-
Kulea Watoto Wachanga Hadi WanapobaleheAmkeni!—2011 | Oktoba
-
-
“Usimnyime Nidhamu”
Watoto wako wanapozidi kukua, ni muhimu wajifunze kwamba mambo wanayofanya yana madhara. Hata wanapokuwa wachanga, lazima watoto wajitiishe chini ya mamlaka, si nyumbani tu bali pia shuleni na katika jamii. Unaweza kuwasaidia watoto wako kujifunza kanuni inayosema kwamba utavuna unachopanda. (Wagalatia 6:7) Jinsi gani?
Biblia inasema: “Usimnyime . . . nidhamu.” (Methali 23:13) Ikiwa umesema wazi kwamba utamwadhibu mtoto kwa sababu ya tendo fulani baya, usiogope kufanya kama ulivyosema na kumtia nidhamu. “Ni muhimu kutobadili-badili msimamo,” anasema Norma, mama mmoja nchini Argentina. “Kubadili-badili msimamo humtia moyo mtoto kufanya anavyotaka.”
Wazazi wanaweza kuepuka ubishi mwingi baada ya mtoto kufanya jambo baya kwa kuhakikisha kwamba mtoto anaelewa mapema matokeo ya kutotii. Watoto watakubali nidhamu kwa urahisi iwapo wanajua sheria na wanajua kitakachotukia wakivunja sheria hizo na ikiwa wana sababu ya kuamini kwamba adhabu haiwezi kubadilishwa.
Bila shaka, ili nidhamu iwe na matokeo, inapaswa kutolewa bila hasira. Biblia inasema: “Uchungu wote wenye uovu na hasira na ghadhabu na kupiga kelele na matukano na viondolewe mbali kutoka kwenu.” (Waefeso 4:31) Nidhamu haipaswi kutolewa kwa ukatili na haipaswi kuwa yenye kudhuru—kimwili au kihisia.
Lakini unaweza kuzuia hasira yako jinsi gani mtoto wako anapokukasirisha kabisa? “Si rahisi kufanya hivyo nyakati zote,” anasema Peter, baba mmoja nchini New Zealand, “lakini watoto wanahitaji kujifunza kwamba nidhamu hutolewa kwa sababu ya tendo walilofanya na si kwa sababu mzazi ameshindwa kujizuia.”
Peter na mke wake hujaribu kuwasaidia watoto wao waone faida ya muda mrefu ya nidhamu wanayopewa. “Hata watoto wanapofanya jambo lenye kuchukiza sana,” anasema, “sisi hujaribu kuwaonyesha tungependa wawe watu wa aina gani badala ya kukazia kosa walilofanya.”
“Usawaziko Wenu na Ujulikane”
Mungu alisema hivi kuhusu nidhamu ambayo angewapa watu wake: “Nitakutia adabu kwa kiwango kinachofaa.” (Yeremia 46:28) Utafanikiwa zaidi ukitoa nidhamu kwa haki na inayolingana na makosa yaliyofanywa. Paulo aliwaandikia Wakristo hivi: “Usawaziko wenu na ujulikane.”—Wafilipi 4:5.
Sehemu moja ya kuwa na usawaziko ni kutoa nidhamu kwa njia ambayo haitawavunjia watoto wako heshima. Santi, baba mmoja nchini Italia, anasema: “Sijawahi kumshushia heshima mwanangu au binti yangu. Badala yake mimi hujaribu kutambua sababu iliyomfanya atende jambo fulani na kushughulikia jambo hilo. Ikiwezekana, siwatii nidhamu watoto wangu mbele ya watu wengine, au hata mbele ya wenzao. Nami sifanyi ucheshi kuhusu udhaifu wao iwe ni mbele ya watu au faraghani.”
Richard, aliyenukuliwa awali, anatambua hekima ya kuwa na usawaziko. “Hupaswi kukusanya makosa kadhaa kisha kutoa nidhamu kwa makosa hayo yote mara moja,” anasema. “Baada ya kutoa nidhamu, ni muhimu kwamba usiendelee kuzungumza kuhusu jambo hilo na kumkumbusha mtoto kuhusu makosa yake.”
-
-
Maoni ya WazaziAmkeni!—2011 | Oktoba
-
-
NIDHAMU
“Tumegundua kwamba kuna njia nyingi zinazofaa za kutoa nidhamu; inategemea hali. Nyakati nyingine, nidhamu inaweza kutia ndani kuzungumzia mambo kwa uzito na mtoto, na wakati mwingine huenda ukahitaji kumzuia asifanye mambo fulani anayopenda.”—Ogbiti, Nigeria.
“Sisi huwaomba watoto wetu warudie maagizo tuliyowapa ili kuhakikisha wameyaelewa vizuri. Halafu tunahakikisha kwamba tumefanya kama tulivyosema. Ikiwa tunataka watoto wetu watii maagizo tunayowapa, ni lazima tuhakikishe kwamba tunatoa nidhamu tuliyosema tutawapa wanapokosa kutii.”—Clive, Australia.
“Mimi huinama ninapowarekebisha watoto wangu ili niwe sawa na kimo chao, na mbinu hiyo ina mafanikio. Kufanya hivyo kunawafanya wanisikilize kwa makini kabisa. Pia kunawasaidia waone ishara zangu za uso zinazokazia maneno ninayowaambia.”—Jennifer, Australia.
“Sisi huepuka kuwaambia watoto wetu, ‘Hakuna wakati wewe unatusikiliza,’ hata kama huo ndio ukweli wa mambo. Pia, hatukemei mtoto mbele ya wenzake. Tunawanong’onezea au tunawapeleka kando na kuongea nao wakiwa peke yao.”—Rudi, Msumbiji.
“Ni rahisi kuwaongoza watoto, na wanapenda kuwaiga wengine. Kwa sababu hiyo, ni lazima tuwalinde wasiathiriwe na watoto wenzao shuleni, vyombo vya habari, na watu wengine katika jamii na tuwasaidie wakuze tabia nzuri zinazotegemea kanuni zinazofaa. Kanuni bora za mwenendo huwasaidia wakatae kitu chochote chenye madhara.”—Grégoire, Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo.
“Ni lazima nidhamu itolewe kwa uthabiti, kwa haki, na bila kubadilika-badilika. Ni lazima watoto waelewe matokeo mabaya ya kuvunja sheria na wajue kwamba unamaanisha kile unachosema.”—Owen, Uingereza.
-