Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Shamba ‘Jeupe kwa Ajili ya Kuvunwa’
    Mnara wa Mlinzi—2007 | Aprili 15
    • Neil, Mhindi wa kabila la Wayuu ambaye aliishi Manaure, alizaliwa akiwa na ulemavu fulani. Neil alimlaumu Mungu na kushuka moyo hivi kwamba akajaribu kujiua. Shahidi mmoja ambaye alihubiri nyumba kwa nyumba alipokuwa akitembelea miji mbalimbali kwa sababu za kikazi alizungumza na Neil kuhusu Ufalme wa Yehova. Neil alikuwa na umri wa miaka 14 tu. Alipotambua kwamba Neil anapendezwa, Shahidi huyo alianza kujifunza Biblia pamoja naye. Neil alifurahi kujifunza kuhusu utu wenye upendo wa Yehova, naye akakata kauli kwamba si Mungu aliyemletea mateso. Aliguswa moyo sana aliposoma ahadi ya Mungu ya kuifanya dunia kuwa paradiso, na kwamba magonjwa hayatakuwapo tena!—Isaya 33:24; Mathayo 6:9, 10.

      Wakati huo, familia ya Neil ilikuwa ikizozana na familia nyingine. Watu wa ukoo wa Neil walifanya matambiko fulani ya kabila lao ili kujaribu kujilinda. Neil anakumbuka hivi: “Mwanzoni, niliogopa kuijulisha familia yangu kuhusu imani yangu mpya, hasa wazee wa familia yetu ambao wanaheshimiwa sana.” Wazazi wa Neil walikasirika waliposikia kwamba hatafuata kamwe imani ambazo hazipatani na maandiko wala kushiriki katika desturi zinazohusiana na pepo. Halafu Neil akahamia Ríohacha na kuanza kushirikiana na kutaniko la huko. Baadaye alibatizwa. Mwaka wa 1993 aliwekwa rasmi kuwa mtumishi wa huduma, na miaka mitatu baadaye akawa painia wa kawaida. Kisha, mwaka wa 1997 akawekwa rasmi kuwa mzee wa kutaniko. Mwaka wa 2000, alipanua huduma yake na kuwa painia wa pekee.

      Pia, fikiria kisa cha Teresa, ambaye ni wa kabila la Wayuu. Alianza kujifunza Biblia pamoja na Mashahidi. Daniel, ambaye aliishi naye bila kufunga ndoa, alimdhihaki na kumtendea vibaya kimwili pamoja na watoto wao watatu. Hata ingawa baadaye alikubali kujifunza Biblia pamoja na Teresa, mara nyingi alienda kulewa pamoja na marafiki wake, na nyakati nyingine alikaa huko kwa siku nne au tano. Familia yake ilibaki maskini. Teresa aliendelea kujifunza kwa uaminifu na kuhudhuria mikutano ya Kikristo. Hilo lilimsaidia Daniel kuona umuhimu wa kujifunza Biblia. Kisha, mmoja wa watoto wake alianguka katika maji yaliyokuwa yakichemka na akachomeka. Mtoto huyo alikufa kutokana na majeraha aliyopata. Zaidi ya kuvumilia huzuni kubwa ya kufiwa na mwana wake, Teresa alisukumwa na marafiki na majirani kushiriki katika desturi za mazishi ambazo hazipatani na maandiko.

      Katika kipindi hicho kigumu, Teresa na mume wake walipokea msaada wenye kutia moyo na faraja kutoka kwa washiriki wa makutaniko ya karibu. Baada ya mazishi, waliendelea kutembelewa na kufarijiwa na washiriki wa kutaniko la karibu la Kiwayuunaiki. Alipoona upendo wa Kikristo ukionyeshwa kwa matendo, Daniel alichochewa kufanya maendeleo ya kiroho. Aliacha kunywa pombe na kumtesa Teresa. Daniel na Teresa walifunga ndoa, naye Daniel akaanza kujitahidi kuitafutia familia yake riziki. Walifanya maendeleo ya kiroho na wakabatizwa mwaka wa 2003. Wote wawili wanaongoza mafunzo kadhaa ya Biblia. Kwa sababu ya ushahidi mzuri ambao Teresa aliwatolea washiriki wa familia yake, sasa watu wake wa ukoo wanawasikiliza Mashahidi wanapowatembelea. Mpwa mmoja wa kiume wa Daniel ni mhubiri ambaye hajabatizwa, na wapwa wake wawili wa kike wanajifunza Biblia na kuhudhuria mikutano ya kutaniko. Shemeji ya Teresa, ambaye mwana wake pia alikufa katika msiba, na familia yake wanapendezwa na funzo la Biblia.

  • Shamba ‘Jeupe kwa Ajili ya Kuvunwa’
    Mnara wa Mlinzi—2007 | Aprili 15
    • Shamba Lenye Kusitawi

      Uribia ni mji ulio kilomita 100 hivi kaskazini-mashariki ya Ríohacha. Kutaniko la Uribia Wayuu lina wahubiri 16 wa Ufalme, wengi wao wanajitahidi zaidi kuwahubiria Wahindi wanaoishi katika maeneo ya mashambani. Mmoja wa wazee wa kutaniko hilo anasema hivi kuhusu safari moja kama hiyo ya kutoa ushahidi: “Tulitembelea shamba moja lenye nyumba 12 hivi ambazo ni fupi na zenye madirisha madogo. Mbele ya kila nyumba kuna paa tambarare lililojengwa kwa yotojolo, shina la ndani la mmea wa dungusi-kakati. Katika nyumba hizo, familia na wageni wanalindwa kutokana na jua kali. Tulifurahi kuona kwamba watu wengi walipendezwa sana, basi tukafanya mipango ya kurudi ili kuanzisha mafunzo ya Biblia. Tuliporudi, tuligundua kwamba wengi hawajui kusoma wala kuandika. Walituambia kwamba kuna shule moja iliyofungwa kwa sababu ya ukosefu wa pesa. Kwa fadhili, msimamizi wa shule hiyo alituruhusu kutumia darasa moja kuwafundisha watu kusoma na kuandika na kuongoza mafunzo ya Biblia. Watu sita wa kabila la Wayuu wamejifunza kusoma na kuandika na wanafanya maendeleo katika funzo lao la Biblia. Tunaguswa moyo na uthamini ambao wanaonyesha. Kwa hiyo, tunapanga kufanya mikutano kwenye shamba hilo.”

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki