-
Je, Watoto Wanapaswa Kujifunza Kumhusu Mungu?Mnara wa Mlinzi—2011 | Agosti 1
-
-
Je, Watoto Wanapaswa Kujifunza Kumhusu Mungu?
“Dini zinatusaidia zaidi kuchukiana kuliko zinavyotusaidia kupendana.”—JONATHAN SWIFT, MWANDISHI MWINGEREZA.
SWIFT alisema maneno hayo karne ya 18, lakini watu wengi leo wangekubaliana naye. Hata wengine wanaamini kwamba wazazi hawapaswi kuwa na haki ya kuwafundisha watoto wao kumhusu Mungu. Wanahisi kwamba watoto wanaolelewa katika familia za kidini wanakosa mambo fulani.
Una maoni gani? Ni hoja gani kati ya hoja zinazofuata ambazo unafikiri zinafaa zaidi?
● Wazazi hawapaswi kuruhusiwa kuwafundisha watoto wao kumhusu Mungu.
● Wazazi wanapaswa kungoja mpaka watoto wao wawe watu wazima kabla ya kuanza kuzungumzia mambo ya dini pamoja nao.
● Wazazi wanapaswa kuwafundisha watoto wao wakiwa wangali wadogo yale wanayoamini kumhusu Mungu. Lakini watoto wanapokuwa watu wazima, wazazi wanapaswa kuwatia moyo wachanganue mafundisho hayo wao wenyewe.
● Watoto wanapaswa kukubali mafundisho ya wazazi wao kumhusu Mungu bila kujali kama ni ya kweli au la.
Je, Dini Inawaathiri Watoto?
Hakuna mzazi anayejali ambaye angependa kumdhuru, au kumuumiza, mtoto wake. Lakini je, mambo ya hakika yanaunga mkono madai ya wale ambao wangetaka kuwazuia wazazi wasiwafundishe watoto wao kumhusu Mungu? Kwa miaka mingi sasa, watafiti wamechunguza sana jinsi imani ya wazazi inavyoweza kuwaathiri watoto. Wamefikia mkataa gani?
Watafiti wametambua kwamba dini inaweza kuwa na matokeo mazuri katika ukuzi wa mtoto, badala ya kumdhuru. Katika mwaka wa 2008, ripoti iliyochapishwa kwenye gazeti la Social Science Researcha ilisema: “Imethibitika kwamba dini inaweza kuboresha uhusiano kati ya mtoto na kila mmoja wa wazazi wake.” Ripoti hiyo pia ilisema: “Inaonekana kwamba dini na kuzingatia mambo ya kiroho ni sehemu muhimu katika maisha ya watoto wengi na ni muhimu pia katika mahusiano ya kifamilia.” Ona jinsi matokeo ya utafiti huo yanavyopatana na yale ambayo Yesu Kristo alisema: “Wenye furaha ni wale wanaotambua uhitaji wao wa kiroho.”—Mathayo 5:3.
Namna gani maoni kwamba watoto wanapaswa kufundishwa kumhusu Mungu na dini wanapokuwa watu wazima? Maoni hayo yanapuuza jambo hili la hakika: Ubongo wa mtoto ni kama ndoo isiyo na kitu ndani ambayo inangoja kujazwa. Kwa kweli, lazima wazazi waamue; ama kujaza “ndoo” hiyo kwa kuwafundisha watoto wao mambo yanayofaa, au wawaache wajifunze kutokana na yale wanayosikia kutoka kwa watu wengine.
Siri ya Kufanikiwa
Historia inathibitisha kwamba dini inaweza kuchochea chuki na ubaguzi. Hivyo, wazazi wanaweza kuepuka jinsi gani matokeo ambayo yalitajwa na Jonathan Swift? Wanawezaje kuwafundisha watoto wao mambo yanayowasaidia kuwapenda wengine?
Siri inapatikana katika majibu ya maswali haya matatu: (1) Watoto wanapaswa kujifunza nini? (2) Ni nani anayepaswa kuwafundisha? (3) Ni njia gani za kufundisha ambazo zinafaa zaidi?
[Maelezo ya Chini]
a Utafiti huu ulitegemea habari zilizokusanywa kutoka kwa watoto zaidi ya 21,000 wanaoishi Marekani, na pia kutoka kwa wazazi na walimu wao.
-
-
Watoto Wanapaswa Kujifunza Nini?Mnara wa Mlinzi—2011 | Agosti 1
-
-
Watoto Wanapaswa Kujifunza Nini?
“Andiko lote limeongozwa na roho ya Mungu nalo ni lenye faida kwa kufundisha, kwa kukaripia, kwa kunyoosha mambo, kwa kutia nidhamu katika uadilifu.” —2 TIMOTHEO 3:16.
WATOTO wanahitaji kufundishwa ukweli kumhusu Mungu. Wanaweza kujifunza ukweli huo wapi? Katika Biblia, kitabu cha kidini kinachoheshimiwa zaidi ulimwenguni.
Biblia ni kama barua kutoka kwa Mungu. Katika barua hiyo, Mungu amefunua sifa zake na amewatolea watoto wake wote, vijana kwa wazee, mwongozo kuhusu maadili. Ona mafundisho machache tu ya Biblia na mambo ambayo hata watoto wadogo wanaweza kujifunza.
Mungu anataka tujue nini kumhusu?
◼ Biblia inafundisha nini? “Wewe, ambaye jina lako ni Yehova, wewe peke yako ndiye Uliye Juu Zaidi, juu ya dunia yote.”—Zaburi 83:18.
Jambo tunalojifunza: Mungu ni halisi na ana jina la kibinafsi.
◼ Biblia inafundisha nini? “Yehova anaichunguza mioyo yote, naye anatambua kila mwelekeo wa fikira. Ukimtafuta, ataacha umpate.”—1 Mambo ya Nyakati 28:9.
Jambo tunalojifunza: Yehova Mungu anatujali sote, hata watoto wadogo. (Zaburi 10:14; 146:9) Anataka tujifunze kumhusu.
◼ Biblia inafundisha nini? ‘Msimtese mvulana yeyote asiye na baba. Mkimtesa hata kidogo, naye anililie hata kidogo, sitakosa kukisikia kilio chake.’—Kutoka 22:22-24.
Jambo tunalojifunza: Yehova anasikiliza hata sala za watoto wadogo. Tunaweza kuzungumza naye kwa ukawaida na kumweleza mawazo na hisia zetu za moyoni.
◼ Biblia inafundisha nini? “Wakawa wakimjaribu Mungu tena na tena, nao wakamtia uchungu Mtakatifu wa Israeli.”—Zaburi 78:41.
Jambo tunalojifunza: Maneno na matendo yetu yanaweza kumhuzunisha au kumfurahisha Yehova, kwa hiyo, inatupasa kufikiri kabla ya kusema na kutenda.
Tunapaswa kuwatendea jinsi gani watu walio tofauti nasi?
◼ Biblia inafundisha nini? “Mungu hana ubaguzi, bali katika kila taifa mtu ambaye anamwogopa na kutenda uadilifu anakubalika kwake.”—Matendo 10:34, 35.
Jambo tunalojifunza: Ikiwa Mungu anakubali watu wa jamii zote, hatupaswi kuwabagua wengine kwa sababu tu rangi ya ngozi yao au sura yao ni tofauti na yetu.
◼ Biblia inafundisha nini? “Sikuzote [iweni] tayari kujitetea mbele ya kila mtu ambaye hutaka kutoka kwenu sababu ya tumaini lililo ndani yenu, lakini mkifanya hivyo kwa tabia-pole na heshima kubwa.”—1 Petro 3:15.
