Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Kufaidika na Ushikamanifu wa Wapendwa Wangu
    Mnara wa Mlinzi—2006 | Septemba 1
    • Ndoa na Kazi ya Kusafiri

      Mwaka wa 1955, nilimfahamu John Cooke. Alisaidia kuanzisha kazi ya kuhubiri huko Ufaransa, Ureno, na Hispania kabla na baada ya Vita vya Pili vya Ulimwengu, naye akatumwa kutumikia akiwa mmishonari barani Afrika mwaka huo niliokutana naye. Baadaye aliandika hivi: “Nilipata mambo matatu yenye kushangaza katika juma moja . . . Ndugu mmoja mkarimu alinipa gari dogo; niliwekwa rasmi kuwa mtumishi wa wilaya; na nikampenda dada mmoja.”a Tulifunga ndoa Desemba 1957.

      Wakati wa uchumba, John alinihakikishia kwamba maisha yetu pamoja yatakuwa yenye kufurahisha kila wakati, na hivyo ndivyo ilivyokuwa. Tulitembelea makutaniko kotekote Afrika Kusini, hasa katika maeneo ya weusi. Kila juma, ilitubidi tupate kibali cha kuingia maeneo hayo na kulala huko usiku kucha. Katika pindi kadhaa tulilala kwenye sakafu katika duka moja lililokuwa bila kitu karibu na eneo la wazungu ambapo tulijaribu kujificha tusionekane na wapita njia. Kwa kawaida tulikaa karibu na Mashahidi wazungu walioishi mbali sana.

      Pia, tulikabili tatizo la kukutana msituni katika sehemu zilizokuwa zimejengwa kwa ajili ya makusanyiko. Tulionyesha sinema zilizotayarishwa na Mashahidi wa Yehova ambazo ziliwasaidia watu kuthamini undugu wetu wa ulimwenguni pote. Tulibeba jenereta yetu kwa sababu maeneo hayo hayakuwa na umeme. Pia, tulikabili matatizo katika maeneo yaliyokuwa chini ya Uingereza ambapo vichapo vyetu vilikuwa vimepigwa marufuku. Isitoshe, tulihitaji kujifunza Kizulu. Hata hivyo, tulifurahia kuwatumikia ndugu zetu.

      Mnamo Agosti 1961, John akawa mwalimu wa kwanza kufundisha Shule ya Huduma ya Ufalme ya majuma manne iliyofanywa Afrika Kusini. Shule hiyo ilikusudiwa kuwasaidia waangalizi wa makutaniko. Alikuwa stadi katika kazi ya kufundisha na alifikia mioyo kwa hoja zinazoeleweka kwa urahisi na mifano iliyo wazi. Kwa karibu mwaka mmoja na nusu, tulisafiri kutoka sehemu moja hadi nyingine kwa ajili ya darasa lililofuata la Kiingereza. John alipokuwa akifundisha, nilihubiri pamoja na Mashahidi wa eneo hilo. Kisha, tulishangaa tulipopata mwaliko wa kutumikia katika ofisi ya tawi ya Afrika Kusini karibu na jiji la Johannesburg, kuanzia Julai 1, 1964.

      Kufikia wakati huo, John alikuwa na ugonjwa ambao ulitutia wasiwasi. Katika 1948 aliugua kifua kikuu, naye alikuwa dhaifu mara nyingi. Alikuwa na dalili kama za mafua na ilimbidi alale mara nyingi, naye hangeweza kufanya chochote wala kumwona yeyote. Daktari tuliyemwomba mashauri kabla ya kualikwa kwenye ofisi ya tawi alisema kwamba John ameshuka moyo.

      Haikuwa rahisi kubadili maisha yetu, kama daktari alivyopendekeza. Kwenye ofisi ya tawi, John alifanya kazi katika Idara ya Utumishi, nami nikapewa kazi ya kukagua makala. Lilikuwa pendeleo kama nini kuwa na chumba chetu wenyewe! John alikuwa ametumika katika maeneo ya Kireno kabla hatujafunga ndoa. Hivyo mnamo 1967, tuliombwa tusaidie familia za Mashahidi Wareno katika eneo hilo ili kuwahubiria Wareno wengi walioishi ndani na nje ya Johannesburg. Hilo lilimaanisha nijifunze lugha nyingine tena.

      Kwa kuwa Wareno walikuwa wametawanyika katika eneo kubwa, tulisafiri sana, wakati mwingine kufikia umbali wa kilometa 300 ili kuwatafuta wanaostahili. Wakati huo, Mashahidi waliozungumza Kireno kutoka Msumbiji walianza kututembelea wakati wa makusanyiko, na jambo hilo liliwasaidia wapya wengi. Kwa miaka 11 tuliyotumia katika eneo la Kireno, tuliona kikundi kidogo cha wahubiri 30 hivi kikipanuka na kuwa makutaniko manne.

  • Kufaidika na Ushikamanifu wa Wapendwa Wangu
    Mnara wa Mlinzi—2006 | Septemba 1
    • Kukabiliana na Ugonjwa wa John

      Kufikia miaka ya 1970, ilikuwa wazi kwamba afya ya John iliendelea kuwa mbaya. Hatua kwa hatua, ilibidi aache baadhi ya mapendeleo yake ya utumishi, kutia ndani kuongoza funzo la Mnara wa Mlinzi la kila juma na mazungumzo ya Biblia ya asubuhi kwenye ofisi ya tawi. Alipelekwa kwenye Idara ya Utumishi, kisha katika ofisi ya barua, halafu kwenye bustani.

      Kwa kuwa John hakukata tamaa kwa urahisi, ilikuwa vigumu kwake kufanya mabadiliko. Niliposisitiza kwamba anahitaji kupumzika, alisema kwa mzaha kwamba mimi ni kizuizi kwake, kisha akanikumbatia kwa upendo. Hatimaye tuliona ni afadhali tutoke katika eneo la Kireno na kutumikia katika kutaniko lililokutana kwenye Jumba la Ufalme la ofisi ya tawi.

      Afya ya John ilipoendelea kuzorota, nilitiwa moyo kuona akiwa na uhusiano wa karibu pamoja na Yehova. Wakati John alipoamka katikati ya usiku akiwa ameshuka moyo sana, tulizungumza pamoja mpaka alipotulia na tukasali ili kumwomba Yehova msaada. Hatimaye, aliweza kukabiliana na hali hizo mbaya akiwa peke yake kwa kujilazimisha kukariri polepole maneno haya ya Wafilipi 4:6, 7: “Msihangaike juu ya kitu chochote . . .” Kisha angetulia kiasi cha kuweza kusali. Mara nyingi nilikuwa macho na ningetazama akifungua mdomo wake huku akimsihi Yehova kwa unyoofu.

      Kwa kuwa ofisi yetu ya tawi ilikuwa ndogo sana, ujenzi wa ofisi kubwa ya tawi ulianza nje ya jiji la Johannesburg. Mimi na John tulitembelea mahali hapo penye utulivu mara nyingi, mbali na kelele na uchafu wa jiji. John alifurahi sana tuliporuhusiwa kuishi huko katika makao ya muda mpaka ofisi mpya ilipokamilika.

      Matatizo Mengine Yatokea

      Kadiri uwezo wa John wa kufikiri ulivyoendelea kuzorota, ndivyo ilivyokuwa vigumu zadi kutimiza migawo yake. Nilitiwa moyo sana nilipoona jinsi wengine walivyomsaidia John. Kwa mfano, ndugu alipotembelea maktaba ya umma ili kufanya utafiti, angeandamana na John. John alijaza trakti na magazeti katika mifuko yake alipokwenda matembezi hayo. Hilo lilimsaidia John kuhisi kwamba anahitajiwa na anatimiza jambo fulani.

      Mwishowe, kwa sababu ya ugonjwa wa kupungua akili (ugonjwa wa Alzheimer), John hangeweza kusoma. Tulifurahi kuwa na kanda za vichapo vya Biblia na nyimbo za Ufalme. Tulizisikiliza tena na tena. Mara nyingi John angekasirika kama singeketi na kusikiliza pamoja naye, hivyo basi nikatumia pindi hizo kushona. Hiyo ilituwezesha kuwa na nguo nyingi za baridi na mablanketi!

      Hatimaye, nilihitaji kumtunza John zaidi kwa sababu hali yake ilizidi kuwa mbaya. Ingawa mara nyingi nilichoka sana na singeweza kusoma wala kujifunza, lilikuwa pendeleo kumtunza mpaka mwisho. Mwisho huo ulifika mwaka wa 1998 John alipokufa akiwa amelala kwa utulivu mikononi mwangu muda mfupi baada ya kufikia umri wa miaka 85, akiwa mshikamanifu mpaka mwisho. Ninatarajia kumwona wakati wa ufufuo akiwa na afya nzuri ya kimwili na ya kiakili!

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki