-
Fanya Maamuzi Ambayo Yanamletea Mungu HeshimaMnara wa Mlinzi—2011 | Aprili 15
-
-
Hatua Sita za Kufanya Maamuzi Mazuri
10, 11. (a) Tunaweza kuepuka jinsi gani kuwa na kimbelembele katika familia? (b) Wazee wanapaswa kukumbuka nini wanapofanya maamuzi ambayo yanahusu kutaniko?
10 Epuka kimbelembele. Kabla ya kuamua jambo la kufanya, tunahitaji kujiuliza, ‘Je, nina mamlaka ya kufanya uamuzi huu?’ Mfalme Sulemani aliandika hivi: “Je, kimbelembele kimekuja? Basi aibu itakuja; lakini wenye kiasi wana hekima.”—Met. 11:2.
11 Wazazi wanaweza kuwapa watoto wao uhuru wa kufanya maamuzi fulani, lakini watoto hawapaswi kujichukulia mamlaka hayo. (Kol. 3:20) Wake na akina mama wana mamlaka ya kadiri fulani katika familia lakini ni vizuri watambue ukichwa wa waume wao. (Met. 1:8; 31:10-18; Efe. 5:23) Vivyo hivyo, waume wanahitaji kutambua kwamba mamlaka yao ina mipaka na kwamba wako chini ya Kristo. (1 Kor. 11:3) Wazee wanafanya maamuzi ambayo yanahusu kutaniko. Hata hivyo, wanahakikisha kwamba ‘hawapiti mambo yaliyoandikwa’ katika Neno la Mungu. (1 Kor. 4:6) Pia, wanafuata kwa makini mwongozo ambao wanapokea kutoka kwa mtumwa mwaminifu. (Mt. 24:45-47) Tunaweza kujiokoa wenyewe na kuwaokoa wengine wasipatwe na mahangaiko na huzuni kubwa tukiwa wenye kiasi na kufanya maamuzi ikiwa tu tumepewa mamlaka ya kufanya hivyo.
12. (a) Kwa nini tunapaswa kufanya utafiti? (b) Eleza jinsi mtu anavyoweza kujifanyia utafiti.
12 Fanya utafiti. Sulemani aliandika hivi: “Mipango ya mwenye bidii bila shaka huleta faida, lakini kila mtu anayetenda haraka-haraka bila shaka huuelekea uhitaji.” (Met. 21:5) Kwa mfano, unafikiria kuanzisha biashara? Usiongozwe na hisia zako. Kusanya habari zote zinazofaa, waombe mashauri wale ambao wanajua mambo kama hayo, na uchunguze kanuni za Biblia ambazo zinahusiana na jambo hilo. (Met. 20:18) Ili utayarishe utafiti wako, andika orodha mbili, orodha moja inapaswa kuonyesha faida, na orodha nyingine hasara. Kabla ya kufanya uamuzi, ‘hesabu gharama.’ (Luka 14:28) Fikiria jinsi uamuzi wako utakavyokuwa na matokeo si juu ya hali yako ya kifedha tu bali pia juu ya hali yako ya kiroho. Unahitaji wakati na jitihada ili kufanya utafiti. Lakini ukifanya hivyo, unaweza kuepuka kufanya maamuzi ya haraka ambayo yanaweza kusababisha mahangaiko yasiyo ya lazima.
13. (a) Andiko la Yakobo 1:5 linatuhakikishia nini? (b) Kusali ili tupate hekima kunaweza kutusaidia jinsi gani?
13 Sali ili upate hekima. Maamuzi yetu yatamletea Mungu heshima ikiwa tu tutamwomba atusaidie kuyafanya. Mwanafunzi Yakobo aliandika hivi: “Ikiwa yeyote kati yenu anakosa hekima, na aendelee kumwomba Mungu, kwa maana yeye huwapa wote kwa ukarimu na bila kushutumu; naye atapewa hiyo.” (Yak. 1:5) Hatupaswi kuona aibu kukubali kwamba tunahitaji hekima ya Mungu ili itusaidie kufanya maamuzi. (Met. 3:5, 6) Bila shaka, kutegemea tu uelewaji wetu wenyewe kunaweza kwa urahisi kutuongoza vibaya. Tunaposali ili tupate hekima na tunapochunguza kanuni za Neno la Mungu, tunaruhusu roho takatifu itusaidie kutambua nia yetu halisi ya kutaka kuchukua hatua fulani.—Ebr. 4:12; soma Yakobo 1:22-25.
14. Kwa nini tunapaswa kuepuka kungoja-ngoja kufanya uamuzi?
14 Fanya uamuzi. Usikimbilie kufanya uamuzi kabla ya kufanya utafiti na kusali ili upate hekima. Mtu mwenye hekima anachukua muda wa ‘kufikiria hatua zake.’ (Met. 14:15) Kwa upande mwingine, usiahirishe au kungoja-ngoja kufanya uamuzi. Mtu anayengoja-ngoja kufanya uamuzi anaweza kutoa visingizio vya kushangaza vya kutochukua hatua. (Met. 22:13) Lakini hata asipochukua hatua bado anafanya uamuzi, ni kana kwamba anaamua kuacha wengine waongoze maisha yake.
15, 16. Ni nini kinachohusika katika kutekeleza uamuzi?
15 Timiza au tekeleza uamuzi wako. Jitihada zetu katika kufanya uamuzi mzuri zinaweza kuwa za bure ikiwa hatufuatilii uamuzi huo na kuutekeleza kwa bidii. Sulemani aliandika hivi: “Yote ambayo mkono wako unapata kufanya, yafanye kwa nguvu zako zote.” (Mhu. 9:10) Ili ufanikiwe, ni lazima uwe tayari kutafuta vitu unavyohitaji ili kutekeleza maamuzi yako. Kwa mfano, huenda mhubiri wa kutaniko akaamua kufanya upainia. Je, atafanikiwa? Inaelekea kwamba atafanikiwa ikiwa hatatumia nguvu zake zote katika kazi ya kimwili ya ziada na vitumbuizo hivi kwamba akose wakati ambao anahitaji kutimiza huduma yake.
16 Kwa kawaida, si rahisi kutekeleza maamuzi yaliyo bora. Kwa nini? Kwa sababu “ulimwengu mzima unakaa katika nguvu za yule mwovu.” (1 Yoh. 5:19) Ni lazima tushindane mweleka juu ya “watawala wa ulimwengu wa giza hili, juu ya majeshi ya roho waovu katika mahali pa kimbingu.” (Efe. 6:12) Mtume Paulo na pia mwanafunzi Yuda walisema kwamba wale ambao wanaamua kumheshimu Mungu watakuwa na pigano.—1 Tim. 6:12; Yuda 3.
17. Inapohusu maamuzi tunayofanya, Yehova anatazamia nini kutoka kwetu?
17 Chunguza tena uamuzi wako na ufanye marekebisho yanayohitajiwa. Si maamuzi yote yanayofanikiwa kama ilivyopangwa. “Wakati na tukio lisilotazamiwa” linatupata sote. (Mhu. 9:11) Hata hivyo, Yehova anatutazamia tuendelee kuvumilia matokeo ya maamuzi fulani hata tukipatwa na majaribu. Mtu hawezi kubadili uamuzi wake wa kujiweka wakfu kwa Yehova au kufanya nadhiri ya ndoa. Mungu anatutazamia tuishi kulingana na maamuzi kama hayo. (Soma Zaburi 15:1, 2, 4.) Hata hivyo, maamuzi mengi si magumu sana. Mtu mwenye hekima atachunguza mara kwa mara maamuzi ambayo amefanya. Hataacha kiburi au ukaidi umzuie kurekebisha au hata kubadili uamuzi fulani. (Met. 16:18) Hangaiko lake kuu ni kuhakikisha kwamba maisha yake yanaendelea kumletea Mungu heshima.
-
-
Fanya Maamuzi Ambayo Yanamletea Mungu HeshimaMnara wa Mlinzi—2011 | Aprili 15
-
-
[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 16]
Hatua za Kufanya Maamuzi Mazuri
1 Epuka Kimbelembele
2 Fanya Utafiti
3 Sali ili Upate Hekima
4 Fanya Uamuzi
5 Timiza au Tekeleza Uamuzi Huo
6 Chunguza Tena na Ufanye Marekebisho
-