-
‘Chagua Uzima Ili Uendelee Kuwa Hai’Mnara wa Mlinzi—2006 | Juni 1
-
-
Waisraeli Walikuwa na Uhuru wa Kuchagua
3. Ni amri gani iliyo ya kwanza kati ya zile Amri Kumi, na Waisraeli waaminifu walitii amri hiyo jinsi gani?
3 Yehova aliwaambia Waisraeli hivi: “Mimi ni Yehova Mungu wako, niliyekutoa katika nchi ya Misri, kutoka katika nyumba ya watumwa.” (Kumbukumbu la Torati 5:6) Katika mwaka wa 1513 K.W.K., taifa la Israeli lilikombolewa kimuujiza kutoka utekwani huko Misri, na hivyo lilipaswa kuamini kabisa maneno hayo. Katika amri ya kwanza kati ya zile Amri Kumi, Yehova alitangaza hivi kupitia Musa msemaji wake: “Usiwe na miungu mingine yoyote dhidi ya uso wangu.” (Kutoka 20:1, 3) Wakati huo, taifa la Israeli lilichagua kutii. Kwa hiari, walijitoa kikamili kwa Yehova.—Kutoka 20:5; Hesabu 25:11.
4. (a) Musa aliwaambia Waisraeli nini kuhusu uchaguzi waliopaswa kufanya? (b) Tunaweza kuchagua nini leo?
4 Miaka 40 hivi baadaye, Musa aliwakumbusha Waisraeli wa kizazi kingine kuhusu uchaguzi waliopaswa kufanya. Alitangaza hivi: “Nachukua mbingu na dunia kuwa mashahidi juu yenu leo, kwamba nimeweka uzima na kifo mbele yako, baraka na laana; nawe lazima uchague uzima ili uendelee kuwa hai, wewe na uzao wako.” (Kumbukumbu la Torati 30:19) Leo, hata sisi tunaweza kuchagua. Naam, tunaweza kuchagua kumtumikia Yehova kwa uaminifu na kupata uzima wa milele, au tunaweza kuchagua kumwasi na kupata matokeo mabaya. Ona mifano miwili ya watu waliofanya uchaguzi uliotofautiana.
-
-
‘Chagua Uzima Ili Uendelee Kuwa Hai’Mnara wa Mlinzi—2006 | Juni 1
-
-
Kufanya Uchaguzi Unaofaa
8. Kulingana na Kumbukumbu la Torati 30:20, ni mambo gani yanayohusika katika kufanya uchaguzi unaofaa?
8 Musa alipowahimiza Waisraeli wachague uzima, alitaja hatua tatu ambazo walipaswa kuchukua: “Kwa kumpenda Yehova Mungu wako, kwa kuisikiliza sauti yake na kwa kushikamana naye.” (Kumbukumbu la Torati 30:20) Acheni tuchunguze kila moja ya hatua hizo ili tufanye uchaguzi unaofaa.
9. Tunaweza kuonyeshaje kwamba tunampenda Yehova?
9 Kwa kumpenda Yehova Mungu wetu: Sisi huchagua kumtumikia Yehova kwa sababu tunampenda. Kwa kutii vielelezo vyenye kuonya vya siku za Waisraeli, sisi hupinga vishawishi vyote vya kujihusisha katika ukosefu wa adili na kuepuka kuishi kwa njia itakayotufanya tunaswe na mtego wa ulimwengu wa kufuatia mali. (1 Wakorintho 10:11; 1 Timotheo 6:6-10) Sisi hushikamana na Yehova na kushika masharti yake. (Yoshua 23:8; Zaburi 119:5, 8) Kabla ya Waisraeli kuingia Nchi ya Ahadi, Musa aliwahimiza hivi: “Tazama! nimewafundisha masharti na maamuzi ya hukumu, kama vile ambavyo Yehova Mungu wangu ameniamuru mimi, ili ninyi mfanye hivyo katikati ya nchi ambayo mnaenda kuimiliki. Nanyi mtazishika na kuzifanya, kwa sababu hiyo ni hekima kwenu na uelewaji kwenu mbele ya macho ya vikundi vya watu watakaosikia juu ya masharti yote haya.” (Kumbukumbu la Torati 4:5, 6) Sasa ndio wakati wa kuonyesha kwamba tunampenda Yehova kwa kutanguliza mapenzi yake maishani mwetu. Tutabarikiwa sana tukichagua kufanya hivyo.—Mathayo 6:33.
10-12. Tunajifunza nini kwa kuchunguza mambo yaliyotukia siku za Noa?
10 Kwa kuisikiliza sauti ya Mungu: Noa alikuwa “mhubiri wa uadilifu.” (2 Petro 2:5) Karibu watu wote walioishi kabla ya Gharika walikengeushwa na “hawakujali” maonyo ya Noa. Matokeo? “Gharika ikaja na kuwafagilia mbali wote.” Yesu alionya kwamba siku zetu, wakati wa “kuwapo kwa Mwana wa binadamu,” zingefanana na wakati huo. Mambo yaliyotukia siku za Noa ni onyo kali kwa watu wanaochagua kupuuza ujumbe wa Mungu.—Mathayo 24:39.
11 Wale wanaodhihaki maonyo ya Mungu ambayo yanatolewa na watumishi wake wa leo wanapaswa kutambua matokeo ya kupuuza maonyo hayo. Mtume Petro alisema hivi kuhusu wadhihaki hao: “Kulingana na kupenda kwao, wao hawalioni jambo hili, kwamba mbingu zilikuwapo tangu zamani za kale na dunia ikisimama imara kutoka katika maji na katikati ya maji kwa neno la Mungu; na kwa njia hizo ulimwengu wa wakati huo uliangamia kwa gharika ya maji. Lakini kwa neno hilohilo mbingu na dunia za sasa zimewekwa akiba kwa ajili ya moto nazo zinahifadhiwa mpaka ile siku ya hukumu na ya kuangamizwa kwa watu wasiomwogopa Mungu.”—2 Petro 3:3-7.
12 Hebu ona tofauti kati ya uchaguzi wa watu hao na uchaguzi wa Noa na familia yake. “Kwa imani Noa, baada ya kupewa onyo la kimungu la mambo ambayo yalikuwa bado hayajaonekana, alionyesha woga wa kimungu na kujenga safina.” Kwa kuwa Noa alitii onyo hilo, familia yake iliokolewa. (Waebrania 11:7) Acheni tuwe wepesi kusikia ujumbe wa Mungu na kutii.—Yakobo 1:19, 22-25.
13, 14. (a) Kwa nini ni muhimu ‘kushikamana na Yehova’? (b) Tunapaswa kufanya nini ili kumruhusu Yehova, “Mfinyanzi wetu,” atufinyange?
13 Kwa kushikamana na Yehova: Ili ‘tuchague uzima na kuendelea kuwa hai,’ hatupaswi tu kumpenda Yehova na kumsikiliza bali tunapaswa pia “kushikamana naye,” yaani, kuendelea kufanya mapenzi yake. Yesu alisema hivi: “Nanyi kwa kuvumilia mtajipatia nafsi zenu.” (Luka 21:19) Uchaguzi wetu kuhusu jambo hilo huonyesha yaliyo moyoni mwetu. Andiko la Methali 28:14 linasema: “Mwenye furaha ni mtu anayehofu sikuzote, lakini yeye anayeufanya moyo wake kuwa mgumu ataanguka katika msiba.” Farao wa Misri ya kale ni mfano wa mtu aliyefanya moyo wake kuwa mgumu. Wakati yale Mapigo Kumi yalipoletwa juu ya Misri, Farao alifanya moyo wake kuwa mgumu badala ya kumwogopa Mungu. Yehova hakumlazimisha Farao asitii, lakini alimwacha mtawala huyo mwenye kiburi afanye uchaguzi. Kama vile mtume Paulo anavyoeleza maoni ya Yehova kuhusu Farao, mapenzi ya Yehova yalitimia: “Kwa sababu hii nimekuacha ubaki, ili kuhusiana na wewe nionyeshe nguvu zangu, na ili jina langu litangazwe katika dunia yote.”—Waroma 9:17.
14 Karne nyingi baada ya Waisraeli kukombolewa kutoka kwa Farao, nabii Isaya alitangaza hivi: “Ee Yehova, wewe ni Baba yetu. Sisi ni udongo, nawe ni Mfinyanzi wetu; nasi sote ni kazi ya mkono wako.” (Isaya 64:8) Tunapomruhusu Yehova atufinyange kupitia funzo la kibinafsi na kutii Neno lake, sisi hujivika utu mpya pole kwa pole. Tunakuwa wapole zaidi na tunakubali kufinyangwa, na hivyo inakuwa rahisi kwetu kushikamana kabisa na Yehova kwa sababu tunataka sana kumpendeza.—Waefeso 4:23, 24; Wakolosai 3:8-10.
-