Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Matarajio Yanapokosa Kutimizwa
    Mnara wa Mlinzi—2007 | Aprili 15
    • Zungumzeni Kuhusu Matarajio Yenu

      Matarajio yasiyotimizwa yanaweza kwa kweli kumfadhaisha mtu. (Methali 13:12) Hata hivyo, kuna jambo unaloweza kufanya kuhusu hali hiyo. Methali moja ya Biblia inasema: “Unaweza kuwashawishi wengine ukiwa na hekima na ukizungumza kupatana na akili.” (Methali 16:23, Contemporary English Version) Kwa hiyo, ukihisi kwamba una matarajio mazuri ambayo hayatimizwi, zungumzia jambo hilo na mwenzi wako.

      Jaribu kuchagua wakati unaofaa, mahali panapofaa, na maneno yanayofaa ili kueleza mambo yanayokuhangaisha. (Methali 25:11) Zungumza kwa utulivu na heshima. Kumbuka kusudi lako si kumshutumu mwenzi wako bali ni kumjulisha kuhusu matarajio na hisia zako.—Methali 15:1.

      Je, una sababu yoyote ya kufanya hivyo? Je, mwenzi mwenye kujali hana uwezo wa kutambua mahitaji yako? Kwa kweli, huenda mwenzi wako ana maoni tofauti lakini angefurahi na kutilia maanani maoni yako ikiwa ungemweleza. Kusema mambo unayotaka au unayohitaji si ishara ya kwamba ndoa yenu haijafaulu wala hakuonyeshi kwamba mwenzi wako hajali.

      Kwa hiyo, usisite kuzungumzia mambo pamoja na mwenzi wako. Kwa mfano, katika kisa kilichotajwa mapema, Mary angemwambia David: “Ninakubali kwamba ninaogopa kukutana na watu wengi wapya. Je, unaweza kunisaidia kuwa mtulivu mpaka nitakapowazoea?”

      “Mwepesi Kuhusu Kusikia”

      Sasa chunguza jambo hilo kwa njia nyingine. Tuseme kwamba mwenzi wako anakufikia, naye amefadhaika kwa sababu hutimizi tarajio fulani zuri. Msikilize mwenzi wako akikufikia! Jitahidi kuepuka kujitetea. Badala yake, ‘uwe mwepesi kuhusu kusikia, si mwepesi wa kusema, si mwepesi wa ghadhabu.’ (Yakobo 1:19; Methali 18:13) Mtume Paulo aliwahimiza hivi Wakristo: “Kila mmoja na aendelee kutafuta, si faida yake mwenyewe, bali ile ya yule mtu mwingine.”—1 Wakorintho 10:24.

      Unaweza kufanya hivyo kwa kujiweka katika hali ya mwenzi wako. Biblia inasema hivi: “Enyi waume, endeleeni kukaa [na wake zenu] vivyo hivyo kulingana na ujuzi,” au, kama tafsiri ya J. B. Philip inavyosema, “ninyi waume mnapaswa kujitahidi kuwaelewa wake mnaoishi nao.” (1 Petro 3:7) Bila shaka, wake wanapaswa pia kujitahidi kufanya vivyo hivyo kuhusu waume zao.

      Kumbuka kwamba hata iwe unapatana kadiri gani na mwenzi wako wa ndoa, hamwoni mambo yote kwa njia ileile. (Ona sanduku “Mandhari Ileile, Maoni Tofauti.”) Kwa kweli, kuna faida ya kuona mambo kulingana na maoni ya mtu mwingine. Nyote wawili, yaani, wewe na mwenzi wako mliingia katika ndoa yenu mkiwa na matarajio ya pekee yaliyotegemea mambo kama vile malezi ya familia na utamaduni. Kwa hiyo, mnaweza kupendana sana na bado muwe na matarajio yasiyopatana.

      Kwa mfano, huenda wenzi Wakristo wakajua kanuni ya Biblia kuhusu ukichwa. (Waefeso 5:22, 23) Lakini, ukichwa utatumiwa kwa njia gani katika familia yenu, na ujitiisho utaonyeshwa jinsi gani? Je, nyote wawili mnaongozwa na kanuni hiyo ya Biblia, na je, mnajitahidi kikweli kuifuata?

      Mnaweza pia kuwa na maoni tofauti kuhusu masuala mengine katika maisha ya kila siku. Ni nani atakayefanya kazi fulani za nyumbani? Ni wakati gani mtakuwa pamoja na watu wa ukoo, na mtakuwa nao kwa muda gani? Wenzi Wakristo wataonyesha jinsi gani kwamba wanatanguliza mambo ya Ufalme maishani mwao? (Mathayo 6:33) Kuhusu pesa, ni rahisi kuwa na madeni, kwa hiyo ni vizuri kutumia pesa kwa busara na kutafuta njia za kuokoa pesa. Lakini kutumia pesa kwa busara na kuziokoa kunamaanisha nini? Mambo kama hayo yanahitaji kuzungumziwa waziwazi na kwa heshima. Mtafaidika sana mkifanya hivyo.

      Mazungumzo kama hayo yanaweza kuwasaidia kupata amani nyingi zaidi katika ndoa yenu, hata ikiwa matarajio fulani hayajatimizwa kufikia sasa. Kwa kweli, mtaweza hata zaidi kufuata himizo hili la mtume Paulo: “Endeleeni kuvumiliana na kusameheana kwa hiari ikiwa yeyote ana sababu ya kulalamika juu ya mwingine.”—Wakolosai 3:13.

  • Matarajio Yanapokosa Kutimizwa
    Mnara wa Mlinzi—2007 | Aprili 15
    • [Sanduku/Picha katika ukurasa wa 10]

      MANDHARI ILEILE, MAONI TOFAUTI

      “Ebu wazia umati wa watalii ukitazama mandhari yenye kuvutia sana. Ingawa kikundi chote kinatazama mandhari ileile, kila mtu aiona kwa njia tofauti. Kwa nini? Kwa sababu kila mtu mmoja-mmoja anaiona kutoka mahali tofauti. Hakuna watu wawili wanaosimama mahali palepale hasa. Zaidi ya hayo, si kila mtu anayekaza macho kwenye sehemu ileile ya mandhari hiyo. Kila mtu aona sehemu tofauti kuwa yenye kuvutia hasa. Ndivyo ilivyo katika ndoa. Hata wanapopatana sana, hakuna wenzi wawili wanaoshiriki maoni yaleyale hasa juu ya mambo. . . . Uwasiliano unatia ndani juhudi ya kupatanisha tofauti hizo katika uhusiano wa mwili mmoja. Hilo lataka kufanyiza wakati wa kuongea.”—Mnara wa Mlinzi, Agosti 1, 1993, ukurasa wa 4.

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki