-
Utatazama Sinema Zipi?Amkeni!—2005 | Mei 8
-
-
Wazazi hasa wanapaswa kuwa waangalifu kuhusu sinema ambazo wanawaruhusu watoto wao kutazama. Lingekuwa jambo la kipumbavu kutazama tu kiwango cha sinema. Huenda sinema inayoonwa kuwa inamfaa mtoto wako mwenye umri fulani ikakazia maadili ambayo wewe ukiwa mzazi hukubali. Jambo hilo haliwashangazi Wakristo hata kidogo kwa kuwa ulimwengu hufikiri na kutenda kinyume na viwango vya Mungu.c—Waefeso 4:17, 18; 1 Yohana 2:15-17.
Hiyo haimaanishi kwamba sinema zote ni mbaya. Lakini tunapaswa kuwa waangalifu. Kuhusiana na hilo, toleo la Amkeni! la Mei 22, 1997 lilisema hivi: “Kila mtu anapaswa kuchanganua mambo kwa uangalifu na kufanya maamuzi ambayo yatamwacha akiwa na dhamiri safi mbele ya Mungu na mwanadamu.”—1 Wakorintho 10:31-33.
Jinsi ya Kupata Vitumbuizo Vinavyofaa
Wazazi wanawezaje kuwa wateuzi wanapochagua sinema ambazo familia zao zitatazama? Fikiria maelezo yafuatayo kutoka kwa wazazi ulimwenguni pote. Huenda maelezo yao yakakusaidia kutafuta vitumbuizo vinavyofaa familia yako.—Ona pia sanduku “Tafrija za Aina Nyingine,” kwenye ukurasa wa 14.
“Sikuzote mimi au mke wangu tuliambatana na watoto wetu kwenda kutazama sinema walipokuwa wachanga,” asema Juan anayeishi Hispania. “Hawakwenda peke yao kamwe au kuambatana na vijana wengine. Sasa, wakiwa vijana, hawaendi kutazama sinema inapoonyeshwa mara ya kwanza; badala yake, sisi huonelea wasubiri hadi tusome maoni ya wachambuzi wa sinema au tusikie maoni ya watu tunaowatumaini. Kisha tukiwa familia tunaamua kama tutatazama sinema hiyo.”
Mark, anayeishi Afrika Kusini, humtia moyo kijana wake aeleze maoni yake kuhusu sinema zinazoonyeshwa katika majumba ya sinema. Mark anasema: “Mimi na mke wangu huanzisha mazungumzo kuhusu sinema fulani na kumwuliza mwana wetu maoni yake. Jambo hilo hutuwezesha kusikiliza maoni yake na kumtolea sababu. Kwa njia hiyo, tunaweza kuchagua sinema ambazo sisi sote tunaweza kufurahia.”
Rogerio, anayeishi Brazili, pia hutumia wakati pamoja na watoto wake kuchanganua filamu wanazotaka kutazama. Anasema: “Tukiwa pamoja, sisi husoma maoni ya wachambuzi. Mimi huambatana nao kwenye maduka ya video ili kuwafundisha jinsi ya kutazama jalada la video kuona kama huenda filamu isifae.”
Matthew anayeishi Uingereza huona kwamba inanufaisha kuzungumza na watoto wake kuhusu sinema wanazotaka kutazama. Anasema: “Tangu wakiwa wachanga, tuliwahusisha watoto wetu katika mazungumzo kuhusu filamu ambazo zingetupendeza tukiwa familia. Ikiwa tungeamua kutoitazama filamu fulani, mimi na mke wangu tungewaeleza sababu badala ya kuwakataza tu.”
Kwa kuongezea, wazazi fulani wameona kwamba inafaa kufanya utafiti kwenye Intaneti kuhusu sinema. Kuna vituo vingi vya Intaneti vinavyotoa habari nyingi kuhusu filamu. Habari hizo zinaweza kutumiwa kuelewa vizuri mambo yanayokaziwa na sinema fulani.
Manufaa ya Dhamiri Iliyozoezwa
Biblia huzungumza kuhusu wale ambao “nguvu zao za ufahamu zimezoezwa kutofautisha yaliyo sawa na yaliyo makosa pia.” (Waebrania 5:14) Kwa hiyo, lengo la wazazi linapaswa kuwa kukazia viwango ambavyo vitawasaidia watoto wao kufanya maamuzi yenye hekima watakapokuwa na uhuru wa kuchagua vitumbuizo vyao.
Kuhusiana na jambo hilo, vijana wengi ambao ni Mashahidi wa Yehova wamezoezwa vizuri na wazazi wao. Kwa mfano, Bill na Cherie, wanaoishi Marekani hufurahia kwenda kutazama sinema pamoja na wavulana wao wawili. Bill anasema, “baada ya kutazama sinema hiyo, mara nyingi sisi huzungumza kuhusu filamu hiyo, ilifundisha maadili gani na ikiwa tunakubaliana na maadili hayo au la.” Bila shaka, Bill na Cherie wanatambua umuhimu wa kuwa wateuzi. Bill anasema, “Sisi hufanya uchunguzi kuhusu filamu hiyo kabla ya kuitazama, na hatuoni aibu kutoka kwenye jumba la sinema ikiwa kuna jambo lisilofaa ambalo hatukuwa tumetarajia.” Kwa kuwahusisha watoto wao kufanya maamuzi mazito, Bill na Cherie wanahisi kwamba wanawasaidia wana wao kusitawisha mtazamo unaofaa kuhusu mema na mabaya. Bill anasema, “wanafanya maamuzi ya hekima zaidi wanapochagua filamu watakazotazama.”
Kama Bill na Cherie, wazazi wengi wamewasaidia watoto wao kuzoeza nguvu zao za ufahamu kuhusiana na vitumbuizo. Ni kweli kwamba sinema nyingi ambazo watayarishaji wa filamu hutokeza hazifai. Kwa upande mwingine, wanapoongozwa na kanuni za Biblia, Wakristo wanaweza kufurahia vitumbuizo vinavyofaa na kuburudisha.
-
-
Utatazama Sinema Zipi?Amkeni!—2005 | Mei 8
-
-
c Wakristo wanapaswa pia kukumbuka kwamba huenda sinema za watoto na vijana zikawa na mambo yanayohusiana na uchawi, kuwasiliana na pepo, au mambo mengine ya kishetani.—1 Wakorintho 10:21.
-
-
Utatazama Sinema Zipi?Amkeni!—2005 | Mei 8
-
-
[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 12]
‘SISI HUFANYA MAAMUZI PAMOJA’
“Nilipokuwa mdogo, tulienda kwenye sinema tukiwa familia. Kwa kuwa sasa nina umri mkubwa, ninaruhusiwa kwenda peke yangu. Hata hivyo, kabla ya kuniruhusu kwenda, wazazi wangu hutaka kujua kichwa cha filamu hiyo na habari inayozungumziwa. Ikiwa hawajui jambo lolote kuhusu sinema hiyo, wao husoma maoni ya wachambuzi au kutazama sehemu ndogo ya sinema hiyo inapoonyeshwa kwenye televisheni. Pia wao hutafuta habari kuhusu sinema hiyo kwenye Intaneti. Wakihisi kwamba sinema hiyo haifai, wao hutoa sababu. Vilevile wao huniruhusu nitoe maoni yangu. Sisi hujieleza waziwazi na kufanya maamuzi pamoja.” —Héloïse, mwenye umri wa miaka 19, anayeishi Ufaransa.
[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 13]
ZUNGUMZIENI MAMBO HAYO!
“Wazazi wakiwakataza watoto wao vitumbuizo fulani na kukosa kuwapa vitumbuizo vinavyofaa, huenda watoto hao wakajaribu kutosheleza tamaa zao kwa siri. Kwa hiyo, watoto wanapotaka kutazama sinema zisizofaa, wazazi fulani hawawakatazi moja kwa moja, wala kuwaruhusu. Badala yake, wao hungoja hali itulie. Bila kukasirika, wao huzungumzia mambo hayo kwa siku kadhaa, wakimwuliza kijana huyo sababu inayofanya ahisi kwamba sinema hiyo inafaa. Wanapozungumzia jambo hilo, mara nyingi vijana hukubaliana na wazazi wao na hata kuwashukuru. Kisha, wakiongozwa na wazazi wao, wao huchagua vitumbuizo vingine wanavyoweza kufurahia pamoja.”—Masaaki, mwangalizi asafiriye huko Japani.
-