-
Kushinda Udhaifu wa KibinadamuMnara wa Mlinzi—2001 | Machi 15
-
-
Kushinda Udhaifu wa Kibinadamu
“Kuweka akili juu ya mwili humaanisha kifo.”—WAROMA 8:6.
1. Watu wengine huuonaje mwili wa binadamu, na ni swali gani linalostahili kuzingatiwa?
“NITAKUSHUKURU kwa kuwa nimeumbwa kwa jinsi ya ajabu ya kutisha.” (Zaburi 139:14) Akaimba mtunga-zaburi Daudi alipokuwa anatafakari juu ya mwili wa binadamu ambao ni mmojawapo wa uumbaji wa Yehova. Badala ya kutoa sifa hiyo ya kweli, walimu fulani wa kidini huuona mwili kuwa mahali dhambi inapojificha, chombo cha dhambi. Umeitwa ‘vazi la ujinga, chanzo cha uovu, maiti iliyo hai, maiti inayotembea.’ Ni kweli vile mtume Paulo alivyosema: “Katika mwili wangu, halikai jambo lolote jema.” (Waroma 7:18) Lakini je, hilo lamaanisha kwamba tumenaswa katika mwili wetu wenye dhambi bila matumaini?
2. (a) “Kuweka akili juu ya mwili” humaanisha nini? (b) Ni mapambano gani kati ya “mwili” na “roho” yanayotukia ndani ya wanadamu wanaotamani kumpendeza Mungu?
2 Mara kwa mara Maandiko hutumia neno “mwili” kurejezea mtu katika hali yake ya kutokamilika akiwa mzao wa Adamu mwasi. (Waefeso 2:3; Zaburi 51:5; Waroma 5:12) Kile tulichorithi kutoka kwa Adamu kimetokeza “udhaifu wa mwili.” (Waroma 6:19) Naye Paulo alionya: “Kuweka akili juu ya mwili humaanisha kifo.” (Waroma 8:6) “Kuweka akili juu ya mwili” humaanisha kuongozwa na kuchochewa na tamaa za mwili wenye dhambi. (1 Yohana 2:16) Kwa hiyo ikiwa tunajitahidi kumpendeza Mungu, kuna mapambano daima kati ya hali yetu ya kiroho na hali yetu yenye dhambi ambayo hutushinikiza bila kukoma tufanye “kazi za mwili.” (Wagalatia 5:17-23; 1 Petro 2:11) Baada ya kueleza mapambano hayo yenye kuumiza yaliyokuwa ndani yake, Paulo alitamka hivi: “Mwenye taabu mimi! Ni nani ataniokoa kutoka katika mwili unaopatwa na kifo hiki?” (Waroma 7:24) Je, Paulo alikuwa mhasiriwa wa kishawishi asiye na kinga? Biblia hujibu kwa mkazo, la!
Uhalisi wa Kishawishi na Dhambi
3. Watu wengi huionaje dhambi na kishawishi, lakini Biblia hutoa onyo gani kuhusu mtazamo kama huo?
3 Dhambi ni dhana isiyokubalika kwa watu wengi leo. Wengine hutumia “dhambi” kiutani kama neno la kizamani la kufafanua dosari ndogondogo za kibinadamu. Hawatambui kwamba “lazima sisi sote tufanywe dhahiri mbele ya kiti cha hukumu cha Kristo, ili kila mmoja apate thawabu yake kwa mambo yaliyofanywa kuupitia mwili, kulingana na mambo ambayo amezoea, kama ni jambo jema au jambo ovu.” (2 Wakorintho 5:10) Huenda wengine wakaonyesha kwamba hawachukui kishawishi kwa uzito. Wengine huishi katika jamii ya watu ambao wanazingatia sana kujitosheleza mara moja, haidhuru ni kwa chakula, ngono, kujifurahisha, au kwa kutimiza jambo fulani. Wanataka kila kitu na wanakitaka sasa hivi! (Luka 15:12) Hawazingatii shangwe ya wakati ujao ya “uhai ulio halisi” bali huzingatia raha ya papo hapo tu. (1 Timotheo 6:19) Hata hivyo, Biblia hutufundisha kufikiria kwa makini na kuzingatia mambo ya wakati ujao, tukiepuka lolote ambalo laweza kutudhuru kiroho au vinginevyo. Mithali moja yenye kupuliziwa yasema: “Mwenye busara huyaona mabaya na kujificha; bali wajinga huendelea mbele wakaumia.”—Mithali 27:12.
4. Paulo alitoa ushauri gani kwenye 1 Wakorintho 10:12, 13?
4 Paulo alipowaandikia Wakristo walioishi Korintho—jiji lililojulikana kwa upotovu wake wa maadili—alitoa onyo la busara dhidi ya kishawishi na nguvu ya dhambi. Alisema: “Acheni yeye ambaye afikiri kuwa amesimama ajihadhari kwamba asianguke. Hakuna kishawishi ambacho kimewapata nyinyi ila kilicho kawaida kwa watu. Lakini Mungu ni mwaminifu, naye hatawaacha nyinyi mshawishwe kupita vile mwezavyo kuhimili, bali pamoja na hicho kishawishi ataifanya pia njia ya kutokea kusudi mweze kuvumilia hilo.” (1 Wakorintho 10:12, 13) Sisi sote—vijana kwa wazee, wanaume kwa wanawake—hukabili vishawishi vingi shuleni, kazini, au kwingineko. Kwa hiyo, acheni tuchunguze maneno ya Paulo na kuona yanamaanisha nini kwetu.
Usijitumaini Kupita Kiasi
5. Kwa nini ni hatari kujitumaini kupita kiasi?
5 Paulo asema: “Acheni yeye ambaye afikiri kuwa amesimama ajihadhari kwamba asianguke.” Ni hatari kutumaini kupita kiasi nguvu zetu za kiadili. Hilo laonyesha hatuelewi hali na nguvu ya dhambi. Kwa kuwa watu kama Musa, Daudi, Solomoni na mtume Petro walifanya dhambi, je, tuhisi kwamba sisi tu salama? (Hesabu 20:2-13; 2 Samweli 11:1-27; 1 Wafalme 11:1-6; Mathayo 26:69-75) “Mwenye hekima huogopa, akajitenga na uovu; bali mpumbavu ana ufidhuli, na kujitumai,” lasema andiko la Mithali 14:16. Isitoshe, Yesu alisema: “Roho ni yenye hamu, lakini mwili ni dhaifu.” (Mathayo 26:41) Kwa kuwa hakuna mwanadamu asiye mkamilifu ambaye hawezi kudhuriwa na tamaa zilizopotoka, twahitaji kuchukua onyo la Paulo kwa uzito na kukinza kishawishi, la sivyo tutakuwa katika hatari ya kuanguka.—Yeremia 17:9.
6. Yatupasa kujitayarisha lini na jinsi gani kwa ajili ya kishawishi?
6 Ni jambo la hekima kujitayarisha kwa matatizo ambayo huenda yakatokea bila kutarajiwa. Mfalme Asa alitambua kwamba kipindi cha amani ndio wakati uliofaa kwake kuimarisha ulinzi wake. (2 Mambo ya Nyakati 14:2, 6, 7) Alijua kwamba ingekuwa kuchelewa mno kujitayarisha wakati wa shambulio. Vivyo hivyo, maamuzi kuhusu yale tupaswayo kufanya vishawishi vinapotokea hufanywa vizuri zaidi wakati akili imetulia na mazingira ni yenye amani. (Zaburi 63:6) Danieli na marafiki wake wenye kumhofu Mungu walifanya uamuzi wao wa kuwa waaminifu kwa sheria ya Yehova kabla hawajashinikizwa kula vyakula vitamu vya mfalme. Hivyo, walishikilia imani yao, wakakataa kula chakula kisicho safi. (Danieli 1:8) Kabla hali zenye kushawishi hazijatokea, acheni tuimarishe azimio letu la kudumu tukiwa safi kiadili. Ndipo tutakapoweza kukinza dhambi.
7. Kwa nini inafariji kujua kwamba wengine wamefaulu kukinza kishawishi?
7 Tunapata faraja iliyoje kutokana na maneno ya Paulo: “Hakuna kishawishi ambacho kimewapata nyinyi ila kilicho kawaida kwa watu”! (1 Wakorintho 10:13) Mtume Petro aliandika: “Chukueni msimamo wenu dhidi ya [Ibilisi], mkiwa thabiti katika imani, mkijua kwamba mambo yaleyale kwa njia ya mateso yanatimizwa katika ushirika mzima wa ndugu zenu katika ulimwengu.” (1 Petro 5:9) Naam, wengine wamekabili vishawishi kama hivyo na kwa msaada wa Mungu wamefaulu kuvikinza, nasi pia twaweza kufanya hivyo. Hata hivyo, tukiwa Wakristo wa kweli tunaoishi katika ulimwengu uliopotoka, sote tunaweza kutarajia kushawishiwa siku moja. Basi, tunawezaje kuwa na hakika kwamba tutashinda udhaifu wa kibinadamu na kishawishi cha kufanya dhambi?
Tunaweza Kukinza Kishawishi!
8. Ni njia ipi rahisi ya kuepuka kishawishi?
8 Njia rahisi ya kuacha “kuwa watumwa wa dhambi” ni kuepuka kishawishi inapowezekana. (Waroma 6:6) Andiko la Mithali 4:14, 15 latusihi: “Usiingie katika njia ya waovu, wala usitembee katika njia ya wabaya. Jiepushe nayo, usipite karibu nayo, igeukie mbali, ukaende zako.” Mara nyingi tunajua kimbele kama hali fulani zingeelekea kutuongoza kwenye dhambi. Kwa hiyo, jambo lifaalo kufanya tukiwa Wakristo ni ‘kwenda zetu,’ tukiepuka yeyote na chochote na mahali popote ambapo panaweza kuamsha tamaa mbaya na kuchochea hisia kali za mapenzi zisizo safi.
9. Kukimbia hali zenye kushawishi kunakaziwaje katika Maandiko?
9 Kukimbia hali yenye kushawishi ni hatua nyingine rahisi ya kushinda kishawishi. Paulo alishauri: “Ukimbieni uasherati.” (1 Wakorintho 6:18) Naye aliandika: “Ikimbieni ibada ya sanamu.” (1 Wakorintho 10:14) Mtume huyo pia alimwonya Timotheo akimbie tamaa inayopita kiasi ya vitu vya kimwili, na vilevile “tamaa zenye kutukia ujanani.”—2 Timotheo 2:22; 1 Timotheo 6:9-11.
10. Ni vielelezo gani viwili vyenye kutofautiana vinavyoonyesha manufaa ya kukimbia kishawishi?
10 Hebu fikiria kisa cha Mfalme Daudi wa Israeli. Alipokuwa akitazama kutoka paa la jumba lake la kifalme, aliona mwanamke mrembo akioga na moyo wake ukajaa tamaa mbaya. Angeondoka kwenye paa hilo na kukimbia kishawishi hicho. Badala yake, aliuliza kuhusu mwanamke huyo—Bathsheba—na matokeo yakawa mabaya sana. (2 Samweli 11:1–12:23) Kwa upande mwingine, Yosefu alitendaje wakati mke mwenye kukosa maadili wa bwana-mkubwa wake alipomsihi alale naye? Simulizi hilo latuambia: “Aliendelea kumshawishi Yosefu siku baada ya siku, lakini Yosefu hakumsikiliza wala kukubali kulala naye kamwe.” Hata bila amri za Sheria ya Kimusa, ambayo haikuwa imetolewa, Yosefu alimjibu kwa kusema: “Nitawezaje basi kufanya uovu mbaya kama huo, na kumkosea Mungu”? Siku moja akamshika, akisema: “Lala na mimi!” Je, Yosefu aliendelea kukaa hapo na kujaribu kusababu naye? La. ‘Alikimbilia nje.’ Yosefu hakuruhusu kishawishi cha kufanya ngono kimshinde. Alikimbia!—Mwanzo 39:7-16, Biblia Habari Njema.
11. Huenda tukafanya nini ikiwa tunakabili kishawishi kinachotokea mara kwa mara?
11 Wakati mwingine kukimbia huonekana kama tendo la woga, lakini mara nyingi kujiondoa kutoka katika hali fulani ndilo jambo la hekima kufanya. Labda tunakabili kishawishi mahali pa kazi ambacho kinatokea mara kwa mara. Ingawa huenda isiwezekane kubadili kazi, kunaweza kuwa na njia nyinginezo za kujiondoa kutoka katika hali zenye kushawishi. Tunahitaji kukimbia chochote tunachojua kuwa hakifai, na kuazimia kufanya tu yale yafaayo. (Amosi 5:15) Kwingineko, kukimbia kishawishi kungemaanisha kuepuka vituo vya ponografia vya Internet na sehemu za vitumbuizo zenye kutilika shaka. Huenda kukimbia kishawishi pia kukamaanisha kuondolea mbali gazeti fulani au kutafuta marafiki wapya—wanaompenda Mungu na wanaoweza kutusaidia. (Mithali 13:20) Litakuwa jambo la hekima kukataa katakata jambo lolote ambalo latushawishi tufanye dhambi.—Waroma 12:9.
Jinsi Sala Iwezavyo Kusaidia
12. Tunamwomba Mungu nini tunaposali: “Usituingize katika kishawishi”?
12 Paulo atoa uhakikisho huu wenye kutia moyo: “Mungu ni mwaminifu, naye hatawaacha nyinyi mshawishwe kupita vile mwezavyo kuhimili, bali pamoja na hicho kishawishi ataifanya pia njia ya kutokea kusudi mweze kuvumilia hilo.” (1 Wakorintho 10:13) Njia moja ambayo Yehova hutusaidia ni kwa kujibu sala zetu za kupata msaada wake wa kupambana na kishawishi. Yesu Kristo alitufundisha kusali hivi: “Usituingize katika kishawishi, bali utukomboe kutokana na yule mwovu.” (Mathayo 6:13) Kwa kujibu sala hiyo ya kutoka moyoni, Yehova hatatuacha tushawishiwe; atatukomboa kutoka kwa Shetani na vitendo vyake vya hila. (Waefeso 6:11, NW, kielezi-chini) Yatupasa kumwomba Mungu atusaidie kutambua vishawishi na kuwa na nguvu za kuvikinza. Tukimsihi asiruhusu tushindwe tunaposhawishiwa, atatusaidia tusidanganywe na “yule mwovu,” Shetani.
13. Tunapaswa kufanya nini tunapokabili kishawishi chenye kuendelea?
13 Tunahitaji hasa kusali kwa bidii tunapokabili kishawishi chenye kuendelea. Vishawishi vingine vinaweza kutokeza mapambano makali sana ya akili, tukipambana na mawazo na mitazamo ambayo hutukumbusha kwa njia yenye kutokeza jinsi tulivyo dhaifu. (Zaburi 51:5) Kwa mfano, twaweza kufanya nini ikiwa tunasumbuliwa na kumbukumbu za zoea fulani potovu la zamani? Namna gani ikiwa tunashawishiwa kulirudia? Badala ya kujaribu tu kuzuia hisia hizo, mjulishe Yehova jambo hilo kupitia sala—tena na tena ikihitajika. (Zaburi 55:22) Kwa nguvu za Neno lake na roho yake takatifu, anaweza kutusaidia kuondoa maelekeo yasiyo safi akilini mwetu.—Zaburi 19:8, 9.
14. Kwa nini sala ni muhimu ili kukabiliana na kishawishi?
14 Alipoona mitume wake wakisinzia katika bustani ya Gethsemane, Yesu aliwasihi: “Fulizeni kulinda na kusali kwa kuendelea, ili msipate kuingia ndani ya jaribu. Bila shaka, roho ni yenye hamu, lakini mwili ni dhaifu.” (Mathayo 26:41) Njia moja ya kushinda kishawishi ni kuwa macho kutambua njia mbalimbali ambazo kishawishi kinaweza kutokea na kujua njia zake zenye hila. Ni muhimu pia kusali bila kukawia kuhusu kishawishi hicho ili tuweze kuwa tayari kiroho kupambana nacho. Kwa kuwa kishawishi hutushambulia sehemu ambazo sisi ni dhaifu zaidi, hatuwezi kukikinza peke yetu. Sala ni muhimu kwa sababu nguvu ambazo Mungu hutoa zaweza kutegemeza kinga yetu dhidi ya Shetani. (Wafilipi 4:6, 7) Huenda pia tukahitaji usaidizi wa kiroho na sala za “wanaume wazee wa kutaniko.”—Yakobo 5:13-18.
Kinza Kishawishi kwa Bidii
15. Ni nini kinachohusika katika kukinza kishawishi?
15 Mbali na kuepuka kishawishi inapowezekana, ni lazima tukikinze kwa bidii hadi kipite au hali ibadilike. Yesu aliposhawishiwa na Shetani, alimkinza hadi Ibilisi akaenda zake. (Mathayo 4:1-11) Mwanafunzi Yakobo aliandika: “Mpingeni Ibilisi, naye atawakimbia.” (Yakobo 4:7) Ukinzani unaanza kwa kuimarisha akili yetu kwa Neno la Mungu na kuazimia kwa dhati kwamba tutashikamana na viwango vyake. Tunafanya vema kukariri na kutafakari maandiko muhimu yanayozungumzia udhaifu wetu hususa. Lingekuwa jambo la hekima kutafuta Mkristo mkomavu—labda mzee—ambaye tunaweza kumwambia mahangaiko yetu na ambaye tunaweza kumwomba msaada tunaposhawishiwa kufanya jambo baya.—Mithali 22:17.
16. Tunawezaje kudumu tukiwa wanyofu kiadili?
16 Maandiko yanatusihi tuvae utu mpya. (Waefeso 4:24) Hilo lamaanisha kuruhusu Yehova atufinyange na kutubadili. Alipomwandikia Timotheo mfanyakazi mwenzake, Paulo alisema: “Fuatia uadilifu, ujitoaji-kimungu, imani, upendo, uvumilivu, tabia-pole. Pigana pigano bora la imani, pata mshiko imara juu ya uhai udumuo milele ambao uliitiwa.” (1 Timotheo 6:11, 12) Tunaweza “kufuatia uadilifu” kwa kusoma Neno la Mungu kwa bidii ili kupata ujuzi kamili wa utu wake, kisha kutenda kupatana na matakwa yake. Ratiba kamili ya utendaji wa Kikristo, kama vile kuhubiri habari njema na kuhudhuria mikutano, ni muhimu pia. Kumkaribia Mungu na kujinufaisha kikamili na maandalizi yake ya kiroho kutatusaidia kukua kiroho na kudumu tukiwa wanyofu kiadili.—Yakobo 4:8.
17. Tunajuaje kwamba Mungu hatatuachilia mbali wakati wa kishawishi?
17 Paulo anatuhakikishia kwamba kishawishi chochote kitupatacho hakitashinda uwezo tuliopewa na Mungu wa kushughulika nacho. Yehova ‘atafanya njia ya kutokea kusudi tuweze kukivumilia.’ (1 Wakorintho 10:13) Naam, Mungu haruhusu kishawishi kiwe chenye kulemea sana hivi kwamba tunakosa nguvu za kiroho za kutosha ili kudumisha uaminifu-maadili wetu ikiwa tunaendelea kumtegemea. Anataka tufaulu kukinza kwa bidii kishawishi cha kufanya yaliyo mabaya machoni pake. Isitoshe, tunaweza kuwa na imani katika ahadi hii yake: “Hakika sitakuacha kwa vyovyote wala kukuachilia mbali kwa vyovyote.”—Waebrania 13:5.
18. Kwa nini tunaweza kuwa na hakika ya kushinda udhaifu wa kibinadamu?
18 Paulo alikuwa na hakika kuhusu matokeo ya pambano lake binafsi dhidi ya udhaifu wa kibinadamu. Hakujiona kuwa mtu wa kusikitikiwa au mtu asiyeweza kushinda tamaa zake za mwili. Kinyume cha hilo, yeye alisema: “Jinsi ninavyokimbia si bila uhakika; jinsi ninavyoelekeza ngumi zangu ni ili nisiwe nikipiga hewa; lakini napiga-piga mwili wangu ngumi na kuuongoza kama mtumwa, ili, baada ya mimi kuwa nimewahubiria wengine, mimi mwenyewe nisiwe mwenye kukataliwa kwa njia fulani.” (1 Wakorintho 9:26, 27) Sisi pia tunaweza kufanya vita kwa mafanikio dhidi ya mwili wetu usio mkamilifu. Kupitia Maandiko, vichapo vinavyotegemea Biblia, mikutano ya Kikristo, na Wakristo wenzetu waliokomaa, Baba yetu wa mbinguni mwenye upendo huandaa vikumbusha daima ambavyo hutusaidia kufuatia mwenendo mnyofu. Kwa msaada wake, tunaweza kushinda udhaifu wa kibinadamu!
-
-
Wekeni Akili Juu ya Roho Mkaishi!Mnara wa Mlinzi—2001 | Machi 15
-
-
Wekeni Akili Juu ya Roho Mkaishi!
“Kuweka akili juu ya roho humaanisha uhai.”—WAROMA 8:6.
1, 2. Biblia huonyesha tofauti ipi baina ya “mwili” na “roho”?
SI JAMBO rahisi kudumisha msimamo safi kiadili mbele za Mungu katika jamii iliyopotoka ambayo hutukuza kutosheleza tamaa za kimwili. Hata hivyo, Maandiko huonyesha tofauti baina ya “mwili” na “roho,” yakionyesha waziwazi matokeo mabaya ya mtu kujiruhusu atawaliwe na mwili wenye dhambi na matokeo mazuri ya kuacha roho takatifu ya Mungu iwaongoze.
2 Kwa mfano, Yesu Kristo alisema: “Ni roho ndiyo ipayo uhai; mwili hauna mafaa hata kidogo. Semi ambazo nimewaambia ni roho na ni uhai.” (Yohana 6:63) Paulo aliwaandikia hivi Wakristo wa Galatia: “Mwili katika tamaa yao ni dhidi ya roho, na roho dhidi ya mwili; kwa maana hivi vyapingana.” (Wagalatia 5:17) Paulo pia alisema: “Yeye anayepanda katika mwili wake atavuna ufisadi kutokana na mwili wake, lakini yeye anayepanda katika roho atavuna uhai udumuo milele kutokana na roho.”—Wagalatia 6:8.
3. Ni nini kinachohitajika ili kuacha tamaa na maelekeo yasiyofaa?
3 Roho takatifu ya Yehova—kani yake ya utendaji—inaweza kuondoa kabisa “tamaa za kimwili” zisizo safi na pia hali ya kutawaliwa na mwili wetu wenye dhambi inayoweza kuleta uharibifu. (1 Petro 2:11) Ili kujiweka huru na utumwa wa maelekeo mabaya, ni muhimu kupata msaada wa roho ya Mungu, kwa kuwa Paulo aliandika: “Kuweka akili juu ya mwili humaanisha kifo, bali kuweka akili juu ya roho humaanisha uhai na amani.” (Waroma 8:6) Inamaanisha nini kuweka akili juu ya roho?
“Kuweka Akili Juu ya Roho”
4. “Kuweka akili juu ya roho” humaanisha nini?
4 Paulo alipoandika kuhusu “kuweka akili juu ya roho,” alitumia neno la Kigiriki ambalo lamaanisha “njia ya kufikiri, (kuweka) akili, . . . lengo, tamaa, jitihada.” Kitenzi kinachohusiana na neno hilo chamaanisha “kufikiri, kuweka akili katika njia fulani.” Hivyo, kuweka akili juu ya roho humaanisha kuongozwa, kutawaliwa, na kuchochewa na kani ya Yehova ya utendaji. Humaanisha kwamba tunakuwa tayari kuacha mawazo yetu, maelekeo yetu, na tamaa zetu ziongozwe kikamili na roho takatifu ya Mungu.
5. Ni kwa kadiri gani sisi twapaswa kukubali kuongozwa na roho takatifu?
5 Paulo alipozungumza juu ya kuwa ‘watumwa kwa roho,’ alikuwa anakazia ni kwa kadiri gani sisi twapaswa kukubali kuongozwa na roho takatifu. (Waroma 7:6) Kwa msingi wa imani yao katika dhabihu ya fidia ya Yesu, Wakristo wamekombolewa kutoka katika utawala wa dhambi na hivyo ‘wamekufa’ kuhusiana na hali yao ya zamani ya kuwa watumwa wa dhambi. (Waroma 6:2, 11) Wale ambao kitamathali wamekufa kwa njia hiyo bado wako hai kimwili na sasa wako huru kumfuata Kristo wakiwa “watumwa wa uadilifu.”—Waroma 6:18-20.
Badiliko Lenye Kutokeza
6. Ni badiliko gani wanalofanya wale wanaokuwa “watumwa wa uadilifu”?
6 Kuacha kuwa “watumwa wa dhambi” na kuanza kumtumikia Mungu tukiwa “watumwa wa uadilifu” ni badiliko lenye kutokeza kwelikweli. Kuhusu watu fulani ambao walifanya badiliko kama hilo, Paulo aliandika: ‘Lakini mmeoshwa mkawa safi, mmetakaswa, mmetangazwa kuwa waadilifu katika jina la Bwana wetu Yesu Kristo na kwa roho ya Mungu wetu.’—Waroma 6:17, 18; 1 Wakorintho 6:11.
7. Kwa nini ni muhimu kuona mambo jinsi Yehova ayaonavyo?
7 Ili kufanya badiliko kama hilo lenye kutokeza, kwanza tunahitaji kujua jinsi Yehova aonavyo mambo. Karne kadhaa zilizopita, mtunga-zaburi Daudi aliomba Mungu kwa bidii sana hivi: “Ee BWANA, unijulishe njia zako . . . Uniongoze katika kweli yako, na kunifundisha.” (Zaburi 25:4, 5) Yehova alimsikiliza Daudi, na Yeye anaweza pia kujibu sala kama hiyo ya watumishi wake leo. Kwa kuwa njia za Mungu na kweli yake ni safi na takatifu, kuzitafakari kutatusaidia ikiwa tunashawishiwa kutosheleza tamaa za mwili zisizo safi.
Fungu Muhimu la Neno la Mungu
8. Kwa nini ni muhimu sana tujifunze Biblia?
8 Neno la Mungu Biblia, limetokana na roho yake. Hivyo, kusoma na kujifunza Biblia—kila siku ikiwezekana—ni njia moja muhimu ya kuruhusu roho hiyo itende kazi juu yetu. (1 Wakorintho 2:10, 11; Waefeso 5:18) Kujaza akili yetu na moyo wetu kweli na kanuni za Biblia kutatusaidia kukinza mashambulio dhidi ya hali yetu ya kiroho. Naam, vishawishi vya ukosefu wa maadili vinapotokea, roho ya Mungu inaweza kutukumbusha Maandiko na kanuni zenye kutoa mwongozo ambazo zaweza kuimarisha azimio letu la kutenda kupatana na mapenzi ya Mungu. (Zaburi 119:1, 2, 99; Yohana 14:26) Kwa hiyo, hatudanganyiki kufuata mwenendo usiofaa.—2 Wakorintho 11:3.
9. Funzo la Biblia huimarishaje azimio letu la kudumisha uhusiano wetu na Yehova?
9 Tuendeleapo kujifunza Maandiko kwa unyofu na kwa bidii, tukisaidiwa na vichapo vinavyotegemea Biblia, roho ya Mungu inaanza kuongoza akili na moyo wetu, ikifanya tustahi zaidi viwango vya Yehova. Uhusiano wetu na Mungu unakuwa jambo lililo muhimu zaidi maishani mwetu. Tunapokabiliwa na kishawishi, hatutaruhusu mawazo juu ya jinsi iwezavyo kufurahisha kutenda mabaya. Badala yake, hangaiko letu la kwanza ni kudumisha uaminifu-maadili wetu kwa Yehova. Kuthamini sana uhusiano wetu pamoja naye hutuchochea kupambana na mwelekeo wowote unaoweza kuudhuru au kuuharibu.
“Sheria Yako Naipenda Mno Ajabu”
10. Kwa nini kutii sheria ya Yehova ni kwa lazima ili kuweka akili juu ya roho?
10 Ikiwa tutaweka akili juu ya roho, basi kujua tu Neno la Mungu hakutoshi. Mfalme Solomoni alijua vizuri sana viwango vya Yehova, lakini baadaye maishani mwake akashindwa kuishi kulingana navyo. (1 Wafalme 4:29, 30; 11:1-6) Ikiwa tunafikiria mambo ya kiroho, tutaona uhitaji wa kujua yale Biblia isemayo na pia kutii sheria ya Mungu kwa moyo wote. Hilo lamaanisha kuchunguza viwango vya Yehova kwa makini na kujitahidi kuvifuata. Mtunga-zaburi alikuwa na mtazamo wa aina hiyo. Aliimba hivi: “Sheria yako naipenda mno ajabu, ndiyo kutafakari kwangu mchana kutwa.” (Zaburi 119:97) Tunapojishughulisha kikweli kufuata sheria ya Mungu, tunachochewa kuonyesha sifa za kimungu. (Waefeso 5:1, 2) Badala ya kuwa hoi na kuvutwa kufanya mabaya, sisi huonyesha matunda ya roho, na tamaa ya kumpendeza Yehova hutuepusha na ‘kazi mbaya za mwili.’—Wagalatia 5:16, 19-23; Zaburi 15:1, 2.
11. Unaweza kuelezaje kwamba sheria ya Yehova inayokataza uasherati ni ulinzi kwetu?
11 Tunawezaje kusitawisha staha yenye kina kirefu na upendo kwa sheria ya Yehova? Njia moja ni kwa kuchunguza thamani yake kwa makini. Hebu fikiria sheria ya Mungu inayoruhusu uhusiano wa kingono katika ndoa tu na kukataza uasherati na uzinzi. (Waebrania 13:4) Je, kutii amri hiyo hutunyima chochote chema? Je, Baba wa mbinguni mwenye upendo angetunga sheria inayotunyima kitu fulani chenye manufaa? La, hasha! Hebu tazama yanayowapata watu wengi ambao hawaishi kupatana na viwango vya maadili vya Yehova. Mara nyingi mimba zisizotakiwa huwafanya watoe mimba au labda kufunga ndoa za mapema zisizo na furaha. Wengi wanalazimika kulea watoto bila mume au mke. Isitoshe, wale wanaofanya uasherati hukabili hatari ya kupatwa na maradhi yanayoambukizwa kingono. (1 Wakorintho 6:18) Na ikiwa mtumishi wa Yehova anafanya uasherati, matokeo ya kihisia-moyo yanaweza kuwa yenye kuumiza. Kujaribu kuzuia kusumbuliwa na dhamiri yenye hatia kwaweza kukukosesha usingizi usiku na kukufanya uumie sana kiakili. (Zaburi 32:3, 4; 51:3) Hivyo basi, si wazi kwamba sheria ya Yehova inayokataza uasherati imekusudiwa kutulinda? Ndiyo, kwa kweli tunanufaika sana tunapodumisha usafi wa kiadili!
Sali Upate Msaada wa Yehova
12, 13. Kwa nini inafaa kusali tunaposongwa na tamaa zenye dhambi?
12 Bila shaka, kuweka akili juu ya roho huhitaji sala ya kutoka moyoni. Inafaa kuomba msaada wa roho ya Mungu, kwa kuwa Yesu alisema: “Ikiwa nyinyi . . . mwajua jinsi ya kuwapa watoto wenu zawadi zilizo njema, je, si zaidi sana yule Baba aliye mbinguni atawapa roho takatifu wale wanaomwomba!” (Luka 11:13) Katika sala, tunaweza kuonyesha kuwa tunategemea roho itusaidie kuhusiana na udhaifu wetu. (Waroma 8:26, 27) Tukitambua kwamba tunaathiriwa na tamaa au mitazamo yenye dhambi, au ikiwa mwamini mwenzetu mwenye upendo anatufahamisha mambo hayo, lingekuwa jambo la hekima kuyataja kihususa katika sala zetu na kumwomba Mungu atusaidie kushinda maelekeo hayo.
13 Yehova anaweza kutusaidia tukazie fikira mambo ya uadilifu, yaliyo safi kiadili, yenye wema wa adili na yenye kustahili sifa. Inafaa kama nini kumwomba dua kwa bidii ili “amani ya Mungu” ilinde mioyo yetu na nguvu zetu za akili! (Wafilipi 4:6-8) Kwa hiyo, acheni tusali kupata msaada wa Yehova ili ‘kufuatia uadilifu, ujitoaji-kimungu, imani, upendo, uvumilivu, tabia-pole.’ (1 Timotheo 6:11-14) Kwa msaada wa Baba yetu wa mbinguni, mahangaiko na vishawishi havitaongezeka hadi vitushinde. Badala yake, maisha yetu yatakuwa na utulivu utokao kwa Mungu.
Msiitie Kihoro Roho
14. Kwa nini roho ya Mungu ni kani ya usafi?
14 Watumishi wa Yehova waliokomaa hutumia kibinafsi ushauri huu wa Paulo: “Msiuzime moto wa ile roho.” (1 Wathesalonike 5:19) Kwa kuwa roho ya Mungu ni “roho ya utakatifu,” ni safi, yenye kutakata na takatifu. (Waroma 1:4) Inapotenda kazi juu yetu, roho hiyo inakuwa kani ya utakatifu, au usafi. Hutusaidia tuendelee kuishi maisha safi yanayoonyesha utii kwa Mungu. (1 Petro 1:2) Zoea lolote lisilo safi laonyesha kupuuza roho hiyo, na hilo laweza kuwa na matokeo yenye maafa. Jinsi gani?
15, 16. (a) Tunawezaje kuitia kihoro roho ya Mungu? (b) Tunawezaje kuepuka kuitia kihoro roho ya Yehova?
15 Paulo aliandika: “Msiwe mkiitia kihoro roho takatifu ya Mungu, ambayo kwayo mmetiwa muhuri kwa ajili ya siku yakuachiliwa kupitia fidia.” (Waefeso 4:30) Maandiko hutambulisha roho ya Yehova kuwa muhuri, au ‘arbuni ya kilichokuwa kije’ kwa ajili ya Wakristo watiwa-mafuta walio waaminifu. Nacho ni uhai wa kimbingu usioweza kufa. (2 Wakorintho 1:22; 1 Wakorintho 15:50-57; Ufunuo 2:10) Roho ya Mungu inaweza kuelekeza watiwa-mafuta na wenzao walio na tumaini la kidunia kuwa waaminifu maishani na inaweza kuwasaidia kuepuka kazi zenye dhambi.
16 Mtume alionya dhidi ya maelekeo ya kusema uwongo, kuiba, mwenendo wa aibu na kadhalika. Kama tungejiruhusu tuvutiwe na mambo hayo, tungekuwa tunatenda kinyume cha ushauri wa Neno la Mungu lililopuliziwa kwa roho. (Waefeso 4:17-29; 5:1-5) Tungekuwa, angalau kwa kadiri fulani, tukiitia kihoro roho ya Mungu, na bila shaka hilo ni jambo tunalotaka kuepuka. Kwa sababu hiyo, yeyote kati yetu akianza kupuuza ushauri wa Neno la Yehova, huenda akaanza kusitawisha mitazamo au tabia ambazo zaweza kufanya atende dhambi ya kukusudia na kupoteza kabisa kibali cha Mungu. (Waebrania 6:4-6) Ingawa huenda tukawa hatuzoei dhambi sasa hivi, tunaweza kuwa tunaelekea kufanya hivyo. Kwa kuendelea kutenda kinyume cha mwongozo wa roho, tungekuwa tunaitia kihoro. Tungekuwa pia tunamkinza na kumtia kihoro Yehova, aliye chanzo cha roho takatifu. Tukiwa watu wampendao Mungu hatutaki kufanya hivyo hata kidogo. Badala yake, na tusali kupata msaada wa Yehova ili tusiitie kihoro roho yake bali tuweze kulitukuza jina lake takatifu kwa kuendelea kuweka akili juu ya roho.
Endelea Kuweka Akili Juu ya Roho
17. Tunaweza kuweka miradi gani ya kiroho, na kwa nini ni jambo la hekima kujitahidi kuifikia?
17 Njia moja yenye kutokeza ambayo tunaweza kuendelea kuweka akili juu ya roho, ni kuweka miradi ya kiroho na kujitahidi kuifikia. Ikitegemea mahitaji na hali zetu, miradi yetu yaweza kutia ndani kuboresha kawaida yetu ya kujifunza, kuongeza utendaji wetu katika kazi ya kuhubiri, au kujitahidi kufikia mapendeleo hususa ya utumishi, kama vile huduma ya wakati wote ya upainia, utumishi wa Betheli, au kazi ya mishonari. Kufanya hivyo kutafanya akili yetu iendelee kushughulika na masilahi ya kiroho na kutatusaidia tusishindwe na udhaifu wetu wa kibinadamu au kuchochewa na miradi ya kujipatia vitu vya kimwili na tamaa zisizopatana na Maandiko ambazo ni za kawaida katika mfumo huu wa mambo. Kwa hakika hilo ndilo jambo la hekima kufanya, kwa kuwa Yesu alisihi hivi: “Komeni kujiwekea akiba ya hazina duniani, ambako nondo na kutu hula kabisa, na ambako wezi huvunja na kuiba. Badala ya hivyo, jiwekeeni akiba ya hazina mbinguni, ambako wala nondo wala kutu haili kabisa, na ambako wezi hawavunji na kuiba. Kwa maana ilipo hazina yako, ndipo moyo wako utakapokuwa pia.”—Mathayo 6:19-21.
18. Kwa nini ni muhimu sana kuendelea kuweka akili juu ya roho siku hizi za mwisho?
18 Bila shaka, kuweka akili juu ya roho na kudhibiti tamaa za kilimwengu ndiyo njia ya hekima katika ‘siku hizi za mwisho.’ (2 Timotheo 3:1-5) Kwani, “ulimwengu unapitilia mbali na ndivyo na tamaa yao, lakini yeye ambaye hufanya mapenzi ya Mungu hudumu milele.” (1 Yohana 2:15-17) Kwa mfano, ikiwa kijana Mkristo afuatia mradi wa utumishi wa wakati wote, huenda huo ukamsaidia wakati wa miaka migumu ya kubalehe au ya ujana. Anaposhinikizwa aache msimamo wake, mtu kama huyo atakuwa na ufahamu mzuri wa mambo ambayo anataka kutimiza katika utumishi wa Yehova. Mtu wa kiroho kama huyo ataliona kuwa jambo lisilo la hekima, hata la kipumbavu, kuacha kutimiza miradi ya kiroho kwa ajili ya kufuatia vitu vya kimwili au kufuatia raha yoyote iwezayo kuletwa na dhambi. Kumbuka kwamba Musa ambaye alikuwa na mwelekeo wa kiroho ‘alichagua kutendwa vibaya pamoja na watu wa Mungu badala ya kuwa na mfurahio wa muda wa dhambi.’ (Waebrania 11:24, 25) Tuwe vijana au wazee, sisi hufanya uchaguzi kama huo tunapoendelea kuweka akili juu ya roho badala ya mwili wenye dhambi.
19. Tutapata manufaa gani tukiendelea kuweka akili juu ya roho?
19 “Kuweka akili juu ya mwili humaanisha uadui na Mungu,” ilhali “kuweka akili juu ya roho humaanisha uhai na amani.” (Waroma 8:6, 7) Tukiendelea kuweka akili juu ya roho, tutapata amani nyingi. Mioyo yetu na nguvu zetu za akili zitalindwa kikamili dhidi ya uvutano wa hali yetu yenye dhambi. Tutaweza kukinza vema zaidi vishawishi vya kutenda mabaya na tutapata msaada wa Mungu kukabiliana na pambano lenye kuendelea baina ya mwili na roho.
20. Kwa nini tunaweza kuwa na hakika kwamba inawezekana kushinda katika pambano baina ya mwili na roho?
20 Kwa kuendelea kuweka akili juu ya roho, tunadumisha uhusiano ulio muhimu kati yetu na Yehova, aliye chanzo cha uhai na roho takatifu pia. (Zaburi 36:9; 51:11) Shetani Ibilisi na wawakilishi wake wanafanya kila wawezalo kuharibu uhusiano wetu pamoja na Yehova Mungu. Wanajaribu kudhibiti akili zetu, wakijua kwamba tukishindwa, hatimaye jambo hilo litasababisha uadui na Mungu, kisha kifo. Lakini tunaweza kushinda katika pambano hili baina ya mwili na roho. Paulo alishinda, kwa kuwa alipoandika juu ya pambano lake mwenyewe, kwanza aliuliza hivi: “Ni nani ataniokoa kutoka katika mwili unaopatwa na kifo hiki?” Kisha, akionyesha kwamba angeweza kuokolewa, akatamka: “Shukrani kwa Mungu kupitia Yesu Kristo Bwana wetu!” (Waroma 7:21-25) Sisi pia tunaweza kumshukuru Mungu kupitia Kristo kwa kutuandalia njia ya kukabiliana na udhaifu wa kibinadamu na kuendelea kuweka akili juu ya roho tukiwa na tumaini zuri sana la kupata uhai udumuo milele.—Waroma 6:23.
-