiki kuwa kizuizi kisichoshindika. Katika Belize mradi wa ujenzi wa haraka ulifanywa, hata ingawa ilimaanisha kusafirisha kila kipande cha kifaa cha ujenzi hadi kwenye kisiwa kilometa 60 kutoka Jiji la Belize. Wakati Jumba la Ufalme lenye kifaa cha kusawazisha hewa lilipojengwa katika Port Hedland, Australia Magharibi, mwisho-juma mmoja, lilijengwa kwa vifaa na wafanyakazi ambao karibu wote walikuja kutoka umbali wa kilometa 1,600 au zaidi. Wafanyakazi wenyewe walijilipia nauli zao wenyewe. Walio wengi kati ya wale walioshiriki sehemu katika mradi huo hawakujua kibinafsi Mashahidi katika Kutaniko la Port Hedland, na ni wachache sana kati yao ambao wangepata kuhudhuria mikutano humo wakati wowote. Lakini hiyo haikuwazuia kuonyesha upendo wao katika njia hiyo.
Hata kukiwa na idadi ndogo ya Mashahidi mahali fulani, hilo halizuii utumizi wa njia hizo za kujenga majumba. Mashahidi kama 800 kutoka Trinidad walijitolea kusafiri hadi Tobago ili kusaidia ndugu na dada zao Wakristo 84 wa huko wajenge jumba katika Scarborough katika 1985. Wale Mashahidi 17 (wengi wao wakiwa wanawake na watoto) katika Goose Bay, Labrador, bila shaka walihitaji msaada ikiwa wangeweza wakati wowote kupata Jumba la Ufalme lao wenyewe. Katika 1985, Mashahidi kutoka sehemu nyingine za Kanada walikodi ndege tatu ili kusafirisha 450 kati yao hadi Goose Bay ili kufanya kazi hiyo. Baada ya siku mbili za kazi ya bidii, walikuwa na programu ya kuwekwa wakfu katika jumba lililokamilika jioni ya Jumapili.
Hiyo haimaanishi kwamba Majumba ya Ufalme yote sasa yanajengwa kwa njia za ujenzi wa haraka, lakini idadi yayo inayozidi kukua yanajengwa hivyo.
Halmashauri za Ujenzi za Kimkoa
Kufikia katikati ya 1986 kadiri ambayo Majumba ya Ufalme yalihitajiwa ilikuwa imeongezeka sana. Wakati wa mwaka uliotangulia, makutaniko mapya 2,461 yalikuwa yameundwa ulimwenguni pote; 207 kati ya hayo yalikuwa katika Marekani. Baadhi ya Majumba ya Ufalme yalikuwa yakitumiwa na makutaniko matatu, manne, au hata matano. Kama vile Maandiko yalivyokuwa yametabiri, kwelikweli Yehova alikuwa akiharakisha kazi ya kukusanya kuleta ndani.—Isa. 60:22.
Ili kuhakikisha utumizi bora zaidi wa wafanyakazi na kuwezesha wote waliokuwa wakijenga Majumba ya Ufalme wanufaike kutokana na ujuzi uliokuwa umepatikana, Sosaiti ilianza kuratibu utendaji wao. Ukiwa mwanzo, katika 1987 Marekani iligawanywa miongoni mwa Halmashauri za Ujenzi za Kimkoa 60. Kulikuwa mengi ya kufanywa na hizo zote; upesi baadhi yazo zilikuwa na miradi iliyopangwa kwa mwaka mmoja au zaidi. Wale waliowekwa kutumikia kwenye halmashauri hizo walikuwa wanaume ambao, kwanza kabisa, walikuwa wamestahili kiroho, wazee katika makutaniko, walio vielelezo vizuri katika kudhihirisha matunda ya roho ya Mungu. (Gal. 5:22, 23) Wengi wao pia walikuwa na ujuzi katika kushughulikia mambo ya mashamba na nyumba, uhandisi, ujenzi, usimamizi wa biashara, usalama, na nyanja zinazohusiana.
Makutaniko yalitiwa moyo yashauriane na Halmashauri ya Ujenzi ya Kimkoa kabla ya kuchagua mahali pa kujenga Jumba la Ufalme jipya. Mahali mlimokuwa na zaidi ya kutaniko moja jijini, walihimizwa pia kushauriana na mwangalizi au waangalizi wa mizunguko, mwangalizi wa jiji, na wazee kutoka makutaniko ya karibu. Makutaniko yaliyokuwa yakipanga urekebishaji mkubwa wa jengo la zamani au ujenzi wa Jumba la Ufalme jipya yalishauriwa yanufaike na ujuzi wa ndugu wa Halmashauri ya Ujenzi ya Kimkoa ya eneo lao na kwa miongozo ambayo Sosaiti ilikuwa imewatolea. Kupitia halmashauri hiyo, mipango ingeratibiwa ili kukusanya wafanyakazi stadi waliohitajiwa kutoka miongoni mwa ndugu na dada katika kazi za ufundi 65 waliokuwa tayari wamejitolea kusaidia kwenye miradi hiyo.
Kadiri taratibu zilivyofanywa kuwa bora zaidi, iliwezekana kupunguza idadi ya wafanyakazi waliohusika katika ujenzi wowote ule mmoja. Badala ya kuwa na maelfu penye ujenzi ama wakitazama ama wakitoa utumishi wao mbalimbali, ni mara chache sana walipokuwapo zaidi ya 200 penye ujenzi kwa wakati wowote ule mmoja. Badala ya kutumia mwisho-juma wote pale, wafanyakazi walikuwapo wakati tu stadi zao hususa zilipohitajiwa. Hivyo walikuwa na wakati zaidi wa kutumia pamoja na familia zao na wa kufanya utendaji pamoja na makutaniko ya kwao. Wakati ndugu wenyeji walipokuwa wanaweza kufanya kazi fulani kwa wakati mzuri, mara nyingi ilionekana kuwa yafaa zaidi kuleta kikundi cha ujenzi wa haraka wakati tu wa zile kazi ambazo walihitajiwa sana kufanya.
Ijapokuwa kazi yote ilisonga mbele kwa mwendo wenye kushangaza, hilo halikuwa ndilo jambo muhimu. Jambo muhimu zaidi lilikuwa kuandaa ujenzi bora wa Majumba ya Ufalme yenye kiasi yaliyokusudiwa kutimiza mahitaji ya mahali. Upangaji-mambo wa uangalifu ulifanywa ili kutimiza jambo hilo huku gharama zikiwa chini iwezekanavyo. Hatua zilichukuliwa kuhakikisha kwamba usalama ulifikiriwa zaidi—usalama wa wafanyakazi, majirani, wapita njia, na watumiaji wa wakati ujao wa Jumba la Ufalme.
Ripoti kuhusu mpango huo wa kujenga Majumba ya Ufalme zilipofikia nchi nyinginezo, ofisi za tawi za Sosaiti ambazo ziliamini kwamba ungekuwa wenye kufaidi katika maeneo yazo ziliandaliwa habari kamili zilizohitaji. Kufikia 1992, Halmashauri za Ujenzi za Kimkoa zilizowekwa rasmi na Sosaiti zilikuwa zikisaidia ujenzi wa Majumba ya Ufalme katika nchi kama vile Afrika Kusini, Argentina, Australia, Japani, Kanada, Mexico, Ufaransa, Hispania, Uingereza, na Ujerumani. Njia za ujenzi zilipatanishwa na hali za mahali. Msaada ulipohitajiwa kutoka kwa tawi jingine kwa ajili ya ujenzi wa Jumba la Ufalme, huo ulipangwa kupitia ofisi ya makao makuu ya Sosaiti. Katika sehemu fulani za ulimwengu, majumba mapya yalikuwa yakijengwa kwa siku kadhaa; kwingineko, kwa majuma kadhaa au labda miezi michache. Kwa kupanga mambo kwa uangalifu na jitihada zilizoratibiwa, bila shaka wakati uliotakwa ili kuandaa Jumba la Ufalme jipya ulikuwa ukipunguzwa.
Utendaji wa ujenzi wa Mashahidi wa Yehova haukuwa wa Majumba ya Ufalme tu. Vifaa vikubwa zaidi huhitajiwa wakati vikundi vya makutaniko vikutanapo kwa ajili ya makusanyiko ya mzunguko na siku za kusanyiko la pekee za kila mwaka.
Kutimiza Uhitaji wa Majumba ya Kusanyiko
Kwa muda wa miaka iliyopita, vifaa vya aina nyingi vimetumiwa kwa ajili ya makusanyiko ya mzunguko. Mashahidi wa Yehova wamekodi mahali kama vile majumba ya umma, shule, majumba ya maonyesho, mabohari ya silaha, viwanja vya michezo, na viwanja vya maonyesho. Katika sehemu chache, vifaa bora sana vilipatikana kwa bei nafuu. Mara nyingi zaidi, wakati na jitihada nyingi vilitakwa ili kusafisha mahali, kuandaa vikuza-sauti, kujenga jukwaa, na kusafirisha viti. Nyakati nyingine mapatano yalifutwa dakika ya mwisho. Kadiri idadi ya makutaniko ilivyoongezeka, ikawa vigumu zaidi na zaidi kupata mahalimahali pafaapo pa kutosha. Ni jambo gani lingeweza kufanywa?
Kwa mara nyingine tena, suluhisho lilikuwa kwamba Mashahidi wa Yehova wawe na mahali pao wenyewe. Hiyo ingehusisha kurekebisha upya majengo yenye kufaa na kujenga mapya. La kwanza la Majumba ya Kusanyiko kama hayo katika Marekani lilikuwa jumba la maonyesho katika Long Island City, New York, lililorekebishwa upya na likaanza kutumiwa na Mashahidi wa Yehova mwishoni-mwishoni mwa 1965.
Karibu wakati uleule, Mashahidi kwenye kisiwa cha Guadeloupe cha Karibea walikuwa wakichora ramani ya Jumba la Kusanyiko la kutimiza mahitaji yao. Walihisi kwamba ingefaidi ikiwa wangekuwa na makusanyiko ya mzunguko katika sehemu nyingi tofauti-tofauti. Lakini miji iliyo mingi haikuwa na vifaa vilivyokuwa vikubwa vya kutosha. Kwa hiyo Mashahidi walijenga muundo uwezao kubebeka uliofanyizwa kwa vyuma na paa ya aluminiamu, kitu ambacho kingetosha kwa watu 700 na ambacho kingeweza kujengwa popote palipokuwa na ardhi iliyokuwa tambarare kidogo. Walilazimika kuongezea ukubwa wa jumba hilo tena na tena, mpaka lilipofikia kuweza kutoshea watu 5,000. Ebu fikiria kusafirisha, kujenga, na kubomoa tani 30 za vifaa kwa kila kusanyiko! Hilo Jumba la Kusanyiko lilijengwa na kubomolewa mara kadhaa kwa mwaka kwa muda wa miaka 13, mpaka ilipokuwa vigumu kupata ardhi kwa ajili ya jumba lenye kubebeka, ikawa lazima kununua ardhi na kujenga Jumba la Kusanyiko la kudumu, ambalo sasa hutumika kwa ajili ya makusanyiko ya mzunguko na mikusanyiko ya wilaya.
Katika sehemu chache, miradi ya Jumba la Kusanyiko ilitumia majengo yaliyokuwako. Katika Uingereza, katika Hays Bridge, Surrey, shule yenye majengo mengi ya miaka 50 ilinunuliwa na kurekebishwa upya. Iko katika uwanja wa hektari 11 katika sehemu nzuri ya mashambani. Yaliyokuwa hapo zamani majengo ya sinema na bohari la bidhaa za viwanda yalijengwa yakiwa na umbo jipya na kuanza kutumiwa katika Hispania; kiwanda cha nguo kisichotumika katika Australia; jumba la dansi katika Quebec, Kanada; jumba la michezo ya kuvingirisha matufe katika Japani; bohari la bidhaa katika Jamhuri ya Korea. Yote hayo yalijengwa upya na kuwa Majumba ya Kusanyiko yenye kuvutia ambayo yangeweza kutumika vyema kuwa vitovu vikubwa vya elimu ya Biblia.
Majumba ya Kusanyiko mengine yalikuwa mapya kabisa, yakiwa yamejengwa toka chini hadi juu. Lile umbo la pembenane la aina yalo la jumba katika Hellaby, South Yorkshire, Uingereza, pamoja na uhakika wa kwamba kazi iliyo nyingi ilifanywa na wafanyakazi wa kujitolea lilitokeza makala katika jarida la Taasisi ya Uhandisi wa Ujenzi. Jumba la Kusanyiko katika Saskatoon, Saskatchewan, katika Kanada, lilikusudiwa litoshee watu 1,200; lakini wakati kuta za ndani zinaposimamishwa mahali pazo, jengo hilo laweza kutumiwa likiwa Majumba ya Ufalme manne yakiwa upande kwa upande. Jumba la Kusanyiko la Haiti (lililotangulia kujengwa na kusafirishwa kutoka Marekani) lilikuwa wazi katika pande mbili ili wale walioketi ndani waweze kupashwa baridi daima na pepo zilizoko—kitulizo chenye kukaribishwa katika jua kali la Haiti. Jumba katika Port Moresby, Papua New Guinea, lilibuniwa kwa njia ya kwamba sehemu za kuta zingeweza kufunguka kama milango ili kuweza kutoshea umati mkubwa kuliko ule ambao ungeweza kutoshea ndani.
Uamuzi wa kujenga Jumba la Kusanyiko haufanywi na kikundi cha waangalizi ambao baada ya hapo hutarajia kila mtu mwingine auunge mkono. Kabla ya Jumba la Kusanyiko jipya lolote kujengwa, Sosaiti huhakikisha kwamba uchanganuzi wa uangalifu umefanywa kuhusu uhitaji walo na ni mara ngapi litatumiwa. Ufikirio hutolewa si kwa idili ya wenyeji kwa ajili ya mradi bali pia mahitaji ya ujumla shambani. Jambo hilo huzungumzwa pamoja na makutaniko yote yatakayohusika, ili kuhakikisha tamaa na uwezo wa akina ndugu wa kuutegemeza.
Hivyo, kazi ianzapo, Mashahidi wa Yehova katika eneo hilo wanaiunga mkono kabisa. Pesa za kila mradi hutolewa na Mashahidi wenyewe. Mahitaji ya kifedha huelezwa, lakini michango ni ya kujitolea na watoaji hawajulikani ni kina nani. Mipango ya uangalifu hutangulia kufanywa, na ujenzi hunufaika kutokana na ujuzi uliokwisha kupatikana katika kujenga Majumba ya Ufalme na, mara nyingi, kutoka kwa miradi ya Majumba ya Kusanyiko katika sehemu nyingine. Inapohitajiwa, pande fulani za kazi zinaweza kupewa wafanyakazi wa mkataba wa kulipwa, lakini kazi iliyo nyingi kwa kawaida hufanywa na Mashahidi wenye idili. Hiyo inaweza kupunguza nusu ya gharama.
Kukiwa na jamii ya wafanyakazi wenye stadi na wengine ambao hutoa wakati na vipawa vyao, kwa kawaida ujenzi wote husonga mbele kwa haraka. Ujenzi fulani waweza kuhitaji zaidi ya mwaka. Lakini kwenye Kisiwa cha Vancouver katika Kanada, katika 1985, wenye kujitolea kama 4,500 walikamilisha Jumba la Kusanyiko la meta za mraba 2,300 kwa siku tisa tu. Jengo hilo latia ndani pia Jumba la Ufalme liwezalo kutoshea watu 200 kwa matumizi ya makutaniko ya mahali hapo. Katika New Caledonia, kafyu iliwekwa na serikali katika 1984 kwa sababu ya msukosuko wa kisiasa, hata hivyo wenye kujitolea kama 400 walifanya kazi kwenye Jumba la Kusanyiko wakati ule, na lilikamilishwa kwa miezi minne tu. Karibu na Stockholm, Sweden, Jumba la Kusanyiko zuri, lenye kufaa, likiwa na viti 900 vya mbao za oki vyenye matakia, lilijengwa kwa miezi saba.
Nyakati nyingine jitihada zenye kuendelea katika mahakama zimehitajiwa ili kupata ruhusa ya kujenga hayo Majumba ya Kusanyiko. Ndivyo ilivyokuwa katika Kanada katika Surrey, British Columbia. Wakati uwanja uliponunuliwa, matakwa ya kisheria ya eneo yaliruhusu ujenzi wa mahali kama hapo pa ibada. Lakini wakati ramani zilipopelekwa kwenye baraza, katika 1974, Baraza la Wilaya ya Surrey lilipitisha sheria ikisema kwamba makanisa na majumba ya kusanyiko yangeweza kujengwa tu katika Eneo la P-3—eneo lisilokuwako! Hata hivyo, makanisa 79 yalikuwa yamejengwa katika manispaa hiyo katika wakati uliopita bila matata. Jambo hilo lilipelekwa mahakamani. Maamuzi mengi yenye kupendelea Mashahidi wa Yehova yalitolewa. Wakati kizuizi cha maofisa wenye chuki zisizo na msingi kilipoondolewa hatimaye, wafanyakazi wa kujitolea walifuatia ujenzi huo kwa idili kubwa hivi kwamba waliukamilisha kwa miezi kama saba. Kama ilivyokuwa kwa habari ya Nehemia katika jitihada zake za kujenga upya kuta za Yerusalemu la kale, walihisi kwamba ‘mkono wa Mungu ulikuwa juu yao’ ili wakamilishe kazi hiyo.—Neh. 2:18.
Wakati Mashahidi wa Yehova katika Marekani waliponunua Stanley Theater katika Jersey City, New Jersey, jengo hilo lilikuwa katika daftari ya mkoa ya mahali pa kihistoria. Ijapokuwa jumba hilo lilikuwa katika hali mbaya yenye kuhitaji marekebisho, lilikuwa na uwezekano mzuri sana wa kutumika likiwa Jumba la Kusanyiko. Hata hivyo, wakati Mashahidi walipotaka kufanya marekebisho yaliyohitajiwa, maofisa wa jiji walikataa kutoa ruhusa. Meya hakutaka Mashahidi wa Yehova katika eneo hilo; yeye alikuwa na mipango mingine kwa ajili ya jengo hilo. Hatua ya kisheria ilihitajiwa ili kuzuia maofisa wasitumie mamlaka yao kinyume cha sheria. Mahakama ilitoa uamuzi wenye kupendelea Mashahidi. Upesi baada ya hapo, wakazi wa eneo hilo walipiga kura kumwondoa meya huyo katika cheo chake. Kazi kwenye jumba ilisonga mbele kwa haraka. Tokeo lilikuwa Jumba la Kusanyiko zuri sana lililotoshea watu zaidi ya 4,000. Ni mahali ambapo wanabiashara na wakazi wa jiji hilo pia huonea fahari.
Wakati wa miaka 27 iliyopita, katika sehemu nyingi za dunia, Majumba ya Kusanyiko yenye kuvutia na yenye kufaa yamejengwa na Mashahidi wa Yehova ili kutumika kuwa vitovu vya elimu ya Biblia. Majumba kama hayo yanapatikana kwa hesabu zenye kuongezeka katika Amerika Kaskazini na Kusini, Ulaya, Afrika, na nch za Mashariki, pamoja na visiwa vingi. Katika nchi fulani—kwa kielelezo, Nigeria, Italia, na Denmark—Mashahidi wa Yehova wamejenga hata vifaa vya kudumu vilivyo vikubwa zaidi katika mahali peupe ambavyo vinaweza kutumiwa kwa ajili ya mikusanyiko yao ya wilaya.
Hata hivyo, Majumba ya Kusanyiko na Majumba ya Ufalme siyo miradi ya ujenzi pekee ambayo Mashahidi wa Yehova huhusika nayo ili kuendeleza kazi ya kupiga mbiu ya Ufalme wa Mungu.
Ofisi, Matbaa, na Makao ya Betheli Ulimwenguni Pote
Ulimwenguni pote katika 1992, kulikuwa ofisi za tawi 99 za Watch Tower Society, kila moja yazo ilitumika katika kuratibu utendaji wa Mashahidi wa Yehova katika sehemu yalo ya shamba la ulimwengu. Zaidi ya nusu ya matawi hayo hufanya uchapaji wa aina tofauti-tofauti ili kusogeza mbele kazi ya elimu ya Biblia. Wengi wa wale wanaofanya kazi katika matawi, huishi wakiwa familia kubwa katika makao yaitwayo Betheli, kumaanisha “Nyumba ya Mungu.” Kwa sababu ya mpanuko wa idadi ya Mashahidi wa Yehova na utendaji wao wa kuhubiri, imekuwa lazima kuongeza ukubwa wa makao hayo na kujenga mapya.
Ukuzi wa tengenezo umekuwa wa kasi sana hivi kwamba mara nyingi kumekuwa programu za upanuzi wa tawi 20 hadi 40 zikiendelea kwa wakati mmoja. Hiyo imetaka programu kubwa mno ya ujenzi wa kimataifa.
Kwa sababu ya kazi kubwa mno ya ujenzi inayofanywa ulimwenguni pote, Watch Tower Society ina Idara ya Uhandisi na Uchoraji-ramani yayo yenyewe kwenye makao makuu yayo ya New York. Wahandisi wenye miaka mingi ya ujuzi wameacha kazi zao za kimwili wakajitolea ili kusaidia kwa wakati wote kwenye miradi ya ujenzi inayohusiana moja kwa moja na utendaji wa Ufalme. Kwa kuongezea, wale ambao wana ujuzi wamefundisha wanaume na wanawake wengine katika kazi ya uhandisi, ubuni, na uchoraji-ramani. Kwa kuratibu kazi kupitia idara hii, ujuzi unaopatikana katika ujenzi wa tawi katika sehemu yoyote ya ulimwengu unaweza kunufaisha wale wanaofanya kazi kwenye miradi katika nchi nyinginezo.
Baada ya wakati, kiasi kikubwa cha kazi inayofanywa kilitokeza uhitaji wa kufungua Ofisi ya Uhandisi ya Kimkoa katika Japani ili kusaidia kufanya uchoraji-ramani kwa ajili ya miradi katika nchi za Mashariki. Ofisi za Uhandisi za Kimkoa nyingine huendesha kazi katika Ulaya na Australia, wafanyakazi wakiwa wametoka katika nchi mbalimbali. Ofisi hizo hufanya kazi kwa ushirikiano wa karibu na ofisi ya makao makuu, na utumishi wazo, pamoja na utumizi wa tekinolojia ya kompyuta, hupunguza idadi ya wafanyakazi wa uchoraji-ramani wenye kuhitajiwa kwenye mahali popote pale pa ujenzi.
Baadhi ya miradi, kidogo ni ya ukubwa wa kiasi. Ndivyo ilivyokuwa kuhusu ofisi ya tawi iliyojengwa katika Tahiti katika 1983. Ilitia ndani nafasi ya ofisi, ghala kadhaa, na makao kwa ajili ya wafanyakazi wanane wa kujitolea. Na ndivyo ilivyokuwa pia kuhusu lile jengo la tawi lenye orofa nne lililojengwa kwenye kisiwa cha Karibea cha Martinique wakati wa miaka ya 1982 hadi 1984. Majengo hayo huenda yasionekane kuwa yenye kutokeza kwa wakazi wa majiji makubwa katika nchi nyinginezo, lakini yalivuta uangalifu wa umma. Gazeti France-Antilles lilijulisha kwamba jengo la tawi katika Martinique lilikuwa “ujenzi wa ustadi mkubwa” ulioonyesha “upendo mkubwa wa kazi iliyofanywa vizuri.”
Kwa kutofautisha, kuhusu ukubwa, majengo yaliyokamilishwa katika Kanada katika 1981 yalitia ndani matbaa, au kiwanda, kikiwa na nafasi ya meta za mraba zaidi ya 9,300 na jengo la makazi kwa ajili ya wenye kujitolea 250. Katika Cesario Lange, katika Brazili, majengo mengi ya Watch Tower yaliyokamilishwa mwaka uo huo yalitia ndani majengo manane, yenye nafasi ya sakafu ya meta za mraba 46,000. Yalihitaji malori 10,000 yaliyojaa saruji, mawe, na mchanga, pamoja na vizingiti vyenye mkorogo wa saruji na kokoto vinavyofika mara mbili ya urefu wa Mlima Everest! Katika 1991, matbaa kubwa mpya ilipokamilishwa katika Filipino, ilihitajiwa pia kuandaa jengo la makazi la orofa 11.
Ili kutimiza mahitaji ya idadi yenye kukua ya wapiga-mbiu wa Ufalme katika Nigeria, mradi mkubwa wa ujenzi ulianzishwa katika Igieduma katika 1984. Ungetia ndani kiwanda, jengo la ofisi lenye nafasi kubwa, majengo manne yaliyounganishwa ya makazi, na vifaa vingine. Mipango ilifanywa kwamba kuta za kiwanda zitangulie kufanyizwa kabisa na kusafirishwa kutoka Marekani. Lakini ndugu walikabiliwa na masharti magumu ya kuingiza vitu nchini yaliyoonekana kuwa hayawezekani. Wakati masharti hayo yalipotimizwa na kila kitu kikawasili salama kwenye mahali pa ujenzi, Mashahidi hawakujipa sifa wenyewe bali walimshukuru Yehova kwa baraka yake.
Upanuzi wa Kasi Duniani Pote
Hata hivyo, ukuzi wa kazi ya kupiga mbiu ya Ufalme umekuwa wa kasi sana hivi kwamba, hata baada ya upanuzi mkubwa wa vifaa vya tawi katika nchi, mara nyingi imekuwa lazima kuanza kujenga tena kwa muda mfupi. Fikiria vielelezo vichache.
Katika Peru tawi jipya zuri—lenye nafasi ya ofisi, vyumba 22 vya kulala pamoja na vifaa vingine vya msingi kwa ajili ya washiriki wa familia ya Betheli, na Jumba la Ufalme moja—vilikamilishwa mwishoni mwa 1984. Lakini itikio kwa ujumbe wa Ufalme katika nchi hiyo ya Amerika Kusini lilikuwa kubwa zaidi ya ilivyotarajiwa. Miaka minne baadaye ilikuwa lazima kurudufisha majengo yaliyokuwako, wakati huu kwa kutumia ubuni unaohimili tetemeko la dunia.
Majengo mapya ya tawi yenye nafasi kubwa yalikamilishwa katika Kolombia katika 1979. Ilionekana kwamba yangeandaa nafasi ya kutosha kwa miaka mingi ijayo. Hata hivyo, katika muda wa miaka saba idadi ya Mashahidi katika Kolombia ilikuwa karibu imerudufika, na sasa tawi lilikuwa likichapa magazeti La Atalaya (Mnara wa Mlinzi) na ¡Despertad! (Amkeni!) si kwa ajili ya Kolombia tu bali pia kwa ajili ya nchi nne jirani. Walilazimika kuanza kujenga tena katika 1987—wakati huu mahali ambapo palikuwa na nafasi zaidi kwa ajili ya upanuzi.
Wakati wa 1980, Mashahidi wa Yehova katika Brazili walitumia saa 14,000,000 hivi kwa kazi ya kuhubiri hadharani ujumbe wa Ufalme. Tarakimu hiyo ilipanda kufikia karibu 50,000,000 katika 1989. Watu wengi zaidi walikuwa wakionyesha tamaa ya kutaka njaa yao ya kiroho itoshelezwe. Yale majengo ya tawi yaliyokuwa yamewekwa wakfu katika 1981 hayakutosha tena. Tayari kufikia Septemba 1988, uchimbuzi kwa ajili ya kiwanda kipya ulikuwa ukiendelea. Hicho kingeandaa asilimia 80 ya nafasi zaidi ya sakafu kuliko iliyokuwako katika kiwanda kilichoko, na bila shaka, makazi ya kutunza familia ya Betheli iliyoongezeka yangehitajiwa pia.
Katika Selters/Taunus, Ujerumani, jengo kubwa la kuchapia la pili kwa ukubwa kati ya viwanda vya kuchapia vya Watch Tower Society liliwekwa wakfu katika 1984. Miaka mitano baadaye, kwa sababu ya maongezeko katika Ujerumani na pia fursa za kupanua kazi ya kutoa ushahidi katika nchi ambazo tawi hilo huchapia fasihi, mipango ilikuwa ikiendelea kuongeza ukubwa wa kiwanda kufikia zaidi ya asilimia 85 na kuongeza vifaa vingine vya utegemezo.
Tawi la Japani lilikuwa limehamia Numazu kutoka Tokyo kwenye makao makubwa mapya katika 1972. Upanuzi zaidi uliokuwa mkubwa ulifanywa katika 1975. Kufikia 1978 mahali pengine palikuwa pamenunuliwa, katika Ebina; na kazi ya kujenga kiwanda kilichozidi ukubwa wa kile kilicho Numazu kwa mara tatu ilianza haraka. Hicho kilikamilishwa katika 1982. Bado hakikutosha; majengo zaidi yaliongezwa kufikia 1989. Je, haingewezekana kujenga mara moja tu na kukifanya kiwe kikubwa vya kutosha? La. Idadi ya wapiga-mbiu wa Ufalme katika Japani imerudufika tena na tena kwa njia ambayo hakuna mtu angeweza kutazamia. Kuanzia 14,199 katika 1972, idadi yao imepanda hadi 137,941 katika 1989, na walio wengi wao walikuwa katika huduma ya wakati wote.
Kiolezo icho hicho kinaonwa katika sehemu nyingine za dunia. Katika muda wa mwongo mmoja—na nyakati nyingine miaka michache—baada ya kujenga matawi makubwa yenye vifaa vya kuchapia, ilikuwa lazima kuanza upanuzi mkubwa. Ilikuwa hivyo katika Mexico, Kanada, Afrika Kusini, na Jamhuri ya Korea, miongoni mwa mengine.
Ni nani ambao hasa hufanya kazi ya ujenzi? Hiyo hutimizwaje?
Maelfu Mengi Wana Hamu ya Kusaidia
Katika Sweden, kati ya Mashahidi 17,000 katika nchi wakati ule wa ujenzi wa tawi lao katika Arboga, 5,000 hivi walijitolea kusaidia kazi. Wengi walikuwa tu wasaidizi wenye moyo wa kupenda, lakini kulikuwa pia wafanyakazi wenye ustadi wa hali ya juu wa kutosha kuhakikisha kwamba kazi ilifanywa sawasawa. Msukumo wao ni nini? Kumpenda Yehova.
Wakati mkuu kwenye ofisi ya upimaji-ardhi katika Denmark aliposikia kwamba kazi kwenye tawi jipya katika Holbæk ingefanywa na Mashahidi wa Yehova, alionyesha kutia shaka. Hata hivyo, miongoni mwa Mashahidi waliojitolea kusaidia, wote wenye ujuzi uliohitajiwa walipatikana. Hata hivyo, je, ingekuwa afadhali kama wafanyakazi wa mkataba wa kibiashara wangalilipwa wafanye kazi hiyo? Baada ya ujenzi huo kukamilishwa, wastadi kutoka idara ya ujenzi ya mji walizuru makao hayo na kueleza juu ya kazi yenye ustadi iliyofanywa—jambo ambalo wao huliona mara chache sana kwenye kazi zilizofanywa na watu wa kulipwa siku hizi. Kwa habari ya yule mkuu aliyetia shaka mapema kidogo, yeye alitabasamu na kusema: “Angalia, wakati ule sikujua nyinyi watu mna tengenezo la aina gani.”
Miji na majiji katika Australia yametawanyika sehemu zilizo mbali; hivyo, wengi kati ya wale 3,000 waliojitolea kufanya kazi kwenye ofisi ya tawi katika Ingleburn kati ya 1978 na 1983 walilazimika kusafiri angalau kilometa 1,600. Hata hivyo, safari za basi za vikundi vya wenye kujitolea ziliratibiwa, na makutaniko njiani yalijitolea kutoa milo na ushirika kwa ukaribishaji-wageni kwa ajili ya akina ndugu kwenye vituo vya kupumzikia. Baadhi ya ndugu waliuza makao yao, wakafunga biashara zao, wakachukua likizo, na kutoa dhabihu nyingine ili kushiriki katika ujenzi. Vikundi vya mafundi stadi vilikuja—baadhi yavyo zaidi ya mara moja—kumwaga kokoto, kuangika dari, na kujenga ua. Wengine walitoa upaji wa vifaa vya ujenzi.
Walio wengi kati ya wenye kujitolea kwenye miradi hiyo walikuwa bila ustadi, lakini kwa kuzoezwa kidogo, baadhi yao walitwaa madaraka makubwa wakafanya kazi bora sana. Walijifunza jinsi ya kutengeneza madirisha, kuendesha matrekta, kuchanganya kokoto, na kujenga matufali. Walifurahia mambo yasiyofurahiwa na wasio-Mashahidi wafanyao aina ileile ya kazi ili kulipwa. Kwa njia gani? Wenye ujuzi walikuwa tayari kushiriki maarifa yao. Hapana yeyote aliyehisi kwamba mtu mwingine angechukua kazi yake; kulikuwa kazi nyingi kwa kila mtu kufanya. Na kulikuwa na msukumo wenye nguvu wa kufanya kazi ya hali ya juu, kwa sababu ilifanywa ikiwa wonyesho wa kumpenda Mungu.
Kwenye mahali pa ujenzi, baadhi ya Mashahidi hufanyiza kiini cha “familia” ya ujenzi. Wakati wa kazi katika Selters/Taunus, Ujerumani, tokea 1979 hadi 1984, mamia kadhaa kwa kawaida walifanyiza kiini hicho cha wafanyakazi. Maelfu wengine walijiunga nao kwa vipindi tofauti-tofauti vya wakati, wengi katika miisho-juma. Kulikuwa mpango wa uangalifu hivi kwamba wenye kujitolea walipowasili, walikuwa na kazi tele ya kufanya.
Maadamu watu si wakamilifu, kutakuwako matatizo, lakini wale ambao hufanya kazi kwenye ujenzi huo hujaribu kutatua matatizo kwa msingi wa kanuni za Biblia. Wanajua kwamba kufanya mambo katika njia ya Kikristo ni jambo la maana zaidi ya kuwa na matokeo. Kikiwa kikumbusho, kwenye mahali pa ujenzi katika Ebina, Japani, kulikuwa ishara kubwa zenye picha za wafanyakazi wenye kuvalia kofia ngumu, na juu ya kila kofia ngumu liliandikwa kwa herufi za Kijapani moja la matunda ya roho ya Mungu: upendo, shangwe, amani, ustahimilivu, fadhili, wema, imani, upole, kujidhibiti. (Gal. 5:22, 23, NW) Wale ambao hutembelea mahali pa kazi wanaweza kuona na kusikia ile tofauti. Akieleza maoni yake mwenyewe, mwandishi mmoja wa habari aliyetembelea mahali pa ujenzi wa tawi katika Brazili alisema hivi: “Hapana machafuko au ukosefu wa ushirikiano . . . Mazingira haya ya Kikristo huifanya iwe tofauti hapa na yale ambayo huonwa kwa kawaida katika ujenzi wa kulipwa katika Brazili.”
Ukuzi Wenye Kuendelea Kwenye Makao Makuu ya Ulimwengu
Wakati matawi ya Watch Tower Society yamekuwa yakikua, imehitajiwa pia kupanua vifaa vya makao makuu ya ulimwengu. Kumekuwa maongezeko makubwa kwenye makao ya kiwanda na ofisi zayo katika Brooklyn na katika mahali pengine katika Jimbo la New York zaidi ya mara kumi tangu Vita ya Ulimwengu 2. Ili kuwapa makao wafanyakazi, imekuwa lazima kujenga au kununua na kurekebisha majengo mengi, makubwa na madogo pia. Upanuzi mwingine mkubwa katika Brooklyn ulitangazwa katika Agosti 1990 na katika Januari 1991—hata ingawa kaskazini mwa New York City ujenzi mkubwa ulioanza katika 1989 ulikuwa ukiendelea kwenye Kitovu cha Elimu cha Watchtower, ambacho kilikusudiwa kuwapa makao watu 1,200, kutia na wafanyakazi na wanafunzi.
Tangu 1972, kazi ya ujenzi haijaacha kufanywa kwenye makao makuu ya ulimwengu katika Brooklyn na vifaa vyayo vinavyohusiana karibukaribu katika sehemu nyingine za New York na katika New Jersey. Baada ya muda, ilipata kuwa wazi kwamba hata ingawa idadi yao ilifikia mamia, wafanyakazi wa ujenzi wa kawaida walishindwa kuiweza kazi. Kwa hiyo, katika 1984 programu yenye kuendelea ya wafanyakazi wa muda ilianzishwa. Barua zilipelekwa kwa yale ambayo wakati huo yalikuwa makutaniko 8,000 katika Marekani kualika ndugu wenye kustahili waje wasaidie kwa juma moja au zaidi. (Programu kama hiyo ilikuwa tayari imefanya kazi vizuri katika baadhi ya yale matawi, kutia na Australia, ambako wale walioweza kukaa majuma mawili walialikwa wajitolee.) Wafanyakazi wangepewa makao na chakula lakini wangelipia gharama zao za usafiri na hawangepokea mishahara. Ni nani wangeitikia?
Kufikia 1992, maombi zaidi ya 24,000 yalikuwa yameshughulikiwa! Angalau 3,900 kati ya hawa walikuwa watu waliokuwa wakirudi kwa mara ya 2, ya 3, hata ya 10 au ya 20. Walio wengi wao walikuwa wazee, watumishi wa huduma, au mapainia—watu binafsi wenye sifa nzuri za kiroho. Wote walikuwa wakijitolea kufanya lolote lililohitajiwa, iwe hiyo iliwataka watumie ufundi wao au la. Mara nyingi kazi ilikuwa nzito na chafu. Lakini walilihesabu kuwa pendeleo kuchanga katika njia hiyo kusogeza mbele masilahi ya Ufalme. Baadhi yao walihisi hiyo iliwasaidia kuthamini vizuri zaidi ile roho ya kujidhabihu inayoonyesha aina ya kazi ifanywayo kwenye makao makuu ya ulimwengu. Wote walihisi kuwa walithawabishwa sana kwa sababu ya kuwapo kwa ajili ya programu ya familia ya Betheli ya ibada ya asubuhi na funzo la Mnara wa Mlinzi la familia lifanywalo kila juma.
Wenye Kujitolea wa Kimataifa
Kadiri uhitaji wa upanuzi wa kasi ulivyokua, mpango wa wenye kujitolea wa kimataifa ulianzishwa katika 1985. Hiyo kwa vyovyote haikuwa ndiyo mara ya kwanza kuwa na ushirikiano wa kimataifa katika ujenzi, lakini sasa mpango huo uliratibiwa kwa uangalifu kutoka makao makuu. Wote ambao hushiriki ni Mashahidi ambao hujitolea kusaidia kazi ya ujenzi nje ya nchi zao wenyewe. Wao ni wafanyakazi stadi, pamoja na wenzi wa ndoa ambao huenda pamoja na waume zao kusaidia kwa njia yoyote wawezayo. Walio wengi wao hulipia nauli zao wenyewe; hakuna wanaopewa mshahara kwa ajili ya kile wafanyacho. Baadhi yao huenda kwa muda mfupi, kwa kawaida wakikaa kuanzia majuma mawili hadi miezi mitatu. Wengine ni wenye kujitolea wa muda mrefu, wakikaa kwa mwaka au zaidi, labda mpaka ujenzi unapokamilika. Mashahidi wa Yehova zaidi ya 3,000 kutoka nchi mbalimbali 30 walishiriki sehemu katika kazi hiyo wakati wa miaka mitano ya kwanza, na wengi zaidi walikuwa na hamu ya kushiriki kadiri stadi zao zilivyohitajiwa. Wao hulihesabu kuwa pendeleo kujitoa wenyewe na mali zao ili kusogeza mbele masilahi ya Ufalme wa Mungu kwa njia hiyo.
Wafanyakazi wa kujitolea wa kimataifa huandaliwa makao na milo. Mara nyingi starehe ni ndogo kabisa. Mashahidi wenyeji huthamini sana yale yanayofanywa na ndugu zao wenye kuzuru, na inapowezekana, wao huwakaribisha nyumbani mwao, hata iwe sahili namna gani. Mara nyingi sana milo huliwa kwenye mahali pa kazi.
Ndugu wa kutoka ng’ambo hawawi hapo ili kufanya kazi yote. Lengo lao ni kufanya kazi pamoja na kikundi cha ujenzi cha wenyeji. Na mamia, hata maelfu, ya wengine katika nchi huenda pia wakaja kusaidia wakati wa miisho-juma au kwa juma moja au zaidi kwa wakati mmoja. Katika Argentina, wenye kujitolea 259 kutoka nchi nyingine walifanya kazi pamoja na maelfu kadhaa ya ndugu wenyeji, baadhi yao walikuwapo kwa ajili ya kazi kila siku, wengine kwa majuma machache, na wengine zaidi wakati wa miisho-juma. Katika Kolombia, wenye kujitolea wa kimataifa zaidi ya 830 walisaidia kwa vipindi mbalimbali vya wakati. Kulikuwa pia wenye kujitolea wenyeji zaidi ya 200 walioshiriki katika mradi huo kwa wakati wote, na wasaidizi wengine 250 au zaidi kila mwisho-juma. Jumla ya zaidi ya watu mmoja-mmoja tofauti 3,600 walishiriki.
Tofauti ya lugha yaweza kutokeza matatizo, lakini haizuii vikundi vya kimataifa visifanye kazi pamoja. Lugha ya ishara, ishara za uso, ucheshi, na tamaa ya kuona kazi itakayomheshimu Yehova ikikamilishwa husaidia kazi ifanywe.
Ukuzi wa tengenezo wenye kutokeza—ukitokeza uhitaji wa makao makubwa ya tawi—nyakati nyingine hutokea katika nchi ambako idadi ya watu wenye stadi katika ufundi wa ujenzi ni ndogo. Lakini hicho si kizuizi miongoni mwa Mashahidi wa Yehova, ambao husaidiana kwa furaha. Wao hufanya kazi pamoja wakiwa sehemu ya familia ya duniani pote ambayo haigawanywi na taifa, rangi ya ngozi, au lugha.
Katika Papua New Guinea, wenye kujitolea waliotoka Australia na New Zealand kila mmoja alizoeza raia wa Papua New Guinea kazi yake ya kiufundi, kupatana na ombi la Idara ya Wafanyakazi ya Serikali. Katika njia hiyo, huku wakijitoa wenyewe, Mashahidi wenyeji walijifunza kazi za ufundi ambazo zingeweza kuwasaidia kutosheleza mahitaji yao wenyewe na ya familia zao.
Wakati tawi jipya lilipohitajiwa katika El Salvador, wenye kujitolea 326 kutoka ng’ambo walijiunga na ndugu wenyeji. Kwa ajili ya mradi wa ujenzi katika Ekuado, Mashahidi 270 kutoka nchi 14 walifanya kazi pamoja na ndugu na dada Waekuado. Baadhi ya wenye kujitolea wa kimataifa walisaidia katika miradi kadhaa ya ujenzi iliyokuwa ikiendelea wakati uleule mmoja. Walifanya kazi kwa zamu katika mahali pa ujenzi katika Ulaya na Afrika, kulingana na uhitaji wa stadi zao za kiufundi.
Kufikia 1992, wenye kujitolea wa kimataifa walikuwa wamepelekwa sehemu 49 za matawi ili kusaidia vikundi vya ujenzi vya wenyeji. Katika visa fulani wale waliopokea msaada kutokana na programu hii waliweza pia kuandaa usaidizi kwa wengine. Hivyo, wakiwa wamenufaika na kazi za bidii za watumishi wa muda mrefu wa kimataifa kama 60 waliosaidia na ujenzi wa mradi wa tawi katika Filipino, pamoja na wenye kujitolea zaidi ya 230 kutoka ng’ambo waliosaidia kwa vipindi vifupi zaidi, baadhi ya Wafilipino walijitoa wenyewe ili kusaidia kujenga vifaa katika sehemu nyingine za Kusini-Mashariki mwa Asia.
Kazi ya ujenzi inafanywa na Mashahidi wa Yehova kwa sababu ya mahitaji yaliyoko sasa kuhusiana na kazi ya kuhubiri habari njema. Kwa msaada wa roho ya Yehova, wanataka kutoa ushahidi ulio mkubwa zaidi iwezekanavyo katika pindi ya wakati unaobaki kabla ya Har–Magedoni. Wanasadiki kwamba ulimwengu mpya wa Mungu u karibu sana, na wana imani kwamba wataokoka wakiwa watu waliofanywa tengenezo waingie katika huo ulimwengu mpya, chini ya utawala wa Ufalme wa Kimesiya wa Mungu. Pia ni tumaini lao kwamba labda vingi kati ya vifaa vizuri ambavyo wamejenga na kuviweka wakfu kwa Yehova vitaendelea kutumiwa baada ya Har–Magedoni vikiwa vitovu vya kueneza ujuzi wa yule Mungu wa kweli peke yake mpaka ujuzi huo ujaze dunia kwelikweli.—Isa. 11:9.
[Maelezo ya Chini]
a Liliitwa Kanisa la “Nuru Mpya” kwa sababu wale walioshirikiana humo walihisi kwamba kama tokeo la kusoma vichapo vya Watch Tower, walikuwa na nuru mpya ya uelewevu juu ya Biblia.
[Blabu katika ukurasa wa 322]
Mashahidi kutoka makutaniko ya karibu walisaidia kazi
[Blabu katika ukurasa wa 323]
Kazi ya ujenzi ilifanywa na wafanyakazi wa kujitolea, wasiolipwa
[Blabu katika ukurasa wa 324]
Mkazo ulitiwa juu ya sifa za kiroho
[Blabu katika ukurasa wa 326]
Ujenzi bora, usalama, gharama ndogo sana, uharaka
[Blabu katika ukurasa wa 328]
Jumba la Kusanyiko lenye kubebeka!
[Blabu katika ukurasa wa 331]
Kwenda mahakamani
[Blabu katika ukurasa wa 332]
Upanuzi wa kimataifa wa kadiri kubwa
[Blabu katika ukurasa wa 333]
Wafanyakazi walitoa sifa kwa Yehova, si kwao wenyewe
[Blabu katika ukurasa wa 334]
Ukuzi kwa kadiri ambayo hakuna binadamu angeweza kubashiri
[Blabu katika ukurasa wa 336]
Walikuhesabu kuwa pendeleo kusaidia kujenga kwenye makao makuu
[Blabu katika ukurasa wa 339]
Wao hufanya kazi wakiwa familia ya duniani pote, ambayo haigawanywi na taifa, rangi ya ngozi, au lugha
[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 320, 321]
Kufanya Kazi Pamoja ili Kujenga Haraka Majumba ya Ufalme
Maelfu ya makutaniko mapya huundwa kila mwaka. Katika visa vingi, Majumba ya Ufalme mapya hujengwa na Mashahidi wenyewe. Picha hizi zilipigwa wakati wa ujenzi wa Jumba la Ufalme katika Connecticut, Marekani, katika 1991
Ijumaa, saa 1:40 asubuhi
Ijumaa, saa 6 adhuhuri
Jumamosi, saa 1:41 jioni
Kazi kubwa yakamilika, Jumapili, saa 12:10 jioni
Wamtegemea Yehova kwa baraka yake, na huchukua wakati kuzungumzia shauri kutoka Neno lake
Wote ni wenye kujitolea wasiolipwa, wenye furaha kufanya kazi mmoja kando ya mwenzake
[Picha katika ukurasa wa 327]
Majumba ya Ufalme Katika Nchi Mbalimbali
Mahali pa mikutano patumiwapo na Mashahidi wa Yehova kwa kawaida huwa penye kiasi. Ni safi, penye starehe, katika mazingira yenye kuvutia
Peru
Filipino
Ufaransa
Jamhuri ya Korea
Japani
Papua New Guinea
Ireland
Kolombia
Norway
Lesotho
[Picha katika ukurasa wa 330]
Majumba ya Kusanyiko ya Mashahidi wa Yehova
Ili kuwa na mahali pa makusanyiko yao ya pindi kwa pindi, Mashahidi wa Yehova katika baadhi ya maeneo wameona kuwa jambo lenye kufaa kujenga Majumba ya Kusanyiko yao wenyewe. Kazi iliyo nyingi hufanywa na Mashahidi wenyeji. Hapa pana machache tu ya majumba hayo yaliyokuwa yakitumiwa katika miaka ya mapema ya 1990
Uingereza
Venezuela
Italia
Ujerumani
Kanada
Japani
[Picha katika ukurasa wa 338]
Programu ya Ujenzi wa Kimataifa Hutimiza Mahitaji ya Haraka
Ukuzi wa kasi wa tengenezo umetaka upanuzi wenye kuendelea wa ofisi, viwanda, na makao ya Betheli duniani pote
Wenye kujitolea wa kimataifa hutoa usaidizi kwa Mashahidi wenyeji
Hispania
Njia za ujenzi zitumiwazo hufanya wenye kujitolea wengi wasiokuwa na ujuzi waweze kufanya kazi yenye thamani
Puerto Riko
Wafanyakazi stadi hutoa huduma zao kwa furaha
New Zealand
Ugiriki
Brazili
Matumizi ya vifaa vyenye kudumu husaidia kupunguza gharama za muda mrefu za udumishaji
Uingereza
Kazi bora sana hutokana na kupendezwa kwa binafsi kwa upande wa wenye kuifanya; hiyo ni wonyesho wa upendo wao kwa Yehova
Kanada
Ujenzi huo mbalimbali ni pindi za shangwe; urafiki mwingi wenye kudumu hufanyizwa
Kolombia
Ishara katika Japani zilikumbusha wafanyakazi juu ya hatua za usalama, pia juu ya uhitaji wa kuonyesha matunda ya roho ya Mungu
[Picha katika ukurasa wa 318]
Jengo la kwanza lililoitwa Jumba la Ufalme, katika Hawaii
[Picha katika ukurasa wa 319]
Majumba ya Ufalme mengi ya mapema yalikuwa majengo yaliyokodiwa au yalikuwa vyumba tu vilivyokuwa juu ya maduka; machache yalijengwa na Mashahidi
[Picha katika ukurasa wa 329]
Mawili ya Majumba ya Kusanyiko ya kwanza
New York City
Guadeloupe
[Picha katika ukurasa wa 337]
Wafanyakazi wa muda wa ujenzi waliotoka tu kuwasili kwenye makao makuu katika New York
Kila kikundi hukumbushwa kwamba kuwa mtu wa kiroho na kufanya kazi bora hutangulizwa juu ya kufanya kazi haraka
-
-
Yote Hayo Hugharimiwaje?Mashahidi wa Yehova—Wapiga-Mbiu wa Ufalme wa Mungu
-
-
Sura ya 21
Yote Hayo Hugharimiwaje?
NI WAZI kwamba kazi inayoendeshwa na Mashahidi wa Yehova hutaka fedha. Kujenga Majumba ya Ufalme, Majumba ya Kusanyiko, ofisi za tawi, viwanda, na makao ya Betheli huhusisha fedha, na fedha zaidi huhitajiwa ili kuyadumisha. Inagharimu pia kutangaza na kugawanya fasihi kwa ajili ya funzo la Biblia. Yote hayo hugharimiwaje?
Mawazo yasiyo na msingi kuhusu jambo hilo yameenezwa hadharani na watu wapingao kazi ya Mashahidi wa Yehova. Lakini mambo ya hakika yanaunga mkono jibu walitoalo Mashahidi wenyewe. Ni jipi hilo? Kazi nyingi hufanywa na watu wenye kujitolea, ambao hawatarajii na hawataki kulipwa fedha kwa ajili ya utumishi wao mbalimbali, na gharama za kitengenezo hulipiwa kwa upaji wa hiari.
“Viti Ni vya Bure. Hakuna Viingilio”
Mapema sana kama toleo la pili la Watch Tower, katika Agosti 1879, Ndugu Russell alitaarifu hivi: “Twaamini ‘Zion’s Watch Tower’ lina YEHOVA akiwa mtegemezaji walo, na inapokuwa hivyo halitaombaomba wala kusihi wanadamu walitegemeze. Wakati Yeye asemaye: ‘Dhahabu na fedha zote za milimani ni zangu,’ ashindwapo kuandaa fedha zihitajiwazo, sisi tutaelewa kwamba ni wakati wa kuacha kuchapa.” Kupatana na hilo, fasihi za Mashahidi wa Yehova haziombiombi fedha.
Kama ilivyo kwa fasihi zao ndivyo ilivyo kwa habari ya mikutano yao. Hakuna maombi ya kuchochea hisiamoyo ili kupata fedha katika mikutano yao au kwenye mikusanyiko yao. Hakuna visahani vya michango ambavyo hupitishwa; hakuna bahasha ambazo hugawanywa za kuweka fedha; hakuna barua za kuombaomba fedha ambazo hupelekwa kwa washiriki wa makutaniko. Makutaniko hayachezi kamari au kushindania zawadi ili kupata fedha. Mapema sana kama 1894, wakati Watch Tower Society ilipotuma wasemaji wasafirio, ilitoa tangazo hili kwa manufaa ya kila mtu: “Na ieleweke tokea mwanzo kwamba kukusanya michango au njia nyinginezo za kuombaomba fedha hazikubaliwi wala kukubaliwa na Sosaiti hii.”
Hivyo, tangu mapema sana katika historia yao ya kisasa, vikaratasi vya mwaliko na mialiko mingineyo inayochapwa kwa ajili ya umma ili kuhudhuria mikutano ya Mashahidi wa Yehova huwa na shime “Viti Ni vya Bure. Hakuna Viingilio.”
Kuanzia mapema katika 1914, Wanafunzi wa Biblia walikodi majumba ya maonyesho pamoja na majumba mengine ya mikutano na kualika umma ili waje kuona “Photo-Drama of Creation.” Huo ulikuwa utoaji wenye sehemu nne, saa nane kwa ujumla, uliofanyizwa kwa slaidi na sinema zilizoambatanishwa na sauti. Wakati wa mwaka wa kwanza pekee, mamilioni ya watu waliuona katika Amerika Kaskazini, Ulaya, Australia, na New Zealand. Ijapokuwa baadhi ya wenyeji wa majumba ya maonyesho walitoza fedha kwa ajili ya viti vilivyohifadhiwa, Wanafunzi wa Biblia hawakuomba kamwe fedha kwa wenye kuingia ili kutazama. Na hakuna michango iliyokusanywa.
Baadaye, kwa miaka zaidi ya 30, Watch Tower Society iliendesha kituo cha redio WBBR katika New York City. Mashahidi wa Yehova walitumia pia utumishi mbalimbali wa mamia ya vituo vingine ili kutangaza programu za elimu ya Biblia. Lakini hawakutumia kamwe vituo kama hivyo ili kuombaomba fedha.
Basi, ule upaji ambao hugharimia utendaji wao hupatikanaje?
Hutegemezwa kwa Upaji wa Kujitolea
Biblia huweka kigezo. Chini ya Sheria ya Musa, kulikuwa michango fulani iliyotolewa kwa hiari. Mingine watu walitakwa waitoe. Kutoa zaka, au sehemu ya kumi, kulikuwa mojayapo michango ya lazima. (Kut. 25:2; 30:11-16; Hes. 15:17-21; 18:25-32) Lakini Biblia huonyesha pia kwamba Kristo alitimiza ile Sheria, naye Mungu akaikomesha; hivyo Wakristo hawafungwi tena na amri zayo. Wao hawatoi sehemu ya kumi, wala hawako chini ya wajibu wa kutoa michango mingine yoyote ya kiasi hususa au kwa wakati hususa.—Mt. 5:17; Rum. 7:6; Kol. 2:13, 14.
Badala ya hivyo, wao hutiwa moyo wasitawishe roho ya ukarimu na upaji wa hiari kwa kuiga kielelezo kizuri ajabu kilichowekwa na Yehova mwenyewe na Mwana wake, Yesu Kristo. (2 Kor. 8:7, 9; 9:8-15; 1 Yoh. 3:16-18) Hivyo, kwa habari ya kutoa, mtume Paulo aliandikia kutaniko la Kikristo katika Korintho hivi: “Acheni kila mmoja afanye kama vile ameazimia moyoni mwake, si kwa kinyongo au kwa shurutisho, kwa maana Mungu hupenda mpaji mchangamfu.” Walipojulishwa juu ya uhitaji fulani, jambo hilo liliwapa ‘jaribu la unyofu wa upendo wao,’ kama vile Paulo alivyoeleza. Yeye alisema pia: “Ikiwa utayari upo kwanza, hukubalika hasa kulingana na alicho nacho mtu, si kulingana na kile ambacho mtu hana.”—2 Kor. 8:8, 12; 9:7, NW.
Kwa kufikiria hayo, maelezo yaliyotolewa na Tertuliano kuhusu mikutano iliyofanywa na watu waliojitahidi kuzoea Ukristo katika siku zake (karibu 155–baada ya 220 W.K.) lapendeza. Yeye aliandika hivi: “Hata ingawa kuna kisanduku cha aina fulani, hakikufanyizwa kwa fedha zilizolipwa zikiwa viingilio, kana kwamba dini ilikuwa jambo la mkataba. Mara moja kwa mwezi kila mtu huleta sarafu ndogo—au wakati wowote atakapo, na ikiwa tu ataka, na ikiwa aweza; maana hapana mtu alazimishwaye; ni toleo la hiari.” (Apology, 39, 5) Hata hivyo, wakati wa karne nyingi tangu hapo, makanisa ya Jumuiya ya Wakristo yamejitia katika kila aina ya mbinu ya kujipatia fedha ili kugharimia shughuli zayo.
Charles Taze Russell alikataa kuiga makanisa. Yeye aliandika hivi: “Ni maoni yetu kwamba fedha zinazopatikana kwa zile mbinu mbalimbali za kuombaomba katika jina la Bwana wetu ni zenye kumchukiza, hazikubaliki kwake, nazo hazileti baraka yake ama juu ya wapaji ama juu ya kazi itimizwayo.”
Badala ya kujaribu kupata upendeleo wa wale waliokuwa na mali, Ndugu Russell alitaarifu waziwazi, kupatana na Maandiko, kwamba wengi wa watu wa Bwana wangekuwa maskini katika mali za ulimwengu huu lakini tajiri katika imani. (Mt. 19:23, 24; 1 Kor. 1:26-29; Yak. 2:5) Badala ya kukazia uhitaji wa fedha ili kueneza kweli ya Biblia, yeye alikazia fikira umaana wa kusitawisha roho ya upendo, tamaa ya kutoa, na tamaa ya kusaidia wengine, hasa kwa kushiriki kweli pamoja nao. Kwa wale waliokuwa na uwezo wa kuchuma fedha na ambao walidokeza kwamba kwa kujitoa wenyewe sana kwa mambo ya kibiashara wangekuwa na vingi zaidi vya kuchanga kifedha, yeye alisema kwamba ingekuwa afadhali wapunguze utendaji huo na kujitoa wenyewe na wakati wao katika kueneza kweli. Huo ungali ndio msimamo uchukuliwao na Baraza Linaloongoza la Mashahidi wa Yehova.a
Kihalisi, watu hutoa kiasi gani? Yale wanayofanya ni uamuzi wao binafsi. Hata hivyo, kwa habari ya kutoa, yapasa kuangaliwa kwamba Mashahidi wa Yehova hawafikiri tu juu ya kutoa mali za kimwili. Kwenye mikusanyiko yao ya wilaya katika 1985-1986, walizungumza juu ya kichwa cha habari “Kumheshimu Yehova kwa Vitu Vyetu vya Thamani.” (Mit. 3:9) Ilikaziwa kwamba vitu hivyo vya thamani hutia ndani si mali za kimwili tu bali pia nguvu zetu za kimwili, za kiakili, na za kiroho.
Huko nyuma katika 1904, Ndugu Russell alitaja kwamba mtu ambaye amejitakasa kabisa (au, kujiweka wakfu, kama tusemavyo sasa) kwa Mungu “amekwisha toa vyote alivyo navyo kwa Bwana.” Hivyo, apaswa sasa “kujifikiria mwenyewe kuwa amewekwa na Bwana kuwa msimamizi wa wakati wake mwenyewe, uvutano, fedha, n.k., na kila mmoja atatafuta kutumia talanta hizo kwa kadiri awezavyo, kwa utukufu wa Bwana-Mkubwa.” Yeye aliongeza kwamba, kwa kuongozwa na hekima kutoka juu, “kwa kadiri upendo na bidii yake vinavyokua kwa ajili ya Bwana siku kwa siku kupitia ujuzi wa Kweli na kupata roho yayo, atajikuta akitoa wakati zaidi na zaidi, na uvutano wake zaidi na zaidi, na mali alizo nazo zaidi na zaidi, kwa ajili ya utumishi wa Kweli.”—Studies in the Scriptures, “The New Creation,” kur. 344-345.
Wakati wa miaka hiyo ya mapema, Watch Tower Society ilikuwa na ile iliyoitwa Hazina ya Tower Tract. Hiyo ilikuwa nini? Habari hii yenye kupendeza iliandikwa upande wa nyuma wa karatasi na bahasha zilizotumiwa nyakati nyingine na Ndugu Russell: “Hazina hii huwa na matoleo ya hiari ya wale ambao wamelishwa na kuimarishwa na ‘nyama kwa wakati wake’ ambayo vichapo vilivyo juu [vitolewavyo na Watch Tower Society], vikiwa vyombo vya Mungu, vinatolea sasa watakatifu waliojitakasa, ulimwenguni pote.
“Hazina hii hutumiwa daima katika kupeleka nje, bila malipo, maelfu ya nakala za ZION’S WATCH TOWER na OLD THEOLOGY TRACTS ziwafaazo sana wasomaji wapya. Husaidia pia katika kueneza vitabu vilivyojalidiwa kwa karatasi vya mfululizo wa DAWN, kwa kusaidia wale walio tayari kuzieneza—makolpota na wengine. Pia huandalia ‘hazina ya maskini’ ambayo yeyote wa watoto wa Bwana ambaye, kwa sababu ya uzee, au ugonjwa, au kwa sababu nyingine, hawawezi kuandikisha WATCH TOWER wanapewa ugavi bila malipo, kwa sharti la kwamba wapeleka barua au kadi mwanzoni mwa kila mwaka, wakitaarifu tamaa na kutoweza kwao.
“Hapana mtu aulizwaye wakati wowote achangie hazina hii: upaji wote lazima uwe wa hiari. Sisi hukumbusha wasomaji wetu maneno ya Mtume (1 Kor. 16:1, 2) na huyathibitisha kwa kusema kwamba wale wanaoweza kutoa na wanaotoa ili kueneza kweli hakika watalipwa kwa mapendeleo ya kiroho.”
Utendaji wa duniani pote wa Mashahidi wa Yehova katika kupiga mbiu ya habari njema za Ufalme wa Mungu huendelea kutegemezwa kwa upaji wa hiari. Kuongezea Mashahidi wenyewe, watu wengi wenye kupendezwa wenye uthamini hulihesabu kuwa pendeleo kutegemeza kazi ya Kikristo kwa michango yao ya kutoa kwa hiari.
Kugharimia Mahalimahali pa Mikutano pa Kwetu
Kila kutaniko la Mashahidi wa Yehova lina visanduku vya mchango vifaavyo mahali ambapo watu waweza kuweka upaji wowote watakao—wapendapo kufanya hivyo na ikiwa wanaweza. Hushughulikiwa kwa njia ya faragha hivi kwamba kwa kawaida wengine huwa hawajui kiasi ambacho mtu anatoa. Ni jambo ambalo ni yeye na Mungu tu hujua.
Hakuna mishahara ya kulipwa, lakini inagharimu fedha kudumisha mahali pa mikutano. Ili kutimiza uhitaji huo, washiriki wa kutaniko lazima waarifiwe. Hata hivyo, zaidi ya miaka 70 iliyopita, The Watch Tower lilijulisha wazi kwamba kwa habari ya michango, hakupasi kuwe na kusihisihi au kuhimiza—ni taarifa tu iliyo wazi, ya unyoofu juu ya mambo ya hakika. Kupatana na maoni hayo, mikutano ya kutaniko haitii ndani mazungumzo ya mara kwa mara ya mambo ya kifedha.
Hata hivyo, nyakati nyingine, kunakuwa na mahitaji ya pekee. Huenda ikawa kwamba mipango inafanywa ya kurekebisha upya au kuongeza ukubwa wa Jumba la Ufalme au labda kujenga jipya. Ili kuhakikisha ni kiasi gani cha fedha kitakachopatikana, wazee waweza kuuliza wale walio kutanikoni waandike juu ya vikaratasi kiasi wanachotarajia kuchangia mradi huo au, ikiwezekana, kufanya kipatikane kwa miaka kadhaa. Kwa kuongezea, wazee waweza kuuliza kwamba watu mmoja-mmoja au familia waandike kwenye vikaratasi kiasi wanachohisi wataweza kuchanga kila juma au kila mwezi, kwa baraka za Yehova. Hakuna majina yanayoandikwa. Hivi si hati za kuahidi kulipa, bali huandaa msingi wa kupanga mambo kwa njia yenye akili.—Luka 14:28-30.
Katika Tarma, Liberia, kutaniko lilipata fedha lilizohitaji kwa njia iliyo tofauti kidogo. Wengine kutanikoni walikuza mpunga kwa ajili ya Shahidi mmoja katika shamba lake huku yeye akijitoa kwa mwaka mzima kwa kazi ya kukata miti na kupasua mbao, ambazo ziliuzwa ili kupata fedha kwa ajili ya mradi wa ujenzi. Katika Paramaribo, Suriname, ijapokuwa vifaa vilihitaji kununuliwa, kutaniko halikuhitaji fedha ili kununua ardhi kwa sababu Shahidi mmoja alichanga ardhi yake kwa ajili ya Jumba la Ufalme, akaomba tu kwamba nyumba yake ihamishiwe nyuma ya kiwanja. Bei kubwa mno ya shamba na nyumba katika Tokyo, Japani, ilifanya iwe vigumu kwa makutaniko ya huko kupata ardhi ya kujengea Majumba ya Ufalme. Ili kusaidia kutatua tatizo hilo, familia kadhaa zilitoa matumizi ya ardhi ambayo juu yayo makao yao wenyewe yalijengwa. Waliomba tu kwamba baada ya Jumba la Ufalme jipya kujengwa mahali makao yao yalipokuwa, waandaliwe chumba juu ya jumba.
Kadiri makutaniko yalivyokua na kugawanywa, wale waliokuwa katika eneo lolote lile walijaribu kusaidiana ili kuandaa Majumba ya Ufalme yafaayo. Ijapokuwa hiyo roho ya ukarimu, jambo jingine lilihitajiwa. Bei za viwanja na gharama za ujenzi ziliongezeka sana, na mara nyingi makutaniko moja moja yaliliona kuwa jambo lisilowezekana kulipa gharama hizo. Ni jambo gani lingeweza kufanywa?
Kwenye “Umoja wa Ufalme” Mikusanyiko ya Wilaya katika 1983, Baraza Linaloongoza lilieleza mpango uliotaka kutumiwa kwa kanuni iliyoandikwa kwenye 2 Wakorintho 8:14, 15 (NW), ambayo hutia moyo kuruhusu ziada ya wale waliyo nayo isawazishe upungufu wa wale wengine ili “usawazisho upate kutukia.” Hivyo wale walio na vichache hawatakuwa na vichache mno hivi kwamba wazuiwe katika jitihada za kumtumikia Yehova.
Kila kutaniko lilialikwa kupanga kuwe na kisanduku kilichoandikwa “Michango kwa Ajili ya Hazina ya Sosaiti ya Jumba la Ufalme.” Kila kitu kilichotiwa humo kingetumiwa kwa kusudi hilo tu. Hivyo, fedha zilizochangwa kotekote nchini zingetumiwa kusawazisha upungufu wa makutaniko yaliyohitaji sana Jumba la Ufalme lakini ambayo hayangeweza kupanga kuwa nalo kwa sababu ya masharti yaliyowekwa na benki za mahali. Baada ya uchunguzi wa uangalifu ili kuhakikisha ni wapi uhitaji ulikokuwa mkubwa kwelikweli, Sosaiti ilianza kufanya fedha hizo zipatikane ili kuwezesha makutaniko yajenge au yajipatie Majumba ya Ufalme mapya. Kadiri michango zaidi ilivyopokewa na (katika nchi ambako ingeweza kufanywa) mikopo ikalipwa, bado makutaniko zaidi yangeweza kusaidiwa.
Mpango huo ulianza kutumiwa kwanza katika Marekani na Kanada, na tangu hapo umeenea kwenye zaidi ya nchi 30 katika Ulaya, Afrika, Amerika ya Latin, na Mashariki ya Mbali. Kufikia 1992, katika nane tu kati ya nchi hizo, fedha zilikuwa zimekwisha tolewa kusaidia kuandaa Majumba ya Ufalme 2,737, yakitumiwa na makutaniko 3,840.
Hata katika nchi ambako mpango huo haukuwa ukitenda, lakini ambako kulikuwa na uhitaji mkubwa wa Majumba ya Ufalme ambayo hayangeweza kugharimiwa na wenyeji, Baraza Linaloongoza lilijitahidi kufanya mipango mingine ili kuhakikisha kwamba msaada uliandaliwa. Hivyo usawaziko ulitukia, hivi kwamba wale waliokuwa na vichache hawakuwa na vichache mno.
Kushughulikia Upanuzi wa Makao Makuu ya Ulimwengu
Uendeshaji wa makao makuu ya ulimwengu umehitaji fedha pia. Kufuatia Vita ya Ulimwengu 1, wakati Watch Tower Bible and Tract Society ilipoliona kuwa jambo lenye kunufaisha kuchapa na kujalidi vitabu vyayo yenyewe, mpango ulifanywa ambao kwao mashine zilizohitajiwa zilinunuliwa kwa majina ya watu binafsi—watumishi wenzi wa Yehova. Badala ya kulipa faida kwa kampuni za kibiashara kwa kutengeneza vitabu, Sosaiti ilitumia kiasi hicho kila mwezi ili kupunguza deni la vifaa. Kadiri manufaa za kufanya hivyo zilivyopatikana, bei ya fasihi kwa umma ilipunguzwa kwa karibu nusu. Jambo lililokuwa likifanywa lilikuwa kusongeza mbele kazi ya kuhubiri habari njema, si kutajirisha Watch Tower Society.
Katika muda wa miaka michache, ilikuwa wazi kwamba vifaa vikubwa zaidi vilihitajiwa kwenye makao makuu ya ulimwengu ili kushughulikia kazi ya duniani pote ya kuhubiri Ufalme. Tena na tena, kadiri ambavyo tengenezo limekua na utendaji wa kuhubiri umeongezwa, imekuwa lazima kuongeza vifaa hivyo. Badala ya kuendea mabenki kupata fedha zilizohitajiwa ili kuongeza na kuzipa vifaa ofisi na viwanda vya makao makuu pamoja na vifaa vya ziada katika New York na viunga vyalo, Sosaiti imeeleza akina ndugu uhitaji huo. Jambo hilo limefanywa, si mara nyingi, bali mara 12 kwa kipindi cha miaka 65.
Hakujapata kamwe kuwa na kuombaomba. Wowote waliotaka kutoa upaji walialikwa kufanya hivyo. Wale waliochagua kutoa fedha walihakikishiwa kwamba kukitokea uhitaji usiotazamiwa na wa haraka, mkopo wao ungelipwa ombi lao lipokewapo. Hivyo katika kushughulikia mambo, Sosaiti ilijitahidi kuepuka kusababisha magumu kwa watu mmoja-mmoja na kwa makutaniko ambayo yalitoa fedha kwa fadhili. Utegemezo uliotolewa na Mashahidi wa Yehova kwa njia ya michango yao umewezesha Sosaiti kulipa mikopo yote sikuzote. Michango hiyo iliyopelekwa kwa Sosaiti haipokewi bila shukrani. Kwa kadiri iwezekanavyo, hiyo hushukuriwa kwa njia ya barua na taarifa nyinginezo za uthamini.
Kazi ya tengenezo haitegemezwi kwa upaji wa kikundi cha wapaji matajiri. Michango mingi hutoka kwa watu mmoja-mmoja ambao wana mali kidogo tu—wengi wao, wakiwa na mali kidogo sana za ulimwengu huu. Wanaotiwa ndani ni watoto wachanga ambao hutaka kushiriki kwa njia hiyo katika kuunga mkono kazi ya Ufalme. Mioyo ya wapaji hao wote husukumwa na uthamini mwingi wa wema wa Yehova na tamaa ya kusaidia wengine wajifunze juu ya maandalizi yake yenye neema.—Linganisha Marko 12:42-44.
Kugharimia Upanuzi wa Vifaa vya Tawi
Kwa kuwa kazi ya kuhubiri Ufalme imeongezeka zaidi katika sehemu mbalimbali za ulimwengu, imehitajika kuongeza ukubwa wa vifaa vya tawi vya tengenezo. Hiyo hufanywa chini ya mwelekezo wa Baraza Linaloongoza.
Hivyo, baada ya kupitia mapendekezo kutoka tawi la Ujerumani, mielekezo ilitolewa katika 1978 ya kupata ardhi ifaayo, kisha kujenga majengo makubwa mapya kabisa. Je, Mashahidi Wajerumani wangeweza kushughulikia gharama zilizohusika? Fursa ilitolewa kwao. Wakati wa kukamilishwa kwa mradi huo katika 1984, katika Selters, kwenye ukingo wa magharibi wa Milima Taunus, ofisi ya tawi iliripoti hivi: “Makumi ya maelfu ya Mashahidi wa Yehova—matajiri kwa maskini, vijana kwa wazee—walichanga mamilioni ya dola ili kusaidia kulipia vile vifaa vipya. Kwa sababu ya ukarimu wao, mradi wote ungeweza kukamilishwa bila uhitaji wa kukopa fedha kutoka mashirika ya kilimwengu au kuingia katika deni.” Kwa kuongezea, karibu 1 kati ya kila Mashahidi 7 katika Jamhuri ya Muungano ya Ujerumani alikuwa ameshiriki kazi yenyewe ya ujenzi katika Selters/Taunus.
Katika nchi fulani, uchumi wa nchi au hali ya kifedha ya Mashahidi wa Yehova imefanya iwe vigumu sana, hata isiwezekane, kwao kujenga ofisi za tawi zilizohitajiwa ili kusimamia kazi au viwanda vya kutangazia fasihi za Biblia kwa lugha za wenyeji. Mashahidi katika nchi wamepewa fursa ya kufanya wawezavyo. (2 Kor. 8:11, 12) Lakini ukosefu wa fedha katika nchi hauruhusiwi uzuie kuenezwa kwa ujumbe wa Ufalme huko ikiwa fedha zilizohitajiwa zapatikana kwingineko.
Hivyo, ingawa Mashahidi wenyeji hufanya wawezayo, katika sehemu kubwa ya ulimwengu kiasi kikubwa cha fedha zinazohitajiwa kwa majengo ya tawi huandaliwa na upaji unaofanywa na Mashahidi wa Yehova katika nchi nyinginezo. Ndivyo ilivyokuwa kuhusiana na ujenzi wa majengo makubwa yaliyokamilishwa katika Afrika Kusini katika 1987, Nigeria katika 1990, na Filipino katika 1991. Ndivyo pia ilivyokuwa kuhusu Zambia, ambako vilivyotazamiwa kuwa vifaa vya kuchapia vilikuwa vingali vinajengwa katika 1992. Hali kadhalika imekuwa hivyo kuhusu miradi mingi ya kadiri ndogo zaidi, kama ile iliyokamilishwa katika India katika 1985; Chile katika 1986; Kosta Rika, Ekuado, Guyana, Haiti, na Papua New Guinea katika 1987; Ghana katika 1988; na Honduras katika 1989.
Hata hivyo, katika nchi fulani, ndugu wameshangaa kuona yale ambayo wangeweza kutimiza nchini mwao kwa baraka ya Yehova juu ya jitihada zao za pamoja. Kwa kielelezo, katika miaka ya mapema ya 1980 tawi katika Hispania lilikuwa likifanya mipango ya nyongeza kubwa kwa vifaa vyalo. Tawi liliomba Baraza Linaloongoza liandae fedha zilizohitajiwa. Lakini kwa sababu ya matumizi makubwa katika pande nyinginezo katika wakati ule, msaada huo haukupatikana wakati ule. Wakipewa fursa, je, Mashahidi Wahispania, wangeweza, kwa mishahara yao ambayo kidogo ni ya chini, kuandaa fedha za kutosha kwa mradi kama huo?
Walielezwa hali. Kwa furaha walitoa vito vyao, pete, na vikuku ili viuzwe na fedha zipatikane. Wakati Shahidi mmoja wa kike mzee-mzee alipoulizwa kama alikuwa na hakika kwamba alitaka kutoa upaji wa kikuku kizito cha dhahabu alichokuwa amechanga, alijibu: “Ndugu, kitatimiza mema mengi zaidi kikilipia Betheli mpya kuliko vile kitatimiza kikiwa katika kiwiko changu!” Dada mmoja wa umri mkubwa zaidi alifukua rundo la manoti yaliyochakaa ambayo alikuwa amefukia chini ya sakafu ya kao lake kwa muda wa miaka mingi iliyopita. Waume na wake walichanga fedha walizokuwa wamehifadhi ili kufunga safari. Watoto walipeleka fedha walizohifadhi. Kijana mmoja aliyekuwa akipanga kununua gitaa alitoa upaji wa fedha hizo kwa ajili ya mradi wa tawi badala ya kununua gitaa. Kama vile Waisraeli wakati tabenakulo lilipojengwa jangwani, Mashahidi Wahispania walithibitika kuwa wachangaji wakarimu na wenye moyo wa kupenda wa vyote vilivyohitajiwa katika vitu vya kimwili. (Kut. 35:4-9, 21, 22) Halafu wakajitolea wenyewe—kwa wakati wote, wakati wa likizo, wakati wa miisho-juma—kufanya kazi yenyewe. Kutoka pande zote za Hispania walikuja—maelfu yao. Mashahidi wengine kutoka Ujerumani, Sweden, Uingereza, Ugiriki, na Marekani, kutaja nchi chache, walijiunga nao ili kukamilisha ile ambayo mwanzoni ilionekana kuwa kazi isiyowezekana.
Je, Kuna Faida Kutokana na Fasihi?
Kufikia 1992, fasihi za Biblia zilikuwa zikichapwa kwenye makao makuu ya ulimwengu na kwenye matawi 32 ulimwenguni pote. Kiasi kikubwa kilikuwa kikitolewa ili kugawanywa na Mashahidi wa Yehova. Lakini hapana yoyote yayo iliyofanywa kwa ajili ya pato la kibiashara. Maamuzi kwa habari ya lugha ambazo katika hizo fasihi zingechapwa na nchi ambako zingesafirishwa yalifanywa si kwa sababu ya faida yoyote ya kibiashara bali kwa sababu tu ya kukamilisha kazi ambayo Yesu Kristo aligawia wafuasi wake.
Mapema kama Julai 1879, wakati toleo la kwanza kabisa la Watch Tower lilipotangazwa, lilikuwa na taarifa ikisema kwamba wale waliokuwa maskini sana wasiweze kulipia uandikishaji (wakati huo ukiwa tu senti 50 za Marekani, kwa mwaka) wangeweza kuupata bila malipo ikiwa wangeandika tu na kutoa ombi. Lengo kuu lilikuwa kusaidia watu wajifunze juu ya kusudi kuu la Yehova.
Kwa kusudi hilo, tangu 1879 kiasi kikubwa cha fasihi za Biblia kimegawanywa miongoni mwa umma bila malipo. Katika 1881 na baada ya hapo, karibu nakala 1,200,000 za Food for Thinking Christians ziligawanywa bila malipo. Nyingi za hizo zilikuwa kwa namna ya kitabu cha kurasa 162; nyingine, katika umbo la gazeti. Trakti nyingi za ukubwa tofauti-tofauti zilitangazwa wakati wa miaka iliyofuata. Kiasi kikubwa cha hizo (kihalisi mamia ya mamilioni ya nakala) kiligawanywa bila malipo. Hesabu ya trakti na vichapo vingine vilivyotolewa bila malipo ilizidi kukua. Katika 1915 pekee, ripoti ilionyesha kwamba nakala 50,000,000 za trakti katika lugha kama 30 zilitolewa ili kugawanywa ulimwenguni pote bila malipo. Fedha za yote hayo zilikuwa zikitoka wapi? Sanasana zilitoka kwa upaji wa hiari kwa Hazina ya Tract Society.
Kulikuwa pia fasihi iliyotolewa kwa mchango wakati wa miongo ya mapema ya historia ya Sosaiti, lakini mchango uliodokezwa uliwekwa ukiwa mdogo sana kadiri ilivyowezekana. Fasihi hiyo ilitia ndani vitabu vilivyojalidiwa vya kurasa 350 hadi 744. Wakati makolpota (kama wahubiri wa wakati wote walivyojulikana wakati ule) wa Sosaiti walipovitoa kwa umma, walitaarifu kiasi kilichodokezwa kuwa mchango. Hata hivyo, lengo lao halikuwa kuchuma fedha bali kutia mikononi mwa watu kweli muhimu za Biblia. Walitaka watu wasome fasihi ili iwanufaishe.
Walikuwa na nia sana ya kumpa mtu fasihi (wakilipia mchango wao wenyewe) ikiwa mwenye nyumba alikuwa maskini sana. Lakini ilikuwa imeonwa kwamba watu wengi walielekea zaidi kusoma kichapo ambacho walikuwa wamelipia kitu fulani, na bila shaka, kile walichochanga kingeweza kutumiwa kuchapa fasihi zaidi. Hata hivyo, kikikazia kwamba Wanafunzi wa Biblia hawakuwa wakitafuta pato la kifedha, kikaratasi cha maagizo ya utumishi cha Sosaiti, Bulletin, cha Oktoba 1, 1920, kilisema hivi: “Siku kumi baada ya kuwa umepeleka kijitabu [kilichokuwa na kurasa 128], watembelee tena watu na kuhakikisha kama wamekisoma. Ikiwa hawajakisoma, waombe wakirudishe na kuwarudishia fedha zao. Waambie kwamba wewe si mwakilishi wa [kampuni ya] vitabu, bali kwamba unapendezwa na kutoa ujumbe huo wa faraja na uchangamfu kwa kila mtu, na kwamba ikiwa wao hawapendezwi vya kutosha na jambo la hakika linalowahusu sana kadiri hiyo . . . , wataka kutia kitabu hicho mikononi mwa mtu mwingine atakayependezwa.” Mashahidi wa Yehova hawakuendelea kutumia njia hiyo, kwa sababu wameona kwamba washiriki wengine wa familia mara nyingi huchukua fasihi na kunufaishwa nayo; lakini jambo lililofanywa huko nyuma hukazia lengo halisi la Mashahidi.
Kwa miaka mingi walirejezea ugawanyaji wao wa fasihi kuwa “kuuza.” Lakini usemi huo ulisababisha mvurugo, na kwa hiyo kuanzia na 1929, uliacha kutumiwa hatua kwa hatua. Usemi huo haukufaana kwelikweli na utendaji wao, kwa kuwa kazi yao haikuwa ya kibiashara. Lengo lao halikuwa kuchuma fedha. Kusudio lao lote lilikuwa kuhubiri habari njema za Ufalme wa Mungu. Kwa sababu hiyo, katika 1943 Mahakama Kuu Zaidi ya Marekani iliamua kwamba Mashahidi wa Yehova hawakutakwa kupata leseni ya kuchuuza kibiashara kabla ya kugawanya fasihi zao. Na mahakama ya Kanada baada ya hapo ilinukuu kwa kupendelea kutoa sababu kulikofanywa na Mahakama Kuu Zaidi ya Marekani katika uamuzi huo.b
Katika nchi nyingi Mashahidi wa Yehova wametoa kwa ukawaida fasihi zao kwa msingi wa mchango. Mchango udokezwao umekuwa chini sana, ukilinganishwa na vitabu na magazeti mengine, hivi kwamba watu wengi wamejitolea kuchanga zaidi. Lakini jitihada kubwa imefanywa kwa upande wa tengenezo kuendeleza michango idokezwayo ikiwa chini ili iwe katika kiwango cha pato la mamilioni mengi ya watu walio na mali kidogo sana za ulimwengu huu lakini ambao hushukuru kupokea Biblia au fasihi za Biblia. Hata hivyo, lengo katika kudokeza mchango limekuwa si kutajirisha tengenezo la Mashahidi wa Yehova.
Mahali ambako sheria hueleza ugawanyaji wowote wa fasihi za Biblia kuwa biashara ikiwa mgawanyaji hudokeza mchango kwa ajili ya fasihi, Mashahidi wa Yehova humwachia kwa furaha yeyote aonyeshaye kupendezwa kwa moyo mweupe na ambaye huahidi kuisoma. Wale ambao hutaka kuchanga kitu fulani kwa ajili ya kusogeza mbele kazi ya elimu ya Biblia waweza kutoa chochote watakacho. Kwa kielelezo, jambo hilo hufanywa katika Japani. Katika Uswisi, kufikia karibuni, michango ya kutoa kwa hiari yalikubaliwa, lakini kufikia kiasi kilichotaarifiwa tu kwa ajili ya kichapo; hivyo ikiwa wenye nyumba walitaka kutoa zaidi, Mashahidi walimrudishia tu au kumwandalia mwenye nyumba fasihi zaidi. Tamaa yao ilikuwa, si kukusanya fedha, bali kuhubiri habari njema za Ufalme wa Mungu.
Katika 1990, kwa sababu ya kashfa za kifedha katika baadhi ya dini za Jumuiya ya Wakristo ambazo zilitangazwa sana kwa umma, pamoja na mwelekeo wenye kuongezeka wa serikali wa kuainisha utendaji wa kidini kuwa shughuli za kibiashara, Mashahidi wa Yehova walifanya marekebisho fulani katika utendaji wao ili kuepuka kueleweka vibaya kwa vyovyote. Baraza Linaloongoza lilielekeza kwamba katika Marekani, fasihi zote ambazo hugawanywa na Mashahidi—Biblia, pamoja na trakti, vijitabu, magazeti, na vitabu vilivyojalidiwa vyenye kuelezea Biblia—vitolewe kwa watu kwa sharti tu la kwamba watavisoma, bila kudokeza mchango. Utendaji wa Mashahidi wa Yehova si wa kibiashara hata kidogo, na mpango huo ulitumika kuwatofautisha zaidi na vikundi vya kidini ambavyo hufanya dini kuwa ya kibiashara. Bila shaka, watu wengi wanajua kwamba inagharimu kuchapa fasihi kama hiyo, na wale ambao huthamini utumishi unaofanywa na Mashahidi waweza kutaka kutoa upaji wa kitu fulani kusaidia kazi. Watu hao wanaelezwa kwamba kazi ya ulimwenguni pote ya elimu ya Biblia iongozwayo na Mashahidi wa Yehova hutegemezwa kwa upaji wa hiari. Upaji hukubaliwa kwa furaha, lakini hauombwiombwi.
Wale ambao hushiriki huduma ya shambani hawaifanyi kwa pato la kifedha. Wao hutoa upaji wa wakati wao, na hulipia usafiri wao wenyewe. Ikiwa mtu aonyesha kupendezwa, wao hupanga kurudi kila juma, bila malipo hata kidogo, ili kutoa maagizo ya kibinafsi katika Biblia. Ni upendo tu kwa Mungu na wanadamu wenzao ndio ungeweza kuwasukuma kuendelea kushiriki katika utendaji huo, mara nyingi kwa kukabiliwa na ubaridi na upinzani wa moja kwa moja.
Fedha zipokewazo kwenye makao makuu ya ulimwengu ya Mashahidi wa Yehova au kwenye ofisi zayo za tawi hutumiwa, si kutajirisha tengenezo au mtu yeyote, bali kuendeleza kazi ya kuhubiri habari njema. Huko nyuma katika 1922, The Watch Tower liliripoti kwamba kwa sababu ya hali ya kiuchumi katika Ulaya, vitabu vilivyochapwa huko kwa ajili ya Sosaiti vilikuwa vikilipiwa sanasana na ofisi ya Amerika na mara nyingi vilikuwa vikiachwa kwa watu kwa bei iliyo chini ya gharama ya kuchapisha. Ingawa sasa Mashahidi wa Yehova huendesha mashirika ya kuchapia katika nchi nyingi, baadhi ya nchi ambako fasihi husafirishwa haziwezi kupeleka fedha zozote nje ya nchi ili kulipia bei. Upaji wa ukarimu wa kutoa kwa hiari wa Mashahidi wa Yehova katika nchi ambazo zina mali ya kutosha ndiyo husaidia kusawazisha upungufu katika nchi ambazo zina mali kidogo.
Sikuzote Watch Tower Society imejitahidi kutumia mali yote iliyo nayo kuendeleza kazi ya kuhubiri habari njema. Katika 1915, akiwa msimamizi wa Sosaiti, Charles Taze Russell alisema: “Sosaiti yetu haikutafuta kuweka akiba ya mali za kilimwengu kwa ajili ya wakati ujao, bali, imekuwa shirika lenye kutumia mali ili kutimiza mambo. Chochote ambacho mwelekezo wa Mungu ulituletea bila kuombaomba tumetafuta kutumia kwa hekima kadiri ilivyowezekana kupatana na Neno na Roho ya Bwana. Muda mrefu uliopita tulitangaza kwamba wakati fedha zingekoma, utendaji wa Sosaiti ungekoma kwa kadiri iyo hiyo; na kwa kadiri fedha zingeongezeka, utendaji wa Sosaiti ungeongezeka.” Sosaiti imeendelea kufanya vivyo hivyo.
Hadi sasa, tengenezo hutumia fedha zipatikanazo kutuma waangalizi wasafirio ili wakaimarishe makutaniko na kuyatia moyo katika huduma ya hadharani. Yaendelea kutuma wamishonari na wahitimu wa Shule ya Mazoezi ya Kihuduma kwenye nchi ambako kuna uhitaji wa pekee. Hutumia pia fedha zozote zipatikanazo kutuma mapainia wa pekee kwenye maeneo ambako ni kazi ndogo sana imefanywa au hakuna kazi ya kuhubiri ujumbe wa Ufalme ambayo imepata kufanywa. Kama ilivyoripotiwa katika Kitabu-Mwaka cha Mashahidi wa Yehova cha 1993, (Kiingereza) wakati wa mwaka wa utumishi uliotangulia huo, dola 45,218,257.56 (Marekani) zilitumiwa katika njia hizo.
Hawatumikii kwa Ajili ya Pato la Kibinafsi
Hakuna mshiriki yeyote wa Baraza Linaloongoza, maofisa wa mashirika yao halali, au watu wengine mashuhuri wanaoshirikiana na tengenezo ambaye hupata faida ya kifedha kutokana na kazi ya Mashahidi wa Yehova.
Kuhusu C. T. Russell, aliyetumikia akiwa msimamizi wa Watch Tower Society kwa zaidi ya miaka 30, mmojawapo washirika wake aliandika hivi: “Ikiwa njia ya kuamulia kama mwendo wake ulipatana na Maandiko, na pia ikiwa njia ya kuonyesha weupe wake mwenyewe wa moyo, yeye aliamua kutahini kibali cha Bwana kama ifuatavyo: (1) Atoe maisha yake kabisa kwa imani aliyotetea; (2) Atumie mali yake katika kuendeleza kazi; (3) Akataze kukusanywa kwa fedha kwenye mikutano yote; (4) Ategemee michango isiyo ya kuombaomba (ya kutoa kwa hiari kabisa) ili kuendeleza kazi baada ya mali yake kumalizika.”
Badala ya kutumia utendaji wa kidini ili kujipatia utajiri wa vitu vya kimwili, Ndugu Russell alitumia rasilimali zake zote katika kazi ya Bwana. Baada ya kifo chake iliripotiwa hivi katika The Watch Tower: “Alitumia mali yake binafsi kabisakabisa katika imani ambayo alitolea maisha yake. Alipokea kiasi kidogo cha dola 11.00 (Marekani) kwa mwezi kwa ajili ya matumizi ya binafsi. Alikufa, asiache mali yoyote hata kidogo.”
Kuhusu wale ambao wangeendesha kazi ya Sosaiti, Ndugu Russell alitoa sharti katika wasia wake kwamba: “Kwa habari ya kulipia gharama, nafikiri ni jambo la hekima kudumisha mwendo wa Sosaiti wa wakati uliopita kwa habari ya mishahara—kwamba yeyote asilipwe; kwamba matumizi ya kiasi tu yaruhusiwe kwa wale ambao hutumikia Sosaiti au kazi yayo kwa njia yoyote.” Wale ambao wangetumikia kwenye makao ya Betheli, ofisi, na viwanda vya Sosaiti, pamoja na wawakilishi wa Sosaiti wasafirio, wangeandaliwa tu chakula, makao, na kiasi kidogo kwa ajili ya gharama—kutosha mahitaji ya wakati uliopo lakini “bila uandalizi . . . wa kuweka akiba ya fedha kwa wakati ujao.” Kiwango icho hicho chatumika leo.
Wale ambao hukubaliwa kwa ajili ya utumishi wa pekee wa wakati wote kwenye makao makuu ya ulimwengu ya Mashahidi wa Yehova wote hukubali nadhiri ya umaskini, kama ilivyo kwa washiriki wote wa Baraza Linaloongoza na washiriki wengine wote wa familia ya Betheli kule. Hiyo haimaanishi kwamba wanaishi maisha yasiyo na furaha, bila starehe yoyote. Lakini yamaanisha kwamba wanashiriki, bila upendeleo, maandalizi ya kiasi ya chakula, makao, na rudishio la gharama vinavyoandaliwa kwa wote walio katika utumishi huo.
Hivyo ndivyo tengenezo huendesha kazi yalo kwa kutegemea kabisa msaada ambao Mungu hutoa. Bila kulazimishwa bali kama udugu halisi wa kiroho ambao hufika sehemu zote za dunia, Mashahidi wa Yehova hutumia kwa furaha rasilimali zao ili kutimiza kazi ambayo Yehova, Baba yao mtukufu wa kimbingu, amewapa wafanye.
[Maelezo ya Chini]
a Ona Mnara wa Mlinzi (Kiingereza), Septemba 1, 1944, ukurasa 269; Desemba 15, 1987, kurasa 19-20.
b Murdock v. Commonwealth of Pennsylvania, 319 U.S. 105 (1943); Odell v. Trepanier, 95 C.C.C. 241 (1949).
[Blabu katika ukurasa wa 340]
‘Kuombaomba fedha hakuruhusiwi wala hakukubaliwi na Sosaiti hii’
[Blabu katika ukurasa wa 342]
Mkazo mkubwa u juu ya ubora wa kushiriki kweli pamoja na wengine
[Blabu katika ukurasa wa 343]
Taarifa iliyo wazi, ya unyoofu juu ya mambo ya hakika
[Blabu katika ukurasa wa 344]
Makutaniko husaidiana yapate Majumba ya Ufalme yanayohitajiwa
[Blabu katika ukurasa wa 345]
Michango mingi hutoka kwa watu mmoja-mmoja ambao wana mali kidogo tu
[Blabu katika ukurasa wa 348]
Fasihi nyingi hugawanywa bila malipo—ni nani huilipia?
[Blabu katika ukurasa wa 349]
Kwa furaha wao huachia fasihi yao yeyote anayeonyesha kupendezwa kwa moyo mweupe na ambaye aahidi kuisoma
[Blabu katika ukurasa wa 350]
Ni jambo gani hufanywa na fedha zinazochangwa?
[Blabu katika ukurasa wa 351]
“Alitumia mali yake binafsi kabisakabisa katika imani ambayo alitolea maisha yake”
[Sanduku katika ukurasa wa 341]
Mungu Haombiombi
“Yeye aliyesema, ‘Kama ningekuwa na njaa singekuambia, maana ulimwengu ni wangu, navyo viujazavyo. . . . Sitatwaa ng’ombe katika nyumba yako, wala beberu katika mazizi yako; maana kila hayawani wa msitu ni wangu, na makundi ya ng’ombe juu ya milima elfu’ (Zab. 50:12, 9, 10), aweza kuendesha kazi yake kuu bila kuombaomba fedha ama kutoka kwa ulimwengu ama kutoka kwa watoto wake. Wala hatashurutisha watoto wake kutoa dhabihu au chochote katika utumishi wake, wala hatakubali chochote kutoka kwao isipokuwa toleo changamfu, la hiari.”—“Zion’s Watch Tower,” Septemba 1886, uku. 6.
[Sanduku katika ukurasa wa 347]
Sikuzote Upaji Haukuwa kwa Namna ya Fedha
Mashahidi katika kaskazini ya mbali katika Queensland walitayarisha na kupeleka kwenye ujenzi wa Watch Tower katika Sydney, Australia, malori manne makubwa yenye kujaa shehena ya mbao bora kabisa ambazo wakati ule zilikadiriwa kuwa na thamani ya dola kati ya 60,000 na 70,000 za Australia.
Wakati kiwanda cha Watch Tower katika Elandsfontein, Afrika Kusini, kilipokuwa kikiongezewa ukubwa, ndugu Mhindi alipiga simu na kuomba kwamba waje tafadhali wachukue upaji wa mifuko 500 (kilo 50 kila mmoja) ya saruji—wakati kulipokuwa na uhaba wayo nchini. Wengine walitoa malori yao yatumiwe na Sosaiti. Dada Mwafrika alilipa kampuni moja ili ipeleke meta za kyubiki 15 za mchanga wa kujengea.
Katika Uholanzi wakati vifaa vipya vya tawi vilipokuwa vikijengwa katika Emmeni, kiasi kikubwa cha vyombo na mavazi ya kujengea vilichangwa. Dada mmoja, ajapokuwa mgonjwa sana, alifuma jozi ya soksi ndefu kwa kila mmoja wa wafanyakazi wakati wa pindi hiyo ya majira ya baridi.
Ili kujenga ofisi ya tawi mpya na kile kilichotazamiwa kuwa kiwanda cha uchapaji katika Lusaka, Zambia, vifaa vya ujenzi vilinunuliwa na fedha zilizotolewa na Mashahidi katika nchi nyinginezo. Vifaa na vyombo ambavyo havikupatikana nchini vilipelekwa Zambia kwa malori vikiwa upaji kwa ajili ya kazi kule.
Shahidi katika Ekuado, katika 1977, alitoa upaji wa kisehemu cha ardhi cha hekta 34. Hapo lilijengwa Jumba la Kusanyiko na majengo ya tawi jipya.
Mashahidi wenyeji katika Panama waliwakaribisha na kuwapa makao wafanyakazi wa kujitolea; baadhi yao waliokuwa na mabasi waliandaa usafiri; wengine walishiriki kuandaa milo 30,000 iliyoandaliwa mahali penye ujenzi.
Kwa ajili ya wafanyakazi kwenye mradi katika Arboga Sweden, kutaniko moja lilioka na kupeleka vitumbua 4,500. Wengine walipeleka asali, matunda, na jemu. Mkulima mmoja karibu na ujenzi, ajapokuwa si Shahidi, aliandaa tani mbili za karoti.
-
-
Makao Makuu ya Ulimwengu na Ofisi ya Tawi Makuu ya Mashahidi wa YehovaMashahidi wa Yehova—Wapiga-Mbiu wa Ufalme wa Mungu
-
-
Makao Makuu ya Ulimwengu na Ofisi ya Tawi Makuu ya Mashahidi wa Yehova
MAKAO MAKUU YA ULIMWENGU YA MASHAHIDI WA YEHOVA
[Picha katika ukurasa wa 352, 353]
Utendaji wa duniani pote wa Mashahidi wa Yehova umeelekezwa kutoka Brooklyn, New York, Marekani, tangu 1909. Majengo haya yamekuwa ofisi za makao makuu tangu 1980
[Picha katika ukurasa wa 352]
Kitovu cha Elimu cha Watchtower, katika Patterson, New York (kilikuwa kikijengwa katika 1992)
[Picha katika ukurasa wa 353]
Baadhi ya majengo ya makao ya maelfu wanaotumikia kwenye makao makuu ya ulimwengu
[Picha katika ukurasa wa 354]
Zile zilizokuwa hoteli katika Brooklyn zimerekebishwa ili kuandaa nafasi kwa ajili ya wafanyakazi wa kujitolea 1,476 zaidi
[Picha katika ukurasa wa 354]
Makao ya familia ya Betheli katika Wallkill, New York
[Picha katika ukurasa wa 354, 355]
Katika majengo haya ya viwanda (katika Brooklyn, New York), Biblia, vitabu, na broshua katika lugha 180 hutokezwa ili zigawanywe duniani pote
[Picha katika ukurasa wa 356]
Mamilioni ya kaseti za habari ya Biblia hutokezwa katika kiwanda hiki katika Brooklyn kila mwaka. Kutoka hapa, usafirishaji hufanywa pia. Kila mwaka fasihi za Biblia na vifaa vinginevyo zaidi ya tani 15,000 husafirishwa hadi kwenye sehemu zote za ulimwengu
[Picha katika ukurasa wa 356]
Katika kiwanda hiki kwenye Watchtower Farms, karibu na Wallkill, New York, mamia ya mamilioni ya nakala za “Mnara wa Mlinzi” na “Amkeni!,” katika lugha 14, huchapwa kila mwaka
Mashahidi wa Yehova na mashirika ya kisheria wanayotumia wana ofisi na viwanda vya kuchapia katika sehemu nyingi za ulimwengu. Picha zilizoko kwenye kurasa zinazofuata zinaonyesha majengo mengi, ingawa si yote. Mahali ambapo majengo mapya yalikuwa yakijengwa katika 1992, michoro yayo imeonyeshwa. Tarakimu zilizotolewa ni za kufikia 1992.
AMERIKA KASKAZINI NA WEST INDIES
ALASKA
[Picha katika ukurasa wa 357]
Wanaozuru ofisi ya tawi ya Sosaiti hukaribishwa kwa uchangamfu. Huku nchini Alaska, kama kwingineko, Mashahidi wa Yehova huhubiri nyumba kwa nyumba, ingawa nyakati nyingine hali-joto hushuka kufikia Sentigredi 50 chini ya sifuri.
[Picha katika ukurasa wa 357]
Ndege inayotumiwa kusafirisha wapiga-mbiu wa Ufalme kwenye sehemu za mbali za eneo
BAHAMAS
[Picha katika ukurasa wa 357]
Vichapo vya Watch Tower vilifika Bahamas kufikia 1901. Kutolewa kwa ushahidi kwa njia ya kawaida kulifanywa huku kwanza katika 1926. Tangu wakati huo fasihi za Biblia zipatazo kuwa zaidi ya 4,600,000 zimegawanywa katika visiwa vinavyosimamiwa sasa na ofisi hii.
BARBADOS
[Picha katika ukurasa wa 358]
Vikundi vya kidini zaidi ya 140 katika Barbados hudai kuwa vya Kikristo. Tangu 1905, Mashahidi wa Yehova wamekuwa wakiwasaidia watu huku wajionee wenyewe yale ambayo Biblia husema.
BELIZE
[Picha katika ukurasa wa 358]
Karibu nusu ya idadi ya watu katika Belize huishi mashambani. Ili kufikia vijiji fulani vya ndanindani, Mashahidi wa Yehova husafiri kila mwaka kwa miguu wakiwa na mifuko na mikoba.
KOSTA RIKA
[Picha katika ukurasa wa 358]
Sosaiti ilifungua ofisi ya tawi katika Kosta Rika kwanza mwaka 1944. Tangu miaka ya 1950, Wakosta Rika wanaoshiriki katika ibada ya kweli wamefikia idadi ya maelfu.
JAMHURI YA DOMINIKA
[Picha katika ukurasa wa 359]
Fasihi za Watch Tower ziligawanywa huku mapema kama 1932. Lakini mafunzo ya binafsi ya watu wanaopendezwa yalianza mwaka 1945, wakati wamishonari wanaoonyeshwa upande wa kushoto walipowasili. Katika miaka ya hivi karibuni, kwa sababu makumi ya maelfu ya watu wamekuwa na hamu ya kujifunza Biblia pamoja na Mashahidi, majengo haya ya tawi yamehitajiwa.
EL SALVADOR
[Picha katika ukurasa wa 359]
Ushahidi fulani ulitolewa huku katika 1916. Hata hivyo, ilikuwa kwanza katika 1945 kwamba angalau mtu mmoja katika El Salvador alikuwa tayari kupata ubatizo wa maji wa Kikristo (kama inavyoonyeshwa hapa). Tangu wakati huo, maelfu zaidi wamekuwa watumishi wa Yehova.
GUADELOUPE
[Picha katika ukurasa wa 359]
Uwiano wa mhubiri na idadi ya watu wote katika eneo linalotumikiwa na ofisi hii ya tawi ni mmojawapo ulio bora sana ulimwenguni. Watu wengi katika Guade- loupe hupokea habari njema kwa uthamini.
KANADA
[Picha katika ukurasa wa 360, 361]
Ofisi ya Sosaiti katika Kanada husimamia kuhubiriwa kwa habari njema katika nchi ya pili kwa ukubwa duniani. Wapiga-mbiu wa Ufalme zaidi ya 100,000 wana shughuli nyingi katika nchi hii.
Jengo la usimamizi (picha iliyo juu ya ile ya jengo la tawi la sasa)
[Picha katika ukurasa wa 360]
Maeneo ya Kaskazini-Magharibi
[Picha katika ukurasa wa 360]
Kambi za ukataji-miti za British Columbia
[Picha katika ukurasa wa 360]
Malisho ya ng’ombe ya Alberta
[Picha katika ukurasa wa 361]
Quebec ya Kifaransa
[Picha katika ukurasa wa 361]
Mikoa ya Pwani
GUATEMALA
[Picha katika ukurasa wa 360]
Ingawa Kihispania ndiyo lugha ya taifa ya Guatemala, namna mbalimbali za lugha ngumu za Kihindi husemwa huku. Ofisi ya Sosaiti hujaribu kuona kwamba kila mtu ana fursa ya kusikia kuhusu Ufalme wa Mungu.
HAITI
[Picha katika ukurasa wa 361]
Kumtumikia Yehova huletea Mashahidi wa Yehova shangwe nyingi katika Haiti, kujapokuwa hali zinazowazunguka ambazo mara nyingi huwa ngumu.
HONDURAS
[Picha katika ukurasa wa 362]
Tangu 1916, muda wa saa zaidi ya 23,000,000 zimetolewa katika kufundisha wenyeji wa nchi hii Biblia. Nyakati nyingine, Mashahidi wa Yehova wamelazimika kufundisha watu jinsi ya kusoma na kuandika (kama uonavyo hapa) ili kuwawezesha wajifunze Neno la Mungu wao wenyewe.
JAMAIKA
[Picha katika ukurasa wa 362]
Mamia katika Jamaika walikuja kuwa watumishi wa Yehova waliojitoa wakati ambapo wale waliotazamia kuwa warithi wa Ufalme wa kimbingu walipokuwa wakikusanywa. Tangu 1935, maelfu zaidi wamejiunga katika kuhubiri ujumbe wa Ufalme. Ofisi hii ya tawi inajengwa ili kusaidia kushughulikia mahitaji yao ya kiroho.
VISIWA VYA LEEWARD (ANTIGUA)
[Picha katika ukurasa wa 362]
Mapema kama 1914, habari njema zilikuwa zikihubiriwa katika visiwa vinavyoshughulikiwa sasa na ofisi hii. Tangu wakati huo, watu katika sehemu hii ya dunia wamealikwa tena na tena ‘wayatwae maji ya uzima bure.’—Ufu. 22:17.
MEXICO
[Picha katika ukurasa wa 363]
Kituo kipya cha kutoa elimu ya Biblia kikijengwa na Mashahidi wa Yehova nchini Mexico
[Picha katika ukurasa wa 363]
Ofisi zikitumiwa katika 1992
[Picha katika ukurasa wa 363]
Fasihi za Biblia zinazochapwa hapa huandalia ugavi Mashahidi zaidi ya 410,000 wenye bidii katika Mexico na nchi nyinginezo za karibu zenye kusema Kihispania
[Picha katika ukurasa wa 363]
Kuanzia 1986 hadi 1992, mafunzo ya Biblia nyumbani zaidi ya asilimia 10 yaliyoongozwa na Mashahidi ulimwenguni pote yalikuwa katika Mexico, mengi yayo yakifanywa kwa vikundi vya familia
[Grafu katika ukurasa wa 363]
(Ona mpangilio kamili katika nakala iliyochapishwa)
Mafunzo ya Biblia Katika Mexico
500,000
250,000
1950 1960 1970 1980 1992
MARTINIQUE
[Picha katika ukurasa wa 364]
Mbegu za ukweli zilipandwa huku mapema kama 1946. Lakini wakati Xavier na Sara Noll (wanaoonyeshwa hapa) walipokuja kutoka Ufaransa katika 1954, walibaki na kusitawisha kupendezwa kulikopatikana. Kufikia 1992, watu zaidi ya 3,200 walikuwa wakishiriki pamoja nao katika kupiga mbiu ya ujumbe wa Ufalme.
ANTILLES YA UHOLANZI (KURASAO)
[Picha katika ukurasa wa 364]
Wamishonari 23 wametumikia katika eneo la ofisi hii ya tawi. Wawili kati ya kikundi cha awali (wanaoonyeshwa hapa) waliowasili mwaka 1946 walikuwa wangali wakifanya kazi katika 1992.
NIKARAGUA
[Picha katika ukurasa wa 364]
Kuanzia 1945, wakati wamishonari walipowasili, Mashahidi wa Yehova katika Nikaragua walianza kuongezeka. Kufikia 1992, idadi yao ilikuwa zaidi ya 9,700. Sasa watu wanaotaka Mashahidi wawafunze Biblia wanapita kwa mbali idadi ya Mashahidi wenyeji.
PANAMA
[Picha katika ukurasa wa 365]
Tangu mwisho wa karne ya 19, watu katika Panama wamekuwa wakipokea msaada wa kujifunza matakwa ya Mungu kwa ajili ya uhai wa milele.
PUERTO RIKO
[Picha katika ukurasa wa 365]
Tangu 1930, fasihi za Biblia zaidi ya 83,000,000 zimegawanywa nchini Puerto Riko, na ziara za kurudia 25,000,000 zimefanywa ili kuandaa msaada zaidi kwa watu wanaopendezwa. Kazi ya kutafsiri inayofanywa huku husaidia kufanya fasihi za Biblia zipatikane kwa watu wapatao 350,000,000 ulimwenguni pote wanaosema Kihispania.
TRINIDAD
[Picha katika ukurasa wa 365]
Kazi ya kupiga mbiu ya habari njema ilikuwa tayari ikifanywa kwa bidii katika Trinidad mapema kama 1912. Mashahidi wengi, kutia hawa watatu waliozoezwa kwenye Shule ya Gileadi, wametoa wakati wao wote kwa kazi hii.
AMERIKA KUSINI
ARGENTINA
[Picha katika ukurasa wa 366]
Mpiga-mbiu wa Ufalme alitumwa kwanza kwa nchi hii katika 1924. Msaada mwingi ulitolewa baadaye na wamishonari waliozoezwa Gileadi, kutia ndani Charles Eisenhower (anayeonyeshwa hapa), aliyewasili na mke wake katika 1948. Kufikia 1992, usimamizi wa ujumla, pamoja na fasihi za Biblia, ulikuwa ukiandaliwa kutoka vifaa hivi kwa ajili ya Mashahidi wa Yehova zaidi ya 96,000 katika Argentina. Fasihi zilikuwa pia zikipelekwa kutoka huku ili kutolea ugavi Mashahidi zaidi ya 44,000 katika Chile.
BOLIVIA
[Picha katika ukurasa wa 367]
Wabolivia wamekuwa wakisikia ujumbe wa Ufalme tangu 1924. Maelfu hupokea fasihi za Biblia kwa uthamini na kunufaika na mafunzo ya Biblia nyumbani yaliyo ya kawaida.
CHILE
[Picha katika ukurasa wa 367]
Kufikia 1919, fasihi za Watch Tower zilikuwa zimefika Chile. Mahubiri yanayosimamiwa na ofisi hii yaenea sasa kutoka malisho ya kondoo yenye upepo mwingi yaliyo kusini hadi kambi za migodi za mbali zilizo kaskazini, kutoka Milima Andes hadi baharini.
EKUADO
[Picha katika ukurasa wa 367]
Mashahidi zaidi ya 870 walioacha nchi zao ili kutumika mahali penye uhitaji zaidi, walifanya sehemu kubwa katika kuhubiri habari njema katika Ekuado (kama hawa wawili wanaoonyeshwa hapa). Tawi hili sasa huandalia msaada wasifaji wa Yehova zaidi ya 22,000 wenye bidii.
BRAZILI
[Picha katika ukurasa wa 368, 369]
Katika 1992, wakati ofisi ya tawi ya Sosaiti, kiwanda cha kuchapia, na Kao la Betheli lilipokuwa likipanuliwa kufikia kiasi hiki, idadi ya Mashahidi wa Yehova katika Brazili ilikuwa zaidi ya 335,000 na walikuwa wakibatiza wanafunzi zaidi ya 27,000 kila mwaka. Kiwanda hapa pia huandaa fasihi za kugawanywa katika Bolivia, Paraguai, na Uruguai.
[Picha katika ukurasa wa 369]
Stediamu mbili kubwa zilizotumiwa kwa ajili ya mkusanyiko wa kimataifa wa Mashahidi wa Yehova katika São Paulo katika 1990; mikusanyiko mingine zaidi ya 100 ilipangwa kufanywa
[Grafu katika ukurasa wa 369]
(Ona mpangilio kamili katika nakala iliyochapishwa)
Wapiga-Mbiu wa Ufalme Katika Brazili
300,000
200,000
100,000
1950 1960 1970 1980 1992
GUYANA
[Picha katika ukurasa wa 368, 369]
Sosaiti imekuwa na ofisi ya tawi katika Guyana tangu 1914. Mashahidi wamefikia ndani sana mashambani na kujitahidi kumtolea kila mtu fursa ya kusikia habari njema. Ingawa hata sasa idadi ya watu wa nchi hiyo ni chini ya milioni moja, Mashahidi wametoa muda wa saa zaidi ya 10,000,000 zimetolewa katika kuhubiri na kufundisha katika nchi hii.
PARAGUAI
[Picha katika ukurasa wa 369]
Kuhubiri habari njema kulianza katika Paraguai katika miaka ya katikati ya 1920. Tangu 1946, wamishonari 112 waliozoezwa Gileadi wamesaidia kutoa ushahidi. Ili kufikia vikundi vya lugha mbali na Kihispania na Kiguarani zinazosemwa huku, Mashahidi wengine wamejitolea pia kuhamia kutoka nchi mbalimbali.
Kutoka Ujerumani
Kutoka Korea
Kutoka Japani
KOLOMBIA
[Ramani/Picha katika ukurasa wa 370, 371]
Mapema kama 1915, kichapo cha Watch Tower kilipelekwa kwa mtu aliyependezwa nchini Kolombia. Kufikia 1992, fasihi za Biblia zilizochapwa katika majengo haya zilikuwa zikisafirishwa ili kushughulikia mahitaji ya waeneza-evanjeli zaidi ya 184,000 katika Kolombia, Ekuado, Panama, Peru, na Venezuela.
[Ramani]
(Ona mpangilio kamili katika nakala iliyochapishwa)
KOLOMBIA
PERU
EKUADOR
PANAMA
VENEZUELA
PERU
[Picha katika ukurasa wa 370]
Mapema katika 1924, fasihi za Biblia ziligawanywa katika Peru na Mwanafunzi wa Biblia aliyekuwa akizuru. Kutaniko la kwanza lilifanyizwa huku miaka 21 baadaye. Sasa kuna wapiga-mbiu wa Ufalme wa Mungu zaidi ya 43,000 wanaotenda katika Peru.
[Picha katika ukurasa wa 370]
Mapainia wakihubiri katika sehemu za juu za Andes
SURINAME
[Picha katika ukurasa wa 371]
Katika 1903 hivi, kikundi cha kwanza cha funzo kilifanyizwa huku. Leo majengo haya ya tawi yanahitajiwa ili kusimamia makutaniko yaliyotawanyika kotekote nchini—katika maeneo yasiyo na maendeleo sana, wilaya, na jijini.
URUGUAI
[Picha katika ukurasa wa 372]
Tangu 1945, wamishonari zaidi ya 80 wamekuwa na sehemu katika kupiga mbiu ya Ufalme katika Uruguai. Wale wanaoonyeshwa hapa wamekuwa wakitumikia katika Uruguai tangu miaka ya 1950. Kufikia 1992, Mashahidi wenyeji zaidi ya 8,600 walikuwa wakitumikia pamoja nao.
VENEZUELA
[Picha katika ukurasa wa 372]
Baadhi ya vichapo vya Watch Tower viligawanywa katika Venezuela katika miaka ya katikati ya 1920. Mwongo mmoja baadaye mama na binti walio mapainia kutoka Marekani pamoja walianza kipindi cha kuhubiri huku kwa bidii, wakieneza jiji kuu tena na tena, pia wakizuru miji kotekote nchini. Sasa kuna Mashahidi zaidi ya 60,000 wenye bidii katika Venezuela.
[Picha katika ukurasa wa 372]
Uwanja wa mchezo wa fahali katika Valencia ukiwa na umati wa 74,600 kwa ajili ya kusanyiko la pekee katika 1988
ULAYA NA NCHI ZA MEDITERANIA
AUSTRIA
[Picha katika ukurasa wa 373]
Mapema kama miaka ya 1890, baadhi ya watu katika Austria walikuwa wakipewa fursa ya kunufaika na habari njema. Tangu miaka ya 1920, kumekuwa na ukuzi wa kiasi lakini wenye kuendelea wa idadi ya wanaosifu Yehova katika nchi hii.
[Picha katika ukurasa wa 373]
Zaidi ya makutaniko 270 hukutana katika Majumba ya Ufalme kotekote Austria
UBELGIJI
[Picha katika ukurasa wa 373]
Ubelgiji imekuja kuwa mojawapo vitovu muhimu ulimwenguni. Ili kushughulikia idadi ya watu wa namna mbalimbali wanaopatikana huku, tawi hili hugawanya fasihi za Biblia katika lugha zaidi ya 100.
UINGEREZA
[Picha katika ukurasa wa 374]
Utendaji wa Mashahidi wa Yehova zaidi ya 125,000 katika Uingereza husimamiwa kutoka ofisi hii ya tawi. Mashahidi kutoka Uingereza wamechukua migawo pia ili kueneza ujumbe wa Ufalme katika nchi nyinginezo za Ulaya pamoja na barani Afrika, Amerika Kusini, Australia, nchi za Mashariki, na visiwa vya bahari.
IBSA House
Watch Tower House
[Picha katika ukurasa wa 374]
Fasihi za Biblia huchapwa huku katika Kiingereza, Kimalta, Kigujarati, na Kiswahili
[Picha katika ukurasa wa 374]
Idara ya Utumishi hushughulikia makutaniko zaidi ya 1,300 katika Uingereza
[Picha katika ukurasa wa 374]
Ugavi wa fasihi hupelekwa kwenye sehemu zote za Uingereza, Scotland, Wales, Ireland, na Malta, kutia na nchi za Afrika na Karibea
UFARANSA
[Picha katika ukurasa wa 375]
Vichapo vyote vya Watch Tower vinavyochapwa ulimwenguni pote kwa ajili ya watu wanaosema Kifaransa, hutafsiriwa na kupangwa chapa kwa picha kwenye tawi katika Ufaransa. (Watu zaidi ya 120,000,000 husema Kifaransa.) Fasihi huchapwa huku kwa ukawaida katika lugha mbalimbali na husafirishwa kwa nchi za Ulaya, Afrika, Mashariki ya Kati, Bahari ya Hindi, na Bahari ya Pasifiki.
Kiwanda cha kuchapia/ofisi katika Louviers
Kutafsiri
Kupanga chapa kwa picha
[Picha katika ukurasa wa 375]
Ofisi/makao katika Boulogne-Billancourt
[Picha katika ukurasa wa 375]
Makao katika Incarville kwa ajili ya familia ya Betheli
UJERUMANI
[Picha katika ukurasa wa 376, 377]
Kujapokuwa jitihada za ukatili ili kuwaangamiza katika Ujerumani wakati wa enzi ya Nazi, Mashahidi wa Yehova hawakuacha imani yao. Tangu 1946, wametumia muda wa saa zaidi ya 646,000,000 katika kueneza kweli ya Biblia kotekote nchini.
Vifaa vilivyopanuliwa katika Selters/Taunus
[Picha katika ukurasa wa 376]
Zaidi ya kutafsiri fasihi za Biblia katika Kijerumani, tawi hili katika Selters/Taunus huchapa katika lugha zaidi ya 40
[Picha katika ukurasa wa 377]
Kiasi kikubwa cha fasihi kinachotokezwa hapa husafirishwa kwa ukawaida kwenye nchi zaidi ya 20; magazeti huchapwa katika lugha nyingi na kupelekwa kwenye nchi zaidi ya 30
[Picha katika ukurasa wa 377]
Malori ya Sosaiti hutumiwa kusafirisha fasihi kotekote katika Ujerumani
SAIPRASI
[Picha katika ukurasa wa 376]
Muda mfupi baada ya kifo cha Yesu Kristo, habari njema zilikuwa zikihubiriwa kwa watu wa Saiprasi. (Mdo. 4:32-37; 11:19; 13:1-12) Katika siku za kisasa, mahubiri hayo yameanzishwa tena, na ushahidi kamili huendelea kutolewa chini ya mwelekezo wa ofisi ya tawi.
DENMARK
[Picha katika ukurasa wa 377]
Tangu miaka ya 1890, ushahidi umetolewa kwa kadiri kubwa katika Denmark. Fasihi za Biblia zimechapiwa huku si katika Kidenmark tu bali pia katika Kifaeroese, Kigreenland, na Kiiceland.
Tawi linavyoonekana kutoka juu (kiingilio kinaonyeshwa katika picha ya ndani)
ITALIA
[Picha katika ukurasa wa 378, 379]
Fasihi ya Biblia ya Kiitalia hutafsiriwa na kuchapwa huku pia. Tawi hili huchapa na kujalidi vitabu viweze kutumiwa hasa katika Italia na nchi nyinginezo jirani.
Sura mbalimbali za majengo ya tawi yaliyo karibu na Roma
[Picha katika ukurasa wa 379]
Makumi ya maelfu ya watu wameanza kukusanyika pamoja na Mashahidi wa Yehova baada ya kuona yale ambayo Biblia husema hasa
[Picha katika ukurasa wa 379]
Wajapokabiliwa na uhasama mwingi kutoka kwa Kanisa la Katoliki ya Roma, Mashahidi wa Yehova katika Italia wametumia muda wa saa zaidi ya 550,000,000 tangu 1946 katika ziara za kibinafsi kwa majirani wao ili kuzungumza nao juu ya Biblia. Kama tokeo, watu 194,000 katika Italia ni waabudu walio watendaji wa Yehova
FINLAND
[Picha katika ukurasa wa 378]
Kweli ya Biblia ilifika Finland kutoka Sweden katika 1906. Tangu wakati huo, imepelekwa kotekote nchini, hata mbali katika Mzingo Aktiki. Wengi kutoka huku wamehudhuria Shule ya Gileadi ili kuzoezwa kwa ajili ya utumishi mahali popote walipohitajiwa katika shamba la ulimwengu. Wengine walihama wao wenyewe ili kutumikia katika nchi ambako uhitaji ulikuwa mkubwa zaidi.
ICELAND
[Picha katika ukurasa wa 379]
Katika Iceland, ambayo ina idadi ya watu karibu 260,000 tu, fasihi za Biblia zaidi ya 1,620,000 zimegawanywa ili kusaidia watu kuchagua uhai. Sasa watu zaidi ya 260 huku humtumikia Yehova, Mungu wa kweli.
[Picha katika ukurasa wa 379]
Georg Lindal, aliyepainia huku kutoka 1929 hadi 1953; kwa muda mrefu wakati huo, yeye alikuwa ndiye Shahidi pekee nchini
UGIRIKI
[Picha katika ukurasa wa 380]
Mtume Paulo alikuwa mmojawapo watu wa kwanza kutangaza habari njema katika Ugiriki. (Mdo. 16:9-14; 17:15; 18:1; 20:2) Ijapokuwa Kanisa Othodoksi la Kigiriki limewanyanyasa sana Mashahidi wa Yehova kwa miaka mingi, sasa kuna watumishi waaminifu wa Yehova zaidi ya 24,000 katika nchi hii. Tawi linaloonyeshwa hapa liko umbali wa karibu kilometa 65 kaskazini mwa Athene.
[Picha katika ukurasa wa 380]
Kutoa ushahidi katika Athene
[Picha katika ukurasa wa 380]
Picha ilipigwa katika 1990 wakati wa maandamano yaliyoongozwa na makasisi dhidi ya Mashahidi
IRELAND
[Picha katika ukurasa wa 380]
Katika Ireland, itikio kwa ujumbe wa Biblia lilikuwa la polepole kwa miaka mingi. Walipata upinzani mwingi wa makasisi. Lakini baada ya miaka 100 ya kufuliza kutoa ushahidi, sasa kuna mavuno mengi ya kiroho.
Ofisi ya tawi katika Dublin
[Picha katika ukurasa wa 380]
Mapainia wawili wa muda mrefu katika utumishi wa shambani
POLAND
[Picha katika ukurasa wa 381]
Vifaa hivi vinatumiwa ili kuandaa msaada kwa Mashahidi zaidi ya 100,000 nchini Poland. Ibada yao ilipigwa marufuku kuanzia 1939 hadi 1945, lakini idadi yao iliongezeka kuanzia 1,039 katika 1939 hadi 6,994 katika 1946. Walipopigwa marufuku tena katika 1950, idadi yao ilikuwa 18,116; lakini muda mfupi baada ya marufuku hiyo kuondolewa katika 1989, ripoti zilionyesha kwamba walikuwa zaidi ya 91,000.
[Picha katika ukurasa wa 381]
Kwa miaka mingi walifanya makusanyiko madogo vichakani; sasa mikusanyiko yao hujaza stediamu kubwa zaidi nchini—na zaidi ya stediamu moja kwa wakati mmoja
Poznan (1985)
LUXEMBOURG
[Picha katika ukurasa wa 382]
Luxembourg ni mojawapo ya nchi ndogo sana za Ulaya. Lakini ujumbe wa Ufalme umehubiriwa huku pia, kwa miaka 70. Hasa kabla ya Vita ya Ulimwengu 2, msaada ulitolewa na Mashahidi waliokuja kutoka Ufaransa, Ujerumani, na Uswisi.
UHOLANZI
[Picha katika ukurasa wa 382]
Kutoka kwa tawi hili katika Emmen, usimamizi huandaliwa kwa ajili ya utendaji wa Mashahidi 32,000 wenye bidii katika Uholanzi. Kazi ya kutafsiri fasihi zote katika Kiholanzi hufanywa katika vifaa hivi. Kazi nyingi ya kutokeza kaseti za vidio za Kibiblia katika lugha za Ulaya hushughulikiwa huku pia.
NORWAY
[Picha katika ukurasa wa 383]
Miaka mia moja iliyopita, Mnorway aliyehamia Marekani na kujifunza kweli za Biblia huko alileta hizo habari njema katika mji alimozaliwa. Tangu wakati huo, Mashahidi wa Yehova wamezuru kila sehemu ya Norway tena na tena ili kuzungumza na watu kuhusu Ufalme wa Mungu.
URENO
[Picha katika ukurasa wa 383]
Kwa miongo ya miaka baada ya serikali kutia sahihi mkataba pamoja na Vatikani, polisi walikamata Mashahidi na kuwafukuza wamishonari wao. Lakini Mashahidi waliobaki waliendelea kukutana kwa ajili ya ibada, kuhubiri wengine, na kuongezeka. Mwishowe, katika 1974 walitambuliwa kisheria.
Ofisi hii husimamia utendaji wa Mashahidi zaidi ya 40,000 katika Ureno. Pia imetoa msaada mwingi kwa nchi za Afrika zilizokuwa na uhusiano wa karibu na Ureno
[Picha katika ukurasa wa 383]
Mkusanyiko wa kimataifa uliofanywa jijini Lisbon mwaka 1978
SWEDEN
[Picha katika ukurasa wa 383]
Kwa miaka zaidi ya 100, Mashahidi wa Yehova wamekuwa wakihubiri nchini Sweden. Katika muda wa miaka kumi iliyopita, wametumia muda wa saa zaidi ya 38,000,000 katika utendaji huu. Makutaniko mengi nchini Sweden sasa husema lugha nyingine nyingi mbali na Kisweden.
[Picha katika ukurasa wa 383]
Ili kusaidia watu wa kila aina nchini Sweden, vichapo hupatikana hapa katika lugha 70
HISPANIA
[Picha katika ukurasa wa 384]
Tawi hili hushughulikia Mashahidi zaidi ya 92,000 katika Hispania. Hilo huchapa “Mnara wa Mlinzi” na “Amkeni!” kwa ajili ya Hispania na Ureno pia. Kujapokuwa jitihada nyingi za makasisi Wakatoliki za kutumia Serikali ili kukomesha Mashahidi wa Yehova, Mashahidi wameshiriki kweli za Biblia na Wahispania tangu 1916. Hatimaye, katika 1970, wakati Mashahidi wa Yehova nchini Hispania walipokuwa zaidi ya 11,000, wao walitambuliwa kisheria. Tangu wakati huo, idadi yao imeongezeka mara nane.
[Picha katika ukurasa wa 384]
Makutaniko zaidi ya 1,100 sasa hukutana kwa uhuru katika Majumba ya Ufalme yanayopatikana kotekote nchini
USWISI
[Picha katika ukurasa wa 384]
Tangu 1903 Watch Tower Society imekuwa na ofisi katika Uswisi. Kimojawapo viwanda vya uchapaji vya Sosaiti vya mapema sana katika Ulaya kilikuwa katika nchi hii. Kwa miaka mingi tawi hapa katika Thun lilichapa magazeti ili yatumiwe katika nchi nyinginezo nyingi.
AFRIKA
BENIN
[Picha katika ukurasa wa 385]
Nchini Benin kuna vikundi vya kikabila vipatavyo 60 vinavyosema lahaja 50. Wakati maelfu ya watu hao walipojiweka huru kutoka kwa dini zao za awa- li, hilo liliwaghadhibisha makuhani wa makago na makasisi wa Jumuiya ya Wakristo pia. Lakini mawi- mbi ya mnyanyaso yenye kurudia-rudia hayaku- komesha ukuzi wa ibada ya kweli katika nchi hii.
[Picha katika ukurasa wa 385]
Mkusanyiko uliofanywa katika 1990
JAMHURI YA AFRIKA YA KATI
[Picha katika ukurasa wa 385]
Mapema kama 1947, ujumbe wa Ufalme ulianza kufikia watu huku. Mwanamume aliyekuwa amehudhuria mikutano fulani ya Mashahidi kwingineko alishiriki na wengine yale aliyokuwa amejifunza. Upesi kukawa na kikundi cha funzo, wale waliohudhuria wakaanza upesi kutoa ushahidi, na wale walioabudu Yehova wakaongezeka idadi.
CÔTE D’IVOIRE
[Picha katika ukurasa wa 386]
Wamishonari waliozoezwa Gileadi walisaidia kuanzisha ibada ya kweli katika nchi hii ya Afrika Magharibi katika 1949. Wamishonari zaidi ya mia moja wametumika huku. Kila mwaka, muda wa saa zaidi za milioni moja unatumiwa sasa katika kuwatafuta watu wenye njaa ya kiroho katika eneo linaloshughulikiwa na ofisi hii ya tawi.
GHANA
[Picha katika ukurasa wa 386, 387]
Kuhubiriwa kwa habari njema katika Ghana kulianza katika 1924. Sasa ofisi hii katika Accra husimamia makutaniko zaidi ya 640 katika Ghana. Pia imeshughulikia kazi ya kutafsiri fasihi za Biblia katika Kiewe, Kiga, na Kitwi na kuichapa katika lugha hizo.
[Picha katika ukurasa wa 387]
Kukutana katika Jumba la Ufalme linalopakana na ofisi ya tawi
KENYA
[Ramani/Picha katika ukurasa wa 387]
Katika 1931, Mashahidi wa Yehova wawili walisafiri kutoka Afrika Kusini ili kuhubiri katika Kenya. Tangu 1963 katika nyakati mbalimbali, ofisi ya Sosaiti nchini Kenya imeandaa usimamizi wa kazi ya kueneza evanjeli katika nchi nyingine nyingi za Afrika Mashariki (kama inavyoonyeshwa chini). Mikusanyiko ya kimataifa nchini Kenya katika 1973, 1978, na 1985 imechangia kwenye ushahidi uliotolewa.
[Ramani]
(Ona mpangilio kamili katika nakala iliyochapishwa)
KENYA
UGANDA
SUDAN
ETHIOPIA
JIBUTI
SOMALIA
YEMENI
SHELISHELI
TANZANIA
BURUNDI
RWANDA
[Picha katika ukurasa wa 387]
Mkusanyiko wa Nairobi (1978)
NIGERIA
[Picha katika ukurasa wa 388, 389]
Habari njema zimehubiriwa katika nchi hii tangu mapema katika miaka ya 1920. Pia waeneza-evanjeli wametumwa kutoka Nigeria hadi kwenye sehemu nyingine za Afrika Magharibi, na fasihi za Biblia zinazochapwa hapa huendelea kujazia mahitaji ya nchi za karibu. Katika Nigeria yenyewe, Mashahidi wa Yehova wamewakabidhi watu fasihi zaidi ya 28,000,000 ili kuwasaidia waelewe Neno la Mungu.
[Picha katika ukurasa wa 388]
Kutoka Idara ya Utumishi, usimamizi huandaliwa kwa ajili ya wapiga-mbiu wa Ufalme zaidi ya 160,000 katika Nigeria
[Picha katika ukurasa wa 389]
Mkusanyiko katika Calabar, Nigeria (1990)
LIBERIA
[Picha katika ukurasa wa 388]
Wale ambao wamekuwa Mashahidi wa Yehova huku wamekabili mitihani mingi ya imani yao—wanapoacha mambo mbalimbali ya ushirikina, wanapoacha kuwa na wake zaidi ya mmoja, wanaponyanyaswa na maofisa walioarifiwa vibaya kuwahusu, na wanapozungukwa na vikundi vya kisiasa na kikabila vinavyopigana. Na bado, ibada ya kweli yaendelea kuunganisha watu wa aina zote katika nchi hii.
MAURITIUS
[Picha katika ukurasa wa 389]
Mapema kama 1933, Mashahidi wenye bidii kutoka Afrika Kusini walizuru kisiwa hiki cha Bahari ya Hindi. Sasa kunao Mashahidi zaidi ya elfu moja katika Mauritius wanaohimiza majirani zao kumtafuta Yehova ili waweze kuonwa naye kwa upendeleo wakati anapoharibu mfumo mwovu wa sasa.—Sef. 2:3.
AFRIKA KUSINI
[Picha katika ukurasa wa 390]
Kwa zaidi ya miaka 80, Watch Tower Society imekuwa na ofisi ya tawi katika Afrika Kusini. Waeneza-evanjeli wenye bidii kutoka huku wamefanya mengi katika kueneza ujumbe wa Ufalme katika nchi nyinginezo za kusini na mashariki mwa Afrika. Katika eneo lililokuwa chini ya tawi hili (ambako kulikuwa na wapiga-mbiu wa Ufalme 14,674 katika 1945), sasa kuna Mashahidi wa Yehova watendaji zaidi ya 300,000.
[Picha katika ukurasa wa 391]
Watafsiri zaidi ya 110 hufanya kazi chini ya mwelekezo wa tawi hili katika kutayarisha fasihi za Biblia katika lugha 16 za Afrika
[Picha katika ukurasa wa 391]
Kazi ya kuchapa hufanyiwa hapa katika lugha zaidi ya 40
SENEGAL
[Picha katika ukurasa wa 390]
Ingawa idadi ya Mashahidi huku ni ndogo, ofisi ya tawi imejaribu kuhakikisha kwamba kila jiji, kila kikundi cha kabila, na watu wa kila dini, si katika Senegal tu bali pia katika nchi zinazozunguka, wana fursa ya kusikia ujumbe wa Biblia wenye kuchangamsha moyo.
SIERRA LEONE
[Picha katika ukurasa wa 391]
Kuhubiriwa kwa habari njema kulianza katika Sierra Leone katika mwaka 1915. Nyakati nyingine ukuzi umekuwa wa polepole. Lakini wakati wale ambao hawakushikilia viwango vya juu vya Yehova walipoondolewa na wale ambao hawakutumikia kwa makusudi mazuri wakaondoka, wale walio waaminifu-washikamanifu kwa Yehova walisitawi kiroho.
ZAMBIA
[Picha katika ukurasa wa 392]
Ofisi hii ya tawi husimamia utendaji wa Mashahidi zaidi ya 110,000 katika Afrika ya kusini na kati. Ofisi ya kwanza ya Sosaiti huku ilifunguliwa katika 1936. Tangu wakati huo, Mashahidi wa Yehova katika Zambia wamefanya ziara za kurudia zaidi ya 186,000,000 ili kutoa msaada zaidi kwa wanaopendezwa. Pia wamefundisha wengi kusoma ili waweze kujifunza Biblia binafsi na kuishiriki na wengine.
[Picha katika ukurasa wa 392]
Mfululizo wa mikusanyiko nchini Zambia katika 1992 ulihudhuriwa na 289,643
ZIMBABWE
[Picha katika ukurasa wa 392]
Mashahidi wa Yehova wamekuwa watendaji katika Zimbabwe tangu miaka ya 1920. Wakati wa miaka iliyofuata, fasihi zao zilipigwa marufuku, wakakatazwa kufanya makusanyiko, na kunyimwa idhini ya wamishonari kuweza kuhubiri wenyeji Waafrika. Hatua kwa hatua, vikwazo vilishindwa, na sasa ofisi hii huwatunza Mashahidi zaidi ya 20,000.
NCHI ZA MASHARIKI
HONG KONG
[Picha katika ukurasa wa 393]
Vichapo vya Watch Tower hutafsiriwa huku katika Kichina, ambacho husemwa na watu zaidi ya bilioni moja katika lahaja zacho nyingi. Katika Hong Kong yenyewe, kazi ya kuhubiri habari njema ilianza wakati C. T. Russell alipohutubu kwenye jumba kuu la jiji katika 1912.
INDIA
[Picha katika ukurasa wa 393]
Tawi hili husimamia kazi ya kupiga mbiu ya ujumbe wa Ufalme kwa zaidi ya moja kwa sita ya idadi ya watu duniani. Wakati huu, ofisi hii huelekeza kazi ya kutafsiri katika lugha 18 na ya kuchapa katika 19. Miongoni mwa hizo ni Kihindi (kinachosemwa na watu milioni 367) pia Kiassami, Kibengali, Kigujarati, Kikanada, Kimaleya, Kimarathi, Kinepali, Kioriya, Kipunjabi, Kitamili, Kitelugu, na Kiurdu (kila moja ikisemwa na makumi ya mamilioni).
[Picha katika ukurasa wa 393]
Mashahidi wanaohubiri katika Kimaleya
. . . katika Kinepali
. . . katika Kigujarati
JAPANI
[Picha katika ukurasa wa 394]
Mashahidi wa Yehova katika Japani, kama kwingineko, ni wapiga-mbiu wa Ufalme wa Mungu wenye bidii. Katika 1992 pekee, walitumia zaidi ya saa 85,000,000 kuhubiri habari njema. Kwa wastani, karibu asilimia 45 ya Mashahidi Wajapani hushiriki katika utumishi wa upainia kila mwezi.
[Picha katika ukurasa wa 394]
Fasihi za Biblia huchapwa huku katika lugha nyingi, kutia na Kijapani, Kichina, na lugha za Filipino
[Picha katika ukurasa wa 394]
Ofisi ya Uhandisi ya Kimkoa husaidia kazi kwenye vifaa vya tawi katika nchi mbalimbali
[Grafu katika ukurasa wa 394]
(Ona mpangilio kamili katika nakala iliyochapishwa)
Mapainia Katika Japani
75,000
50,000
25,000
1975 1980 1985 1992
JAMHURI YA KOREA
[Picha katika ukurasa wa 395]
Fasihi za Biblia zipatazo milioni 16, kuongezea trakti, hutokezwa huku kila mwaka ili kutoa ugavi kwa Mashahidi zaidi ya 70,000 katika Jamhuri ya Korea. Karibu asilimia 40 ya Mashahidi Wakorea wako katika utumishi wa painia.
MYANMAR
[Picha katika ukurasa wa 395]
Wakati Watch Tower Society ilipofungua ofisi ya tawi huku katika 1947, kulikuwa Mashahidi wa Yehova 24 pekee nchini. Mashahidi watendaji zaidi ya 2,000 sasa katika Myanmar hujaribu kufikia si wenyeji tu wa majijini, bali pia idadi kubwa ya watu wa mashambani.
FILIPINO
[Picha katika ukurasa wa 396]
Katika 1912, C. T. Russell alihutubu katika Grand Opera House la Manila juu ya kichwa “Wafu Wako Wapi?” Tangu wakati huo Mashahidi wa Yehova huku wametumia muda wa saa zaidi ya 483,000,000 katika kutoa ushahidi kwa watu wanaopatikana katika visiwa vinavyokadiriwa kuwa 900 vya Filipino. Usimamizi wa ujumla wa Mashahidi zaidi ya 110,000 katika makutaniko 3,200 huandaliwa kutoka tawi hili. Uchapaji hufanywa hapa katika lugha nane ili kujazia mahitaji ya wenyeji.
[Picha katika ukurasa wa 396]
Mashahidi kutoka kwa baadhi ya vikundi vya lugha kuu katika Filipino
SRI LANKA
[Picha katika ukurasa wa 397]
Kabla ya Vita ya Ulimwengu 1, habari njema ilikuwa ikihubiriwa katika Ceylon (sasa Sri Lanka), kusini mwa India. Kikundi cha funzo kilipangwa upesi. Tangu 1953 Sosaiti imekuwa na ofisi ya tawi katika jiji kuu, ili kuwapa Wasinhalisi, Watamili, na vikundi vinginevyo vya kikabila nchini fursa ya kusikia ujumbe wa Ufalme.
TAIWAN
[Picha katika ukurasa wa 397]
Ushahidi fulani ulitolewa huku katika miaka ya 1920. Lakini ulitolewa kwa kuendelea zaidi katika miaka ya 1950. Sasa vifaa hivi vipya vya tawi vinajengwa ili kuandaa kitovu cha utendaji ulioongezeka katika sehemu hii ya dunia.
[Picha katika ukurasa wa 397]
Kutaniko katika Taipei
THAILAND
[Picha katika ukurasa wa 397]
Wakati wa miaka ya 1930, Mashahidi mapainia walikuja kutoka Uingereza, Ujerumani, Australia, na New Zealand ili kushiriki kweli ya Biblia na Wathailand (wakati huo ikiitwa Siam). Wajumbe kutoka nchi nyingi walihudhuria mikusanyiko ya kimataifa huku katika 1963, 1978, 1985, na 1991 ili kuwatia moyo Mashahidi wenyeji na kuchochea kuenezwa kwa ujumbe wa Ufalme.
[Picha katika ukurasa wa 397]
Mkusanyiko wa 1963
[Picha katika ukurasa wa 397]
Wajumbe kutoka ng’ambo katika 1991
VISIWA VYA PASIFIKI
FIJI
[Picha katika ukurasa wa 398]
Ofisi katika Fiji ilifunguliwa katika 1958. Kwa muda fulani ilisimamia kazi ya kupiga mbiu ya Ufalme katika nchi 12 na lugha 13. Sasa tawi la Fiji hukazia fikira visiwa karibu mia moja vinavyokaliwa vya kikundi cha Fiji.
[Picha katika ukurasa wa 398]
Mikusanyiko ya kimataifa hapa katika 1963, 1969, 1973, na 1978 ilisaidia kuwaleta Mashahidi wenyeji karibu zaidi na wale wa nchi nyinginezo
GUAM
[Picha katika ukurasa wa 398]
Ofisi katika Guam huelekeza kuhubiriwa kwa habari njema katika visiwa vilivyoenea kilometa 7,770,000 za mraba katika Bahari ya Pasifiki. Kazi ya kutafsiri fasihi za Biblia katika lugha tisa imo chini ya usimamizi wayo.
[Picha katika ukurasa wa 398]
Mara nyingi mwangalizi wa mzunguko husafiri kwa ndege kati ya visiwa
[Picha katika ukurasa wa 398]
Mashahidi wenyeji (kama wanavyoonyeshwa hapa katika Maikronesia) waweza kutumia mashua ili kufikia eneo lao
HAWAII
[Picha katika ukurasa wa 399]
Watch Tower Society imekuwa na ofisi ya tawi katika Honolulu tangu 1934. Wengine kutoka Hawaii wameshiriki kazi ya kueneza evanjeli si katika visiwa vya Hawaii tu bali pia katika Japani, Taiwan, Guam, na visiwa vya Maikronesia.
NEW CALEDONIA
[Picha katika ukurasa wa 399]
Kujapokuwa vizuizi kutoka kwa wapinzani wa kidini, Mashahidi wa Yehova walileta ujumbe wa Ufalme wa Mungu katika New Caledonia. Watu wengi walisikiliza kwa uthamini. Katika 1956 kutaniko la kwanza lilifanyizwa. Sasa huku kuna wasifaji wa Yehova zaidi ya 1,300.
NEW ZEALAND
[Picha katika ukurasa wa 399]
Katika 1947 Watch Tower Society ilifungua ofisi ya tawi katika New Zealand ili kuandaa usimamizi wa karibu zaidi wa kazi ya kuhubiri habari njema huku.
[Picha katika ukurasa wa 399]
Kazi ya kutafsiri inayofanywa katika tawi hili huwezesha wenyeji wa Samoa, Rarotonga, na Niue kupokea ujenzi wa kiroho kwa kawaida.
[Picha katika ukurasa wa 399]
Watafsiri na wasahihishaji hushirikiana ili kuandaa vichapo vya hali ya juu
AUSTRALIA
[Picha katika ukurasa wa 400]
Watch Tower Society imekuwa na ofisi ya tawi katika Australia tangu 1904. Zamani tawi hili lilisimamia kazi ya kupiga mbiu ya Ufalme kwa karibu robo ya dunia yote, kutia na China, Kusini-Mashariki mwa Asia, na visiwa vya Pasifiki Kusini.
[Picha katika ukurasa wa 400]
Ofisi ya Uhandisi ya Kimkoa husaidia katika ujenzi wa tawi katika Pasifiki Kusini na Kusini-Mashariki mwa Asia
[Picha katika ukurasa wa 400]
Wakati huu, tawi hili huchapa fasihi za Biblia katika lugha zaidi ya 25. Kiwanda cha uchapaji huku husaidia kutoa ugavi wa fasihi zinazohitajiwa na Mashahidi wapatao 78,000 walio katika sehemu zinazosimamiwa na matawi manane katika Pasifiki Kusini.
[Ramani/Picha katika ukurasa wa 400]
Nchi zinazopewa ugavi wa fasihi kutoka tawi la Australia
[Ramani]
(Ona mpangilio kamili katika nakala iliyochapishwa)
AUSTRALIA
PAPUA NEW GUINEA
NEW CALEDONIA
VISIWI VYA SOLOMON
FIJI
WESTERN SAMOA
TAHITI
NEW ZEALAND
PAPUA NEW GUINEA
[Picha katika ukurasa wa 400]
Magumu ya pekee hukabili Mashahidi wa Yehova katika nchi hii—watu husema lugha mbalimbali zipatazo 700. Mashahidi kutoka angalau nchi kumi nyingine wamehamia huku ili kushiriki kazi. Wamejitahidi kujifunza lugha za wenyeji. Wenye kupendezwa hutafsiria wale wanaosema lugha nyingine. Picha pia hutumiwa kwa matokeo zikiwa misaada katika kufundisha.
VISIWA VYA SOLOMON
[Picha katika ukurasa wa 401]
Funzo la Biblia lililoongozwa kimataifa kwa posta lilileta ujumbe wa Ufalme kwenye Visiwa vya Solomon kufikia mapema miaka ya 1950. Kujapokuwa vizuizi vikubwa, kweli ya Biblia ilienea. Ofisi hii ya tawi na Jumba la Kusanyiko lenye nafasi kubwa ni tokeo la ustadi mwingi wa wenyeji, ushirikiano wa kimataifa, na utele wa roho ya Yehova.
TAHITI
[Picha katika ukurasa wa 401]
Kufikia miaka ya 1930, Mashahidi wa Yehova walikuwa wamefika Tahiti na ujumbe wa Ufalme. Huku, katika Bahari ya Pasifiki, ushahidi mwingi unatolewa. Wakati wa miaka minne tu iliyopita, ushahidi uliofanywa unajumlika kuwa wastani wa muda wa saa zaidi ya tano za kusema, kwa kila mwanamume, mwanamke, na mtoto katika kisiwa hicho.
SAMOA MAGHARIBI
[Picha katika ukurasa wa 401]
Samoa Magharibi ni mojawapo mataifa yaliyo madogo zaidi ulimwenguni, lakini Mashahidi wa Yehova wana ofisi ya tawi huku pia. Jengo hili lilikuwa likijengwa katika 1992 ili kushughulikia utendaji katika kisiwa hiki na vinginevyo vilivyoko karibu, kutia na Samoa ya Amerika.
-