Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Pumziko la Mungu Ni Nini?
    Mnara wa Mlinzi—2011 | Julai 15
    • ‘Usianguke Katika Kielelezo Kilekile cha Kutotii’

      6. Ni mifano gani inayotuonya sisi, na tunaweza kujifunza nini kutokana nayo?

      6 Mungu aliwaeleza waziwazi Adamu na Hawa kusudi lake kwa ajili ya dunia, lakini walitenda kinyume na kusudi hilo. Bila shaka, Adamu na Hawa ndio wanadamu wa kwanza ambao hawakumtii Mungu. Tangu wakati huo kumekuwa na mamilioni ya watu wengine ambao wametenda vivyo hivyo. Hata watu wa Mungu waliochaguliwa, taifa la Israeli, walikosa tena na tena kumtii Mungu. Na jambo la maana zaidi ni kwamba Paulo aliwaonya Wakristo wa karne ya kwanza kuwa hata wengine kati yao wangeanguka katika mtego huohuo wa Waisraeli wa kale. Aliandika hivi: “Kwa hiyo acheni sisi tufanye yote tunayoweza ili kuingia katika pumziko hilo, yeyote asije akaanguka katika kielelezo kilekile cha kutotii.” (Ebr. 4:11) Maneno ya Paulo yanaonyesha kwamba watu wasiotii hawawezi kuingia katika pumziko la Mungu. Hilo linamaanisha nini kwetu? Je, linamaanisha kwamba tukiasi na kutenda kwa njia fulani kinyume na kusudi la Mungu, hatutaingia katika pumziko la Mungu? Ni wazi kwamba jibu la swali hilo ni la maana sana, na tutalichunguza kwa undani zaidi. Hata hivyo, acheni sasa tuone jambo lingine tunaloweza kujifunza kuhusu kuingia katika pumziko la Mungu kwa kuchunguza mfano mbaya wa Waisraeli.

      “Hawataingia Katika Pumziko Langu”

      7. Yehova alikuwa na kusudi gani alipowakomboa Waisraeli kutoka utumwani huko Misri, na aliwatazamia wafanye nini?

      7 Katika mwaka wa 1513 K.W.K., Yehova alimfunulia Musa mtumishi wake kusudi lake kuhusu Waisraeli. Mungu alisema hivi: “Ninashuka ili kuwakomboa kutoka katika mkono wa Wamisri na kuwatoa katika nchi hiyo [ya Misri] mpaka kwenye nchi nzuri na kubwa, nchi inayotiririka maziwa na asali.” (Kut. 3:8) Kama vile tu Yehova alivyomwahidi babu yao, Abrahamu, kusudi la Mungu la kuwakomboa Waisraeli “kutoka katika mkono wa Wamisri” lilikuwa kuwafanya wawe watu wake. (Mwa. 22:17) Mungu aliwapa Waisraeli sheria ambazo zingewasaidia kuwa na uhusiano wenye amani pamoja naye. (Isa. 48:17, 18) Aliwaambia Waisraeli hivi: “Ikiwa mtaitii sauti yangu kabisa na kulishika kwa kweli agano langu [kama ilivyoonyeshwa katika ile Sheria iliyoandikwa], ndipo hakika mtakapokuwa mali yangu ya pekee kutoka kati ya vikundi vingine vyote vya watu, kwa sababu dunia nzima ni yangu.” (Kut. 19:5, 6) Kwa hiyo, Waisraeli wangeendelea kufurahia pendeleo la kuwa na uhusiano mzuri pamoja na Mungu ikiwa tu wangetii sauti yake.

      8. Ni maisha ya aina gani ambayo Waisraeli wangekuwa nayo ikiwa wangemtii Mungu?

      8 Fikiria maisha ambayo Waisraeli wangekuwa nayo ikiwa tu wangetii sauti ya Mungu! Yehova angebariki mashamba yao, mizabibu yao, na wanyama wao. Aliahidi pia kwamba angewalinda kutokana na maadui wao. (Soma 1 Wafalme 10:23-27.) Wakati Masihi angetokea, inaelekea kwamba angewakuta Waisraeli wakijitawala wenyewe kama taifa huru, na si chini ya ukandamizaji wa Waroma. Yehova alitaka taifa la Israeli liwe mfano mzuri kwa mataifa mengine. Alitaka kila mtu aelewe waziwazi kwamba wale wanaomtii yeye akiwa Mungu wa kweli, wanapata baraka nyingi kutoka kwake.

      9, 10. (a) Kwa nini lilikuwa kosa zito kwa Waisraeli kutamani kurudi Misri? (b) Je, Waisraeli wangemwabudu Yehova kwa njia aliyotaka ikiwa wangerudi Misri?

      9 Waisraeli walikuwa na pendeleo la pekee kama nini la kumruhusu Yehova awatumie ili kutimiza kusudi lake! Wangepokea baraka za Yehova na pia wangeziletea familia zote za dunia baraka nyingi. (Mwa. 22:18) Hata hivyo, Waisraeli wengi hawakuchukua kwa uzito pendeleo la kuwa taifa la Mungu na kuwa mfano mzuri kwa mataifa mengine. Hata walisema kwamba walitaka kurudi Misri! (Soma Hesabu 14:2-4.) Sasa, ikiwa wangerudi Misri wangetimiza jinsi gani kusudi la Mungu la kufanya ufalme wa Israeli uwe mfano mzuri kwa mataifa mengine? Hilo halingewezekana. Kwa kweli, ikiwa Waisraeli wangerudi kuwa tena watumwa huko Misri, hawangeweza kamwe kufuata Sheria ya Musa na kufaidika na mpango wa Yehova wa kuwasamehe dhambi zao. Walikuwa wakijifikiria wenyewe tu bila kufikiria kusudi la Mungu! Haishangazi kwamba Yehova aliwaambia hivi waasi hao: “Nikachukizwa na kizazi hiki, nikasema, ‘Wao hupotea sikuzote katika mioyo yao, nao wenyewe hawajapata kuzijua njia zangu.’ Kwa hiyo niliapa kwa hasira yangu, ‘Hawataingia katika pumziko langu.’”—Ebr. 3:10, 11; Zab. 95:10, 11.

      10 Kwa kutamani kurudi Misri, taifa hilo lililopotea lilionyesha kwamba halikuthamini baraka za kiroho ambazo lilipokea, na badala yake likapendelea vitunguu vya majani, vitunguu, na vitunguu saumu ambavyo vilikuwa Misri. (Hes. 11:5) Kama Esau asiye na shukrani, waasi hao walikuwa tayari kupoteza urithi wa kiroho wenye thamani kwa kubadilishana na chakula kitamu.—Mwa. 25:30-32; Ebr. 12:16.

      11. Kwa kuwa Waisraeli wa siku za Musa hawakuwa waaminifu, je, hilo lilibadili kusudi la Mungu?

      11 Ingawa Waisraeli hao waliotoka Misri hawakuwa waaminifu, Yehova ‘aliendelea kufanya kazi’ kwa subira ili kutimiza kusudi lake kuelekea taifa hilo, akikazia uangalifu wake kizazi kilichofuata. Washiriki wa kizazi hicho kipya walikuwa watiifu zaidi kuliko baba zao. Kulingana na amri ya Yehova, waliingia katika Nchi ya Ahadi na wakaanza kuimiliki. Tunasoma hivi katika Yoshua 24:31: “Israeli wakaendelea kumtumikia Yehova siku zote za Yoshua na siku zote za wale wanaume wazee walioendelea kuishi baada ya Yoshua, waliokuwa wamejua kazi yote ya Yehova ambayo alifanya kwa ajili ya Israeli.”

      12. Tunajua jinsi gani kwamba inawezekana leo kuingia katika pumziko la Mungu?

      12 Hata hivyo, kizazi hicho kilichotii kilikufa hatua kwa hatua na kizazi kingine ambacho “hakikumjua Yehova wala ile kazi ambayo alikuwa amewafanyia Israeli” kikachukua mahali pake. Kwa hiyo, “wana wa Israeli wakaanza kufanya yaliyo mabaya machoni pa Yehova, wakatumikia Mabaali.” (Amu. 2:10, 11) Kwa kweli, Nchi hiyo ya Ahadi haikuwa “mahali pa pumziko” kwao. Kwa sababu ya kutotii kwao, hawakufurahia amani yenye kudumu pamoja na Mungu. Baadaye, Paulo aliandika hivi kuhusu Waisraeli hao: “Kama Yoshua angekuwa amewaingiza [Waisraeli] katika mahali pa pumziko, Mungu hangesema baadaye juu ya siku nyingine. Kwa hiyo bado limebaki pumziko la sabato kwa ajili ya watu wa Mungu.” (Ebr. 4:8, 9) “Watu wa Mungu” ambao Paulo alikuwa akizungumzia walikuwa Wakristo. Je, hilo linamaanisha kwamba Wakristo wangeweza kuingia katika pumziko la Mungu? Bila shaka, hilo lilitia ndani Wakristo Wayahudi na Wakristo wasio Wayahudi!

      Wakristo Wengine Hawakuingia Katika Pumziko la Mungu

      13, 14. Kulikuwa na uhusiano gani kati ya kufuata Sheria ya Musa na kuingia katika pumziko la Mungu (a) katika siku za Musa? (b) katika karne ya kwanza?

      13 Paulo aliwaandikia Wakristo Waebrania kwa sababu wengine wao walikuwa wakitenda kinyume na kusudi la Mungu. (Soma Waebrania 4:1.) Katika maana gani? Jambo la kushangaza ni kwamba bado walikuwa wakifuata Sheria ya Musa. Ni kweli kwamba kwa miaka 1,500 hivi, Mwisraeli yeyote ambaye alitaka kuishi kulingana na kusudi la Mungu alipaswa kufuata Sheria ya Musa. Hata hivyo, baada ya kifo cha Yesu, Sheria hiyo iliondolewa. Wakristo fulani walikosa kutambua jambo hilo, na walisisitiza kuendelea kufuata mambo fulani katika Sheria ya Musa.b

      14 Paulo aliwaeleza Wakristo waliokuwa na mwelekeo wa kufuata Sheria ya Musa kwamba ukuhani mkuu wa Yesu, agano jipya, na hekalu la kiroho, vyote hivyo vilikuwa bora zaidi kuliko agano la Mungu pamoja na Waisraeli. (Ebr. 7:26-28; 8:7-10; 9:11, 12) Kwa hiyo, inaelekea kwamba akifikiria wale walioshika Sabato ya kila juma chini ya Sheria, Paulo aliandika kuhusu pendeleo la kuingia katika siku ya pumziko la Yehova: “Bado limebaki pumziko la sabato kwa ajili ya watu wa Mungu. Kwa maana mtu ambaye ameingia katika pumziko la Mungu yeye mwenyewe pia amepumzika kutokana na kazi zake mwenyewe, kama Mungu alivyopumzika kutokana na kazi zake mwenyewe.” (Ebr. 4:8-10) Wakristo hao Waebrania walipaswa kuacha kufikiri kwamba wangeweza kukubaliwa na Yehova kwa kufuata matendo yaliyotegemea Sheria ya Musa. Tangu Pentekoste ya mwaka wa 33 W.K., ni wale tu ambao wanamwamini Yesu Kristo ndio wanaopata kwa rehema kibali cha Mungu.

      15. Kwa nini kutii ni jambo la maana ikiwa tunataka kuingia katika pumziko la Mungu?

      15 Ni nini kilichowazuia Waisraeli wa siku za Musa kuingia katika ile Nchi ya Ahadi? Ni kutotii. Ni nini kilichokuwa kikiwazuia Wakristo fulani katika siku za Paulo kuingia katika pumziko la Mungu? Ni jambo lilelile, kutotii. Walishindwa kutambua kwamba Sheria ilitimiza kusudi lake na kwamba Yehova alikuwa akiwaongoza watu wake katika njia tofauti.

      Kuingia Katika Pumziko la Mungu Leo

      16, 17. (a) Inamaanisha nini kuingia katika pumziko la Mungu leo? (b) Tutazungumzia nini katika habari inayofuata?

      16 Ni Wakristo wachache leo ambao wanaweza kusisitiza kufuata sehemu fulani za Sheria ya Musa ili kupata wokovu. Maneno ya Paulo yaliyoongozwa na roho ya Mungu ambayo aliwaandikia Waefeso yako wazi kabisa: “Kwa fadhili hizi zisizostahiliwa, kwa kweli, ninyi mmeokolewa kupitia imani; na hiyo si kutokana na ninyi, ni zawadi ya Mungu. Hapana, si kutokana na matendo, ili mtu yeyote asiwe na sababu ya kujisifu.” (Efe. 2:8, 9) Hivyo basi, inamaanisha nini kwa Wakristo kuingia katika pumziko la Mungu? Kumbuka kwamba Yehova alichagua siku ya saba kuwa siku yake ya pumziko ili kutimiza kusudi lake kwa ajili ya dunia kwa njia yenye utukufu. Tunaweza kuingia katika pumziko la Yehova au kujiunga naye katika pumziko lake, kwa kutii na kufanya kazi kulingana na kusudi lake linalosonga mbele kama linavyofunuliwa kwetu kupitia tengenezo lake.

      17 Kwa upande mwingine, tukipuuza mashauri yanayotegemea Biblia ambayo tunapata kupitia jamii ya mtumwa mwaminifu na mwenye busara, huku tukichagua kujitegemea wenyewe, tutakuwa tunapinga kusudi la Mungu ambalo linatimizwa hatua kwa hatua. Jambo hilo lingehatarisha uhusiano wetu wenye amani pamoja na Yehova. Katika habari inayofuata, tutazungumza kuhusu hali fulani za kawaida ambazo zinatupatia nafasi ya kuonyesha kwamba sisi ni watiifu. Maamuzi tunayofanya katika hali hizo yanaweza kuonyesha ikiwa kwa kweli tumeingia katika pumziko la Mungu.

  • Je, Umeingia Katika Pumziko la Mungu?
    Mnara wa Mlinzi—2011 | Julai 15
    • Je, Umeingia Katika Pumziko la Mungu?

      “Neno la Mungu liko hai nalo lina nguvu.”—EBR. 4:12.

      1. Tunaingia jinsi gani katika pumziko la Mungu leo, lakini kwa nini inaweza kuwa vigumu kutii?

      KATIKA habari iliyotangulia, tuliona kwamba tunaweza kuingia katika pumziko la Mungu kwa kumtii na kufanya kazi pamoja na tengenezo lake ili kutimiza makusudi yake. Lakini nyakati fulani inaweza kuwa vigumu kutii. Kwa mfano, tunapojifunza kwamba Yehova anachukizwa na jambo fulani ambalo sisi tunapenda sana, huenda isiwe rahisi kutii haraka. Hilo linaonyesha kwamba tunahitaji kujifunza kuwa “tayari kutii.” (Yak. 3:17) Katika habari hii, tutachunguza hali fulani ambazo zinaweza kutujaribu na kuonyesha ikiwa tuko tayari kutii kutoka moyoni ili kutenda kulingana na kusudi la Mungu.

      2, 3. Tunapaswa kufanya nini ili kuendelea kuwa wenye kutamanika machoni pa Yehova?

      2 Je, uko tayari kutii unapojifunza katika Biblia kwamba unahitaji kufanya mabadiliko fulani katika maisha yako? Maandiko yanatuambia kwamba Mungu anataka kujikusanyia “vitu vyenye kutamanika vya mataifa yote.” (Hag. 2:7) Bila shaka, kabla ya kujifunza kweli za Biblia wengi wetu hatukuwa wenye kutamanika. Hata hivyo, kumpenda Mungu na Mwana wake mpendwa kulitulazimisha kufanya mabadiliko makubwa katika mtazamo na tabia zetu ili tuweze kumpendeza Mungu kikamili. Mwishowe, baada ya kusali sana na kujitahidi, siku yenye baraka ilifika na tulijitoa kwa ajili ya ubatizo wa Kikristo.—Soma Wakolosai 1:9, 10.

      3 Hata hivyo, kupambana na hali yetu ya kutokamilika hakukumalizika baada ya ubatizo wetu. Mapambano yaliendelea na yataendelea kwa sababu bado sisi si wakamilifu. Lakini tunahakikishiwa kwamba tukiendelea kufanya bidii na kuazimia kuwa wenye kutamanika zaidi machoni pa Yehova Mungu, atabariki jitihada zetu.

      Tunapohitaji Mashauri

      4. Yehova anatumia njia gani tatu ili kutuonyesha kwamba tunahitaji kufanya mabadiliko?

      4 Kabla ya kuanza kufanya mabadiliko katika maisha yetu, tunapaswa kujua ni mabadiliko gani ambayo tunahitaji kufanya. Yehova anatusaidia kufanya mabadiliko hayo katika njia tofauti-tofauti. Anaweza kutumia hotuba kwenye Jumba la Ufalme au habari fulani katika magazeti yetu ili kutuonyesha kwamba kuna jambo fulani lenye makosa katika matendo na kufikiri kwetu. Nyakati nyingine hatuelewi kwamba tunahitaji kufanya mabadiliko hata baada ya kusikia hotuba fulani au kusoma kitabu fulani, hivyo Yehova anaweza kumtumia ndugu au dada fulani katika kutaniko ili kuturekebisha kwa fadhili.—Soma Wagalatia 6:1.

      5. Nyakati nyingine tunatenda jinsi gani mtu fulani anapoturekebisha, na kwa nini wachungaji Wakristo wanapaswa kuendelea katika jitihada zao za kutusaidia?

      5 Si jambo rahisi kukubali shauri kutoka kwa mwanadamu mwenzetu asiye mkamilifu, hata shauri hilo likitolewa kwa busara na kwa njia ya upendo kadiri gani. Hata hivyo, kama andiko la Wagalatia 6:1 linavyoonyesha, Yehova anawaamuru wale walio na sifa za kustahili za kiroho ‘wajaribu’ kuturekebisha, wakifanya hivyo “katika roho ya upole.” Tukikubali msaada wao, tutakuwa wenye kutamanika hata zaidi machoni pa Mungu. Bila shaka, katika sala zetu, mara nyingi tunakubali kwamba sisi si wakamilifu. Hata hivyo, mtu fulani anapotuonyesha udhaifu wetu, mwelekeo wetu ni kujaribu kujitetea, kupunguza uzito wa tatizo hilo, kutilia shaka nia ya mtu anayetushauri, au kunung’unika juu ya namna shauri hilo lilivyotolewa. (2 Fal. 5:11) Na ikiwa shauri hilo linagusa jambo fulani ambalo hatupendi watu wazungumzie, kama vile matendo ya mshiriki fulani wa familia yetu, jinsi tunavyovaa na kujipamba, usafi wetu, au aina fulani ya vitumbuizo ambavyo tunapenda lakini vinamchukiza Yehova, tunaweza kukasirika na kumhuzunisha yule anayejaribu kutusaidia! Lakini baada ya kutulia, kwa kawaida tunakubali kwamba shauri hilo lilifaa.

      6. Neno la Mungu linafunua jinsi gani “fikira na makusudio ya moyo”?

      6 Andiko la msingi la habari hii linatukumbusha kwamba neno la Mungu “lina nguvu.” Ndiyo, neno la Mungu lina nguvu za kubadili maisha. Biblia ilitusaidia kufanya mabadiliko tuliyohitaji kufanya kabla ya kubatizwa. Katika barua yake kwa Waebrania, Paulo pia anaandika kwamba neno la Mungu “huchoma hata kufikia kugawanya nafsi na roho, na viungo na urojorojo wake, nalo linaweza kutambua fikira na makusudio ya moyo.” (Ebr. 4:12) Kwa maneno mengine, tunapoelewa vizuri kusudi la Mungu kwa ajili yetu, namna tunavyoitikia kusudi hilo kunaonyesha jinsi tulivyo kwa ndani kabisa. Je, nyakati nyingine kuna tofauti kati ya jinsi tunavyoonekana kwa nje (“nafsi”) na jinsi tulivyo kikweli kwa ndani (“roho”)? (Soma Mathayo 23:27, 28.) Chunguza jinsi ambavyo ungetenda katika hali zinazofuata.

      Endelea Kusonga Mbele Pamoja na Tengenezo la Yehova

      7, 8. (a) Huenda Wakristo fulani Waebrania walichochewa na nini kuendelea kufuata mazoea fulani ya Sheria ya Musa? (b) Kwa nini tunaweza kusema kwamba walikuwa wakitenda kinyume na kusudi la Yehova?

      7 Wengi wetu tunajua vizuri maneno ya andiko la Methali 4:18: “Njia ya waadilifu ni kama nuru inayong’aa, inayozidi kuongezeka mpaka mchana mkamilifu.” Hilo linamaanisha kwamba mwenendo wetu na uelewaji wetu wa kusudi la Mungu utakuwa mzuri zaidi kadiri siku zinavyopita.

      8 Kama tulivyozungumzia katika habari iliyotangulia, baada ya kifo cha Yesu ilikuwa vigumu kwa Wakristo wengi Wayahudi kuacha kufuata Sheria ya Musa. (Mdo. 21:20) Ingawa Paulo alieleza kwa ustadi kwamba Wakristo hawakuwa tena chini ya Sheria, wengine walikataa wazo hilo la Paulo lililoongozwa na roho ya Mungu. (Kol. 2:13-15) Labda walihisi kwamba ikiwa wangeendelea kufuata sehemu fulani za Sheria, wangeepuka kuteswa. Kwa vyovyote vile, Paulo aliwaandikia Wakristo Waebrania na kuwaeleza waziwazi kwamba hawangeingia katika pumziko la Mungu kama wangeendelea kukataa kufanya kazi kupatana na kusudi la Mungu linalofunuliwa hatua kwa hatua.a (Ebr. 4:1, 2, 6; soma Waebrania 4:11.) Ili wakubaliwe na Yehova, wangelazimika kutambua ukweli wa kwamba alikuwa akiongoza watu wake katika njia tofauti.

      9. Tunapaswa kuwa na mtazamo gani wakati marekebisho yanapofanywa kuhusu uelewaji wetu wa Maandiko?

      9 Katika nyakati zetu, kumekuwa na marekebisho katika uelewaji wetu wa mafundisho fulani ya Biblia. Jambo hilo halipaswi kutuvuruga; badala yake linapaswa kutuchochea kuitumaini zaidi jamii ya mtumwa mwaminifu na mwenye busara. Wakati washiriki wanaowakilisha “mtumwa” wanapotambua kwamba maoni yetu kuhusu kweli fulani za Biblia yanahitaji kufafanuliwa au kurekebishwa, hawasiti kufanya marekebisho. Washiriki wa jamii ya mtumwa wanataka sana kutenda kupatana na kusudi la Mungu linalofunuliwa hatua kwa hatua na hawaogopi kuchambuliwa kwa sababu ya kurekebisha mafundisho fulani. Wewe unaitikia jinsi gani wakati marekebisho yanapofanywa kuhusu uelewaji wetu wa Maandiko?—Soma Luka 5:39.

      10, 11. Ni mambo gani tunayoweza kujifunza kutokana na jinsi watu fulani walivyotenda wakati njia mpya za kuhubiri habari njema zilipoanzishwa?

      10 Acheni tuzungumzie mfano mwingine. Karibu miaka mia moja hivi iliyopita, Wanafunzi fulani wa Biblia ambao walitoa hotuba nzuri sana walifikiri kwamba kutoa hotuba ilikuwa njia bora zaidi ya kuhubiri. Walipenda sana kutoa hotuba mbele ya watu wengi, na wengine wao walifurahia sana kusifiwa na wasikilizaji wao. Lakini baadaye, watu wa Yehova walielewa wazi zaidi kwamba Yehova alitaka watu wake wafanye mengi zaidi ya kutoa tu hotuba za watu wote. Aliwataka wahubiri nyumba kwa nyumba na kuhubiri kwa njia nyingine mbalimbali. Wengine kati ya wasemaji hao wazuri hawakutaka kufanya hivyo. Kwa nje, walionekana kuwa wanaume wa kiroho ambao walijitoa kabisa kwa Bwana. Hata hivyo, walipoonyeshwa wazi kusudi la Mungu kuhusu kazi ya kuhubiri, mawazo yao, nia yao, na makusudi yao ya ndani kabisa yalionekana wazi. Yehova alihisi namna gani kuwahusu? Hakuwabariki. Waliacha tengenezo.—Mt. 10:1-6; Mdo. 5:42; 20:20.

      11 Ilikuwa pia vigumu kwa wanafunzi wengi wa Biblia waliobaki washikamanifu kwa tengenezo kuhubiri nyumba kwa nyumba, hasa mwanzoni. Lakini walitii. Baada ya muda, ilikuwa rahisi kwao kuhubiri nyumba kwa nyumba, na Yehova aliwabariki sana. Wewe unafanya nini unapoombwa ushiriki katika njia fulani ya kuhubiri ambayo haikupendezi? Je, uko tayari kujaribu njia hiyo mpya ya kuhubiri?

      Mtu Tunayempenda Anapomwacha Yehova

      12, 13. (a) Ni nini kusudi la Yehova la kuamuru wakosaji wasiotubu watengwe na ushirika? (b) Ni jaribu gani ambalo wazazi fulani Wakristo wanakabili, na ni nini kinachofanya jaribu hilo liwe gumu?

      12 Bila shaka sote tunakubaliana na kanuni ya kwamba ni lazima tuwe safi kimwili, kiadili, na kiroho ili kumpendeza Mungu. (Soma Tito 2:14.) Hata hivyo, nyakati fulani ushikamanifu wetu kwa sehemu hiyo ya kusudi la Mungu unaweza kujaribiwa kabisa. Kwa mfano, tuseme kwamba mwana pekee wa wenzi wa ndoa Wakristo ambao ni mfano mzuri anaacha kweli. Kwa kuwa anapendelea zaidi “kufurahia dhambi kwa muda” kuliko uhusiano wake pamoja na Yehova na pamoja na wazazi wake wanaomwogopa Mungu, kijana huyo anatengwa na ushirika.—Ebr. 11:25.

      13 Wazazi wanavunjika moyo kabisa! Bila shaka, kuhusu kutengwa na ushirika, wanajua kwamba Biblia inasema “mwache kuchangamana katika ushirika pamoja na mtu yeyote anayeitwa ndugu ambaye ni mwasherati au mtu mwenye pupa au mwabudu-sanamu au mtukanaji au mlevi au mnyang’anyi, hata msile chakula pamoja na mtu wa namna hiyo.” (1 Kor. 5:11, 13) Wanatambua pia kwamba maneno “mtu yeyote” katika mstari huo yanatia ndani washiriki wa familia ambao hawaishi nyumbani. Lakini wazazi hao wanampenda sana mwana wao! Hisia zenye nguvu zinaweza kufanya wafikiri hivi: ‘Tunaweza kumsaidia kijana wetu jinsi gani amrudie Yehova tukikatisha kabisa uhusiano wetu pamoja naye? Je, hatuwezi kumsaidia zaidi kwa kuendelea kushirikiana naye kwa ukawaida?’b

      14, 15. Wazazi wa watoto waliotengwa na ushirika wanapaswa kufanya uamuzi gani hasa?

      14 Tunahuzunika pamoja na wazazi hao. Hata hivyo, mwana wao alipaswa kufanya uamuzi, na aliamua kufuatia mwenendo usio wa Kikristo badala ya kuendelea kufurahia kushirikiana kwa ukaribu pamoja na wazazi wake na waamini wenzake. Kwa upande mwingine, wazazi wake hawangeweza kumwamulia jambo la kufanya. Haishangazi kwamba wanaumia sana moyoni!

      15 Lakini wazazi hao wapendwa watafanya nini? Je, watatii mwongozo wa Yehova ulio wazi? Au je, watapunguza uzito wa mwongozo huo kwa kufikiri kwamba wanaweza kuendelea kushirikiana kwa ukawaida na mwana wao aliyetengwa na ushirika na kusema kwamba hayo ni “mambo ya lazima ya familia”? Wanapofanya uamuzi wao, hawapaswi kamwe kusahau jinsi Yehova anavyohisi kuhusu yale wanayofanya. Kusudi lake ni kwamba tengenezo liendelee kuwa safi na, ikiwezekana, kuwachochea wakosaji kurudiwa na fahamu zao. Wazazi Wakristo wanaweza jinsi gani kuunga mkono kusudi hilo?

      16, 17. Tunaweza kujifunza nini kwa kutafakari juu ya mfano wa Haruni?

      16 Haruni, ndugu ya Musa, alikuwa katika hali ngumu kwa sababu ya mambo ambayo wawili kati ya watoto wake wa kiume walifanya. Fikiria jinsi ambavyo huenda alihisi vijana wake wawili Nadabu na Abihu walipotoa moto haramu mbele za Yehova naye Akawaua mara moja. Bila shaka, wanaume hao walipokufa uhusiano wowote ambao wangekuwa nao pamoja na wazazi wao ulikoma. Lakini kulikuwa na jambo lingine zaidi ya hilo. Yehova alimwamuru hivi Haruni na watoto wake wa kiume waaminifu: “Msiache vichwa vyenu vikose kuwa nadhifu, wala msiyararue mavazi yenu [kwa kuomboleza], msije mkafa wala [Yehova] asije akalikasirikia kusanyiko lote.” (Law. 10:1-6) Ujumbe uko wazi. Ni lazima upendo wetu kwa Yehova uwe wenye nguvu zaidi kuliko upendo wetu kwa washiriki wa familia ambao si waaminifu.

      17 Leo, Yehova hawaangamizi papo hapo wale wanaovunja sheria zake. Kwa upendo, anawapa nafasi ya kutubu kutokana na matendo yao yasiyo ya uadilifu. Hata hivyo, Yehova atahisi namna gani ikiwa wazazi wa mkosaji asiyetubu wanaendelea kumjaribu Yehova kwa kushirikiana isivyo lazima na mwana au binti yao aliyetengwa na ushirika?

      18, 19. Ni baraka gani ambazo washiriki wa familia wanaweza kupata kwa kufuata maagizo ya Yehova kuhusu watu waliotengwa na ushirika?

      18 Watu wengi ambao wakati fulani walikuwa wametengwa na ushirika, sasa wanakubali waziwazi kwamba msimamo imara wa marafiki wao na washiriki wa familia zao uliwasaidia kurudiwa na fahamu. Kwa mfano, mwanamke mmoja aliwaambia wazee wakati wa kurudishwa kwake kwamba jambo moja lililomsaidia kubadili njia yake ya maisha “ni jinsi ndugu yake wa kimwili alivyotenda kwa kuheshimu mpango wa kutenga na ushirika.” Mwanamke huyo alisema kwamba “kilichomsaidia kutaka kurudi ni kwamba ndugu yake alishikamana kwa uaminifu na miongozo ya Kimaandiko.”

      19 Basi, tunahitaji kufanya nini? Tunahitaji kupambana na mwelekeo wa mioyo yetu isiyo mikamilifu wa kuasi mashauri ya Kimaandiko. Tunapaswa kusadiki kabisa kwamba njia ya Mungu ya kushughulikia matatizo yetu sikuzote ni bora kabisa kwetu.

      “Neno la Mungu Liko Hai”

      20. Tunaweza kuelewa andiko la Waebrania 4:12 katika njia gani mbili? (Ona maelezo ya chini.)

      20 Paulo alipoandika kwamba “neno la Mungu liko hai,” hakuwa akizungumzia hasa Neno la Mungu lililoandikwa, yaani, Biblia.c Mistari mingine katika sura hiyo inaonyesha kwamba alikuwa akizungumza kuhusu ahadi za Mungu. Paulo alikuwa akisema kwamba sikuzote Mungu anatimiza ahadi zake. Yehova alionyesha ukweli wa jambo hilo kupitia nabii Isaya kwa kusema: “Neno langu . . . halitarudi kwangu bila matokeo, bali . . . litafanikiwa katika yale ambayo nimelituma.” (Isa. 55:11) Hivyo, tunahitaji kuwa wenye subira ikiwa mambo hayafanyiki haraka kama tunavyotazamia. Tunaweza kuwa na hakika kwamba Yehova ‘anaendelea kufanya kazi’ ili kutimiza kabisa kwa mafanikio kusudi lake.—Yoh. 5:17.

      21. Andiko la Waebrania 4:12 linaweza jinsi gani kuwatia moyo washiriki waaminifu waliozeeka wa “umati mkubwa”?

      21 Washiriki waaminifu waliozeeka wa “umati mkubwa” wamemtumikia Yehova kwa makumi ya miaka. (Ufu. 7:9) Wengi wao hawakutazamia kwamba wangezeeka katika mfumo huu wa mambo. Hata hivyo, hawavunjiki moyo. (Zab. 92:14) Wanajua kwamba ahadi za Mungu ni za kweli, ziko hai, na Yehova anafanya kazi ili kuzitimiza. Kwa kuwa Mungu anathamini kutoka moyoni kusudi lake, tunamfanya ashangilie tunapoonyesha kwamba kusudi hilo ni la maana kwetu pia. Katika siku hii ya saba ya pumziko, hakuna jambo ambalo litamzuia Yehova kukamilisha kusudi lake. Na anajua kwamba watu wake, wakiwa kikundi, wataendelea kutenda kupatana na kusudi lake. Namna gani wewe? Je, wewe binafsi umeingia katika pumziko la Mungu?

      [Maelezo ya Chini]

      a Viongozi wengi kati ya Wayahudi walifuata kwa uangalifu sana Sheria ya Musa, lakini Masihi alipofika, walishindwa kumtambua. Hawakutenda kulingana na kusudi la Mungu lenye kuendelea.

      b Ona kitabu “Jitunzeni Katika Upendo wa Mungu,” ukurasa wa 207-209.

      c Leo, Mungu anazungumza nasi kupitia Neno lake lililoandikwa, Biblia, ambalo lina nguvu ya kubadili maisha yetu. Kwa hiyo, yale tunayosoma katika Waebrania 4:12 ni kweli pia kuhusu Biblia.

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki