-
Uigizaji-Vitu—Tatizo la Ulimwenguni PoteAmkeni!—1996 | Machi 22
-
-
Uigizaji-Vitu—Tatizo la Ulimwenguni Pote
Hadi mwishoni mwa karne ya 18, katika Ufaransa watu walikuwa wakichemshwa wangali hai kwa sababu ya kosa hilo. Kuanzia 1697 hadi 1832, katika Uingereza, kosa hilo lilikuwa uhalifu ambao adhabu ilikuwa kifo, na tendo hilo lilionwa kuwa uhalifu dhidi ya serikali. Zaidi ya Waingereza 300 walinyongwa kwa sababu yalo, huku idadi zisizohesabika zikihamishwa hadi kwenye koloni ya adhabu katika Australia ili kufanya kazi ngumu ikiwa adhabu.
KWA zaidi ya miaka 130, serikali ya Marekani imekuwa ikifunga wale wenye hatia ya kosa hilo hadi miaka 15 katika magereza ya serikali. Na zaidi, maelfu ya dola yakiwa faini yamekuwa yakitozwa ili kuongezea hiyo adhabu. Hata leo hii, bado adhabu ya kifo inatolewa katika Urusi na China.
Licha ya hizo adhabu kali zinazoamriwa na mataifa mengi, uhalifu huo bado waendelea. Hata hofu ya kifo haijatosha kuzuia mipango ya kuwa-tajiri-haraka ya wale walio na stadi za kiufundi zinazohitajiwa. Wakuu wa serikali wamefadhaika. “Itakuwa vigumu kupata kizuizi kifaacho,” wao husema, “kama ambavyo imekuwa kwa karne nyingi.”
Uigizaji-vitu! Mmojawapo uhalifu wa kale zaidi katika historia. Mwishoni mwa karne hii ya 20, umekuwa tatizo la ulimwenguni pote na waendelea kuongezeka. Robert H. Jackson, hakimu mshirika wa Mahakama Kuu Zaidi ya Marekani, alisema hivi kuuhusu: “Uigizaji-vitu ni kosa ambalo halifanywi kiaksidenti kamwe, wala kwa kutojua, wala kwa msukumo wa tamaa, wala kwa sababu ya umaskini wa kupindukia. Ni uhalifu uliobuniwa kwa ustadi na mtu ambaye ana ustadi wa kiufundi na anayetumia fedha nyingi sana kwa vifaa.”
Kwa kielelezo, fedha za Kimarekani zinatokezwa kinyume cha sheria ulimwenguni pote na kwa kiwango kikubwa zaidi ya wakati mwingineo wote. “Fedha za Kimarekani,” akasema msemaji mmoja wa Idara ya Hazina, “sizo fedha zenye kutamanika tu kuliko zote ulimwenguni. Pia hizo ndizo zilizo rahisi zaidi kuigizwa.” Kile ambacho kimefadhaisha serikali ya Marekani ni kwamba nyingi za noti hizo bandia zinatengenezwa nje ya Marekani.
Fikiria hili: Katika 1992, noti bandia zenye thamani ya dola milioni 30 zilikamatwa ng’ambo, likaripoti gazeti Time. “Mwaka uliopita jumla ilifikia dola 120 milioni, na inatarajiwa kuvunja rekodi hiyo katika mwaka wa 1994. Kiwango kikubwa zaidi ya hicho huenezwa bila kugunduliwa,” likaripoti hilo gazeti. Tarakimu hizi hazielezi habari kamili. Inaaminiwa na wataalamu wa tatizo la uigizaji-vitu kwamba jumla ya noti bandia zinazoenezwa nje ya Marekani yaweza kuwa juu sana kufikia dola bilioni kumi.
Kwa kuwa fedha za Kimarekani zinatamaniwa sana na nchi nyingi—hata kuliko fedha zazo zenyewe—na kwa kuwa ni rahisi sana kuzinakili, mataifa mengi na watu wafanyao mambo kichinichini wanazitengeneza. Katika Amerika Kusini, walanguzi wa dawa za kulevya wa Kolombia wamekuwa wakiigiza fedha za Kimarekani kwa miaka mingi ili kuongeza mapato yao yasiyo halali. Sasa nchi fulani za Mashariki ya Kati zinakuwa washirika wakubwa katika biashara ya duniani kote ya kuigiza vitu, likaripoti U.S.News & World Report. Hilo gazeti liliongeza kwamba moja ya nchi hizo “inatumia njia tata za uchapaji zinazoiga zile zinazotumiwa na Idara ya Hazina ya Marekani. Likiwa tokeo, [inaweza] kutengeneza noti bandia za dola 100 zinazoitwa ‘noti bora zaidi,’ ambazo zaelekea kutoweza kugunduliwa kabisa.”
Watu katika Urusi, China, na nchi nyinginezo za Asia pia wanajiunga na utengenezaji wa fedha bandia—hasa fedha za Kimarekani. Inashukiwa kwamba asilimia 50 ya fedha za Kimarekani zinazoenezwa katika Moscow leo ni bandia.
Baada ya Vita ya Ghuba, katika 1991, kulipokuwa na uenezaji wa mamilioni ya dola za Kimarekani, “wanabanki wa kimataifa walishtuka kupata kwamba asilimia 40 ya noti za dola 100 zilikuwa bandia,” likasema Reader’s Digest.
Ufaransa ina matatizo yayo yenyewe yanayohusu fedha bandia, sawa na nchi nyinginezo nyingi za Ulaya. Kuigiza fedha si tatizo la Marekani pekee, kama mataifa mengine duniani pote yawezavyo kutoa ushahidi.
Kuigiza Vitu Kwarahisishwa
Hadi kufikia miaka kadhaa iliyopita, ilichukua mafundi wa kisiri—wasanii, wachoraji stadi, wakata nakshi, na wachapishaji—saa nyingi za kazi yenye kuchosha kunakili fedha za taifa lolote, ikitokeza, nakala hafifu za fedha halisi. Hata hivyo, leo, kukiwa na mashine za kufanya nakala za tekinolojia ya hali ya juu zenye rangi nyingi, mashine za kuchapa pande zote mbili za karatasi, na vifaa vinavyorekodi picha kwenye karatasi kwa kutumia miale vinavyopatikana katika maofisi na nyumbani, inawezekana kiufundi kwa yeyote kufanya nakala za fedha anazotaka.
Enzi ya kuigiza vitu kwa kutumia kompyuta imefika! Kile ambacho wakati mmoja kilihitaji stadi za wachoraji na wachapishaji wataalamu sasa kinaweza kufanywa na wafanyikazi wa ofisini na watu walio na kompyuta nyumbani. Mifumo ya uchapishaji ya kompyuta ndogo sana za kibinafsi ambayo haigharimu zaidi ya dola 5,000 yaweza kutengeneza fedha bandia ambazo zaweza kuwa vigumu sana kugunduliwa hata na wataalamu waliozoezwa. Hii ingeweza kumaanisha kwamba mtu ambaye anahitaji fedha anaweza kuepuka kisafari cha kwenda banki kwa kuchapisha fedha zake mwenyewe—na kwa thamani itakayotosheleza mahitaji yake! Tayari mifumo hii ni vifaa vyenye nguvu mikononi mwa watengenezaji wa leo wa vitu vya kuigiza. “Wanapofanya hivyo, wahalifu hawa wenye akili wanashinda mamlaka za kutekeleza sheria na siku moja wangeweza kutokeza hatari kwa fedha zenye thamani kubwa sana ulimwenguni,” likaandika U.S.News & World Report.
Kwa kielelezo, katika Ufaransa, asilimia 18 ya Franka milioni 30 (dola milioni 5, za Kimarekani) za fedha bandia zilizokamatwa katika 1992 zilitengenezwa kwenye mashine za ofisini. Ofisa mmoja wa Banque de France aona hili kuwa tisho si kwa mfumo wa kiuchumi tu bali pia kwa itibari ya umma katika serikali. “Watu wajuapo kwamba unaweza kuigiza noti iliyo halali kwa tekinolojia inayopatikana kwa watu wengi, itibari yaweza kutoweka,” akaomboleza.
Ikiwa sehemu ya jitihada ya kupambana na wingi wa fedha bandia katika Marekani na nchi nyinginezo, namna mpya za noti za banki ziko katika hatua ya kutengenezwa, na katika nchi fulani noti mpya tayari zinaenezwa. Kwa kielelezo, kwenye fedha za Kimarekani, ile picha ya Benjamin Franklin kwenye noti ya dola 100 itaongezwa ukubwa kwa nusu na itasogezwa robo tatu za inchi kwenda upande wa kushoto. “Mabadiliko mengine 14 katika michoro na maumbo mengineyo ya kisiri ya kusaidia usalama yatawekwa pia,” likaripoti Reader’s Digest. Mabadiliko mengine mengi, kama vile alama na wino ambazo hubadilika rangi zinapoangaliwa kutoka pembe tofauti, yanafikiriwa.
Kwa muda fulani Ufaransa imekuwa ikiingiza vizuizi vipya katika namna zayo za noti za banki ambavyo, yatumainiwa, vitakinza kwa kiwango fulani watengenezaji wa fedha bandia. Hata hivyo, msemaji wa Banque de France akiri kwamba “bado hakuna njia madhubuti kabisa ya kiufundi ya kushinda wawezao kuwa watengenezaji wa noti bandia, lakini,” akaongeza, “sasa twaweza kuunganisha vizuizi vingi sana katika noti ya banki yenyewe hivi kwamba ni kazi [ngumu], na yenye gharama sana kuigiza.” Yeye afafanua vizuizi hivi kuwa “hatua ya kwanza ya kulinda dhidi ya uigizaji.”
Ujerumani na Uingereza zimekuwa zikifanya mabadiliko ya usalama katika fedha zazo kwa muda fulani sasa kwa kuongeza nyuzi za usalama ambazo hufanya iwe vigumu zaidi kufanya nakala ya fedha zao. Noti ya Kanada ya dola 20 ina mraba mdogo wenye kung’aa unaoitwa kifaa cha usalama cha kinuru, ambacho hakiwezi kuigizwa kwenye mashine za kufanyia nakala. Australia ilianza kuchapisha noti za banki za plastiki katika 1988 ili kutia maumbo ya kusaidia usalama ambayo haingewezekana kutiwa katika karatasi. Finland na Austria hutumia jaribosi za msambazo kwa noti. Hizi humetameta na kubadilika rangi kama ifanyavyo hologramu. Hata hivyo, watu wenye mamlaka serikalini wanahofu, kwamba haitawachukua watengenezaji wa fedha bandia muda mrefu kufanya marekebisho yanayohitajiwa ili kuendeleza utendaji wao wa kihalifu—kwamba haidhuru ni hatua zipi za kurekebisha zichukuliwazo, jitihada zao za uvumbuzi huenda zikakosa kuwa na matokeo kama ambavyo zimekuwa wakati uliopita. “Ni kama usemavyo ule msemo wa kale,” akasema ofisa mmoja wa Idara ya Hazina, “unajenga ukuta wa futi nane, na jamaa wabaya wanajenga ngazi ya futi kumi.”
Kuchapisha fedha bandia ni upande mmoja tu wa ubingwa wa mtengenezaji wa vitu vya kuigiza, kama makala zifuatazo zitakavyoonyesha.
-
-
Kadi za Mkopo na Hundi za Malipo—Halisi au Bandia?Amkeni!—1996 | Machi 22
-
-
Kadi za Mkopo na Hundi za Malipo—Halisi au Bandia?
ZINAFAA kama nini! Ndogo mno, rahisi mno kubeba. Zatoshea vizuri sana katika pochi ya mwanamume au katika kibeti cha mwanamke. Bila hata ndururu mfukoni mwako, unaweza kununua vitu vingi mno. Utumizi wa kadi za mkopo unatiwa moyo na makampuni ya ndege, meli, mahoteli, na makao ya starehe ya waenda likizo ulimwenguni pote. Watu wanashauriwa hivi: “Usiondoke nyumbani bila hiyo.” Biashara fulani huona ni afadhali kukubali kadi za mkopo kuliko fedha taslimu. Tofauti na fedha taslimu, hizo zikiibwa au kupotea, nyingine zaweza kutolewa badala yazo. Ni fedha zako mwenyewe zilizofanywa kuwa za kibinafsi, zikiwa na jina lako na nambari ya akaunti ikiwa imetiwa nakshi upande wa mbele wa kadi.
Nyingi mwazijua kuwa fedha za plastiki—kadi za mkopo na za kutozwa. Katika 1985 banki fulani zilianzisha hologramu zazo zenyewe zilizobuniwa kwa leza, ambazo zaonekana kana kwamba zina pande tatu, na zenye maumbo mengine ya kusaidia usalama, kuanzia mfumo wa kipekee wa viishara katika ukanda wa kismaku unaopita nyuma hadi alama isiyoweza kuonekana isipokuwa chini ya nuru ya kiukaurujuani. Yote hayo ni kwa ajili ya kuzuia uigizaji! Inakadiriwa kwamba zaidi ya kadi za mkopo milioni 600 zinatumiwa duniani pote.
Inafikiriwa kwamba hasara ya ulimwenguni pote kutokana na aina tofauti za kadi za mkopo za ulaghai katika miaka ya mapema ya 1990 ilikuwa angalau dola bilioni moja. Kati ya namna hizo tofauti, uigizaji unaripotiwa kuwa wenye kuongezeka kwa haraka zaidi—angalau kwa asilimia 10 ya hasara zote.
Kwa kielelezo, katika 1993, uigizaji uligharimu banki zinazoshirikiana na moja ya kampuni kubwa zaidi zenye kutoa kadi za mkopo dola 133.8 milioni, ongezeko la asilimia 75 kuliko mwaka uliotangulia. Kampuni nyingine kuu ya kadi za mkopo, yenye ukubwa wa kimataifa, pia iliripoti hasara zenye kushangaza kwa sababu ya uigizaji. “Hilo lafanya uigizaji wa kadi kuwa tatizo kubwa si kwa banki, kampuni za kadi na wanabiashara wanaozikubali kwa malipo tu bali pia kwa wateja ulimwenguni pote,” likaandika gazeti moja la habari la New Zealand. Ingawa wenye kadi halali si wenye kusababisha hasara hizo, kwa wazi gharama hupitishwa kwa wateja.
Namna gani maumbo ya kusaidia usalama yaliyofanyizwa ndani ya kadi ambayo yalikuwa kama kizuizi kwa waigizaji—kama vile hologramu zilizobuniwa kwa leza na kanda za kipekee zenye mfumo wa kismaku? Kwa kipindi cha mwaka mmoja baada ya maumbo hayo kuanzishwa, kadi za kwanza zilizoigizwa za hali ya chini zilianza kutokea. Muda mfupi baada ya hapo, maumbo yote ya kusaidia usalama yaliigwa au kufichuliwa kwa wahalifu. “Ni lazima sikuzote mboreshe,” akasema ofisa mmoja wa banki wa Hong Kong. “Wahalifu sikuzote hujaribu kuwashinda kiakili.”
Kwa kupendeza, nusu ya hasara zote zilizotokana na uigizaji wa kadi katika miaka ya mapema ya 1990 zilitokea katika Asia, kulingana na wataalamu, na karibu nusu yazo zilifuatiwa hadi Hong Kong. “Kama tu vile Paris lajulikana sana kwa kutengeneza mavazi ya fashoni ya juu ndivyo Hong Kong ilivyo na sifa mbaya ya kutengeneza kadi bandia za mkopo,” akatangaza mtaalamu mmoja. Wengine wameshutumu Hong Kong kwa kuwa jiji lenye kutokeza ulimwenguni la kitovu cha duniani pote cha utendaji wa kihila katika uigizaji wa kadi za mkopo hilo latia ndani Thailand, Malasia na sasa kusini mwa China. “Polisi wa Hong Kong wanasema kwamba vikundi vya huko vinavyohusiana na vikundi vilivyopangwa vya Wachina vya uhalifu wa kisiri huchora, kukata nakshi na kubadili kadi bandia vikitumia nambari zilizotolewa na wachuuzi wafisadi. Kisha wanapeleka tu kadi bandia ng’ambo,” likaripoti hilo gazeti la habari la New Zealand.
“Mashine ya kukata nakshi kwenye kadi ya mkopo, iliyonunuliwa [katika Kanada] na washiriki wa genge la Asia, sasa inatumika kutengeneza kadi bandia za mkopo. Mashine hiyo huchapisha kadi za mkopo 250 kwa saa moja, na polisi wanaamini kwamba imetumiwa kwa ulaghai wa mamilioni ya dola,” likaripoti gazeti la habari la Kanada Globe & Mail. Kwa miaka michache iliyopita, Wachina wa kutoka Hong Kong wameshikwa wakitumia kadi bandia za mkopo katika angalau nchi 22 kutoka Austria hadi Australia, kutia ndani Guam, Malasia, na Uswisi. Kadi za mkopo za Japani ndizo hasa zinatafutwa, kwa kuwa hizo hutoa kiwango cha juu sana cha mkopo kwa watumizi wazo.
Ongezeko hili katika visa vya udanganyifu wa uigizaji wa kadi za mkopo humaanisha kwamba “wenye kuzitoa wanalazimika kusambaza miongoni mwa watumizi wazo gharama ya kiwango kinachoongezeka cha ulaghai,” akasema ofisa mmoja wa banki wa Kanada. Kwa kuhuzunisha, ndilo jambo linalotukia. Kwa kweli huenda kadi ya mkopo ikafaa na kusaidia sana wakati mtumizi wayo hana fedha taslimu za kutosha. Hata hivyo, kumbuka kwamba kitu tu wanachohitaji waigizaji ni nambari yako ya akaunti na tarehe ya kumalizika kwa kadi nao wanaingia kazini. “Ni fedha za plastiki,” akaonya mkuu mmoja wa usalama wa mkoa wa American Express International, “lakini watu hawajaanza kuzitumia kwa busara kama wanavyozitumia fedha taslimu.”
“Udhaifu mwingi umejaa katika mfumo wa kadi za mkopo,” akasema msimamizi mmoja wa polisi. “Na walaghai wamepata udhaifu wa huo mfumo. Na lo, wametumia udhaifu huo kwa ukatili,” akasema kuhusu waigizaji-vitu.
Uigizaji wa Hundi
Kukiwa na enzi mpya ya uchapishaji wa kikompyuta ambao waweza kufanya nakala ya karibu kila noti bila kasoro, kile kilichofuata kilikuwa kisichoepukika. Waigizaji-vitu wangeweza sasa kufanya nakala za hati aina nyingi mno: pasipoti, vyeti vya kuzaliwa, kadi za uhamiaji, vyeti vya umiliki wa hisa, vyeti vya ruhusa ya kufanya biashara, agizo la daktari la kupokea dawa, na hati nyinginezo nyingi. Lakini faida kubwa kuliko zote ingechumwa kutokana na kufanya nakala ya hundi za malipo.
Ufundi huo ni rahisi ajabu. Mara hundi ya malipo kutoka kampuni kubwa yenye mamilioni ya dola akibani katika banki za mahali fulani au zilizoenea taifani ipatikanapo na mtengenezaji wa vitu vya kuigiza, yuko tayari kuiigiza. Kwa mashine yake ya kuchapisha ya juu ya dawati, mashine iwezayo kusoma mwandiko wa mkono na kufanya nakala, na vifaa vingine vya kielektroni vipatikanavyo kwa utayari, yeye anaweza kubadili hundi hiyo ifae kusudi lake mwenyewe—akibadili tarehe, kufuta jina la mwenye kulipwa na kuweka lake, na kuongeza sufuri kadhaa kwenye kiasi cha dola. Kisha anachapa hundi hiyo iliyobadilishwa kwenye mashine yake mwenyewe ya kuchapia ya leza, akitumia karatasi aliyonunua kwenye duka la vifaa vya ofisini lililo karibu yenye rangi sawa na hiyo hundi. Akichapa hundi bandia nyingi, au zaidi kwa wakati mmoja, yeye aweza kwenda kutoa fedha kwenye tawi lolote la banki hiyo katika jiji lolote.
Ongezeko la uigizaji wa hundi kwa njia hii rahisi na isiyo ghali ni kubwa sana, wanasema maofisa wa banki na wa kutekeleza sheria, hivi kwamba gharama ya uchumi ingefika dola bilioni moja. Katika kisa kimoja chenye ujasiri mno, likaripoti The New York Times, genge lenye makao katika Los Angeles lilisafiri kote nchini likitoa fedha kwa hundi bandia za malipo kwenye banki mbalimbali, fedha hizo zikifikia zaidi ya dola milioni mbili. Wachanganuzi wa viwanda wanakadiria kwamba gharama ya jumla ya kila mwaka ya ulaghai wa hundi sasa ni dola bilioni kumi katika Marekani pekee. “Tatizo la uhalifu Na. 1 kwa mashirika ya kifedha,” akasema ofisa mmoja wa FBI, “ni vifaa viwezavyo kubadilishwa, kama vile ulaghai wa hundi na wa hawala za fedha.”
Akisema juu ya uigizaji-vitu wa kikompyuta, mpelelezi wa Idara ya Polisi ya Los Angeles alisema: “Kila kitu tunachoona kinatokezwa na kompyuta, kwa hiyo vitu vilivyoigizwa vinafanana sana na vile vya asili—kwa kweli kuliko vilivyokuwa zamani. Mambo yalianza kukosa udhibiti karibu miaka mitatu hivi iliyopita na sasa yameenda zaidi ya hapo—kwa wazi yamekosa udhibiti kabisa.”
Kuigiza fedha, hundi, na hati kwaweza kupimwa kwa hasara ya fedha iletwayo kwa biashara, viwanda, na watu mmoja-mmoja. Lakini kuna visa vya uigizaji-vitu ambao waweza kupimwa kwa hasara ya uhai, kama makala ifuatayo itakavyoonyesha.
-
-
Wanunuzi Jihadharini! Uigizaji-Vitu Waweza Kugharimu UhaiAmkeni!—1996 | Machi 22
-
-
Wanunuzi Jihadharini! Uigizaji-Vitu Waweza Kugharimu Uhai
WENYE kudanganywa wasiozoezwa, wasioshuku wanaweza kupumbazwa. Ile saa ionekanayo kuwa ghali unayotolewa na mchuuzi wa barabarani kwa nusu ya bei—je, ni halisi au ni bandia? Je, utainunua? Lile koti la anasa la manyoya unalotolewa na mchuuzi aliye garini kando ya barabara—mchuuzi aahidi kwamba hilo ni koti la manyoya ya bei ghali. Je, uvutio walo na bei iliyoshushwa itakuzuia kutumia uamuzi bora? Ile pete ya almasi kidoleni mwa eti mke aliyetalikiwa hivi majuzi—sasa akiwa hana fedha wala makao, anayengoja gari-moshi katika stesheni moja ya New York ya gari-moshi la chini ya ardhi—unaweza kuipata kwa bei ya chini mno. Je, ungefikiri kwamba bei hiyo ni nzuri mno hivi kwamba huwezi kuiacha? Kwa sababu maswali haya yanaulizwa katika makala hii inayoshughulikia uigizaji-vitu na kwa sababu ya hali zinazotolewa, yaelekea utajibu “SIWEZI KAMWE!”
Ahaa, lakini ebu tubadili mahali na hali tuone majibu yako yatakuwa nini. Namna gani kibeti kizuri kipendwacho sana kinachouzwa katika duka halali lenye kuuza vitu kwa bei iliyopunguzwa sana? Aina ijulikanayo sana ya wiski inayouzwa katika duka la vileo pembeni mwa barabara? Kwa hakika hapangekuwa na tatizo hapa. Fikiria pia, ukanda wa filamu wenye jina lijulikanalo ambao umepunguzwa bei katika duka la dawa au duka la kuuza kamera. Wakati huu ile saa ya bei ya juu yenye kugharimu maelfu ya fedha inatolewa kwako, si na mchuuzi wa barabarani, bali na duka lenye sifa nzuri. Bei imepunguzwa sana. Ikiwa ungekuwa unapendezwa na saa kama hiyo ya bei ya juu, je, ungeinunua? Kisha kuna aina zijulikanazo sana za viatu kwa bei zenye kuokoa fedha katika duka moja hususa ambalo unaelekezwa na rafiki zako. Je, una uhakika hivyo si miigizo hafifu tu?
Katika ulimwengu wa sanaa, kwenye majengo ya kuonyeshea vitu vya sanaa yenye picha za kupendeza, kuna mauzo mengi ya mnada kwa wanaopendezwa na sanaa ya bei ya juu. “Tahadhari,” akaonya mtaalamu mmoja wa sanaa. “Wataalamu wenye miaka mingi ya uzoefu hupumbazwa. Na ndivyo na wauzaji. Na ndivyo na wasimamizi wa majumba ya hifadhi ya vitu vya kale.” Je, umesoma sana hivi kwamba ungeweza kutoshana akili na waelekeao kuwa waigizaji wa vitu? Jihadhari! Vitu vyote vilivyoonyeshwa pichani vyaweza kuwa bandia. Mara nyingi ndivyo huwa. Kumbuka, kitu kikiwa nadra kukipata na kina thamani, mtu fulani mahali fulani atajaribu kukiigiza.
Bidhaa zilizoigizwa ni utendaji wa dola bilioni 200 ulimwenguni pote nao “unastawi kwa haraka kuliko viwanda vingi ambavyo ni windo lavyo,” likaandika gazeti Forbes. Visehemu bandia vya gari hugharimu watengenezaji na waandaaji wa Marekani wa magari dola bilioni 12 kila mwaka katika mapato yanayopotea ulimwenguni pote. “Kiwanda cha magari cha Marekani chasema kwamba kingeweza kuajiri watu wengine 210,000 ikiwa kingeweza kukomesha waandaaji wa visehemu bandia kufanya biashara,” hilo gazeti likasema. Inaripotiwa kwamba karibu nusu ya viwanda vya uigizaji-vitu viko nje ya Marekani—karibu kila mahali.
Vitu Bandia Vinavyoweza Kuua
Namna fulani za bidhaa bandia ni zenye kudhuru. Nati, bolti na skrubu zilizoagizwa kutoka nje hufanyiza asilimia 87 ya dola bilioni 6 za soko la Marekani. Hata hivyo, uthibitisho kufikia sasa unaonyesha kwamba asilimia 62 ya vikazaji hivi vina majina yaliyotungwa ili kudanganya au vina mihuri isiyo halali ya gredi. Ripoti ya 1990 iliyotolewa na General Accounting Office (GAO) ilipata kwamba angalau “viwanda vya nyuklia [72 vya Marekani] vilikuwa vimeweka vikazaji vyenye ubora wa chini sana kuliko ule unaohitajiwa na sheria, vingine katika mifumo ya kuzima kitendanishio aksidenti itokeapo. Tatizo hili lazidi kuwa baya, yasema GAO. . . . Ukubwa wa tatizo hilo, gharama kwa walipa-kodi au hatari ziwezazo kutokea kutokana na kutumia bidhaa hizo [za hali ya chini] hazijulikani,” likaripoti Forbes.
Bolti za chuma, ambazo nguvu zazo hazitoshi kwa matumizi, zimeigizwa na kuingizwa Marekani kisiri na wanakandarasi wasio wanyoofu. “Zinaweza kutisha usalama wa majengo ya ofisi, viwanda vya umeme, madaraja na vifaa vya kijeshi,” kulingana na American Way.
Papi bandia za breki ndizo zilizolaumiwa kusababisha kuanguka kwa basi moja katika Kanada miaka kadhaa iliyopita ambapo watu 15 walikufa. Imeripotiwa kwamba visehemu bandia vimepatikana katika mahali ambapo mtu hangefikiria vingepatikana kama vile kwenye helikopta za kijeshi na chombo cha anga cha Marekani. “Mtumiaji wa wastani hajali sana unapozungumza kuhusu saa zilizo bandia aina ya Cartier au Rolex,” akasema mchunguzi mmoja maarufu wa uigizaji-vitu, “lakini afya na usalama zinapokuwa hatarini, wanahangaikia sana hiyo hali.”
Orodha ya vitu bandia viwezavyo kuwa hatari yatia ndani mashine za kusaidia moyo kupiga zilizouzwa kwa hospitali 266 za Marekani; vibonge bandia vya kupanga uzazi ambavyo vilifikia soko la Marekani katika 1984; na viuakuvu, ambavyo ni chokaa tu, vilivyoharibu mazao ya kahawa ya Kenya katika 1979. Kuna dawa bandia zilizoenea sana ambazo zaweza kuhatarisha maisha ya watumiaji. Vifo vinavyotokana na dawa bandia ulimwenguni pote vyaweza kushangaza.
Kuna wasiwasi wenye kuongezeka kuhusu vyombo vidogo vya nyumbani vya umeme vilivyo bandia. “Baadhi ya bidhaa hizi huwa na majina bandia ya kibiashara au idhini kama vile katika orodha ya Underwriters Laboratory,” likaripoti American Way. “Lakini havitengenezwi kufikia kiwango cha usalama icho hicho, na kama tokeo vitalipuka, kusababisha moto wa nyumbani na kufanya uwekaji wote usiwe salama,” akasema mhandisi mmoja wa usalama.
Katika Marekani na Ulaya, vikundi vya elimu ya kuruka kwa ndege vinatiwa wasiwasi vilevile. Kwa kielelezo, katika Ujerumani, mashirika ya ndege yamepata injini na visehemu vya breki vilivyo bandia katika orodha ya vitu walivyo navyo. Uchunguzi “unafanywa katika Ulaya, Kanada, na United Kingdom, ambako visehemu (nati za ufito wa kijembe kilicho mkiani) visivyoidhinishwa vimehusianishwa na anguko hatari la hivi majuzi la helikopta,” wasema maofisa wa uchukuzi. “Maajenti wamekamata visehemu vingi bandia vya injini ya ndege, mkusanyo wa breki, bolti na vikazaji vyenye ubora wa chini, visehemu vyenye kasoro vya mifumo ya mafuta na ya vifaa vya kiumeme vya kuongozea ndege, vifaa vya kuongozea ndege visivyoidhinishwa na visehemu vya mifumo ya kuongozea ndege ya kompyuta ambavyo ni hatari kwa usalama wa safari ya angani,” likaripoti Flight Safety Digest.
Katika 1989 ndege ya kukodiwa iliyokuwa ikielekea Ujerumani kutoka Norway ilianza ghafula kushuka chini kwa mwinamo kutoka mruko wayo wa mwinuko wa meta 6,600. Sehemu ya mkiani ilipasuliwa, ikifanya ndege hiyo ishuke vibaya sana kuelekea chini kwa mwinamo mkali hivi kwamba mabawa yote mawili yalivunjika. Nafsi zote 55 zilizokuwa ndani zilikufa. Baada ya uchunguzi wa miaka mitatu, wataalamu wa Norway wenye elimu ya kuruka kwa ndege waligundua kwamba anguko hilo lilisababishwa na bolti zenye kasoro, ziitwazo pini za kukaza, zilizounganisha sehemu ya mkiani na ile sehemu kuu ya ndege. Uchanganuzi wa mkazo ulionyesha kwamba hizo bolti zilitengenezwa kwa metali ambayo ni dhaifu sana kuweza kustahimili nguvu zenye kupiga za safari ya ndege. Pini za kukaza zenye kasoro zilikuwa bandia—neno ambalo ni la kawaida sana kwa wataalamu wa elimu ya kuruka kwa ndege kila mahali, kwa kuwa uigizaji-vitu ni tatizo lenye kuongezeka sana ambalo huhatarisha maisha ya wafanyakazi wa ndege na abiria.
Televisheni ya kitaifa ilipomhoji inspekta mkuu wa Idara ya Uchukuzi ya Marekani alisema hivi: “Mashirika yote ya ndege yamepata visehemu bandia. Yote yanayo. Yote yana tatizo.” Yeye aliongeza kwamba biashara ya ndege inakiri “kwamba yaelekea ina orodha ikadiriwayo kugharimu dola bilioni mbili au tatu ya bidhaa walizo nazo ambazo haziwezi kutumiwa.” Madalali na wafanyibiashara wasio wanyoofu ambao hawahitaji kupewa leseni katika kushughulika na visehemu vya ndege mara nyingi huwa wenye utayari mno kuuza kwa udanganyifu visehemu vibaya kama kwamba ni vizuri.
Katika mahojiano ayo hayo, mshauri wa usalama wa elimu ya kuruka kwa ndege, ambaye ameshauri FBI juu ya utendaji kadhaa wa kichinichini unaohusisha visehemu bandia, alionya kwamba visehemu bandia hutokeza hatari ya kweli. “Nafikiri, likiwa tokeo, kwa hakika tunatazamia msiba mkubwa wa ndege wakati fulani ujao usio mbali,” yeye akasema.
Siku ya hukumu inakaribia kwa wale ambao pupa yao huwaruhusu kuweka tamaa zao wenyewe za kichoyo mbele ya maisha za wengine. Neno la Mungu lililopuliziwa lataarifu kwamba kwa hakika watu wenye pupa hawataurithi Ufalme wa Mungu.—1 Wakorintho 6:9-10.
-