-
Kampeni ya Pekee Nchini Bulgaria YafanikiwaMnara wa Mlinzi—2010 | Septemba 15
-
-
Kwa sababu ya itikio hilo kubwa, wajitoleaji hao wangeweza kutumwa katika majiji matatu mbalimbali nchini Bulgaria: Kazanlak, Sandanski, na Silistra. Waangalizi wa mzunguko nchini Bulgaria waliwaalika mapainia wenyeji na wahubiri waunge mkono pia kampeni hiyo. Mwishowe, wajitoleaji 382 walikuwa wakihubiri kwa bidii katika maeneo ambayo hayakuwa yamehubiriwa habari njema kwa ukawaida.
Akina ndugu kutoka katika makutaniko ya karibu walitumwa mapema ili wawatafutie mahali pa kuishi. Walikodi nyumba za kuishi na wakahifadhi vyumba vya hoteli vya bei ya chini. Ndugu hao wenyeji walifanya kazi kwa bidii ili kuwasaidia wajitoleaji waliokuwa wakiwasili kupata mahali pa kuishi na kisha wakashughulikia mahitaji yao. Katika majiji yote matatu, walikodi mahali pa kufanyia mikutano. Mipango ilifanywa ili mikutano ya kutaniko iongozwe na ndugu waliotoka nchi nyingine. Ilisisimua kama nini kuona wahubiri 50 wakikutana ili kumsifu Yehova katika maeneo ambayo hakuna hata Shahidi mmoja anayeishi huko.
Wahubiri waliokuja kutoka nchi nyingine kwa ajili ya kampeni hiyo walikuwa na bidii nyingi sana. Wakati wa majira ya joto, kiwango cha joto nchini Bulgaria kinaweza kupita digrii 40 Selsiasi. Ingawa hivyo, hakuna jambo ambalo lingewazuia ndugu na dada hao wenye bidii. Silistra, jiji lililo kando ya Mto Danube ambalo lina wakaaji zaidi ya 50,000, lilipata ushahidi kamili kwa majuma matatu ya kwanza. Vivyo hivyo, akina ndugu waliendelea na bidii hiyohiyo na wakafika kwenye vijiji vilivyo karibu, hata walifika Tutrakan, kijiji kilicho kilomita 55 magharibi ya Silistra. Kwa kawaida walianza kuhubiri saa tatu na nusu asubuhi. Baada ya kupumzika kwa ajili ya chakula cha mchana, mara nyingi waliendelea mpaka saa moja jioni au hata usiku. Vivyo hivyo, kwa sababu ya bidii nyingi ya wajitoleaji hao, kampeni huko Kazanlak na Sandanski ilifanywa mpaka kwenye vijiji na majiji yaliyo karibu.
Ni Nini Kilichotimizwa?
Ushahidi mkubwa ulitolewa katika majuma hayo saba. Kama ilivyosemwa wakati wa mitume, wakaaji wa majiji hayo wangesema hivi: ‘Mmejaza majiji yetu na fundisho lenu.’ (Mdo. 5:28) Mashahidi walioshiriki waliwaachia watu magazeti 50,000 hivi na wakaanzisha mafunzo 482 ya Biblia. Jambo la kufurahisha ni kwamba kufikia Septemba 1, 2009, kutaniko lilianzishwa huko Silistra, na kuna vikundi huko Kazanlak na Sandanski. Inachangamsha moyo kuona watu ambao walisikia habari njema kwa mara ya kwanza wakati wa kampeni hiyo wakifanya maendeleo mazuri ya kiroho.
-
-
Kampeni ya Pekee Nchini Bulgaria YafanikiwaMnara wa Mlinzi—2010 | Septemba 15
-
-
Huko Kazanlak, ndugu mmoja Mbulgaria anayeitwa Orlin, ambaye alikuja kwa ajili ya kampeni hiyo kutoka Italia, alikuwa akitembea baada ya utumishi wa shambani kurudi mahali alipokuwa akiishi. Akiwa njiani, Orlin aliwahubiria wanaume wawili vijana ambao walikuwa wameketi kwenye kiti katika bustani. Aliwaachia kitabu Biblia Inafundisha na akapanga kuwatembelea tena siku iliyofuata. Siku iliyofuata, Orlin alianzisha funzo la Biblia pamoja na Svetomir na walijifunza tena siku iliyofuata. Kwa muda wa siku tisa, Orlin alijifunza na Svetomir mara nane. Svetomir alisema hivi: “Siku mbili kabla ya kukutana na wewe, nilikuwa nimesali kwa Mungu ili anisaidie kumjua. Na nilimwahidi kwamba kama angenisaidia, ningeweka wakfu maisha yangu kwake.” Baada ya Orlin kurudi Italia, ndugu wenyeji waliendelea kujifunza na Svetomir, na anafanya kweli iwe mali yake.
-