-
Jinsi Tunavyoweza Kuushinda WogaJifunze Kutoka kwa Mwalimu Mkuu
-
-
Sura Ya 30
Jinsi Tunavyoweza Kuushinda Woga
JE, UNAONA ikiwa rahisi kumtumikia Yehova?— Mwalimu Mkuu hakusema itakuwa rahisi. Usiku kabla ya Yesu kuuawa, aliwaambia mitume wake hivi: ‘Ulimwengu ukiwachukia ninyi, mnajua kwamba huo umenichukia kabla ya kuwachukia.’—Yohana 15:18.
Petro alijigamba kwamba hawezi kamwe kumwacha Yesu, lakini Yesu akasema kwamba Petro angemkana mara tatu usiku huohuo. Na kwa kweli Petro akamkana! (Mathayo 26:31-35, 69-75) Iliwezekanaje hivyo?— Iliwezekana kwa sababu kama wale mitume wengine, Petro pia alishikwa na woga.
Je, unajua ni kwa nini mitume waliogopa?— Walikosa kufanya jambo fulani muhimu. Kujifunza kuhusu jambo hilo kutatusaidia tumtumikie Yehova bila kujali watu watasema nini au kututendea nini. Kwanza, hebu tujikumbushe matukio ya usiku wa mwisho wa Yesu akiwa pamoja na mitume wake.
Kwanza, walisherehekea pamoja Pasaka. Huo ulikuwa mlo wa pekee ulioadhimishwa kila mwaka kuwakumbusha watu wa Mungu kuhusu ukombozi wao kutoka utumwani huko Misri. Kisha Yesu akaanzisha mlo mwingine wa pekee pamoja na mitume. Tutazungumzia mlo huo katika sura nyingine baadaye na tueleze namna mlo huo unavyotusaidia kumkumbuka Yesu. Baada ya mlo huo na baada ya Yesu kuwatia moyo mitume wake, Yesu akawapeleka nje katika bustani ya Gethsemane. Walipenda mahali hapo sana na mara nyingi walienda huko.
Yesu anaenda mbali kidogo peke yake ili asali kwenye bustani. Anawaambia pia Petro, Yakobo, na Yohana wasali. Lakini usingizi unawashika na wanaanza kulala. Mara tatu Yesu anaenda mbali peke yake ili asali, na mara tatu anaporudi anawakuta Petro na wenzake wamelala usingizi! (Mathayo 26:36-47) Unajua ni kwa nini walipaswa kukesha na kusali?— Hebu tuzungumzie jambo hilo.
Mapema jioni hiyo, Yuda Iskariote pamoja na Yesu na mitume wengine walihudhuria sherehe ya Pasaka. Kumbuka kwamba Yuda alikuwa amekuwa mwizi. Na sasa anakuwa msaliti. Anajua mahali ambapo Yesu na mitume wake walizoea kukutana katika bustani ya Gethsemane. Kwa hiyo, Yuda anawapeleka askari huko ili wamkamate Yesu. Wanapofika, Yesu anawauliza: “Mnamtafuta nani?”
Askari wanamjibu: “Yesu.” Yesu anawajibu bila woga: ‘Ndiye mimi.’ Askari wanashangazwa na ujasiri wa Yesu, wanarudi nyuma na kuanguka chini. Kisha Yesu anasema: ‘Ikiwa ni mimi mnayetafuta, acheni mitume wangu waende.’—Yohana 18:1-9.
Askari wanapomkamata Yesu na kumfunga mikono, mitume wanaogopa na kutoroka. Lakini Petro na Yohana wanawafuata kwa umbali ili kujua kitakachotokea. Hatimaye, Yesu anapelekwa kwa Kayafa, kuhani mkuu. Kwa sababu Yohana anajulikana na kuhani mkuu, mtunza-mlango anawaruhusu yeye na Petro waingie ndani ya ua wake.
Makuhani tayari wamekuja nyumbani kwa Kayafa ili kuanzisha kesi. Wanataka Yesu auawe. Basi wanaleta mashahidi ambao wanasema uwongo kumhusu Yesu. Watu wanampiga Yesu ngumi na kumzaba makofi. Petro yuko karibu mambo hayo yanapoendelea.
Msichana mmoja mtumishi, mtunza-mlango aliyewaruhusu Petro na Yohana kuingia, anamtambua. Anamwambia, “Wewe, pia, ulikuwa pamoja na Yesu!” Lakini Petro anakataa kwamba hamjui Yesu. Baadaye kidogo msichana mwingine anamtambua Petro na kuwaambia watu waliokuwa wamesimama karibu nao: “Mtu huyu alikuwa pamoja na Yesu.” Kwa mara nyingine Petro anasema hamjui Yesu. Baadaye tena watu wengine wanamwona Petro na kumwambia: “Hakika wewe pia ni mmoja wao.” Kwa mara ya tatu, Petro anakataa na kusema: “Simjui mtu huyo!” Petro hata anaapa kwamba anasema kweli, na Yesu anageuka na kumtazama.—Mathayo 26:57-75; Luka 22:54-62; Yohana 18:15-27.
Unajua ni kwa nini Petro alisema uwongo?— Ndiyo, kwa sababu aliogopa. Lakini kwa nini aliogopa? Alikosa kufanya nini ili kupata ujasiri? Lifikirie jambo hilo. Yesu alifanya nini ili kupata ujasiri?— Alisali kwa Mungu, naye Mungu akamsaidia kuwa na ujasiri. Kumbuka pia kwamba Yesu alikuwa amemwambia Petro mara tatu asali na kukesha na kuendelea kuwa macho. Lakini ikawaje?—
Kila mara Petro alilala. Hakusali, wala hakuendelea kulinda. Kwa hiyo Yesu alipokamatwa Petro hakutazamia. Baadaye kesi ilipokuwa ikiendelea, Petro aliogopa alipoona Yesu akipigwa na mipango ikifanywa auawe. Lakini muda wa saa chache tu awali, Yesu aliwaambia mitume wake watazamie nini?— Yesu aliwaambia kwamba kama vile ulimwengu ulivyomchukia, ungewachukia wao pia.
Sasa tufikirie jambo ambalo linaweza kutupata ambalo ni sawa na lililompata Petro. Vipi ukiwa darasani na wengine wanaanza kusema mambo mabaya kuhusu watu wasioisalimu bendera au wasiosherehekea Krismasi. Utafanyaje mmoja akikugeukia na kukuuliza: “Je, ni kweli kwamba wewe husalimu bendera?” Au wengine wanaweza kusema: “Tunasikia eti husherehekei Krismasi kamwe!” Je, utaogopa kusema kweli?— Je, utashawishika kudanganya kama Petro?—
Baadaye, Petro alisikitika sana kwamba amemkana Yesu. Alipogundua alilokuwa amefanya, alitoka nje akalia sana. Ndiyo, alirudi kwa Yesu. (Luka 22:32) Hebu fikiria. Ni nini kinachoweza kutusaidia tusiwe na woga sana hivi kwamba tuseme kama Petro?— Kumbuka, Petro alikosa kusali na kuendelea kuwa macho. Basi, unafikiri tunahitaji kufanya nini ili tuwe wafuasi wa Mwalimu Mkuu?—
Bila shaka tunahitaji kusali ili Yehova atusaidie. Yesu aliposali, unajua Mungu alifanya nini?— Alimtuma malaika ili amtie nguvu. (Luka 22:43) Je, malaika wa Mungu wanaweza kutusaidia?— Biblia inasema: “Malaika wa Yehova anapiga kambi pande zote kuwazunguka wanaomwogopa, na yeye huwaokoa.” (Zaburi 34:7) Lakini ili tupate msaada wa Mungu, tunahitaji kufanya zaidi ya kusali tu. Unajua kitu kingine tunachohitaji kufanya?— Yesu aliwaambia wafuasi wake wakeshe na kuendelea kuwa macho. Unafikiri tunaweza kufanyaje hivyo?—
Tunaweza kupata msaada tukisikiliza kwa makini yale yanayosemwa katika mikutano yetu ya Kikristo na kutilia maanani yale tunayosoma katika Biblia. Lakini tunahitaji pia kusali kwa Yehova kwa ukawaida na kumwomba atusaidie tumtumikie. Tukifanya hivyo, tutapata msaada wa kuushinda woga. Kisha tutafurahi tunapokuwa na nafasi ya kuwaambia wengine kumhusu Mwalimu Mkuu na Baba yake.
Maandiko haya yanaweza kutusaidia tusiruhusu kuogopa watu kutuzuie kufanya yaliyo mema: Mithali 29:25; Yeremia 26:12-15, 20-24; na Yohana 12:42, 43.
[Picha katika ukurasa wa 159]
Kwa nini Petro, Yakobo, na Yohana walipaswa kukesha?
[Picha katika ukurasa wa 160]
Kwa nini Petro aliogopa sana hata akadanganya kwamba hamjui Yesu?
[Picha katika ukurasa wa 160]
Unawezaje kujikuta katika hali kama ya Petro?
-
-
Mahali pa Kupata FarajaJifunze Kutoka kwa Mwalimu Mkuu
-
-
Sura Ya 31
Mahali pa Kupata Faraja
JE, KUNA nyakati ambazo unahuzunika na kujihisi mpweke?— Je, kuna wakati unahisi kwamba hakuna mtu anayekupenda?— Watoto wengine hupatwa na hali hiyo. Lakini Mungu anaahidi: “Mimi mwenyewe sitakusahau.” (Isaya 49:15) Je, hilo si jambo la kupendeza?— Ndiyo, kwa kweli Yehova Mungu anatupenda sana!
Mwandikaji mmoja wa Biblia alisema: ‘Hata baba yangu na mama yangu waniache, Yehova mwenyewe angenichukua.’ (Zaburi 27:10) Kujua hivyo kunatupa faraja ya kweli, sivyo?— Ndiyo, Yehova anatuambia: “Usiogope, kwa maana mimi nipo pamoja nawe. . . . Nitakusaidia kwelikweli.”—Isaya 41:10.
Hata hivyo, wakati mwingine Yehova humruhusu Shetani atuletee magumu. Yehova hata humruhusu Shetani awajaribu watumishi Wake. Wakati mmoja Ibilisi alimfanya Yesu ateseke sana mpaka akalia kwa sauti kubwa hivi kwa Yehova: “Mungu wangu, Mungu wangu, kwa nini umeniacha?” (Mathayo 27:46) Ijapokuwa Yesu aliteseka, bado alijua kwamba Yehova anampenda. (Yohana 10:17) Lakini Yesu alijua pia kwamba Mungu humruhusu Shetani awajaribu watumishi Wake na kuwatesa. Katika sura nyingine tutaeleza sababu ya Mungu kumruhusu Shetani afanye hivyo.
Tunapokuwa wachanga, inakuwa rahisi kuogopa wakati mwingine. Kwa mfano, umewahi kupotea?— Je, uliogopa?— Watoto wengi huogopa. Wakati mmoja Mwalimu Mkuu alizungumza kuhusu kupotea. Lakini aliyepotea hakuwa mtoto. Alikuwa kondoo.
Katika njia fulani wewe ni kama kondoo. Inawezekanaje hivyo? Kondoo ni wadogo na hawana nguvu sana. Nao wanahitaji mtu wa kuwatunza na kuwalinda. Mtu anayechunga kondoo anaitwa mchungaji.
Katika hadithi yake, Yesu alizungumzia mchungaji aliyekuwa na kondoo mia moja. Lakini mmoja wao akapotea. Labda kondoo huyo alitaka kuona ni nini kilichokuwa upande ule mwingine wa mlima. Baada ya muda mfupi tu, kondoo huyo akaenda mbali sana na wengine. Unaweza kuwazia jinsi kondoo huyo alivyohisi alipoangalia huku na huku na kushtuka kwamba yuko peke yake?—
Mchungaji angefanya nini akigundua kwamba kondoo huyo amepotea? Je, angesema potelea mbali na asihangaike kumtafuta? Au angewaacha wale kondoo 99 mahali salama na kwenda kumtafuta yule mmoja tu? Je, kondoo mmoja tu anastahili kutafutwa kwa bidii hivyo?— Kama ungalikuwa huyo kondoo aliyepotea, je, hungalipenda mchungaji akutafute?—
Mchungaji aliwapenda kondoo wake wote, hata yule aliyepotea. Basi akaenda kumtafuta. Hebu fikiria jinsi kondoo huyo alivyofurahi alipomwona mchungaji akija! Na Yesu alisema kwamba mchungaji alifurahi kumpata kondoo wake. Alimfurahia sana kuliko wale 99 ambao hawakuwa wamepotea. Basi, ni nani aliye kama yule mchungaji katika hadithi ya Yesu? Ni nani anayetujali sana kama vile yule mchungaji alivyomjali kondoo wake?— Yesu alisema kwamba ni Baba yake wa mbinguni. Na Baba yake ni Yehova.
Yehova Mungu ndiye Mchungaji Mkuu wa watu wake. Anawapenda wote wanaomtumikia, kutia ndani wachanga kama wewe. Yeye hataki yeyote kati yetu aumie. Kwa hakika inafariji kujua kwamba Mungu anatujali sana hivyo!—Mathayo 18:12-14.
Je, kweli wewe unamwamini Yehova Mungu?— Je, unamwona kama mtu halisi?— Ni kweli kwamba hatuwezi kumwona Yehova. Hii ni kwa sababu yeye ni Roho. Ana mwili ambao hatuwezi kuuona kwa macho yetu. Lakini yeye ni halisi, na anaweza kutuona. Anajua wakati tunapohitaji msaada. Na tunaweza kuzungumza naye katika sala, kama vile tu tunavyoweza kuzungumza na mtu mwingine duniani. Yehova anataka tuzungumze naye katika sala.
Kwa hiyo ukihisi huzuni au upweke, unapaswa kufanya nini?— Zungumza na Yehova. Mkaribie, naye atakufariji na kukusaidia. Kumbuka kwamba Yehova anakupenda, hata wakati unapohisi upweke. Hebu tuchukue Biblia yetu. Tunaambiwa hivi katika Zaburi 23 kuanzia mstari wa 1: “Yehova ni Mchungaji wangu. Sitakosa chochote. Ananilaza katika malisho yenye majani mengi; ananiongoza kando ya mahali pa kupumzika palipo na maji ya kutosha.”
Ona kile mwandikaji anaongezea kutaja katika mstari wa 4: “Hata ingawa ninatembea katika bonde lenye kivuli kizito, siogopi chochote kibaya, kwa maana wewe uko pamoja nami; fimbo yako na gongo lako ndivyo vitu vinavyonifariji.” Hivyo ndivyo watu wanavyohisi iwapo Mungu wao ni Yehova. Wanapata faraja wakati wa taabu. Je, hivyo ndivyo unavyohisi?—
Kama vile mchungaji mwenye upendo anavyowatunza kondoo wake, ndivyo Yehova anavyowatunza watu wake sana. Anawaonyesha njia iliyo bora, nao wanafurahi kuifuata. Hata wanapokuwa na matatizo mengi, hawahitaji kuogopa. Mchungaji hutumia fimbo kuwalinda kondoo kutokana na wanyama ambao wanaweza kuwaumiza. Biblia inasimulia jinsi kijana mchungaji Daudi alivyowalinda kondoo wake dhidi ya simba na dubu. (1 Samweli 17:34-36) Na watu wa Mungu wanajua kwamba Yehova atawalinda pia. Wanaweza kujihisi wakiwa salama kwa sababu Mungu yuko pamoja nao.
Kwa kweli Yehova anawapenda kondoo wake, naye anawatunza kwa fadhili. Biblia inasema: ‘Atawachunga kondoo wake mwenyewe kama mchungaji. Atawakusanya pamoja wana-kondoo kwa mkono wake.’—Isaya 40:11.
Je, hufurahi kujua kwamba hivyo ndivyo Yehova alivyo?— Ungependa kuwa kondoo wake?— Kondoo wanasikiliza sauti ya mchungaji wao. Wanakaa karibu naye. Je, wewe unamsikiliza Yehova?— Je, unakaa karibu naye?— Basi huhitaji kuogopa kamwe. Yehova atakuwa pamoja nawe.
Kwa upendo Yehova anawatunza wale wanaomtumikia. Tusome pamoja yale ambayo Biblia inasema kuhusu jambo hili katika Zaburi 37:25; 55:22; na Luka 12:29-31.
[Picha katika ukurasa wa 163]
Unafikiri huyu mwana-kondoo aliyepotea anahisije?
[Picha katika ukurasa wa 164]
Ni nani aliye kama mchungaji anayeokoa kondoo wake?
[Picha katika ukurasa wa 165]
Je, unamwona Yehova akiwa halisi kama unavyomwona baba yako au mtu mwingine?
[Picha katika ukurasa wa 166]
Tunapokuwa na matatizo, ni nani anayeweza kutusaidia kama mchungaji anayelinda kondoo wake?
-