Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Jipeni Moyo Kadiri Ukombozi Ukaribiavyo
    Mnara wa Mlinzi—1997 | Aprili 1
    • Jipeni Moyo Kadiri Ukombozi Ukaribiavyo

      “Nipo pamoja nawe, asema BWANA, ili nikuokoe [“nikukomboe,” “NW”].”—YEREMIA 1:19.

      1, 2. Kwa nini familia ya kibinadamu inahitaji ukombozi?

      UKOMBOZI! Ni neno lenye kufariji kama nini! Kukombolewa kwamaanisha kuokolewa, kuwekwa huru kutokana na hali mbaya isiyofurahisha. Huko hutia ndani wazo la kuletwa kwenye hali nzuri zaidi, na zenye furaha zaidi.

      2 Sasa jamii ya kibinadamu yahitaji ukombozi huo sana kama nini! Watu kila mahali wanalemewa na kuvunjwa moyo na matatizo magumu—ya kiuchumi, ya kijamii, ya kimwili, ya kiakili, na ya kihisia-moyo. Watu walio wengi hawaridhishwi na wametamaushwa na jinsi ulimwengu unavyoelekea nao wangependa hali ibadilike iwe nzuri.—Isaya 60:2; Mathayo 9:36.

      “Nyakati za Hatari Zilizo Ngumu Kushughulika Nazo”

      3, 4. Kwa nini kuna uhitaji mkubwa zaidi wa ukombozi sasa?

      3 Kwa kuwa karne hii ya 20 imekuwa na kuteseka kwingi zaidi ya karne nyingine yoyote, kuna uhitaji mkubwa zaidi wa ukombozi sasa kuliko wakati mwingine wowote. Leo, zaidi ya watu bilioni moja wanaishi katika ufukara, na watu wapatao milioni 25 wanaongezeka kwenye idadi hiyo kila mwaka. Kila mwaka watoto wapatao milioni 13 hufa kutokana na utapiamlo au sababu nyingine zinazohusiana na umaskini—watoto zaidi ya 35,000 kila siku! Na mamilioni ya watu wazima hufa mapema kutokana na magonjwa mbalimbali.—Luka 21:11; Ufunuo 6:8.

      4 Vita na misukosuko ya kiraia yamesababisha kuteseka kwingi sana. Kitabu Death by Government chasema kwamba vita, zogo la kikabila na la kidini, na serikali mbalimbali kuwaua kimakusudi wengi wa raia zazo zenyewe “zimesababisha vifo vya watu zaidi ya milioni 203 katika karne hii.” Chaendelea kusema hivi: “Idadi kamili ya waliokufa ingeweza kuwa karibu watu milioni 360. Ni kana kwamba spishi yetu imeangamizwa kabisa na Tauni Nyeusi. Kwa kweli imeangamizwa kabisa, sio kwa viini bali kwa tauni ya Mamlaka.” Mwandishi Richard Harwood alisema hivi: “Vita vya ujahili vya karne zilizopita kwa ulinganifu vilikuwa vidogo na visivyotokeza kamwe.”—Mathayo 24:6, 7; Ufunuo 6:4.

      5, 6. Ni nini kinachofanya wakati wetu uwe wenye kusononesha sana?

      5 Kwa kuongezea zile hali za kusononesha za miaka ya majuzi ni lile ongezeko kubwa katika uhalifu wenye jeuri, ukosefu wa adili, na kuvunjika kwa familia. William Bennett, aliyekuwa Katibu wa Elimu wa Marekani hapo zamani alisema kwamba katika miaka 30 idadi ya watu wa Marekani iliongezeka kwa asilimia 41, lakini uhalifu wenye jeuri uliongezeka kwa asilimia 560, kuzaliwa kwa watoto haramu kwa asilimia 400, talaka kwa asilimia 300, na kiwango cha kujiua kwa matineja kwa asilimia 200. John DiIulio, Jr., Profesa wa Chuo Kikuu cha Princeton alionya juu ya idadi yenye kuongezeka ya “wanyama-wawindaji walio hodari,” ambao “huua kimakusudi, hushambulia, hubaka, hunyang’anya, huvunja nyumba na kusababisha matatizo mazito ya kijumuiya. Hawahofu fedheha ya kukamatwa, maumivu ya kufungwa, au utungu wa dhamiri.” Katika nchi hiyo, kuua watu wengine sasa ndiko kisababishi kikuu cha pili cha vifo miongoni mwa wenye umri wa kati ya miaka 15 na miaka 19. Na watoto wengi zaidi walio chini ya umri wa miaka minne wanakufa kutokana na kutumiwa vibaya kuliko kutokana na maradhi.

      6 Uhalifu na ujeuri wa aina hiyo haupatikani katika taifa moja tu. Nchi nyingi huripoti maelekeo hayohayo. Lenye kuchangia hayo ni lile ongezeko la matumizi ya dawa za kulevya yanayofisidi mamilioni ya watu. Gazeti la habari la Australia Sydney Morning Herald lilisema hivi: “Ulanguzi wa dawa za kulevya wa kimataifa umekuwa biashara ya pili kwa ukubwa ulimwenguni ikifuata biashara ya silaha.” Jambo lingine ni ujeuri na ukosefu wa adili ambao kwa sasa umejaa katika televisheni. Katika nchi nyingi, kufikia wakati ambapo mtoto hufikia umri wa miaka 18, huwa ameona makumi ya maelfu ya matendo ya ujeuri katika televisheni na matendo yasiyo ya adili yasiyohesabika. Huo ni uvutano mkubwa wenye kufisidi, kwa kuwa utu wetu hufanyizwa kwa yale tunayolisha akili zetu kwa ukawaida.—Waroma 12:2; Waefeso 5:3, 4.

      7. Unabii wa Biblia ulitabirije hali mbaya zilizopo leo?

      7 Unabii wa Biblia ulitabiri kwa usahihi mwelekeo huu mbovu wa matukio katika karne yetu. Ulisema kwamba kungekuwako vita vya tufeni pote, mweneo wa maradhi, upungufu wa chakula, na uasi-sheria wenye kuongezeka. (Mathayo 24:7-12; Luka 21:10, 11) Na tunapofikiria unabii uliorekodiwa kwenye 2 Timotheo 3:1-5, ni sawa na kusikiliza taarifa ya habari ya kila siku. Huo hutambulisha muhula wetu kuwa “siku za mwisho” nao hufafanua watu kuwa ‘wenye kujipenda wenyewe, wapenda-fedha, wasiotii wazazi, wasio waaminifu-washikamanifu, wasio na shauku ya kiasili, wasio na hali ya kujidhibiti, wakali, wenye kututumuka kwa kiburi, wenye kuzipenda raha badala ya kuwa wapenda-Mungu.’ Hivyo ndivyo ulimwengu ulivyo kabisa leo. Kama alivyokiri William Bennett: “Kuna ishara nyingi mno za . . . ustaarabu uliooza.” Hata imesemwa kwamba ustaarabu uliisha wakati wa Vita ya Ulimwengu ya Kwanza.

      8. Kwa nini Mungu alileta lile Furiko katika siku ya Noa, na hilo lahusianaje na siku yetu?

      8 Hali sasa ni mbaya zaidi kuliko ile ya kabla ya Furiko la siku ya Noa, ‘dunia ilipojaa dhuluma.’ Wakati huo, watu kwa ujumla walikataa kutubu njia zao mbaya. Hivyo, Mungu akasema: “Wameijaza dunia dhuluma, basi nitawaharibu pamoja na dunia.” Gharika ilikomesha ulimwengu huo wenye jeuri.—Mwanzo 6:11, 13; 7:17-24.

      Hakuna Wokovu Kupitia Wanadamu

      9, 10. Kwa nini tusiwategemee wanadamu waandae ukombozi?

      9 Je, jitihada za kibinadamu zaweza kutukomboa kutokana na hali hizi mbaya? Neno la Mungu lajibu hivi: “Msiwatumainie wakuu, wala binadamu ambaye hakuna wokovu kwake.” “Kuelekeza hatua zake si katika uwezo wa mwanadamu.” (Zaburi 146:3; Yeremia 10:23) Maelfu ya miaka ya historia yamethibitisha kweli hizo. Wanadamu wamejaribu kila mfumo uwezao kuwaziwa wa kisiasa, wa kiuchumi, na wa kijamii, lakini hali zimekuwa mbaya zaidi. Kungalikuwa na suluhisho la kibinadamu, ingalikuwa wazi kufikia sasa. Badala ya hivyo, uhalisi ni kwamba “mtu mmoja anayo mamlaka juu ya mwenziwe kwa hasara yake.”—Mhubiri 8:9, Union Version chapa ya 1989; Mithali 29:2; Yeremia 17:5, 6.

      10 Miaka michache iliyopita, Zbigniew Brzezinski, aliyekuwa mshauri wa usalama wa kitaifa hapo zamani, alisema hivi: “Mkataa usioepukika wa uchanganuzi wowote usiopendelea upande wowote wa mielekeo ya tufeni pote ni kwamba msukosuko wa kijamii, ghasia za kisiasa, matatizo ya kiuchumi, na ugomvi kati ya mataifa huenda yakasambaa zaidi.” Aliongeza hivi: “Tisho wanaloelekeana nalo wanadamu [ni] mchafuko wa utawala duniani pote.” Makadirio hayo juu ya hali za ulimwengu ni yenye nguvu hata zaidi leo. Ukieleza juu ya muhula huu wa ujeuri ulioongezeka, uhariri katika gazeti Register la New Haven, Connecticut, ulitangaza hivi: “Yaonekana tumeenda sana tusiweze kusimama.” La, kuharibika kwa ulimwengu huu hakutasimama, kwa kuwa unabii juu ya “siku [hizi] za mwisho” ulisema hivi pia: “Watu waovu na walaghai wataendelea kutoka ubaya hadi ubaya zaidi, wakiongoza vibaya na kuwa wenye kuongozwa vibaya.”—2 Timotheo 3:13.

      11. Kwa nini hali zinazozidi kuharibika hazitarekebishwa na jitihada za kibinadamu?

      11 Wanadamu hawawezi kubadili mielekeo hiyo kwa kuwa Shetani ndiye “mungu wa huu mfumo wa mambo.” (2 Wakorintho 4:4) Ndiyo, “ulimwengu mzima unakaa katika nguvu ya mwovu.” (1 Yohana 5:19; ona pia Yohana 14:30.) Kwa hakika Biblia husema hivi juu ya siku yetu: “Ole wa dunia na wa bahari, kwa sababu Ibilisi ameteremka kwenu, akiwa na hasira kubwa, akijua ana kipindi kifupi cha wakati.” (Ufunuo 12:12) Shetani ajua kwamba utawala wake na ulimwengu wake wakaribia kwisha, kwa hiyo yeye ni kama “simba anayenguruma, akitafuta sana kunyafua mtu fulani.”—1 Petro 5:8.

      Ukombozi Wakaribia —Kwa Ajili ya Nani?

      12. Ukombozi wakaribia kwa ajili ya nani?

      12 Hali za dunia zinazozidi kuwa ngumu ni uthibitisho wenye kutokeza kwamba badiliko kubwa—kwelikweli, ukombozi mtukufu—wakaribia! Kwa ajili ya nani? Ukombozi wakaribia kwa ajili ya wale wanaokazia uangalifu zile ishara za kuonya na wanaotenda kupatana nazo. Yohana wa Kwanza 2:17 huonyesha jambo ambalo lazima lifanywe: “Ulimwengu [mfumo wa mambo wa Shetani] unapitilia mbali na ndivyo na tamaa yao, lakini yeye ambaye hufanya mapenzi ya Mungu hudumu milele.”—Ona pia 2 Petro 3:10-13.

      13, 14. Yesu alikaziaje uhitaji wa kukaa macho?

      13 Yesu alitabiri kwamba jamii yenye ufisadi ya leo itafagiliwa mbali karibuni katika wakati wa taabu “namna ambayo haijapata kutukia tangu mwanzo wa ulimwengu hadi sasa, la, wala haitatukia tena.” (Mathayo 24:21) Hiyo ndiyo sababu alionya hivi: “Kazieni uangalifu kwa nyinyi wenyewe kwamba mioyo yenu isiwe kamwe yenye kulemewa na kula kupita kiasi na kunywa sana na mahangaiko ya maisha, na kwa ghafula siku hiyo iwe juu yenu mara hiyo kama mtego. Kwa maana itakuja juu ya wote wale wanaokaa juu ya uso wa dunia yote. Basi, fulizeni kuwa macho wakati wote mkiomba dua ili mpate kufanikiwa kuponyoka mambo yote hayo yaliyokusudiwa kutukia.”—Luka 21:34-36.

      14 Wale ‘wanaokazia uangalifu’ na ‘kufuliza kuwa macho’ watatafuta mapenzi ya Mungu na kuyafanya. (Mithali 2:1-5; Waroma 12:2) Hao ndio ‘watakaofanikiwa kuponyoka’ uharibifu wa mfumo wa Shetani utakaoletwa hivi karibuni. Nao wanaweza kuwa na uhakika kamili kwamba watakombolewa.—Zaburi 34:15; Mithali 10:28-30.

      Mkombozi Mkuu

      15, 16. Mkombozi mkuu ni nani, na kwa nini tuna hakika kwamba hukumu zake zitakuwa adilifu?

      15 Ili watumishi wa Mungu wakombolewe, Shetani na mfumo wake wote wa mambo ahitaji kuondolewa. Hilo lataka chanzo cha ukombozi chenye nguvu zaidi ya wanadamu. Chanzo hicho ni Yehova Mungu, Mwenye Enzi Kuu Mkuu Kuliko Wote, Muumba mweza yote wa ulimwengu wote mzima wenye kutisha. Yeye ndiye Mkombozi mkuu: “Mimi, naam, mimi, ni BWANA, zaidi yangu mimi hapana mwokozi.”—Isaya 43:11; Mithali 18:10.

      16 Katika Yehova hukaa kiasi kikubwa zaidi cha nguvu, hekima, haki, na upendo. (Zaburi 147:5; Mithali 2:6; Isaya 61:8; 1 Yohana 4:8) Kwa hiyo atekelezapo hukumu zake, twaweza kuwa na hakika kwamba matendo yake yatakuwa maadilifu. Abrahamu aliuliza hivi: “Mhukumu ulimwengu wote asitende haki?” (Mwanzo 18:24-33) Paulo alitangaza hivi: “Je, kwa Mungu kuna ukosefu wa haki? Hilo lisipate kuwa hivyo kamwe!” (Waroma 9:14) Yohana aliandika hivi: “Ndiyo, Yehova Mungu, Mweza-Yote, ni ya kweli na ya uadilifu maamuzi yako ya kihukumu.”—Ufunuo 16:7.

      17. Watumishi wa Yehova wa wakati uliopita wameonyeshaje uhakika katika ahadi zake?

      17 Yehova anapoahidi ukombozi, bila shaka atautimiza. Yoshua alisema hivi: “Halikuanguka neno lolote katika jambo lolote lililokuwa ni jema ambalo BWANA alikuwa amelinena.” (Yoshua 21:45) Solomoni alitaarifu hivi: “Halikukosa kupatikana neno lolote katika ahadi yake njema.” (1 Wafalme 8:56) Mtume Paulo alisema kwamba Abrahamu “hakusitasita kwa ukosefu wa imani, . . . akisadikishwa kikamili kwamba alilokuwa ameahidi [Mungu] alikuwa na uwezo pia wa kufanya.” Sara hali kadhalika “alimkadiria [Mungu] kuwa mwaminifu yeye aliyekuwa ameahidi.”—Waroma 4:20, 21; Waebrania 11:11.

      18. Kwa nini watumishi wa Yehova leo wanaweza kuwa na uhakika kwamba watakombolewa?

      18 Tofauti na wanadamu, Yehova ni mwenye kutumainika kabisa, wa kweli katika neno lake. ‘BWANA wa majeshi ameapa, akisema, Hakika yangu kama vile nilivyoazimia, ndivyo itakavyokuwa; na kama nilivyokusudia, ndivyo itakavyotokea.’ (Isaya 14:24) Kwa hiyo Biblia isemapo kwamba “Yehova ajua jinsi ya kukomboa watu wenye ujitoaji-kimungu kutoka katika jaribu, bali kuweka akiba watu wasio waadilifu kwa ajili ya siku ya hukumu ili kukatiliwa mbali,” twaweza kuwa na uhakika kwamba hilo litatukia. (2 Petro 2:9) Hata watishwapo kuharibiwa na adui wenye nguvu, watumishi wa Yehova hujipa moyo kwa sababu ya nia yake, inayoonyeshwa katika ahadi yake kwa mmojawapo wa manabii wake: “Nao watapigana nawe; lakini hawatakushinda; maana nipo pamoja nawe, asema BWANA, ili nikuokoe.”—Yeremia 1:19; Zaburi 33:18, 19; Tito 1:2.

      Ukombozi Mbalimbali Katika Wakati Uliopita

      19. Yehova alimkomboaje Loti, kukiwa na ufanani gani kwa wakati wetu?

      19 Twaweza kutiwa moyo sana kwa kukumbuka baadhi ya matendo ya Yehova ya kuokoa ya wakati uliopita. Mathalani, Loti ‘alitaabishwa sana’ na uovu wa Sodoma na Gomora. Lakini Yehova aliona “kilio” dhidi ya majiji hayo. Kwa wakati ufaao, alituma wajumbe wasihi Loti na familia yake waondoke eneo hilo mara moja. Tokeo likawa nini? Yehova “alimkomboa Loti mwadilifu,” na “kugeuza majiji ya Sodoma na Gomora kuwa majivu.” (2 Petro 2:6-8; Mwanzo 18:20, 21) Leo pia, Yehova huona kilio kwa habari ya uovu mzito wa ulimwengu huu. Wajumbe wake wa siku ya kisasa watakapokuwa wamemaliza kazi yao muhimu ya kuhubiri kufikia kiwango anachotaka, atatenda dhidi ya ulimwengu huu na kuwakomboa watumishi wake kama alivyomkomboa Loti.—Mathayo 24:14.

      20. Fafanua ukombozi wa Yehova wa Israeli la kale kutoka Misri.

      20 Katika Misri ya kale mamilioni ya watu wa Mungu walifanywa watumwa. Yehova alisema hivi juu yao: “Nimesikia kilio chao . . . nayajua maumivu yao; nami nimeshuka ili niwaokoe.” (Kutoka 3:7, 8) Hata hivyo, baada ya kuwaacha watu wa Mungu waende, Farao alibadili akili yake, akawafuatia akiwa na jeshi lake lenye uweza. Waisraeli walionekana wamenaswa kwenye Bahari Nyekundu. Hata hivyo Musa alisema hivi: “Msiogope, simameni tu, mkauone wokovu wa BWANA atakaowafanyia leo.” (Kutoka 14:8-14) Yehova alitenganisha Bahari Nyekundu, na Waisraeli wakaponyoka. Majeshi ya Farao yakawafuatia mbio, lakini Yehova alitumia nguvu zake hivi kwamba “bahari ikawafunikiza; wakazama kama risasi ndani ya maji makuu.” Baadaye Musa alichachawa katika kumwimbia Yehova hivi: “Ni nani aliye kama wewe, mtukufu katika utakatifu, mwenye kuogopwa katika sifa zako, mfanya maajabu?”—Kutoka 15:4-12, 19.

      21. Watu wa Yehova waliokolewaje kutoka Amoni, Moabu, na Seiri?

      21 Kwenye pindi nyingine, mataifa adui ya Amoni, Moabu, na Seiri (Edomu) yalitisha kuwaharibu watu wa Yehova. Yehova alisema hivi: “Msiogope, wala msifadhaike kwa ajili ya jeshi kubwa hili; kwani vita si yenu bali ni ya Mungu. . . . Hamtahitaji kupigana vita . . . simameni mkauone wokovu wa BWANA ulio pamoja nanyi.” Yehova aliwakomboa watu wake kwa kuwavuruga wale adui wengi hivi kwamba walichinjana.—2 Mambo ya Nyakati 20:15-23.

      22. Ni ukombozi gani wa kimuujiza kutoka Ashuru alioandaa Yehova kwa ajili ya Israeli?

      22 Serikali ya Ulimwengu ya Ashuru ilipokuja dhidi ya Yerusalemu, Mfalme Senakeribu alimdhihaki vikali Yehova kwa kuwaambia watu waliokuwa ukutani hivi: “Katika miungu yote ya nchi hizi [nilioshinda] waliookoa nchi yao na mkono wangu hata BWANA auokoe Yerusalemu na mkono wangu?” Kwa watumishi wa Mungu alisema hivi: “Wala msimwache Hezekia kuwatia moyo wa kumtumaini BWANA; akisema, BWANA bila shaka atatuokoa.” Kisha Hezekia akasali kwa bidii kwa ajili ya ukombozi, “falme zote za dunia zipate kujua kwamba wewe ndiwe BWANA, wewe peke yako.” Yehova aliwaangamiza askari-jeshi 185,000 wa Ashuru, na watumishi wa Mungu wakakombolewa. Baadaye, Senakeribu alipokuwa akiabudu mungu asiye wa kweli, wana wake walimuua.—Isaya, sura ya 36 na ya 37.

      23. Ni maswali yapi juu ya ukombozi leo yanayohitaji kujibiwa?

      23 Kwa kweli twaweza kujipa moyo tuonapo jinsi Yehova alivyowakomboa kiajabu watu wake katika nyakati zilizopita. Namna gani leo? Hivi karibuni watumishi wake waaminifu wataingia katika hali gani hatari ambayo itataka ukombozi wake wa kimuujiza? Kwa nini amengoja hadi sasa kabla ya kuleta ukombozi wao? Kutakuwa na utimizo gani wa maneno haya ya Yesu: “Mambo haya yaanzapo kutukia, jisimamisheni wenyewe wima na kuinua vichwa vyenu juu, kwa sababu ukombozi wenu unakaribia”? (Luka 21:28) Na ukombozi wa watumishi wa Mungu ambao tayari wamekufa utakujaje? Makala ifuatayo itachunguza maswali hayo.

  • Ukombozi Kuingia Katika Ulimwengu Mpya Mwadilifu
    Mnara wa Mlinzi—1997 | Aprili 1
    • Ukombozi Kuingia Katika Ulimwengu Mpya Mwadilifu

      “Watajifurahisha kwa wingi wa amani.”—ZABURI 37:11.

      1, 2. (a) Ukombozi wa Yehova katika wakati wetu utatofautianaje na ukombozi mbalimbali wa nyakati za kale? (b) Yehova atawaingiza watu wake katika ulimwengu wa aina gani?

      YEHOVA ni Mungu wa ukombozi. Nyakati za kale, aliwakomboa watu wake katika pindi nyingi. Ukombozi huo mbalimbali ulikuwa wa kipindi fulani, kwa kuwa Yehova hakutekeleza hukumu yake yenye kudumu dhidi ya ulimwengu mzima wa Shetani katika vyovyote vya visa hivyo. Lakini katika siku yetu, Yehova karibuni atatekeleza ukombozi ulio mtukufu kuliko ukombozi mwingineo wote kwa niaba ya watumishi wake wote. Wakati huo ataharibu kila ishara ya mfumo wa Shetani ulimwenguni pote, naye ataingiza watumishi wake katika ulimwengu mpya wenye kudumu, ulio mwadilifu.—2 Petro 2:9; 3:10-13.

      2 Yehova anaahidi hivi: “Bado kitambo kidogo asiye haki hatakuwapo, . . . Bali wenye upole watairithi nchi, watajifurahisha kwa wingi wa amani.” (Zaburi 37:10, 11) Kwa muda gani? “Wenye haki watairithi nchi, nao watakaa humo milele.” (Zaburi 37:29; Mathayo 5:5) Hata hivyo, kabla ya hayo kutukia, ulimwengu huu utapatwa na wakati wa taabu kubwa kupita zote ambazo umepata kujua.

      “Dhiki Kubwa”

      3. Yesu alifafanuaje “dhiki kubwa”?

      3 Katika 1914 ulimwengu huu uliingia “siku [zayo] za mwisho.” (2 Timotheo 3:1-5, 13) Sasa tumeingia miaka 83 ndani ya kipindi hicho na twakaribia mwisho wacho wakati ambapo, kama alivyotabiri Yesu, jambo lifuatalo litatukia: “Kutakuwa na dhiki kubwa ya namna ambayo haijapata kutukia tangu mwanzo wa ulimwengu hadi sasa, la, wala haitatukia tena.” (Mathayo 24:21) Ndiyo, mbaya hata zaidi ya Vita ya Ulimwengu 2, watu wapatao milioni 50 walipouawa. Ni kipindi chenye kutikisa ulimwengu kama nini kinachokaribia mbiombio!

      4. Kwa nini hukumu ya Mungu yamjia “Babiloni Mkubwa”?

      4 “Dhiki kubwa” itakuja kwa ghafula yenye kushangaza, “katika saa moja.” (Ufunuo 18:10) Kuzuka kwayo kutatiwa alama na kutekeleza hukumu kwa Mungu dhidi ya dini zote zisizo za kweli, ambazo Neno la Mungu huziita “Babiloni Mkubwa.” (Ufunuo 17:1-6, 15) Jambo kuu katika Babiloni la kale lilikuwa dini isiyo ya kweli. Babiloni la kisasa lafanana na jenzile la kale nalo lawakilisha milki ya ulimwengu ya dini isiyo ya kweli. Limefanya ukahaba kwa kuridhiana na matengenezo ya kisiasa. Limetegemeza vita vyayo na kubariki majeshi kwenye pande zenye kupingana, kukitokeza kuchinjana kwa watu wa dini ileile. (Mathayo 26:51, 52; 1 Yohana 4:20, 21) Limepuuza mazoea yenye ufisadi ya waumini wake na kuwanyanyasa Wakristo wa kweli.—Ufunuo 18:5, 24.

      5. “Dhiki kubwa” yaanzaje?

      5 “Dhiki kubwa” huanza matengenezo ya kisiasa yamshambuliapo ghafula “Babiloni Mkubwa.” Wao “watamchukia kahaba na watamfanya ukiwa na kuwa uchi, na watakula kabisa sehemu zake zenye nyama na watamchoma kabisa kwa moto.” (Ufunuo 17:16) Baada ya hapo, waliokuwa wategemezaji wake hapo zamani “watatoa machozi na kujipiga wenyewe kwa kihoro juu yake.” (Ufunuo 18:9-19) Lakini watumishi wa Yehova wametarajia hilo kwa muda mrefu, nao watapaaza sauti hivi: “Sifuni Yah, . . . kwa maana ametekeleza hukumu juu ya kahaba mkubwa aliyeifisidi dunia kwa uasherati wake, na amelipizia kisasi damu ya watumwa wake mkononi mwake.”—Ufunuo 19:1, 2.

      Watumishi wa Mungu Washambuliwa

      6, 7. Kwa nini watumishi wa Yehova wanaweza kuwa na uhakika washambuliwapo wakati wa “dhiki kubwa”?

      6 Baada ya kuharibu dini isiyo ya kweli, matengenezo ya kisiasa yatageukia watumishi wa Yehova. Shetani, “Gogu, wa nchi ya Magogu” katika unabii, asema hivi: “Nitawaendea watu wanaostarehe, wanaokaa salama.” Akidhani ya kuwa wao ni mawindo rahisi, awashambulia kwa “jeshi kuu . . . , kama wingu kuifunika nchi.” (Ezekieli 38:2, 10-16) Watu wa Yehova wanajua kwamba shambulio hilo halitafua dafu kwa sababu wanamtumaini Yehova.

      7 Farao na majeshi yake walipohisi kwamba walikuwa wamewanasa watumishi wa Mungu kwenye Bahari Nyekundu, Yehova aliwakomboa watu wake kimuujiza na kuyaharibu majeshi ya Misri. (Kutoka 14:26-28) Wakati wa “dhiki kubwa,” mataifa yanapohisi kwamba yamewanasa watu wa Yehova, kwa mara nyingine tena awaokoa kimuujiza: “Katika siku hiyo . . . ghadhabu yangu itapanda katika mianzi ya pua yangu. Kwa maana katika wivu wangu na katika moto wa ghadhabu yangu nimenena.” (Ezekieli 38:18, 19) Ndipo upeo wa “dhiki kubwa” utakapokaribia!

      8. Ni matukio gani yasiyo ya kawaida yanayotukia kabla ya Yehova kufisha waovu, na kukiwa na tokeo jipi?

      8 Kufikia hatua fulani baada ya “dhiki kubwa” kuanza, lakini kabla ya Yehova kutekeleza hukumu yake dhidi ya ulimwengu uliosalia, matukio yasiyo ya kawaida yatatukia. Ona matokeo yatakayokuwa nayo. “Ndipo ishara ya Mwana wa binadamu [Kristo] itakapoonekana mbinguni, na ndipo makabila yote ya dunia yatakapojipiga yenyewe kwa maombolezo, nayo yatamwona Mwana wa binadamu akija juu ya mawingu ya mbinguni na nguvu na utukufu mkubwa.” (Mathayo 24:29, 30) “Kutakuwa na ishara katika jua na mwezi na nyota, . . . huku watu wakizimia moyo kutokana na hofu na tarajio la mambo yanayokuja juu ya dunia inayokaliwa.”—Luka 21:25, 26.

      “Ukombozi Wenu Unakaribia”

      9. Kwa nini watumishi wa Yehova wanaweza ‘kuinua vichwa vyao’ matukio yasiyo ya kawaida yatukiapo?

      9 Wakati huo mahususi, unabii wa Luka 21:28 wapata utimizo. Yesu alisema hivi: “Mambo haya yaanzapo kutukia, jisimamisheni wenyewe wima na kuinua vichwa vyenu juu, kwa sababu ukombozi wenu unakaribia.” Adui wa Mungu watakuwa wakitetemeka kwa hofu kwa sababu watajua kwamba matukio yasiyo ya kawaida yanayotukia yatoka kwa Yehova. Lakini watumishi wa Yehova watashangilia kwa kuwa watajua kwamba ukombozi wao unakaribia.

      10. Neno la Mungu hufafanuaje upeo wa “dhiki kubwa”?

      10 Kisha Yehova atokeza pigo la kifo dhidi ya mfumo wa Shetani: “Nami nitamhukumu [Gogu] kwa tauni, na kwa damu; nami nitanyesha mvua ifurikayo, na mvua ya mawe makubwa sana, na moto na kiberiti juu yake, na vikosi vyake . . . Nao watajua ya kuwa mimi ndimi BWANA.” (Ezekieli 38:22, 23) Masalio yote ya mfumo wa Shetani yanaharibiwa. Jamii yote ya kibinadamu ya watu wenye kumpuuza Mungu inaangamizwa. Huo ndio upeo wa “dhiki kubwa,” Har–Magedoni.—Yeremia 25:31-33; 2 Wathesalonike 1:6-8; Ufunuo 16:14, 16; 19:11-21.

      11. Kwa nini watumishi wa Yehova wanakombolewa kutoka “dhiki kubwa”?

      11 Mamilioni ya waabudu wa Yehova duniani pote watakombolewa kutoka “dhiki kubwa.” Hao hufanyiza “umati mkubwa” ambao umekuja “kutoka katika mataifa yote na makabila na vikundi vya watu na lugha.” Kwa nini wanakombolewa katika njia yenye kutia kicho hivyo? Kwa sababu humtolea Yehova “utumishi mtakatifu mchana na usiku.” Kwa hiyo wanaokoka mwisho wa ulimwengu huu nao wanaingizwa katika ulimwengu mpya mwadilifu. (Ufunuo 7:9-15) Hivyo, washuhudia utimizo wa ahadi hii ya Yehova: “Umngoje BWANA, uishike njia yake, naye atakutukuza uirithi nchi, wasio haki watakapoharibiwa utawaona.”—Zaburi 37:34.

      Ulimwengu Mpya

      12. Waokokaji wa Har–Magedoni waweza kutazamia nini?

      12 Huo utakuwa wakati wenye kusisimua kama nini—kuondolewa kwa uovu na mwanzo wa muhula mtukufu zaidi katika historia yote ya kibinadamu! (Ufunuo 20:1-4) Waokokaji wa Har–Magedoni watakuwa wenye shukrani kama nini kwa Yehova kwa sababu ya kuingia ustaarabu mwangavu, safi uliofanywa na Mungu, ulimwengu mpya, juu ya dunia itakayogeuzwa iwe paradiso! (Luka 23:43) Nao hawatahitaji kufa tena kamwe! (Yohana 11:26) Kwelikweli, kuanzia hapo na kuendelea, watakuwa na tazamio lenye kushangaza, la ajabu la kuishi kwa kadiri ambavyo Yehova huishi!

      13. Yesu airudiaje kazi ya kuponya aliyoanza alipokuwa duniani?

      13 Yesu, ambaye Yehova amemweka rasmi kuwa Mfalme wa kimbingu, atatolea uangalifu baraka za kimuujiza ambazo waliokombolewa watafurahia. Alipokuwa duniani, alifumbua macho ya vipofu na masikio ya viziwi na kuponya “kila namna ya maradhi na kila namna ya udhaifu.” (Mathayo 9:35; 15:30, 31) Katika ulimwengu mpya, atarudia kazi hiyo kubwa ya kuponya lakini tufeni pote. Akiwa Mwakilishi wa Mungu, atatimiza ahadi hii: “[Mungu] atafuta kabisa kila chozi kutoka katika macho yao, na kifo hakitakuwapo tena, wala ombolezo wala kupaaza kilio wala umivu halitakuwapo tena kamwe. Mambo ya zamani yamepitilia mbali.” (Ufunuo 21:4) Hakutakuwa tena na uhitaji wa madaktari au wazishi!—Isaya 25:8; 33:24.

      14. Ni ukombozi gani utakaowajia watumishi wa Yehova ambao tayari wamekufa?

      14 Watakaokombolewa pia ni watumishi wote waaminifu wa Mungu waliokufa wakati uliopita. Katika ulimwengu mpya, wataokolewa kutoka kwa mafumbato ya kaburi. Yehova ahakikisha hivi: “Kutakuwa na ufufuo wa waadilifu na wasio waadilifu pia.” (Matendo 24:15) Yamkini, “waadilifu” watafufuliwa mapema na wachangie kuenea kwa Paradiso. Itapendeza kama nini kwa waokokaji wa Har–Magedoni kusikia mambo yaliyoonwa ya wale wafu waaminifu wa zamani za kale, waliotoka kurudishwa kwenye uhai!—Yohana 5:28, 29.

      15. Fafanua baadhi ya hali zitakazokuwako katika ulimwengu mpya.

      15 Kisha wote hao wanaoishi watajionea yale aliyosema mtunga-zaburi juu ya Yehova: “Waufumbua mkono wako, wakishibisha kila kilicho hai matakwa yake.” (Zaburi 145:16) Hakuna njaa tena: Dunia itarudishwa kwenye usawaziko wa kiekolojia na izae kwa wingi. (Zaburi 72:16) Hakuna watu wasio na makao tena: “Watajenga nyumba, na kukaa ndani yake,” kila mmoja ataketi “chini ya mzabibu wake, na chini ya mtini wake; wala hapana mtu atakayewatia hofu.” (Isaya 65:21, 22; Mika 4:4) Hakuna hofu tena: Hakutakuwa na vita, jeuri, au uhalifu. (Zaburi 46:8, 9; Mithali 2:22) “Dunia yote inastarehe na kutulia; hata huanzilisha kuimba.”—Isaya 14:7.

      16. Kwa nini uadilifu utapenya katika ulimwengu mpya?

      16 Katika ulimwengu mpya, propaganda ya Shetani itakuwa imeondolewa. Badala yayo, ‘watu wakaao duniani watajifunza haki.’ (Isaya 26:9; 54:13) Kukiwa na maagizo yenye kufaa ya kiroho mwaka baada ya mwaka, “dunia itajawa na kumjua BWANA, kama vile maji yanavyoifunika bahari.” (Isaya 11:9) Mawazo na matendo yenye kujenga yatawapenya wanadamu. (Wafilipi 4:8) Wazia, jamii ya ulimwenguni pote ya watu walio huru kutokana na uhalifu, kujipenda, wivu—udugu wa kimataifa ambao katika huo matunda ya roho ya Mungu yatatokezwa na wote. Kwelikweli, hata sasa sifa kama hizo zinakuzwa na umati mkubwa.—Wagalatia 5:22, 23.

      Mbona Muda Mrefu Hivyo?

      17. Kwa nini Yehova amengoja muda mrefu hivyo kabla ya kukomesha uovu?

      17 Hata hivyo, kwa nini Yehova amengoja kwa muda mrefu hivyo kabla ya kuondoa uovu na kuwakomboa watu wake waingie ndani ya ulimwengu mpya? Fikiria yale yaliyohitaji kutimizwa. La maana zaidi ni kutetewa kwa enzi kuu ya Yehova, haki yake ya kutawala. Kwa kuruhusu wakati wa kutosha upite, ameonyesha pasipo shaka lolote kwamba utawala wa kibinadamu nje ya enzi kuu yake umeshindwa vibaya sana. (Yeremia 10:23) Kwa hiyo sasa Yehova ana haki kabisa ya kuuondoa utawala wa kibinadamu na kuweka utawala wa Ufalme wake wa kimbingu chini ya Kristo mahali pao.—Danieli 2:44; Mathayo 6:9, 10.

      18. Wazao wa Abrahamu wangerithi nchi ya Kanaani lini?

      18 Yale yote ambayo yametukia katika karne hizi yafanana na yale yaliyotukia wakati wa Abrahamu. Yehova alimwambia Abrahamu kwamba wazao wake wangerithi nchi ya Kanaani—lakini walilazimika kungoja miaka mia nne ‘maana haukuwa umetimia uovu wa Waamori.’ (Mwanzo 12:1-5; 15:13-16) Neno “Waamori” (kabila kubwa) yamkini lawakilisha watu wa Kanaani kwa ujumla. Kwa hiyo karne nne zingepita kabla ya Yehova kuwawezesha watu wake kutwaa Kanaani. Katika wakati huo Yehova aliyaacha mataifa katika Kanaani yakuze jamii zayo. Kukiwa na tokeo jipi?

      19, 20. Ni jamii za aina gani walizotokeza Wakanaani?

      19 Kitabu Bible Handbook, cha Henry H. Halley, chasema kwamba katika Megido, waakiolojia walipata magofu ya hekalu la Ashtorethi, mungu wa kike aliye mke wa Baali. Yeye aandika hivi: “Hatua chache tu kutoka hekalu hilo kulikuwa na makaburi, ambapo magudulia mengi yalipatikana, yakiwa na mabaki ya vitoto vichanga vilivyokuwa vimetolewa dhabihu katika hekalu hilo . . . Manabii wa Baali na Ashtorethi walikuwa wauaji kimakusudi rasmi wa watoto wadogo.” “Zoea lingine lenye kutisha lilikuwa [lile] lililoitwa ‘dhabihu za msingi.’ Nyumba ilipojengwa, mtoto angetolewa akiwa dhabihu, na mwili wake ujengewe ndani ya ukuta.”

      20 Halley aeleza hivi: “Ibada ya Baali, Ashtorethi, na miungu ya Kanaani ilikuwa na sherehe zilizopotoka zaidi; mahekalu yao yalikuwa vitovu vya uovu. . . . Wakanaani waliabudu, kwa kujitia sana katika ukosefu wa adili, . . . na kisha, kwa kuua kimakusudi watoto wao wazaliwa wa kwanza, wakiwatoa wawe dhabihu kwa miungu hiyohiyo. Yaonekana kwamba, kwa kadiri kubwa, nchi ya Kanaani ilikuwa imekuwa namna ya Sodoma na Gomora kwa kadiri ya taifa zima. . . . Je, ustaarabu mchafu wenye kuchukiza na wa kinyama hivyo ulikuwa na haki ya kuendelea kuwapo? . . . Waakiolojia ambao huchimbua kwenye magofu ya majiji ya Kikanaani hujiuliza ni kwa nini Mungu hakuwaangamiza mapema zaidi ya wakati Alipofanya hivyo.”—Linganisha 1 Wafalme 21:25, 26.

      21. Ni ufanani gani uliopo kati ya hali ya Wakanaani na ile ya siku yetu?

      21 Uovu wa Waamori ulikuwa ‘umetimia.’ Kwa hiyo wakati huo Yehova alikuwa na haki kabisa ya kuwaharibu kabisa. Hivyo ndivyo ilivyo leo. Ulimwengu huu umejaa jeuri, ukosefu wa adili, na kutoheshimu sheria za Mungu. Na kwa kuwa twashangazwa ifaavyo na watoto waliotolewa wakiwa dhabihu zenye kuchukiza katika Kanaani la kale, namna gani zile dhabihu za mamilioni ya vijana katika vita vya ulimwengu huu, vilivyo vibaya hata zaidi kuliko chochote katika Kanaani? Bila shaka, kwa sasa Yehova ana haki kabisa ya kuukomesha mfumo huu.

      Kutimiza Jambo Lingine

      22. Ni nini kinachotimizwa na subira ya Yehova katika wakati wetu?

      22 Subira ya Yehova katika siku hizi za mwisho yatimiza jambo lingine. Anaruhusu wakati wa kukusanya na kuelimisha umati mkubwa, ambao tayari unajumuika kuwa zaidi ya milioni tano. Chini ya mwelekezo wa Yehova, wamefanywa kuwa tengenezo lenye kusonga mbele. Wanaume, wanawake, na vijana wanazoezwa kuwafundisha wengine kweli za Biblia. Kupitia mikutano yao na vichapo vya Biblia, wanajifunza njia za upendo za Mungu. (Yohana 13:34, 35; Wakolosai 3:14; Waebrania 10:24, 25) Kwa kuongezea, wanakuza stadi katika ujenzi, elektroni, uchapaji, na nyanja nyinginezo ili kutegemeza kazi ya kuhubiri “habari njema.” (Mathayo 24:14) Yamkini ufundishaji huo na stadi za kujenga zitatumika sana kwenye ulimwengu mpya.

      23. Kwa nini ni pendeleo kuwa hai wakati huu?

      23 Ndiyo, leo Yehova anawatayarisha watumishi wake kupita “dhiki kubwa” na kuingia ulimwengu mpya mwadilifu. Wakati huo hakutakuwa na Shetani na ulimwengu wake mwovu wa kushindana naye, hakuna ugonjwa, majonzi, na kifo. Kwa idili na shangwe kubwa, watu wa Mungu wataendelea na kazi yenye furaha ya kufanya paradiso, ambamo kila siku itakuwa “wingi wa amani.” Tu wenye pendeleo kama nini kuishi katika upeo huu wa hizi enzi, kumjua na kumtumikia Yehova, na kutambua kwamba upesi sana ‘tutainua vichwa vyetu kwa sababu ukombozi wetu unakaribia’!—Luka 21:28; Zaburi 146:5.

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki