-
Je, Kuna Mwasi Nyumbani?Siri ya Furaha ya Familia
-
-
Yaelekea, watoto watakua wawe wenye uthabiti zaidi ikiwa wazazi wao wanawasaidia wakabiliane na matatizo yao ya utineja
14, 15. Wazazi waoneje ukuzi wa mtoto wao?
14 Ingawa wazazi hushangilia wanapoona kijana wao akikua kimwili kutoka utoto hadi utu mzima, huenda wakahisi kusumbuka wakati mtoto wao mbalehe anapoanza kutoka katika hali ya kutegemea wengine hadi hali ya kujitegemea ifaavyo. Katika kipindi hiki cha badiliko, usishangae ikiwa pindi fulani-fulani tineja wako anakuwa kidogo mshupavu au si mwenye ushirikiano. Kumbuka kwamba lengo la wazazi Wakristo linapaswa kuwa kumlea Mkristo mkomavu, aliye thabiti, na mwenye kuchukua madaraka.—Linganisha 1 Wakorintho 13:11; Waefeso 4:13, 14.
15 Hata liwe ni jambo gumu jinsi gani, wazazi wanahitaji kuvunja tabia ya kukataa ombi lolote kutoka kwa mbalehe wao la kutaka kujitegemea zaidi. Mtoto anahitaji kukua awe mtu binafsi, kwa njia bora. Kwa kweli, kuanzia umri mchanga kwa kulinganishwa, matineja fulani huanza kusitawisha mtazamo wa utu mzima sana. Kwa kielelezo, Biblia husema juu ya Mfalme mchanga Yosia: “Naye akali mchanga [wa umri wa miaka 15], alianza kumtafuta Mungu wa Daudi.” Tineja huyu mwenye kutokeza alikuwa kwa wazi mtu mwenye kuchukua madaraka.—2 Mambo ya Nyakati 34:1-3.
-