-
Jiji la Kale la Yerusalemu Liliharibiwa Mwaka Gani?—Sehemu ya PiliMnara wa Mlinzi—2011 | Novemba 1
-
-
● Mabamba ya wataalamu wa nyota.
Mabamba hayo ni nini? Hayo ni mabamba ya kikabari yenye maelezo ya mpangilio wa jua, mwezi, sayari, na nyota, pamoja na habari za kihistoria kama vile mwaka wa utawala wa mfalme hususa. Kwa mfano, maandishi ya wataalamu wa nyota yaliyo hapa chini yanaonyesha kupatwa kwa mwezi kulikotokea mwezi wa kwanza wa mwaka wa kwanza wa utawala wa Mfalme Mukin-zeri.11
Wataalamu wamesema nini? Wanakubali kwamba Wababiloni walikuwa na chati na orodha nyingi sana waliyotumia kufanya hesabu ili kubashiri wakati ambapo yaelekea mwezi ungepatwa.12
Lakini je, Wababiloni wangeweza kuhesabu kwa kurudi nyuma ili kujua wakati ambapo kupatwa kwa mwezi kulitokea wakati uliopita? Profesa John Steele anasema: “Inawezekana kwamba baadhi ya ubashiri wa kwanza kabisa ulitolewa kwa kuhesabu kurudi nyuma wakati maandishi hayo yalipokuwa yakiandikwa.” (Italiki ni zetu.)13 Profesa David Brown, anayeamini kwamba chati hizo kuhusu mpangilio wa mwezi, sayari, na nyota zilikuwa na ubashiri uliokuwa umetolewa muda mfupi kabla ya matukio yaliyotajwa kutokea, anasema inawezekana kwamba baadhi ya “hesabu hizo zilifanywa kwa kurudi nyuma na waandishi katika karne ya nne Kabla ya Kristo na karne za baadaye.”14 Ikiwa hesabu hizo zilifanywa kwa kurudi nyuma, je, zinaweza kutegemeka kabisa bila kuungwa mkono na uthibitisho mwingine?
Hata kama kupatwa kwa mwezi kulitokea tarehe fulani, je, hilo linamaanisha kwamba habari za kihistoria ambazo mwandishi anahusianisha na tarehe hiyo ni sahihi? Si lazima iwe hivyo. Msomi R. J. van der Spek anaeleza: “Walioandika habari hizo walikuwa wataalamu wa nyota bali si wanahistoria.” Anaeleza kwamba habari za kihistoria kwenye sehemu fulani za mabamba hayo ni “za kijuujuu tu,” na kuonya kwamba ni lazima “zitumiwe kwa tahadhari.”15
Maandishi hayo yanaonyesha nini? Kwa mfano, fikiria bamba la VAT 4956. Mstari wa kwanza katika bamba hilo unasema: “Mwaka wa 37 wa Nebukadneza, mfalme wa Babiloni.”16 Kisha, linaeleza kwa undani mahali ambapo mwezi na sayari zilikuwa angani kwa kulinganishwa na nyota na makundi ya nyota. Pia, lina habari kuhusu tukio moja la kupatwa kwa mwezi. Wasomi wanasema kwamba mipangilio hiyo ya mwezi, sayari, na nyota ilitukia mwaka wa 568/567 K.W.K., kumaanisha kwamba mwaka wa 18 wa utawala wa Nebukadneza wa Pili ulikuwa 587 K.W.K., wakati alipoharibu jiji la Yerusalemu. Lakini je, marejeo hayo yanayotegemea uchunguzi wa mpangilio wa mwezi, sayari, na nyota yanaonyesha tu mwaka wa 568/567 K.W.K.?
Bamba hilo linataja tukio la kupatwa kwa mwezi ambalo hesabu za wataalamu wa nyota zinaonyesha lilitokea siku ya 15 ya mwezi wa tatu, au Simanu, katika kalenda ya Babiloni. Hapana shaka kwamba tukio hilo la kupatwa kwa mwezi lilitokea mwezi huo wa Simanu, tarehe inayolingana na Julai 4 (katika kalenda ya Yulio), mwaka wa 568 K.W.K. Hata hivyo, kulikuwa na tukio lingine la kupatwa kwa mwezi miaka 20 mapema, mnamo Julai 15, mwaka wa 588 K.W.K.17
Ikiwa mwaka 588 K.W.K. ndio mwaka wa 37 wa Nebukadneza wa Pili, basi mwaka wa 18 wa utawala wake ulikuwa 607 K.W.K.—mwaka ambao jiji la Yerusalemu liliharibiwa kulingana na mfuatano wa matukio ya Biblia! (Ona mfuatano wa matukio ulio hapa chini.) Lakini je, bamba la VAT 4956 lina habari zaidi zinazounga mkono mwaka wa 607 K.W.K.?
Mbali na tukio la kupatwa kwa mwezi ambalo limetajwa, bamba hilo lina rekodi 13 za uchunguzi wa mwezi, na rekodi 15 za uchunguzi wa sayari. Rekodi hizo zinaonyesha mahali ambapo mwezi au sayari zilikuwa angani kwa kulinganishwa na nyota au makundi ya nyota.18 Pia, kuna vipindi vinane vya wakati, kati ya kuchomoza na kutua kwa jua au mwezi.18a
Kwa sababu habari kuhusu mahali ambapo mwezi ulikuwa angani kwa kulinganishwa na nyota nyingine zinategemeka sana, watafiti wamechunguza kwa makini rekodi hizo 13 kwenye bamba la VAT 4956. Walichunguza rekodi hizo kwa kutumia programu fulani ya kompyuta inayoweza kuonyesha mipangilio ya mwezi, sayari, na nyota katika tarehe fulani wakati uliopita.19 Uchunguzi wao ulifunua nini? Ingawa si rekodi zote kuhusu mipangilio hiyo zinazolingana na mwaka wa 568/567 K.W.K., zile rekodi 13 zinapatana na mahali ambapo mwezi ulikuwa angani miaka 20 mapema, yaani, mwaka wa 588/587 K.W.K.
Kuna sehemu moja ya bamba la 4956 ambayo imeonyeshwa kwenye kurasa hizi inayoonyesha kwamba mpangilio wa mwezi na nyota nyingine ulilingana na mwaka wa 588 K.W.K. vizuri zaidi kuliko mwaka wa 568 K.W.K. Mstari wa 3 wa bamba hilo unasema kwamba mwezi ulikuwa mahali fulani angani mnamo “usiku wa tarehe 9 [mwezi wa Nisanu].” Hata hivyo, wasomi walioonyesha mara ya kwanza kuwa mpangilio huo ulitokea mwaka wa 568 K.W.K. walisema kwamba katika mwaka huo wa 568 K.W.K., mwezi ulikuwa mahali hapo “tarehe 8 ya mwezi wa Nisanu, bali si tarehe 9.” Ili waunge mkono mwaka huo wa 568 K.W.K., walisema kwamba mwandishi aliandika kimakosa nambari “9” badala ya “8.”20 Lakini mahali ambapo mwezi ulikuwa kulingana na mstari wa 3 panalingana kabisa na Nisanu 9, mwaka wa 588 K.W.K.21
Kwa wazi, habari za wataalamu wa nyota katika bamba la VAT 4956 zinaonyesha kuwa mwaka wa 588 K.W.K. ndio mwaka wa 37 wa Nebukadneza wa Pili. Kwa hiyo, jambo hilo linaunga mkono mwaka wa 607 K.W.K. kuwa mwaka ambao jiji la Yerusalemu liliharibiwa—kama Biblia inavyoonyesha.
-
-
Jiji la Kale la Yerusalemu Liliharibiwa Mwaka Gani?—Sehemu ya PiliMnara wa Mlinzi—2011 | Novemba 1
-
-
[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 24]
MAANDISHI YA WATAALAMU WA NYOTA KWENYE BAMBA LA BM 32238
Bamba hili lina habari kuhusu matukio ya kupatwa kwa mwezi, lakini habari hizo ziliandikwa baada ya tukio la mwisho la kupatwa kwa mwezi, lililotokea miaka 400 hivi baada ya tukio la kwanza. Kwa kuwa mwandishi wa matukio hayo hakuyaona yote, huenda alifanya hesabu ili kuamua wakati matukio yaliyotangulia tukio la mwisho yalipotokea. Lakini bila uthibitisho unaounga mkono maamuzi yake, huenda matokeo ya hesabu zake yasiwe chanzo chenye kutegemeka kuhusu mfuatano wa matukio.
[Hisani]
© The Trustees of the British Museum
-