Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Baraka au Laana—Kuna Chaguo!
    Mnara wa Mlinzi—1996 | Juni 15
    • Baraka au Laana—Kuna Chaguo!

      “Nimekuwekea mbele yako uzima na mauti, baraka na laana; basi chagua uzima, ili uwe hai.”—KUMBUKUMBU LA TORATI 30:19.

      1. Ni uwezo gani waliopewa wanadamu?

      YEHOVA MUNGU alikusudia sisi—viumbe vyake vya kibinadamu vyenye akili—tuwe wajumbe wenye hiari ya kuchagua. Sisi hatukuumbwa tuwe mashine tu, au roboti, bali tulipewa pendeleo na daraka la kufanya machaguo. (Zaburi 100:3) Wanadamu wa kwanza—Adamu na Hawa—walikuwa huru kuchagua mwendo wao, nao walipaswa kumtolea Mungu hesabu kwa ajili ya chaguo lao.

      2. Adamu alifanya chaguo gani, na tokeo likawa nini?

      2 Muumba ameandaa kwa wingi ili uhai wa kibinadamu uwe wenye baraka za daima kwenye dunia iliyo paradiso. Kwa nini kusudi hilo halijatimizwa bado? Kwa sababu Adamu alifanya chaguo baya. Yehova alikuwa amemwamuru huyo mwanadamu hivi: “Matunda ya kila mti wa bustani waweza kula, walakini matunda ya mti wa ujuzi wa mema na mabaya usile, kwa maana siku utakapokula matunda ya mti huo utakufa hakika.” (Mwanzo 2:16, 17) Ikiwa Adamu angalichagua kutii, wazazi wetu wa kwanza wangalibarikiwa. Kutokutii kulileta kifo. (Mwanzo 3:6, 18, 19) Kwa hiyo dhambi na kifo zimepitishwa kwa wazao wote wa Adamu.—Warumi 5:12.

      Baraka Zafanywa Ziwezekane

      3. Mungu aliandaaje uhakikishio kwamba kusudi lake kwa ajili ya wanadamu lingetimizwa?

      3 Yehova Mungu alifanyiza njia ambayo kwayo kusudi lake la kubariki wanadamu lingetimizwa hatimaye. Yeye mwenyewe alitabiri kuhusu Mbegu, akitoa unabii hivi katika Edeni: “Nami nitaweka uadui kati yako na huyo mwanamke, na kati ya uzao wako na uzao wake [“mbegu yako na mbegu yake,” NW]; huo utakuponda kichwa, na wewe utamponda kisigino.” (Mwanzo 3:15) Baadaye Mungu aliahidi kwamba baraka zingewajia wanadamu watiifu kupitia Mbegu hiyo, mzao wa Abrahamu.—Mwanzo 22:15-18.

      4. Yehova amefanya mpango gani kwa ajili ya kubariki wanadamu?

      4 Mbegu hiyo ya baraka iliyoahidiwa ilithibitika kuwa Yesu Kristo. Kuhusu fungu la Yesu katika mpango wa Yehova wa kubariki wanadamu, mtume Mkristo, Paulo, aliandika hivi: “Mungu aonyesha pendo lake yeye mwenyewe kwetu sisi, kwa kuwa Kristo alikufa kwa ajili yetu, tulipokuwa tungali wenye dhambi.” (Warumi 5:8) Baraka zitafurahiwa na wale kati ya wanadamu wenye dhambi wanaomtii Mungu na kujinufaisha wenyewe na fadhili za dhabihu ya fidia ya Yesu Kristo. (Matendo 4:12) Je, utachagua utii na baraka? Kutokutii kutakuwa na matokeo yaliyo tofauti kabisa.

      Namna Gani Laana?

      5. Maana ya neno “laana” ni nini?

      5 Kinyume cha baraka ni laana. Neno “laana” lamaanisha kusema vibaya juu ya mtu fulani au kutamka maovu dhidi yake. Neno la Kiebrania qela·lahʹ linatokana na kitenzi cha msingi qa·lalʹ, linalomaanisha kihalisi “kuwa mwepesi.” Hata hivyo, litumiwapo kwa njia ya kitamathali, lamaanisha ‘kulaani’ au ‘kudharau.’—Mambo ya Walawi 20:9; 2 Samweli 19:43.

      6. Ni jambo gani lenye kuhusisha Elisha lililotukia karibu na Betheli la kale?

      6 Chunguza kielelezo chenye kusisimua cha hatua ya upesi iliyohusisha laana. Hiyo ilitukia wakati Elisha nabii wa Mungu alipokuwa akitembea kutoka Yeriko hadi Betheli. Simulizi lataarifu hivi: “Alipokuwa akienda njiani, wakatoka vijana katika mji, wakamfanyizia mzaha, wakamwambia, Paa wewe mwenye upaa! Paa wewe mwenye upaa! Akatazama nyuma akawaona, akawalaani kwa jina la BWANA. Wakatoka dubu wawili wa kike mwituni, wakawararua vijana arobaini na wawili miongoni mwao.” (2 Wafalme 2:23, 24) Maneno hasa ambayo Elisha alitumia alipowalaani wale watoto wenye kufanyiza mzaha hayafunuliwi. Hata hivyo, tamko hilo la maneno lilikuwa na matokeo kwa sababu lilisemwa kwa jina la Yehova na nabii wa Mungu aliyekuwa akitenda kupatana na mapenzi ya kimungu.

      7. Ni nini kilichowapata wale watoto waliomfanyizia Elisha mzaha, na kwa nini?

      7 Jambo linaloonekana kuwa sababu ya huko kufanyiza mzaha ni kwamba Elisha alikuwa amevaa vazi rasmi la Eliya lililojulikana, na hao watoto hawakutaka mwandamizi yeyote wa nabii huyo awe mahali hapo. (2 Wafalme 2:13) Ili kushindana na upinzani wa kuwa kwake mwandamizi wa Eliya na ili kufundisha vijana hao na wazazi wao staha ifaayo kwa nabii wa Yehova, Elisha alilaani kwa jina la Mungu wa Eliya, kundi hilo lenye kufanyiza mzaha. Yehova alidhihirisha kukubali kwake Elisha kuwa nabii wake kwa kusababisha wale dubu wawili wa kike watoke mwituni na kuwararua vipande-vipande vijana 42 wa wale wenye kudhihaki. Yehova alishughulika kwa njia ya mkataa kwa sababu ya ukosefu wao mbaya sana wa staha kuelekea njia ya uwasiliano aliyokuwa akitumia duniani wakati huo.

      8. Watu wa Israeli walikubali kufanya nini, na wakawa na mataraja yapi?

      8 Miaka kadhaa mapema, Waisraeli walionyesha ukosefu uo huo wa staha kuelekea mipango ya Mungu. Hivi ndivyo ulivyodhihirika: Katika 1513 K.W.K., Yehova alionyesha watu wa Israeli upendeleo kwa kuwakomboa kutoka katika utumwa wa Kimisri kana kwamba “juu ya mbawa za tai.” Muda mfupi baadaye, waliahidi kumtii Mungu. Ona jinsi utii ulivyofungamanishwa sikuzote na kupokea kibali cha Mungu. Yehova alisema hivi kupitia Musa: “Ikiwa mtaitii sauti yangu kweli kweli, na kulishika agano langu, hapo ndipo mtakapokuwa tunu kwangu kuliko makabila yote ya watu; maana dunia yote pia ni mali yangu.” Baadaye, watu wakaitikia kwa kukubali, wakisema: “Hayo yote aliyoyasema BWANA tutayatenda.” (Kutoka 19:4, 5, 8; 24:3) Waisraeli walidai kumpenda Yehova, walijiweka wakfu kwake, wakaapa kutii sauti yake. Kufanya hivyo kungetokeza baraka kubwa.

      9, 10. Musa alipokuwa juu ya Mlima Sinai, Waisraeli walifanya nini, na matokeo yakawa nini?

      9 Lakini, kabla ya kanuni za msingi za mwafaka huo kuchongwa katika jiwe kwa “chanda cha Mungu,” laana za kimungu zikawa za lazima. (Kutoka 31:18) Kwa nini matokeo hayo yenye kuhuzunisha yalistahili? Je, Waisraeli hawakuwa wameonyesha tamaa ya kufanya yote ambayo Yehova alikuwa amesema? Ndiyo, kwa maneno walitaka baraka, lakini kwa vitendo vyao walichagua mwendo uliostahili laana.

      10 Katika kipindi cha siku 40 Musa alipokuwa juu ya Mlima Sinai akipokea zile Amri Kumi, Waisraeli walivunja ahadi yao ya mapema ya uaminifu-mshikamanifu kwa Yehova. “Hata,” simulizi lasema, “watu walipoona ya kuwa Musa amekawia kushuka katika mlima, wakakusanyana wakamwendea Haruni, wakamwambia, Haya! katufanyizie miungu itakayokwenda mbele yetu, kwa maana Musa huyo aliyetutoa katika nchi ya Misri hatujui yaliyompata.” (Kutoka 32:1) Hiki ni kielelezo kingine cha mtazamo usio wenye staha kuelekea binadamu ambaye Yehova alikuwa akitumia wakati huo ili kuwaongoza na kuwaelekeza watu wake. Waisraeli walivutwa kuiga ibada ya sanamu ya Kimisri wakavuna matokeo mabaya wakati watu wapatao 3,000 kati yao walipouawa kwa upanga katika siku moja.—Kutoka 32:2-6, 25-29.

      Tamko la Baraka na Laana

      11. Ni maagizo gani kuhusu baraka na laana yaliyotekelezwa na Yoshua?

      11 Karibu na mwisho wa safari ya Israeli ya miaka 40 nyikani, Musa alitaja baraka moja-moja ambazo zingevunwa kwa kuchagua mwendo wa utii kwa Mungu. Pia alitaja laana moja-moja ambazo Waisraeli wangejionea ikiwa wangechagua kutomtii Yehova. (Kumbukumbu la Torati 27:11–28:10) Muda mfupi baada ya Israeli kuingia Bara Lililoahidiwa, Yoshua alitekeleza maagizo ya Musa yaliyohusisha baraka na laana hizo. Makabila sita ya Israeli yalisimama chini ya Mlima Ebali, na yale mengine sita yalisimama mbele ya Mlima Gerizimu. Walawi walisimama katika lile bonde katikati. Yaonekana yale makabila yaliyokuwa mbele ya Mlima Ebali yalisema “Amina!” kwa laana, zilizosomwa kuelekea upande huo. Wengine waliziitikia baraka ambazo Walawi walisoma kuelekea upande wao wakiwa chini ya Mlima Gerizimu.—Yoshua 8:30-35.

      12. Ni baadhi ya laana gani zilizotamkwa na Walawi?

      12 Ebu wazia kwamba unasikia Walawi wakisema: “Na alaaniwe mtu afanyaye sanamu ya kuchonga, au ya kusubu, machukizo kwa BWANA, kazi ya mikono ya fundi, akaisimamisha kwa siri. . . . Na alaaniwe amdharauye baba yake au mama yake. . . . Na alaaniwe aondoaye mpaka wa jirani yake. . . . Na alaaniwe ampotezaye kipofu akakosa njia. . . . Na alaaniwe apotoaye hukumu ya mgeni, na yatima, na mjane aliyefiliwa na mumewe. . . . Na alaaniwe alalaye na mke wa baba yake, kwa kuwa amefunua mavazi ya babaye. . . . Na alaaniwe alalaye na mnyama wa aina yoyote. . . . Na alaaniwe alalaye na umbu lake, binti ya babaye, au binti ya mamaye. . . . Na alaaniwe alalaye na mkwewe, mamaye mkewe. . . . Na alaaniwe ampigaye mwenzake kwa siri. . . . Na alaaniwe atwaaye ujira wa kumwua asiye makosa. . . . Na alaaniwe asiyeyaweka imara maneno ya torati hii kwa kuyafanya.” Baada ya kila laana, makabila yaliyo mbele ya Mlima Ebali yasema, “Amina!”—Kumbukumbu la Torati 27:15-26.

      13. Kwa maneno yako mwenyewe, ungeelezaje baraka fulani ambazo Walawi walitamka?

      13 Sasa ebu wazia kwamba wasikia wale walio mbele ya Mlima Gerizimu wakiitikia kwa sauti kila baraka huku Walawi wakipaaza sauti hivi: “Utabarikiwa mjini, utabarikiwa na mashambani. Utabarikiwa uzao wa tumbo lako, na uzao wa nchi yako, na uzao wa wanyama wako wa mifugo, maongeo ya ng’ombe wako, na wadogo wa kondoo zako. Litabarikiwa kapu lako, na chombo chako cha kukandia unga. Utabarikiwa uingiapo, utabarikiwa na utokapo.”—Kumbukumbu la Torati 28:3-6.

      14. Waisraeli wangepokea baraka kwa msingi upi?

      14 Msingi wa kupokea baraka hizi ulikuwa nini? Simulizi lasema hivi: “Itakuwa utakaposikia sauti ya BWANA, Mungu wako, kwa bidii, kutunza kuyafanya maagizo yake yote nikuagizayo leo, ndipo BWANA, Mungu wako, atakapokutukuza juu ya mataifa yote ya duniani; na baraka hizi zote zitakujilia na kukupata usikiapo sauti ya BWANA, Mungu wako.” (Kumbukumbu la Torati 28:1, 2) Ndiyo, ufunguo wa kufurahia baraka za kimungu ulikuwa utii kwa Mungu. Lakini namna gani sisi leo? Je, sisi mmoja-mmoja tutachagua baraka na uhai kwa kuendelea ‘kusikiliza sauti ya Yehova’?—Kumbukumbu la Torati 30:19, 20, NW.

      Kuchunguza kwa Ukaribu Zaidi

      15. Ni jambo gani lililoonyeshwa katika baraka iliyorekodiwa kwenye Kumbukumbu la Torati 28:3, na twaweza kunufaikaje nalo?

      15 Acheni tufikirie baraka fulani ambazo Mwisraeli angeweza kufurahia kwa kumtii Yehova. Kwa kielelezo, Kumbukumbu la Torati 28:3 yasema: “Utabarikiwa mjini, utabarikiwa na mashambani.” Kubarikiwa na Mungu hakutegemei mahali wala mgawo. Huenda watu fulani wakahisi wamezuiwa katika hali zao, labda kwa sababu wanaishi katika eneo lililokumbwa na uharibifu wa mali za kimwili au katika nchi iliyogawanywa na vita. Huenda wengine wakatamani sana kumtumikia Yehova wakiwa kwingineko. Huenda wanaume fulani Wakristo wakavunjika moyo kwa sababu hawajawekwa rasmi kuwa watumishi wa huduma au kuwa wazee kutanikoni. Nyakati nyingine, wanawake Wakristo huhisi kufa moyo kwa sababu hawawezi kushiriki katika huduma ya wakati wote wakiwa mapainia au wamishonari. Hata hivyo, kila mtu ambaye ‘asikiliza sauti ya Yehova na kufanya kwa uangalifu yote anayotaka’ (NW) atabarikiwa sasa na kwa umilele wote.

      16. Kanuni ya Kumbukumbu la Torati 28:4 inaonwaje na tengenezo la Yehova leo?

      16 Kumbukumbu la Torati 28:4 yasema: “Utabarikiwa uzao wa tumbo lako, na uzao wa nchi yako, na uzao wa wanyama wako wa mifugo, maongeo ya ng’ombe wako, na wadogo wa kondoo zako.” Matumizi ya kiwakilishi cha Kiebrania katika hali ya umoja kinachofasiriwa ‘-ako’ huonyesha kwamba hilo lingekuwa ono la kibinafsi la Mwisraeli mtiifu. Namna gani watumishi watiifu wa Yehova leo? Ongezeko na upanuzi wa ulimwenguni pote unaoendelea katika tengenezo la Mashahidi wa Yehova unatokana na baraka ya Mungu juu ya jitihada zenye bidii za wapiga-mbiu zaidi ya 5,000,000 wa habari njema za Ufalme. (Marko 13:10) Na uwezekano wa kuwa na ongezeko kubwa zaidi ni wazi kwa sababu watu zaidi ya 13,000,000 walihudhuria mwadhimisho wa Mlo wa Jioni wa Bwana wa 1995. Je, wewe unafurahia baraka za Ufalme?

      Chaguo la Israeli Lilileta Matokeo Tofauti

      17. ‘Kupatwa’ na baraka au laana kulitegemea nini?

      17 Kwa kweli, baraka zingemfuatia Mwisraeli mtiifu. Iliahidiwa hivi: “Baraka hizi zote zitakujilia na kukupata.” (Kumbukumbu la Torati 28:2) Vivyo hivyo, ilisemwa hivi juu ya laana: “Ndipo zitakapokujia laana hizi zote na kukupata.” (Kumbukumbu la Torati 28:15) Ikiwa ungalikuwa Mwisraeli wa nyakati za kale, je, ‘ungalipatwa’ na baraka au na laana? Hilo lingalitegemea kama ulimtii Mungu au ulikosa kumtii.

      18. Waisraeli wangaliweza kuepukaje laana?

      18 Kwenye Kumbukumbu la Torati 28:15-68, matokeo yenye maumivu ya kutokutii yanaonyeshwa yakiwa laana. Baadhi yayo ni kinyume kabisa cha baraka za utii zinazotajwa moja-moja kwenye Kumbukumbu la Torati 28:3-14. Mara nyingi, watu wa Israeli walivuna matokeo mabaya sana ya laana kwa sababu walichagua kushiriki katika ibada isiyo ya kweli. (Ezra 9:7; Yeremia 6:6-8; 44:2-6) Hilo lilihuzunisha kama nini! Matokeo hayo yangaliweza kuepukwa kwa kufanya chaguo lililofaa, la kutii sheria na kanuni za Yehova zenye kufaa, zinazofasili kwa wazi yaliyo mema na yaliyo mabaya. Watu wengi leo hupatwa na maumivu na msiba kwa sababu wamechagua kutenda kinyume cha kanuni za Biblia kwa kuzoea dini isiyo ya kweli, kushiriki katika ukosefu wa adili katika ngono, kwa kutumia madawa haramu, kwa kutumia kupita kiasi vinywaji vya alkoholi, na mambo kama hayo. Kama vile katika Israeli na Yuda ya kale, kufanya machaguo hayo mabaya hutokeza hali ya kutokubaliwa kimungu na maumivu ya moyoni yasiyo ya lazima.—Isaya 65:12-14.

      19. Fafanua hali zilizofurahiwa wakati Yuda na Israeli yalipochagua kumtii Yehova.

      19 Baraka zilikuwa nyingi na utulivu ulienea wakati tu ambapo Israeli walimtii Yehova. Kwa kielelezo, kuhusu siku za Mfalme Sulemani, twasoma hivi: “Yuda na Israeli walikuwa wengi kama mchanga wa pwani kwa wingi, wakila, na kunywa, na kufurahi. . . . Yuda na Israeli wakakaa salama, kila mtu chini ya mzabibu wake na chini ya mtini wake, tokea Dani mpaka Beer-sheba, siku zote za Sulemani.” (1 Wafalme 4:20-25) Hata wakati wa Mfalme Daudi, uliokuwa wenye upinzani mwingi kutoka kwa maadui wa Mungu, taifa lilihisi utegemezo na baraka ya Yehova wakati lilipochagua kumtii Mungu wa ukweli.—2 Samuel 7:28, 29; 8:1-15.

      20. Mungu ana uhakika juu ya nini kuhusu wanadamu?

      20 Je, utamtii Mungu, au utakosa kumtii? Waisraeli walikuwa na chaguo. Ingawa sisi sote tumerithi mwelekeo wenye dhambi kutoka kwa Adamu, tumepokea pia zawadi ya kuchagua kwa hiari. Ajapokuwa Shetani, ulimwengu huu mwovu, na kutokamilika kwetu, twaweza kufanya chaguo linalofaa. Zaidi ya hayo, Muumba wetu ana uhakika kwamba ingawa kutakuwa na majaribu na vishawishi vingi, kutakuwa na wale wafanyao chaguo linalofaa, si kwa maneno tu bali pia kwa vitendo. (1 Petro 5:8-10) Je, wewe utakuwa miongoni mwao?

      21. Ni jambo gani litakalochunguzwa katika makala ifuatayo?

      21 Katika makala ifuatayo, tutaweza kuchunguza kwa uangalifu mitazamo na vitendo vyetu kwa kufikiria vielelezo vya wakati uliopita. Kila mmoja wetu na ayaitikie kwa shukrani maneno haya ya Mungu kupitia Musa: “Nimekuwekea mbele yako uzima na mauti, baraka na laana; basi chagua uzima, ili uwe hai.”—Kumbukumbu la Torati 30:19.

  • Baraka au Laana—Vielelezo kwa Ajili Yetu Leo
    Mnara wa Mlinzi—1996 | Juni 15
    • Baraka au Laana—Vielelezo kwa Ajili Yetu Leo

      “Mambo hayo yaliyowapata wao ni kielelezo kwa wengine, na yaliandikwa ili kutuonya sisi, ambao mwisho wa nyakati unatukabili.”—1 WAKORINTHO 10:11, HNWW.

      1. Sawa na vile mtu akaguavyo chombo cha kazi, sisi tufanye ukaguzi gani?

      KUTU isiyoonwa chini ya mpako wa rangi, yaweza kuanza kuharibu chombo cha kazi chenye kufanyizwa kwa chuma. Huenda ikachukua muda fulani kabla ya hiyo kutu kuonekana juu. Vivyo hivyo, mitazamo na tamaa za moyo wa mtu huenda zikaanza kuzorota muda mrefu kabla ya kuzorota huko kuwa na matokeo mazito au hata kuonwa na wengine. Sawa na vile tungekagua kwa hekima chombo cha kazi ili kuona kama kinapata kutu, ndivyo ukaguzi wa karibu wa mioyo yetu na udumishaji wayo kwa wakati unaofaa huenda ukahifadhi uaminifu-maadili wetu wa Kikristo. Yaani, twaweza kupokea baraka za Mungu na twaweza kuepuka laana za kimungu. Huenda watu fulani wakafikiri kwamba baraka na laana zilizotamkwa juu ya Israeli la kale hazina maana sana kwa wale wanaokabili umalizio wa mfumo huu wa mambo. (Yoshua 8:34, 35; Mathayo 13:49, 50; 24:3) Hata hivyo, sivyo ilivyo. Twaweza kunufaika sana na vielelezo vya kuonya vilivyohusisha Israeli, kama vionyeshwavyo katika 1 Wakorintho sura ya 10.

      2. Wakorintho wa Kwanza 10:5, 6 lasema nini kuhusu maono ya Israeli jangwani?

      2 Mtume Paulo alinganisha Waisraeli waliokuwa chini ya Musa na Wakristo walio chini ya Kristo. (1 Wakorintho 10:1-4) Ingawa watu wa Israeli wangaliweza kuingia Bara Lililoahidiwa, “wengi sana katika wao, Mungu hakupendezwa nao; maana waliangamizwa jangwani.” Kwa hiyo Paulo aliwaambia Wakristo wenzake hivi: “Basi mambo hayo yalikuwa mifano kwetu, kusudi sisi tusiwe watu wa kutamani mabaya, kama wale nao walivyotamani.” (1 Wakorintho 10:5, 6) Tamaa zinasitawishwa moyoni, kwa hiyo twahitaji kutii vielelezo vya kuonya ambavyo Paulo ataja.

      Onyo Dhidi ya Ibada ya Sanamu

      3. Waisraeli walifanyaje dhambi kuhusiana na yule ndama wa dhahabu?

      3 Onyo la Paulo la kwanza ni: “Wala msiwe waabudu sanamu, kama wengine wao walivyokuwa; kama ilivyoandikwa, Watu waliketi kula na kunywa, kisha wakasimama wacheze.” (1 Wakorintho 10:7, italiki ni zetu.) Kielelezo hiki cha kuonya ni cha Waisraeli kurudia njia za Misri na kufanya ndama wa dhahabu wa ibada ya sanamu. (Kutoka, sura ya 32) Mwanafunzi Stefano alionyesha tatizo la msingi aliposema: “Mtu huyo [Musa, mwakilishi wa Mungu] baba zetu hawakutaka kumtii, bali wakamsukumia mbali, na kwa mioyo yao wakarejea Misri, wakamwambia Haruni, Tufanyie miungu, watakaotutangulia; maana huyo Musa, aliyetutoa katika nchi ya Misri, hatujui lililompata. Wakafanya ndama siku zile, wakaleta dhabihu kwa sanamu ile, wakafurahia kazi za mikono yao.” (Matendo 7:39-41) Ona kwamba “kwa mioyo yao” hawa Waisraeli wakaidi walikuwa na tamaa mbaya zilizowaongoza kwenye ibada ya sanamu. “Wakafanya ndama . . . wakaleta dhabihu kwa sanamu ile.” Zaidi ya hayo, “wakafurahia kazi za mikono yao.” Kulikuwa na muziki, kuimba, kucheza dansi, kula, na kunywa. Kwa wazi, ibada ya sanamu ilikuwa yenye kuvutia na yenye kutumbuiza.

      4, 5. Ni mazoea gani ya kuabudu sanamu twahitaji kuepuka?

      4 Misri ya ufananisho—ulimwengu wa Shetani—kwa kweli huabudu vitumbuizo. (1 Yohana 5:19; Ufunuo 11:8) Unaabudu waigizaji, waimbaji, na wachezaji mashuhuri, na pia kucheza kwao dansi, muziki wao, dhana zao juu ya raha na nyakati za kupendeza. Wengi wameshawishwa kushiriki kikamili katika vitumbuizo huku bado wakidai kumwabudu Yehova. Wakati ambapo ni lazima Mkristo akaripiwe kwa sababu ya kosa, hali yake ya kiroho iliyodhoofika yaweza mara nyingi kufuatishwa kurudi nyuma hadi kwenye kunywa vinywaji vya alkoholi, kucheza dansi, na kuwa na wakati wa kupendeza kwa njia fulani ambayo huenda ikakaribia ibada ya sanamu. (Kutoka 32:5, 6, 17, 18) Vitumbuizo fulani vyafaa na ni vyenye kufurahisha. Hata hivyo, leo muziki, kucheza dansi, sinema, na vidio za kilimwengu zilizo nyingi hutosheleza tamaa za kimwili zilizo zenye ufisadi.

      5 Wakristo wa kweli hawashindwi na ibada ya sanamu. (2 Wakorintho 6:16; 1 Yohana 5:21) Kila mmoja wetu na awe mwangalifu vilevile asije akawa mraibu wa vitumbuizo vya kuabudu sanamu na kuwa na hatari ya kupatwa na matokeo yenye kudhuru ya kushughulikia sana kuwa na wakati wenye kupendeza kwa njia ya kilimwengu. Tukijitiisha wenyewe chini ya mavutano ya kilimwengu, tamaa na mitazamo yenye madhara yaweza kukazwa akilini na moyoni kwa hila sana. Isiposahihishwa, hiyo yaweza hatimaye kuwa na tokeo la ‘kuangamizwa jangwani’ mwa mfumo wa Shetani.

      6. Ni hatua gani chanya huenda tukahitaji kuchukua kuhusu vitumbuizo?

      6 Sawa na Musa wakati wa tukio la yule ndama wa dhahabu, kwa kweli “mtumwa mwaminifu mwenye akili” anasema hivi: “Mtu awaye yote aliye upande wa BWANA, na aje kwangu.” Kuchukua hatua chanya ili kuonyesha kwamba twasimama imara kwa ajili ya ibada ya kweli kwaweza kuokoa uhai. Kabila la Musa la Lawi lilitenda upesi kuondolea mbali mavutano yenye kushusha heshima. (Mathayo 24:45-47; Kutoka 32:26-28) Kwa hiyo basi, chunguza kwa uangalifu chaguo lako la vitumbuizo, muziki, vidio, na mambo kama hayo. Ikiwa ni yenye ufisadi kwa njia fulani, chukua msimamo wako upande wa Yehova. Kwa kumtegemea Mungu kwa sala, fanya mabadiliko katika chaguo lako la vitumbuizo na muziki, na uharibu vitu vyenye kudhuru kiroho, sawa na vile Musa alivyoharibu yule ndama wa dhahabu.—Kutoka 32:20; Kumbukumbu la Torati 9:21.

      7. Twaweza kulindaje moyo wa kitamathali?

      7 Twaweza kupingaje uharibifu wa moyo? Kwa kujifunza Neno la Mungu kwa bidii, tukiruhusu kweli zalo zipenyeze ndani ya akili zetu na mioyo yetu. (Warumi 12:1, 2) Bila shaka twapaswa kuhudhuria mikutano ya Kikristo kwa ukawaida. (Waebrania 10:24, 25) Kuhudhuria mikutano kwa kujikalia tu kungeweza kufananishwa na kupaka rangi mahali penye kutu. Hilo huenda likatuchangamsha kwa muda mfupi, lakini halitatui tatizo la msingi. Badala ya hivyo, kwa utayarishaji wa kimbele, kutafakari, na kushiriki kwa bidii katika mikutano, twaweza kwa juhudi nyingi kuondoa mambo yaletayo uharibifu ambayo huenda yakaendelea kukaa ndani ya moyo wetu wa kitamathali. Hilo litatusaidia kushikamana na Neno la Mungu na kutatuimarisha kuvumilia mitihani ya imani na kuwa “watimilifu bila kupungukiwa na neno.”—Yakobo 1:3, 4; Mithali 15:28.

      Onyo Dhidi ya Uasherati

      8-10. (a) Ni kielelezo gani cha kuonya kinachorejezewa kwenye 1 Wakorintho 10:8? (b) Maneno ya Yesu yanayopatikana kwenye Mathayo 5:27, 28 yaweza kutumiwaje kwa njia ya kunufaisha?

      8 Katika kielelezo kifuatacho cha Paulo, tunashauriwa hivi: “Wala msifanye uasherati, kama wengine wao walivyofanya, wakaanguka siku moja watu ishirini na tatu elfu.”a (1 Wakorintho 10:8) Mtume alikuwa akirejezea wakati Waisraeli walipoinamia miungu isiyo ya kweli “wakaanza kuzini pamoja na wanawake wa Moabu.” (Hesabu 25:1-9) Ukosefu wa adili katika ngono unastahili kifo! Kuruhusu mawazo na tamaa zisizo za adili kuendelea bila kuzuiwa ni kama kuruhusu moyo “kuwa na kutu.” Yesu alitaarifu hivi: “Mmesikia kwamba imenenwa, Usizini; lakini mimi nawaambia, Kila mtu atazamaye mwanamke kwa kumtamani, amekwisha kuzini naye moyoni mwake.”—Mathayo 5:27, 28.

      9 Jambo linaloshuhudia matokeo ya ‘kutazama mwanamke kwa kumtamani’ ni tokeo la kule kufikiri kwenye kushusha heshima kwa wale malaika waliokosa kutii, kabla ya Furiko la siku ya Noa. (Mwanzo 6:1, 2) Kumbuka pia, kwamba mojawapo mambo ya kuhuzunisha zaidi maishani mwa Mfalme Daudi lilichochewa na kuendelea kwake kumtazama mwanamke kusivyofaa. (2 Samweli 11:1-4) Kinyume cha hilo, yule mwanamume mwadilifu Ayubu aliyekuwa ameoa ‘alifanya agano na macho yake ili asiweze kumwangalia msichana,’ hivyo akiepuka ukosefu wa adili na akithibitika kuwa mwenye kushika uaminifu-maadili. (Ayubu 31:1-3, 6-11) Macho yaweza kufananishwa na madirisha ya moyo. Na mambo mengi maovu hutoka katika moyo wenye ufisadi.—Marko 7:20-23.

      10 Tukiyatumia maneno ya Yesu, hatutaruhusu mawazo mabaya yaendelee kwa kutazama habari ya kiponografia au kwa kufikiria mawazo yasiyo ya adili kuhusu Mkristo mwenzetu, mfanyakazi mwenzetu, na mtu mwingine yeyote. Kutu haiondolewi kutoka chuma kwa kupangusa tu mahali palipoharibiwa nayo. Kwa hiyo, usiondoshe kijuujuu tu mawazo na mielekeo isiyo ya adili kana kwamba hiyo si ya maana sana. Chukua hatua zenye nguvu kujiondoshea mielekeo isiyo ya adili. (Linganisha Mathayo 5:29, 30.) Paulo ahimiza waamini wenzake hivi: “Vifisheni viungo vyenu vilivyo katika nchi, uasherati, uchafu, tamaa mbaya, mawazo mabaya, na kutamani, ndiyo ibada ya sanamu; kwa ajili ya mambo hayo huja ghadhabu ya Mungu.” Ndiyo, kwa ajili ya mambo kama ukosefu wa adili katika ngono, “huja ghadhabu ya Mungu” ikiwa wonyesho wa laana yake. Kwa hiyo twahitaji ‘kuvifisha’ viungo vyetu kwa habari ya mambo hayo.—Wakolosai 3:5, 6.

      Onyo Dhidi ya Malalamiko Yenye Uasi

      11, 12. (a) Ni onyo gani linalotolewa kwenye 1 Wakorintho 10:9, na ni tukio gani lililorejezewa? (b) Onyo la Paulo lituathirije?

      11 Paulo afuata na onyo hili: “Wala tusimjaribu Bwana, kama wengine wao walivyomjaribu, wakaharibiwa na nyoka.” (1 Wakorintho 10:9) Walipokuwa wakisafiri karibu na mpaka wa Edomu, Waisraeli “wakamnung’unikia Mungu, na Musa, Mbona mmetupandisha huku kutoka nchi ya Misri, ili tufe jangwani? maana hapana chakula, wala hapana maji, na roho zetu zinakinai chakula hiki dhaifu,” ile mana iliyoandaliwa kimuujiza. (Hesabu 21:4, 5) Ebu fikiria! Wale Waisraeli ‘walimnung’unikia Mungu’ wakiyaita maandalizi yake kuwa yenye kudharaulika!

      12 Kwa malalamiko yao, Waisraeli walikuwa wakitahini subira ya Yehova. Adhabu haikukosa kutolewa, kwani Yehova alituma nyoka zenye sumu miongoni mwao, na wengi wakafa kutokana na maumo ya nyoka. Baada ya watu kutubu na Musa kuomba kwa niaba yao, hilo pigo lilikomeshwa. (Hesabu 21:6-9) Kwa hakika tukio hilo lapaswa litumikie likiwa onyo kwetu kutoonyesha roho ya kulalamika, yenye uasi, hasa dhidi ya Mungu na mipango yake ya kitheokrasi.

      Onyo Dhidi ya Kunung’unika

      13. Wakorintho wa Kwanza 10:10 laonya dhidi ya nini, na Paulo alikuwa akifikiria uasi upi?

      13 Akitaja kielelezo chake cha mwisho kilichohusisha Waisraeli jangwani, Paulo aandika hivi: “Wala msinung’unike, kama wengine wao walivyonung’unika, wakaharibiwa na mharabu.” (1 Wakorintho 10:10) Uasi ulitokea wakati Kora, Dathani, Abiramu, na washiriki wao walipotenda kwa njia isiyo ya kitheokrasi wakapinga mamlaka ya Musa na Haruni. (Hesabu 16:1-3) Baada ya uharibifu wa wale waasi, Waisraeli walianza kunung’unika. Hiyo ilikuwa kwa sababu walianza kusababu kwamba uharibifu wa wale waasi haukuwa wenye haki. Hesabu 16:41 lataarifu hizi: “Siku ya pili yake mkutano wote wa wana wa Israeli wakamnung’unikia Musa, na Haruni, wakasema, Ninyi mmewaua watu wa BWANA.” Tokeo la kuchambua kwao njia ambayo haki ilitekelezwa katika pindi hiyo lilikuwa kuangamia kwa Waisraeli 14,700 kutokana na tauni iliyopelekwa kimungu.—Hesabu 16:49.

      14, 15. (a) Dhambi moja ya wale “watu wasiomcha Mungu” waliopenyeza ndani ya kutaniko, ilikuwa nini? (b) Ni somo gani liwezalo kupatikana kutokana na tukio lililohusisha Kora?

      14 Katika karne ya kwanza W.K., “watu wasiomcha Mungu” waliopenyeza ndani ya kutaniko la Kikristo walithibitika kuwa walimu wasio wa kweli na pia wanung’unikaji. Watu hao walikuwa ‘wakidharau mamlaka ya Mungu na kuvitukana viumbe vitukufu,’ wanaume watiwa-mafuta waliokabidhiwa uangalizi wa kutaniko wakati huo. Kuhusu hao waasi-imani wasiomcha Mungu, mwanafunzi Yuda alisema hivi pia: “Watu hawa wananung’unika daima na kuwalaumu watu wengine [“walalamikaji juu ya fungu lao maishani,” NW]. Hufuata tamaa zao.” (Yuda 3, 4, 8, 16, HNWW) Leo, watu fulani mmoja-mmoja wanakuwa wanung’unikaji kwa sababu wanaruhusu mtazamo ulioharibiwa kiroho ukue moyoni mwao. Mara nyingi wao hukazia hali za kutokamilika za wale wenye wadhifa wa uangalizi kutanikoni na kuanza kunung’unika dhidi yao. Kunung’unika na kulalamika kwao huenda hata kukafikia kadiri ya kuchambua vichapo vya ‘mtumwa mwaminifu.’

      15 Inafaa kuuliza maswali ya moyo mweupe kuhusu habari ya Kimaandiko. Lakini namna gani ikiwa tungekuza mtazamo hasi ujionyeshao katika mazungumzo ya uchambuzi miongoni mwa kikundi cha marafiki wa karibu? Ingefaa tujiulize wenyewe, ‘Matokeo ya kunung’unika huku yaelekea kuwa nini? Je, isingefaa zaidi kuacha kunung’unika na kusali kwa unyenyekevu ili kupata hekima?’ (Yakobo 1:5-8; Yuda 17-21) Kora na wale waliomuunga mkono, walioasi dhidi ya mamlaka ya Musa na Haruni, huenda wakawa walisadikishwa sana kwamba maoni yao yalikuwa halali hivi kwamba hawakuchunguza nia zao. Hata hivyo, walikuwa wamekosea kabisa. Ndivyo na wale Waisraeli walionung’unika kuhusu uharibifu wa Kora na wale waasi wengine. Ni jambo la hekima kama nini kuruhusu vielelezo hivyo vitusukume kuchunguza nia zetu, kuondosha hali ya kunung’unika au kulalamika, na kumruhusu Yehova atutakase!—Zaburi 17:1-3.

      Jifunze, na Ufurahie Baraka

      16. Maana ya himizo kwenye 1 Wakorintho 10:11, 12, ni nini?

      16 Chini ya upulizio wa kimungu, Paulo amalizia orodha ya ujumbe mbalimbali wenye onyo kwa himizo hili: “Basi, mambo hayo yaliyowapata wao ni kielelezo kwa wengine, na yaliandikwa ili kutuonya sisi, ambao mwisho wa nyakati unatukabili. Anayedhani amesimama imara ajihadhari asianguke.” (1 Wakorintho 10:11, 12, HNWW) Sisi na tusipuuze msimamo wetu mzuri katika kutaniko la Kikristo.

      17. Tukihisi nia isiyofaa moyoni mwetu, tufanye nini?

      17 Sawa na vile chuma kilicho na mwelekeo wa kupata kutu, ndivyo sisi wazao wa Adamu mwenye dhambi tumerithi mwelekeo wa kutenda mabaya. (Mwanzo 8:21; Warumi 5:12) Kwa hiyo, hatupaswi kuvunjika moyo tukihisi nia isiyofaa moyoni mwetu. Badala ya hivyo, acheni tuchukue hatua ya mkataa. Chuma kinapowekwa katika hewa yenye unyevu au katika mazingira ya kubabua, kuharibika kwacho kunaongezeka sana. Twahitaji kuepuka kujiweka katika “hewa” ya ulimwengu wa Shetani, yenye vitumbuizo vyao vibaya, ukosefu wao wa adili ulioenea, na mwelekeo wao wa akili ulio hasi.—Waefeso 2:1, 2.

      18. Yehova amefanya nini kuhusiana na mielekeo mibaya ya wanadamu?

      18 Yehova ameandalia jamii ya kibinadamu njia ya kupingana na mielekeo mibaya ambayo tumerithi. Alimtoa Mwana wake mzaliwa-pekee ili wale wanaodhihirisha imani katika yeye waweze kuwa na uhai udumuo milele. (Yohana 3:16) Tukifuata nyayo za Yesu kwa ukaribu na kudhihirisha utu ulio kama wa Kristo, tutakuwa baraka kwa wengine. (1 Petro 2:21) Pia tutapokea baraka za kimungu, wala si laana.

      19. Twaweza kunufaikaje kwa kufikiria vielelezo vya Kimaandiko?

      19 Ingawa sisi leo tunaweza kufanya kosa kwa urahisi kama vile Waisraeli wa zamani, tuna Neno kamili la Mungu lililoandikwa ili kutuongoza. Kutoka katika kurasa zalo twajifunza kuhusu shughuli za Yehova pamoja na wanadamu na pia sifa zake kama zilivyoonyeshwa katika Yesu, ‘mng’ao wa utukufu wake [Mungu] na chapa ya nafsi Yake.’ (Waebrania 1:1-3; Yohana 14:9, 10) Kupitia sala na funzo la Maandiko lenye bidii, twaweza kuwa na “nia ya Kristo.” (1 Wakorintho 2:16) Tunapokabiliwa na vishawishi na mitihani mingine ya imani yetu, twaweza kunufaika kwa kufikiria vielelezo vya Kimaandiko vya kale na hasa kile kielelezo bora kuliko vyote cha Yesu Kristo. Tukifanya hivyo, hatutalazimika kujionea wenyewe utimizo wa laana za kimungu. Badala ya hivyo, tutafurahia upendeleo wa Yehova leo na baraka zake milele.

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki