Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Nilijifunza Kumtegemea Yehova
    Mnara wa Mlinzi—1998 | Septemba 1
    • Nilijifunza Kumtegemea Yehova

      KAMA ILIVYOSIMULIWA NA JÁN KORPA-ONDO

      Ulikuwa mwaka wa 1942, nami nilikuwa nikilindwa na wanajeshi wa Hungaria karibu na Kursk, Urusi. Tulikuwa wafungwa wa serikali ya Ujerumani, Italia, na Japani, ambazo zilikuwa zikipigana na Urusi kwenye Vita ya Ulimwengu ya Pili. Kaburi langu lilichimbwa, nami nikapewa dakika kumi za kuamua ikiwa ningetia sahihi hati iliyosema kwamba tangu wakati huo sikuwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova. Kabla sijasimulia lililotukia baadaye, acheni niwaambie nilivyopata kuwa hapo.

      NILIZALIWA mwaka wa 1904 katika kijiji kidogo cha Zahor, kilicho mashariki mwa Slovakia sasa. Baada ya Vita ya Ulimwengu ya Kwanza, kijiji cha Zahor kilipata kuwa sehemu ya nchi ya Chekoslovakia, iliyotoka tu kuundwa.

  • Nilijifunza Kumtegemea Yehova
    Mnara wa Mlinzi—1998 | Septemba 1
    • Mwanzo wa Majaribu Makali

      Mwaka wa 1938, eneo letu lilitawalwa na Hungaria, iliyounga mkono Ujerumani wakati wa Vita ya Ulimwengu ya Pili. Kufikia wakati huo tulikuwa na Mashahidi wapatao 50 katika kijiji chetu chenye watu waliopungua elfu moja. Tuliendelea kuhubiri ingawa kufanya hivyo kulihatarisha maisha zetu na uhuru wetu.

      Katika 1940, niliandikishwa katika jeshi la Hungaria. Ningefanyaje? Nilikuwa nimesoma unabii mbalimbali wa Biblia juu ya watu kubadili silaha zao za vita kuwa vyombo vya amani, na nilijua kwamba, hatimaye, Mungu angeondolea mbali vita vyote duniani. (Zaburi 46:9; Isaya 2:4) Hivyo, nilichukia vita, nami niliamua kutojiunga na jeshi, bila kujali matokeo.

      Nilihukumiwa kifungo cha miezi 14 gerezani nami nikafungwa huko Pécs, Hungaria. Mashahidi wengine watano walikuwa katika gereza iyo hiyo, nasi tulithamini sana kuweza kushirikiana pamoja. Hata hivyo, kwa muda fulani, nilikuwa katika kifungo cha upweke nikiwa na minyororo katika miguu yangu. Tulipokataa kufanya kazi iliyohusiana na jitihada za kivita, tulipigwa. Pia, tulilazimishwa kusimama wima siku nzima, isipokuwa muda wa saa mbili wakati wa adhuhuri. Masaibu hayo yaliendelea kwa miezi kadhaa. Hata hivyo tulikuwa wenye furaha kwa sababu tulikuwa na dhamiri safi mbele za Mungu wetu.

      Suala la Kuridhiana

      Siku moja kikundi cha makasisi 15 Wakatoliki kilikuja ili kujaribu kutusadikisha kwamba ilikuwa muhimu tutegemeze jitihada za kivita kwa kujiunga na jeshi. Wakati wa mazungumzo hayo tulisema hivi: “Ikiwa mwaweza kuthibitisha kutoka katika Biblia kwamba nafsi haiwezi kufa na kwamba tutaenda mbinguni tukifa vitani, tutajiunga na jeshi.” Bila shaka, hawangeweza kuthibitisha hilo, nao hawakutaka kuendeleza mazungumzo hayo.

      Mwaka wa 1941 kifungo changu gerezani kiliisha, nami nilikuwa nikitarajia kuungana tena na familia yangu. Badala yake, nilipelekwa nikiwa nimefungwa kwa minyororo hadi kwenye kituo cha jeshi katika Sárospatak, Hungaria. Tulipofika, nilipewa fursa ya kuachiliwa. “Unalopaswa kufanya tu,” nikaambiwa, “ni kutia sahihi ahadi hii ya kwamba utalipa pengö 200 urudipo nyumbani.”

      “Hilo lawezekanaje?” nikauliza. “Mwataka fedha hizo kwa kusudi gani?”

      “Ukilipa fedha hizo,” nikaambiwa, “utapokea cheti cha kusema kwamba hukupita mtihani wa kitiba wa kuingia jeshini.”

      Huo ulikuwa uamuzi mgumu kwangu. Kwa zaidi ya mwaka mmoja, nilikuwa nimetendwa kinyama; nilikuwa naanza kuchoka. Sasa, kwa kulipa kiasi fulani cha fedha, ningeweza kuwa huru. “Nitafikiria hilo,” nikanong’ona.

      Ningeamua nini? Nilikuwa na mke na watoto ambao nilipaswa kuwafikiria. Basi, karibu wakati uo huo, nilipokea barua kutoka kwa Mkristo mwenzangu, aliyenitia moyo katika barua hiyo. Alinukuu Waebrania 10:38, ambapo mtume Paulo anukuu maneno ya Yehova hivi: “‘Mwadilifu wangu ataishi kwa sababu ya imani,’ na, ‘ikiwa yeye ajikunyata, nafsi yangu haina upendezi katika yeye.’” Punde baadaye, maofisa wawili Wahungaria kwenye kambi wakazungumza nami, mmoja wao akisema: “Huna habari juu ya jinsi tunavyokustahi kwa sababu ya kutegemeza kanuni za Biblia kwa uthabiti hivyo! Usikate tamaa!”

      Siku iliyofuata niliwaendea walionitolea uhuru wangu kwa malipo ya pengö 200 na kusema: “Kwa kuwa Yehova Mungu ameniruhusu nifungwe, atashughulikia kuachiliwa kwangu. Sitalipa fedha ili niachiliwe.” Kwa hiyo nikahukumiwa kifungo cha miaka kumi gerezani. Lakini huo haukuwa mwisho wa kujaribu kunifanya niridhiane. Mahakama ilikuwa tayari kunisamehe ikiwa ningekubali kutumikia katika jeshi kwa miezi miwili tu, nami hata singebeba silaha yoyote! Toleo hilo nalo nililikataa, nacho kifungo changu gerezani kikaanza.

      Mnyanyaso Waongezeka

      Nilipelekwa tena gerezani Pécs. Wakati huu mateso yalikuwa makali hata zaidi. Mikono yangu ilikuwa imefungwa ikiwa nyuma mgongoni, nami nilining’inizwa kwayo kwa muda wa saa mbili. Kwa sababu hiyo, mabega yangu yote mawili yaliteguka. Mateso hayo yalirudiwa-rudiwa kwa kipindi cha miezi sita hivi. Naweza kumshukuru Yehova kwamba sikukata tamaa.

      Mwaka wa 1942 kikundi chetu—wafungwa wa kisiasa, Wayahudi, na Mashahidi wa Yehova 26 —kilipelekwa katika jiji la Kursk katika eneo lililokuwa limetwaliwa na vikosi vya Ujerumani. Tulichukuliwa na Wajerumani, nao wakawapa wafungwa kazi ya kubeba chakula, silaha, na mavazi na kupelekea wanajeshi kwenye mapigano. Sisi Mashahidi tulikataa kufanya kazi hiyo kwa sababu ilihalifu kutokuwamo kwetu kwa Kikristo. Kwa hiyo, tukarudishwa kwa Wahungaria.

      Hatimaye, tuliwekwa katika gereza la Kursk. Kwa siku kadhaa tulichapwa kwa viboko vya mpira mara tatu kwa siku. Nilipigwa kwenye panda, nikaanguka chini. Nilipokuwa nikipigwa, nilifikiri, ‘Si vigumu sana kufa.’ Mwili wangu wote ukafa ganzi, kwa hiyo sikuweza kuhisi chochote. Kwa siku tatu hatukupewa chakula chochote. Kisha tukapelekwa mahakamani, na sita kati yetu wakahukumiwa kifo. Hukumu hiyo ilipotekelezwa, tulisalia watu 20.

      Majaribu ya imani tuliyopata siku hizo huko Kursk, katika Oktoba ya mwaka wa 1942, yalikuwa ndiyo majaribu makali zaidi ambayo nimepata kukabili. Hisia zetu za moyoni zilionyeshwa vema na Mfalme Yehoshafati wa kale wakati ambapo watu wake walikabiliwa na mambo yenye kupita kiasi: “Sisi hatuna uwezo juu ya jamii kubwa hii, wanaotujia juu yetu; wala hatujui tufanyeje; lakini macho yetu yatazama kwako.”—2 Mambo ya Nyakati 20:12.

      Sisi tukiwa 20 tulipelekwa nje tukachimbe kaburi la ujumla, tukilindwa na askari 18 wa Hungaria. Tulipomaliza kuchimba, tuliambiwa kwamba tulikuwa na dakika kumi za kutia sahihi hati, iliyosema hivi kwa sehemu: “Mafundisho ya Mashahidi wa Yehova ni yenye kosa. Sitayaamini wala kuyategemeza tena kamwe. Nitaipigania nchi yangu, Hungaria . . . nathibitisha kwa kutia sahihi kwamba najiunga na Kanisa Katoliki la Kiroma.”

      Baada ya dakika kumi hivi amri ikatolewa: “Geukeni kuelekea upande wa kulia! Pigeni hatua kuelekea kaburi!” Kisha, amri ikatolewa: “Mfungwa wa kwanza na wa tatu ingieni shimoni!” Hao wawili walipewa dakika nyingine kumi za kuamua kutia sahihi hati hiyo. Mmojawapo wa askari alisihi hivi: “Acheni imani yenu, mtoke kaburini!” Hakuna aliyesema lolote. Kisha ofisa msimamizi akawapiga risasi.

      “Vipi waliosalia?” askari mmoja akamwuliza ofisa msimamizi.

      “Wafunge,” akajibu. “Tutawatesa zaidi na kuwapiga risasi saa 12 alfajiri.”

      Ghafula nikaogopa, si kwamba ningekufa, lakini kwamba singeweza kuvumilia mateso na kwamba ningeridhiana. Kwa hiyo nikajitokeza na kusema: “Bwana, tumekosea sawa na ndugu zetu ambao umetoka kuwapiga risasi. Mbona usitupige risasi pia?”

      Lakini hawakutupiga risasi. Tulifungwa mikono yetu ikiwa nyuma mgongoni. Kisha tukaning’inizwa kwa mikono yetu. Tulipopoteza fahamu, walitumwagia maji. Maumivu yalikuwa makali sana kwa sababu uzito wa mwili ulitegua mabega yetu. Mateso hayo yaliendelea kwa muda wa saa tatu. Kisha, bila kutarajia, amri ya kutowapiga risasi Mashahidi wa Yehova wowote zaidi ikatolewa.

      Kwenda Mashariki—Kisha Kutoroka

      Majuma matatu baadaye tulipiga mwendo tukiwa kikundi kwa siku chache hadi tukafika kingo za Mto Don. Tuliambiwa na wasimamizi kwamba hatungerudishwa tukiwa hai. Siku hiyo, tulipewa kazi isiyo na kusudi, kuchimba mitaro na kuifunika tena. Jioni, tulikuwa na kiasi fulani cha uhuru wa kutembea-tembea.

      Kwa maoni yangu, tungeweza kufanya mambo mawili. Tungeweza kufa papo hapo, au tungeweza kuwatoroka Wajerumani na kujiuzulu kwa Warusi. Ni watatu tu kati yetu tulioamua kujaribu kutoroka kwa kuvuka Mto Don uliokuwa umeganda. Desemba 12, 1942, tulisali kwa Yehova na kuondoka. Tulifika yalipokuwa majeshi ya Urusi na mara moja tukawekwa katika gereza la kambi pamoja na wafungwa 35,000. Kufikia masika, ni wafungwa 2,300 waliokuwa wangali hai. Wale wengine walikuwa wamekufa njaa.

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki