Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Mkumbuke Muumba Wako Mtukufu!
    Mnara wa Mlinzi—1999 | Novemba 15
    • Mkumbuke Muumba Wako Mtukufu!

      “Mkumbuke Muumba wako . . . kabla hazijaja siku zilizo mbaya.”—MHUBIRI 12:1.

      1. Inafaa vijana ambao wamejiweka wakfu kwa Mungu watumieje ujana wao na nguvu zao?

      YEHOVA huwapa watumishi wake nguvu za kufanya mapenzi yake. (Isaya 40:28-31) Yeye huwapa nguvu bila kubagua umri wao. Lakini ingefaa sana vijana ambao wamejiweka wakfu kwa Mungu watumie ujana wao na nguvu zao kwa hekima. Kwa kufanya hivyo, wao wazingatia shauri la “mhubiri,” Mfalme Solomoni wa Israeli la kale. Yeye alihimiza hivi: “Mkumbuke Muumba wako siku za ujana wako, kabla hazijaja siku zilizo mbaya, wala haijakaribia miaka utakaposema, Mimi sina furaha katika hiyo.”—Mhubiri 1:1; 12:1.

      2. Watoto wa Wakristo waliojiweka wakfu wapaswa kufanya nini?

      2 Kwanza Solomoni aliwapa vijana wa Israeli shauri hili la kumkumbuka Muumba Mtukufu siku za ujana. Wao walizaliwa katika taifa lililokuwa limejiweka wakfu kwa Yehova. Namna gani watoto wa Wakristo waliojiweka wakfu wakati wetu? Kwa kweli, wao wapaswa kumkumbuka Muumba wao Mtukufu. Wakifanya hivyo, watamheshimu na kujinufaisha.—Isaya 48:17, 18.

      Vielelezo Vyema vya Wakati Uliopita

      3. Yosefu, Samweli, na Daudi waliweka vielelezo gani?

      3 Vijana wengi wanaotajwa katika Biblia waliweka vielelezo vyema kwa kumkumbuka Muumba wao Mtukufu. Tangu utotoni, Yosefu, mwana wa Yakobo, alimkumbuka Muumba wake. Mke wa Potifa alipojaribu kumshawishi Yosefu afanye ngono naye, Yosefu alikataa katakata akisema: “Nifanyeje ubaya huu mkubwa nikamkose Mungu?” (Mwanzo 39:9) Samweli aliyekuwa Mlawi alimkumbuka Muumba wake utotoni na hata muda wote wa maisha yake. (1 Samweli 1:22-28; 2:18; 3:1-5) Kwa hakika kijana Daudi wa Bethlehemu alimkumbuka Muumba wake. Tumaini lake kwa Mungu lilidhihirika alipokabili lile jitu Goliathi Mfilisti na kutangaza: “Wewe unanijia mimi na upanga, na fumo, na mkuki, bali mimi ninakujia wewe kwa jina la BWANA wa majeshi, Mungu wa majeshi ya Israeli uliowatukana. Siku hii ya leo BWANA atakuua mkononi mwangu, nami nitakupiga, na kukuondolea kichwa chako, . . . dunia nzima wajue ya kuwa yuko Mungu katika Israeli. Nao jamii ya watu wote pia wajue ya kwamba BWANA haokoi kwa upanga wala kwa mkuki; maana vita ni vya BWANA, naye atawatia ninyi mikononi mwetu.” Punde si punde Goliathi alikuwa amekufa, Wafilisti nao wakatoroka.—1 Samweli 17:45-51.

      4. (a) Ni nini kinachoonyesha kwamba msichana Mwisraeli aliyekuwa mateka katika Siria, na vilevile Mfalme Yosia aliyekuwa kijana, walimkumbuka Muumba wetu Mtukufu? (b) Alipokuwa na umri wa miaka 12, Yesu alionyeshaje kwamba alimkumbuka Muumba wake?

      4 Kijana mwingine aliyemkumbuka Muumba Mtukufu ni msichana Mwisraeli aliyekuwa mateka. Alimtolea ushahidi mzuri sana mke wa Naamani, mkuu wa jeshi la Siria, hivi kwamba mkuu huyo alimwendea nabii wa Mungu, akaponywa ugonjwa wa ukoma, akawa mwabudu wa Yehova. (2 Wafalme 5:1-19) Mfalme Yosia aliyekuwa kijana aliendeleza kwa ujasiri ibada safi ya Yehova. (2 Wafalme 22:1–23:25) Lakini Yesu wa Nazareti ndiye kielelezo chema kabisa cha mtu ambaye alimkumbuka Muumba wake Mtukufu akiwa angali mchanga. Fikiria mambo yaliyotokea alipokuwa mwenye umri wa miaka 12. Wazazi wake walimpeleka Yerusalemu kwa ajili ya Sikukuu ya Kupitwa. Walipokuwa wakirudi nyumbani, wakatambua kwamba Yesu hakuwa pamoja nao; basi wakarudi wamtafute. Siku ya tatu, wakampata hekaluni akizungumza na walimu kuhusu maswali ya Kimaandiko. Akimjibu mamake swali lake lenye hangaiko, Yesu aliuliza: “Kwa nini iliwabidi kunitafuta? Je, hamkujua kwamba ni lazima mimi niwe katika nyumba ya Baba yangu?” (Luka 2:49) Yesu alinufaika kupata habari za kiroho kwenye hekalu, ‘nyumba ya Baba yake.’ Leo, Jumba la Ufalme la Mashahidi wa Yehova ni mahali bora pa kupata ujuzi sahihi juu ya Muumba wetu Mtukufu.

      Mkumbuke Yehova Sasa!

      5. Kwa maneno yako mwenyewe, unaweza kuelezaje maneno ya mhubiri yanayopatikana katika Mhubiri 12:1?

      5 Mtu anayemwabudu Yehova kwa moyo wote hutamani kufanya utumishi wa Yehova haraka iwezekanavyo na kumtumikia kwa maisha yake yote. Lakini ana matazamio gani mtu anayetumia ujana wake kwa mambo yasiyofaa kwa sababu hamkumbuki Muumba? Mhubiri alipuliziwa na Mungu kusema hivi: “Mkumbuke Muumba wako siku za ujana wako, kabla hazijaja siku zilizo mbaya, wala haijakaribia miaka utakaposema, Mimi sina furaha katika hiyo.”—Mhubiri 12:1.

      6. Kuna uthibitisho gani kwamba Simeoni na Ana ambao walikuwa wazee walimkumbuka Muumba wao Mtukufu?

      6 Hakuna mtu anayefurahia “siku zilizo mbaya” za uzee. Lakini wazee wanaomkumbuka Mungu ni wenye shangwe. Kwa mfano, yule Simeoni mzee alimpokea Yesu akiwa mtoto mchanga mkononi mwake katika hekalu na kutangaza hivi kwa shangwe: “Sasa, Bwana Mwenye Enzi Kuu, unamwacha mtumwa wako aende huru katika amani kulingana na tangazo lako; kwa sababu macho yangu yameona njia yako ya kuokoa ambayo umefanya tayari mbele ya vikundi vyote vya watu, nuru ya kuondoa shela kwa mataifa na utukufu wa watu wako Israeli.” (Luka 2:25-32) Ana mwenye umri wa miaka 84 pia alimkumbuka Muumba wake. Yeye alikuwa hekaluni sikuzote na alikuwako Yesu alipopelekwa huko akiwa mtoto mchanga. “Na saa hiyohiyo akaja karibu akaanza kumshukuru Mungu akisema juu ya huyo mtoto kwa wale wote wenye kungojea ukombozi wa Yerusalemu.”—Luka 2:36-38.

      7. Wale ambao wamezeeka wakifanya utumishi wa Mungu wana hali gani?

      7 Mashahidi wa Yehova wa wakati huu ambao wamezeeka wakifanya utumishi wa Mungu huenda wakapata maumivu na magumu yaletwayo na uzee. Lakini, wao wana furaha iliyoje, nasi huthamini kama nini utumishi wao mwaminifu! Wao wana “furaha ya BWANA,” kwa kuwa wanajua kwamba ametumia uwezo wake mwingi kutawala dunia na kumweka Yesu Kristo kuwa Mfalme wa kimbingu mwenye nguvu. (Nehemia 8:10) Huu ndio wakati wa vijana kwa wazee kutii himizo hili: “Vijana waume, na wanawali, wazee, na watoto; na walisifu jina la BWANA, maana jina lake peke yake limetukuka; adhama yake i juu ya nchi na mbingu.”—Zaburi 148:12, 13.

      8, 9. (a) Ni nani ambao hawathawabishwi na “siku zilizo mbaya,” na kwa nini? (b) Unaweza kufafanuaje Mhubiri 12:2?

      8 “Siku zilizo mbaya” za uzee hazithawabishi—na labda ni zenye kusononesha sana—kwa wale ambao hawamkumbuki Muumba wao Mtukufu na ambao hawajui makusudi yake matukufu. Hawana ufahamu wa kiroho unaoweza kukabili majaribu yanayotokana na uzee na ole ambao umekumba wanadamu tangu Shetani atupwe kutoka mbinguni. (Ufunuo 12:7-12) Kwa hiyo, mhubiri atuhimiza tumkumbuke Muumba wetu “kabla jua, na nuru, na mwezi, na nyota, havijatiwa giza; kabla ya kurudi mawingu baada ya mvua.” (Mhubiri 12:2) Maneno haya yamaanisha nini?

      9 Solomoni alinganisha wakati wa ujana na majira ya kiangazi ya Palestina wakati ambapo jua, mwezi, na nyota vinaangaza katika anga lisilo na mawingu. Wakati huo vitu huonekana kuwa vyangavu sana. Lakini, wakati wa uzee maisha ya mtu ni kama majira ya baridi kali ya mvua, yakiwa na matatizo mengi. (Ayubu 14:1) Ingehuzunisha kama nini kwa mtu kujua juu ya Muumba na asimtumikie katika kiangazi cha maisha! Katika baridi kali ya maisha ya uzee, hamna furaha, hasa kwa wale ambao walipuuza fursa za kumtumikia Yehova wakati wa ujana wao kwa sababu ya kufuatilia mambo yasiyofaa. Lakini hata tuwe na umri gani, na ‘tumfuate BWANA kwa utimilifu,’ kama alivyofanya Kalebu mwaminifu, ambaye alikuwa mwandamani mwaminifu-mshikamanifu wa nabii Musa.—Yoshua 14:6-9.

      Matokeo ya Kuzeeka

      10. Ni nini kinachowakilishwa na (a) “walinzi wa nyumba”? (b) “wenye nguvu”?

      10 Kisha Solomoni ataja magumu katika “siku ile walinzi wa nyumba watakapotetema; hapo wenye nguvu watakapojiinamisha; na wasagao kukoma kwa kuwa ni haba; na hao wachunguliao madirishani kutiwa giza.” (Mhubiri 12:3) “Nyumba” hiyo yamaanisha mwili wa binadamu. (Mathayo 12:43-45; 2 Wakorintho 5:1-8) “Walinzi” wake ni mikono, ambayo huulinda mwili na kuupa mahitaji yake. Wakati wa uzee mara nyingi mikono hutetemeka kwa sababu ya udhaifu, wasiwasi, na ugonjwa wa kutetemeka. “Wenye nguvu”—miguu—hawana nguvu tena bali wamedhoofika na kuinama hivi kwamba hao hujikokota tu. Lakini, je, wewe hufurahi kuona waamini wenzi waliozeeka kwenye mikutano ya Kikristo?

      11. Kwa njia ya mfano, ni nani hao “wasagao” na “wachunguliao madirishani”?

      11 ‘Wasagao wamekoma kwa kuwa ni haba’—kwa njia gani? Huenda meno yameoza au yameng’olewa, na sasa yamebaki machache tu au hata hayapo. Kusaga chakula kigumu ni kazi ngumu au hata haiwezekani. ‘Hao wachunguliao madirishani’—macho na sehemu nyinginezo zinazohusika na ufahamu zinazotusaidia kuona—hudhoofika, au hata kushindwa kuona kabisa.

      12. (a) ‘Milango imefungwaje katika njia kuu’? (b) Unawaonaje wahubiri wa Ufalme ambao ni wazee?

      12 “Na,” aendelea kusema mhubiri, “milango kufungwa katika njia kuu; sauti ya kinu itakapokuwa ni ndogo; na mtu kusituka kwa sauti ya ndege; nao binti za kuimba watapunguzwa.” (Mhubiri 12:4) Milango miwili ya kinywa—midomo—sasa haifunguki sana au hata imefungwa kabisa isiweze kueleza jambo ambalo limo katika “nyumba,” au mwili, ya wale ambao ni wazee lakini hawamtumikii Mungu. Hakuna jambo linalopelekwa kwenye “njia kuu” ya maisha ya umma. Lakini wahubiri wa Ufalme wenye bidii ambao wamezeeka wana hali gani? (Ayubu 41:14) Huenda wakatembea polepole nyumba hadi nyumba na huenda wengine wakapata shida ya kuongea, lakini kwa hakika wao humsifu Yah!—Zaburi 113:1.

      13. Mhubiri afafanuaje matatizo mengine ya wazee, lakini Wakristo waliozeeka wana hali gani?

      13 Sauti ya kinu inakuwa ndogo kwa sababu chakula hutafunwa kwa fizi zisizo na meno. Akiwa kitandani mzee halali vizuri. Hata sauti za ndege humsumbua. Hawezi kuimba nyimbo nyingi, na wimbo wowote auimbao ni dhaifu. “Binti za kuimba”—yaani sauti za kuimba—‘wamepunguzwa.’ Mzee hasikii vizuri muziki na wimbo unaoimbwa na wengine. Lakini, watiwa-mafuta ambao wamezeeka na waandamani wao, ambao wengine wao pia si wachanga, huendelea kuinua sauti zao katika nyimbo zinazomsifu Mungu kwenye mikutano ya Kikristo. Tunafurahi kama nini kuwa pamoja nao, wakimhimidi Yehova kutanikoni!—Zaburi 149:1.

      14. Wazee husumbuliwa na hofu zipi?

      14 Hali ya wazee inasikitisha kama nini, hasa wale ambao wamepuuza Muumba wao! Mhubiri asema: “Naam, wataogopa kilichoinuka na vitisho vitakuwapo njiani; na mlozi utachanua maua; na panzi atakuwa ni mzigo mzito [“ajikokota,” NW]; na pilipili hoho itapasuka; maana mtu aiendea nyumba yake ya milele, nao waombolezao wazunguka njiani.” (Mhubiri 12:5) Wakiwa juu kwenye ngazi ndefu, wazee wengi huogopa kuanguka. Hata kutazama kitu kilicho juu kwaweza kuwatia kizunguzungu. Kama ni lazima waende kwenye njia zenye watu wengi, wao huogopa sana kujeruhiwa au kushambuliwa na wezi.

      15. ‘Mlozi huchanuaje maua,’ na panzi ‘hujikokotaje’?

      15 Kwa habari ya mzee, inaonekana ‘mlozi unachanua maua’ kwa njia ya kwamba mvi hutokea, kisha nywele huwa nyeupe pepepe. Mvi huanguka kama maua meupe ya mlozi. ‘Anapojikokota,’ labda akiwa ameinama na mikono ikining’inia au ikiwa mikono imewekwa kwenye nyonga navyo viwiko vikiwa vimejikunja kuelekea juu, yeye hufanana na panzi. Lakini ikiwa mmoja wetu yuko hivyo, wengine watambue kwamba tumo katika jeshi la Yehova la panzi, lenye nguvu na kasi!—Ona Mnara wa Mlinzi, Mei 1, 1998, ukurasa wa 8-13.

      16. (a) Ni nini linalodokezwa na ‘kupasuka kwa pilipili hoho’? (b) ‘Nyumba ya milele’ ya mwanadamu ni nini, na ni ishara zipi za kifo kinachokaribia ambazo hudhihirika?

      16 Mzee hana hamu tena ya chakula, hata kama chakula kilicho mbele yake ni kitamu kama pilipili hoho. Pilipili hoho zimetumiwa kwa muda mrefu kuamsha hamu ya kula. ‘Kupasuka kwa pilipili hoho’ kwadokeza kwamba hamu ya mzee ya kula inapopungua, hata pilipili hoho haiwezi kuamsha hamu yake. Mambo hayo yaonyesha kwamba anakaribia “nyumba yake ya milele,” kaburi. Kaburi litakuwa nyumba yake ya milele ikiwa hakumkumbuka Muumba wake na amefuatia mwenendo mwovu hivi kwamba Mungu hamkumbuki katika ufufuo. Ishara za kwamba kifo chakaribia hudhihirishwa na sauti zenye kuomboleza na manung’uniko yanayotoka kwenye milango ya kinywa cha mzee.

      17. “Kamba ya fedha” hukatikaje, na huenda “bakuli la dhahabu” lawakilisha nini?

      17 Tunahimizwa tumkumbuke Muumba wetu “kabla haijakatika kamba ya fedha; au kuvunjwa bakuli la dhahabu; au mtungi kuvunjika kisimani; au gurudumu kuvunjika birikani.” (Mhubiri 12:6) Huenda “kamba ya fedha” ikawa ni uti wa mgongo. Kwa hakika mtu hufa ikiwa njia hii ya ajabu ya kupeleka ujumbe kwenye ubongo yapatwa na madhara yasiyoweza kurekebika. Huenda “bakuli la dhahabu” likarejezea ubongo, ambao upo kwenye fuvu linalofanana na bakuli, na ambao umeunganishwa na uti wa mgongo. Ubongo ni kama dhahabu kwa sababu una thamani sana, na mtu hufa ubongo unapokoma kufanya kazi.

      18. ‘Mtungi kisimani’ wa mfano ni nini, na nini hutendeka unapovunjika?

      18 ‘Mtungi kisimani’ ni moyo, ambao hupokea damu na kuizungusha tena kote mwilini. Mtu akifa, moyo huwa kama mtungi uliovunjika, uliovunjika kisimani kwa sababu hauwezi tena kupokea, kubeba, na kupiga damu iliyo muhimu kwa lishe na burudisho la mwili. ‘Gurudumu linalovunjika birikani’ huacha kuzunguka, na kukomesha mzunguko wa damu unaoendeleza uhai. Kwa njia hiyo Yehova alimfunulia Solomoni mzunguko wa damu muda mrefu kabla ya tabibu wa karne ya 17, William Harvey, kudhihirisha kwamba damu huzunguka mwilini.

      19. Maneno ya Mhubiri 12:7 hutumikaje wakati wa kifo?

      19 Mhubiri aliongezea kusema: “Nayo mavumbi kuirudia nchi kama yalivyokuwa, nayo roho kumrudia Mungu aliyeitoa.” (Mhubiri 12:7) “Gurudumu” likiwa limevunjika, mwili wa binadamu, ambao uliumbwa kwa mavumbi ya ardhi, hurudia mavumbi. (Mwanzo 2:7; 3:19) Nafsi hufa kwa sababu roho, au kani ya uhai, inayotolewa na Mungu humrudia na kubaki na Muumba wetu.—Ezekieli 18:4, 20; Yakobo 2:26.

      Kuna Wakati Ujao wa Aina Gani kwa Wale Wanaomkumbuka?

      20. Musa alikuwa akiomba nini alipotoa sala ambayo inapatikana kwenye Zaburi 90:12?

      20 Solomoni alionyesha vizuri sana umuhimu wa kumkumbuka Muumba wetu Mtukufu. Kwa hakika, wale wanaomkumbuka Yehova na kufanya mapenzi yake kwa moyo wote hawatazamii tu kuishi maisha ambayo kwa ujumla ni mafupi na yenye matatizo. Wawe vijana au wazee, wao wana mtazamo kama wa Musa, ambaye alisali hivi: “Utujulishe kuzihesabu siku zetu, tujipatie moyo wa hekima.” Nabii huyo mnyenyekevu wa Mungu alitamani sana Yehova amwonyeshe, au amfundishe, yeye na Waisraeli jinsi ya kutenda kwa hekima kwa ‘kuhesabu miaka yao’ na kuitumia kwa njia anayoikubali Mungu.—Zaburi 90:10, 12.

      21. Ikiwa tutahesabu siku zetu kwa utukufu wa Yehova, ni lazima tufanye nini?

      21 Hasa vijana Wakristo wanapaswa kuazimia kutii shauri la mhubiri la kumkumbuka Muumba. Wao wana fursa bora kama nini za kumtolea Mungu utumishi mtakatifu! Lakini, hata tuwe na umri gani, tukijifunza kuhesabu siku zetu kwa utukufu wa Yehova katika “wakati [huu] wa mwisho,” twaweza kuendelea kuzihesabu milele na milele. (Danieli 12:4; Yohana 17:3) Bila shaka, ni lazima tumkumbuke Muumba wetu Mtukufu ili tufaulu. Ni lazima pia tutimize wajibu wetu wote kwa Mungu.

  • Je, Unatimiza Wajibu Wako Wote kwa Mungu?
    Mnara wa Mlinzi—1999 | Novemba 15
    • Je, Unatimiza Wajibu Wako Wote kwa Mungu?

      “Mungu ataleta hukumuni kila kazi, pamoja na kila neno la siri, likiwa jema au likiwa baya.”—MHUBIRI 12:14.

      1. Yehova amewafanyia watu wake maandalizi gani?

      YEHOVA huwategemeza wale ambao daima humkumbuka kuwa Muumba wao Mtukufu. Neno lake lililopuliziwa huwapa ujuzi unaohitajika ili wampendeze kikamili. Roho takatifu ya Mungu huwaongoza wafanye mapenzi ya kimungu na “kuzaa matunda katika kila kazi njema.” (Wakolosai 1:9, 10) Pia Yehova huandaa chakula cha kiroho na mwongozo wa kitheokrasi kupitia “mtumwa mwaminifu na mwenye busara.” (Mathayo 24:45-47) Basi, kwa njia nyingi, watu wa Mungu hupata baraka za kimbingu wanapomtumikia Yehova na kufanya kazi muhimu ya kuhubiri habari njema za Ufalme.—Marko 13:10.

      2. Kuhusu kumtumikia Yehova, ni maswali gani yanayoweza kutokea?

      2 Wakristo wa kweli wanafurahi kumtolea Yehova utumishi mtakatifu. Lakini, huenda wengine wakavunjika moyo na kufikiria kwamba jitihada zao hazifai. Kwa mfano, nyakati nyingine huenda Wakristo waliojiweka wakfu wakawa na shaka kama kweli jitihada zao za kudhamiria zinafaa. Kichwa cha familia anapofikiria funzo la familia na utendaji mwingine, yeye aweza kujiuliza maswali kama haya: ‘Je, kweli Yehova anapendezwa na yale tunayofanya? Je, tunatimiza wajibu wetu wote kwa Mungu?’ Maneno yenye hekima ya mhubiri yanaweza kutusaidia kuyajibu maswali hayo.

      Je, Mambo Yote Ni Ubatili?

      3. Kupatana na Mhubiri 12:8, ubatili mkubwa kabisa ni nini?

      3 Huenda wengine wakafikiria kwamba maneno haya ya mwenye hekima yanavunja moyo mtu yeyote—awe kijana au mzee. “Mhubiri asema, Ubatili mtupu; mambo yote ni ubatili!” (Mhubiri 12:8) Kwa kweli, ni ubatili mkubwa kabisa kumpuuza Muumba Mtukufu ujanani, kuzeeka bila kumtumikia, na kwamba jambo pekee ambalo umetimiza maishani ni kuishi maisha marefu. Yote yamekuwa ubatili, au bure, kwa mtu kama huyo, hata akifa akiwa na mali au akiwa mashuhuri katika ulimwengu huu ambao umo katika uwezo wa yule mwovu, Shetani Ibilisi.—1 Yohana 5:19.

      4. Kwa nini inaweza kusemwa kwamba mambo yote si ubatili?

      4 Mambo yote si ubatili kwa wale ambao wanaweka hazina mbinguni wakiwa watumishi waaminifu wa Yehova. (Mathayo 6:19, 20) Wao wana mengi ya kufanya katika kazi ya Bwana yenye kuthawabisha, na kwa hakika kazi hiyo si bure. (1 Wakorintho 15:58) Lakini ikiwa sisi ni Wakristo waliojiweka wakfu, je, tunaendelea kujishughulisha na kazi ambayo Mungu alituagiza tufanye katika hizi siku za mwisho? (2 Timotheo 3:1) Ama tumeanza kuishi maisha ambayo hayatofautiani sana na yale ya jirani zetu kwa ujumla? Huenda wao ni wafuasi wa dini mbalimbali na huenda wakawa wenye kushikilia dini, wakihudhuria ibada zao kwa ukawaida na kujaribu kutimiza matakwa ya ibada yao. Lakini, wao si wahubiri wa ujumbe wa Ufalme. Hawana ujuzi sahihi wa kwamba huu ndio “wakati wa mwisho” na hawana uharaka wowote kuhusu siku hizi tunamoishi.—Danieli 12:4.

      5. Kama hangaiko letu kubwa limekuwa kufuatia mambo ya kawaida ya maisha, tunapaswa kufanya nini?

      5 Yesu Kristo alisema hivi kuhusu nyakati zetu zenye hatari: “Kama vile siku za Noa zilivyokuwa, ndivyo kuwapo kwa Mwana wa binadamu kutakavyokuwa. Kwa maana kama walivyokuwa katika siku hizo kabla ya furiko, wakila na kunywa, wanaume wakioa na wanawake wakiozwa, hadi siku ambayo Noa aliingia ndani ya safina; nao hawakujali mpaka furiko likaja na kuwafagilia mbali wote, ndivyo kuwapo kwa Mwana wa binadamu kutakavyokuwa.” (Mathayo 24:37-39) Hakuna ubaya wowote wa kula na kunywa ikiwa kunafanywa kwa kiasi, na ndoa ni mpango ulioanzishwa na Mungu mwenyewe. (Mwanzo 2:20-24) Lakini tukitambua kwamba hangaiko letu kubwa limekuwa kufuatia mambo ya kawaida ya maisha, kwa nini tusisali juu ya jambo hilo? Yehova anaweza kutusaidia kutanguliza mambo ya Ufalme, kufanya yaliyo sawa, na kutimiza wajibu wetu kwake.—Mathayo 6:33; Waroma 12:12; 2 Wakorintho 13:7.