Jambo tunalojifunza: Tunapozungumzia dini, tunapaswa kueleza maoni yetu kwa uhakika lakini kwa fadhili. Tunapaswa pia kuwaonyesha heshima wale ambao imani yao ni tofauti na yetu.
Tunapaswa kuwatendea jinsi gani watu wa familia?
◼ Biblia inafundisha nini? “Watoto, watiini wazazi wenu katika kila jambo, kwa maana hilo linapendeza vema katika Bwana.”—Wakolosai 3:20.
Jambo tunalojifunza: Watoto wanapowatii wazazi wao wanaonyesha kwamba wanawapenda na wanataka kumfurahisha Mungu.
◼ Biblia inafundisha nini? “Endeleeni kuvumiliana na kusameheana kwa hiari ikiwa yeyote ana sababu ya kulalamika juu ya mwingine. Kama vile Yehova alivyowasamehe ninyi kwa hiari, nanyi fanyeni vivyo hivyo pia.”—Wakolosai 3:13.
Jambo tunalojifunza: Mara kwa mara, watu wengine na hata watu wa familia yetu, watatuvunja moyo. Lakini kama tunataka Mungu atusamehe, tunapaswa kujifunza kuwasamehe wengine.—Mathayo 6:14, 15.
Kwa nini useme ukweli na uwe mwenye fadhili?
◼ Biblia inafundisha nini? ‘Ondoleeni mbali uwongo na mseme kweli kila mmoja wenu na jirani yake.’—Waefeso 4:25.
Jambo tunalojifunza: Tunaposema kweli, tunamwiga Mungu na kumfurahisha. Tukiwa na tabia ya kusema uwongo, tunakuwa kama Ibilisi, adui ya Mungu. Ibilisi ndiye “baba ya uwongo.”—Yohana 8:44; Tito 1:2.
◼ Biblia inafundisha nini? “Watendeeni wengine yale mnayotaka wawatendee ninyi.”—Mathayo 7:12, “Habari Njema kwa Watu Wote.”
Jambo tunalojifunza: Tunapaswa kujali hisia, maoni, na mahitaji ya watu wa familia yetu na wengine katika jamii. Tunapowaonyesha wengine “hisia-mwenzi,” au huruma, yaelekea watatutendea kwa fadhili.—1 Petro 3:8; Luka 6:38.
Kama mifano hiyo inavyoonyesha, mambo ambayo Biblia inafundisha yanaweza kuwasaidia watoto wawe na uthamini, heshima, na huruma watakapokuwa watu wazima. Lakini ni nani anayepaswa kuwafundisha watoto mambo hayo?
-
-
Ni Nani Anayepaswa Kuwafundisha Watoto Kumhusu Mungu?Mnara wa Mlinzi—2011 | Agosti 1
-
-
Ni Nani Anayepaswa Kuwafundisha Watoto Kumhusu Mungu?
“Mwanafunzi hampiti mwalimu wake, lakini kila mtu aliyefundishwa kikamili atakuwa kama mwalimu wake.”—LUKA 6:40.
BAADHI ya wazazi huhisi kwamba hawana uwezo wa kuwafundisha watoto wao kumhusu Mungu. Huenda wakafikiri kwamba hawawezi kuwa walimu wazuri kwa sababu hawana elimu wala ujuzi wa kutosha kuhusu dini. Kwa hiyo, huenda wakamwachia mtu wa ukoo au kiongozi wa dini daraka hilo muhimu.
Ni nani basi , anayefaa zaidi kuwafundisha watoto kweli za kidini na maadili mazuri? Ona yale Biblia inayosema kuhusu jambo hilo, na uyalinganishe na yale ambayo watafiti wamegundua.
Baba Ana Daraka Gani?
Biblia inafundisha nini? “Akina baba, msiwachokoze watoto wenu; bali waleeni katika adabu na maonyo ya Bwana.”—Waefeso 6:4, “Union Version.”
Watafiti wamegundua nini? Akina baba wananufaika jinsi gani wanapositawisha imani yenye nguvu? Makala Fathers’ Religious Involvement and Early Childhood Behavior, iliyochapishwa mwaka wa 2009, ilisema: “Kushirikiana na kikundi fulani cha kidini kunaweza kuwasaidia wanaume kuwa baba wazuri. Dini inaandaa utegemezo na mwelekezo na pia mafundisho na miongozo katika maisha.”
Biblia inaonyesha kwamba baba ana daraka kubwa katika kulea na kufundisha watoto. (Methali 4:1; Wakolosai 3:21; Waebrania 12:9) Lakini shauri hilo linafaa leo? Katika mwaka wa 2009, Chuo Kikuu cha Florida kilichapisha makala iliyozungumzia uvutano ambao akina baba wanakuwa nao juu ya watoto wao. Watafiti hao walitambua kwamba kuna uwezekano mkubwa kwa watoto ambao baba zao walijihusisha sana katika malezi yao kuwa wenye huruma na wenye kujiheshimu. Pia, walitambua kwamba wasichana walikuwa na afya nzuri zaidi ya kiakili, huku wavulana wakiwa wenye adabu zaidi. Bila shaka, shauri la Biblia bado linafaa.
Daraka la Mama Ni Muhimu Kadiri Gani?
Biblia inafundisha nini? “Usiiache sheria ya mama yako.”—Methali 1:8.
Yale ambayo watafiti wamegundua: Katika mwaka wa 2006 kitabu Handbook of Child Psychology kilisema: “Kwa kawaida wakati ambao akina mama wanatumia pamoja na kila mtoto ni kati ya asilimia 65 na 80 zaidi ya ule unaotumiwa na akina baba. Na hali iko hivyo katika nchi nyingi.” Kwa kuwa mama anatumia wakati mwingi hivyo pamoja na mtoto wake, basi maneno, matendo, na mtazamo wake unakuwa na uvutano mkubwa katika ukuzi wa mtoto.
Wazazi wanaposhirikiana kuwafundisha watoto wao ukweli kumhusu Mungu, wanawapa angalau zawadi mbili zenye thamani. Kwanza, watoto wanapata nafasi ya kufanya urafiki pamoja na Baba yao wa mbinguni, urafiki ambao unaweza kuwanufaisha katika maisha yao yote. Pili, kutokana na mfano huo wa wazazi wao, watoto wanajifunza jinsi mume na mke wanavyopaswa kushirikiana ili kufikia malengo muhimu. (Wakolosai 3:18-20) Ingawa huenda wengine wakawasaidia wazazi, wazazi hao ndio wenye daraka la kuwafundisha watoto wao kumhusu Mungu na jinsi anavyotaka familia iwe.
Hivyo basi, wazazi wanapaswa kuwafundisha watoto wao jinsi gani? Ni njia gani za kufundisha ambazo inaelekea zitafaa zaidi?
-
-
Jinsi ya Kuwafundisha Watoto Kumhusu Mungu—Ni Njia Gani Zinazofaa Zaidi?Mnara wa Mlinzi—2011 | Agosti 1
-
-
Jinsi ya Kuwafundisha Watoto Kumhusu Mungu—Ni Njia Gani Zinazofaa Zaidi?
“Maneno haya ninayokuamuru leo lazima yawe moyoni mwako; nawe uyakazie kwa mwana wako na kuyasema unapoketi katika nyumba yako na unapotembea barabarani na unapolala na unapoamka.”—KUMBUKUMBU LA TORATI 6:6, 7.
HUENDA nyakati nyingine wazazi wakahisi wamelewa na daraka la kuwafundisha watoto wao. Hata hivyo, wanapotafuta ushauri kuhusu jambo hilo, huenda wakapata habari nyingi sana zinazofanya wachanganyikiwe. Mara nyingi, watu wa ukoo na marafiki hupenda kutoa mashauri pia. Navyo vitabu, magazeti, na vituo vya Intaneti huwapa mashauri mengi ambayo nyakati nyingine hupingana.
Kwa upande mwingine, Biblia inawapa wazazi mashauri yanayotegemeka kuhusu yale wanayopaswa kuwafundisha watoto wao na pia mwongozo unaofaa kuhusu jinsi ya kuwafundisha. Kama vile mistari ya Biblia iliyonukuliwa juu inavyoonyesha, kila siku wazazi wanahitaji kutafuta njia ya kuzungumza pamoja na watoto wao kumhusu Mungu. Yafuatayo ni madokezo manne tu yanayotegemea Biblia ambayo yamewasaidia maelfu ya wazazi kuwafundisha watoto wao kumhusu Mungu.
1. Unayoweza kuwafundisha kutokana na uumbaji. Mtume Paulo aliandika: “Sifa [za Mungu] ambazo hazionekani, zinaonekana waziwazi tangu kuumbwa kwa ulimwengu na kuendelea, kwa sababu zinaeleweka kwa vitu vilivyofanywa, yaani, nguvu zake za milele na Uungu.” (Waroma 1:20) Wazazi wanaweza kufanya mengi ili kuwasaidia watoto wao waelewe kwamba wanaweza kuwa na uhusiano wa karibu pamoja na Mungu. Wanaweza kufanya hivyo kwa kuhakikisha kwamba watoto wameelewa na kuthamini kazi za Mungu za uumbaji, kisha kuwasaidia kutambua sifa zake ambazo uumbaji huo unafunua.
Yesu alitumia mbinu hiyo alipowafundisha wanafunzi wake. Kwa mfano, alisema: “Waangalieni kwa makini ndege wa mbinguni, kwa sababu hawapandi mbegu au kuvuna au kukusanya ghalani; na bado Baba yenu wa mbinguni huwalisha wao. Je, ninyi si bora kuliko wao?” (Mathayo 6:26) Hapa Yesu alikazia sifa mbili za Yehova—upendo na huruma. Lakini alifanya mengi zaidi. Aliwasaidia wanafunzi wake watambue jinsi Mungu alivyowaonyesha watoto wake sifa hizo.
Mfalme Sulemani mwenye hekima alizungumzia hekima ya kisilika ambayo Mungu aliwapa chungu, kisha Sulemani akatumia viumbe hao wadogo kukazia jambo fulani muhimu. “Mwendee chungu, ewe mvivu,” akaandika, “zitazame njia zake upate kuwa na hekima. Ijapokuwa hana kiongozi, ofisa wala mtawala, yeye hutayarisha chakula chake wakati wa kiangazi; amekusanya akiba ya chakula chake wakati wa mavuno.” (Methali 6:6-8) Hiyo ni njia nzuri kama nini ya kuwafundisha watoto umuhimu wa kujiwekea malengo yanayofaa na kutumia nguvu zinazotoka kwa Mungu ili kuyafikia!
Kwa kufanya mambo yafuatayo, wazazi wanaweza kuiga njia ya kufundisha yenye matokeo mazuri ambayo Yesu na Sulemani walitumia: (1) Kuwauliza watoto wao wanapendezwa na miti na wanyama gani. (2) Kujifunza mengi zaidi kuhusu miti na wanyama hao. (3) Kuwafundisha kumhusu Mungu wakitumia uumbaji huo.
2. Igeni mtazamo wa Yesu kuelekea wale aliowafundisha. Kati ya watu wote ambao wamewahi kuishi duniani, Yesu ndiye aliyesema mambo muhimu zaidi. Hata hivyo, alitumia wakati wake mwingi akiuliza maswali. Alipendezwa sana kujua maoni na hisia za wale aliowafundisha. (Mathayo 17:24, 25; Marko 8:27-29) Vivyo hivyo, wazazi wana mambo mengi sana ya kuwafundisha watoto wao. Ili wawe na matokeo mazuri, wanahitaji kumwiga Yesu na kuwatia moyo waeleze hisia zao waziwazi.
Namna gani ikiwa watoto wana mwelekeo usiofaa au inawachukua muda mrefu kujifunza jambo fulani muhimu? Fikiria jinsi Yesu alivyowafundisha mitume wake. Walibishana vikali mara kwa mara na iliwachukua muda mrefu kujifunza manufaa ya kuwa wanyenyekevu. Hata hivyo, Yesu alikuwa mwenye subira na alizungumza nao tena na tena kuhusu uhitaji wa kuwa wanyenyekevu. (Marko 9:33, 34; Luka 9:46-48; 22:24, 25) Wazazi wanaomwiga Yesu watawarekebisha watoto wao kwa subira na, ikihitajika, watarudia jambo tena na tena mpaka watoto waelewe kikamili umuhimu wake.a
3. Fundisha kwa kuweka mfano mzuri. Wazazi wanahitaji kufuata shauri ambalo mtume Paulo aliwapa Wakristo walioishi Roma. Aliwaandikia hivi: “Je, wewe unayemfundisha mtu mwingine, hujifundishi mwenyewe? Wewe, unayehubiri ‘Usiibe,’ je, wewe huiba?”—Waroma 2:21.
Shauri hilo linafaa kwa sababu watoto wanavutiwa zaidi na matendo ya wazazi wao kuliko maneno yao. Kwa kweli, ikiwa wazazi watatenda kulingana na yale wanayowafundisha watoto wao, inaelekea kwamba watoto hao watayafuata.
4. Anza kumfundisha mtoto akiwa bado mdogo. Timotheo aliyeandamana na mtume Paulo katika safari zake za umishonari alikuwa na sifa nzuri sana katika jamii. (Matendo 16:1, 2) Sababu moja ni kwamba “tangu utoto mchanga” Timotheo alifundishwa “maandishi matakatifu.” Mama na nyanya ya Timotheo walimsomea Maandiko na pia wakamsaidia kuchanganua kweli walizomfundisha kutokana na maandishi hayo.—2 Timotheo 1:5; 3:14, 15.
Unaweza Kupata Msaada Wapi?
Mashahidi wa Yehova wameandaa machapisho kadhaa yanayokusudiwa kuwasaidia wazazi wawafundishe watoto wao ukweli kumhusu Mungu. Mengine yameandikwa ili kuwasaidia watoto wadogo. Nayo mengine yanaweza kuwasaidia wazazi na vijana wao kuwa na mawasiliano mazuri.b
Bila shaka, ili wazazi waweze kuwafundisha watoto wao kumhusu Mungu, wanahitaji kujua majibu ya maswali fulani magumu ambayo watoto huuliza. Kwa mfano, unaweza kujibu jinsi gani maswali yafuatayo: Kwa nini Mungu anaruhusu watu wateseke? Kusudi la Mungu ni nini kuhusu dunia? Wafu wako wapi? Mashahidi wa Yehova watafurahi kukusaidia kupata majibu ya maswali hayo na mengine ili wewe na familia yako mweze kuwa na uhusiano wa karibu pamoja na Mungu.—Yakobo 4:8.
[Maelezo ya Chini]
a Neno la Kiebrania linalotafsiriwa ‘kazia’ katika Kumbukumbu la Torati 6:7 linamaanisha kurudia jambo mara nyingi.
b Ili kuwafundisha watoto wadogo, wazazi wanaweza kutumia kitabu Jifunze Kutoka kwa Mwalimu Mkuu, kinachokazia mafundisho ya Yesu Kristo, au Kitabu Changu cha Hadithi za Biblia, ambacho kinasimulia kwa lugha rahisi mambo muhimu kutoka katika Biblia. Ili kuwafundisha vijana, wazazi wanaweza kutumia kitabu Maswali Ambayo Vijana Huuliza—Majibu Yafanyayo Kazi, Buku la 1 na la 2.
-