-
“Kutetea na Kuthibitisha Kisheria Habari Njema”Mashahidi wa Yehova—Wapiga-Mbiu wa Ufalme wa Mungu
-
-
Kuelimishwa juu ya Haki na Utaratibu wa Kisheria
Kadiri ambavyo hesabu ya kesi za mahakama iliongezeka katika miaka ya mwisho ya 1920 na baada ya hapo, ikawa lazima Mashahidi wa Yehova wafunzwe juu ya taratibu za kisheria. Kwa kuwa J. F. Rutherford alikuwa wakili na yeye mwenyewe alikuwa ametumikia akiwa hakimu, yeye alifahamu uhitaji wa Mashahidi kupata mwelekezo katika mambo hayo. Hasa tangu 1926 Mashahidi walikuwa wamekuwa wakikazia kuhubiri nyumba hadi nyumba siku za Jumapili, kwa kutumia vitabu vinavyoeleza juu ya Biblia. Kwa sababu ya upinzani dhidi ya kugawanya kwao fasihi za Biblia siku ya Jumapili, Ndugu Rutherford alitayarisha kijitabu Liberty to Preach ili kusaidia wale walioko Marekani waelewe haki zao chini ya sheria. Hata hivyo, yeye binafsi hangeweza kufanya kazi yote ya kisheria, kwa hiyo alipanga ili mawakili wengine watumike wakiwa sehemu ya wafanya kazi wa makao makuu ya Sosaiti. Kwa kuongezea, mawakili wengine waliokuwa sehemu mbalimbali nchini, walishirikiana kwa ukaribu.
Mawakili hawangeweza kuwapo kwa ajili ya kusikizwa kwa maelfu ya kesi zilizohusu utendaji wa kuhubiri wa Mashahidi wa Yehova, lakini wangeweza kutoa shauri lenye thamani. Kwa kusudi hilo, mipango ilifanywa ili kuzoeza Mashahidi wa Yehova wote taratibu za sheria za msingi. Hilo lilifanywa kwenye makusanyiko ya pekee katika Marekani katika 1932 na baadaye, kwenye programu za kawaida za Mikutano ya Utumishi makutanikoni. Sehemu ya “Utaratibu wa Mashtaka” yenye kutia mambo mengi ilichapwa katika Kitabu-Mwaka cha 1933 cha Mashahidi wa Yehova (baadaye ikiwa karatasi iliyotenganishwa). Maagizo hayo yalirekebishwa kulingana na hali. Katika toleo la Consolation la Novemba 3, 1937, shauri zaidi la kisheria lilitolewa kuhusu hali hususa zilizokuwa zikikabiliwa.
Kwa kutumia habari hiyo, mara nyingi Mashahidi walishughulikia utetezi wao wenyewe katika mahakama za kwao, badala ya kupata utumishi wa wakili. Walipata kwamba kwa njia hiyo mara nyingi wangeweza kutoa ushahidi mahakamani na kutoa masuala ifaavyo kwa hakimu, badala ya kesi zao kuamuliwa kwa kutegemea utaratibu wa kisheria tu. Wakati kesi ilipoamuliwa isivyopendeleka, mara nyingi rufani ilikatwa, ingawa baadhi ya Mashahidi walifungwa badala ya kumtumia wakili, ambaye utumishi wake ungehitajiwa katika mahakama ya rufani.
Kadiri ambavyo hali mpya zilitokea na vigezo vikawekwa kwa maamuzi katika mahakama, habari zaidi iliandaliwa ili kuwaweka Mashahidi wakiwa na habari za kisasa. Hivyo, katika 1939 kijitabu Advice for Kingdom Publishers kilichapwa ili kusaidia akina ndugu katika vita vya mahakamani. Miaka miwili baadaye mazungumzo yenye kutia mambo mengi zaidi yaliandaliwa katika kijitabu Jehovah’s Servants Defended. Kilinukuu au kuzungumzia maamuzi 50 tofauti ya mahakama ya Amerika yaliyohusu Mashahidi wa Yehova, pamoja na kesi nyinginezo nyingi, na kikaeleza jinsi vigezo hivyo vya kisheria vingeweza kutumiwa kwa manufaa. Kisha katika 1943, nakala ya Freedom of Worship ilitolewa kwa kila Shahidi na ikasomwa kwa bidii kwenye Mikutano ya Utumishi makutanikoni. Zaidi ya kuandaa muhtasari wa thamani wa kesi za kisheria, kijitabu hicho kilionyesha kikamili sababu za Kimaandiko za kushughulikia mambo kwa njia fulani hususa. Hicho kilifuatwa, katika 1950, na kijitabu chenye habari za wakati huo Defending and Legally Establishing the Good News.
Hiyo yote ilikuwa elimu ya kisheria yenye kuendelea. Hata hivyo, kusudi halikuwa kuwafanya Mashahidi wawe mawakili bali ni kufungua njia ya kuhubiri habari njema za Ufalme wa Mungu hadharani na nyumba hadi nyumba.
-
-
“Kutetea na Kuthibitisha Kisheria Habari Njema”Mashahidi wa Yehova—Wapiga-Mbiu wa Ufalme wa Mungu
-
-
[Picha katika ukurasa wa 692]
Ikawa lazima kufundisha Mashahidi wa Yehova taratibu za kisheria ili waweze kushughulika na upinzani katika huduma yao; hivi ni baadhi ya vichapo vya kisheria walivyotumia
-