      Wakfu na Wajibu Wetu kwa Mungu

      6. Watu fulani waliobatizwa hushindwa kutimiza wajibu wao kwa Mungu katika njia gani muhimu?

      6 Wakristo wengine waliobatizwa wanahitaji kusali kwa bidii kwa sababu hawaishi kwa kupatana na wajibu wa huduma ambao walijitwika walipojiweka wakfu kwa Mungu. Kwa miaka kadhaa sasa zaidi ya watu 300,000 wamekuwa wakibatizwa kila mwaka, lakini jumla ya Mashahidi wa Yehova ambao ni watendaji iko chini kwa kulinganishwa na idadi ya hao wanaobatizwa. Wengine ambao walikuwa wahubiri wa Ufalme wameacha kutangaza habari njema. Lakini, ni lazima watu washiriki ifaavyo katika huduma ya Kikristo kabla ya kubatizwa. Kwa hiyo wanajua agizo ambalo Yesu aliwapa wafuasi wake: “Nendeni mkafanye wanafunzi kutoka kwa watu wa mataifa yote, kuwabatiza katika jina la Baba na la Mwana na la roho takatifu, kuwafundisha kushika mambo yote ambayo mimi nimewaamuru nyinyi.” (Mathayo 28:19, 20) Ila tu wawe na matatizo ya kipekee sana ya kiafya au mambo mengine ambayo yanashinda uwezo wao, watu waliobatizwa ambao hawaendelei kutumikia wakiwa Mashahidi watendaji wa Mungu na wa Kristo, hawaishi kwa kupatana na wajibu wao wote kwa Muumba wetu Mtukufu.—Isaya 43:10-12.

      7. Kwa nini twapaswa kukutana pamoja kwa ukawaida kwa ajili ya ibada?

      7 Israeli la kale ni taifa lililojiweka wakfu kwa Mungu, na kulingana na agano la Sheria, watu wake walikuwa na wajibu mbele za Yehova. Kwa mfano, wanaume wote walipaswa kukusanyika kwa ajili ya sherehe tatu za kila mwaka, na mtu ambaye hakushika kimakusudi Sikukuu ya Kupitwa ‘alikatiliwa mbali,’ afe. (Hesabu 9:13; Mambo ya Walawi 23:1-43; Kumbukumbu la Torati 16:16) Ili watimize wajibu wao kwa Mungu wakiwa watu wake waliojiweka wakfu, Waisraeli walipaswa kukusanyika kwa ajili ya ibada. (Kumbukumbu la Torati 31:10-13) Hakuna sehemu ya Sheria iliyosema, ‘Fanya hivyo ikiwa hali zinakufaa.’ Kwa wale ambao sasa wamejiweka wakfu kwa Yehova, kwa hakika kukusanyika kwa ajili ya ibada kwakazia maneno ya Paulo: “Acheni tufikiriane ili kuchocheana kwenye upendo na kazi zilizo bora, si kuachilia mbali kukusanyika pamoja sisi wenyewe, kama vile wengine walivyo na desturi, bali kutiana moyo, na zaidi sana hivyo kwa kadiri mwonavyo siku ikikaribia.” (Waebrania 10:24, 25) Naam, kukusanyika kwa ukawaida na waamini wenzetu ni sehemu ya wajibu kwa Mungu wa Mkristo aliyejiweka wakfu.

      Pima Maamuzi Yako kwa Uangalifu!

      8. Kwa nini kijana aliyejiweka wakfu anapaswa kufikiria kwa sala utumishi wake mtakatifu?

      8 Labda wewe ni kijana ambaye amejiweka wakfu kwa Yehova. Utapata baraka tele ukitanguliza daima masilahi ya Ufalme maishani. (Mithali 10:22) Kwa kusali na kupanga mambo kwa uangalifu, unaweza kutumia angalau miaka ya ujana wako katika utumishi fulani wa wakati wote—njia nzuri ya kuonyesha kwamba unamkumbuka Muumba wako Mtukufu. La sivyo, mapendezi ya mambo ya kimwili huenda yakaanza kuchukua muda wako mwingi na fikira zako. Kama watu kwa ujumla, huenda ukafunga ndoa mapema maishani na kuwa na madeni ili upate vitu vya kimwili. Kazi yenye ufanisi yaweza kuchukua wakati wako mwingi na nguvu zako. Ikiwa una watoto, utalazimika kubeba madaraka ya familia kwa miaka mingi. (1 Timotheo 5:8) Labda hutakuwa umemsahau Muumba wako Mtukufu, lakini ni hekima kutambua kwamba kupangia mambo mapema, au kutoyapangia, kwaweza kuamua maisha yako yatakuwaje ukiwa mtu mzima. Katika miaka ya baadaye, unaweza kufikiria yaliyopita na kutamani kwamba laiti ungalitumia angalau maisha yako ya ujana kikamili zaidi katika utumishi mtakatifu kwa Muumba wetu Mtukufu. Mbona usiyafikirie matazamio yako kwa sala sasa, ili upate uradhi katika utumishi wako mtakatifu kwa Yehova katika miaka yako ya ujana?

      9. Ni jambo gani linalowezekana kwa mtu ambaye amezidi kuzeeka na ambaye pindi moja alikuwa na madaraka mazito kutanikoni?

      9 Ebu fikiria hali nyinginezo—hali ya mtu ambaye pindi moja alitumikia akiwa mchungaji wa “kundi la Mungu.” (1 Petro 5:2, 3) Kwa sababu fulani, yeye aliacha kwa hiari mapendeleo hayo. Ni kweli kwamba sasa amezidi kuzeeka, na huenda ikawa vigumu kwake kuendelea kufanya utumishi wa Mungu. Lakini, je, yeye anapaswa kufikia tena mapendeleo ya kitheokrasi? Mtu kama huyo anaweza kuwa baraka iliyoje kwa wengine ikiwa anaweza kuwa na madaraka zaidi kutanikoni! Na kwa kuwa hakuna mtu anayeishi kwa ajili yake mwenyewe tu, marafiki na wapendwa watafurahi kwamba yeye ameweza kuongeza utumishi wake, kwa utukufu wa Mungu. (Waroma 14:7, 8) Zaidi ya yote, Yehova hatasahau kile ambacho mtu yeyote anafanya katika utumishi wake. (Waebrania 6:10-12) Basi, ni nini kinachoweza kutusaidia kumkumbuka Muumba wetu Mtukufu?

      Mambo Yanayotusaidia Kumkumbuka Muumba Wetu Mtukufu

      10. Kwa nini mhubiri alikuwa na uwezo wa kuandaa miongozo kuhusu suala la kumkumbuka Muumba wetu Mtukufu?

      10 Mhubiri alikuwa na uwezo wa kuandaa miongozo ya kumkumbuka Muumba wetu Mtukufu. Yehova alikuwa amejibu sala yake ya kutoka moyoni kwa kumpa hekima nyingi sana. (1 Wafalme 3:6-12) Solomoni alichunguza sana mambo yanayohusu masuala yote ya wanadamu. Isitoshe, yeye alipuliziwa na Mungu aandike mambo aliyoyapata ili awanufaishe watu wengine. Aliandika hivi: “Walakini, kwa sababu huyo mhubiri alikuwa na hekima, aliendelea kuwafundisha watu maarifa, naam, akatafakari, akatafuta-tafuta, akatunga mithali nyingi. Huyo Mhubiri akatafuta-tafuta ili apate kuona maneno yapendezayo, na yale yaliyoandikwa kwa unyofu, yaani, maneno ya kweli.”—Mhubiri 12:9, 10.

      11. Kwa nini tunapaswa kukubali mashauri ya Solomoni yenye hekima?

      11 Katika Septuagint ya Kigiriki maneno hayo yametafsiriwa kama ifuatavyo: “Na zaidi, kwa sababu mhubiri alikuwa mwenye hekima, kwa sababu alifundisha wanadamu hekima; ili sikio liweze kusikia maneno yenye kupendeza kutokana na mifano, mhubiri alitafuta kwa bidii maneno yapendezayo na maandishi ya unyofu—maneno ya kweli.” (The Septuagint Bible, iliyotafsiriwa na Charles Thomson) Solomoni alijaribu kufikia mioyo ya wasomaji wake kwa maneno yapendezayo na kwa mambo ambayo kweli yalivutia na kufaa. Kwa kuwa alipuliziwa na roho takatifu kuandika maneno yanayopatikana katika Maandiko, twaweza kukubali mara moja matokeo ya uchunguzi wake na mashauri yake yenye hekima.—2 Timotheo 3:16, 17.

      12. Kwa maneno yako mwenyewe, unaweza kuelezaje maneno ya Solomoni katika Mhubiri 12:11, 12?

      12 Hata bila mbinu za kisasa za uchapishaji, kulikuwa na vitabu vingi katika siku za Solomoni. Fasihi kama hizo zilipasa kuonwaje? Yeye alisema: “Maneno yao wenye hekima huwa mfano wa michokoro; na kama misumari iliyogongomewa sana; ndivyo yalivyo maneno yao walio wakuu wa makusanyiko [“mikusanyo ya maneno,” NW], ambayo yatoka kwa mchungaji mmoja. Tena, zaidi ya hayo, mwanangu, kubali maonyo; hakuna mwisho wo wote wa kutunga vitabu vingi; na kusoma sana huuchosha mwili.”—Mhubiri 12:11, 12.

      13. Maneno ya wale ambao wana hekima ya kimungu yanawezaje kuwa kama michokoro, na ni nani walio kama ‘misumari inayogongomewa sana’?

      13 Maneno ya wale wenye hekima ya kimungu huwa kama michokoro. Kwa njia gani? Hayo huwachochea wasomaji au wasikilizaji wafanye maendeleo kwa kupatana na maneno yenye hekima yanayosomwa au kusikizwa. Pia wale ambao wanajishughulisha mno na “mikusanyo ya maneno,” au maneno ambayo kwa kweli ni yenye hekima na yanafaa, ni kama ‘misumari inayogongomewa sana,’ au inayopigiliwa kabisa. Huenda ikawa hivyo kwa sababu maneno mema ya watu hao yanaonyesha hekima ya Yehova na basi yanaweza kuwategemeza wasomaji au wasikilizaji na kuwafanya wawe thabiti. Ikiwa wewe ni mzazi anayemcha Mungu, je, hupaswi kufanya jitihada nyingi za kukazia kikiki hekima kama hiyo katika akili na moyo wa mtoto wako?—Kumbukumbu la Torati 6:4-9.

      14. (a) Hainufaishi “kusoma sana” vitabu vya aina gani? (b) Tunapaswa kuzingatia sana fasihi gani, na kwa nini?

      14 Lakini, kwa nini Solomoni aseme hivyo kuhusu vitabu? Kwa kulinganisha na Neno la Yehova, vitabu vingi sana vya ulimwengu huu vina fikira za wanadamu tu. Vingi vinaonyesha fikira za Shetani Ibilisi. (2 Wakorintho 4:4) Kwa hiyo, hakuna manufaa ya kudumu ya ‘kuvisoma sana’ vitabu hivyo vya kilimwengu. Vingi vya vitabu hivyo hata vinaweza kudhuru kiroho. Kama Solomoni, na tutafakari yale ambayo Neno la Mungu lisemayo kuhusu uhai. Kufanya hivyo kutaimarisha imani yetu na kutufanya tuwe karibu zaidi na Yehova. Kuvisoma sana vitabu vingine au mafundisho mengine kunaweza kutuchosha sana. Hasa kama maandishi hayo yanatokana na kusababu kwa kilimwengu ambako kunahitilafiana na hekima ya kimungu basi hayafai na yanaweza kuharibu imani katika Mungu na makusudi yake. Basi, na tukumbuke kwamba maandishi mengi yenye kunufaisha katika siku za Solomoni na katika siku zetu ni yale yaonyeshayo hekima ya “mchungaji mmoja,” Yehova Mungu. Ameandaa vitabu 66 vya Maandiko Matakatifu, na tunapaswa kuvizingatia sana. Biblia na vichapo vyenye msaada vya ‘mtumwa mwaminifu’ hutuwezesha kupata ‘kumjua Mungu.’—Mithali 2:1-6.

      Wajibu Wetu Wote kwa Mungu

      15. (a) Unaweza kuelezaje maneno ya Solomoni kuhusu “wajibu wote wa mwanadamu”? (b) Ni lazima tufanye nini ili tutimize wajibu wetu kwa Mungu?

      15 Akijumlisha uchunguzi wake wote, mhubiri, Solomoni, asema: “Hii ndiyo jumla ya maneno; yote yamekwisha sikiwa; mche Mungu, nawe uzishike amri zake, maana kwa jumla ndiyo impasayo mtu [“ndiyo wajibu wote wa mwanadamu,” NW]. Kwa maana Mungu ataleta hukumuni kila kazi, pamoja na kila neno la siri, likiwa jema au likiwa baya.” (Mhubiri 12:13, 14) Kumcha au kumstahi Muumba wetu Mtukufu kwa njia ifaayo, kutatulinda, na twatumaini kutalinda familia zetu pia, tusifuate mwenendo wa kipumbavu wa maisha ambao unaweza kutuletea sisi na wapendwa wetu matatizo mengi na huzuni nyingi. Kicho kifaacho cha Mungu ni safi na ndicho mwanzo wa hekima na ujuzi. (Zaburi 19:9; Mithali 1:7) Tukiwa na ufahamu wa ndani wa Neno la Mungu lililopuliziwa na kutumia mashauri yake katika mambo yote, tutatimiza “wajibu [wetu] wote” kwa Mungu. Kufanya hivyo hakumaanishi kuorodhesha wajibu mbalimbali. Badala yake, inatakikana tuchunguze Maandiko tunapotatua matatizo ya maisha na sikuzote kufanya mambo kwa njia ya Mungu.

      16. Kuhusu hukumu, Yehova atafanya nini?

      16 Tunapaswa kutambua kwamba hakuna jambo ambalo Muumba wetu Mtukufu hawezi kuona. (Mithali 15:3) Yeye “ataleta hukumuni kila kazi.” Ndiyo, Aliye Juu Zaidi atahukumu mambo yote, hata yale ambayo hayaonekani kwa macho ya wanadamu. Kujua mambo hayo kwaweza kutuchochea tutii amri za Mungu. Lakini kichocheo kikubwa zaidi chapaswa kuwa upendo wetu kwa Baba yetu wa kimbingu, kwa kuwa mtume Yohana aliandika: “Kwa maana hivi ndivyo kumpenda Mungu humaanisha, kwamba tushike amri zake; na bado amri zake si zenye kulemea.” (1 Yohana 5:3) Na kwa kuwa amri za Mungu zimekusudiwa ziendeleze hali-njema yetu ya milele, kwa hakika ni jambo linalofaa na hata lenye hekima kuzitimiza. Huo si mzigo kwa wapendao Muumba Mtukufu. Wanataka kutimiza wajibu wao kwake.

      Timiza Wajibu Wako Wote

      17. Tutafanya nini ikiwa kwa kweli tunataka kutimiza wajibu wetu wote kwa Mungu?

      17 Ikiwa sisi ni wenye hekima na kwa kweli tunatamani kutimiza wajibu wetu wote kwa Mungu, mbali na kuzishika amri zake, tutakuwa na hofu yenye staha ya kutompendeza. Kwa kweli, “kumcha BWANA ndio mwanzo wa hekima,” na wale wanaozishika amri zake wana “akili njema.” (Zaburi 111:10; Mithali 1:7) Basi na tuendelee kutenda kwa hekima na kumtii Yehova katika mambo yote. Na ni muhimu sana sasa kufanya hivyo, kwa kuwa Mfalme Yesu Kristo yupo, na siku yake ya hukumu akiwa Hakimu aliyewekwa na Mungu imekaribia.—Mathayo 24:3; 25:31, 32.

      18. Tutapata matokeo gani tukitimiza wajibu wetu wote kwa Yehova Mungu?

      18 Kila mmoja wetu sasa anachunguzwa na Mungu. Je, tuna mtazamo wa kiroho, ama tumeruhusu uvutano wa kilimwengu udhoofishe uhusiano wetu pamoja na Mungu? (1 Wakorintho 2:10-16; 1 Yohana 2:15-17) Tuwe vijana au wazee, na tufanye yote tuwezayo ili tumpendeze Muumba wetu Mtukufu. Tukimtii Yehova na kuzishika amri zake, tutakataa mambo ya ubatili ya ulimwengu huu wa kale unaopitilia mbali. Ndipo tunapoweza kuwa na tumaini la uhai udumuo milele katika mfumo mpya wa Mungu ambao aliahidi. (2 Petro 3:13) Hayo ni matazamio mazuri ajabu kama nini kwa wale wote wanaotimiza wajibu wao wote kwa Mungu!

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki