-
Mtegemee Yehova Ili Kupata FarajaMnara wa Mlinzi—1996 | Novemba 1
-
-
Mtegemee Yehova Ili Kupata Faraja
“Na Mungu mwenye [“apaye,” “NW”] saburi na faraja awajalie kunia mamoja ninyi kwa ninyi, kwa mfano wa Kristo Yesu.”—WARUMI 15:5.
1. Kwa nini kila siku huleta uhitaji mkubwa zaidi wa kupata faraja?
KILA siku inayopita huleta uhitaji unaoongezeka wa kupata faraja. Kama vile mwandikaji mmoja wa Biblia alivyoona miaka zaidi ya 1,900 iliyopita, “viumbe vyote pia vinaugua pamoja, navyo vina utungu pamoja hata sasa.” (Warumi 8:22) Katika wakati wetu ‘kuugua’ na “utungu” umekuwa mkubwa zaidi kuliko wakati mwingine wowote. Tangu Vita ya Ulimwengu I, wanadamu wamekuwa na tatizo moja baada ya jingine kwa namna ya vita, uhalifu, na misiba ya asili ambayo mara nyingi huhusianishwa na kule kuitumia dunia vibaya kwa mwanadamu.—Ufunuo 11:18.
2. (a) Ni nani astahiliye kulaumiwa zaidi kwa ajili ya ole za wanadamu za sasa? (b) Ni uhakika gani hutupa sisi msingi wa faraja?
2 Kwa nini kumekuwa na kuteseka kwingi sana katika wakati wetu? Ikifafanua kutupwa kwa Shetani kutoka mbinguni kufuatia kuzaliwa kwa Ufalme katika 1914, Biblia yajibu hivi: “Ole wa nchi na bahari! kwa maana yule Ibilisi ameshuka kwenu mwenye ghadhabu nyingi, akijua ya kuwa ana wakati mchache tu.” (Ufunuo 12:12) Uthibitisho ulio wazi wa utimizo wa unabii huo humaanisha kwamba karibu tumefikia mwisho wa utawala mwovu wa Shetani. Yafariji kama nini kujua kwamba karibuni uhai duniani utarudia ile hali yenye amani iliyokuwako kabla ya Shetani kuwaongoza wazazi wetu wa kwanza kwenye uasi!
3. Ni lini ambapo wanadamu hawakuhitaji faraja?
3 Mwanzoni, Muumba wa mwanadamu aliandaa shamba zuri likiwa makao ya wenzi wa kwanza wa kibinadamu. Lilikuwa katika eneo liitwalo Edeni, likimaanisha “Mapendezi” au “Raha.” (Mwanzo 2:8, NW, kielezi-chini) Zaidi, Adamu na Hawa walikuwa na afya kamilifu, wakiwa na taraja la kutokufa kamwe. Ebu wazia zile nyanja nyingi ambazo katika hizo wangaliweza kusitawisha uwezo wao mbalimbali—ulimaji wa bustani, usanii, ujenzi, muziki. Wazia pia zile kazi zote za uumbaji ambazo wangaliweza kujifunza huku wakitimiza utume wao wa kuitiisha dunia na kuifanya iwe paradiso. (Mwanzo 1:28) Kwa kweli, maisha ya Adamu na Hawa yangalikuwa yamejawa na mapendezi na raha, wala si na hali ya kuugua na ya utungu. Kwa wazi, wao wasingalikuwa na uhitaji wa faraja.
4, 5. (a) Kwa nini Adamu na Hawa walianguka mtihani wa utii? (b) Wanadamu walikujaje kuhitaji faraja?
4 Hata hivyo, walichohitaji Adamu na Hawa kilikuwa ni kukuza upendo wenye kina na uthamini kumwelekea Baba yao wa kimbingu mwenye fadhili. Upendo huo ungaliwahamasisha kumtii Mungu chini ya hali zote. (Linganisha Yohana 14:31.) Kwa kuhuzunisha, wazazi wetu wawili wa kwanza walishindwa kumtii Mwenye Enzi Kuu wao wa haki, Yehova. Badala ya hivyo, walijiruhusu waje chini ya utawala mwovu wa malaika aliyeshushwa, Shetani Ibilisi. Shetani ndiye aliyemshawishi Hawa atende dhambi na kula tunda lililokatazwa. Kisha Adamu akatenda dhambi wakati ambapo yeye pia alikula tunda la mti ambao kuuhusu Mungu alikuwa ameonya waziwazi hivi: “Siku utakapokula matunda ya mti huo utakufa hakika.”—Mwanzo 2:17.
5 Kwa njia hiyo, hao wenzi wenye dhambi wakaanza kufa. Alipokuwa akitangaza hukumu ya kifo, Mungu alitaarifu hivi pia kwa Adamu: “Ardhi imelaaniwa kwa ajili yako; kwa uchungu utakula mazao yake siku zote za maisha yako; michongoma na miiba itakuzalia, nawe utakula mboga za kondeni.” (Mwanzo 3:17, 18) Hivyo Adamu na Hawa wakapoteza lile taraja la kuifanya dunia ambayo haikuwa imelimwa iwe paradiso. Wakiwa wamefukuzwa kutoka Edeni, walilazimika kutumia nishati zao ili kujitahidi kupata chakula kutoka kwenye ardhi iliyolaaniwa. Wazao wao, wakiwa wamerithi hali hiyo yenye dhambi na kufa, wakaja kuwa na uhitaji mkubwa wa kupata faraja.—Warumi 5:12.
Ahadi Yenye Kufariji Yatimizwa
6. (a) Ni ahadi gani yenye kufariji ambayo Mungu alitoa baada ya wanadamu kutumbukia katika dhambi? (b) Lameki alitoa unabii gani juu ya faraja?
6 Alipokuwa akimhukumu mwanzilishi wa uasi wa mwanadamu, Yehova alithibitika kuwa ‘Mungu apaye faraja.’ (Warumi 15:5) Alifanya hivyo kwa kuahidi kutuma “mbegu” ambayo hatimaye ingekomboa wazao wa Adamu kutokana na matokeo yenye msiba ya uasi wa Adamu. (Mwanzo 3:15) Baada ya muda, Mungu aliandaa pia mimweko ya kimbele ya ukombozi huo. Kwa kielelezo, alimpulizia Lameki, mzao wa mbali wa Adamu kupitia mwana wake Sethi, atabiri juu ya jambo ambalo mwana wa Lameki angefanya: “Huyu ndiye atakayetufariji kwa kazi yetu na kwa taabu ya mikono yetu katika nchi aliyoilaani BWANA.” (Mwanzo 5:29) Kwa kupatana na ahadi hiyo, mvulana huyo aliitwa Noa, jina lielewekalo kumaanisha “Pumziko” au “Kitulizo.”
7, 8. (a) Ni hali gani iliyomwongoza Yehova aghairi kwa kumuumba mwanadamu, na Yeye alikusudia kufanya nini likiwa itikio? (b) Noa aliishije kulingana na maana ya jina lake?
7 Wakati uo huo, Shetani alikuwa akipata wafuasi miongoni mwa baadhi ya malaika wa kimbingu. Hao walichukua miili ya wanadamu na kutwaa wazao wa kike wenye kuvutia wa Adamu, wawe wake. Muungano huo usio wa asili ulifisidi zaidi jamii ya kibinadamu ukatokeza jamii isiyomcha Mungu ya Wanefili, “waangushaji,” waliojaza dunia jeuri. (Mwanzo 6:1, 2, 4, 11; Yuda 6) “BWANA akaona ya kuwa maovu ya mwanadamu ni makubwa duniani . . . BWANA akaghairi kwa kuwa amemfanya mwanadamu duniani, akahuzunika moyo.”—Mwanzo 6:5, 6.
8 Yehova alikusudia kuuharibu ulimwengu huo mwovu kupitia furiko la kitufe, lakini kwanza akamwagiza Noa ajenge safina ili kuhifadhi uhai. Hivyo, jamii ya kibinadamu na aina za wanyama zikaokolewa. Noa na familia yake lazima wawe walihisi wametulizwa kama nini baada ya hilo Furiko walipokuwa wakitoka nje ya safina na kuingia dunia iliyosafishwa! Ilifariji kama nini kukuta kwamba ile laana juu ya ardhi ilikuwa imeondolewa, ikifanya utendaji wa kilimo uwe rahisi zaidi sana! Kwa kweli, unabii wa Lameki ulithibitika kuwa kweli, na Noa aliishi kulingana na maana ya jina lake. (Mwanzo 8:21) Akiwa mwabudu mwaminifu wa Mungu, Noa alitumika katika kuletea wanadamu kiasi fulani cha “faraja.” Hata hivyo, ule uvutano mwovu wa Shetani na roho wake waovu haukuishia na Furiko, nao wanadamu huendelea kuugua chini ya mzigo wenye kulemea wa dhambi, ugonjwa, na kifo.
Mtu Aliye Mkubwa Zaidi Kuliko Noa
9. Yesu Kristo amethibitikaje kuwa msaidiaji na mfariji wa wanadamu wenye kutubu?
9 Hatimaye, mwishoni mwa miaka ipatayo 4,000 ya historia ya kibinadamu, Mbegu iliyoahidiwa ikafika. Akisukumwa na upendo mkubwa kwa wanadamu, Yehova Mungu alimtuma Mwana wake mzaliwa-pekee duniani ili afe akiwa fidia kwa ajili ya jamii ya kibinadamu yenye dhambi. (Yohana 3:16) Yesu Kristo huleta kitulizo kikubwa kwa watenda-dhambi wenye kutubu wanaodhihirisha imani katika kifo chake cha kidhabihu. Wale wote wanaoweka wakfu maisha zao kwa Yehova na kuwa wanafunzi waliobatizwa wa Mwana wake hupata burudisho na faraja yenye kudumu. (Mathayo 11:28-30; 16:24) Licha ya kutokamilika kwao, wanapata shangwe nyingi katika kumtumikia Mungu wakiwa na dhamiri safi. Inawafariji kama nini kujua kwamba wakiendelea kudhihirisha imani katika Yesu, watathawabishwa kwa kupewa uhai udumuo milele! (Yohana 3:36; Waebrania 5:9) Ikiwa kwa sababu ya udhaifu wanatenda dhambi nzito, basi wana msaidiaji, au mfariji, akiwa Bwana Yesu Kristo aliyefufuliwa. (1 Yohana 2:1, 2) Kwa kuungama dhambi hizo na kwa kuchukua hatua za Kimaandiko za kuepuka kuwa wazoeaji wa dhambi, wanapata kitulizo, wakijua kwamba ‘Mungu ni mwaminifu na wa haki hata atuondolee dhambi zetu.’—1 Yohana 1:9; 3:6; Mithali 28:13.
10. Twajifunza nini kutokana na miujiza aliyofanya Yesu alipokuwa duniani?
10 Alipokuwa duniani, Yesu alileta pia burudisho kwa kuwaweka huru wale waliokuwa wamepagawa na roho waovu, kwa kutibu kila aina ya ugonjwa, na kwa kufufua wapendwa waliokufa kwenye uhai tena. Ni kweli kwamba miujiza hiyo ilikuwa na manufaa ya muda mfupi tu, kwa kuwa wale waliobarikiwa hivyo baadaye walizeeka na kufa. Hata hivyo, kwa njia hiyo Yesu alielekezea baraka za kudumu za wakati ujao atakazowamwagia wanadamu wote. Sasa akiwa Mfalme wa kimbingu mwenye uweza, karibuni atafanya mengi zaidi ya kuwafukuza roho waovu tu. Atawaweka katika abiso pamoja na kiongozi wao, Shetani, katika hali ya kutotenda. Ndipo utakapoanza ule Utawala wa Miaka Elfu wenye utukufu wa Kristo.—Luka 8:30, 31; Ufunuo 20:1, 2, 6.
11. Kwa nini Yesu alijiita “Bwana wa sabato”?
11 Yesu alisema kwamba alikuwa “Bwana wa sabato,” na mengi ya maponyo yake yalifanywa siku ya Sabato. (Mathayo 12:8-13; Luka 13:14-17; Yohana 5:15, 16; 9:14) Kwa nini? Sabato ilikuwa sehemu ya Sheria ya Mungu kwa Israeli na hivyo ilitumika ikiwa “kivuli cha mema yatakayokuwa.” (Waebrania 10:1) Zile siku sita za juma za kazi hutukumbusha juu ya miaka 6,000 iliyopita ya utumwa wa mwanadamu kwa utawala wenye uonevu wa Shetani. Siku ya Sabato mwishoni mwa juma hukumbusha lile pumziko lenye kufariji ambalo wanadamu watapata wakati wa ule Utawala wa Miaka Elfu wa Noa Mkubwa Zaidi, Yesu Kristo.—Linganisha 2 Petro 3:8.
12. Twaweza kutazamia kuona mambo gani yenye kufariji?
12 Raia wa kidunia wa utawala wa Kristo watahisi kitulizo kama nini wakati ambapo, hatimaye, watajikuta wakiwa huru kabisa kutoka katika uvutano mwovu wa Shetani! Faraja zaidi itakuja huku wakiponywa udhaifu wao mbalimbali wa kimwili, kihisia-moyo, na kiakili. (Isaya 65:17) Kisha, ebu fikiria furaha yao huku wakianza kuwakaribisha wapendwa kutoka kwa wafu! Katika njia hizo Mungu “atafuta kila chozi katika macho yao.” (Ufunuo 21:4) Huku manufaa za dhabihu ya fidia ya Yesu zitumiwapo hatua kwa hatua, raia watiifu wa Ufalme wa Mungu watakua kufikia ukamilifu, wakiwa huru kabisa kutoka katika matokeo yote mabaya ya dhambi ya Adamu. (Ufunuo 22:1-5) Kisha Shetani atafunguliwa “muda mchache.” (Ufunuo 20:3, 7) Wanadamu wote wanaotegemeza kwa uaminifu enzi kuu ya Yehova yenye haki watathawabishwa kwa kupewa uhai udumuo milele. Wazia ile shangwe na kitulizo kisichoelezeka cha ‘kuwekwa huru na kutolewa katika utumwa wa uharibifu’! Hivyo wanadamu watiifu watafurahia “uhuru wa utukufu wa watoto wa Mungu.”—Warumi 8:21.
13. Kwa nini Wakristo wote wa kweli wanahitaji faraja ambayo Mungu hupa?
13 Kwa wakati uliopo, twaendelea kupatwa na hali ya kuugua na ya utungu uwapatao wote wanaoishi katikati ya mfumo mwovu wa Shetani. Ongezeko la ugonjwa wa kimwili na miparaganyo ya kihisia-moyo huathiri aina zote za watu, kutia na Wakristo waaminifu. (Wafilipi 2:25-27; 1 Wathesalonike 5:14) Kwa kuongezea, tukiwa Wakristo mara nyingi sisi hupata dhihaka na mnyanyaso usio wa haki ambao Shetani hurundika juu yetu kwa sababu ya “kumtii Mungu kuliko wanadamu.” (Matendo 5:29) Hivyo, ikiwa tutavumilia katika kufanya mapenzi ya Mungu hadi mwisho wa ulimwengu wa Shetani, twahitaji faraja, msaada, na nguvu ambayo Yeye hupa.
Mahali pa Kupata Faraja
14. (a) Yesu alitoa ahadi gani usiku wa kutangulia kifo chake? (b) Ni nini cha lazima ikiwa tutanufaika kikamili kutokana na faraja ya roho takatifu ya Mungu?
14 Usiku wa kabla ya kifo chake, Yesu aliwadhihirishia wanafunzi wake kwamba karibuni angewaacha na kurudi kwa Baba yake. Hilo liliwataabisha na kuwahuzunisha. (Yohana 13:33, 36; 14:27-31) Akitambua uhitaji wao wa faraja yenye kuendelea, Yesu aliahidi hivi: “Nami hakika nitamwomba Baba naye atawapa nyinyi mfariji mwingine awe pamoja nanyi milele.” (Yohana 14:16, NW, kielezi-chini) Hapa Yesu alirejezea roho takatifu ya Mungu, iliyomwagwa juu ya wanafunzi wake siku 50 baada ya kufufuliwa kwake.a Miongoni mwa mambo mengine, roho ya Mungu iliwafariji wakati wa majaribu yao na kuwatia nguvu ili waendelee kufanya mapenzi ya Mungu. (Matendo 4:31) Hata hivyo, msaada huo haupasi kuonwa ukiwa kitu cha moja kwa moja. Ili kunufaishwa nao kikamili, kila Mkristo lazima aendelee kusali ili kupata msaada wenye kufariji ambao Mungu huandaa kupitia roho yake takatifu.—Luka 11:13.
15. Ni zipi baadhi ya njia ambazo Yehova hutupa faraja?
15 Njia nyingine ambayo kwayo Mungu huandaa faraja ni kupitia Neno lake, Biblia. Paulo aliandika hivi: “Yote yaliyotangulia kuandikwa yaliandikwa ili kutufundisha sisi; ili kwa saburi na faraja ya maandiko tupate kuwa na tumaini.” (Warumi 15:4) Hilo laonyesha uhitaji wetu wa kujifunza na kutafakari kwa ukawaida mambo ambayo yameandikwa katika Biblia na vichapo vyenye kutegemea Biblia. Pia twahitaji kuhudhuria mikutano ya Kikristo kwa ukawaida, ambapo mawazo yenye kufariji kutoka katika Neno la Mungu hushirikiwa. Mojawapo makusudi makubwa ya makusanyiko hayo ni kutiana moyo.—Waebrania 10:25.
16. Maandalizi ya Mungu yenye kufariji yapaswa kutuhamasisha tufanye nini?
16 Barua ya Paulo kwa Warumi yaendelea kuonyesha matokeo mazuri tupokeayo kwa kutumia ifaavyo maandalizi yenye kufariji ya Mungu. “Mungu mwenye [“apaye,” NW] saburi na faraja,” akaandika Paulo, “awajalie kunia mamoja ninyi kwa ninyi, kwa mfano wa Kristo Yesu; ili kwa moyo mmoja na kwa kinywa kimoja mpate kumtukuza Mungu, Baba wa Bwana wetu Yesu Kristo.” (Warumi 15:5, 6) Ndiyo, kwa kutumia kwa faida kamili maandalizi yenye kufariji ya Mungu, tutazidi kuwa sawa na Kiongozi wetu mwenye moyo mkuu, Yesu Kristo. Hilo litatuhamasisha tuendelee kutumia vinywa vyetu ili kumtukuza Mungu katika kazi yetu ya kuhubiri, kwenye mikutano yetu, katika mazungumzo ya kibinafsi pamoja na waamini wenzetu, na katika sala zetu.
Katika Nyakati za Majaribu Makali
17. Yehova alimfariji Mwana wake jinsi gani, na kukiwa na tokeo jipi?
17 Yesu ‘alisononeka’ na ‘kuhuzunika’ usiku uliotangulia kifo chake chenye maumivu makuu. (Mathayo 26:37, 38) Kwa hiyo akaondoka kwenda umbali fulani kutoka walipokuwa wanafunzi wake na kusali kwa Baba yake apate msaada. “Akasikilizwa kwa jinsi alivyokuwa mcha Mungu.” (Waebrania 5:7) Biblia huripoti kwamba “malaika kutoka mbinguni akamtokea akamtia nguvu.” (Luka 22:43) Njia yenye moyo mkuu na ya kimwanamume ambayo kwayo Yesu alienda kukabili wapinzani wake ni uthibitisho kwamba njia ya Mungu ya kufariji Mwana wake ilikuwa na matokeo zaidi.—Yohana 18:3-8, 33-38.
18. (a) Ni kipindi kipi maishani mwa Paulo kilichokuwa hasa chenye kujaribu? (b) Twaweza kuwaje wenye kufariji kwa wazee wenye bidii, na wenye huruma?
18 Mtume Paulo pia alipitia vipindi vya jaribu kali. Kwa kielelezo, huduma yake katika Efeso ilitiwa alama na ‘machozi, na majaribu yaliyompata kwa hila za Wayahudi.’ (Matendo 20:17-20) Mwishowe, Paulo akaondoka Efeso baada ya waungaji-mkono wa mungu wa kike Artemisi walipokuwa wamezusha ghasia jijini kwa sababu ya utendaji wake wa kuhubiri. (Matendo 19:23-29; 20:1) Paulo alipokuwa akielekea kaskazini kwenye jiji la Troa, jambo jingine lilimlemea sana akilini mwake. Wakati fulani kabla ya ile ghasia katika Efeso, alikuwa amepata ripoti yenye kusumbua. Lile kutaniko changa katika Korintho lilikumbwa na mgawanyiko, nalo lilikuwa likiendekeza uasherati. Kwa hiyo akiwa Efeso, Paulo alikuwa ameandika barua ya karipio thabiti akiwa na matumaini ya kurekebisha hiyo hali. Hilo halikuwa jambo rahisi kwake kufanya. “Katika dhiki nyingi na taabu ya moyo niliwaandikia na machozi mengi,” akafunua baadaye katika barua ya pili. (2 Wakorintho 2:4) Sawa na Paulo, wazee wenye huruma hawaoni ikiwa rahisi kutoa shauri lenye kusahihisha na karipio, kwa sehemu fulani ni kwa sababu wanatambua udhaifu wao wenyewe mbalimbali. (Wagalatia 6:1) Basi, na tuwe wenye kufariji kwa wale wanaoongoza miongoni mwetu kwa kuitikia kwa utayari shauri la upendo, lenye kutegemea Biblia.—Waebrania 13:17.
19. Kwa nini Paulo aliendelea na safari kutoka Troa hadi Makedonia, naye alipataje kitulizo hatimaye?
19 Alipokuwako Efeso, zaidi ya kuwaandikia ndugu katika Korintho, Paulo alimtuma Tito awasaidie, akimpa utume wa kuripoti juu ya itikio lao kwa ile barua. Paulo alitumaini kumkuta Tito, Troa. Huko Paulo alibarikiwa kwa fursa nzuri za kufanya wanafunzi. Lakini hilo halikumwondolea hangaiko lake kwa sababu Tito hakuwa amefika bado. (2 Wakorintho 2:12, 13) Kwa hiyo, akaendelea na safari kuelekea Makedonia, akitumainia kukutana na Tito huko. Hali ya kuhangaika ya Paulo iliongezwa na upinzani mwingi dhidi ya huduma yake. “Tulipokuwa tumefika Makedonia,” aeleza, “miili yetu haikupata nafuu; bali tulidhikika kote kote; nje palikuwa na vita, ndani hofu. Lakini Mungu, mwenye kuwafariji wanyonge, alitufariji kwa kuja kwake Tito.” (2 Wakorintho 7:5, 6) Kilikuwa kitulizo kama nini Tito alipofika mwishowe ili kumwambia Paulo juu ya itikio chanya la Wakorintho kwa barua yake!
20. (a) Kama ilivyokuwa katika kisa cha Paulo, ni ipi njia nyingine ya maana ambayo kwayo Yehova hupa faraja? (b) Ni nini kitakachochunguzwa katika makala inayofuata?
20 Mambo aliyojionea Paulo hufariji watumishi wa Mungu leo, ambao wengi wao hukabili majaribu ambayo huwafanya wawe “wanyonge” au “washuke moyo.” (Phillips) Ndiyo, ‘Mungu apaye faraja’ hujua mahitaji yetu mmoja-mmoja naye aweza kututumia tufarijiane, kama vile Paulo alivyopata faraja kupitia ripoti ya Tito juu ya mwelekeo wa kutubu wa Wakorintho. (2 Wakorintho 7:11-13) Katika makala yetu inayofuata, tutachunguza itikio changamfu la Paulo kwa Wakorintho na jinsi liwezavyo kutusaidia tuwe washiriki wenye matokeo wa faraja ya Mungu leo.
-
-
Kushiriki Faraja Ambayo Yehova HuandaaMnara wa Mlinzi—1996 | Novemba 1
-
-
Kushiriki Faraja Ambayo Yehova Huandaa
“Tumaini letu kwa ajili yenu ni imara, tukijua ya kuwa kama vile mlivyo washiriki wa yale mateso, vivyo hivyo mmekuwa washiriki wa zile faraja.”—2 WAKORINTHO 1:7.
1, 2. Wengi ambao wamekuwa Wakristo leo wamepatwa na nini?
WENGI wasomao Mnara wa Mlinzi sasa walikua wakiwa bila ujuzi wa kweli ya Mungu. Labda hiyo ni kweli kukuhusu. Ikiwa ndivyo, kumbuka jinsi ulivyohisi huku macho yako ya uelewevu yalipoanza kufunguka. Kwa kielelezo, mara ya kwanza ulipoelewa kwamba wafu hawateseki bali hawana ufahamu, je, hukutulizwa? Na ulipojifunza juu ya tumaini la wafu, kwamba mabilioni ya watu watafufuliwa warudie uhai katika ulimwengu mpya wa Mungu, je, hukufarijiwa?—Mhubiri 9:5, 10; Yohana 5:28, 29.
2 Vipi juu ya ahadi ya Mungu ya kukomesha uovu na kugeuza dunia hii iwe paradiso? Ulipojifunza juu ya jambo hilo, je, halikukufariji na kukujaza tazamio lenye hamu? Ulihisije ulipojifunza mara ya kwanza juu ya uwezekano wa kutokufa kamwe bali kusalimika na kuingia Paradiso hiyo ya kidunia ijayo? Bila shaka ulisisimuliwa. Ndiyo, ulikuwa umekuwa mpokeaji wa ujumbe wenye kufariji wa Mungu ambao sasa wahubiriwa ulimwenguni pote na Mashahidi wa Yehova.—Zaburi 37:9-11, 29; Yohana 11:26; Ufunuo 21:3-5.
3. Kwa nini wale ambao hushiriki pamoja na wengine ujumbe wenye kufariji wa Mungu hupatwa na dhiki pia?
3 Hata hivyo, ulipojaribu kushiriki ujumbe wa Biblia pamoja na wengine, ulikuja kutambua pia kwamba “si wote walio na imani.” (2 Wathesalonike 3:2) Huenda ikawa baadhi ya marafiki wako wa zamani walikudhihaki kwa kuonyesha imani katika ahadi za Biblia. Labda hata ulinyanyaswa kwa sababu ya kuendelea kujifunza Biblia kwa kushirikiana na Mashahidi wa Yehova. Pengine upinzani uliongezeka ulipoanza kufanya mabadiliko ili kupatanisha maisha yako na kanuni za Biblia. Ulianza kupatwa na dhiki ambazo Shetani na ulimwengu wake huleta juu ya wote wanaokubali faraja ya Mungu.
4. Wale ambao wameanza kupendezwa karibuni waweza kuitikia dhiki katika njia zipi tofauti?
4 Kwa kuhuzunisha, sawa na alivyotabiri Yesu, dhiki huwafanya wengine wakwazwe na kuacha ushirika wao pamoja na kutaniko la Kikristo. (Mathayo 13:5, 6, 20, 21) Watu wengine huvumilia dhiki kwa kudumisha akili zao zikiwa zimekaziwa ahadi zenye kufariji ambazo wanajifunza. Hatimaye wanaweka maisha zao wakfu kwa Yehova na kubatizwa wakiwa wanafunzi wa Mwana wake, Yesu Kristo. (Mathayo 28:19, 20; Marko 8:34) Bila shaka, dhiki haiishi mara tu Mkristo abatizwapo. Kwa kielelezo, kudumisha usafi wa kiadili kwaweza kuwa shindano gumu kwa mtu ambaye amekuwa na mwenendo usio wa adili. Wengine lazima washindane na upinzani wenye kuendelea kutoka kwa washiriki wa familia wasioamini. Hata dhiki iwe ipi, wote ambao hufuatia kwa uaminifu maisha yaliyo wakfu kwa Mungu waweza kuwa na uhakika wa jambo moja. Kwa njia ya kibinafsi sana, watapata faraja na msaada wa Mungu.
“Mungu wa Faraja Yote”
5. Pamoja na majaribu mengi ambayo Paulo alipatwa nayo, yeye alijionea nini pia?
5 Mmoja ambaye alithamini sana faraja ambayo Mungu hupa alikuwa mtume Paulo. Baada ya wakati wenye kujaribu hasa katika Asia na Makedonia, alipata kitulizo kikubwa aliposikia kwamba kutaniko la Korintho lilikuwa limeitikia vema barua yake ya karipio. Hilo lilimsukuma awaandikie barua ya pili, ambayo ina maneno yafuatayo ya sifa: “Na ahimidiwe Mungu, Baba wa Bwana wetu Yesu Kristo, Baba wa rehema [“nyororo,” NW], Mungu wa faraja yote; atufarijiye katika dhiki zetu zote.”—2 Wakorintho 1:3, 4.
6. Twajifunza nini kutokana na maneno ya Paulo yapatikanayo kwenye 2 Wakorintho 1:3, 4?
6 Maneno hayo yaliyopuliziwa hutuandalia habari nyingi. Acheni tuyachunguze. Paulo atoapo sifa au shukrani kwa Mungu au kumwomba jambo fulani katika barua zake, kwa kawaida twapata kwamba yeye hutia ndani pia uthamini wenye kina kwa ajili ya Yesu, aliye Kichwa cha kutaniko la Kikristo. (Warumi 1:8; 7:25; Waefeso 1:3; Waebrania 13:20, 21) Kwa sababu hiyo, Paulo anamsifu “Mungu, Baba wa Bwana wetu Yesu Kristo.” (Italiki ni zetu.) Kisha, kwa mara ya kwanza katika uandikaji wake mbalimbali, anatumia nomino ya Kigiriki itafsiriwayo “rehema nyororo.” Nomino hiyo yatokana na neno litumiwalo ili kuonyesha huzuni kuelekea kuteseka kwa mwingine. Hivyo Paulo anafafanua hisia nyororo za Mungu kwa wowote wa watumishi Wake waaminifu wanaopatwa na dhiki—hisia nyororo ambazo humsukuma Mungu atende kwa rehema kwa niaba yao. Mwishowe, Paulo alimtegemea Yehova kuwa chanzo cha sifa hiyo yenye kutamanika kwa kumwita “Baba wa rehema [“nyororo,” NW].”—Italiki ni zetu.
7. Kwa nini yaweza kusemwa kwamba Yehova ndiye “Mungu wa faraja yote”?—Italiki ni zetu.
7 “Rehema nyororo” za Mungu hutokeza kitulizo kwa yule apatwaye na dhiki. Kwa hiyo, Paulo aendelea kumfafanua Yehova kuwa “Mungu wa faraja yote.” Hivyo, faraja yoyote tuwezayo kupata kutoka kwa fadhili ya waamini wenzetu, twaweza kumwona Yehova kuwa ndiye chanzo chayo. Hakuna faraja halisi, yenye kudumu ambayo haitokani na Mungu. Zaidi, yeye ndiye aliyemuumba mwanadamu katika mfano wake, hivyo akituwezesha kuwa wafariji. Na roho takatifu ya Mungu ndiyo huwahamasisha watumishi wake waonyeshe rehema nyororo kuelekea wale wanaohitaji kupata faraja.
Waliozoezwa Kuwa Wafariji
8. Ingawa Mungu siye chanzo cha majaribu yetu, kuvumilia kwetu dhiki kwaweza kuwa na tokeo jipi lenye manufaa juu yetu?
8 Ingawa Yehova Mungu huruhusu majaribu mbalimbali yawajiayo watumishi wake waaminifu, yeye hawi kamwe chanzo cha majaribu hayo. (Yakobo 1:13) Hata hivyo, faraja anayoandaa tuvumiliapo dhiki yaweza kutuzoeza kutambua upesi zaidi mahitaji ya wengine. Kukiwa na tokeo jipi? “Tupate kuwafariji wale walio katika dhiki za namna zote, kwa faraja hizo tunazofarijiwa na Mungu.” (2 Wakorintho 1:4) Hivyo Yehova hutuzoeza tuwe washiriki wenye matokeo wa faraja yake pamoja na waamini wenzetu na pamoja na wale tunaokutana nao katika huduma yetu tumwigapo Kristo na “kuwafariji wote waliao.”—Isaya 61:2; Mathayo 5:4.
9. (a) Ni nini kitakachotusaidia kuvumilia mateso? (b) Wengine hufarijiwaje tunapovumilia dhiki kwa uaminifu?
9 Paulo alivumilia mateso yake mengi, kwa sababu ya faraja nyingi aliyopokea kutoka kwa Mungu kupitia Kristo. (2 Wakorintho 1:5) Sisi pia twaweza kupata wingi wa faraja kwa kutafakari juu ya ahadi zenye thamani za Mungu, kwa kusali ili tupate utegemezo wa roho yake takatifu, na kwa kujionea majibu ya Mungu kwa sala zetu. Hivyo tutatiwa nguvu tuendelee kuunga mkono enzi kuu ya Yehova na kumthibitisha Ibilisi kuwa mwongo. (Ayubu 2:4; Mithali 27:11) Tukiwa tumesha vumilia kwa uaminifu aina yoyote ya dhiki, sawa na Paulo, twapaswa kumpa Yehova sifa yote, ambaye faraja yake huwawezesha Wakristo wabaki wakiwa waaminifu chini ya jaribu. Uvumilivu wa Wakristo waaminifu una matokeo yenye kufariji juu ya udugu, ukiwafanya wengine waazimie “kustahimili mateso yale yale.”—2 Wakorintho 1:6.
10, 11. (a) Ni baadhi ya mambo gani yaliyolisababishia kutaniko la Korintho la kale mateso? (b) Paulo alilifarijije kutaniko la Korintho, naye alionyesha tumaini jipi?
10 Wakorintho walishiriki sehemu ya mateso yaliyowapata Wakristo wote wa kweli. Kwa kuongezea, walihitaji shauri ili watenge na ushirika mwasherati asiyetubu. (1 Wakorintho 5:1, 2, 11, 13) Kushindwa kuchukua hatua hiyo na kukomesha zogo na migawanyiko kulikuwa kumeletea kutaniko aibu. Lakini hatimaye walitumia shauri la Paulo na kuonyesha toba ya kweli. Kwa sababu hiyo, aliwapongeza kwa uchangamfu na kutaarifu kwamba itikio lao zuri kwa barua yake lilikuwa limemfariji. (2 Wakorintho 7:8, 10, 11, 13) Yaonekana, yule aliyetengwa na ushirika alikuwa ametubu pia. Kwa hiyo Paulo aliwashauri ‘wamsamehe na kumfariji, mtu kama huyo asije akamezwa katika huzuni yake ipitayo kiasi.’—2 Wakorintho 2:7.
11 Barua ya Paulo ya pili lazima iwe ililifariji kutaniko la Korintho. Na hilo lilikuwa mojawapo makusudio yake. Yeye alieleza hivi: “Tumaini letu kwa ajili yenu ni imara, tukijua ya kuwa kama vile mlivyo washiriki wa yale mateso, vivyo hivyo mmekuwa washiriki wa zile faraja.” (2 Wakorintho 1:7) Kwenye umalizio wa barua yake, Paulo alisihi sana hivi: “Endeleeni . . . kufarijiwa, . . . na Mungu wa upendo na amani atakuwa pamoja nanyi.”—2 Wakorintho 13:11, NW.
12. Wakristo wote wana uhitaji upi?
12 Ni somo la maana kama nini tuwezalo kujifunza kutokana na hilo! Washiriki wote wa kutaniko la Kikristo wanahitaji ‘kushiriki faraja’ ambazo Mungu huandaa kupitia Neno lake, roho yake takatifu, na tengenezo lake la kidunia. Hata waliotengwa na ushirika huenda wakahitaji kupata faraja ikiwa wametubu na kurekebisha mwendo wao wenye kosa. Hivyo, “mtumwa mwaminifu mwenye akili” ameanzisha uandalizi wenye rehema wa kuwasaidia. Mara moja kila mwaka wazee wawili waweza kutembelea watu fulani-fulani waliotengwa na ushirika. Huenda hao wasionyeshe tena mwelekeo wa uasi au kuhusika katika dhambi nzito na huenda wakahitaji msaada ili kuchukua hatua za lazima za kurejeshwa.—Mathayo 24:45; Ezekieli 34:16.
Dhiki ya Paulo Katika Asia
13, 14. (a) Paulo alifafanuaje wakati wa dhiki kali aliyojionea Asia? (b) Huenda ikawa Paulo alikuwa akifikiria kisa kipi?
13 Aina ya mateso ambayo kutaniko la Korintho lilikuwa limepatwa nayo kufikia wakati huo haingeweza kulinganishwa na zile dhiki nyingi ambazo Paulo alilazimika kuvumilia. Hivyo, aliweza kuwakumbusha hivi: “Maana ndugu, hatupendi, msijue habari ya dhiki ile iliyotupata katika Asia, ya kwamba tulilemewa mno kuliko nguvu zetu, hata tukakata tamaa ya kuishi. Naam, sisi wenyewe tulikuwa na hukumu ya mauti katika nafsi zetu ili tusijitumainie nafsi zetu, bali tumtumaini Mungu awafufuaye wafu, aliyetuokoa sisi katika mauti kuu namna ile; tena atatuokoa; ambaye tumemtumaini kwamba atazidi kutuokoa.”—2 Wakorintho 1:8-10.
14 Wasomi fulani wa Biblia huamini kwamba Paulo alikuwa akirejezea ghasia katika Efeso, ambayo ingewagharimu Paulo na pia waandamani wake wawili Wamakedonia waliosafiri naye, Gayo na Aristarko, uhai wao. Wakristo hao wawili waliingizwa kwa nguvu mahali pa michezo palipokuwa pamejaa kikundi cha wafanya-ghasia ‘waliopiga kelele wote pia kwa sauti moja kwa muda wa kama saa mbili, wakisema, Artemi [mungu wa kike] wa Waefeso ni mkuu.’ Hatimaye, ofisa wa jiji alifaulu kuunyamazisha umati. Tisho hilo kwa uhai wa Gayo na Aristarko lazima liwe lilimtaabisha sana Paulo. Kwa hakika, alitaka kuingia na kusababu na hicho kikundi cha wafanya-ghasia chenye ushupavu, lakini alizuiwa asihatarishe uhai wake katika njia hiyo.—Matendo 19:26-41.
15. Ni hali ipi ya kupita kiasi ambayo huenda ikafafanuliwa kwenye 1 Wakorintho 15:32?
15 Hata hivyo, huenda ikawa Paulo alikuwa akifafanua hali mbaya zaidi kuliko tukio hilo ambalo limetangulia. Katika barua yake ya kwanza kwa Wakorintho, Paulo aliuliza hivi: “Ikiwa, kwa jinsi ya kibinadamu, nalipigana na hayawani wakali kule Efeso, nina faida gani?” (1 Wakorintho 15:32) Huenda hilo likamaanisha kwamba uhai wa Paulo ulihatarishwa na watu walio kama hayawani na pia wanyama-mwitu halisi katika stediamu ya Efeso. Nyakati nyingine wahalifu waliadhibiwa kwa kulazimishwa kupigana na hayawani-mwitu huku umati wenye tamaa ya kumwaga damu ukitazama. Ikiwa Paulo alimaanisha kwamba alikuwa amekabili hayawani-mwitu halisi, lazima awe alihifadhiwa kimuujiza katika dakika ya mwisho ili asife kifo chenye jeuri, kama vile Danieli alivyookolewa kutoka katika vinywa vya simba halisi.—Danieli 6:22.
Vielelezo vya Siku ya Kisasa
16. (a) Kwa nini wengi wa Mashahidi wa Yehova waweza kufananisha hali zao na dhiki zilizompata Paulo? (b) Twaweza kuwa na uhakika gani kuhusu wale waliokufa kwa sababu ya imani yao? (c) Kuponea kifo chupuchupu kwa Wakristo fulani kumekuwa na matokeo gani mazuri?
16 Wakristo wengi wa siku ya kisasa waweza kuhusianisha hali zao na dhiki zilizompata Paulo. (2 Wakorintho 11:23-27) Leo, pia, Wakristo ‘wamelemewa mno kuliko nguvu zao,’ na wengi wamekabili hali ambamo ‘wamekata tamaa ya kuishi.’ (2 Wakorintho 1:8) Watu kadhaa wamekufa mikononi mwa wauaji wa kimakusudi wa watu wengi na wanyanyasaji wakatili. Twaweza kuwa na uhakika kwamba uwezo wa Mungu wenye kufariji uliwawezesha kuvumilia na kwamba walikufa, mioyo na akili zikiwa zimekazwa kikiki kwenye utimizo wa tumaini lao, liwe la kimbingu au la kidunia. (1 Wakorintho 10:13; Wafilipi 4:13; Ufunuo 2:10) Katika visa vingine, Yehova ameelekeza mambo, na ndugu zetu wameokolewa kutoka kifo. Hakuna shaka kwamba wale ambao wamepitia wokovu huo wamekuza tumaini lililoongezeka “katika Mungu, awafufuaye wafu.” (2 Wakorintho 1:9) Baadaye, waliweza kusema wakiwa na usadikisho mkubwa hata zaidi walipokuwa wakishiriki pamoja na wengine ujumbe wenye kufariji wa Mungu.—Mathayo 24:14.
17-19. Ni mambo gani yaliyoonwa yanayoonyesha kwamba ndugu zetu huko Rwanda wamekuwa washiriki katika faraja ya Mungu?
17 Majuzi ndugu zetu wapendwa huko Rwanda walipatwa na mambo yanayofanana na yale ya Paulo na waandamani wake. Wengi walipoteza uhai wao, lakini jitihada za Shetani zilishindwa kuharibu imani yao. Badala ya hivyo, ndugu zetu katika nchi hiyo wamepata faraja ya Mungu katika njia nyingi za kibinafsi. Wakati wa yale maangamizi ya jamii nzima-nzima ya Watutsi na Wahutu wanaoishi Rwanda, kulikuwa na Wahutu waliohatarisha uhai wao ili kuwalinda Watutsi na Watutsi waliowalinda Wahutu. Baadhi yao walikuwa Mashahidi Wahutu waliouawa na watu wenye siasa kali kwa sababu waliwalinda waamini wenzao. Kwa kielelezo, Shahidi Mhutu aitwaye Gahizi aliuawa baada ya kumficha dada Mtutsi aitwaye Chantal. Mume wa Chantal Mtutsi, Jean, alifichwa kwingineko na dada Mhutu aitwaye Charlotte. Kwa siku 40 Jean na ndugu mwingine Mtutsi walibaki wakiwa wamefichwa katika dohani kubwa, wakitoka kwa vipindi vifupi tu wakati wa usiku. Wakati wote huo, Charlotte aliwaandalia chakula na ulinzi, ingawa alikuwa akiishi karibu na kambi ya kijeshi ya Wahutu. Kwenye ukurasa huu, waweza kuona picha ya Jean na Chantal walioungana tena, ambao ni wenye shukrani kwamba waabudu wenzao Wahutu walikuwa “tayari hata kukatwa kichwa,” kwa ajili yao, kama tu Priska na Akila walivyomfanyia mtume Paulo.—Warumi 16:3, 4.
18 Shahidi mwingine Mhutu, Rwakabubu, alisifiwa na gazeti la habari Intaremara kwa kuwalinda waamini wenzake Watutsi.a Gazeti hilo lilitaarifu hivi: “Pia kuna Rwakabubu, mmoja wa Mashahidi wa Yehova, aliyeendelea kuwaficha watu huku na huku miongoni mwa ndugu zake (hivyo ndivyo waamini wenzi huitana). Alikuwa akishinda mchana kutwa akibeba chakula na maji ya kunywa kwa ajili yao ingawa ana ugonjwa wa pumu. Lakini Mungu alimpa nguvu zisizo za kawaida.”
19 Pia, fikiria wenzi Wahutu wenye kupendezwa waitwao Nicodeme na Athanasie. Kabla ya maangamizi ya jamii nzima-nzima kuanza, wenzi hao wa ndoa walikuwa wakijifunza Biblia na Shahidi Mtutsi aitwaye Alphonse. Kwa kuhatarisha uhai wao, walimficha Alphonse nyumbani mwao. Baadaye walitambua kwamba nyumba hiyo haikuwa mahali salama kwa sababu majirani wao Wahutu walijua juu ya rafiki yao Mtutsi. Kwa hiyo, Nicodeme na Athanasie wakamficha Alphonse ndani ya shimo uwanjani mwao. Hiyo ilikuwa hatua nzuri kwa sababu majirani walianza kuja kumtafuta Alphonse karibu kila siku. Huku akiwa amefichwa ndani ya shimo hilo kwa siku 28, Alphonse alitafakari juu ya masimulizi ya Biblia kama lile juu ya Rahabu, aliyewaficha Waisraeli wawili kwenye dari ya nyumba yake katika Yeriko. (Yoshua 6:17) Leo Alphonse anaendelea na utumishi wake huko Rwanda akiwa mhubiri wa habari njema, mwenye shukrani kwa sababu wanafunzi wake wa Biblia Wahutu walihatarisha uhai wao kwa ajili yake. Na vipi Nicodeme na Athanasie? Wao sasa ni Mashahidi wa Yehova waliobatizwa na wanaongoza mafunzo zaidi ya 20 ya Biblia na watu wenye kupendezwa.
20. Yehova amewafariji ndugu zetu huko Rwanda katika njia ipi, lakini wengi wao wana uhitaji upi wenye kuendelea?
20 Hayo maangamizi ya jamii nzima-nzima yalipoanza huko Rwanda, kulikuwa na wapiga-mbiu 2,500 wa habari njema katika hiyo nchi. Ingawa mamia ya watu walipoteza uhai wao au walilazimishwa kutoroka hiyo nchi, idadi ya Mashahidi imeongezeka kufikia zaidi ya 3,000. Hiyo ni ithibati kwamba Mungu kwa kweli aliwafariji ndugu zetu. Vipi wale mayatima na wajane wengi miongoni mwa Mashahidi wa Yehova? Kiasili, hao bado hupatwa na dhiki na wanahitaji kupata faraja yenye kuendelea. (Yakobo 1:27) Machozi yao yatafutwa kabisa wakati tu ufufuo utukiapo katika ulimwengu mpya wa Mungu. Hata hivyo, kwa sababu ya uhudumiaji mbalimbali wa ndugu zao na kwa sababu wao ni waabudu wa “Mungu wa faraja yote,” wanaweza kukabiliana na maisha.
21. (a) Ni wapi kwingineko ambako ndugu zetu wamekuwa na uhitaji mkubwa wa kupata faraja ya Mungu, na ni ipi njia moja ambayo kwayo sisi sote twaweza kusaidia? (Ona Sanduku “Faraja Wakati wa Miaka Minne ya Vita.”) (b) Ni lini uhitaji wetu wa kupata faraja utakapotoshelezwa kabisa?
21 Katika sehemu nyingine nyingi, kama vile Eritrea, Singapore, na iliyokuwa Yugoslavia, ndugu zetu wanaendelea kumtumikia Yehova kwa uaminifu licha ya dhiki. Na tuwasaidie ndugu hao kwa kuomba dua za ukawaida ili wapokee faraja. (2 Wakorintho 1:11) Na tuvumilie kwa uaminifu mpaka wakati ambapo Mungu kupitia Yesu Kristo ‘atafuta kila chozi katika macho yetu’ katika maana iliyo kamili zaidi. Ndipo tutakapojionea kwa kiwango kamili faraja ambayo Yehova atatoa katika ulimwengu wake mpya wa uadilifu.—Ufunuo 7:17; 21:4; 2 Petro 3:13.
-
-
Faraja Wakati wa Miaka Minne ya VitaMnara wa Mlinzi—1996 | Novemba 1
-
-
Faraja Wakati wa Miaka Minne ya Vita
WAKATI wa ile miaka minne ya vita katika eneo la iliyokuwa Yugoslavia, watu wengi walipatwa na magumu na upungufu mkali mbalimbali. Waliotiwa ndani yao walikuwa mamia ya Mashahidi wa Yehova, walioendelea kumtumikia “Mungu wa faraja yote” kwa uaminifu.—2 Wakorintho 1:3.
Katika Sarajevo, watu walipatwa na ule ugumu wa ziada wa kuishi katika jiji kubwa lililozingiwa wakati wote wa vita. Kulikuwa na upungufu wa nguvu za umeme, maji, kuni, na chakula. Kutaniko la Mashahidi wa Yehova la Sarajevo lilitendaje chini ya hali hizo zenye kupita kiasi? Wakristo kutoka nchi jirani walihatarisha uhai wao ili kuingiza kiasi kikubwa cha ugavi wa kitulizo. (Ona Mnara wa Mlinzi, Novemba 1, 1994, kurasa 23-27.) Pia, ndugu katika Sarajevo walishiriki mmoja na mwenzake, vitu walivyokuwa navyo, wakikazia zaidi kushiriki mambo ya kiroho. Wakati wa mazingiwa mwangalizi Mkristo kutoka jiji hilo alitoa ripoti ifuatayo:
“Twaithamini mikutano yetu sana. Mke wangu nami, pamoja na watu wengine 30, hutembea kilometa 15 [maili 9] kila safari kwenda mikutanoni. Wakati mwingine ilitangazwa kwamba maji yangetolewa wakati ambapo mikutano ilifanywa. Ndugu wangefanya nini? Je, wangekaa nyumbani au wangehudhuria mikutano? Ndugu zetu walipendelea kuihudhuria mikutano. Sikuzote ndugu husaidiana; chochote walicho nacho wao hushiriki mmoja na mwenzake. Dada mmoja kutanikoni mwetu huishi kwenye viunga vya hilo jiji, karibu na msitu; kwa hiyo ni rahisi zaidi kwake kupata kuni. Yeye pia hufanya kazi mahali pa kuokea mikate, na mshahara wake ni unga. Iwezekanapo, yeye huoka mkate mkubwa na kuuleta mkutanoni. Baada ya mkutano, aondokapo, yeye humpa kila mtu kipande.
“Ni jambo la maana kusiwe na ndugu na dada wowote wapatao kuhisi kuwa wameachwa peke yao. Hakuna ajuaye ni nani kati yetu atakayehitaji msaada wakati mwingine katika hali isiyopendeza. Tulipokuwa na barabara zenye barafu na dada mmoja alikuwa mgonjwa, ndugu wachanga, wenye nguvu, walimvuta hadi mikutanoni akiwa kwenye gari la kuteleza.
“Sisi sote hushiriki katika kazi ya kuhubiri, naye Yehova amebariki jitihada zetu. Ameona uhitaji wetu mkubwa katika Bosnia, lakini ametubariki kwa ongezeko—ongezeko ambalo hatukuwa tumeona kabla ya vita.”
Vivyo hivyo, katika sehemu nyingine zilizokumbwa na vita za iliyokuwa Yugoslavia, Mashahidi wa Yehova wamefurahia maongezeko licha ya magumu makali. Kutoka ofisi ya Kroatia ya Mashahidi wa Yehova yatoka ripoti hii juu ya kikundi cha Mashahidi: “Ndugu wanaoishi Velika Kladuša walikuwa na nyakati ngumu sana za kushughulika nazo. Mji huo ulishambuliwa kwenye pindi kadhaa. Ndugu walilazimika kueleza majeshi ya Kroatia, Serbia, na majeshi kadha wa kadha ya Kiislamu juu ya kutokuwamo kwao. Kwa hakika, walilazimika kuvumilia mengi—kufungwa gerezani, kuchapwa, njaa, hatari ya kifo. Na bado, wote walibaki wakiwa waaminifu na wana lile pendeleo lenye kutokeza la kuona baraka za Yehova juu ya utendaji wao mbalimbali.”
Yajapokuwa magumu hayo, Mashahidi wa Yehova katika Velika Kladuša na Bihać mji ulio jirani wanaendelea kufurahia maongezeko huku wakishiriki pamoja na jirani zao kwa bidii ujumbe wa Mungu wa faraja. Jumla ya watangazaji 26 wa Ufalme kutoka sehemu hizo mbili wanaongoza mafunzo ya Biblia ya nyumbani 39!
-