-
Yote Hayo Hugharimiwaje?Mashahidi wa Yehova—Wapiga-Mbiu wa Ufalme wa Mungu
-
-
“Viti Ni vya Bure. Hakuna Viingilio”
Mapema sana kama toleo la pili la Watch Tower, katika Agosti 1879, Ndugu Russell alitaarifu hivi: “Twaamini ‘Zion’s Watch Tower’ lina YEHOVA akiwa mtegemezaji walo, na inapokuwa hivyo halitaombaomba wala kusihi wanadamu walitegemeze. Wakati Yeye asemaye: ‘Dhahabu na fedha zote za milimani ni zangu,’ ashindwapo kuandaa fedha zihitajiwazo, sisi tutaelewa kwamba ni wakati wa kuacha kuchapa.” Kupatana na hilo, fasihi za Mashahidi wa Yehova haziombiombi fedha.
Kama ilivyo kwa fasihi zao ndivyo ilivyo kwa habari ya mikutano yao. Hakuna maombi ya kuchochea hisiamoyo ili kupata fedha katika mikutano yao au kwenye mikusanyiko yao. Hakuna visahani vya michango ambavyo hupitishwa; hakuna bahasha ambazo hugawanywa za kuweka fedha; hakuna barua za kuombaomba fedha ambazo hupelekwa kwa washiriki wa makutaniko. Makutaniko hayachezi kamari au kushindania zawadi ili kupata fedha. Mapema sana kama 1894, wakati Watch Tower Society ilipotuma wasemaji wasafirio, ilitoa tangazo hili kwa manufaa ya kila mtu: “Na ieleweke tokea mwanzo kwamba kukusanya michango au njia nyinginezo za kuombaomba fedha hazikubaliwi wala kukubaliwa na Sosaiti hii.”
Hivyo, tangu mapema sana katika historia yao ya kisasa, vikaratasi vya mwaliko na mialiko mingineyo inayochapwa kwa ajili ya umma ili kuhudhuria mikutano ya Mashahidi wa Yehova huwa na shime “Viti Ni vya Bure. Hakuna Viingilio.”
Kuanzia mapema katika 1914, Wanafunzi wa Biblia walikodi majumba ya maonyesho pamoja na majumba mengine ya mikutano na kualika umma ili waje kuona “Photo-Drama of Creation.” Huo ulikuwa utoaji wenye sehemu nne, saa nane kwa ujumla, uliofanyizwa kwa slaidi na sinema zilizoambatanishwa na sauti. Wakati wa mwaka wa kwanza pekee, mamilioni ya watu waliuona katika Amerika Kaskazini, Ulaya, Australia, na New Zealand. Ijapokuwa baadhi ya wenyeji wa majumba ya maonyesho walitoza fedha kwa ajili ya viti vilivyohifadhiwa, Wanafunzi wa Biblia hawakuomba kamwe fedha kwa wenye kuingia ili kutazama. Na hakuna michango iliyokusanywa.
Baadaye, kwa miaka zaidi ya 30, Watch Tower Society iliendesha kituo cha redio WBBR katika New York City. Mashahidi wa Yehova walitumia pia utumishi mbalimbali wa mamia ya vituo vingine ili kutangaza programu za elimu ya Biblia. Lakini hawakutumia kamwe vituo kama hivyo ili kuombaomba fedha.
Basi, ule upaji ambao hugharimia utendaji wao hupatikanaje?
Hutegemezwa kwa Upaji wa Kujitolea
Biblia huweka kigezo. Chini ya Sheria ya Musa, kulikuwa michango fulani iliyotolewa kwa hiari. Mingine watu walitakwa waitoe. Kutoa zaka, au sehemu ya kumi, kulikuwa mojayapo michango ya lazima. (Kut. 25:2; 30:11-16; Hes. 15:17-21; 18:25-32) Lakini Biblia huonyesha pia kwamba Kristo alitimiza ile Sheria, naye Mungu akaikomesha; hivyo Wakristo hawafungwi tena na amri zayo. Wao hawatoi sehemu ya kumi, wala hawako chini ya wajibu wa kutoa michango mingine yoyote ya kiasi hususa au kwa wakati hususa.—Mt. 5:17; Rum. 7:6; Kol. 2:13, 14.
Badala ya hivyo, wao hutiwa moyo wasitawishe roho ya ukarimu na upaji wa hiari kwa kuiga kielelezo kizuri ajabu kilichowekwa na Yehova mwenyewe na Mwana wake, Yesu Kristo. (2 Kor. 8:7, 9; 9:8-15; 1 Yoh. 3:16-18) Hivyo, kwa habari ya kutoa, mtume Paulo aliandikia kutaniko la Kikristo katika Korintho hivi: “Acheni kila mmoja afanye kama vile ameazimia moyoni mwake, si kwa kinyongo au kwa shurutisho, kwa maana Mungu hupenda mpaji mchangamfu.” Walipojulishwa juu ya uhitaji fulani, jambo hilo liliwapa ‘jaribu la unyofu wa upendo wao,’ kama vile Paulo alivyoeleza. Yeye alisema pia: “Ikiwa utayari upo kwanza, hukubalika hasa kulingana na alicho nacho mtu, si kulingana na kile ambacho mtu hana.”—2 Kor. 8:8, 12; 9:7, NW.
Kwa kufikiria hayo, maelezo yaliyotolewa na Tertuliano kuhusu mikutano iliyofanywa na watu waliojitahidi kuzoea Ukristo katika siku zake (karibu 155–baada ya 220 W.K.) lapendeza. Yeye aliandika hivi: “Hata ingawa kuna kisanduku cha aina fulani, hakikufanyizwa kwa fedha zilizolipwa zikiwa viingilio, kana kwamba dini ilikuwa jambo la mkataba. Mara moja kwa mwezi kila mtu huleta sarafu ndogo—au wakati wowote atakapo, na ikiwa tu ataka, na ikiwa aweza; maana hapana mtu alazimishwaye; ni toleo la hiari.” (Apology, 39, 5) Hata hivyo, wakati wa karne nyingi tangu hapo, makanisa ya Jumuiya ya Wakristo yamejitia katika kila aina ya mbinu ya kujipatia fedha ili kugharimia shughuli zayo.
Charles Taze Russell alikataa kuiga makanisa. Yeye aliandika hivi: “Ni maoni yetu kwamba fedha zinazopatikana kwa zile mbinu mbalimbali za kuombaomba katika jina la Bwana wetu ni zenye kumchukiza, hazikubaliki kwake, nazo hazileti baraka yake ama juu ya wapaji ama juu ya kazi itimizwayo.”
Badala ya kujaribu kupata upendeleo wa wale waliokuwa na mali, Ndugu Russell alitaarifu waziwazi, kupatana na Maandiko, kwamba wengi wa watu wa Bwana wangekuwa maskini katika mali za ulimwengu huu lakini tajiri katika imani. (Mt. 19:23, 24; 1 Kor. 1:26-29; Yak. 2:5) Badala ya kukazia uhitaji wa fedha ili kueneza kweli ya Biblia, yeye alikazia fikira umaana wa kusitawisha roho ya upendo, tamaa ya kutoa, na tamaa ya kusaidia wengine, hasa kwa kushiriki kweli pamoja nao. Kwa wale waliokuwa na uwezo wa kuchuma fedha na ambao walidokeza kwamba kwa kujitoa wenyewe sana kwa mambo ya kibiashara wangekuwa na vingi zaidi vya kuchanga kifedha, yeye alisema kwamba ingekuwa afadhali wapunguze utendaji huo na kujitoa wenyewe na wakati wao katika kueneza kweli. Huo ungali ndio msimamo uchukuliwao na Baraza Linaloongoza la Mashahidi wa Yehova.a
Kihalisi, watu hutoa kiasi gani? Yale wanayofanya ni uamuzi wao binafsi. Hata hivyo, kwa habari ya kutoa, yapasa kuangaliwa kwamba Mashahidi wa Yehova hawafikiri tu juu ya kutoa mali za kimwili. Kwenye mikusanyiko yao ya wilaya katika 1985-1986, walizungumza juu ya kichwa cha habari “Kumheshimu Yehova kwa Vitu Vyetu vya Thamani.” (Mit. 3:9) Ilikaziwa kwamba vitu hivyo vya thamani hutia ndani si mali za kimwili tu bali pia nguvu zetu za kimwili, za kiakili, na za kiroho.
Huko nyuma katika 1904, Ndugu Russell alitaja kwamba mtu ambaye amejitakasa kabisa (au, kujiweka wakfu, kama tusemavyo sasa) kwa Mungu “amekwisha toa vyote alivyo navyo kwa Bwana.” Hivyo, apaswa sasa “kujifikiria mwenyewe kuwa amewekwa na Bwana kuwa msimamizi wa wakati wake mwenyewe, uvutano, fedha, n.k., na kila mmoja atatafuta kutumia talanta hizo kwa kadiri awezavyo, kwa utukufu wa Bwana-Mkubwa.” Yeye aliongeza kwamba, kwa kuongozwa na hekima kutoka juu, “kwa kadiri upendo na bidii yake vinavyokua kwa ajili ya Bwana siku kwa siku kupitia ujuzi wa Kweli na kupata roho yayo, atajikuta akitoa wakati zaidi na zaidi, na uvutano wake zaidi na zaidi, na mali alizo nazo zaidi na zaidi, kwa ajili ya utumishi wa Kweli.”—Studies in the Scriptures, “The New Creation,” kur. 344-345.
Wakati wa miaka hiyo ya mapema, Watch Tower Society ilikuwa na ile iliyoitwa Hazina ya Tower Tract. Hiyo ilikuwa nini? Habari hii yenye kupendeza iliandikwa upande wa nyuma wa karatasi na bahasha zilizotumiwa nyakati nyingine na Ndugu Russell: “Hazina hii huwa na matoleo ya hiari ya wale ambao wamelishwa na kuimarishwa na ‘nyama kwa wakati wake’ ambayo vichapo vilivyo juu [vitolewavyo na Watch Tower Society], vikiwa vyombo vya Mungu, vinatolea sasa watakatifu waliojitakasa, ulimwenguni pote.
“Hazina hii hutumiwa daima katika kupeleka nje, bila malipo, maelfu ya nakala za ZION’S WATCH TOWER na OLD THEOLOGY TRACTS ziwafaazo sana wasomaji wapya. Husaidia pia katika kueneza vitabu vilivyojalidiwa kwa karatasi vya mfululizo wa DAWN, kwa kusaidia wale walio tayari kuzieneza—makolpota na wengine. Pia huandalia ‘hazina ya maskini’ ambayo yeyote wa watoto wa Bwana ambaye, kwa sababu ya uzee, au ugonjwa, au kwa sababu nyingine, hawawezi kuandikisha WATCH TOWER wanapewa ugavi bila malipo, kwa sharti la kwamba wapeleka barua au kadi mwanzoni mwa kila mwaka, wakitaarifu tamaa na kutoweza kwao.
“Hapana mtu aulizwaye wakati wowote achangie hazina hii: upaji wote lazima uwe wa hiari. Sisi hukumbusha wasomaji wetu maneno ya Mtume (1 Kor. 16:1, 2) na huyathibitisha kwa kusema kwamba wale wanaoweza kutoa na wanaotoa ili kueneza kweli hakika watalipwa kwa mapendeleo ya kiroho.”
Utendaji wa duniani pote wa Mashahidi wa Yehova katika kupiga mbiu ya habari njema za Ufalme wa Mungu huendelea kutegemezwa kwa upaji wa hiari. Kuongezea Mashahidi wenyewe, watu wengi wenye kupendezwa wenye uthamini hulihesabu kuwa pendeleo kutegemeza kazi ya Kikristo kwa michango yao ya kutoa kwa hiari.
-
-
Yote Hayo Hugharimiwaje?Mashahidi wa Yehova—Wapiga-Mbiu wa Ufalme wa Mungu
-
-
[Sanduku katika ukurasa wa 341]
Mungu Haombiombi
“Yeye aliyesema, ‘Kama ningekuwa na njaa singekuambia, maana ulimwengu ni wangu, navyo viujazavyo. . . . Sitatwaa ng’ombe katika nyumba yako, wala beberu katika mazizi yako; maana kila hayawani wa msitu ni wangu, na makundi ya ng’ombe juu ya milima elfu’ (Zab. 50:12, 9, 10), aweza kuendesha kazi yake kuu bila kuombaomba fedha ama kutoka kwa ulimwengu ama kutoka kwa watoto wake. Wala hatashurutisha watoto wake kutoa dhabihu au chochote katika utumishi wake, wala hatakubali chochote kutoka kwao isipokuwa toleo changamfu, la hiari.”—“Zion’s Watch Tower,” Septemba 1886, uku. 6.
-