-
Kufanya Maamuzi Ni Jambo Gumu Lisiloweza KuepukikaMnara wa Mlinzi—2003 | Oktoba 15
-
-
Kufanya Maamuzi Ni Jambo Gumu Lisiloweza Kuepukika
NAPOLEON BONAPARTE, maliki wa Ufaransa wa karne ya 19, alisema hivi wakati mmoja: “Hakuna jambo lililo gumu au lenye thamani zaidi kuliko kuwa na uwezo wa kufanya maamuzi.” Yaelekea utakubaliana na maneno hayo, kwa kuwa watu kwa ujumla huthamini sana kuwa na uwezo wa kuongoza maisha yao. Wakati huohuo, watu wamejifunza kwamba nyakati nyingine ni vigumu sana kufanya maamuzi.
Hatuwezi kuepuka kufanya maamuzi, yawe rahisi au yawe magumu. Inatubidi kufanya maamuzi kila siku. Baada ya kuamka asubuhi, lazima tuamue tutavaa nini, ni kiamsha kinywa gani tutakachokula, na pia tuamue jinsi tutakavyoshughulika na mambo mbalimbali mchana kutwa. Mengi ya maamuzi hayo si muhimu sana. Mara nyingi hatuyafikirii sana. Ni mara chache tutakosa usingizi hata kama maamuzi hayo ni ya hekima au si ya hekima.
Kwa upande mwingine, maamuzi mengine ni muhimu sana. Lazima vijana wengi katika ulimwengu wa sasa waamue ni miradi ya aina gani watakayofuatia. Huenda ikawabidi kuamua watasomea nini na kwa muda gani. Baadaye wengi wao wataamua kama watafunga ndoa au watabaki waseja. Wale wanaotaka kufunga ndoa lazima waamue: ‘Je, nina umri wa kutosha na nimekomaa vya kutosha kufunga ndoa? Ninataka mwenzi wa aina gani, au jambo lililo muhimu zaidi, ninahitaji mwenzi wa aina gani?’ Kuchagua mwenzi wa ndoa ni uamuzi unaoweza kuathiri sana maisha yetu.
Tunapaswa kufanya maamuzi ya hekima kuhusiana na mambo muhimu, kwa kuwa furaha yetu inategemea sana maamuzi tunayofanya. Huenda wengine wakahisi kwamba wana uwezo wa kufanya maamuzi hayo na huenda wakakataa kusaidiwa. Je, ni jambo la hekima kufanya hivyo? Acheni tuone.
-
-
Unawezaje Kufanya Maamuzi ya Hekima?Mnara wa Mlinzi—2003 | Oktoba 15
-
-
Unawezaje Kufanya Maamuzi ya Hekima?
MFALME Sulemani wa Israeli la kale alisema: “Mwenye hekima asikie na kuongezewa elimu.” Nyakati fulani wengi wetu tumefanya maamuzi yasiyo ya hekima kwa sababu tu tulikataa kusikiliza mashauri ya wengine.—Mithali 1:5.
Baadaye, maneno hayo ya Sulemani yaliandikwa katika Biblia, pamoja na ‘methali nyingine elfu tatu’ alizotunga. (1 Wafalme 4:32, Biblia Habari Njema) Je, tunaweza kunufaika kwa kujua na kutii maneno yake ya hekima? Ndiyo. Yanatusaidia “kujua hekima na adabu; kutambua maneno ya ufahamu; kufundishwa matendo ya busara, katika haki na hukumu na adili.” (Mithali 1:2, 3) Acheni tuzungumzie kanuni tano zinazotegemea Biblia ambazo zinaweza kutusaidia kufanya maamuzi ya hekima.
Fikiria Matokeo ya Muda Mrefu
Maamuzi fulani yatakuwa na matokeo muhimu. Kwa hiyo, jaribu kujua mapema matokeo yatakavyokuwa. Uwe mwangalifu manufaa ya muda mfupi yasikupumbaze ukose kuona matokeo mabaya ya muda mrefu. “Mwenye busara huyaona mabaya na kujificha; bali wajinga huendelea mbele wakaumia,” linaonya andiko la Mithali 22:3.
Huenda ikafaa kuandika orodha ya matokeo ya muda mfupi na ya muda mrefu. Huenda matokeo ya muda mfupi ya kuchagua kazi fulani yakawa mshahara mnono au kazi yenye kufurahisha. Lakini je, matokeo ya muda mrefu yanaweza kutia ndani kuwa na kazi ambayo haina matarajio mazuri ya baadaye? Je, huenda mwishowe kazi hiyo ikakufanya uhamie mahali pengine, labda mbali na marafiki au familia? Je, huenda ikakulazimu kukaa katika mazingira yasiyofaa au huenda isiwe yenye kupendeza na hivyo kukukatisha tamaa sana? Fikiria faida na madhara, kisha uamue utatanguliza nini.
Tumia Wakati wa Kutosha
Ni rahisi kufanya maamuzi yasiyo ya hekima ikiwa utayafanya haraka-haraka. Andiko la Mithali 21:5, NW, linaonya: “Mipango ya mwenye bidii bila shaka huleta faida, lakini kila mtu anayetenda haraka-haraka bila shaka huulekea uhitaji.” Kwa mfano, vijana waliopumbazika kimahaba hawapaswi kuamua kufunga ndoa haraka-haraka. La sivyo, huenda wakakubaliana na maneno haya ya mwandishi Mwingereza wa michezo ya kuigiza, William Congreve, aliyeandika miaka ya mapema ya 1700: “Watu wanaofunga ndoa haraka-haraka huenda wakajuta kwa muda mrefu.”
Hata hivyo, kutumia wakati wa kutosha hakumaanishi kukawia-kawia. Maamuzi mengine ni muhimu sana hivi kwamba ni jambo la hekima kuyafanya haraka iwezekanavyo. Kukawia-kawia isivyofaa kunaweza kutuletea sisi au wengine hasara kubwa. Huenda kuahirisha kufanya uamuzi fulani, kukawa kwenyewe uamuzi mwingine, lakini hilo si jambo la hekima.
Kubali Mashauri
Kwa kuwa hali haziwezi kufanana kabisa, huenda watu wawili wakafanya maamuzi tofauti ingawa wanakabili matatizo yaleyale. Hata hivyo, inafaa kusikiliza jinsi wengine walivyoamua mambo katika hali zinazofanana na zetu. Waulize jinsi wanavyoyaona maamuzi yao sasa. Kwa mfano, unapochagua kufanya biashara fulani, waulize wale ambao tayari wanaifanya wakueleze faida na hasara za biashara hiyo. Wamepata manufaa gani kwa kuchagua kufanya biashara hiyo, na wamepata hasara gani au biashara hiyo inaweza kuwa na hatari gani?
Tunaonywa kwamba “pasipo mashauri makusudi hubatilika; bali kwa wingi wa washauri huthibitika.” (Mithali 15:22) Bila shaka, tunapotafuta mashauri na kujifunza kutokana na mambo yaliyowapata wengine, tunapaswa kutambua kabisa kwamba sisi wenyewe ndio tutakaofanya uamuzi wa mwisho na pia kuwajibika kwa uamuzi huo.—Wagalatia 6:4, 5.
Sikiliza Dhamiri Iliyozoezwa Vizuri
Dhamiri inaweza kutusaidia kufanya maamuzi yanayopatana na kanuni za msingi tunazochagua kufuata maishani. Kwa Mkristo, hilo linamaanisha kuzoeza dhamiri ili itende kupatana na mawazo ya Mungu. (Waroma 2:14, 15) Neno la Mungu linatuambia hivi: “Katika njia zako zote mkiri yeye, naye atayanyosha mapito yako.” (Mithali 3:6) Bila shaka, katika hali fulani, huenda watu wawili—kila mmoja akiwa na dhamiri iliyozoezwa vizuri—wakafikia mikataa tofauti na hivyo kufanya maamuzi yaliyo tofauti.
Hata hivyo, dhamiri iliyozoezwa vizuri itamzuia mtu kuamua kutofanya mambo yanayoshutumiwa moja kwa moja na Neno la Mungu. Kwa mfano, huenda dhamiri ambayo haijazoezwa na kanuni za Biblia ikamruhusu mwanamume na mwanamke kuishi pamoja kabla ya kufunga ndoa ili kuona kama wanafaana. Huenda wakafikiri kwamba wamefanya uamuzi wa hekima, wakisema kwamba hatua hiyo itawazuia kufanya jambo lisilo la hekima la kufunga ndoa haraka-haraka. Huenda wasisumbuliwe na dhamiri yao. Lakini, yeyote aliye na maoni kama ya Mungu kuhusu ngono na ndoa hataamua kuchukua hatua hiyo ya muda na isiyo ya adili.—1 Wakorintho 6:18; 7:1, 2; Waebrania 13:4.
Jinsi Maamuzi Yako Yanavyowaathiri Wengine
Mara nyingi, huenda maamuzi yako yakawaathiri wengine. Kwa hiyo, usifanye kimakusudi maamuzi yasiyo ya hekima au hata ya kipumbavu ambayo yanaweza kuhatarisha uhusiano wako wenye thamani pamoja na marafiki na watu wa ukoo, na hasa pamoja na Mungu. Andiko la Mithali 10:1 linasema: “Mwana mwenye hekima humfurahisha babaye; bali mwana mpumbavu ni mzigo wa mamaye.”
Kwa upande mwingine, unapaswa kutambua kwamba nyakati nyingine utalazimikakuamua ni nani watakaokuwa marafiki wako. Kwa mfano, huenda ukaamua kukataa maoni ya kidini uliyokuwa nayo zamani kwa kuwa sasa unajua kwamba yanapingana na Maandiko. Au huenda ukaamua kufanya mabadiliko makubwa kuhusiana na utu wako kwa sababu unatamani kuishi kupatana na kanuni za Mungu ambazo sasa umekubali. Huenda baadhi ya marafiki au watu wa ukoo wasipendezwe na uamuzi wako, lakini uamuzi wowote unaompendeza Mungu ni wa hekima.
-