Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Waandishi wa Zamani na Neno la Mungu
    Mnara wa Mlinzi—2007 | Machi 15
    • Waandishi wa Zamani na Neno la Mungu

      KUANDIKWA kwa Maandiko ya Kiebrania kulikamilishwa kufikia mwishoni mwa karne ya tano K.W.K. Katika karne zilizofuata, wasomi Wayahudi, hasa Wasoferi na baadaye Wamasora, walijitahidi sana kuhakikisha kwamba usahihi wa maandishi ya Kiebrania unadumishwa. Hata hivyo, vitabu vya kale zaidi vya Biblia viliandikwa katika siku za Musa na Yoshua, miaka elfu moja kabla ya Wasoferi kutokea. Vitabu hivyo viliandikwa kwenye hati ambazo ziliharibika haraka; kwa hivyo, ni lazima iwe vitabu hivyo vya kukunjwa vilinakiliwa mara nyingi. Tunajua nini kuhusu kazi ya uandishi iliyofanywa siku hizo za zamani? Je, kulikuwa na waandishi stadi katika Israeli la kale?

      Hati za kale zaidi zilizopo leo za Biblia ni visehemu vya vitabu vya kukunjwa vya Bahari ya Chumvi. Baadhi ya hati hizo zilinakiliwa katika karne ya pili na ya tatu K.W.K. “Nakala za mapema zaidi za kitabu chochote cha Biblia hazipatikani,” anaeleza Profesa Alan R. Millard, msomi wa lugha na akiolojia ya Mashariki ya Karibu. Anaongeza hivi: “Tamaduni za jamii jirani zinaweza kuonyesha jinsi waandishi wa zamani walivyofanya kazi yao, na ujuzi huo unaweza kusaidia katika kuchanganua maandishi ya Kiebrania na historia yake.”

  • Waandishi wa Zamani na Neno la Mungu
    Mnara wa Mlinzi—2007 | Machi 15
    • Waandishi Katika Israeli la Kale

      Musa alilelewa katika nyumba ya Farao. (Kutoka 2:10; Matendo 7:21, 22) Kulingana na mtaalamu mmoja wa mambo ya kale ya Misri, huenda elimu ya Musa ilitia ndani kujifunza kusoma na kuandika maandishi ya Kimisri na angalau ustadi fulani-fulani wa uandishi. Katika kitabu chake (Israel in Egypt), Profesa James K. Hoffmeier anasema: “Kuna msingi wa kuamini wazo la kibiblia kwamba Musa alikuwa na uwezo wa kuandika matukio, kukusanya habari kuhusu safari, na kufanya kazi nyinginezo za uandishi.”b

      Biblia inawataja watu fulani waliokuwa na ustadi wa uandishi katika Israeli la kale. Kulingana na kichapo kimoja (The Cambridge History of the Bible), Musa “aliweka rasmi maofisa waliojua kusoma na kuandika . . . ili waandike habari kuhusu maamuzi na orodha za watu waliopangwa katika vikundi mbalimbali.” Kauli hiyo inategemea Kumbukumbu la Torati 1:15, linalosema: “Basi [mimi Musa] nikawachukua vichwa vya makabila yenu . . . na kuwaweka kuwa vichwa juu yenu, wakuu wa maelfu na wakuu wa mamia na wakuu wa 50 na wakuu wa makumi na maofisa wa makabila yenu.” Maofisa hao walikuwa nani?

      Neno “ofisa” katika Kiebrania linapatikana mara kadhaa katika maandishi ya Biblia yanayozungumza kuhusu siku za Musa na Yoshua. Wasomi mbalimbali wameeleza kwamba neno hilo linamaanisha “mwandishi wa habari,” “yule ‘anayeandika’ au ‘kurekodi,’” na “ofisa aliyemsaidia mwamuzi kuandika habari.” Kwa kuwa neno hilo la Kiebrania limerudiwa-rudiwa, ni wazi kwamba kulikuwa na waandishi wengi kama hao katika Israeli na kwamba walikuwa na wajibu mkubwa katika usimamizi wa mapema wa taifa hilo.

      Mfano wa tatu unahusu makuhani wa Israeli. Kitabu kimoja (Encyclopaedia Judaica) kinasema kwamba “walipaswa kujua kusoma na kuandika kwa sababu ya wajibu wao wa kidini na wa kiserikali.” Kwa mfano, Musa aliwaamuru hivi wana wa Lawi: “Mwishoni mwa kila miaka saba, . . . mtasoma sheria hii mbele ya Israeli wote.” Makuhani wakawa watunzaji wa nakala rasmi ya Sheria. Waliidhinisha na kusimamia kazi ya kunakili sheria.—Kumbukumbu la Torati 17:18, 19; 31:10, 11.

      Fikiria jinsi nakala ya kwanza ya Sheria ilivyotengenezwa. Katika mwezi wa mwisho wa maisha yake, Musa aliwaambia hivi Waisraeli: ‘Utakapovuka Yordani kuingia katika nchi ambayo Yehova Mungu wako anakupa wewe, utajiwekea pia mawe makubwa na kuyapaka chokaa. Nawe utaandika juu yake maneno yote ya sheria hii.’ (Kumbukumbu la Torati 27:1-4) Baada ya uharibifu wa Yeriko na Ai, Waisraeli walikusanyika kwenye Mlima Ebali, uliokuwa katikati ya Nchi ya Ahadi. Kwa hakika, wakiwa kwenye mlima huo, Yoshua aliandika juu ya mawe ya madhabahu “nakala ya maandishi ya sheria ya Musa.” (Yoshua 8:30-32) Waandishi na wasomaji walihitajiwa ili kunakili maandishi kama hayo. Hilo linaonyesha kwamba Waisraeli wa kale walikuwa na ustadi uliohitajiwa ili kuhifadhi kwa usahihi maandishi yao matakatifu.

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki