-
Je, Inawezekana Kuwa na Uradhi?Mnara wa Mlinzi—2010 | Novemba 1
-
-
Je, Inawezekana Kuwa na Uradhi?
“Kuridhika kunawatajirisha maskini; kutoridhika kunawafanya matajiri wawe maskini.”—Benjamin Franklin.
KAMA msemo huo unavyoonyesha, watu wengi wamegundua kwamba uradhi hauwezi kununuliwa kama bidhaa. Si ajabu kwamba ni vigumu kuwa na uradhi—ile hali ya ndani ya kuhisi kuwa umeridhika au umetosheka—kwa kuwa tunaishi katika ulimwengu unaotuchochea kuwa na tamaa ya kupata mali nyingi, kutimiza mengi, au kufurahia maisha kama wengine wanavyofurahia! Je, umewahi kupatwa na hali yoyote kati ya hizi zifuatazo?
• Matangazo ya biashara yanayokuchochea uamini kwamba licha ya vitu vingi ambavyo tayari umenunua, unahitaji kununua vitu vingine zaidi ili uridhike.
• Mashindano kazini au shuleni yanayokuchochea ulinganishe uwezo wako na wa wengine.
• Kutothaminiwa kwa mambo unayowafanyia wengine.
• Kuchochewa na marafiki utamani vitu walivyo navyo.
• Kukosa majibu kwa maswali muhimu kuhusu maisha.
Ikiwa umepatwa na hali kama hizo, je, unaweza kuwa mwenye uradhi? Mtume Paulo alisema ‘nimejifunza jinsi ya kuridhika.’ Nyakati fulani alikuwa na vitu vingi na nyakati nyingine vitu vichache. Marafiki zake walimheshimu lakini wengine walimdharau. Hata hivyo, alisema “nimejizoeza kuridhika katika kila hali na mahali.”—Italiki ni zetu; Wafilipi 4:11, 12, Biblia Habari Njema.
Kuridhika ni fumbo kwa wale ambao hawajawahi kuchukua hatua ya kusitawisha hali hiyo, lakini kama Paulo alivyosema, mtu anaweza kujizoeza kuwa mwenye uradhi. Tunakualika uchunguze njia tano zinazoweza kukusaidia kuwa mwenye kuridhika, ambazo zinapatikana katika Neno la Mungu, Biblia.
-
-
Wapende Watu, Bali Si Pesa na MaliMnara wa Mlinzi—2010 | Novemba 1
-
-
Njia ya 1
Wapende Watu, Bali Si Pesa na Mali
BIBLIA INAFUNDISHA NINI? “Kupenda pesa ni chanzo cha mambo mabaya ya namna zote.”—1 Timotheo 6:10.
KWA NINI INAWEZA KUWA VIGUMU? Matangazo ya biashara yanatuchochea kutoridhika na vitu tulivyo navyo. Wanaotoa matangazo hayo wanataka tufanye kazi kwa muda mrefu ili tupate pesa za kununulia vitu vya kisasa zaidi, vizuri zaidi, na vikubwa zaidi. Pesa ni kishawishi, na ni rahisi sana kuanza kuzipenda. Hata hivyo, Biblia inaonya kwamba mtu anayependa pesa hatatosheka kamwe. Mfalme Sulemani aliandika hivi: “Anayependa fedha hatatosheka na fedha, wala anayependa mali hatatosheka na mapato.”—Mhubiri 5:10.
UNAWEZA KUFANYA NINI? Mwige Yesu, na ujifunze kuwapenda watu zaidi kuliko mali. Yesu alikuwa tayari kutoa vyote alivyokuwa navyo, hata uhai wake mwenyewe, kwa sababu aliwapenda watu. (Yohana 15:13) Alisema: “Kuna furaha zaidi katika kutoa kuliko ilivyo katika kupokea.” (Matendo 20:35) Tukijizoeza kutumia wakati na mali zetu kuwasaidia wengine, wao pia watatutendea vivyo hivyo. Yesu alisema, “Muwe na mazoea ya kuwapa watu, na watu watawapa ninyi.” (Luka 6:38) Wale wanaofuatilia pesa na mali wanapata mateso na maumivu. (1 Timotheo 6:9, 10) Kwa upande mwingine, uradhi wa kweli unatokana na kupendwa na kuwapenda wengine.
Kwa nini usijaribu kuchanganua hali zako na kuona kama unaweza kurahisisha maisha yako? Je, unaweza kupunguza vitu ulivyo navyo, au vitu unavyotaka kununua? Ukifanya hivyo, huenda ukagundua kwamba una muda na nguvu zaidi za kufanya mambo muhimu katika maisha, yaani, kuwasaidia watu na kumtumikia Mungu, ambaye amekupa vyote ulivyo navyo.—Mathayo 6:24; Matendo 17:28.
[Picha katika ukurasa wa 4]
“Muwe na mazoea ya kuwapa watu, na watu watawapa ninyi”
-
-
Dumisha Mtazamo wa Kuwa na ShukraniMnara wa Mlinzi—2010 | Novemba 1
-
-
Njia ya 3
Dumisha Mtazamo wa Kuwa na Shukrani
BIBLIA INAFUNDISHA NINI? “Kuhusiana na kila jambo toeni shukrani.”—1 Wathesalonike 5:18.
KWA NINI INAWEZA KUWA VIGUMU? Tumezungukwa na watu wenye kiburi na wasio na shukrani, na tunaweza kuanza kuwaiga. (2 Timotheo 3:1, 2) Zaidi ya hilo, tunaweza kuhisi kwamba tunasukumwa kuwa na mambo mengi zaidi ya kufanya katika maisha yetu ambayo tayari yana shughuli nyingi. Tunaweza kulemewa na matatizo au kufuatilia sana mapendezi yetu wenyewe hivi kwamba tunakosa kuthamini mambo mazuri ambayo tayari tunayo, au kuwashukuru wengine kwa mambo wanayotufanyia.
UNAWEZA KUFANYA NINI? Tenga wakati wa kutafakari mambo mazuri ambayo sasa unafurahia. Bila shaka, unaweza kuhisi kwamba umelemewa na matatizo. Lakini fikiria mfano wa Mfalme Daudi. Wakati fulani alihisi kuwa amevunjika moyo na kulemewa na majaribu. Hata hivyo, alisali kwa Mungu hivi: “Nimetafakari juu ya utendaji wako wote; kwa kupenda niliendelea kuhangaikia kazi ya mikono yako mwenyewe.” (Zaburi 143:3-5) Ingawa alipatwa na majaribu, Daudi alidumisha mtazamo wa kuwa mwenye shukrani na mwenye kuridhika.
Fikiria mambo ambayo wengine wamefanya ili kukusaidia, na uwashukuru kwa jitihada zao. Yesu aliweka kielelezo kizuri sana katika jambo hilo. Kwa mfano, wakati rafiki yake Maria alipommiminia kichwani na miguuni mafuta ya bei ya juu, watu fulani waliuliza: “Kwa nini hasara hii ya mafuta yenye marashi?”a Walalamikaji hao walihisi kwamba mafuta hayo yalipaswa kuuzwa, kisha maskini wapewe pesa hizo. Yesu aliwajibu hivi: “Mwacheni. Kwa nini mnataka kumsumbua?” Kisha akaongeza: “Amenifanyia tendo zuri.” (Marko 14:3-8; Yohana 12:3) Badala ya kukazia kile ambacho Maria hakufanya, Yesu alishukuru kwa kile alichofanya.
Watu fulani huanza kuthamini watu wa familia, marafiki, au baraka nyingine baada ya kupoteza watu hao au baraka hizo. Unaweza kuepuka hali hiyo kwa kutafakari kuhusu mambo mazuri unayofurahia sasa! Tunakutia moyo ufikirie au kuandika mambo ambayo yanakufanya uwe mwenye shukrani.
Kwa kuwa “kila zawadi njema” hutoka kwa Mungu, tunafanya vizuri kumshukuru katika sala. (Yakobo 1:17) Kufanya hivyo kila wakati, kunaweza kutusaidia kudumisha mtazamo wa kuwa wenye shukrani na wenye kuridhika.—Wafilipi 4:6, 7.
[Maelezo ya Chini]
a Katika karne ya kwanza, kumimina mafuta juu ya kichwa cha mgeni ilikuwa ishara ya kumkaribisha; kummiminia mafuta miguuni ilikuwa ishara ya unyenyekevu.
[Picha katika ukurasa wa 6]
Je, unawashukuru wengine kwa mambo wanayokufanyia?
-
-
Chagua Marafiki Zako kwa HekimaMnara wa Mlinzi—2010 | Novemba 1
-
-
Njia ya 4
Chagua Marafiki Zako kwa Hekima
BIBLIA INAFUNDISHA NINI? “Anayetembea na watu wenye hekima atakuwa na hekima.”—Methali 13:20.
KWA NINI INAWEZA KUWA VIGUMU? Marafiki zetu wanaweza kutusaidia tuwe na uradhi au tusiwe na uradhi. Mtazamo na maongezi yao yanaweza kuathiri mtazamo wetu kuelekea maisha.—1 Wakorintho 15:33.
Kwa mfano, fikiria simulizi la Biblia kuhusu wanaume 12 waliorudi kutoka kupeleleza nchi ya Kanaani. Wengi wao ‘walizidi kuwaletea wana wa Israeli habari mbaya juu ya nchi waliyokuwa wameipeleleza.’ Hata hivyo, wawili kati yao waliisifu nchi ya Kanaani, wakiiita “nchi nzuri sana, sana.” Lakini mtazamo usiofaa wa wale wapelelezi kumi ulienea kati ya watu. “Kusanyiko lote likapaaza sauti zao,” simulizi hilo linasema, “na wana wote wa Israeli wakaanza kunung’unika.”—Hesabu 13:30–14:9.
Vivyo hivyo leo, watu wengi ni “wanung’unikaji, walalamikaji juu ya fungu lao maishani.” (Yuda 16) Ni vigumu sana kuridhika ikiwa una marafiki ambao hawaridhiki kamwe.
UNAWEZA KUFANYA NINI? Chunguza mazungumzo kati yako na marafiki zako. Je, mara nyingi marafiki hao hujisifu kwa sababu ya vitu walivyo navyo, au nyakati zote wanalalamika kwa sababu ya vitu ambavyo hawana? Nao wanakuona kuwa rafiki wa aina gani? Je, unajaribu kuwafanya marafiki zako wakuonee wivu, au unawatia moyo waridhike na vitu walivyo navyo?
Fikiria mfano uliowekwa na Daudi, ambaye angekuja kuwa mfalme, na Yonathani, mwana wa Mfalme Sauli. Daudi alikuwa akiishi nyikani kama mkimbizi. Mfalme Sauli alihisi kwamba cheo chake akiwa mfalme kilikuwa kinahatarishwa na Daudi na hivyo akataka kumuua. Hata ingawa Yonathani angekuwa mfalme baada ya baba yake, tayari alikuwa mmoja wa marafiki wa karibu wa Daudi. Yonathani alitambua kwamba Mungu alikuwa amemweka rasmi Daudi kuwa mfalme, na aliridhika kumuunga mkono rafiki yake.—1 Samweli 19:1, 2; 20:30-33; 23:14-18.
Unahitaji marafiki kama hao, ambao wanajitahidi kuridhika na wanaokutakia mema. (Methali 17:17) Bila shaka, ili upate marafiki kama hao, wewe pia unahitaji kuwa na sifa nzuri.—Wafilipi 2:3, 4.
[Picha katika ukurasa wa 7]
Je, marafiki zako wanakusaidia uwe na uradhi au usiwe na uradhi?
-
-
Tosheleza Uhitaji Wako wa KirohoMnara wa Mlinzi—2010 | Novemba 1
-
-
Njia ya 5
Tosheleza Uhitaji Wako wa Kiroho
BIBLIA INAFUNDISHA NINI? “Wenye furaha ni wale wanaotambua uhitaji wao wa kiroho.”—Mathayo 5:3.
KWA NINI INAWEZA KUWA VIGUMU? Kuna maelfu ya dini tofauti-tofauti, na nyingi ya dini hizo zinafundisha njia zinazopingana za kutosheleza uhitaji wako wa kiroho. Unaweza kujua jinsi gani dini inayofundisha ukweli na inayompendeza Mungu kikweli? Baadhi ya waandishi maarufu wa vitabu wanadai kuwa kumwamini Mungu na kujitoa kwake ni jambo lisilopatana na akili na lina madhara. Gazeti Maclean’s linaeleza kifupi maoni ya mtu mmoja maarufu asiyeamini kuwa kuna Mungu, likisema hivi: “Fundisho la Wakristo kwamba kuna jambo fulani tusiloweza kuthibitisha kisayansi wala kulitambua kupitia hisi zetu . . . linafanya maisha haya yaonekane kuwa yasiyo na thamani na kutufanya tuwe na mwelekeo wa kusababisha vurugu.”
UNAWEZA KUFANYA NINI? Chunguza mambo yanayothibitisha kwamba kuna Mungu. (Waroma 1:20; Waebrania 3:4) Usimruhusu yeyote akuvunje moyo ili usitafute majibu ya maswali muhimu, kama vile, Kwa nini tupo hapa? Je, kuna uhai baada ya kifo? Kwa nini tunateseka sana? Mungu anataka nifanye nini? Kupata majibu yenye kuridhisha kwa maswali hayo ni muhimu ili upate uradhi wa kudumu.
Hata hivyo, usikubali tu kila kitu unachoambiwa bila kufikiri. Neno la Mungu linakutia moyo utumie ‘nguvu zako za kufikiri’ ili ujihakikishie lile linalokubalika kwake. (Waroma 12:1, 2) Ukifanya hivyo utabarikiwa sana. Ikiwa unatenga wakati ili kujifunza Biblia na kutumia mashauri yake, utaepuka matatizo, kupunguza mahangaiko, na kuongeza furaha yako maishani. Hiyo ni ahadi ya kweli. Mamilioni ya watu wa malezi mbalimbali wamefaidika kwa kujifunza kweli kumhusu Mungu na makusudi yake. Kwa mfano, soma masimulizi halisi ya maisha katika ukurasa wa 18 mpaka 21 wa gazeti hili.
Unapoendelea kunufaika kwa kutumia mashauri ya Biblia yenye hekima, ujitoaji wako kwa Mungu unaimarika zaidi. Tunakutia moyo ukubali mwaliko wa kujifunza Biblia pamoja na Mashahidi wa Yehova. Ukifanya hivyo, yaelekea utakubaliana na mtume Paulo, aliyeandika: “Huo ni njia ya kupata faida kubwa, huu ujitoaji-kimungu pamoja na ujitoshelevu [au, uradhi].”—1 Timotheo 6:6.
[Picha katika ukurasa wa 8]
Jihakikishie lile linalokubalika kwa Mungu
-
-
Epuka Kujilinganisha na WengineMnara wa Mlinzi—2010 | Novemba 1
-
-
Njia ya 2
Epuka Kujilinganisha na Wengine
BIBLIA INAFUNDISHA NINI? “Fanya kazi yako vizuri, na utakuwa na jambo la kujivunia. Lakini usijilinganishe na wengine.”—Wagalatia 6:4, Contemporary English Version.
KWA NINI INAWEZA KUWA VIGUMU? Huenda tukawa na mwelekeo wa kujilinganisha na wengine—nyakati nyingine na wale wenye vitu vichache kuliko tulivyo navyo, lakini mara nyingi na wale wenye nguvu nyingi zaidi, wenye utajiri zaidi, au wenye uwezo mwingi zaidi. Vyovyote vile, matokeo huwa si mazuri. Tunajidanganya kwa kufikiri kwamba thamani ya mtu inapimwa kulingana na vitu alivyo navyo au yale anayoweza kufanya. Huenda pia tukachochea hisia za wivu na roho ya mashindano.—Mhubiri 4:4.
UNAWEZA KUFANYA NINI? Jaribu kujiona kama vile Mungu anavyokuona. Ruhusu maoni yake yaongoze jinsi unavyojiona. “Mwanadamu huona kile kinachoonekana kwa macho, lakini Yehovaa huona jinsi moyo ulivyo.” (1 Samweli 16:7) Yehova anapima thamani yako si kwa kukulinganisha na mtu mwingine, bali kwa kusoma moyo wako, na kwa kuchunguza mawazo, hisia, na nia yako. (Waebrania 4:12, 13) Anaelewa udhaifu wako na angependa wewe pia utambue hali hiyo. Ikiwa unapima thamani yako kwa kujilinganisha na wengine, utaishia ama kuwa na majivuno au kukosa uradhi sikuzote. Hivyo, uwe mnyenyekevu na ukubali kwamba huwezi kufanikiwa katika kila jambo.—Methali 11:2.
Unapaswa kufanya nini hasa ili uwe na thamani machoni pa Mungu? Mungu alimwongoza nabii Mika kuandika hivi: “Ee mtu wa udongo, yeye amekuambia yaliyo mema. Na Yehova anataka nini kutoka kwako ila kutenda haki na kupenda fadhili na kuwa na kiasi katika kutembea na Mungu wako?” (Mika 6:8) Ikiwa utafuata shauri hilo, Mungu atakutunza. (1 Petro 5:6, 7) Bila shaka, hiyo ni sababu kubwa sana ya kutufanya turidhike.
[Maelezo ya Chini]
a Jina la Mungu kama linavyopatikana katika Biblia.
[Picha katika ukurasa wa 5]
Yehova anapima thamani yetu kwa jinsi tulivyo moyoni
-