Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Sheria ya Kristo
    Mnara wa Mlinzi—1996 | Septemba 1
    • Sheria ya Kristo

      “Nalikuwa . . . mwenye sheria mbele za Kristo.”—1 WAKORINTHO 9:21.

      1, 2. (a) Mengi ya makosa ya wanadamu yangeweza kuepukwaje? (b) Jumuiya ya Wakristo ilishindwa kujifunza nini kutokana na historia ya Dini ya Kiyahudi?

      “WATU na serikali hawajajifunza kamwe chochote kutokana na historia, wala kutenda kulingana na kanuni zilizopatikana kwayo.” Ndivyo alivyosema mwanafalsafa Mjerumani wa karne ya 19. Kwa kweli, mwendo wa historia ya kibinadamu umefafanuliwa kuwa “mfuatano wa makosa,” mfululizo wa makosa na taabu zisizopendeza, ambazo nyingi zazo zingaliepukwa ikiwa tu wanadamu wangalikuwa tayari kujifunza kutokana na makosa yaliyopita.

      2 Kukataa huko-huko kujifunza kutokana na makosa ya wakati uliopita kwaonyeshwa katika mazungumzo haya ya sheria ya kimungu. Yehova Mungu aliweka sheria iliyo bora zaidi badala ya ile Sheria ya Kimusa—sheria ya Kristo. Hata hivyo, viongozi wa Jumuiya ya Wakristo, wanaodai kufundisha na kuishi kulingana na sheria hiyo, wameshindwa kujifunza kutokana na makosa mabaya sana ya Mafarisayo. Hivyo Jumuiya ya Wakristo imepinda na kutumia vibaya sheria ya Kristo sawa na vile Dini ya Kiyahudi ilivyoifanya Sheria ya Musa. Hilo lingewezekanaje? Kwanza, acheni tuizungumzie sheria hii yenyewe—hiyo ni nini, ni nani inaowaongoza na jinsi gani, na ni nini kinachoitofautisha na Sheria ya Kimusa. Kisha tutachunguza jinsi Jumuiya ya Wakristo imeitumia vibaya. Na tujifunze kwa njia hiyo kutokana na historia na kufaidika nayo!

      Agano Jipya

      3. Yehova alitoa ahadi gani kuhusu agano jipya?

      3 Isipokuwa Yehova Mungu, ni nani mwingine ambaye angeweza kuboresha Sheria iliyo kamilifu? Agano la Sheria ya Kimusa lilikuwa kamilifu. (Zaburi 19:7) Hata hivyo, Yehova aliahidi hivi: “Angalia, siku zinakuja, . . . nitakapofanya agano jipya na nyumba ya Israeli, na nyumba ya Yuda. Si kwa mfano wa agano lile nililolifanya na baba zao.” Amri Kumi—kitovu cha Sheria ya Kimusa—ziliandikwa juu ya mabamba ya mawe. Lakini kuhusu agano jipya, Yehova alisema hivi: “Nitatia sheria yangu ndani yao, na katika mioyo yao nitaiandika.”—Yeremia 31:31-34.

      4. (a) Ni Israeli jipi linalohusika katika agano jipya? (b) Ni nani wengine zaidi ya Waisraeli wa kiroho walio chini ya sheria ya Kristo?

      4 Ni nani ambao wangeingizwa katika agano hilo jipya? Bila shaka si “nyumba ya Israeli” halisi, iliyomkataa Mpatanishi wa agano hilo. (Waebrania 9:15) La, “Israeli” jipya lingekuwa “Israeli wa Mungu,” taifa la Waisraeli wa kiroho. (Wagalatia 6:16; Warumi 2:28, 29) Kikundi hicho kidogo cha Wakristo watiwa-mafuta kwa roho kingeungwa baadaye na “mkutano mkubwa” kutoka kwa mataifa yote ambao ungejitahidi pia kumwabudu Yehova. (Ufunuo 7:9, 10; Zekaria 8:23) Ingawa hawashiriki katika agano jipya, wao pia wangekuwa chini ya sheria. (Linganisha Mambo ya Walawi 24:22; Hesabu 15:15.) Wakiwa “kundi moja” chini ya “mchungaji mmoja,” wote wangekuwa ‘wenye sheria mbele za Kristo,’ sawa na alivyoandika mtume Paulo. (Yohana 10:16; 1 Wakorintho 9:21) Paulo aliliita agano hilo jipya “agano lililo bora.” Kwa nini? Kwanza, lilitegemea ahadi zilizotimizwa badala ya vivuli vya mambo yajayo.—Waebrania 8:6; 9:11-14.

      5. Ni nini kusudi la agano jipya, na kwa nini litafanikiwa?

      5 Kusudi la agano hilo ni nini? Ni kutokeza taifa la wafalme na makuhani ili kubariki wanadamu wote. (Kutoka 19:6; 1 Petro 2:9; Ufunuo 5:10) Agano la Sheria ya Kimusa halikutokeza kamwe taifa hilo kwa maana kamili, kwa kuwa Israeli kwa ujumla liliasi nalo likapoteza fursa yalo. (Linganisha Warumi 11:17-21.) Hata hivyo, agano jipya hakika litafaulu, kwa kuwa linahusianishwa na aina tofauti kabisa ya sheria. Tofauti katika njia zipi?

      Sheria Iliyo ya Uhuru

      6, 7. Sheria ya Kristo huandaaje uhuru mkubwa zaidi kuliko ilivyofanya Sheria ya Kimusa?

      6 Sheria ya Kristo hushirikishwa na uhuru mara kwa mara. (Yohana 8:31, 32) Hiyo hurejezewa kuwa “sheria ya watu huru” na “sheria kamilifu iliyo ya uhuru.” (Yakobo 1:25; 2:12, NW) Bila shaka, uhuru wote miongoni mwa wanadamu ni wa kadiri. Licha ya hilo, sheria hii hutoa uhuru mkubwa zaidi kuliko ile iliyoitangulia, Sheria ya Kimusa. Jinsi gani?

      7 Kwa kielelezo, hakuna anayezaliwa chini ya sheria ya Kristo. Mambo kama jamii na mahali pa kuzaliwa hayahusiki. Wakristo wa kweli huchagua mioyoni mwao kwa hiari kukubali nira ya utii kwa sheria hiyo. Kwa kufanya hivyo, wao huona kwamba hiyo ni nira ya fadhili, mzigo mwepesi. (Mathayo 11:28-30) Ikiwa mwakumbuka, Sheria ya Kimusa ilikusudiwa pia kumfundisha mtu kwamba yeye ni mwenye dhambi na mwenye uhitaji mkubwa wa dhabihu ya fidia ili imkomboe. (Wagalatia 3:19) Sheria ya Kristo hufundisha kwamba Mesiya amekuja, akalipa bei ya fidia kwa kutoa uhai wake, na kutufungulia njia tuweze kuwekwa huru kutoka katika utumwa mbaya sana wa dhambi na kifo! (Warumi 5:20, 21) Ili kufaidika, twahitaji ‘kudhihirisha imani’ katika dhabihu hiyo.—Yohana 3:16, NW.

      8. Sheria ya Kristo hutia ndani nini, lakini kwa nini kuishi kulingana nayo hakuhitaji kujua kwa moyo mamia ya sheria halali?

      8 ‘Kudhihirisha imani’ huhusisha kuishi kulingana na sheria ya Kristo. Hilo hutia ndani kutii amri zote za Kristo. Je, hilo humaanisha kujua moyoni mamia ya sheria na maagizo? La. Ingawa Musa, mpatanishi wa agano la kale, aliandika Sheria ya Kimusa, Yesu, Mpatanishi wa agano jipya, hakuandika hata sheria moja. Badala ya hivyo, aliishi kulingana na sheria hiyo. Kupitia mwendo wake wa maisha ulio mkamilifu, aliacha kigezo ili wote wafuate. (1 Petro 2:21) Huenda hiyo ndiyo sababu ibada ya Wakristo wa mapema ilirejezewa kuwa “ile Njia.” (Matendo 9:2; 19:9, 23; 22:4; 24:22) Kwao, sheria ya Kristo ilitolewa kielelezi katika maisha ya Kristo. Kumwiga Yesu kulikuwa kutii sheria hiyo. Upendo wao mwingi kwake ulimaanisha kwamba sheria hiyo kwelikweli iliandikwa mioyoni mwao, jinsi ilivyotolewa unabii. (Yeremia 31:33; 1 Petro 4:8) Na aliye mtiifu kwa sababu ya upendo hahisi kamwe kuwa anaonewa—sababu nyingine inayofanya sheria ya Kristo iweze kuitwa “sheria ya watu huru.”

      9. Ni nini kiini chenyewe cha sheria ya Kristo, na ni jinsi gani sheria hiyo huhusisha amri mpya?

      9 Ikiwa upendo ulikuwa wa maana katika Sheria ya Kimusa, huo ndio kiini chenyewe cha sheria ya Kikristo. Kwa njia hiyo sheria ya Kristo hutia ndani amri mpya—lazima Wakristo wawe na upendo wa kujidhabihu kuelekea mmoja na mwenzake. Wao wapaswa kupenda kama alivyopenda Yesu; aliutoa uhai wake kwa hiari kwa niaba ya rafiki zake. (Yohana 13:34, 35; 15:13) Kwa hiyo yaweza kusemwa kwamba sheria ya Kristo ni wonyesho wa theokrasi ulio wa juu hata zaidi kuliko vile Sheria ya Musa ilivyokuwa. Kama vile jarida hili limeonyesha hapo mbele: “Theokrasi ni utawala wa Mungu; Mungu ni upendo; kwa hiyo theokrasi ni utawala wa upendo.”

      Yesu na Mafarisayo

      10. Ufundishaji wa Yesu ulitofautianaje na ule wa Mafarisayo?

      10 Basi, haishangazi hata kidogo kwamba Yesu alipambana na viongozi wa kidini Wayahudi wa siku yake. Waandishi na Mafarisayo hawakuwa wamefikiria kamwe “sheria kamilifu iliyo ya uhuru.” Walijaribu kudhibiti watu kupitia maagizo yaliyofanyizwa na mwanadamu. Mafundisho yao yakawa yenye kuonea, ya kulaumu, yasiyofaa. Tofauti kabisa na hivyo, mafundisho ya Yesu yalikuwa yenye kujenga na ya kufaa sana! Alifundisha mambo yenye kutumika naye akashughulikia mahitaji na mahangaiko halisi ya watu. Alifundisha kwa njia sahili na akiwa na hisia za kutoka moyoni, akitumia vielezi vya maisha ya kila siku na kufundisha kutokana na mamlaka ya Neno la Mungu. Kwa njia hiyo, “makutano walishangaa mno kwa mafundisho yake.” (Mathayo 7:28) Ndiyo, ufundishaji wa Yesu ulifikia mioyo yao!

      11. Yesu alionyeshaje kwamba Sheria ya Kimusa ilipaswa kutumiwa kwa kiasi na kwa rehema?

      11 Badala ya kuongezea Sheria ya Kimusa maagizo zaidi, Yesu alionyesha jinsi Wayahudi walipaswa kuwa wakitumia Sheria wakati wote—kwa kiasi na rehema. Kumbukeni, kwa kielelezo, ile pindi alipofikiwa na mwanamke aliyekuwa akitokwa damu. Kulingana na Sheria ya Kimusa, yeyote ambaye mwanamke huyo aligusa angekuwa najisi, kwa hiyo bila shaka hakupaswa kuchangamana na umati wa watu! (Mambo ya Walawi 15:25-27) Lakini alitaka sana kuponywa hivi kwamba alipitia katikati ya umati naye akagusa vazi la nje la Yesu. Kutokwa damu kukakoma mara moja. Je, Yesu alimkemea kwa ajili ya kuikiuka Sheria? La; badala ya kufanya hivyo, alielewa hali yake mbaya na akaonyesha kwa matendo ile amri kubwa kupita zote ya Sheria—upendo. Kwa hisia-mwenzi alimwambia mwanamke huyo hivi: “Binti, imani yako imekuponya, enenda zako kwa amani, uwe mzima, usiwe na msiba wako tena.”—Marko 5:25-34.

      Je, Sheria ya Kristo Ni Yenye Uendekevu?

      12. (a) Kwa nini tusikate maneno kwamba Kristo ni mwendekevu? (b) Ni nini kinachoonyesha kwamba kufanyizwa kwa sheria nyingi huongoza kwenye kufanyizwa kwa njia nyingi za kuzikiuka?

      12 Basi, je, tukate maneno kwamba kwa kuwa sheria ya Kristo ‘ni ya uhuru,’ ni yenye uendekevu, ilhali Mafarisayo, wakiwa na mapokeo yao yote ya mdomo, angalau waliwekea mienendo ya watu mipaka yenye ukali? La. Mifumo ya kisheria ya leo yatolea kielezi kwamba mara nyingi kadiri sheria zilivyo nyingi, ndivyo watu hupata njia nyingi katika hizo za kuzikiuka.a Katika siku ya Yesu wingi wa sheria za Mafarisayo ulitia moyo kutafuta njia za kuzikiuka, kule kufanya kazi kijuu-juu tu bila upendo, na kule kukuza sura ya nje ya kuwa mwenye kujihesabia uadilifu ili kufunika ufisadi wa ndani.—Mathayo 23:23, 24.

      13. Kwa nini sheria ya Kristo inatokeza kiwango cha juu zaidi cha mwenendo kuliko mfumo wowote wa sheria ulioandikwa?

      13 Kwa kutofautisha, sheria ya Kristo haikuzi mitazamo hiyo. Kwa hakika, kutii sheria yenye kutegemea kumpenda Yehova na inayotiiwa kwa kuiga upendo wa Kristo wa kujidhabihu kwa ajili ya wengine hutokeza kiwango cha juu zaidi cha mwenendo kuliko kitokezwacho kwa kufuata mfumo rasmi wa kisheria. Upendo hautafuti njia za kukiuka jambo; huo hutuzuia tusifanye madhara ambayo mfumo wa sheria huenda usikataze waziwazi. (Ona Mathayo 5:27, 28.) Kwa njia hiyo, sheria ya Kristo itatuchochea kuwafanyia wengine mambo—kuonyesha ukarimu, ukaribishaji-wageni, na upendo—katika njia ambazo hakuna sheria yoyote rasmi ingeweza kutuchochea tufanye.—Matendo 20:35; 2 Wakorintho 9:7; Waebrania 13:16.

      14. Kuishi kulingana na sheria ya Kristo kulikuwa na tokeo gani juu ya kutaniko la Kikristo la karne ya kwanza?

      14 Kwa kadiri ambavyo washiriki walo waliishi kulingana na sheria ya Kristo, kutaniko la Kikristo la mapema lilifurahia hali yenye uchangamfu, yenye upendo, yenye uhuru kadiri fulani kutoka katika mitazamo migumu, yenye kuhukumu, na ya kinafiki iliyoenea sana katika masinagogi ya siku hiyo. Ni lazima iwe washiriki wa makutaniko hayo mapya kwa kweli walihisi kwamba walikuwa wakiishi kulingana na “sheria ya watu huru”!

      15. Ni zipi baadhi ya jitihada za mapema za Shetani za kufisidi kutaniko la Kikristo?

      15 Hata hivyo, Shetani alitamani kulifisidi kutaniko la Kikristo kutoka ndani, jinsi tu alivyokuwa amelifisidi taifa la Israeli. Mtume Paulo alionya juu ya watu walio kama mbwa-mwitu ambao ‘wangesema mapotovu’ na kuonea kundi la Mungu. (Matendo 20:29, 30) Yeye alilazimika kukabiliana na Wayudaiza (wageuzao watu wafuate Dini ya Kiyahudi), waliojitahidi kubadili uhuru wa kadiri wa sheria ya Kristo na utumwa wa Sheria ya Kimusa, iliyokuwa imetimizwa katika Kristo. (Mathayo 5:17; Matendo 15:1; Warumi 10:4) Baada ya mtume wa mwisho kufa, hakukuwa na kizuizi tena dhidi ya uasi-imani huo. Kwa hiyo ufisadi ukaenea sana.—2 Wathesalonike 2:6, 7.

      Jumuiya ya Wakristo Yachafua Sheria ya Kristo

      16, 17. (a) Ufisadi ulikuwa wa namna gani mbalimbali katika Jumuiya ya Wakristo? (b) Sheria za Kanisa Katoliki ziliendelezaje maoni yaliyopotolewa juu ya ngono?

      16 Sawa na Dini ya Kiyahudi, ufisadi ulikuwa wa namna mbalimbali katika Jumuiya ya Wakristo. Hiyo pia ikawa mawindo ya mafundisho yasiyo ya kweli na maadili malegevu. Na mara nyingi jitihada zayo za kulinda kundi layo dhidi ya mavutano ya nje zilithibitika kuwa zenye kubabua chochote kilichosalia cha ibada ya kweli. Sheria ngumu na zisizo za kimaandiko zikakua upesi.

      17 Kanisa Katoliki limeongoza katika kuunda idadi kubwa ya sheria za kanisa. Sheria hizo zilikuwa zimepotolewa hasa juu ya mambo yanayohusu ngono. Kulingana na kitabu Sexuality and Catholicism, kanisa lilitwaa falsafa ya Kigiriki ya Ustoiki, iliyoshuku aina zote za raha. Kanisa lilikuja kufundisha kwamba raha yote ya kingono, kutia ndani ile ya mahusiano ya ndoa ya kawaida, ilikuwa yenye dhambi. (Tofautisha Mithali 5:18, 19.) Ngono ilidaiwa kuwa ya uzazi tu, wala si ya raha ya kingono. Kwa njia hiyo sheria ya kanisa ililaumu njia yoyote ya kuzuia mimba kuwa dhambi nzito sana, nyakati nyingine ikihitaji adhabu ya kutubisha ya miaka mingi. Zaidi, ukuhani ulikatazwa kuoa, amri ambayo imetokeza ongezeko kubwa la ngono haramu, kutia na kuwatenda watoto vibaya.—1 Timotheo 4:1-3.

      18. Matokeo ya kuongezeka kwa sheria za kanisa yalikuwa nini?

      18 Kadiri sheria za kanisa zilivyoongezeka, zilikusanywa kuwa vitabu. Vitabu hivyo vikaanza kuifunika na kuchukua mahali pa Biblia. (Linganisha Mathayo 15:3, 9.) Sawa na Dini ya Kiyahudi, Ukatoliki uliyashuku maandishi ya kibinadamu na kuyaona mengi yayo kuwa tisho. Upesi maoni hayo yakapita mno onyo la Biblia lifaalo juu ya habari hiyo. (Mhubiri 12:12; Wakolosai 2:8) Jerome, mwandikaji wa kanisa wa karne ya nne W.K. alipaaza sauti hivi: “Ee Bwana, nikipata wakati wowote tena kuwa na vitabu vya kilimwengu au kuvisoma, nimekukana.” Baada ya muda, kanisa likajitwalia kazi ya kukagua vitabu—hata vitabu juu ya habari za kilimwengu. Kwa njia hiyo katika karne ya 17 mwastronomia Galileo alilaumiwa kwa sababu ya kuandika kwamba dunia hulizunguka jua. Kusisitiza kwa kanisa kuwa mamlaka ya mwisho katika kila jambo—hata katika maswali juu ya astronomia—hatimaye kungedhoofisha imani katika Biblia.

      19. Makao ya watawa yaliendelezaje umabavu ulio mgumu?

      19 Uundaji-sheria wa kanisa ulisitawi katika makao ya watawa ambapo, watawa wa kiume walijitenga na ulimwengu huu ili waishi katika hali ya kujikana. Makao mengi ya watawa ya Katoliki yalishikamana na “Kanuni ya Mtakatifu Benedict.” Abati (jina lililotokana na neno la Kiaramu “baba”) alitawala akiwa na mamlaka kamili. (Linganisha Mathayo 23:9.) Ikiwa mtawa alipokea zawadi kutoka kwa wazazi wake, abati alikuwa akiamua ikiwa mtawa huyo au mwingine ndiye angeipokea. Zaidi ya kulaumu maneno machafu, kanuni moja ilikataza porojo na mizaha yote, ikisema hivi: “Hakuna mwanafunzi yeyote atakayeongea mambo hayo.”

      20. Ni nini kinachoonyesha kwamba Uprotestanti pia ulichochea umabavu usio wa kimaandiko?

      20 Uprotestanti, uliojitahidi kupindua mambo yenye kupita kiasi ya Ukatoliki, upesi ukawa stadi vilevile wa kufanyiza sheria za kimabavu zisizo na msingi katika sheria ya Kristo. Kwa mfano, mpinduzi wa kidini mkuu John Calvin alikuja kuitwa “mfanya sheria wa Kanisa lililofanywa upya.” Aliongoza kanisa la Protestanti la Geneva akiwa na sheria ngumu nyingi ambazo zilitekelezwa na “Wazee” ambao “kazi” yao, akaandika Calvin, “ni kusimamia maisha ya kila mmoja.” (Tofautisha 2 Wakorintho 1:24.) Kanisa lilidhibiti hoteli mbalimbali na kuamua ni vichwa gani vya mazungumzo vilivyoruhusiwa. Kulikuwa na adhabu kali kwa makosa kama kuimba nyimbo zisizo na staha au kucheza dansi.b

      Kujifunza Kutokana na Makosa ya Jumuiya ya Wakristo

      21. Matokeo ya ujumla ya mwelekeo wa Jumuiya ya Wakristo wa ‘kupita yaliyoandikwa’ yamekuwa nini?

      21 Je, kanuni na sheria zote hizo zimeilinda Jumuiya ya Wakristo dhidi ya ufisadi? Tofauti kabisa! Leo Jumuiya ya Wakristo imegawanyika katika mamia ya mafarakano, kuanzia yale yenye kufuata sheria sana hadi yale yaliyo yenye uendekevu sana. Yote hayo, kwa njia moja au nyingine, ‘yamepita yale yaliyoandikwa,’ yakiruhusu kufikiri kwa kibinadamu kuongoze kundi na kuingilia sheria ya kimungu.—1 Wakorintho 4:6.

      22. Kwa nini uasi wa Jumuiya ya Wakristo haukumaanisha mwisho wa sheria ya Kristo?

      22 Hata hivyo, historia ya sheria ya Kristo haina mwisho wenye msiba. Yehova Mungu hataruhusu kamwe wanadamu duni waifagilie mbali sheria ya kimungu. Sheria ya Kikristo ina nguvu sana leo miongoni mwa Wakristo wa kweli, nao wana lile pendeleo kubwa la kuishi kulingana nayo. Lakini baada ya kuchunguza kile ambacho Dini ya Kiyahudi na Jumuiya ya Wakristo zimefanyia sheria ya kimungu, twaweza kwa kufaa kuuliza, ‘Twaishije kulingana na sheria ya Kristo huku tukiepuka ule mtego wa kuchafua Neno la Mungu kwa kusababu kwa kibinadamu na kanuni zinazodhoofisha maana yenyewe ya sheria ya kimungu? Sheria ya Kristo yapaswa kutupa maoni gani yenye usawaziko leo?’ Makala inayofuata itashughulikia maswali hayo.

  • Kuishi Kulingana na Sheria ya Kristo
    Mnara wa Mlinzi—1996 | Septemba 1
    • Kuishi Kulingana na Sheria ya Kristo

      “Mchukuliane mizigo na kuitimiza hivyo sheria ya Kristo.”—WAGALATIA 6:2.

      1. Kwa nini yaweza kusemwa kwamba sheria ya Kristo ni uvutano wenye nguvu unaotokeza mema leo?

      KATIKA Rwanda, Mashahidi wa Yehova Wahutu na Watutsi walihatarisha maisha zao ili kulindana dhidi ya uchinjaji wa kikabila ambao majuzi uliikumba nchi hiyo. Mashahidi wa Yehova huko Kobe, Japani, waliopoteza washiriki wa familia katika tetemeko la dunia lililosababisha uharibifu mkubwa waliathiriwa vibaya sana na hasara waliyopata. Hata hivyo, walitenda upesi kuwaokoa wahasiriwa wengine. Ndiyo, vielelezo vyenye kuchangamsha moyo kutoka ulimwenguni pote huonyesha kwamba sheria ya Kristo inafanya kazi leo. Hiyo ni uvutano wenye nguvu unaotokeza mema.

      2. Jumuiya ya Wakristo imeshindwaje kuielewa sheria ya Kristo, nasi twaweza kufanya nini ili kuitimiza sheria hiyo?

      2 Wakati uleule, unabii wa Biblia juu ya “siku [hizi] za mwisho” za hatari unatimizwa. Wengi wana “mfano wa utauwa” lakini ‘wanakana nguvu zake.’ (2 Timotheo 3:1, 5) Hasa katika Jumuiya ya Wakristo, mara nyingi dini ni jambo la kidesturi, wala si jambo la moyoni. Je, hilo ni kwa sababu ni vigumu sana kuishi kulingana na sheria ya Kristo? La. Yesu hangetupatia sheria ambayo haingeweza kufuatwa. Jumuiya ya Wakristo imeshindwa tu kuielewa sheria ya Kristo. Imeshindwa kutii maneno haya yaliyopuliziwa: “Mchukuliane mizigo na kuitimiza hivyo sheria ya Kristo.” (Wagalatia 6:2) Sisi ‘huitimiza sheria ya Kristo’ kwa kuchukuliana mizigo, wala si kwa kuwaiga Mafarisayo na kuwaongezea ndugu zetu mizigo isivyo haki.

      3. (a) Ni zipi baadhi ya amri zinazotiwa ndani katika sheria ya Kristo? (b) Kwa nini lingekuwa kosa kukata maneno kwamba kutaniko la Kikristo halipaswi kuwa na kanuni nyingine zaidi ya zile amri za moja kwa moja za Kristo?

      3 Sheria ya Kristo hutia ndani amri zote za Kristo Yesu—ziwe ni kuhubiri na kufundisha, kuliweka jicho likiwa safi na sahili, kujitahidi kudumisha amani na jirani yetu, au kuondoa uchafu kutoka kutanikoni. (Mathayo 5:27-30; 18:15-17; 28:19, 20; Ufunuo 2:14-16) Kwa kweli, Wakristo wanawajibika kushika amri zote zilizomo katika Biblia ambazo zaelekezwa kwa wafuasi wa Kristo. Na kuna mengine zaidi. Tengenezo la Yehova, na pia makutaniko moja-moja, lazima liweke kanuni na taratibu za lazima ili kudumisha utaratibu mzuri. (1 Wakorintho 14:33, 40) Kwani, Wakristo hata hawangekutana pamoja ikiwa hawakuwa na kanuni zozote juu ya wakati, mahali, na jinsi ya kufanya mikutano hiyo! (Waebrania 10:24, 25) Kushirikiana na miongozo yenye kiasi iliyotolewa na wale waliopewa mamlaka katika tengenezo ni sehemu pia ya kuitimiza sheria ya Kristo.—Waebrania 13:17.

      4. Ni nini kinachoichochea ibada safi?

      4 Hata hivyo, Wakristo wa kweli hawaruhusu ibada yao iwe mpangilio wa sheria usio na maana. Hawamtumikii Yehova kwa sababu tu mtu fulani au tengenezo fulani lawaambia wafanye hivyo. Badala ya hivyo, kani inayochochea ibada yao ni upendo. Paulo aliandika hivi: “Upendo wa Kristo hutushurutisha.” (2 Wakorintho 5:14, NW, kielezi-chini) Yesu aliwaamuru wafuasi wake wapendane. (Yohana 15:12, 13) Upendo wenye kujidhabihu ndio msingi wa sheria ya Kristo, nao hushurutisha au kuchochea Wakristo wa kweli kotekote, katika familia na katika kutaniko. Acheni tuone ni jinsi gani.

      Katika Familia

      5. (a) Wazazi waweza kutimizaje sheria ya Kristo nyumbani? (b) Watoto wanahitaji nini kutoka kwa wazazi wao, na wazazi fulani wahitaji kushinda vizuizi vipi ili kuutoa?

      5 Mtume Paulo aliandika hivi: “Enyi waume, wapendeni wake zenu, kama Kristo naye alivyolipenda Kanisa, akajitoa kwa ajili yake.” (Waefeso 5:25) Mume amwigapo Kristo na kumtendea mkeye kwa upendo na uelewevu, mume hutimiza sehemu ya maana ya sheria ya Kristo. Zaidi, Yesu aliwaonyesha watoto wadogo shauku waziwazi, akiwakumbatia, akiweka mikono yake juu yao, na kuwabariki. (Marko 10:16) Wazazi wanaotimiza sheria ya Kristo pia huonyesha watoto wao shauku. Ni kweli, kuna wazazi wanaoliona kuwa jambo gumu kuiga kielelezo cha Yesu katika jambo hili. Wengine hawana mwelekeo wa kuonyesha hisia waziwazi. Wazazi, msiruhusu fikira hizo ziwazuie kuwaonyesha watoto wenu upendo mnaohisi kwao! Haitoshi kwako kujua kwamba unawapenda watoto wako. Wao wapaswa kujua hilo pia. Na hawatajua isipokuwa utafute njia za kuonyesha upendo wako.—Linganisha Marko 1:11.

      6. (a) Je, watoto wanahitaji kanuni za wazazi, na kwa nini wajibu hivyo? (b) Watoto wahitaji kuelewa sababu gani ya msingi ya kuwa na kanuni za nyumbani? (c) Ni hatari gani zinazoepukwa sheria ya Kristo ieneapo nyumbani?

      6 Wakati uleule, watoto wanahitaji mipaka, jambo ambalo lamaanisha kwamba wazazi wao wanahitaji kuweka kanuni na nyakati nyingine kuzitekeleza kanuni hizo kwa kutia nidhamu. (Waebrania 12:7, 9, 11) Hata hivyo, lazima watoto wasaidiwe hatua kwa hatua kuona sababu ya msingi ya kanuni hizo: wazazi wao wawapenda. Nao lazima wajifunze kuwa upendo ndio sababu yao bora ya kuwatii wazazi wao. (Waefeso 6:1; Wakolosai 3:20; 1 Yohana 5:3) Mradi wa mzazi mwenye utambuzi ni kuwafundisha wachanga kutumia ‘nguvu zao za kufikiri’ ili hatimaye waweze kufanya maamuzi mazuri wakiwa peke yao. (Warumi 12:1, NW; linganisha 1 Wakorintho 13:11.) Kwa upande mwingine, kanuni hazipasi kuwa nyingi sana au nidhamu kuwa kali sana. Paulo asema hivi: “Ninyi akina baba, msiwachokoze watoto wenu, wasije wakakata tamaa.” (Wakolosai 3:21; Waefeso 6:4) Sheria ya Kristo ieneapo nyumbani, hakuna nafasi ya nidhamu itolewayo kukiwa na hasira isiyodhibitiwa au usemi wa kuumiza na wenye kudhuru. Katika nyumba ya aina hiyo, watoto huhisi wakiwa wenye usalama na wenye kujengwa, si wenye kulemezwa au kuvunjiwa heshima.—Linganisha Zaburi 36:7.

      7. Ni katika njia gani makao ya Betheli yawezavyo kuandaa kielelezo kwa habari ya kuweka kanuni nyumbani?

      7 Watu fulani ambao wametembelea makao ya Betheli ulimwenguni pote wanasema kwamba hayo ni vielelezo vizuri vya usawaziko kwa habari ya kanuni kwa ajili ya familia. Ingawa makao ya Betheli huwa na watu wazima, mashirika hayo hutenda kama familia.a Utendaji-kazi wa Betheli ni wenye utata na huhitaji idadi kadhaa ya kanuni—bila shaka nyingi kuliko zihitajiwazo na familia ya kawaida. Hata hivyo, wazee waongozao katika makao, ofisi, na kazi za viwanda vya Betheli, hujitahidi kutumia sheria ya Kristo. Wao huona kuwa mgawo wao si kupanga kazi tu bali pia kuendeleza maendeleo ya kiroho na “shangwe ya Yehova” miongoni mwa wafanyakazi wenzao. (Nehemia 8:10, NW) Kwa hiyo, wao hujitahidi kufanya mambo katika njia ifaayo na yenye kutia moyo na kujaribu kuwa wenye kukubali sababu. (Waefeso 4:31, 32) Si ajabu familia za Betheli hujulikana kwa sababu ya mtazamo wazo wenye shangwe!

      Katika Kutaniko

      8. (a) Mradi wetu kutanikoni uwe nini sikuzote? (b) Ni zipi baadhi ya hali ambazo chini yazo watu fulani wameomba wapewe kanuni au wamejaribu kufanya kanuni?

      8 Katika kutaniko ni mradi wetu vilevile kujengana kwa roho ya upendo. (1 Wathesalonike 5:11) Kwa hiyo Wakristo wote wapaswa kuwa waangalifu wasiongezee mizigo ya wengine kwa kujitwalia daraka la kutoa maoni yao wenyewe katika mambo ya uchaguzi wa kibinafsi. Nyakati nyingine, watu fulani huandikia Watch Tower Society wakiomba wapewe kanuni juu ya mambo kama ni maoni gani wapaswayo kuwa nayo juu ya filamu, vitabu, na hata vichezeo hususa. Walakini, Sosaiti haikupewa mamlaka ya kuchunguza mambo hayo na kutoa maamuzi juu yayo. Katika visa vilivyo vingi, hayo ni mambo ambayo kila mtu mmoja-mmoja au kichwa cha familia apaswa kuamua, ikitegemea kupenda kwake kanuni za Biblia. Wengine huelekea kugeuza madokezo na miongozo ya Sosaiti kuwa kanuni. Kwa kielelezo, katika toleo la Mnara wa Mlinzi la Machi 15, 1996, kulikuwa na makala nzuri iwatiayo moyo wazee kuwafanyia washiriki wa kutaniko ziara za uchungaji za kawaida. Je, kusudi lilikuwa kuweka kanuni? La. Ingawa wale wawezao kufuata madokezo hayo hupata manufaa mengi, wazee fulani hawawezi kufanya hivyo. Vivyo hivyo, ile makala “Maswali Kutoka kwa Wasomaji” katika toleo la Mnara wa Mlinzi la Aprili 1, 1995, ilionya dhidi ya kupunguza adhama ya pindi ya ubatizo kwa kufanya mambo kupita kiasi, kama karamu zisizodhibitiwa au kupanga misherehekeo. Wengine wametumia shauri hilo komavu kupita kiasi, hata wakiweka kanuni kwamba kutuma kadi ya kutia moyo kwenye pindi hiyo kungekuwa kosa!

      9. Kwa nini ni jambo la maana kwamba tuepuke kuwa wenye kuchambuana au kuhukumiana kupita kiasi?

      9 Fikiria pia, kwamba ikiwa “sheria kamilifu iliyo ya uhuru” itaenea miongoni mwetu, lazima tukubali kwamba si dhamiri zote za Wakristo zinazofanana. (Yakobo 1:25) Je, tuudhike watu wakiwa na machaguo ambayo hayakiuki kanuni za Kimaandiko? La. Kufanya kwetu hivyo kutakuwa jambo lisababishalo migawanyiko. (1 Wakorintho 1:10) Paulo, alipokuwa akituonya dhidi ya kuhukumu Mkristo mwenzetu, alisema hivi: “Kwa bwana wake mwenyewe yeye husimama au huanguka. Naam, atasimamishwa, kwa kuwa Bwana aweza kumsimamisha.” (Warumi 14:4) Tusemapo dhidi ya mmoja na mwenzake juu ya mambo yapaswayo kuachiwa dhamiri ya mtu mmoja-mmoja twaingia hatarini mwa kumchukiza Mungu.—Yakobo 4:10-12.

      10. Ni nani ambao wamepewa mgawo wa kulinda kutaniko, nasi tuwaungeje mkono?

      10 Acheni tukumbuke, pia, kwamba wazee wamepewa mgawo wa kulichunga kundi la Mungu. (Matendo 20:28) Wapo ili wasaidie. Twapaswa kuhisi tukiwa huru kuwafikia ili kupata shauri, kwa kuwa wao ni wanafunzi wa Biblia nao wajua yale ambayo yamezungumziwa katika fasihi za Watch Tower Society. Wazee waonapo mwenendo ambao yamkini utaelekeza kwenye ukiuko wa kanuni za Kimaandiko, wao hutoa bila hofu shauri linalohitajiwa. (Wagalatia 6:1) Washiriki wa kutaniko hufuata sheria ya Kristo kwa kushirikiana na wachungaji hao wapendwa, waongozao miongoni mwao.—Waebrania 13:7.

      Wazee Hutumia Sheria ya Kristo

      11. Wazee hutumiaje sheria ya Kristo kutanikoni?

      11 Wazee wanatamani kuitimiza sheria ya Kristo kutanikoni. Wao huongoza katika kuhubiri habari njema, kufundisha kutokana na Biblia ili wafikie mioyo na, wakiwa wachungaji wenye upendo na upole, husema na “nafsi zilizoshuka moyo.” (1 Wathesalonike 5:14, NW) Wao huepuka mitazamo isiyo ya Kikristo iliyopo katika dini nyingi sana za Jumuiya ya Wakristo. Ni kweli, ulimwengu huu unazorota upesi, na sawa na Paulo, huenda wazee wakahisi hangaiko kwa ajili ya kundi; lakini wao hudumisha usawaziko watendapo kulingana na mahangaiko hayo.—2 Wakorintho 11:28.

      12. Mkristo amfikiapo mzee ili kupata msaada, mzee aweza kuitikiaje?

      12 Kwa kielelezo, huenda Mkristo akataka kumwona mzee kuhusu jambo la maana ambalo halishughulikiwi na rejezo la moja kwa moja la Kimaandiko au lihitajilo kusawazisha kanuni tofauti za Kikristo. Huenda ikawa amepandishwa cheo kazini kilicho na mshahara mkubwa zaidi lakini chenye madaraka makubwa zaidi. Au baba asiyeamini wa Mkristo mchanga huenda akawa anamdai mwanawe mambo ambayo yangeweza kuathiri huduma yake. Katika hali hizo mzee huepuka kutoa maoni ya kibinafsi. Badala ya hivyo, yamkini atafungua Biblia na kumsaidia mtu huyo kusababu juu ya kanuni zihusikazo. Huenda akatumia kichapo Watch Tower Publications Index, ikiwa chapatikana, ili kupata lile ambalo “mtumwa mwaminifu mwenye akili” amesema juu ya habari hiyo katika kurasa za Mnara wa Mlinzi na vichapo vingine. (Mathayo 24:45) Namna gani ikiwa baadaye Mkristo huyo afanya uamuzi usioonekana kuwa wenye hekima machoni pa mzee huyo? Ikiwa uamuzi haupingi moja kwa moja kanuni au sheria za Biblia, huyo Mkristo atagundua kwamba huyo mzee anatambua haki ya mtu mmoja-mmoja ya kufanya uamuzi huo, akijua kwamba “kila mtu atalichukua furushi lake mwenyewe.” Hata hivyo, huyo Mkristo apaswa kukumbuka kwamba “cho chote apandacho mtu, ndicho atakachovuna.”—Wagalatia 6:5, 7.

      13. Badala ya kutoa majibu ya moja kwa moja au kutoa maoni yao wenyewe, kwa nini wazee huwasaidia wengine kusababu juu ya mambo?

      13 Kwa nini mzee mwenye uzoefu atenda hivyo? Kwa angalau sababu mbili. Kwanza, Paulo aliliambia kutaniko moja kuwa hakuwa ‘bwana-mkubwa juu ya imani yalo.’ (2 Wakorintho 1:24, NW) Huyo mzee, kwa kumsaidia ndugu yake kusababu kwa kutumia Maandiko na kufanya uamuzi wake mwenyewe wenye kutegemea ujuzi, anaiga mtazamo wa Paulo. Yeye anatambua kwamba mamlaka yake ina mipaka, sawa na Yesu alivyotambua kwamba kulikuwa na mipaka katika mamlaka yake. (Luka 12:13, 14; Yuda 9, linganisha NW.) Wakati uleule, wazee hutoa msaada kwa utayari, hata shauri kali la Kimaandiko lihitajiwapo. Pili, yeye anamzoeza Mkristo mwenzake. Mtume Paulo alisema hivi: “Chakula kigumu ni cha watu wazima, ambao akili zao, kwa kutumiwa, zimezoezwa kupambanua mema na mabaya.” (Waebrania 5:14) Basi, ili kukua kufikia ukomavu, lazima tutumie akili zetu, si kwa kutegemea sikuzote mtu mwingine atupe majibu. Mzee, kwa kumwonyesha Mkristo mwenzake jinsi ya kusababu kwa kutumia Maandiko, kwa njia hiyo anamsaidia kufanya maendeleo.

      14. Walio wakomavu waweza kuonyeshaje kwamba wanamtumaini Yehova?

      14 Twaweza kuwa na imani kwamba Yehova Mungu kupitia roho yake takatifu atachochea mioyo ya waabudu wa kweli. Hivyo, Wakristo wakomavu huvutia mioyo ya ndugu zao, wakiwasihi, kama alivyofanya mtume Paulo. (2 Wakorintho 8:8; 10:1; Filemoni 8, 9) Paulo alijua kwamba ni wasio waadilifu hasa, wala si waadilifu, wahitajio sheria zinazotia ndani kila kitu ili kuwafanya waenende ifaavyo. (1 Timotheo 1:9) Alionyesha imani katika ndugu zake, wala si hali ya kuwashuku au ukosefu wa kuwatumaini. Aliandikia hivi kutaniko moja: “Tuna uhakika katika Bwana kuhusu nyinyi.” (2 Wathesalonike 3:4, NW) Imani, tumaini na uhakika wa Paulo kwa hakika ulichangia sana kuwachochea Wakristo hao. Wazee na waangalizi wasafirio leo wana makusudi yayo hayo. Wanaume hao waaminifu wanaburudisha kama nini, huku wakilichunga kundi la Mungu kwa upendo!—Isaya 32:1, 2; 1 Petro 5:1-3.

      Kuishi Kulingana na Sheria ya Kristo

      15. Ni yapi baadhi ya maswali tuwezayo kujiuliza ili kuona ikiwa tunaitumia sheria ya Kristo katika uhusiano wetu pamoja na ndugu zetu?

      15 Sote twahitaji kujichunguza kwa ukawaida tuone ikiwa tunaishi kulingana na, na kuiendeleza sheria ya Kristo. (2 Wakorintho 13:5) Kwa kweli, sisi sote twaweza kunufaika kwa kuuliza: ‘Je, mimi ni mwenye kujenga au mwenye kuchambua? Je, mimi ni mwenye usawaziko au mwenye kupita kiasi? Je, mimi huonyesha wengine ufikirio au husisitizia haki zangu mwenyewe?’ Mkristo hajaribu kuamuru ni hatua zipi ambazo ndugu yake anapaswa au hapaswi kuchukua katika mambo ambayo hayashughulikiwi kihususa katika Biblia.—Warumi 12:1; 1 Wakorintho 4:6.

      16. Twaweza kuwasaidiaje wale walio na maoni yasiyofaa juu yao wenyewe, kwa njia hiyo tukitimiza sehemu ya maana ya sheria ya Kristo?

      16 Katika nyakati hizi za hatari, ni jambo la maana kwetu kutafuta njia za kutiana moyo. (Waebrania 10:24, 25; linganisha Mathayo 7:1-5.) Tuwatazamapo ndugu na dada zetu, je, sifa zao nzuri si za maana zaidi kwetu kuliko udhaifu wao mbalimbali? Machoni pa Yehova, kila mmoja ni mwenye thamani. Kwa kusikitisha, si wote wahisio hivyo, hata juu yao wenyewe. Wengi huelekea kuona tu makosa na kutokamilika kwao binafsi. Ili kuwatia moyo hao—na wengine—je, twaweza kujaribu kuongea na mtu mmoja au wawili kwenye kila mkutano, tukiwajulisha ni kwa nini twathamini kuwapo kwao na mchango wa maana watoao kutanikoni? Ni furaha kama nini kupunguza mzigo wao kwa njia hiyo na hivyo kutimiza sheria ya Kristo!—Wagalatia 6:2.

      Sheria ya Kristo Inafanya Kazi!

      17. Unaiona sheria ya Kristo ikifanya kazi katika njia zipi tofauti katika kutaniko lako?

      17 Sheria ya Kristo inafanya kazi katika kutaniko la Kikristo. Twaiona kila siku—Mashahidi wenzetu washirikipo kwa bidii habari njema, wafarijianapo na kutiana moyo, wang’ang’anapo kumtumikia Yehova licha ya matatizo yaliyo magumu zaidi, wazazi wajitahidipo kulea watoto wao ili wampende Yehova kwa mioyo yenye shangwe, waangalizi wafundishapo Neno la Mungu kwa upendo na uchangamfu, wakihimiza kundi liwe na bidii yenye kuwaka ya kumtumikia Yehova milele. (Mathayo 28:19, 20; 1 Wathesalonike 5:11, 14) Sisi mmoja-mmoja tuitumiapo sheria ya Kristo maishani mwetu wenyewe, moyo wa Yehova hushangalia kama nini! (Mithali 23:15) Yeye ataka wote wapendao sheria yake kamilifu waishi milele. Katika Paradiso ijayo, tutaona wakati ambapo wanadamu watakuwa wakamilifu, wakati usio na wavunjaji wa sheria, na wakati ambapo kila mwelekeo wa mioyo yetu utadhibitiwa. Ni thawabu iliyoje ya kuishi kulingana na sheria ya Kristo!

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki